Dar es Salaam. Wakati Ramadhani Gembe (pichani)
anafanya mtihani wa Taifa wa kidato cha sita miezi miwili iliyopita,
hakuwahi kufikiri angeshika namba moja kwa ufaulu kitaifa licha ya
jitihada zake za kujituma.
Lakini siku zote Mungu hamtupi mja wake. Kama jina
lake linavyosadifu mwezi mtukufu unaomalizika siku mbili zijazo,
Ramadhani ambaye amehitimu Shule ya Wavulana ya Feza jijini Dar es
Salaam, ameibuka mwanafunzi bora nchini kati ya waliofanya mtihani huo
wa kujiandaa kwa masomo ya elimu ya juu.
“Nilitegemea ningefaulu lakini siyo kwa kiwango
hicho… hii ni ‘surprise’ (shtukizo),” alisema Gembe alipohojiwa na
Mwananchi baada ya matokeo ya kidato cha sita kutangazwa na Baraza la
Mitihani la Taifa.
“Nawashukuru wazazi, walimu, ndugu na wanafunzi
wenzangu kwa kunipa ushirikiano. Nilikuwa nafanya sana ibada hivyo haya
matokeo ni juhudi binafsi na majibu ya Mungu,” alisema Ramadhani
aliyesoma mchepuo wa fizikia, kemia na baiolojia (PCB).
Historia ya Ramadhani darasani si haba kwani mwaka
2008 alikuwa ni mwanafunzi pekee aliyejiunga na shule ya vipaji maalumu
ya Ilboru, Arusha akitokea shule ya Msingi Mombo na alipata daraja la
kwanza akiwa na pointi 11 katika matokeo ya kidato cha nne.
“Siku zote kilichonifanya niongeze juhudi katika
masomo yangu ni malengo ya baadaye... mimi nataka kuwa daktari wa
binadamu hivyo sikutaka kulegalega kusoma. Pia, wazazi wangu pamoja na
hali ngumu walijitahidi kunisaidia kimawazo, kirasilimali na
kimaadili…naomba na wazazi wengine wawafanyie hivyo watoto wao,”
alisema.
Baba azungumza
Nurdin Gembe, ambaye ni mzazi wa Ramadhani,
alisema familia imepokea kwa furaha matokeo hayo na kwamba alikuwa
akiyategemea kuwa mazuri kutokana historia ya kijana wake katika
madarasa ya nyuma.
“Huyu mtoto namlea kawaida japo zamani alikuwa
mtundu sana… ilibidi nimpe mafundisho mengi sana ya kidini bila kupoteza
ratiba ya kusoma shuleni. Nashukuru kuwa alizingatia na amefika hapo
alipofika,” alieleza Gembe ambaye ni bwana shamba kitaaluma.
Mwanafunzi wa tisa
Kwa upande wake Yonazi Senkondo, aliyeshika nafasi
ya tisa kitaifa, alisema matokeo hayo ni majibu ya maombi kwa Mungu na
juhudi zake kusoma na ushirika na wanafunzi wenzie.
“Siku zote nilikuwa naombea niingie 10 bora, najua
leo Mungu amejibu maombi yangu. Nilikuwa nafanya mijadala na wanafunzi
wenzangu hasa huyo aliyeshika namba moja. Sishangai yeye kuwa katika
ngazi hiyo.
“Siku zote naamini maombi na nidhamu ndiyo msingi wa yote kwa
sababu unaweza kukesha unasoma, lakini matokeo yakaja tofauti,” alisema
Yonazi aliyekuwa akisoma fizikia, kemia na bailojia (PCB) katika Shule
ya Sekondari ya Wavulana ya Feza, jijini Dar es Salaam.
Mama yake, Jeanette Senkondo alisema matokeo ya
kuingia 10 bora ni kama shtukizo kwa kuwa alikuwa anajua mwanaye ana
uwezo wa kufaulu ila siyo kwa kiwango hicho na kwamba ni mafanikio ya
sala, juhudi na mipango, ushirikiano, nidhamu na malezi bora ya
mwanafunzi.
“Tangu chekechea alikuwa na juhudi za masomo na
siku zote akipanga kitu lazima akitimizie… pia huwa anasali na kufunga
hata mimi wakati wa majuma mawili ya mtihani nilifunga kumuombea. Bila
shaka Mungu amejibu maombi,” alisema Senkondo ambaye ni mhadhili wa Chuo
Kikuu cha Kumbukumbu ya Hurbert Kairuki.
Mkuu wa Feza alonga
Makamu Mkuu wa Shule ya Wavulana ya Feza, Ali
Nungo alisema kitendo cha kuingiza wanafunzi 10 bora ni changamoto
wanayotakiwa kuliendeleza siku zote kwani hawajawahi kufanya kwa kiasi
hicho.
“Vijana hawajatuangusha, tulitegema watafanya
vizuri ila siyo kiwango hicho. Sisi kama walimu na uongozi wa shule
tumefanya tuwezalo kuwawezesha kwa kuwafundisha na kuwapa ushirikiano
lakini lazima wazazi watambue kumleta mtoto tu Feza si kwamba anakuwa
bora, lazima kuwe na ushirikiano mzuri baina ya pande zote,” alisema.
No comments:
Post a Comment