Sunday 24 August 2014

Rasimu ya Warioba ‘yachanwachanwa’

Dodoma. Kuna kila dalili kwamba mabadiliko mengi yaliyopendekezwa katika Rasimu ya Katiba yakigusa miundo ya taasisi nyeti za umma yatawekwa kando na huenda Bunge Maalumu likatoa Katiba isiyokuwa na mabadiliko makubwa kama ilivyotarajiwa.
Gazeti hili limebaini kuwa kamati nyingi za Bunge hilo zimebadili mapendekezo mengi hasa yanayowagusa viongozi na taasisi nyeti kama Bunge, tofauti na ilivyopendekezwa katika Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya uongozi wa Jaji Joseph Warioba.
Miongoni mwa mambo ambayo yamependekezwa kurejeshwa kama yalivyokuwa ni muundo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambalo kwa mujibu taarifa kutoka kwenye kamati mbalimbali, ni kuendelea na muundo wa sasa unaowajumuisha wabunge kutoka Zanzibar.
Katika maelezo yake, Jaji Warioba alisema moja ya kero za muungano katika eneo la Bunge ni malalamiko kwamba wabunge kutoka Zanzibar wamekuwa wakishiriki katika Bunge la Muungano na kushiriki kujadili mambo yanayohusu Tanzania Bara.
Kupitia mfumo wa Serikali tatu, Rasimu ilikuwa na mapendekezo ya kuwapo kwa Bunge la Muungano lenye wabunge 75, lakini mapendekezo hayo pia yamefutwa katika kamati karibu zote na kurejesha mfumo wa sasa pamoja na uwapo wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.
Mwenyekiti wa Kamati Namba Tano, Hamad Rashid Mohamed alisema jana kuwa suala la muundo wa Bunge lilisababisha mvutano mkubwa katika kamati yake na baadhi ya wajumbe walikuwa wakihoji uwakilishi mkubwa wa wabunge wa Zanzibar katika Bunge la Muungano hata kwa mambo ya Tanzania Bara.
Hata hivyo, alitetea hali hiyo akisema uwapo wa wabunge kutoka Zanzibar ni moja ya masharti yaliyowekwa na Katiba. “Hata Katiba ya sasa imeweka sharti la idadi ya wabunge wa Zanzibar, hilo nalo ni sharti la Katiba huwezi kuliondoa, kama unataka kuliondoa unapotunga Katiba maana yake ni lazima uvunje muungano.”
Alisema mwaka 1964 mambo yote ya Tanganyika yaliingizwa kwenye Serikali ya Muungano... “Kwa hiyo ni lazima ukafumue Muungano, useme haya ni ya Tanganyika na haya ni ya Muungano,” alisema.
Hamad alisema katika hadidu ya rejea, Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilikatazwa kugusa mambo ya Muungano. “Hivi wabunge 70 wanaokuja kutoka Zanzibar wakazungumzia mambo ya Bara, hivi kuna dhambi gani, sioni kosa kabisa.” Mwenyekiti huyo alisema kamati yake imebaini kwamba Rasimu ya Warioba ina upungufu mwingi kwani hata baadhi ya kero zilizotajwa zilishafanyiwa kazi na Serikali.
Hoja ya ushiriki wa Wazanzibari katika masuala ya Tanzania Bara iliripotiwa kuibuka katika Kamati Namba Moja ambako mmoja wa wajumbe, Ally Keissy alinikuliwa akihoji sababu za wajumbe wa Zanzibar kushiriki mambo ambayo wao siyo sehemu yake.
Mbali na muundo wa Bunge, kamati nyingi pia zimefuta mapendekezo kadhaa yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba ambayo ni pamoja na wabunge kutokuwa mawaziri, ukomo wa ubunge kwa vipindi vitatu vya miaka mitano mitano, wabunge kuwajibishwa na wananchi, kupunguzwa kwa madaraka na kinga ya rais.
Katika Kamati Namba Tano, Hamad alisema suala la wananchi kumuondoa mbunge lilikataliwa. “Hivi ni kigezo gani ambacho kinaonyesha mbunge hakuweza kuwaletea wananchi maendeleo. Nini utatumia cha kupima ufanisi wa huyu mbunge?”
Alisema kuliweka jambo hilo katika Katiba ni kuleta matatizo na kwamba wameliacha suala hilo mikononi mwa vyama vya siasa kuangalia kama mbunge anafanya kazi ya ilani zao au la.
Mgawanyiko mpya
Habari zaidi zinasema kuwekwa kando kwa mapendekezo mengi yaliyolenga kurekebisha mifumo ya uongozi na utawala, kumesababisha mgawanyiko hasa miongoni mwa wajumbe watetezi wa muungano wa serikali mbili, ambao awali, waliahidiwa kwamba muundo huo usingekuwa na sura yake ya sasa, bali ungeboreshwa.
Mmoja wa wabunge wa CCM alisema jana kwamba: “Tutawapa wapinzani sifa maana umma utaamini kwamba bila wao hakuna kinachoweza kubadilika, sasa kama tunarejesha kila kitu ambacho kiko kwenye Katiba tuliyonayo kuna maana gani ya kuwa na mchakato?”
Mmoja wa wenyeviti wa kamati za Bunge Maalumu naye alisema kinachoendelea ndani ya kamati nyingi ni kufuta mapendekezo ya Rasimu na kuleta mapendekezo mapya ambayo ni sawa na yaliyomo kwenye Katiba ya sasa.
“Ndani ya chama (CCM) tuliamua kupinga mapendekezo ya serikali tatu baada ya kuahidiwa kwamba tutakuja na muundo wa serikali mbili zilizoboreshwa, lakini hata hizo hatuzioni. Kwa hiyo wananchi wataamini kwamba kilichosemwa na Ukawa (Umoja wa Katiba ya Wananchi), ni cha kweli,” alisema mwenyekiti huyo.
Utata wa akidi
Mwenyekiti wa Kamati Namba Tatu, Dk Francis Michael aliamua kuahirisha kikao jana saa tano asubuhi kutokana na kile alichokiita kuwa ni kuwapa muda wajumbe waende kusoma zaidi sura ya tisa ambayo inahusu muundo wa Bunge.
Hata hivyo, habari ambazo zilikuwa zimelifikia gazeti hili mapema zinasema kuahirishwa kwa kikao hicho kulitokana na akidi kutotimia, taarifa ambazo Dk Michael alizikanusha kwa kuonyesha idadi ya wajumbe ambao walikuwa wamesaini karatasi ya mahudhurio.
Katika maelezo yake Mwenyekiti huyo alikiri kwamba hadi ilipotimu saa 4:00 asubuhi jana kamati yake ilikuwa ikikabiliwa na upungufu wa wajumbe wanne, hivyo waliwapigia simu na kubaini kwamba walikuwa katika shughuli nyingine ikiwamo kumpokea Rais Jakaya Kikwete.
“Baadhi ya wajumbe ni mawaziri kwa hiyo baada ya kukamilisha majukumu yao walifika na saa tano hivi akidi ilikuwa imetimia,” alisema Dk Michael.

Profesa Mbilinyi afichua siri nzito

Dar es Salaam. Aliyekuwa Waziri wa Fedha, Profesa Simon Mbilinyi amefichua siri na kueleza kwamba wakati alipochaguliwa kuiongoza wizara hiyo nchi ilikuwa imefilisika.
Hata hivyo, alisema kuwa kwa ushirikiano na rais wa wakati huo, aliweza kuimarisha uchumi ndani ya siku 365 alizofanya kazi.
Profesa Mbilinyi aliyeshika wadhifa huo katika Serikali ya Awamu ya Tatu iliyoongozwa na Rais Benjamin William Mkapa, alisema hayo kwenye mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake Upanga, Dar es Salaam, ambapo alieleza hali ya uchumi ilivyo sasa ikilinganishwa na miaka 19 iliyopita.
Alisema wakati alipopewa jukumu la kuiongoza wizara hiyo mwaka 1995 na Rais Benjamin Mkapa, alikuta uchumi umetetereka kwa kiasi kikubwa, hata taifa kushindwa kukubalika na taasisi za fedha za kimataifa na wafadhili waliosusa kutoa misaada wala kuikopesha fedha.
“Mkapa aliniteua kuwa waziri wake wa fedha, lakini wakati ananikabidhi ofisi hiyo, hali ya uchumi ilikuwa ni mbaya sana. Nilikuta uchumi umetetereka, sababu hatukulipa madeni ya kimataifa, wakasusa. Kimsingi nchi ilifilisika, lakini hatukuweza kusema mbele ya wananchi,”alisema Profesa Mbilinyi na kuongeza:
“Nilikubali na kuanza kufanya kazi kama waziri tukishirikaina naye (Mkapa), katika mambo mbalimbali ili kuweka uchumi katika hali nzuri. Uhusiano baina ya Serikali na taasisi hizo za kimataifa pia nchi wafadhili haukuwa mzuri, kwa hiyo tukajitahidi kurudisha heshima yetu. Tulirudisha heshima na kukubali masharti machache ya msingi ya Shirika la Fedha Duniani(IMF) na Benki ya Dunia, ikiwamo suala la uanachama, uchumi ukaanza kufufuka.”
“Kwa kipindi hicho hatukuingia kwenye makubaliano mengine ya mikopo hadi baadaye sana. Kwa hiyo ndiyo ilikuwa njia ya kurudi kwa IMF na WB kwa kuzingatia hayo,”alifafanua Profesa Mbilinyi.
Baada ya muda kiasi alisema wakaanza tena kufanya makubaliano ya baina ya nchi mbili na kuanza tena kupata misaada hasa kutoka Korea Kaskazini, India, Japan na Urusi na baadaye uchumi ukaanza kuonekana unaweza kufufuka ndipo Benki ya Dunia ikarejea na makubaliano ya kawaida.
“Hata hivyo, sikukaa hapo muda mrefu. Nilifanya kazi zote ndani ya mwaka mmoja nikamaliza. Hapo tulishainua uchumi hadi ukakaa sawa, tulikuwa kwenye nafasi nzuri kiuchumi kama nchini nyingine wanachama wa Benki ya Dunia,”alisema.
Kiongozi huyo mkongwe wa masuala ya uchumi alisema, licha ya kuwa alifanya kazi kwa juhudi na bidii kwa ajili ya masilahi ya taifa katika Wizara ya Fedha, baadhi wa watu hawakuona jema katika hilo.
“Licha ya kuwa mambo yalienda vizuri, kipindi hicho cha mwaka mmoja nilijenga uadui na watu wengi kwani niliwazibia mianya ya ulaji. Hata hivyo, jambo hilo ndilo lililosababisha kuachia nafasi hiyo na kumwambia Mkapa:“Naenda kuendelea na ubunge wangu, mchague mwingine akusaidie katika masuala ya fedha,”alisema Mbilinyi na kuongeza kuwa hilo ni moja kati ya mambo yaliyoweka historia katika maisha yake ya kulitumikia taifa la Tanzania.
Profesa Mbilinyi ambaye pia amewahi kuwa mashauri wa kiuchumi wa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, alisema baada ya uamuzi huo aliamua kujikita kwenye ubunge pekee.
“Wakati Mkapa aliponiteua kuwa waziri wake wa fedha nilikuwa mbunge wa Peramiho, hivyo baada ya mwaka mmoja na kama mwezi mmoja hivi nilipoamua kuachia wadhafa huo, nikawa mbunge kwa jimbo langu kwa miaka kumi, kabla ya kuacha kujihusisha na masuala ya kisiasa. Huo ndiyo ukawa mwisho na siasa zangu. Ilikuwa mwaka 2005,” alisema Profesa Mbilinyi.
Akilinganisha hali ya uchumi wakati alipokuwa waziri na sasa, Profesa Mbilinyi ambaye sasa anafanya shughuli za mshauri wa uchumi akiwa pia mkulima na mfugaji alisema kuwa kwa mtazamo wake mwenendo wa uchumi ni mzuri.
“Sasa hivi nadhani una matatizo ya kawaida, lakini tunaendelea vizuri. Kwa mwendo huu, nadhani tutafikia malengo ya kuwa kati ya mataifa yenye uchumi wa kati duniani ifikapo mwaka 2025, kama tukiendelea hivi ,” alisema Profesa Mbilinyi na kuongeza:
“Kwa gesi iliyogunduliwa, uwezekano wa kupatikana mafuta na madini, inatia imani kwamba tunaweza kufika mbali. Rais Kikwete awe wa mwisho kuiongoza Tanzania ikiwa katika hali ya umasikini. Lakini pia nampongeza Rais Kikwete kwa kufikisha uchumi wa nchi ulipo sasa.”
Kuteuliwa na Nyerere
Akizungumzia kuteuliwa kwake na Nyerere alisema: “Alikuwa mwalimu wangu nilipokuwa nasoma Shule ya Sekondari Pugu. Wakati anaondoka kwenda kuanza siasa mwaka 1955 alituacha pale. Nilimaliza shule 1956 nikawa nafanya kazi ya kuuza mafuta Sheli BP, Pugu.
Lakini wakati huo nilikuwa namsaidia Mwalimu kufundisha makada wa TANU ambao ni vijana.
Niliwafundisha hesabu na Kiingereza wakati wa usiku katika Mtaa wa Lumumba kwa sababu wakati ule watumishi wa Serikali walikuwa hawaruhusiwi kuingia kwenye siasa” alisema Profesa Mbilinyi.
Aliongeza: “Alipokuwa rais akakumbuka kuwa Mbilinyi yupo Chuo Kikuu na kwa vile nilikuwa nafundisha vijana wa TANU, basi akaniita mimi pamoja na Justine Rweyemamu tumsaidie kumsomea makaratasi yake ya uchumi.
Alikuwa anasema kuwa uchumi wake ni wa kisiasa, hivyo tukawa wasaidizi wake wa masuala ya uchumi pamoja na vijana wengine kama saba hivi.”
Alielezea kuwa alifanya kazi na Mwalimu Nyerere kwa maika minane na kwamba anamkumbuka kwa mambo mengi.

Kesi yafunguliwa Bunge la Katiba, Kesi ya kuhoji uhalali wake yafunguliwa

Dar es Salaam/Dodoma. Bunge la Katiba linaloendelea mjini Dodoma kwa sasa liko katika hatihati ya kuendelea baada ya kufunguliwa kesi ya kuhoji madaraka yake.
Kesi hiyo ilifunguliwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam jana na Mwandishi wa Habari Saidi Kubenea, kupitia kwa wakili wake Peter Kibatala, dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Katika kesi hiyo iliyopewa usajili wa namba  28 ya mwaka 2014, Kubenea anaiomba mahakama hiyo itoe tafsiri sahihi ya Mamlaka ya Bunge la Katiba. Kubenea amefungua kesi hiyo akiomba mahakama itoe tafsiri hiyo, chini ya  vifungu vya 25 (1) na 25 (2) vya Sheria ya Marekebisho ya Katiba namba Namba 83 ya mwaka  2011.
Sambamba na kesi hiyo ya kuomba tafsiri ya mamlaka ya Bunge  hilo, pia Kubenea amewasilisha maombi mahakamani hapo akiiomba mahakama itoe zuio la muda la kusimamisha Bunge hilo ili kusubiri uamuzi wa maombi ya tafsiri hiyo.
Maombi hayo ya kusimamisha Bunge hilo kwa muda yaliyopewa usajili wa namba 29 ya mwaka 2014, pamoja na maombi ya msingi ya tafsiri ya mamlaka ya Bunge yote yalifunguliwa mahakamani hapo jana chini ya Hati ya Dharura.
Katika kesi hiyo ya msingi anaiomba Mahakama hiyo itoe tafsiri sahihi ya masharti ya vifungu hivyo vya sheria hiyo na pia itamke kama Bunge hilo lina mamlaka ya kubadilisha maudhui ya Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kwa kiwango gani.
Kwa mujibu wa hati ya madai, Kubenea anadai kuwa msingi wa kesi hiyo unatokana na uamuzi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Desemba Mosi, 2011, lililopitisha  Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Anasema sheria hiyo ilikuwa na lengo la kuratibu mchakato wa kutungwa kwa Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Anaendelea kusema kuwa kutokana na sheria hiyo,  Rais aliunda Tume ya Mabadiliko ya Katiba pamoja na mambo mengine vilevile kukusanya maoni ya wananchi kuhusu mapendekezo ya Katiba Mpya na kwamba kwa msingi huo Tume hiyo iliandaa Rasimu ya Katiba.
Anadai kuwa baada ya Tume hiyo kuundwa iliendelea kukusanya maoni ya wananchi yaliyotolewa katika mikutano ya hadhara na katika miundo tofauti ikiwamo mabaraza ya Katiba yaliyoanzishwa kila wilaya kwa lengo hilo.
Hati hiyo inaendelea kueleza kuwa kwa mujibu wa takwimu halisi za tume hiyo,  jumla ya watu 333,537 walitoa maoni yao katika nyanja tofauti, tofauti za mapendekezo ya Katiba, ambayo ndiyo Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyatumia kuandaa Rasimu ya Katiba Mpya.
Inaendelea kueleza hati hiyo kuwa baada ya Rais kukabidhiwa rasimu ya mwisho Desemba 8, 2013, kwa mujibu wa vifungu vingine vya sheria hiyo, aliunda Bunge la Katiba kwa lengo la kujadili Rasimu ya Katiba na hatimaye kupata Katiba Mpya.
Hata hivyo, kwa mujibu wa hati hiyo baada ya Bunge la Katiba kuundwa, mjadala uliibuka ndani na nje  ya  misingi ya kisheria kuhusu mamlaka yake, kama Bunge linaweza kwenda kinyume na Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na tume hiyo.
Inaendelea hati hiyo kubainisha kuwa mjadala huu pia uliibuka ndani ya Bunge la Katiba lenyewe kuhusiana na mamlaka yake katika utekelezaji wa majukumu yake kama lina mipaka au la kwa mujibu wa vifungu hivyo 25 (1) na 25 (2) vya sheria hiyo.
Katika kusisitiza mjadala kuhusu mamlaka ya bunge hilo, hati hiyo inatoa mfano wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) katika mkutano wake wa mwaka, ambacho kilisema kuwa vifungu hivyo havilipi bunge hilo mamlaka ya kubadili rasimu hiyo.
Hati hiyo inaongeza kuwa wakati TLS wakitoa msimamo huo, kuna wataalamu wengine wa sheria wanadai kuwa  Bunge hilo linaweza kubadilisha na kuongeza ibara kadri itakavyoona inafaa bila kujali rasimu hiyo.
Kwa mujibu wa hati hiyo, mvutano huo ndani ya Bunge hilo ulisababisha baadhi ya wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutoka nje na kususia vikao, wakidai kuwa  rasimu hiyo haiwezi kubadilishwa. Msimamo huo wa wajumbe wa Ukawa, kwa mujibu wa hati hiyo ni  tofauti na wajumbe wengine waliobaki wanaodai kuwa Bunge hilo lina mamlaka ya kubadili vifungu vya rasimu.
Kwa mujibu wa hati hiyo, utungaji wa Katiba ni jambo la kitaifa ambalo si tu kwamba linabeba matumaini ya Watanzania bali pia linabeba mustakabali na ustawi wa nchi.
Hivyo, hati hiyo inaeleza kuwa tafsiri sahihi ya mamlaka ya Bunge la Katiba dhidi ya Rasimu ya Katiba ni jambo  muhimu sana katika kuongoza mchakato huo ili kuhakikisha kuwa unakwenda kwa mujibu wa sheria zinazohusika.
Katika hati ya maombi, Kubenea anaomba mahakama itoe amri ya kusimamisha kwa muda vikao vya Bunge la Katiba vinavyoendelea Dodoma, kusubiri uamuzi wa  Mahakama kuhusu mamlaka yake.
Katika hati ya kiapo chake aliyoiambatanisha na kesi na maombi hayo, Kubenea anadai kuwa hata baada ya Wajumbe wa Ukawa kutoka nje, wajumbe waliobaki wanaendelea kujadili rasimu hiyo.
Hati hiyo ya kiapo inaeleza kuwa kufunguliwa kwa kesi hiyo sambamba na maombi hayo ya kusimamisha kwa muda Bunge la Katiba si tu kunalenga kupata tafsiri ya Kimahakama kuhusu mamlaka ya Bunge la Katiba.
Rafu Kamati za Bunge Maalumu
Wakati kesi hiyo ikifunguliwa, kumekuwa na taarifa ndani ya kamati za Bunge zinazoendelea kuchambua rasimu hiyo zinazoeleza kuchezwa rafu ili kuwezesha upatikanaji wa akidi kwa ajili ya hatua ya kupiga kura kupitisha ibara za rasimu hiyo katika baadhi ya kamati.
Hivi sasa kamati nyingi ziko katika hatua ya kupiga kura ili kupitisha ibara za Rasimu ya Katiba, kazi ambayo inahitaji theluthi mbili ya wajumbe kutoka pande za muungano kwa mujibu wa kanuni za Bunge Maalumu.

 Ili kutimiza matakwa hayo, gazeti hili limebaini kuwa rafu zimeanza kuchezwa hasa katika kamati ambazo zimeshindwa kutimiza sharti hilo. Moja ya rafu hizo ni ile ya mjumbe wa Kamati namba tano, Maida Hamad Abdallah kuhamishiwa kinyemela katika Kamati namba 8, kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni kuwezesha upatikanaji wa akidi katika kamati aliyohamia.
 Habari zinasema mjumbe huyo kutoka Zanzibar alishiriki kupiga kura juzi mchana na wajumbe wa kamati hiyo walielezwa kuwa amepelekwa ili kuziba nafasi ya Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum ambaye hawezi kushiriki vikao hivyo kutokana na kwamba ni mgonjwa.
 Hata hivyo, suala hilo lilizua mvutano kiasi baada ya baadhi ya wajumbe kuhoji uhalali wa uhamisho huo ambao ni kinyume cha kanuni za Bunge Maalumu, hasa ikizingatiwa kwamba alipigia kura mambo ambayo hakushiriki kuyajadili na kuyafanyia uamuzi.
Mwenyekiti wa Kamati namba tano, Hamad Rashid Mohamed alithibitisha Abdallah kuhamia kamati namba nane inayoongozwa na Naibu Spika wa Bunge la Muungano, Job Ndugai kwa maelezo kwamba aliomba mwenyewe.
“Ni jambo ambalo ameomba mwenyewe kuhamia huko na ameruhusiwa maana hilo ni jambo la kawaida kama ambavyo wajumbe wengine kama kina Mbowe (Freeman) waliwahi kuomba, siyo jambo geni,” alisema Rashid.
 Hata hivyo, Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad alisema hakuwa na taarifa za uhamisho huo. Alipoulizwa kuhusu iwapo Kanuni zinaruhusu alisema suala la kupanga ujumbe wa kamati liko chini ya mamlaka ya mwenyekiti wa Bunge hilo.
 “Kwa kweli sifahamu na wala sina taarifa hiyo, hilo suala la kanuni pengine hebu zisome ili ufahamu zinasemaje kuhusu mjumbe kuhama kutoka kwenye kamati moja kwenda kamati nyingine,” alisema Hamad.
 Wajumbe wa Bunge Maalumu waliokwisharipoti wanakaribia 450, idadi ambayo ni zaidi ya theluthi mbili ya akidi inayotakiwa, lakini hali ni tofauti kwenye kamati kutokana na sababu mbalimbali, utoro ikiwa mojawapo.
 Kutokana na mwenendo huo na wajumbe wengi kutoingia kwenye vikao licha ya kuripoti, kuna wasiwasi iwapo akidi itapatikana wakati wa kupitisha rasimu hiyo wakati Bunge Maalumu litakapoanza kukutana kwa umoja Septemba 2 mwaka huu.
Matakwa ya kanuni
Kanuni ya 55 (1) ya Kanuni za Bunge Maalumu Toleo la 2014 inasema: “Kamati zinaundwa na mwenyekiti kwa namna ambayo itawezesha kila mjumbe kuteuliwa kuwa mjumbe wa kamati mojawapo.”
Fasili ya pili ya kanuni inasema wakati wa kufanya uteuzi wa wajumbe hao, mwenyekiti atazingatia kwa kadri inavyowezekana idadi ya wajumbe inalingana kwa kila kamati na uwiano kutoka pande zote za muungano.
Kadhalika kanuni hiyo inasema katika uteuzi wake mwenyekiti atazingatia idadi ya kila aina ya wajumbe ilivyo katika Bunge Maalumu, jinsia, wajumbe wenye mahitaji maalumu na uwepo wa wajumbe wenye utaalamu wa sheria.
Kanuni hiyo iko kimya kuhusu uhamishaji wa wajumbe na fasili yake ya nne inasema: “Ujumbe katika kamati utadumu kwa kipindi chote cha maisha ya Bunge Maalum.”
Waraka wa uchambuzi wa mgawanyo wa wajumbe katika kamati unaonyesha kuwa Kamati namba tano alikotoka Maida ina wajumbe 52 na kati yao 34 wanatoka Tanzania Bara na 18 Zanzibar wakati kamati alikohamia pia ina wajumbe 52; 35 kutoka Tanzania Bara na 17 kutoka Zanzibar.
Kwa maana hiyo hata kama uhamisho wa Maida ungekuwa na lengo la kuimarisha uwiano kwa maana ya pande za muungano, ni dhahiri kwamba unaathiri kwa maana ya idadi wajumbe kutoka Zanzibar katika kamati namba tano.
Gazeti hili lilimtafuta Ndugai kwa lengo la kupata maelezo jinsi alivyompokea mjumbe huyo, lakini kutwa nzima ya jana simu yake ilikuwa ikiita bila majibu. Kadhalika Maida naye alitafutwa lakini simu yake ilikuwa imezimwa wakati wote. Maida hakuwamo kwenye kamati yake ya awali namba nne ilipokutana jana mchana baada ya kuwa wamepumzika asubuhi kupitia sura za nyongeza.
Kupitisha uamuzi
Kanuni hizo pia zinaelekeza kwamba wakati wa kupitisha uamuzi lazima wajumbe wawe wamefikia theluthi mbili kwa pande zote za muungano, jambo ambalo limekuwa gumu kutokana na mahudhurio hafifu kwenye kamati husika.

Pinda abadili upepo urais CCM

Dodoma. Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ameingia rasmi katika mbio za kuwania urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), hatua ambayo imebadili mwelekeo wa kinyang’anyiro cha nafasi hiyo kubwa ya uongozi nchini kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015.
 Gazeti hili limethibitisha kwamba Pinda tayari ameamua kujitosa kuwania nafasi hiyo kupitia CCM ambayo tayari inawaniwa na makada wa chama hicho wasiopungua 15 na baadhi yao wameishatangaza nia zao kwa nyakati tofauti.
Habari kutoka ndani ya CCM zinasema uamuzi wa Pinda kuwania urais mwaka mmoja tu kabla ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwakani, umesababisha kiwewe miongoni mwa wagombea na kunakifanya kinyang’anyiro hicho kuchukua sura mpya.
Kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM aliliambia gazeti hili siku chache zilizopita mjini Dodoma kuwa: “Na sisi tumesikia kwamba PM (Waziri Mkuu) amejitosa na kama ni kweli atawasumbua wagombea wengi kutokana na rekodi yake hasa katika uadilifu.”
“Yeye (Pinda) ana faida tatu kubwa; kwanza hana kundi katika chama, anaelewana na watu wote, pili nafasi yake ya uwaziri mkuu inampa nafasi ya kufahamika kwa watu wengi na tatu rekodi yake ya uadilifu, hana kashfa za ovyoovyo, labda kama ataharibu dakika hizi za mwisho,” alisema kiongozi huyo ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe.
Wengine ambao wamekuwa wakitajwa kuwania uraia kupitia CCM ni Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa na mtangulizi wake katika nafasi hiyo, Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
 Wegine ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta. Wengine wanaotajwa ni Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Waziri wa Katiba, Asha-Rose Migiro.
 Pia wamo Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja, Mbunge wa Msalala, Ezekiel Maige na aliyewahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Ujerumani, Balozi Ali Karume.
Wasomi
Profesa wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, George Shumbusho alisema wingi wa wanaojitokeza kutaka kuwania urais ni njia ya kuunda mtandao utakaomwezesha mtu fulani au mmoja kunyakua tiketi hiyo.
“Watu wanapiga kampeni katika harambee kwa njia ya kutengeneza mitandao, kwani ukifika wakati wa chama kumpitisha mgombea, asiposhinda ataibuka na kuwaeleza kuwa mnaoniunga mkono mimi muungeni fulani,” alisema.
Naye Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Richard Mbunda alisema kujitokeza kwa idadi kubwa ya wanaowania nafasi ya urais, kutatoa fursa ya wananchi kutambua udhaifu wa kila mmoja jambo litakalowezesha kupatikana kwa mtu sahihi wa kupeperusha bendera ya chama hicho.

“Wakiwa wengi, kila mmoja atataka kuonyesha umahiri wake na sisi ambao ni wananchi watawaliwa tutaweza kutambua upungufu wa kila mmoja, jambo litakalosaidia kupatikana kwa mtu sahihi,” alisema Mbunda
Kambi ya Pinda 
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwa siku kadhaa mjini Dodoma ambako vikao vya Bunge Maalumu vinaendelea umebaini kuwa kambi ya Pinda inaongozwa na Mwenyekiti wa Mamlaka za Mitaa Tanzania (ALAT) ambaye pia ni Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk Didas Masaburi.
 Inadhaniwa kuwa Dk Masaburi atatumia ushawishi wake kwa viongozi wa mamlaka za miji na wilaya zinazoongozwa na wenyeviti wa halmashauri na mameya wa miji, manispaa na majiji kumuunga mkono mgombea huyo ambaye pia hivi sasa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ziko chini ya ofisi yake.
Wiki hii kundi la wafuasi wa Pinda likiongozwa na Dk Masaburi lilikuwa mjini Dodoma likijaribu kutafuta kuungwa mkono na makada viongozi wa CCM ambao walikuwa wakishiriki kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho pamoja na wale walioko katika Bunge Maalumu.  Habari zinasema mbali na Dodoma, tayari kambi hiyo imeshafanya vikao kadhaa jijini Dar es Salaam na Visiwani Zanzibar lengo likiwa ni kutafuta kuungwa mkono na makada wa CCM katika sehemu hizo. Hivi sasa nguvu za Pinda zinaelekezwa katika mikoa mingine nchini kwa lengo hilohilo. Kutokana na kasi ya kambi yake, wafuasi wa baadhi ya wagombea wameanza kufuatilia mwenendo wao kwa lengo la kukusanya ushahidi wa kile wanachokiita ‘rafu’ zinazochezwa ili kupata ushahidi unaoweza kutumika dhidi ya mgombea huyo wakati mchakato wa uchaguzi ndani ya CCM utakapoanza mapema mwakani.
Itakumbukwa kwamba makada watano wa chama hicho ambao ni Lowassa, Membe, Makamba, Wassira na Ngeleja wanatumikia adhabu na wapo chini ya uangalizi wa chama hicho baada ya kutiwa hatiani kwa makosa ya kuanza kampeni za urais kabla ya muda kutangazwa. 
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alisema hivi sasa ni mapema mno kusema ni lini mchakato wa kupata wagombea wa nafasi za uongozi ndani ya chama hicho utaanza na kwamba wakati mwafaka ukiwadia wananchi watafahamishwa.
Uwezo, udhaifu wake
Hata hivyo wakosoaji wake wanasema Pinda akiwa Waziri Mkuu hana cha kujivunia na kwamba amekuwa mzito kufanya uamuzi mara kadhaa kiasi cha kusababisha baadhi ya mambo muhimu ya nchi kukwama na kwamba kwa maana hiyo hastahili kuwa rais.
“Ni kitu gani ambacho nchi inakikumbuka kuhusu huyu bwana ambacho alikifanya katika miaka yake ya uwaziri mkuu, kama alikuwa kwenye nafasi kubwa kiasi hicho na hakuna alichofanya, atawezaje kumudu madaraka ya mkuu wa nchi?” alihoji mmoja wa makada wakongwe wa CCM.
Waziri mmoja wa sasa (jina tumelihifadhi), alisema Pinda hana uwezo wa kuongoza nchi, kwani wao wakiwa mawaziri ameshindwa kuwasaidia katika kero mbalimbali walizokuwa wakimfikishia kama kiongozi wao.
 “Muulize waziri yeyote kuhusu uwezo wa jamaa, kila kukicha tunampelekea mambo tunayokutana nayo, lakini hakuna kinachowezekana kwake, atakwambia subiri leo, subiri kesho na hatimaye jambo linaishia hivyohivyo,” alisema.
Kwa upande mwingine, watetezi wake wanasema Pinda wanayemnadi ni yule aliyepata kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa – Tamisemi) kiasi cha kuonekana anafaa kuwa Waziri Mkuu.
 Wanasema kushindwa kwake kufanya kazi ipasavyo ni matokeo ya sababu zilizomfanya mtangulizi wake, Lowassa kung’oka katika nafasi yake.

Friday 1 August 2014

AJIRA: Watu 6,740 kuwania nafasi 47 za kazi TBS

Dar es Salaam. Watu 6,740 leo wanatarajia kufanyiwa usaili wa kuwania nafasi 47 zilizotangazwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Aprili, mwaka huu.
Usaili huo unataka kufanana na ule wa Idara ya Uhamiaji ambao ulihusisha waombaji 10,000 waliokuwa wakiwania nafasi 70, utafanyika leo na kesho katika Ukumbi wa Yombo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Ili kuepuka kuchaguliwa kwa waombaji wenye uhusiano na wafanyakazi wa shirika hilo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wake, Joseph Masikitiko aliliambia gazeti hili jana kuwa kazi ya usaili itafanywa na taasisi nyingine na TBS itapelekewa majina 47 ya watakao kuwa wamekidhi vigezo.
Masikitiko alisema ili kuepuka upendeleo pia, wameamua kujivua kusimamia mchakato huo na utafanywa na taasisi mbalimbali, na akiitaja moja ya taasisi hizo kuwa ni ya Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (Sua).
“Kuna taasisi tumezichagua zisimamie usaili huo, wao watasimamia na wakikamilisha watatuletea majina hayo,” alisema.
Alisema wameamua kufanya hivyo ili kuepuka yale yaliyowakumba wenzao wa Idara ya Uhamiaji.
Aliongeza: “Hata hizo taasisi tulizoomba zinapaswa zitende haki na ziepuke kutumiwa na baadhi ya watu ambao siyo waaminifu, tunahitaji wafanyakazi watakaopatikana wawe wenye sifa zinazotakiwa.”
Usaili wa Uhamiaji uliofanyika katika Uwanja wa Taifa Dar es Salasam, ulihusisha zaidi ya watu 6,000 kati ya watu 10,000 walioomba nafasi hizo.
Baada ya usaili wa watu 6,115, walipatikana 1,681 ambao waliingia katika kinyang’ayiro cha kusaka watumishi 70.
Hata hivyo, Serikali ilisitisha ajira hizo 70 baada ya kuzuka kwa tuhuma za upendeleo uliokithiri wakati wa usaili.
Kati ya nafasi za kazi 22 zilizoombwa, nafasi iliyoombwa na watu wachache ni ya ofisa maabara msaidizi ambayo imeombwa na watu 61 na anatakiwa mtu mmoja.
Katika nafasi ya mhasibu msaidizi, wameomba watu 1,360, lakini wanaotakiwa kuajiriwa ni watu watatu tu.
Nafasi zilizotangazwa na shirika hilo na idadi ya walioziomba katika mabano ni ya mhasibu msaidizi (1,350), mkaguzi msaidizi wa ndani (266), msaidizi wa mahesabu (305), ofisa rasilimali watu (857), Ofisa viwango (211), maofisa ubora wa viwango (752) na wataalamu wa hali ya hewa (117).
Wengine ni mhandisi wa mitambo (89), fundi mchundo (88), ofisa maabara msaidizi (61), msaidizi wa maabara (141), Mtaalam wa mifumo ya kompyuta (307), katibu muhtasi (247) na ofisa uhusiano wa kampuni na umma (342).
Pia kuna nafasi ya dereva (408), wahariri (71), mwanasheria (140), mkutubi (80), msimamizi msaidizi wa kumbukumbu namba moja (230), msimamizi msaidizi wa kumbukumbu namba mbili (501) na ofisa masoko mwandamizi (167).

Malecela: Wakati utafika wasomi watabaki kwenye taaluma zao

Katika toleo la jana Waziri Mkuu mstaafu, John Malecela alizungumzia historia yake katika siasa na mchakato wa Katiba Mpya. Katika sehemu ya pili ya mahojiano na gazeti hili, anaeleza pamoja na mambo mengine, ubinafsishaji, ajira na ushiriki wa wasomi kwenye siasa.
Swali: Kuna taarifa kwamba uliwahi kuwekwa ndani kutokana na ushiriki wako katika harakati za ukombozi kupitia Tanu. Hili likoje?
Malecela: Sikuwekwa ndani kwasababu ya harakati za Tanu, hapana. Wakati narudi kutoka India baada ya kumaliza masomo yangu ya shahada ya kwanza, nilipita njia ya Mombasa, kutoka Mombasa nikaja Arusha. Arusha pale alikuwepo Nsilo Swai ambaye alikuwa mwalimu wangu Mazengo halafu India tukasoma wote, kwa hiyo alikuwa pale kama Katibu Mkuu wa Meru Cooperative Union. Nikaona nipite kwake nikae pale siku mbili, tatu hivi, kutoka Arusha nikaja Dodoma. Nilipofika tu nikaitwa kituo cha polisi. Nilipofika pale wakapekua mizigo yangu sasa wakanikuta na kitabu kimoja cha George Padimo ambacho kilikuwa kinaitwa Pan Africanism or Communism, wale wapekuzi kwa bahati mbaya hawakuwa Wazungu walikuwa ni weusi wenzangu.
Basi wakasema huyu mtu ana chembe-chembe za ukomunisti huyu ngoja tumweke ndani. Nililala mahabusu pale siku mbili aliyekuja kunitoa alikuwa ni Mzungu. Wakati huo wa Waingereza kila siku lazima mkuu wa polisi aende akaripoti kwa Mkuu wa Wilaya akieleza kwake ana watu wangapi mahabusu na makosa yao.
Sasa alipokwenda kuripoti kwamba kwenye mahabusu wana kijana ametoka India na wanafikiri kwamba ni mkomunisti, akawaambia kwamba mleteni. Mkuu wa Wilaya huyo alikuwa anaitwa Eyas, nikaenda ofisini kwake bahati yule Eyas alikuwa ni raia wa Ireland. Sasa nilipofika ofisini kwake akaagiza chai tukawa tunakunywa, akasema Waingereza hawa wabaya ndio maana sisi tunapigana nao we kijana angalia usifanye ovyoovyo.
Wakati huo ulikuwa mwaka 1959. Basi akanihubiria hapo, baada ya hapo akawaambia wale polisi ujinga huo, huyu hawezi kuwa mkomunisti, huyu ni Mgogo mwacheni arudi kwao. Na kweli yule Mkuu wa Wilaya alifurahi kuona kuwa mimi nimetoka kijijini huko akanipeleka mpaka nyumbani Mvumi kwa gari yake.
Swali: Hapa tulipo kuna tatizo kubwa la ajira na wengi wamelizungumzia, wewe unalizungumzia vipi?
Malecela: Kwanza nataka muelewe huku tulikotoka chama kilikuwa kinasema nini. Chama kilikuwa kinawakilisha siasa ya ujamaa na kujitegemea ndio maana katika miongozo mingi ya Tanu na baadaye Chama Cha Mapinduzi, ilikuwa kila siku inaomba watu wajiunge pamoja katika vikundi ili kuzalisha. Nitawapa ushahidi wakati nikiwa kwenye Baraza la Mawaziri.
Mara tu tulipopata uhuru Nsilo Swali alikuwa ndio Waziri wa Mipango wakalizungumzia hilo la ajira ya vijana Dar es Salaam. Wakasema si tunayo mashamba ya sukari Kilombero, basi wakachukua vijana pale zaidi ya 3,000 wakakaa nao, nakumbuka walisindikizwa na treni la kwenda Kidatu kuwapeleka vijana waende wakafanye kazi na walipewa mishahara kama ya miezi miwili na vifaa vyote vya kwenda kukata miwa. Hiyo yote ilikuwa ni nguvu za kuwapa vijana ajira.
Wakaenda kule miezi mitatu baadaye hakuna hata mmoja aliyebaki. Niwape ushuhuda wa karibuni wakati Mama Kunambi (Bernadetha, DC wa Dar es Salaam) aliwahi kuja na wazo lilelile, mimi nikamwambia wazo hili huko nyuma tulijaribu, lakini baada ya miezi mitatu wote wakawa wamerudi hapa. Kwanza tukapita kwenye mashamba ya mkonge tukatafuta vibarua, sio ya wasomi hapana, ni ya vijana kufanya kazi kwa mikono. Mama Kunambi akahesabu vijana wake 3,000, hizi rekodi sijui kama Ilala wanazo, tukahangaika, tukawapeleka hawa vijana kwamba waende wakafanye kazi huko na wao wakakubali.
Tukawapa mishahara miezi miwili kabla hata hawajafika huko. Baada ya miezi mitatu minne wote wakawa wamesharudi Dar es Salaam. Sijui kwa nini tukianza kusema ajira mimi nahisi mara nyingine sisi Watanzania tunaanza kujiona Serikali yetu haifanyi chochote, ndio maana tunakuwa na matatizo haya tunasahau hili ni tatizo la ulimwengu mzima.
Ni kweli wenzetu walioendelea tatizo hili linakuwa tofauti, kwa mfano Uingereza utakuta vijana wasiokuwa na ajira ni wengi, lakini kule mara nyingine ni kwa sababu ya kuchagua kazi ambayo ni sawa na huku ambako watu wanafikiri kuwa bado wanaweza kupata kazi ya kufagia ofisini na siyo kwenda kukata mkonge.
Kwa hiyo hili tatizo la vijana tunalo, lakini sisi kama Tanzania tunachotakiwa kufanya ni vitu viwili ambavyo kweli tuvifanye kwa juhudi kubwa kabisa maana yake ndio urithi ambao baba wa taifa ametuachia wa kukabiliana na matatizo yetu. Kama tunaweza kuboresha maisha ya vijijini kweli huwezi kupata wamachinga Dar es Salaam. Jamani kwa sababu ninyi ni watu wa habari naomba muende mkachunguze Dar es Salaam, muone hawa watu wa Lushoto, Wasambaa nenda kahesabu hawa watu kama utamkuta Msambaa Dar, hakuna, kwanini?
Mimi nimekwenda Lushoto unakuta kijana ana eka yake ya nyanya, anailima vizuri kweli kweli na kiutaalamu. Ukiilima eka moja vizuri, inakupa zaidi ya tani mia moja za nyanya na kule wanalima mara tatu kwa mwaka.
Kwa hiyo kule Lushoto hupati vijana wa kuja kuwa wamachinga, hapana.
Swali: Viwanda vingi vilibinafsishwa haiwezi kuwa sababu ya tatizo la ajira?
Malecela: Mimi sisemi kuwa viwanda vingi vimebinafsishwa ndio tatizo la ajira, hapana. Ninachosema kuna wakati katika miaka ya 1970 Tanzania ilikuwa na viwanda vingi vya nguo. Kiwanda cha Urafiki kilikuwa kimeajiri zaidi ya vijana 3,000, Ufi (Kiwanda cha zana za kilimo) kiliajiri watu 1,000 na Tanita (cha kubangua korosho) kiliajiri wafanyakazi 2,000.
Sasa vyote hivyo akaja mtu akutuambia ohhh kuendeshwa na Serikali haifai, hivi vinatakiwa viende binafsi. Tulivyosema hivyo viendeshwe na watu binafsi, Wahindi wakaja kwanza wakapandisha bei ya korosho. Korosho kilo moja Sh800.
Viwanda vyetu vikakosa korosho kwa hiyo vikasimama na hii imetokea juzi juzi hapa bei ya korosho imeanguka kutoka Sh800 kwa kilo hadi Sh120. Walipoona viwanda vimedorora havifanyi kazi na vyama vya ushirika vimekufa kwa sababu vilikuwa vikiendeshwa na hii biashara ya korosho, wakapunguza bei.
Nenda Morogoro yaani unajua vitu vingine tunasema tu, lakini mimi ambaye niliona viwanda vikifanya kazi leo napita Morogoro unaweza kuona ni mji unaokufa, lakini vilipokuwa vinafanya kazi pita pale saa 10:00 jioni unaona watu wanatoka kule kwenye viwanda sasa wanakuja mjini we mwenyewe unashangaa hivi hii ni Tanzania.
Kwa viwanda tukadanganywa ohh vitu vinavyoendeshwa na serikali haviendi, vibinafsishwe tukasahau kwamba vingine watu wale wanakuja na nia kabisa anakinunua kiwanda palepale anakifunga.
Nenda Mwanza mfano mzuri na huu ndio huwa unanisikitisha kweli kweli, ukiwa unakwenda uwanja wa ndege mkono wako wa kushoto utaona magofu makubwa, yale magofu yalikuwa majengo ya kiwanda kikubwa cha ngozi.
Akaja mtu akabinafsisha akachukua mitambo yote kauza Kenya sasa ukienda pale unalikuta jumba tu tupu.
Swali. Kwa hiyo kwa kifupi ubinasfisishaji haukuwa kitu kizuri?
Malecela: Kwanza binafsi nisingependa kuhukumu kuhusu ubinafsishaji. Mimi ninasema kila kitu mnapokifanya jamani mkifanye hatua kwa hatua. Siku za nyuma tulikuwa hatuna haja ya kuleta hizi juisi kutoka nje ya nchi, tulikuwa na kiwanda cha kutengeneza juisi ya machungwa lakini hata kilivyokufa sijui. Tulikuwa na kiwanda cha betri Matshushita. Unajua Matshushita kilivyokufa? Tajiri mmoja aliingiza betri za matshushita kutoka Indonesia akauza, Matshushita wakaja serikalini wakasema kama hivi tutafunga, wakafunga.
Barabara ya Pugu (Nyerere) ilikuwa mahali ambapo ikifika jioni watu wanatoka kazini unaangalia unajua kweli tuna viwanda, lakini vingi vimefungwa. Pale Dar es Salaam tulikuwa na viwanda vya nguo tulikuwa na Sungura Textile, tulikuwa na Tasini, tulikuwa na kama viwanda vinne vya kutengeneza nguo. Arusha General Tyre, tulikuwa na viwanda viwili vya nguo hiki A-Z kilifikia wakati hadi kinatengeneza nguo za ndani wakiziweka lebo ya mark Spencer, unatoka hapa unakwenda kununua vest Uingereza kumbe inatengenezwa Arusha.
Swali: Kuna wimbi sasa kila mtu anagombea ubunge, maprofesa, madaktari wanaacha kazi zao wanagombea ubunge. Unafikiri ni kwanini?
Malecela: Nadhani hasa kwa wasomi mimi nasema Mungu anisamehe kama ninawasingizia, wengi walifikiri nikiwa mbunge nitakuwa waziri. Kwa huko nyuma maprofesa wachache walipata uwaziri kweli. Walipoanza kuja kwa fujo na kwa wingi ikawa haiwezekani tena, halafu wengine hata ufanisi wao ulikuwa mdogo.
Swali; Pamoja na hapo kuna wimbi hili la watoto wa viongozi nalo linakuja kwa kasi!
Malecela; Mimi nataka kuwaambia kwa kweli hilo la kusema watoto wa wanasiasa mnawaonea. Unamkuta mzee yeye mfua vyuma, anatengeneza visu amekaa na mfuko wake. Mtoto anakaa pembeni anaona baba yake anapopuliza moto, anaona mpaka chuma kinavyokuwa chekundu. Anamwona baba yake anavyokwenda kukigongagonga hadi kinakuwa kisu, ama kama jembe na kadhalika.
Sasa mbona watoto wa walimu wakichukua ualimu hatusemi? Watoto wa madereva wakiwa madereva hatusemi, ila watoto wa viongozi wakiwa wanasiasa mnasema. Sisi tuna msemo kwamba; ukimwangalia ng’ombe mguu wa mbele utakapokanyaga na huu wa nyuma utakuja kukanyaga hapohapo.
Kwa hiyo hawa watoto wa wanasiasa bwana wakati mwingine wanaongozana na baba anapokwenda mahali, mara nyingine haendi kwa sababu anavutiwa na mkutano hapana, yeye anakwenda tu ili apande gari la baba. Kwa hiyo anakwenda pale baba anahutubia pale anaona, sasa watakuwa wajinga sana kama hawajifunzi. Kwa hiyo mimi nasema watoto wa viongozi tuwahukumu kwa utendaji wao.
Kweli kama mtu akianza kutumia jina la baba yake ohh mimi mtoto wa fulaniatashindwa.
Swali: Unatoa ushauri gani kwenye hili wimbi la wasomi maprofesa na madaktari kukimbilia kwenye siasa?
Malecela: Mimi sina ushauri wowote. Ni kama nguo, zilikuja watu wakaanza kulalamika jamani wasichana lakini baadaye ni mtindo ulipita. Hata hivi sasa wengi watakwenda kwenye siasa lakini muda ukifika watagundua kuwa kwenda kwenye siasa ni kupoteza muda.
Swali.Ukiwa Waziri Mkuu, ulikuwa ndio msimamizi wa shughuli zote za Bunge. Kuna kipindi Bunge lilikuwa moto na hasa wakati wa G 55 unaweza kulizungumzia hili?
Malecela: Siwezi kulizungumzia sana kwa sababu kipindi hicho kilipita. Ni kweli kulikuwa na kundi la G 55 ambao walikuwa wanataka Tanganyika. Katika Muungano Tanganyika nayo ionekane iwe Serikali ya Tanganyika ya Zanzibar halafu Muungano. Ilikwenda ilivyokwenda lakini mwisho ikaishia kwenye chama ambacho kilipeleka kwa wanachama basi mambo yakamalizika.
Swali: Ukiwa Waziri Mkuu changamoto uliyoipata unaizungumziaje?
Malecela: Changamoto huwezi kuizungumzia kwa sababu hizi ndizo zinazokujenga kwa wakati huo kwamba ukisikia jina Malecela unalinganisha na hiki na hiki; vizuri na vibaya.
Swali: Ukiwa Waziri Mkuu, uliwahi kujionyesha hadharani kuwa wewe ni mpenzi wa timu ya mpira ya Simba Sports Club, uliwahi kukacha safari yako moja kwa ajili ya kwenda kushuhudia Simba ikifanya vitu vyake uwanjani. Sijui kwa sasa hali yako ikoje kimichezo?
Malecela: Mechi zote ambazo nimewahi kuwa mgeni rasmi Simba inacheza, ilishinda. Ngojeni niwape historia kidogo, mimi wakati nikisoma Shule ya Sekondari Minaki, Dar es Salaam kulikuwa na timu tatu. Kulikuwa na timu ya Wazungu, timu ya Wahindi, Magoha na Waarabu na timu ya Waafrika.
Nendeni kwenye historia mchele walikuwa wanakula Wahindi, Wasomali na wengine Mwafrika ulikuwa huruhusiwi kununua mchele mpaka upate kibali. Sasa hata kama ukiwa mchezaji namna gani, timu ya wazungu ilikuwa ikiitwa Sunderland sasa hata uwe nani ilimradi wewe ni mweusi huwezi kuichezea timu hiyo.
Hii ya wahindi, magoha na waarabu ilikuwa ikiitwa Cosmo Club hata uwe nani huwezi kujiunga na kama sio wa jamii hizo.
Kwa watu weusi ilikuwa Yanga Africans, sasa wewe hata utake kucheza mpira wa namna gani lazima ukawe Yanga. Kwa hiyo hakukuwa na chaguo hivyo mtu ukiwa mpenzi wa mpira lazima tu uwe mwana Yanga.
Kwa hiyo wazungu walipoanza kuondoka ile Sunderland ikaanza kupungukiwa nguvu wakajitahidi kujiunga na Cosmo.
Nao walipoanza kuondoka na kuhama ndio baadaye wakaanza, jamani tuwachukue na wenzetu. Wakawachukua na waafrika na mwenyekiti wa kwanza na ndio akaleta na jina la Simba alikuwa Amon Nsekela. Karume alikuwa Yanga kwa sababu wakati ule hakuwa na chaguo.
Swali: Hadi sasa bado wewe ni shabiki wa Simba?
Malecela: Mimi napenda mpira mzuri tu. Kuna wakati nilikuwa nafikiri hii vita ya Yanga na Simba ilikuwa inadumaza mpira. Nilipokuwa Waziri wa Kilimo kwa kweli nilijitahidi nikaunda timu ikaenda kucheza na hizi timu kubwa zikaenda droo. Baada ya hapo wachezaji wangu wakachukuliwa mmoja mmoja na mtu wa kilimo akafanywa kuwa Mwenyekiti wa Yanga na timu yetu ya Kilimo ikafa.

Swali Kuna jambo ambalo ungependa lifahamike kwa wananchi?
Malecela: Ningependa wananchi wafahamu kwamba maendeleo ni hatua. Mimi nimekwenda Nigeria nimeendesha gari kutoka Abuja kwa barabara mpaka Port Harcourt jamani, umaskini niliouona kule ni wa kupindukia, huwezi kuulinganisha na wetu hata kidogo.
Mimi nilipokwenda kuripoti Tukuyu ilinichukua siku mbili kufika. Siku ya kwanza niliondoka Dodoma na basi nikalala Iringa. Kutoka pale kesho yake nikalala Mbeya ndio nikafika Tukuyu. Lakini sasa ukitoka Dodoma saa 12:00 asubuhi Mbeya saa tisa umeshafika.
Hapa ilikuwa safari ya hapa (Dodoma) hadi Iringa ilikuwa ni maili 240 ilikuwa ni ya kutwa nzima. Unaondoka hapa asubuhi na mabasi haya ya Urafiki unafika kule jioni, lakini sasa hivi unaondoka Iringa saa 12:00 asubuhi saa 4:00 asubuhi uko Dodoma.
Kinyago
Katika sebule ya Mzee Malecela mjini Dodoma ameweka kinyango kikubwa mfano wa mti ambao umebeba watu wakiwa wamebeba vitu mbalimbali.
Malecela anakizungumzia kinyago hicho kilimgharimu sh 300,000 wakati akiwa Waziri Mkuu miaka ya tisini na kilichongwa kwa muda wa miezi miwili.
Kama hiyo haitoshi anasema mchongaji wa kinyago hicho ambaye sasa ni marehemu alikuwa akiifanya kazi hiyo tu kwa kipindi cha miezi miwili ambapo ilimlazimu kumuwekea wafanyakazi kwa ajili ya kumfulia, kumpikia na kumfanyia vitu vingine ili atumie muda mwingi kuchonga kinyago hicho.
Anasema kinyago hicho kimetengenezwa kwa kutumia shina la mti aina ya mpingo na hata kuingia katika sebule yake ilimlazimu kuvunja moja ya dirisha kutokana na ukubwa wa kinyago hicho ambacho ilishindikana kupita mlangoni.
Twende kwenye elimu, nimekuwa Chancellor (Mkuu wa Chuo) wa Open University (Kikuu Huria) kwa miaka 20 tumekuwa na mikutano ya ‘machancellors’. Bado Tanzania tuna vyuo vikuu vingi kuliko jirani zetu Kenya, Uganda na sasa ukishakuwa kuliko Kenya na Uganda sembuse Rwanda na Burundi. Hata Zambia, hata Msumbiji hawajafika hivyo mimi nasema kuwa hili jambo la Watanzania kunung’unika kila siku kwamba hatuna hiki hatujafanya hivi, ni kana kwamba hatujafanya maendeleo nasikitika sana tunajitukana.
Wengine wanaosema hivyo hawajatoka waende wakaone na mahali pengine palivyo. Nenda Horohoro mpaka wa Tanzania na Kenya, ukija kwetu unaona watu, vijiji na nyumba za bati, palepale unapita mpaka unaenda Kenya, utaona tofauti.
Ukiangalia ukubwa wa nchi ukichukua Kenya na Uganda ukaziweka pamoja bado Tanzania ni kubwa kuliko nchi hizo kwa zaidi ya maili 6,000. Kwa hiyo wenzetu wakijenga barabara ya lami zaidi ya km 150 wameshafika kwenye mpaka wa nchi, lakini sisi kujenga barabara kutoka Dar es Salaam hadi Tunduma ni zaidi ya Km 1000.
Nafikiri kwa nyinyi watu wa habari ukianza kuzungumzia vitu vizuri ambavyo Serikali imefanya wataanza kutukana huyo amekuwa CCM number two au CCM B .
Swali.Sasa hivi tunaona vyuo vyote vinatoa shahada, hata vyuo vya kutoa vyeti au stashahada vinabadilishwa, unalizungumziaje hili?
Malecela: Na hilo ni kosa kubwa sana unapokuwa na mhandisi lazima huku chini uwe na watu wa kukuunga mkono, sasa hao ndio tulikuwa tunawatoa mafundi, Mbeya, Dar Technical ni kweli ulivyosema.
CBE sasa imekuwa chuo kikuu. Chuo cha Mipango kilijengwa kwa lengo la kusaidia maendeleo vijijini, malengo ya Mwalimu (Nyerere) kila kijiji kiwe na mtu ambaye anaweza akasaidia mipango ya maendeleo sasa ni chuo kikuu.
Mimi nilipokuwa India, nimeona mtu na shahada ya uzamili lakini ni kondakta wa daladala, kwa nini? Kwa sababu Chuo Kikuu cha Bombay kilikuwa kinapokea zaidi ya wanafunzi 60,000 kila mwaka.Ndio nakwambia sasa tuna viwanda vya kutengeneza mabomu.

JOTO 2015: Mrema asema yuko tayari kumkabili Mbatia

Moshi. Mbunge wa Vunjo, Augustino Mrema (TLP) amesema amejiandaa kuingia ‘vitani’ na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia ambaye ametangaza kuwania ubunge katika jimbo hilo, mwaka 2015.
“Siogopi mtu yeyote. Nimejiandaa vilivyo kwa mpambano huu. Najivunia rekodi yangu nzuri ya utendaji wala sitishiki na wananchi wangu nimewauliza wameniambia nisihofu,” alisema Mrema.
Kwa mujibu wa Mrema, anaamini rekodi yake nzuri ya utendaji ndiyo itakayomuuza mwaka 2015 na kwamba, ni rekodi hiyo nzuri ndiyo iliyowafanya wananchi wa jimbo hilo wakamchagua mwaka 2010.
“Umesahau nilikuwa mbunge wa Moshi Vijijini wakati huo ikiwa ni pamoja na Vunjo? Rekodi yangu nilipokuwa naibu waziri mkuu inajieleza. Yeye (Mbatia) aje nimejiandaa kwa mpambano,” alisema.
Juzi, Mbatia ambaye pia ni mbunge wa kuteuliwa, alisema kwa sasa ameelemewa na maombi ya makundi mbalimbali ya jamii yakimtaka agombee ubunge katika jimbo hilo mwakani.
“Nimefuatwa mara kadhaa na viongozi wa dini wakiniomba nigombee tena 2015. Wapo wananchi wamenifuata hadi bungeni. Simu yangu imejaa meseji nyingi za kuniomba,” alisema Mbatia.
Mbatia ambaye pia ni mwenyekiti mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), aliwahi pia kuwa mbunge wa kwanza wa jimbo hilo chini ya mfumo wa vyama vingi mwaka 1995 hadi mwaka 2000.
“Hayo maombi ya wananchi siwezi kusema nawakatalia, mimi ni nani nikatae kuwatumikia Watanzania wenzangu? Niko tayari kuwatumikia ila wajue kwa sasa kuna mbunge,” alisema.
Mbatia aliongeza, “Natarajia kwenda Vunjo wakati wowote kuanzia leo ili nitoe jibu rasmi mbele ya Wanavunjo. Nashukuru kwa heshima hii waliyonipa. Naahidi sitawaangusha.”
Wiki iliyopita, baadhi ya wananchi waliodai kuwawakilisha wenzao kutoka kata zote za jimbo hilo, walitoa tamko lililosomwa na Mathew Temu wakimtaka Mbatia agombee ubunge kupitia vyama vya NCCR, Chadema na CUF vinavyounda Ukawa. Katika tamko hilo, wananchi hao walisema rekodi ya Mbatia alipokuwa mbunge haijawahi kuvunjwa.

Uongozi mbaya wa shule chanzo cha ugonjwa wa watoto kupagawa

Mara nyingi tumekuwa tukishuhudia wasichana wengi hasa wakiwa shuleni wakipata matatizo ya kuweweseka, kupiga kelele na kuchanganyikiwa kiasi cha kushindwa kuendelea na masomo.
Ingawa watu wa jinsia zote, wakubwa kwa wadogo wanaweza kupata tatizo hili, wanaoathirika zaidi ni wanawake hasa wasichana wa umri kati ya miaka 12 na18.
Matukio ya wanafunzi kupagawa, kuweweseka na kupiga kelele yametokea jijini Dar es Salaam katika shule kadhaa za msingi. Agosti 2005, wanafunzi 24 wa Shule ya Msingi ya Uwanja wa Ndege walipata tatizo hilo na Novemba 2006, wanafunzi 15 wa darasa la tano katika Shule ya Msingi ya Mbuyuni.
Matukio kama yayo yametokea katika mikoa mingine kama tukio la Machi 2007 kwenye Shule ya Msingi ya Lewa wilayani Korogwe, Tanga, Mei  2008 lilipotokea kwa wanafunzi 50 na mwalimu wao mkoani Dodoma na wanafunzi 30 wa Shule ya Msingi ya Mang’ula mkoani Morogoro mwaka 2009.
Hali hii imekuwa ikipokewa kwa hisia tofauti na watu mbalimbali katika jamii. Wengine huihusisha na imani za kishirikina, kupagawa na pepo au kudhuriwa na mizimu.
Ingawa jamii ina maoni tofauti kuhusu tatizo hili, wanasayansi wanaamini kuwa hali hii inatokana na matatizo ya afya ya akili yanayojulikana kama hysteria.
Kihistoria ugonjwa huu ulianza zamani hata kabla ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Jina la ugonjwa huu lilitokana na mawazo ya madaktari wa zamani wa Kigiriki waliokuwa wanafikiria kwamba chanzo cha ugonjwa huu ni matatizo katika mfuko au mji wa mimba wa mwanamke, ambao kwa Kigiriki unaitwa hystera.
Madaktari wa Kigiriki walidhani kuwa huu ni ugonjwa unaowapata wanawake pekee. Hii ilitokana na idadi kubwa ya wagonjwa wa tatizo hili kuwa wanawake, na hata pale wanaume walipokuwa na dalili za tatizo la hysteria ilidhaniwa kuwa wana tatizo jingine kwa vile hawakuwa na mfuko au mji wa mimba.
Dhana ya madaktari wa kipindi hicho juu ya ugonjwa huu ilikuwa kwamba mfuko wa kizazi (mji wa mimba) unabana na kukauka kutokana na kutokufanya ngono kwa muda mrefu au kuzidiwa na hamu ya ngono.  Matibabu ya enzi hizo yalihusisha kumtekenya mwanamke katika sehemu zake za siri ili apate kumaliza hamu ya ngono, lakini matibabu hayo yalikuwa hayatoi matokeo ya uponaji yaliyotarajiwa.
Hata hivyo, sayansi ya tiba ya binadamu imethibitisha kuwa hysteria ni ugonjwa wa akili unaotokana na msongo mkali wa mawazo na hisia.
Linaonekana ni tatizo zaidi la afya ya akili na kisaikolojia.
Tatizo hili hutokea pale mtu anapopata msongo wa kihisia maishani zaidi ya vile alivyojiandaa au anavyoweza kukabiliana nao. Mara nyingi msongo huu hutokana na hisia au mgogoro wa fikra, kutokuwa na uhakika wa usalama katika siku za usoni, kutengwa na jamii au kutosikilizwa kwa upendo. Tamaa kali ya kutaka kupendwa kuliko kawaida isipotimizwa, pia huleta tatizo hili.
Wakati mwingine hisia na fikra hutokana na matatizo ya kawaida, lakini akili huyakuza sana na mhusika akajiona hawezi kuyakabili, hafai na hathaminiwi.
Mgonjwa anaweza kujilaumu na kupata hisia za kupoteza ulinzi au kupata kumbukumbu isiyonyamazishwa ya tukio la kinyama alilotendewa kama vile kubakwa, kunyanyaswa au ukatili  wa kijinsia.
Watu wanaopata ugonjwa wa hysteria huwa na matatizo ya kihisia ambayo mara nyingi hawapendi kuyazungumzia na kwa sababu hiyo, matatizo hayo huwaelemea sana.
Katika utafiti uliofanywa na Altamura AC na wenzake nchini Malawi, iligundulika kuwa wanawake wengi, hasa wasichana hupata msongo mkali sana wa mawazo, kujilaumu na kushuka sana moyo pale wasiporidhishwa na hali ya maisha waliyo nayo. 
Mwanasaikolojia Mareesa Dannielle wa New Zealand, katika utafiti wake mwaka 2007, alibaini kuwa uongozi mbaya wa watu unaweza kuchangia kwa namna moja ama nyingine kutokea kwa tatizo hilo.
Kaimu mganga mkuu wa Wilaya ya Ulanga,  Eddy Mjungu anasema: “Hii inaweza kuwa watoto kutolelewa vizuri, uhusiano wao na wazazi, walimu na hata migogoro ya kimapenzi.”
Ugonjwa huu unaweza kumpata mtu mmoja pekee lakini pia unaweza kusambaa kwa wengine katika kundi la watu wanaokabiliwa na msongo wa kisaikolojia unaofanana na wanaokaa au kufanya kazi katika mazingira yanayofanana.
Hysteria inayosambaa huanza na mtu mmoja na anapoonyesha dalili, wengine nao huanza kujenga hofu na hisia za kuathirika baada ya kumwona mwenzao.
Mara nyingi dalili za hysteria inayosambaa hazionyeshi chanzo bayana na hazitafasiriki sawasawa lakini zinaenea kwa haraka miongoni mwa walioona mgonjwa wa kwanza aliyepata tatizo.
Hofu huongezeka zaidi na tatizo husambaa zaidi pale linapoanza kuhusishwa na imani za kishirikina, mambo ya kimizimu na kupagawa na majini au pepo wabaya.
Hofu huzidi pale timu ya wataalamu wa uchunguzi wa vyanzo vya magonjwa wanaposhindwa kubaini chanzo bayana cha tatizo.
Hysteria ingawa ni tatizo la  afya ya akili, pia hudhuru afya ya mwili kwa kiwango kikubwa. Hofu, woga na wasiwasi husababisha mapigo ya moyo wa mgonjwa kwenda haraka, kutapika, kupata kichefuchefu, mwili kuishiwa nguvu na maumivu ya kichwa.
Matatizo mengine ni pamoja na miguu kufa ganzi, kushindwa kutembea, kupiga kelele au kucheka sana bila sababu za msingi na  kupata degedege.
Wagonjwa wengine hupoteza hamu ya chakula, kutokupata choo kabisa au kuharisha na wengine hutokwa jasho jingi, kutetemeka, kupumua kwa shida au kushindwa kupumua vizuri kiasi kwamba hewa chafu ya ukaa haitolewi mwilini kwa kiwango cha kutosha.

Ukawa, CCM kucheza kete ya mwisho leo

Ni katika kikao cha maridhiano chini ya Msajili wa Vyama vya Siasa
Dar es Salaam. Kete ya mwisho ya kuamua iwapo wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) watarejea katika Bunge la Katiba au la itachezwa leo katika kikao cha maridhiano baina ya umoja huo na CCM, chini ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi.
Kikao hicho kinafanyika siku nne kabla Bunge hilo kuendelea na vikao vyake Jumanne ijayo licha ya msimamo wa Ukawa wa kuendelea kuvisusia.
Kikao hicho kinachovikutanisha vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na CCM ni cha mwisho baada ya kile cha kwanza kilichofanyika wiki moja iliyopita kumalizika bila mwafaka wowote.
Akizungumza na waandishi wa habari jana akiwa na wenyeviti wenzake, James Mbatia (NCCR-Mageuzi) na Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema hadi jana msimamo wao ni kutohudhuria vikao vya Bunge hilo labda ikitokea miujiza katika kikao cha leo.
Mbowe alisema ni miujiza kwa sababu kwa madai ya Ukawa, ni lazima mjadala huo ujikite kwenye Rasimu ya Katiba, ambayo imebeba mapendekezo ya wananchi na kutaka wajumbe wenzao, hasa kutoka CCM, kuacha kujenga hoja kwa kutumia kejeli, matusi na mizaha ambayo si rahisi wenzao kuyakubali.
Moja ya ajenda ya kikao hicho ambacho leo kitakuwa na wajumbe 20 kutoka kila chama, ni kuwashawishi Ukawa kurejea bungeni ili kuendelea na mchakato wa Katiba Mpya.
Ukawa walisusia vikao vya Bunge la Katiba hilo Aprili 16 wakipinga kubadilishwa Rasimu ya Katiba na wajumbe wa CCM kwa maelezo kuwa ni kinyume na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Mbowe alisema ni jambo la kushangaza kuona Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Samuel Sitta wakitoa kauli za kuwashutumu Ukawa wakati wakijua wazi kuwa kuna mazungumzo kati ya vyama vya siasa na Jaji Mutungi vinaendelea.
Juzi pia, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), liliisihi Ukawa kurudi bungeni ili kukamilisha mchakato wa kupata Katiba Mpya, lakini likasema mjadala huo uzingatie Rasimu ya Katiba.
“Hata viongozi wa dini nao wametoa matamko wakitaka Ukawa turejee bungeni, tunashukuru maoni yao. Ila wanatakiwa kujua sababu zilizotufanya mpaka tukasusia. Wanatakiwa kuwaonya CCM wanaokwenda kinyume na mchakato huo,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Wakati tupo katika mazungumzo, Sitta anaanzisha kikao chake na kutoa tamko kuwa Bunge litaendelea wakati akijua Ukawa wapo katika kikao pamoja na viongozi wa chama chake cha CCM. Kauli hizi zinazokosa umoja zinaonyesha Serikali na timu nzima haiko tayari kutafuta mwafaka wa suala hili.”
Profesa Lipumba
Akieleza sababu nyingine za Ukawa kususia vikao vya Bunge la Katiba, Profesa Lipumba aliwataka viongozi wa dini kutambua kuwa CCM ndiyo chanzo cha mchakato huo kuingia dosari, kwamba wanatakiwa kukionya chama hicho kiheshimu maoni ya wananchi.
“Tuliondoka bungeni kwa sababu Sitta alishindwa kuwadhibiti wajumbe wa Bunge la Katiba waliokuwa wakizungumza lugha za matusi, kejeli, uchochezi na ubaguzi, alivunja kanuni za Bunge kwa kuruhusu Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba kuwasilisha Rasimu ya Katiba bungeni kabla ya Bunge kusikiliza hotuba ya ufunguzi ya Rais Jakaya Kikwete.”
Alitaja sababu nyingine kuwa ni kauli ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kueleza kanisani kuwa nchi itaingia vitani iwapo muundo wa serikali tatu utapita, kwamba Zanzibar inataka serikali tatu ili kurejesha Waarabu visiwani humo.
“Lukuvi aliyasema hayo kanisani akimwakilisha Waziri Mkuu Pinda. Licha ya kutoa maneno ya uchochezi hakuna mamlaka iliyo juu ya Lukuvi iliyoomba radhi kwa kauli yake,” alisema.
Mbatia
Mbatia alisema rasimu inayotakiwa kujadiliwa ni ile iliyopendekezwa na Tume ya Warioba yenye muundo wa Serikali tatu.
“Hata kuhusu Tunu za Taifa zilizotajwa katika rasimu; yaani utu, uzalendo, uadilifu, uwazi, umoja, uwajibikaji na lugha ya taifa wenzetu wa CCM wameyakataa. Sasa sijui wanataka kulipeleka wapi hili taifa. Tutaendeleaje kujadili?” alihoji.
Hofu ya wajumbe
Katika hatua nyingine, baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo wamesema kutorejea bungeni kwa Ukawa kutaathiri upatikanaji wa Katiba Mpya yenye maridhiano.
Mmoja wa wajumbe hao, Charles Mwijage alipendekeza kusitishwa kwa mchakato huo kwa kuwa maridhiano ni jambo muhimu katika kutengeneza Katiba.
“Kukosekana kwa Ukawa bungeni kutaathiri upatikanaji wa Katiba Mpya kwa sababu suala hili linahitaji zaidi maridhiano ya pande zinazotofautiana kiitikadi,” alisema Mwijage ambaye pia ni Mbunge wa Muleba Kaskazini (CCM).
“Ningekuwa na uwezo, ningeamua mchakato huu wa  Katiba usitishwe na tuendelee kutumia Katiba iliyopo kwa sababu suala hili linahitaji zaidi maridhiano,” alisema.
Mbunge huyo alisema, “Ukawa wanataka kujenga mazingira ya kuja kuikataa Katiba itakayopatikana ili watusababishie vurugu na mapigano.”
Alisema Rais aliona kwamba kundi la wajumbe 629 likikaa pamoja linaweza kutengeneza Katiba Mpya kwa maridhiano, lakini kama kuna kundi linajitoa ni wazi kwamba kutakuwa na dosari katika utengenezaji.
Mjumbe mwingine, Ezekiah Oluoch alisema iwapo wajumbe wa CUF kutoka Zanzibar ambao wanaunda Ukawa hawatarejea bungeni, Katiba Mpya haiwezi kupatikana kwa sababu theluthi mbili haziwezi kupatikana.
“Katiba haipatikani kwa ubabe au wengi-wape, bali inapatikana kwa maridhiano na mwafaka bila kujali idadi ya wingi wa wajumbe,” alisema Oluoch ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT).
Alisema Bunge hilo litatumia fedha nyingi za walipa kodi bila kupata Katiba Mpya, hivyo akashauri mchakato huo usogezwe mbele hadi baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Mbunge wa Mbeya Vijijini (CCM), Lackson Mwanjali alisema kitendo cha Ukawa kukataa kurejea bungeni ni pigo katika mchakato wa Katiba Mpya kwa sababu inatengenezwa kwa majadiliano na kufikia mwafaka.
“Tunapokuwa bungeni watu kutoka vyama na itikadi tofauti tunajadiliana, tunabishana na baadaye kufikia mwafaka na kufanya maridhiano, sasa wenzetu hawapo ni tatizo kubwa,” alisema.
Mwanjale alisema ingawa wanakwenda kwenye Bunge Maalumu la Katiba itakuwa vigumu kupata Katiba bora.
Hata hivyo, Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Diana Chilolo alisema wangependa Ukawa warejee bungeni lakini kama hawaendi watawakilishwa na wenzao.
“Wapo watu kutoka katika vyama vya upinzani pale ambao watawawakilisha. Yupo Mbunge wa Vunjo (TLP), Augustine Mrema na Mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), John Cheyo watawawakilisha na tutapata Katiba bora,” alisema Chilolo.
Mbunge wa Sikonge (CCM), Saidi Mkumba alisema Katiba inayotafutwa ni ya Watanzania wote hivyo kundi la Ukawa kukataa kurudi bungeni hakuwezi kusimamisha mchakato huo.
Mambo sita ya kuzingatia
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Khoti Kamanga amebainisha mambo sita yanayotakiwa kufanyiwa kazi kabla ya Bunge hilo kuanza vikao vyake Agosti 5.
Akizungumza katika kilele cha Siku ya Wanawake Afrika iliyoandaliwa na Shirika la Wanawake Katika Sheria na Maendeleo Barani Afrika (WilDAF), Dk Kamanga alisema:
“Mosi, huu utaratibu wa wengi-wape ni mzuri lakini tusiung’ang’anie ingawa demokrasia inaruhusu na kinachotakiwa ni kuweka mbele masilahi ya taifa.”
“Kuna wachache wanakuwa na hoja za kutosha lakini kutokana na uchache wao demokrasia inawatupa. Katika suala la Katiba maridhiano ni jambo la muhimu na suala la wengi-wape liwekwe kando.”
Pili, alisema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inatakiwa kufanyiwa marekebisho hasa Kifungu cha 36 (5) kilichobainisha kuwa endapo mwafaka hautapatikana Katiba ya mwaka 1977 itaendelea kutumika.
“Unapoanza safari huwezi kushindwa na ukarudi nyuma, kwa kuwa kila mmoja amekiri kwamba Katiba ya sasa ina viraka 14 ambavyo ni vingi sana,” alisema.
Jambo la tatu, Dk Kamanga alisema kunahitajika ujasiri katika kubaini na kukubali ni wapi mchakato wa Katiba ulipojikwaa. Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inatakiwa kuheshimiwa na si kukiukwa.
Jambo la nne ni kuwa, Bunge linatakiwa kujadili rasimu na kutokwenda kinyume na sheria ilivyo kama ilivyoandaliwa na Tume ya Katiba  kwa mujibu wa sheria.
“Rasimu iliyopo ya Desemba 2013 iliandaliwa na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba iliyounda Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokusanya maoni ya wananchi, hivyo sheria haitakiwi kuvunjwa, pia Bunge linatakiwa kuizingatia,” alisema.
“Tano, tunatakiwa kusoma rasimu ili unapochangia au kuona mtu akichangia uwe unajua anachokisema na jambo la mwisho ni ngumu kwa vyama kuweka kando masilahi yao lakini kwa jambo hili wanatakiwa kutanguliza mbele masilahi ya taifa,” alisema Dk Kamanga.