Friday 27 December 2013

Viatu hatari kwa afya ya miguu ya wanawake

‘Mchuchumio’ ama viatu vyenye visigino virefu, ni mojawapo ya vitu vinavyopendwa na baadhi ya wanawake mbalimbali, si katika Tanzania bali dunia nzima.
Wataalamu wanaeleza kuwa viatu hivi huharibu pingili za uti wa mgongo na huvunjavunja mifupa ya visigino.
Wanawake wenye maumbo ya kati, ambao si wanene wala wembamba wamekuwa wakipendelea viatu virefu.
Kwa kiasi kikubwa wasichana wafupi, wamekuwa wakipendelea kuvaa viatu virefu ili angalau na wao waonekane warefu.
Ashura Mgweno, mfanyakazi wa Kampuni ya Usafi jijini Dar es Salaam, anasema: “Nimetumia viatu kwa muda mrefu, lakini sasa sitaki kusikia viatu virefu. Mimi ni mfupi, nilikuwa navaa sana, lakini sasa sitaki hata kuviona jinsi vilivyonitesa,” anasema.
Anasema kuwa viatu virefu muda wake ni miaka mitatu, inaharibu visigino na misuli ya miguu na kutengeneza vigimbi ambavyo baadaye husababisha maumivu makali.
Akizungumzia hili, Ruth Erasto ambaye anafanya kazi katika ofisi moja jijini Dar es Salaam, anasema aliacha kuvaa ‘mchuchumio’ kwa maagizo ya daktari.
“Niligawa viatu vyangu vyote virefu baada ya kupatwa na maumivu ya mgongo. Viatu virefu havilinganishi mwili wakati wa kutembea na niliagizwa na daktari kuachana na viatu virefu...hiyo ilitokana na mimi kuanza kupatwa na matatizo ya mgongo,” anasema.
Anasema kuwa alipatwa na matatizo hayo bila kufahamu, lakini baada ya kuchunguzwa, ndipo ikabainika kupatwa na matatizo hayo.
Mwanamama mwingine aliyepatwa na matatizo hayo, Victoria, anasema kuwa inamlazimu kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kila mara kwa ajili ya kuangaliwa maendeleo ya mgongo baada ya kuvaa viatu virefu kwa muda mrefu na kumletea athari hizo.
Victoria ambaye ni mfupi na mnene kiasi kwa umbile, anasema kuwa pamoja na kupenda kuvaa viatu hivyo, hataki kusikia habari zake.
“Nakuambia sina hamu na viatu hivi, acha kabisa, nimekoma...nimekwenda Muhimbili hadi nimechoka, maumivu kuanzia kiuno hadi mgongo,” anasema. 
Jozi mbili
Hakika, wapo wanawake wanaofahamu madhara ya kuvaa viatu hivyo, lakini wengine wanafahamu, lakini wanapuuza. Baadhi ya wanaopuuza ni kutaka kuonekana wa kisasa zaidi, licha ya kuwa wanahisi maumivu makali wanapovaa.
Mara kwa mara, wengi wa wanawake hulazimika kubeba viatu jozi zaidi ya moja, vile vya chini (flat shoes) kwa ajili ya kubadilisha pindi mambo yanapokuwa magumu.
Christina Mdete, Mkazi wa Yombo Buza, Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam anasema amekuwa akibeba jozi mbili za viatu anapotoka nyumbani na kuvaa viatu virefu anapoingia ofisini. “Hata ninapokuwa ofisini, navua kisha navaa ‘flat’...ah! siwezi wewe, kutwa nzima, vinaumiza halafu hauko na raha ukivaa muda wote.
Anasema hata wanaokwenda kwenye sherehe, hutumia muda mfupi kuvaa, kwani ni pale wanapokwenda kutoa zawadi na baada ya hapo, vinavuliwa na kuvaliwa viatu vya chini.
Wasichana wengi wanafahamu ‘mchuchumio’ husababisha maumivu makali lakini je, ndiyo kutimiza usemi wa ukitaka uzuri shurti udhurike? Kwa kawaida, urembo hauwezi kusababisha maumivu, lakini kuvaa viatu virefu kuna athari kubwa.
Utafiti mbalimbali wa hivi karibuni unaonyesha kuwa viatu virefu havifai hata kidogo. Kimsingi, uvaaji wa viatu virefu husababisha maumivu makali ya misuli ya miguu pamoja na nyama za nyuma kwenye maungio ya magoti na enka.
Uharibifu ni mkubwa pia huweza kutokea ndani ya magoti kwa kuhamisha maungio (dislocate). Kwa jinsi mhusika anapovaa viatu virefu kwa muda mrefu, ndipo inaposababisha madhara ya muda mrefu.
Mbali na hayo, vilevile, husababisha mwili kukosa usawa wakati wa kutembea, misuli ya miguu kubana, kupoteza mwelekeo wa mwendo halisi na wakati mwingine husababisha mhusika kuanguka na kumsababishia maumivu makali.
Madaktari wanashauri kuvaa viatu virefu kuwe kwa muda maalumu kwa shughuli maalumu na visizidi urefu wa inchi mbili.
Kama mtu alizoea kuvaa viatu virefu kwa muda mrefu, inashauriwa kuacha taratibu badala ya kubadilika haraka kwenda kwenye viatu. Kama viatu virefu vitavaliwa kazini, ni vizuri kuwepo na viatu vingine vya kubadilisha.
Utafiti mwingine unaonyesha kuwa viatu virefu husababisha maumivu makali ya dole gumba la mguu, kuzuia ukuaji wa kucha na matatizo mengine. Watafiti hao wa Chuo Kikuu cha Griffith kwenye mji wa Queensland, Australia wakiongozwa na Dk Neil Cronin, katika utafiti wao, waliliambia gazeti la New York Times kwamba wanaendelea kufanya utafiti kuona madhara zaidi yanayoweza kupatika.
Katika uchunguzi uliochapishwa kwenye jarida la Journal of Applied Physiology, Dk Cronin anasema wanawake wengi waliofanyiwa utafiti wamebainika kutokuwa imara katika miguu yao, kupatwa na maumivu makali na kuharibiwa misuli na enka ya mguu.
Naye Dk Orly Avitzur, Mganga Mshauri kwenye kitongoji cha Tarrytown, New York, Marekani anasema kuwa alifanya utafiti kwa wanawake wa zaidi ya miaka 40 kuwa hawawezi kuvaa viatu virefu kwa kuwa miguu yao tayari imeharibiwa.
“Kama ni miaka 20 sawa, ni kitu kingine,” Avitzur anasema. “Kama ikiwa ni zaidi ya miaka 40 ni tatizo na itakuwa suala lingine mtu akivaa viatu hivyo, lakini chini ya hapo haina shida sana.”
Mtaalamu wa Mifupa katika Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam, Dk Edemeza Machange anasema kuwa matatizo ni makubwa kwa mtumiaji wa viatu virefu na athari zaidi huwakumba wanawake wanene.
“Ni mbaya sana...kwa wanawake wanene haishauriwi watumie viatu virefu kwa kuwa vitawaletea matatizo mengi katika miili yao,” anasema.
Kama walivyosema wataalamu waliotangulia, Machange anasema kuwa kubwa linaloumiza wanawake wengi ni kuvaa viatu virefu kwa kipindi kirefu na matokeo yake ni kuumwa mgongo kwani uharibu mpangilio wa pingili za uti wa mgongo.
“Kwa kawaida mtu anapoteza mwendo halisi, sasa kutotembea kwa mpangilio, huharibu mfumo wa pingili za mgongo, hata kiuno na kusababisha maumivu makali...tumekataza wengi kuvaa viatu virefu baada ya kupatwa na matatizo ya mgongo.”
Anawashauri kinamama hasa wasichana, wafahamu kuwa pamoja na kutaka urembo, lazima wajali afya zao kwa kuvaa viatu virefu katika kipindi kifupi na zaidi ni kuangalia madhara kwa baadaye kuliko kukimbilia kuvaa viatu virefu kwa ajili ya urembo.

Makamba ajipigia debe la urais kiaina

Mwanza. Katika kile kinachoonekana kama kujipigia debe katika kinyang’anyiro cha urais katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba amewaambia viongozi wa dini Kanda ya Ziwa kwamba vijana wanapofika kuomba ridhaa yao, muwaangalie, msiwabeze.
Huku akikataa kuweka bayana nia yake ya kuwania urais kwa maelezo kwamba muda wa kufanya hivyo haujawadia, Makamba aliwaambia viongozi hao wa dini kwamba wagombea hao wanapopita wawasomee sifa za uongozi katika Biblia na kusema kumekuwapo mjadala wa sifa za uongozi kuhusu kijana na kusema amekuwa akitoa mwito kwa vijana wasiokuwa na makandokando kushiriki na kujitokeza katika kusaidia nchi ipone.
Akizungumza juzi usiku mjini hapa katika chakula cha pamoja na maaskofu na wachungaji kutoka Umoja wa Makanisa ya Kikristo wa Mikoa ya Kanda ya Ziwa, Makamba ambaye pia ni mbunge wa Bumbuli (CCM), alisema: “Huu ni wakati wa kila mmoja kutafakari hatima ya nchi yetu. Ndugu zangu… nadhani tuzungumze machache yanayohusu nchi yetu na Taifa letu, kwa sababu sote ni Watanzania na wote tuna hamu ya kujua na kutafakari mustakabali wa nchi yetu, umoja wetu, amani yetu na utulivu wetu.”
Alisema vijana wengi wamekuwa waoga kwa madai kwamba hawana fedha, uzoefu lakini akasema maaskofu na wachungaji wanapaswa kuwa mashahidi kupitia vitabu kwani katika Yeremia imeelezwa jinsi Mungu alivyompatia unabii Yeremia ambaye alidai yeye bado mdogo.
“Yeremia alipopewa unabii alilalamika mimi mdogo mimi siwezi, lakini Mungu alimwambiaje, ngoja nisome, (Yeremia 1: 4-10) …. Kabla sijakuumba ndani ya tumbo la mama yako nilikujua, kabla hujazaliwa nilikutenga kwa kazi maalumu, nilikuweka uwe nabii kwa mataifa,” alisema na kuongeza:
“Bwana alimwambia usiseme, mimi ni mtoto mdogo. Utakwenda popote nitakapokutuma na kunena lolote nitakalokuagiza, usiwaogope, kwa maana niko pamoja nawe nikuokoe.”
Alisema Tanzania inapita katika kipindi kigumu, hivyo viongozi wa dini wanapaswa kuongoza maombi yatakayoiwezesha kupata kiongozi mwenye sifa ya kuivusha katika kipindi hicho.
Makamba amesema nchi inakabiliwa na nyufa kama vile rushwa, udini, ukabila, Uzanzibari na Uzanzibara, huku akirejea hotuba ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ya Machi 1995, ambayo aliyataja mambo hayo kuwa nyufa zinazoweza kuliangamiza taifa.
Alisema Tanzania inahitaji uponyaji na ikibidi kuanza upya kwa maana ya aina ya uongozi unaohitajika hivi sasa na kwamba ili kutimiza lengo hilo, viongozi wa dini wana nafasi kubwa ya kutafakari na kuielekeza nchi njia sahihi ya kufuata.
“Shughuli za siasa zimeingiliwa na matapeli, lakini hata shughuli yenu pia imeingiliwa na matapeli. Sasa tunapotafuta uponywaji wa nchi yetu ninyi mna nafasi kubwa kwani uponyaji tunaouzungumzia ni wa maovu ya kiroho, uongo, ubakaji na vitu kama hivyo, ninyi mna nafasi kubwa sana,” alisema.
Alisema viongozi wa kisiasa pia wanayo nafasi yao katika kuponya taifa lakini lazima wanapofanya kazi hiyo wawe wasafi.Alisema askofu au mchungaji akihubiri anapaswa kuwa msafi na hata katika uongozi wa siasa anaposimama mtu na kusema yeye ni jawabu la matatizo ya wananchi ni vizuri kumtazama sura yake kama ameacha (maovu) 
“Tunapoomba uongozi wa kisiasa zipo sifa kwani tunaomba kuongoza watu wa Mungu ambao ni walewale wanaokuja kanisani ndiyo wanaokuja katika siasa, kuongoza watu wa Mungu siyo kitu kidogo…… hivyo lazima vigezo vya kuongoza watu hawa viwe vikubwa sana,” alisema
Rasilimali za nchi
Alisema Tanzania hivi sasa inakabiliwa na changamoto zinazoweza kuitwa kuwa ni za kidunia na za kibinadamu zinazojumuisha masuala kama vile upatikanaji wa huduma za afya, maji na elimu.
“Tunagawanyika ingawa migawanyiko hiyo si ya kidini, rangi na kikabila... iko ya namna gani, watu wachache wananufaika na keki (rasilimali) ya taifa kuliko wengine,” alisema Makamba na kuongeza:
“Sasa Serikali, hili kwetu ni muhimu sana…. hakuna kitu muhimu kama kuendelea kujenga umoja wa taifa letu, migawanyiko hii ndiyo changamoto. Elimu anayoipata mtoto wangu ndiyo anaipata mtoto wa Rwamgasa, Kwimba na Nyarugusu?”
Alisema usawa katika elimu pamoja na huduma nyingine kama afya na nyingine muhimu, ndiyo msingi wa ujenzi wa taifa lenye amani na umoja kwani kila mmoja atajihisi kunufaika na rasilimali za nchi.
Naibu Waziri huyo alisema changamoto nyingine zinazoikabili nchi ni vitendo vya rushwa, ubadhirifu na wizi wa mali ya umma, ubakaji, utapeli na kuporomoka kwa maadili.
Alisema taifa halipaswi kusubiri adhabu kutoka kwa Mungu kama inavyosomeka katika vitabu vitakatifu ambako kuna ushahidi kuhusu gharika wakati wa Nuhu, pia moto wakati wa Sodoma na Gomora, huku akiwapa changamoto viongozi wa dini kukabiliana uovu unaoshika kasi.
“Sasa taifa letu lina miaka 52 ya Uhuru wa Tanganyika na mwakani tunaadhimisha miaka 50 ya Uhuru wa Zanzibar. Miaka 50 ni mingi kwa binadamu, lakini ukweli ni kwamba kazi ya kulijenga taifa letu ndiyo inaanza.”
Shinikizo la maaskofu
Baada ya hotuba yake, baadhi ya maaskofu na wachungaji walisikika wakimshinikiza Makamba atangaze nia ya kugombea urais lakini alisema atafanya hivyo wakati mwafaka ukiwadia.
Mwenyekiti wa Umoja wa Makanisa hayo ya Kikristo, Askofu Charles Sekelwa alisema: “Viongozi wa dini tukubaliane kuwa walezi na tusimkatae mtu kwa dini yake wala kabila lake. Wakijitokeza vijana huko mbele tuwaunge mkono, hayo maneno ni ya mtu mwenye hekima”.Askofu Jacob Lutabija alisema amepokea ujumbe mzito ambao atakwenda kuutangaza kwa waumini wake wa Musoma akisema kwa watu wenye hekima zao wametambua nini wanapaswa kufan



Kuundwa Tume Huru ya Uchaguzi kunasubiri kuwapo machafuko?

Kama kuna jambo ambalo limewafanya wananchi wengi kukuna vichwa kwa muda mrefu pasipo kupata majibu, ni kutoundwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi kusimamia chaguzi mbalimbali na mchakato wa kupata Katiba Mpya katika ngazi zote zilizosalia, baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kumaliza kazi yake rasmi wiki ijayo.

Kwa maana hiyo, mchakato wa Katiba Mpya unaingia katika awamu ya pili kwa Tume hiyo ya Warioba kukabidhi kijiti cha mbio za mchakato huo kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), ambayo majukumu yake sasa ni pamoja na kusimamia mambo muhimu mwakani ambayo ni pamoja na: Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura; Kura ya Maoni kuhusu Rasimu ya Tatu ya Katiba Mpya; Utoaji wa Elimu ya Uraia kuhusu upigaji wa kura hiyo na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Nec pia ndiyo itasimamia na kuendesha Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Majukumu hayo hakika ni mazito mno kutekelezwa na Nec, ambayo imekuwa na udhaifu mkubwa kiasi cha kupoteza mwelekeo na imani kwa wananchi. Tangu kuanzishwa kwake na Sheria ya Bunge mwaka 1977, Tume hiyo imedhihirisha kwamba siyo huru hata kidogo kutokana na kuonekana machoni mwa wananchi kwamba imo mfukoni mwa Serikali na chama tawala, kwani yamejitokeza matukio mengi ya aibu katika uhai wake wa miaka 36, ikiwa ni pamoja na kuegemea upande wa watawala.
Ndiyo maana siyo wananchi wengi walioshangazwa na kauli ya Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Damian Lubuva alipokiri miezi michache iliyopita wakati akitoa maoni ya Tume yake mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuwa, Tume yake siyo huru. Alishauri kwamba katika mazingira ya sasa ya kuwapo mchakato wa kupata Katiba Mpya, iundwe Tume Huru ya Uchaguzi ili chombo hicho kipate mwafaka wa kitaifa ili kiweze kusimamia mchakato mzima kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, chini ya Katiba Mpya.
Kauli ya Jaji Lubuva imethibitisha pasipo kuacha chembe ya shaka kwamba hoja za muda mrefu za vyama vya upinzani na asasi zisizo za kiserikali kwamba Tume hiyo siyo huru zina mashiko. Tafsiri sahihi ya hoja hizo ni kuwa, siyo tu kwamba Tume hiyo siyo huru, bali pia chombo hicho hakina uwezo wa kusimamia majukumu yake kwa ufanisi kutokana na matatizo ya kisera na kimfumo. Kukosekana kwa utashi wa kisiasa pia kumechangia mno katika kudumaza Tume hiyo, ambayo kwa mujibu wa Katiba iliyopo wajumbe wake wanateuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano, ambaye ni kada namba moja wa chama tawala.
Kitendawili kinachoshindikana kuteguliwa hadi sasa ni sababu za mamlaka husika kutoona umuhimu wa kuwapo mfumo wa kupata Tume Huru ya Uchaguzi ili uende sambamba na kupatikana kwa Katiba Mpya. Lazima tukubali ukweli kwamba Tume iliyopo sasa haikubaliki katika mazingira tuliyomo na ya baadaye. Kama Tume hiyo imekataa kuboresha Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa miaka mingi sasa, kwa mfano, tutegemee nini zaidi ya vurugu, machafuko na umwagaji damu huko tuendako?





Sunday 22 December 2013

Wabunge wa CCM wamgomea Waziri Mkuu Pinda

Dodoma. Wabunge wa CCM jana mchana walimgomea Mwenyekiti wa Kamati ya Wabunge (Party Cocas) ya chama hicho, Mizengo Pinda na kushinikiza mawaziri watatu ambao wizara zao zimetajwa kushindwa kusimamia vyema Operesheni Tokomeza Ujangili wajiuzulu.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinaeleza kuwa mawaziri walioshinikizwa kujiuzulu wenyewe ni pamoja na Balozi Khamisi Kagasheki ambaye ni Waziri wa Maliasili na Utalii,  Dk Emmanuel Nchimbi (Waziri wa Mambo ya Ndani)  na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha.
Kikao hicho kilichofanyika katika Ukumbi wa Pius Msekwa bungeni jana kiliitishwa na Pinda ambaye pia ni Waziri Mkuu kwa lengo lililoelezwa ni kuwapoza wabunge.
Chanzo cha habari kutoka katika kikao hicho kilisema kuwa wabunge hao walitaka mawaziri hao kujiuzulu wenyewe ili kukinusuru chama  mbele ya wananchi.
“Tumemtaka Waziri Mkuu akakae na wenzake na kutuambia kama wanajiuzulu au la na kutupa jibu kabla ya kuahirishwa kwa Bunge, mtasikia wenyewe baadaye ndani ya Bunge,”kilisema chanzo hicho.
Hata hivyo, baada ya kukamilika kwa kikao hicho na wabunge kurejea bungeni, Pinda hakurejea bungeni, badala yake ilidaiwa kwamba alikuwa na kikao katika ofisi zake zilizopo bungeni.
Hadi  saa 11.25 alasiri  wakati kikao cha Bunge kikiendelea Waziri Mkuu alikuwa hajarejea bungeni, huku ikielezwa kwamba katika kikao alichokuwepo hakikuwahusisha mawaziri wanne waliokuwa katika shinikizo la kujiuzulu.


Malipo ya fidia yawatoa machozi wananchi Dar

Dar es Saalam. Wananchi wa Mji Mpya Majohe, Guluka Kwalala na Ulongoni katika Manispaa ya Ilala  wameiomba Serikali kuingilia kati na kumwamuru mwekezaji wa ujenzi wa njia ya umeme wa  kilovoti 220 kutoka Somanga Mtama  mpaka Kinyerezi, Kilwa Enegy kuwalipa gharama zinazoendana na hali ya maisha ya sasa.
Ombi hilo walilitoa  jana walipokuwa wakijadili kuhusu  dodoso la uhakiki wa mali zao na malipo, walilopewa lilivyokuwa na  upungufu, mapunjo ya mali zao hasa thamani  za nyumba kuwa kidogo  tofauti na gharama  za ujenzi na ununuzi wa kiwanja walizotumia.
Utathmini wa mali na nyumba za wananchi unadaiwa kufanywa na kampuni binafsi iliyofahamika kwa jina la Joransa, ambapo tathmini katika maeneo hayo ilifanyika mwaka 2011 na kutolewa ahadi kuwa malipo ya fidia yangeanza kulipwa baada ya miezi mitatu .
.Baruani Kanoze  akilalamikia kulipwa  fedha kidogo tofauti na thamani ya mali zake, alisema mwekezaji huyo awali aliwahi kusema kuwa atawalipa kwa kiwango kinachoendana na gharama za maisha zilivyo kwa wakati husika jambo ambalo limewashangaza sana. hasa kulingana na kiwango cha malipo kilichotolewa.
‘Ni jambo ambalo haliingii akilini baada ya kuangalia karatasi za tathmini na kukuta gharama zilivyowekwa za viwanja na kupangisha nyumba, kiwanja umewekewa Sh1 milioni na gharama ya kupanga nyumba eti Sh20,000 kwa mwezi, sijui unakwenda kupanga wapi nyumba’ alisema mkazi wa Guluka Kwalala ambaye hakutaka kutajwa gazetini.
 Alisema yeye anamiliki nyumba ya vyumba  vitano, yenye umeme, choo bora pamoja na  kisima cha maji alivyovijenga   kwa zaidi ya Sh40 milioni,  kwenye dodoso la uhakiki wa mali  anaambiwa thamani ya nyumba yake ni Sh6 milioni.
Aidha, walishauri kuliko Serikali kujiingiza katika maafa kwa kukubali mradi huo utekelezwe wakati wananchi hawajaridhika na fidia ao, ni vyema ikafanyika tathmini nyingine ambayo itakuwa ya haki .
Hata hivyo, uongozi wa Kilwa Energy ulipotafutwa kufafanua malipo hayo ya wananchi, simu zao hazikuweza kupatikana.

Kufutwa kodi ya simu, Bunge aibu tupu

Hatua ya Rais Jakaya Kikwete kutia saini hati ya dharura ili Muswada wa Fedha wa mwaka 2013 ufanyiwe marekebisho na kuondoa tozo ya kodi kwa laini za simu imeliacha Bunge katika fadhaa na fedheha kubwa.
Bunge la Bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2013 lilishuhudia wabunge wa chama tawala wakitumia wingi wao bungeni kupitisha kodi hiyo ambayo iliamsha hasira na vilio kutoka kwa wananchi kutoka kila kona ya nchi.
Tunasema hatua hiyo ya Rais imeleta fadhaa na fedheha kwa Bunge kutokana na kuwapo matukio mengi ya aina hiyo katika kipindi kifupi, ambapo Bunge limekuwa likipitisha miswada mingi muhimu kwa ushabiki wa kisiasa badala ya kuangalia masilahi mapana ya taifa. Rais kwa kuwasitiri  wabunge wa chama chake amekuwa akitia saini miswada hiyo na kuwa sheria, lakini baadaye amekuwa akisikiliza hoja za wapinzani na kulazimika kurudisha sheria hizo bungeni ili zifanyiwe marekebisho.
Siyo nia yetu hata kidogo kuorodhesha hapa sheria zote ambazo Rais amezirudisha bungeni kufanyiwa marekebisho katika miaka ya hivi karibuni. Hata hivyo, wasomaji wetu watakumbuka kuwa, moja ya sheria nyeti zilizorudishwa bungeni ni Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ambayo ndiyo hasa iliyoanzisha mchakato wa kupata Katiba Mpya yapata miezi 18 iliyopita. Kama tulivyosema hapo juu, muswada wa sheria hiyo na miswada mingine mingi muhimu ilipitishwa na Bunge kwa ushabiki wa kisiasa na kiitikadi, kwa maana ya hoja za wabunge wa upinzani kuzimwa au kujadiliwa kwa kejeli, vijembe na matusi na hatimaye kupuuzwa.
Ni katika muktadha huo, Sheria ya Fedha ya mwaka 2013 iliyoanzisha tozo ya kodi kwa laini za simu inapaswa kuangaliwa. Bunge kwa staili hiyohiyo ya ushabiki wa kisiasa na kiitikadi lilipitisha muswada wa sheria hiyo, huku wabunge wa upinzani wakipinga na kuainisha athari zake kwa wananchi na uchumi wa taifa. Ni kweli Rais alisaini muswada huo na kuwa sheria, lakini kutokana na athari zake kwa uchumi na wananchi kwa jumla, sasa  ameirudisha bungeni kwa hati ya dharura akitaka ifanyiwe marekebisho na kuifuta kodi hiyo mara moja.
Ni aibu kwa Bunge, Serikali na Kamati ya Bajeti iliyobuni tozo hiyo kutoona mapema madhara ambayo yangesababishwa na kodi hiyo ya Sh1,000 (kwa kila laini ya simu kila mwezi) kwa wananchi maskini ambao  wanahangaika kupata mlo mmoja kwa siku. Spika wa Bunge, Anne Makinda na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa kutojua hali halisi ilivyo, hasa vijijini walikaririwa bungeni wakitetea kwa nguvu hoja ya kuwekwa kwa tozo hiyo,  wakidai kila mwananchi anao uwezo wa kuilipa kila mwezi.
Kutokana na utata uliosababishwa na tozo hiyo, kodi hiyo ilikuwa haijaanza kulipwa mpaka sasa, licha ya Bunge kupitisha muswada huo Julai, mwaka huu. Rais Kikwete baadaye aliingilia kati kwa kuagiza mamlaka zote husika  kukutana mara moja kumaliza mvutano wa kodi hiyo kwa kutafuta vyanzo mbadala vya kodi ili kuziba pengo la Sh178 bilioni ambazo zingetokana na kodi kwenye laini za simu. Ni matarajio yetu kwamba Bunge letu litakuwa limepata somo la kutosha, hivyo litakuwa makini siku zijazo kwa kuhakikisha linapitisha miswada pasipo hila wala ushabiki wa kisiasa.

Wednesday 18 December 2013

Wabunge waliokwepa safari watakiwa kurejesha posho

Dodoma.Sakata la wabunge waliochukua posho kwa ajili ya safari za mafunzo nje ya nchi na kuacha kusafiri, limeingia hatua mpya baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda kuwataka wazirudishe.
Katika orodha ya wabunge wanaotajwa katika sakata hilo, wamo baadhi ya wabunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha NCCR-Mageuzi.
Sakata hilo liliibuliwa bungeni wiki iliyopita mjini Dodoma na Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally Keissy (CCM) wakati akichangia taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (Laac).
Keissy alisema baadhi ya wabunge wanapaswa kuchunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa kuchukua posho za safari za nje ya nchi lakini hawakwenda safari hizo.
Mbunge huyo alifafanua kuwa mbali na kutokwenda kabisa safari hizo, lakini wapo ambao walikwenda na hawakukaa siku zote zilizopangwa.
“Tunawajua na wapo humu ndani,” alisema huku baadhi ya wabunge wakipaza sauti wakitaka awataje, lakini yeye akasema siyo jukumu lake kuwataja kwani Ofisi ya Bunge inawajibika kufanya hivyo.
Mbunge huyo alienda mbali na kudai mbunge mmoja alikatisha safari ya kwenda Marekani na kuamua kwenda Dubai kwa safari binafsi ambayo haikuwepo katika ratiba ya ziara hiyo ya mafunzo.
Habari za uhakika zilizopatikana jana zilisema wabunge wanane walichukua posho ya safari ya kati ya Sh5 milioni na Sh6 na Spika amewaandikia barua akiwataka warudishe fedha hizo.
Majina ya wabunge hao tunayo, lakini kwa sababu za maadili ya uandishi wa habari, gazeti hili halitaweza kuwataja kwa kuwa hawakupatikana ili kujibu tuhuma hizo kama maadili yanavyoelekeza.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake bungeni mjini Dodoma jana, Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel, alisema kuwa Spika ameshaliona jambo hilo na kulichukulia hatua za kiutawala.
“Spika amewaandikia barua akiwataka kurejesha fedha zote za safari ambazo hawakwenda. Ni lazima wazirudishe hakuna namna,” alisema Joel ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Shughuli za Bunge.
Alipoulizwa kuhusiana na majina yao na kiasi walichochukua, Joel alisema hilo ni jambo la kiutawala na kwamba Spika ndiyehuarifiwa na kamati kuhusiana na wabunge ambao hawakusafiri.
“Spika ndiye anayearifiwa na wenyeviti wa kamati husika juu ya wabunge waliosafiri na wasiosafiri kwa sababu wao ndiyo wanapanga safari na sisi tunawapa posho,” alisema.
Akizungumzia malalamiko ya wabunge juu ya baadhi ya wabunge wasiofika bungeni kusaini ili wapate posho ya kikao, Joel alisema tatizo hilo limepungua kwa kiasi kikubwa.
“Lilikuwepo lakini limepungua kwa kiasi kikubwa baada ya kugundua wakifika kwenye malipo majina yao waliosainiwa yamekatwa,” alisema Joel.
Alipoulizwa kuhusiana na tatizo hilo la kupokea posho za safari za nje ya nchi bila kwenda, Mnadhimu wa Kambi ya Rasmi ya Upinzani bungeni, Tundu Lissu alisema kuwa bado hajapata taarifa hizo.
“Lakini muhimu hapa ni Bunge kuandaa utaratibu wa kurejesha mrejesho wa jinsi walivyozitumia na hapo ndipo watagundulika wabunge wanaosafiri kweli na muda waliokaa mahali husika,” alisema Lissu.
Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema) ambaye anatajwa kuwemo kwenye orodha ya wabunge waliopokea posho bila kusafiri, alikiri na tayari alishamuandikia barua Katibu wa Bunge akimueleza kwamba hakusafiri na kuomba utaratibu wa kurejesha fedha hizo.
Nasari alisema yeye alikuwa Jimboni kwake kwa shughuli za wananchi wake, hivyo hakuweza kusafiri na suala hilo alilifikisha mapema kwa Katibu ili ampe maelekezo namna ya kurejesha fedha hizo.

Slaa: Aliyeteua mawaziri mizigo awajibishwe

Tabora. Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk Willibroad Slaa amesema, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kisitafute dawa ya mawaziri ‘Mizigo’ badala yake wamwajibishe aliyewateua hao wanaowaita mzigo.
Alisema badala ya kuwahangaisha Watanzania kwa kujadili majina ya mawaziri mizigo, wanapaswa kuchukua hatua za kinidhamu kama wana uhakika na mawaziri hao na kushauri kuangalia upatikanaji wao hadi kufikia nafasi hizo nyeti za kuwatumikia watu.
Akihutubia mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Shule ya Sekondari Uyui mjini Tabora juzi,Dk Slaa alisema kinachoendelea ndani ya Serikali hivi sasa ambacho kinaitwa ‘mawaziri mizigo’ ni moja ya dalili ya tatizo katika mamlaka ya uteuzi alibainisha pia kuwa, kuwatimua mawaziri hao siyo dawa bali kushughulikia chanzo cha tatizo.
Amesema kwa muda mrefu Serikali ya Rais Jakaya Kikwete imekuwa lawamani kutokana na kushindwa kazi kwa mawaziri wake, jambo ambalo Dk Slaa amesema, limetokana na kutofanyika kwa umakini wa kuzingatia vigezo, bali uswahiba.
Alisisitiza kuwa kinachofanyika sasa kwa Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kuzunguka nchi nzima na kutaja majukwaani mawaziri mzigo ni njia ya kusukuma agenda ya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri,lakini rais anapaswa kuchukua uamuzi sahihi wakati wa kuwawajibisha hao ‘mizigo’ ambao ni maswahiba.
Dk Slaa anaendelea na ziara ya kuimarisha na kukagua uhai wa chama hicho mkoani Tabora,juzi alitembelea maeneo ya Ugoweko, Kakola na Tabora mjini na kudai kuwa mabadiliko ya mara kwa mara ya Baraza la Mawaziri katika Serikali ya Rais Kikwete hayana tija kwa Watanzania na ni dalili za tatizo la ukosefu wa uwajibikaji.

Mawaziri matumbo joto

Dodoma.Kamati ya Bunge ya kuchunguza athari za Operesheni Tokomeza Ujangili inatarajiwa kuwasilisha ripoti yake leo, ambayo inaelezwa kuwa imependekeza kuchukuliwa kwa hatua dhidi ya vigogo kadhaa wa Serikali.
Taarifa ya kamati hiyo ndogo itasomwa leo wakati Kamati ya Bunge ya Ardhi, Mazingira na Maliasili itakapokuwa inawasilisha taarifa yake ya utendaji kazi bungeni.
Wajumbe wengi wa kamati hiyo ndogo wanatokana na Kamati ya Bunge ya Ardhi, Mazingira na Maliasili. Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo ya uchunguzi alimdokeza mwandishi wetu jana kuwa uchunguzi wa kamati hiyo umegundua udhaifu mkubwa katika wizara na idara za Serikali.
Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Kahama (CCM), James Lembeli imependekeza kuchukuliwa hatua kwa baadhi ya maofisa waandamizi wa Wizara za Maliasili na Utalii na Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi. Mjumbe huyo alisema kwa upande wa Wizara ya Maliasili na Utalii, watakaoguswa na ripoti hiyo ni baadhi ya maofisa waandamizi wanaosimamia wanyamapori na hata wale wa maliasili.
Kamati hiyo iliyoanza kazi Novemba 25, mwaka huu inawasilisha ripoti yake baada ya kumaliza kazi ya kuwahoji watu mbalimbali wakiwamo mawaziri watatu ambao wizara zao zilihusika moja kwa moja na operesheni hiyo.
Mawaziri waliohojiwa katika Hoteli ya Bahari Beach, Dar es Salaam ni pamoja na Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emanuel Nchimbi na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa (JKT), Shamsi Vuai Nahodha.
Hata hivyo, taarifa zilizopatikana jana zilisema kuna uwezekano mkubwa taarifa hiyo ‘ikamkaanga’ Dk Mathayo kutokana na mapendekezo ya wabunge katika mkutano wa 13.
Wabunge walikerwa zaidi na kauli ya Dk Mathayo alipopata fursa ya kuchangia taarifa ya Serikali kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili na kuishia kuwapa pole wafugaji ambao mifugo yao iliuawa kwa risasi.
Katika operesheni hiyo, wabunge walipaza sauti wakidai wapo raia wasio na hatia waliouawa na kuteswa, huku mifugo ikiporwa na mingine kama ng’ombe ikiuawa kwa kupigwa risasi.
Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola ndiye aliyekuwa mwiba kwa mawaziri hao aliposema ana kitabu kilichosheheni ushahidi dhidi ya vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu. Habari zaidi zinasema kamati hiyo ya uchunguzi imelazimika kutofanyia shughuli zake katika kumbi za Bunge ili kukwepa vishawishi kutoka kwa watu wa karibu na vigogo wanaotuhumiwa.
“Wamejificha katika hoteli moja tangu waliporudi Dodoma wiki iliyopita ili kuandaa ripoti yao kwa sababu hawataki kuingiliwa ingiliwa na hili ndilo linalowatia hofu mawaziri,” alisema mjumbe huyo.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, pamoja na kasoro za operesheni hiyo, ilisaidia kuwabaini maofisa walioko katika mtandao wa ujangili na baadhi yao walikamatwa na nyara za Serikali.
Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel alithibitisha kuwasilishwa kwa ripoti hiyo leo wakati kamati itakapowasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli zake... Hata hivyo, alisema hana uhakika wa asilimia 100. Ripoti hiyo itawasilishwa huku kukiwa na vuguvugu la kung’olewa kwa mawaziri saba wanaodaiwa mzigo katika utendaji wao na tayari wamehojiwa na Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi iliyokutana wiki iliyopita chini ya Mwenyekiti wake, Rais Kikwete.
Mbali na vuguvugu hilo, ripoti ya uchunguzi pia inawasilishwa wakati tayari Bunge limepitisha azimio la kuwataka mawaziri watatu wajipime kama bado wanatosha kuongoza Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).
Mawaziri hao ni Waziri wa Nchi wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia na Manaibu wake, Aggrey Mwanry na Kassim Majaliwa. Ripoti kama hiyo inayotarajiwa kuwasilishwa bungeni leo na Lembeli ndiyo iliyochangia kumng’oa aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige kutokana na kashfa ya ugawaji vitalu vya uwindaji.

Upangaji madaraja kidato cha 4 gizani

Dodoma.Serikali bado haijaamua utaratibu utakaotumika katika kupanga madaraja ya watahiniwa wa mitihani ya kidato cha nne iliyofanyika mwaka huu.
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo alisema juzi jioni katika Viwanja vya Bunge kuwa, uamuzi juu ya utaratibu utakaotumika kupanga matokeo hayo utaamuliwa katika vikao vya watendaji wa wizara hiyo.
“Baada ya mkutano wa Bunge kumalizika, tutakwenda kukaa na kuamua utaratibu tutakaotumia lakini sasa sina majibu,” alisema na kuongeza kuwa baada ya wiki mbili atakuwa katika nafasi ya kusema utaratibu utakaotumika kupanga matokeo hayo.
Hivi karibuni Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii, katika taarifa yake ya utekelezaji wa shughuli zake katika kipindi cha Machi hadi Desemba 2013, iliitaka Serikali kusitisha utaratibu mpya wa upangaji wa matokeo ya mitihani.
Mabadiliko hayo, daraja ziro ambalo kwa muundo wa zamani lilikuwa na alama 34-35 sasa litakuwa daraja la tano likiwa na alama 48-49.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Sifuni Mchome alikaririwa na vyombo vya habari akisema muundo huo mpya utatumika kwa mzunguko katika kipindi cha miaka minne.
Daraja la kwanza halijaathiriwa na muundo mpya, kwani alama zake zimebaki pale pale ambazo ni 7-17. Daraja la pili alama za muundo wa zamani zilikuwa 18-21 na sasa ni 18-24. Alama za daraja la tatu zilikuwa 22-25 na chini ya muundo mpya zitakuwa 25-31, wakati daraja la nne alama zimebadilika.

Thursday 5 December 2013

Wingu jeusi chadema: Zitto amlima barua Dk Slaa


Dar es Salaam. Mgogoro ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), umeingia katika sura mpya baada ya viongozi wake wawili waandamizi, Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila Mkumbo kuuandikia uongozi wa chama hicho wakitaka uikane taarifa inayowachafua mitandaoni.
Zitto na Dk Mkumbo wanatuhumiwa kupokea fedha na kushirikiana na viongozi wa Idara ya Usalama wa Taifa na wale wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa nia ya kuivuruga Chadema.
Taarifa hiyo yenye kichwa cha habari `Ripoti ya siri juu ya Zitto Kabwe’, ambayo imesambaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii katika siku za karibuni inadaiwa kuwa iliandaliwa na Kitengo cha Upelelezi cha Chadema baada ya uchunguzi wa mwenendo wa Zitto ndani na nje ya nchi kuanzia mwaka 2008.
Sehemu ya taarifa hiyo ya mtandaoni inadai kuwa Zitto alipelekewa kiasi cha Dola za Marekani 266,000 (Sh416 milioni) huko Ujerumani na maofisa wa Usalama wa Tanzania, Desemba 16, 2009.
Ripoti hiyo inadai kuwa fedha hizo zilipitishwa katika Benki ya Berliner ya Ujerumani kwenye akaunti ya raia wa nchi hiyo, Andrea Cordes, ambaye anadaiwa kumpelelekea Zitto.
Taarifa zaidi zinadai kuwa fedha hizo ziligawiwa kwa wafuasi mbalimbali wa chama hicho na miongoni mwao ni Dk Mkumbo.
Zitto amlima barua Dk Slaa
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Zitto alisema amemwandikia barua Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa kumwomba athibitishe ‘Taarifa ya Siri ya Chadema’ kama ni ya kweli au chama hicho kiikanushe ili aweze kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waandishi wa kile alichokiita ‘hekaya.’
“Taarifa ya Chadema inasema kwamba chama hicho (chama changu), kilikuwa kimechunguza mwenendo wangu tangu mwaka 2008 hadi 2010 na kubaini kuwa mimi ninapokea fedha kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuivuruga Chadema,” alisema Zitto kwenye taarifa yake.
Zitto alisema taarifa hiyo ni ya kutunga na iliyojaa uongo wa kiwango cha kutisha, imemfedhehesha, imemsikitisha na kumkasirisha.
Alisema taarifa hiyo iliibuliwa katika kipindi ambacho alikuwa ziarani barani Ulaya katika nchi za Uswisi na Uingereza ambako alikuwa anafuatilia fedha zilizofichwa na Watanzania katika nchi hizo.
“Pengine lengo la ripoti hiyo lilikuwa ni kutaka kunipoteza kutoka katika nia na dhamira yangu ya dhati ya kutaka Watanzania wafaidike na utajiri wao. Muda ambao watunzi wa ripoti hiyo waliamua kutoa taarifa yao unazua maswali mengi kuliko majibu,” alieleza Zitto katika taarifa yake.


Dk Mkumbo alia na uenezi
Dk Mkumbo alieleza kusikitishwa na Idara ya Uenezi ya Chadema kwa kukaa kimya bila kutoa maelezo juu ya suala hilo.
“Hasa pale ambapo tumeambiwa waraka huu umetoka makao makuu. Hii si kawaida kwa idara yetu hii nyeti iliyosheheni watu mahiri. Mara zote huwa wepesi kabisa kwa vijana wetu katika idara hii kutoa ufafanuzi, tena kwa mambo mepesi kabisa yanayokigusa chama, vipi makamanda kwenye jambo hili imekuwaje?” aliandika Dk Mkumbo kwenye ukurasa wake wa mtandao wa Facebook jana na kuthibitisha kwa simu.
Dk Kitila alisema pamoja na umaskini wake, hajawahi kuhongwa popote na wala hatarajii.
“Taarifa zinazosambazwa kuhusu mimi ni za uongo wa kijinga na uzushi wa kitoto kwa malengo ya siasa nyepesi. Ni wazi kwamba wanaosambaza habari chafu kunihusu hawanijui na ndiyo maana wanaweza kudiriki kuzusha kwamba mimi Kitila Mkumbo naweza kuhongwa Sh200,000.”
Alihoji pia Chadema ilikuwa na siri gani za hatari kiasi cha kumfanya Zitto, ambaye ni rafiki yake wa siku nyingi kuhongwa kiasi hicho kikubwa cha fedha.
Mnyika awajibu
Hata hivyo, Katibu Mwenezi wa Chadema, John Mnyika ameikana ripoti hiyo na kueleza kuwa haijaandikwa na makao makuu ya Chadema.
Mnyika alisema Zitto ameibua kitu ambacho anafahamu kuwa kimeshughulikiwa na uongozi wa chama hicho.
“Zitto anajua kuwa Andrea Cordes aliniandikia baruapepe na nakala kwake nikawajibu kuwa ripoti hiyo haijaandikwa na makao makuu ya chama na tukipokea malalamiko rasmi tutachunguza kwa sasa chama kinaichukulia ripoti hiyo kama ripoti nyingine zinazosambazwa mitandaoni,” alifafanua Mnyika.
Akizungumzia malalamiko ya Dk Mkumbo, Mnyika alisema alikuwa anapaswa kufuata taratibu za chama kama alikuwa na malalamiko.
Alisema baada ya taarifa hiyo ya siri kusambaa mtandaoni, Zitto alitoa kauli na kama Dk Mkumbo hakuridhika, alipaswa kuonana na watu wa Idara ya Uenezi ya Chadema.
“Idara ingetoa ufafanuzi zaidi. Mjadala huu usikuzwe bila sababu za msingi na kufunika masuala mengine muhimu ya kitaifa,” alisema Mnyika.

Watanzania changamkieni fursa hizi Burundi

Moja ya sababu kuu za kuanzishwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), ni kutoa wigo mpana wa soko na shughuli za kiuchumi miongoni mwa nchi wanachama.
Tanzania na Burundi ni kati ya nchi tano zinazounda Jumuiya ya Afrika Mashariki. Nchi nyingine wanachama ni Kenya, Uganda na Rwanda, wakati nchi ya Sudan Kusini ikiwa imetuma maombi rasmi ya kujiunga.
Hivi karibuni, EAC iliandaa mafunzo ya siku tano kwa waandishi 25 wa Ukanda huo, mafunzo yaliyoambatana na mkutano wa pili wa siku tatu kuhusu Amani na Usalama miongoni mwa nchi wanachama.
Nilipata fursa ya kuwa kati ya waandishi watano waliowakilisha Tanzania kwenye mafunzo hayo yaliyolenga kuwanoa wanahabari namna ya kuandika habari za machafuko na migogoro bila kuleta madhara kwa jamii.
Pamoja na mafunzo, waandishi wa habari kutoka Tanzania walipata fursa ya kutembelea ubalozi wa Tanzania nchini Burundi. Walipata fursa ya kujifunza mambo kadhaa, mojawapo ni fursa za uwekezaji zinazopatikana nchini Burundi.
Katika mazungumzo yake na ujumbe wa waandishi wa habari kutoka Tanzania, Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Dk James Mwasi Nzagi pamoja na mengine alizungumzia fursa ambazo Watanzania wanapaswa kuzichangamkia hivi sasa.
Uwekezaji katika sekta ya elimu, hasa lugha ya Kiswahili
Burundi ikiwa moja ya nchi zinazoongea lugha ya Kifaransa na Kirundi kama lugha rasmi ya kiofisi na mawasiliano, imeanza kutilia mkazo lugha za Kiswahili na Kiingereza ambazo ni lugha rasmi ya mawasiliano ndani ya EAC.
Serikali ya Burundi hivi sasa inahimiza wananchi wake kujifunza na kumudu lugha za Kiswahili na Kiingereza. Lugha hizo zinapaswa kufundishwa kuanzia elimu ya msingi, sekondari hadi Chuo Kikuu.
Katika miaka ya hivi karibuni, Tanzania imekuwa ikizalisha idadi kubwa ya wahitimu katika sekta ya elimu kuanzia ngazi ya cheti, diploma na shahada.
Uzalishaji nishati ya umeme
Baada ya kumalizika kwa vita na machafuko, nchi ya Burundi hivi sasa inaelekeza nguvu nyingi kwenye kujenga na kuinua uchumi wa Taifa hilo kwa kuhimiza uwekezaji katika sekta ya viwanda, hasa vya uzalishaji.

Hata hivyo, juhudi hizo za serikali zinakwamishwa kwa kukosekana kwa nishati ya umeme ya uhakika, hali inayofanya viwanda vingi kutumia umeme unaozalishwa kwa kutumia jenereta.
Matumizi ya umeme wa jenereta hunasababisha bei ya bidhaa za viwandani kuwa kubwa kiasi cha kupunguza uwezo wa ununuzi kwa wananchi wa kawaida wa Burundi wanaokadiriwa kuwa zaidi ya 9 milioni.
Huduma katika sekta ya hoteli za kitalii na kumbi za mikutano
Kutokana na kukua kwa kasi kwa uchumi wa Burundi na uwepo wa mikutano ya kimataifa na wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa na mabalozi wa nchi mbalimbali, ujenzi wa hoteli za kitalii nchini humo, hasa Mji Mkuu, Bujumbura umeanza kwa kasi na hivyo kusababisha uhaba wa wafanyakazi wenye ujuzi.
Sekta ya usafirishaji wa anga, barabara, reli na majini
Burundi ina mikoa 17 ambayo yote imeunganishwa kwa barabara ya lami na hivyo kutoa fursa ya uwekezaji katika sekta ya usafirisha wa mizigo na abiria kwa gharama nafuu.
Barabara za lami ambazo zote zimeunganishwa na Mji Mkuu, Bujumbura ni fursa nyingine ya kibiashara kati ya mikoa mingine, wilaya na vijiji vya Burundi kwa Watanzania wanaofanya biashara ya usafirishaji abiria na mizigo kwa njia ya barabara.
Usafiri wa Anga
Hadi sasa hakuna ndege zinazofanya safari ya moja kwa moja kutoka Bujumbura hadi Jijini Dar es Salaam ambapo abiria wote hulazimika ama kupitia Nairobi Kenya, Kampala Uganda au Kigali Rwanda ndipo waweze kufika Dar es Salaam au miji mingine nchini.
Usafiri wa maji (meli)
Tanzania na Burundi zinaunganishwa na Ziwa Tanganyika na hivyo kutoa fursa ya uwekezaji kwenye sekta ya usafirishaji kwa njia ya maji.
Hivi sasa meli pekee inayotoa huduma ya usafiri kati ya Burundi na Tanzania ni Mv Liemba ambayo umri wake ni zaidi ya miaka 50

Sekta ya Gesi, hasa za hospitalini
Kuna tatizo la upatikanaji wa uhakika wa gesi za hospitalini ambapo wakati mwingine taifa hilo hulazimika kupata huduma hiyo kutoka nchini Kenya.
Kutokana na Tanzania kufanikiwa kuwa na utajiri mkubwa wa nishati ya gesi, hii ni fursa nyingine ya uwekezaji na kibiashara kwa Watanzania wenye uwezo, ujuzi, utaalamu na uzoefu katika biashara hii kujitanua katika soko la Burundi.
Uwekezaji katika viwanda vya Saruji
Hadi sasa, hakuna kiwanda cha Saruji nchini Burundi. Saruji yote inayotumika nchini humo huagizwa kutoka nje ya nchi na hivyo kufanya saruji kuwa moja ya bidhaa adimu na muhimu.
Kiwanda cha kutengeneza vyuma
Vyuma vyote vinavyotumika Burundi huagizwa kutoka nje ya nchi, hasa nchini Ukraine. Mfanyabiashara atakayejenga kiwanda cha chuma atakuwa na uhakika wa soko.
Kiwanda cha kutengeneza viatu
Kama ilivyo kwa nchi nyingi za Kiafrika, suala la utengenezaji na uvaaji wa viatu nchini Burundi bado liko katika viwango visivyoridhisha na siyo ajabu kukuta watu wazima wakitembea pekupeku katika mitaa ya mji mkuu wa Bujumbura.
Siyo kwamba wananchi nchini Burundi wanatembea peku kwa kupenda. La hasha!
Bei ya viatu iko juu kiasi kwamba wananchi wenye kipato cha chini hushindwa kumudu kununua viatu ambavyo vingi huagizwa kutoka nje ya nchi.
Hii ni fursa mwafaka kwa Watanzania wenye uwezo kuwekeza kwenye eneo hili kwani siyo tu watajihakikishia soko la Burundi lakini pia wataweza kujipenyeza hadi kwenye soko la nchi jirani ya Rwanda ambako tayari Rais wake, Paul Kagame amepiga marufuku watu kutembea peku katika mitaa ya mji mkuu, Kigali.

Kushika soko la Burundi ni njia ya kuingia soko la DRC.
Kutoka mji mkuu wa Burundi, Bujumbura hadi mpakani na nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ni chini ya Kilomita 20 pekee. Ukaribu huu unafanya wafanyabiashara nyingi kuingiliana kati ya Burundi (Bujumbura) na DRC na hivyo kuongeza fursa za kibiashara kwa Watanzania watakaowekeza Burundi.
Baadhi ya taarifa muhimu
Ukubwa wa nchi na idadi ya watu:
Nchi ya Burundi iliyopata uhuru Julai Mosi, 1962, ina ukubwa wa kilomita za mraba 28,000 na idadi ya watu zaidi ya 8 milioni.
Makabila Makuu Burundi
Wahutu: Hili ndilo kabila linaloongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya watu nchini Burundi kama ilivyo nchini Rwanda. Inakadiriwa kuwa kabila hili ni asilimia 85 ya wananchi wote Burundi.
Kiasilia, Wahutu ni Wabantu ambao hujihusisha na kilimo kama njia kuu ya kipato pamoja na ufugaji kwa kiwango kidogo.
Watutsi: Hili ni kabila linalofuata kwa uwingi wa watu nchini Burundi ikiwa na asilimia 14 ya wakazi wote wa nchi hiyo. Asili yao ni ufugaji ingawa pia wanashiriki shughuli za kilimo.
Watwa: Hili ni kabila dogo lenye asilimia moja tu ya wakazi wa Burundi ingawa ndilo kabila la watu wa asili nchini humo.
Kiasilia Watwa ni wawindaji, warina asali na waokota matunda (hunters and gatherers) kama walivyo makabila ya Wahadzabe, Wandorobo, Wasandawe kwa hapa Tanzania.
Chakula: Chakula kikuu nchini Burundi ni ugali na matoke inayoliwa kwa nyama, mboga za majani na samaki wanaopatikana Ziwa Tanganyika, hasa mukake ambao kwa Tanzania, hasa kwa wakazi wa mikoa ya Kigoma, Rukwa na Katavi hujulikana kwa jina la migebuka
Burundi pia imejaaliwa kuwa na uwingi wa aina mbalimbali za matunda na vyakula vitokanavyo na mizizi kama mihogo, viazi vitamu na viazi mviringo.
Kilimo:Mazao ya kilimo na chakula Burundi ni pamoja na kahawa, pamba, chai, mahindi, mtama, ndizi na viazi vitamu.
Muziki:Muziki maarufu unaopendwa na wananchi Burundi ni ngoma ya Karyenda ambayo huchezwa kwa mtindo wa kuvutia ukishirikisha wanawake na wanaume.
Ukiwa Burundi ekupa kuuliza zilipo kambi za jeshi au ofisi za usalama. Tofauti na Tanzania ni kawaida kumsikia mtu akisema kambi ya jeshi ya Mgulani, oohh Morogoro kuna kambi ya mizinga n.k. Aidha, huruhisiwi kupiga picha mitaani bila kibali cha Meya wa mji, kwa sababu za kiusalama.

Polisi yaituhumu Chadema moto Arusha,Lema aja juu

Arusha.Polisi mkoani Arusha imekamilisha uchunguzi wake kuhusiana na kuungua kwa Ofisi za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na kusema wanachama wa chama hicho ndio waliohusika.
Hata hivyo, Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema amepinga kauli hiyo na kulipa jeshi hilo siku nne kuwakamata na kuwahoji watuhumiwa watano baada ya kulipatia majina hayo akidai kuwa ndio wanaohusika na uchomaji moto ofisi za chama hicho.
“Tumewapatia polisi majina... tunaamini walihusika moja kwa moja la sivyo, chama kitatumia vijana wetu wa Red Brigade kuwakamata na kuwafikisha polisi,” Lema aliwaambia waandishi wa habari jana.
Ofisi cha Chadema zilizoko katika eneo la Ngarenaro, zilinusurika kuteketea kwa moto juzi baada ya watu wasiojulikana kuwasha moto katika moja ya vyumba vyake.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Japhet Lusinga alisema:
“Katika uchunguzi wetu, tumebaini kuwa hakuna mahali palipovunjwa kutoka nje ya uzio na kuruhusu watu kuingia ndani... tumegundua kuna tundu dogo darini eneo la kuelekea bafuni la upana wa futi moja na nusu kiasi haliwezi kuruhusu mtu kupita.
“Tumejiridhisha kuwa hakuna mtu anayeweza kupita hapo na ndani tulikuta majivu na baadhi ya vitu vilivyoungua na vifaa vingine.”
Lema akiwa na Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Arusha, Ephata Nanyaro alisema: “Tumebaini polisi wanataka kulifanya jambo hili kama la siasa ndiyo sababu juzi badala ya kuanza kuchunguza waliohusika, waliwakamata Mtunza Ofisi na mlinzi wetu na kuwalaza rumande hadi leo (jana) asubuhi kwa madai eti wanawahoji.
“Hatukubaliani na taarifa yao, hii ni siasa. Kulitokea mauaji ya bomu, wakasema Chadema wamejilipua, leo ofisi imechomwa wanasema Chadema wenyewe, hili hatukubali, “ alisema.
Msajili alaani
Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi amelaani tukio la kuchomwa moto ofisi hizo za Chadema na kusisitiza kuwa wananchi hususan wanasiasa wasiwe wepesi kuingiza hisia kwenye makosa ya kijinai.
Alisema kuwa tukio hilo linapaswa kukemewa kwa hali yoyote ile kwa kuwa linavuruga na kuhatarisha amani ya nchi.
Dk Slaa aanza ziara
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Wilbrod Slaa amesema hakuna mtu yeyote mkubwa kuliko katiba ya chama hicho.
Dk Slaa aliyasema hayo jana kwenye Uwanja wa CDT, Kahama mkoani Shinyanga, alipokuwa akihutubia mamia ya wanachama na mashabiki wa chama hicho akiwa katika ziara yake kuimarisha chama katika mikoa ya Shinyanga na Kigoma.
“Chadema ni chama makini, kina kila kitu kwenye katiba yake kuliko hata CCM, kina itifaki, kina maadili hata mimi na Mwenyekiti Mbowe (Freeman) imetuwekea mipaka ya utendaji... “Chama hakiwezi kumwonea mtu, kinatenda haki na yanayotokea sasa ni msukumo wa baadhi ya vyombo vya usalama na hayakuanza leo.”
Kauli yake ilionekana kutoa ufafanuzi wa hatua ya Kamati Kuu ambayo ilimvua nyadhifa zake zote aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe na wenzake wawili kwa madai ya kuandaa waraka kuhamasisha mabadiliko hatua iliyosababisha mvutano mkubwa ndani ya chama hicho kikuu cha upinzani nchini.

Lissu: Muswada wa kura za maoni ni kinyume cha Katiba

Dodoma.Kambi ya Rasmi ya Upinzani Bungeni imetaka Muswada wa Kura ya Maoni uondolewe bungeni hadi hapo Bunge litakapofanya marekebisho ya Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa unapingana nayo.
Awali, muswada huo ulikuwa ujadiliwe katika Mkutano wa 12 wa Bunge lakini uliahirishwa kutokana na wajumbe wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ya Bunge wanaotoka Zanzibar kupinga vikali kura ya maoni kupigwa visiwani humo kwa kuwa tayari huko kuna sheria hiyo.
Akiwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni jana, Waziri Kivuli wa Katiba na Sheria, Tundu Lissu alisema katika Katiba ya sasa, hakuna mahali ambako kura ya maoni inatajwa.
Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki alisema tofauti na Katiba ya Jamhuri, Katiba ya Zanzibar imetambua kura ya maoni kwa kuitaja rasmi katika Katiba na kuiwekea utaratibu.
“Kwa maoni ya kambi ya upinzani, Serikali ya CCM inaogopa kufungua mjadala wa marekebisho ya Katiba ili kuruhusu kura ya maoni kwa hofu kuwa mjadala huo, utapanuliwa kwa kuhoji uhuru wa Tume ya Uchaguzi katika kuendesha na kusimamia uchaguzi,” alisema.
Alisema hofu ya CCM haiwezi kukubaliwa na Bunge kama sababu ya msingi ya kutunga sheria ambazo zinapingana na Katiba.
“Kwani kwa kufanya hivyo itakuwa sawa na kubariki ukiukwaji wa Katiba ambao wabunge wote tuliopo ndani ya ukumbi huu tuliapa kuhifadhi, kuilinda na kuitetea,” alisema Lissu ambaye pia ni Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani bungeni.
Awali, akiwasilisha muswada huo bungeni kwa niaba ya Waziri Mkuu, Waziri wa Nchi (Ofisi ya Waziri Mkuu), Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi alisema: “Ili kuepuka mkanganyiko unaojitokeza iwapo sheria za uchaguzi zilizopo zitatumika kusimamia uendeshaji wa kura ya maoni, Serikali imeona umuhimu wa kutumia kura ya maoni kwenye mchakato wa kutunga Katiba Mpya.
“Sheria hii si ya kudumu na itafikia ukomo wake, mara tu baada ya Katiba Mpya kupatikana na haya ndiyo madhumuni makuu ya kupendekeza kutungwa kwa sheria hii ya kura ya maoni,” alisema.
Alisema mpigakura aliyesajiliwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura la Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), au Daftari la Kudumu la Wapiga Kura la Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), atakuwa na haki ya kupiga kura ya maoni.
Kamati
Kwa upande wake, Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala, imeshauri muda wa kukata rufaa kuongezwa hadi siku saba badala ya tano zilizopendekezwa katika muswada huo. Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Pindi Chana alisema Ibara ya 45 ya muswada huo, inaweka masharti kwa kamati ya kura ya maoni ambayo haikuridhika na uamuzi wa mahakama ya chini, kuwasilisha rufaa yake ndani ya siku tano tangu tarehe iliyopata nakala ya hukumu.

Kamati hiyo pia imeshauri Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lianze kuboreshwa kwa sababu vijana wengi wamefikisha umri wa kupiga kura na hawajaandikishwa.
Chana alisema kamati inaunga mkono mapendekezo ya muswada huo kuwa kura zitangazwe ndani ya saa 72 tangu kufungwa kwa vituo vya kupigia kura.
“Kamati inashauri Serikali kuandaa vifaa vya kisasa na kuwajengea uwezo watendaji wa tume zote mbili ili waweze kumudu usimamizi wa mchakato wa upigaji wa kura ya maoni kwa weledi na umahiri wa hali ya juu,” alisema. Aidha, alisema kamati inaunga mkono mapendekezo ya muswada huo kuwa matokeo ya kura ya maoni yataamuliwa kwa kigezo cha asilimia 50 ya kura halali zilizopigwa za kuunga mkono swali la kura ya maoni kwa pande zote mbili za Muungano.
“Ibara ya 34(2) inaweka sharti la wingi wa kura halali zilizopigwa katika suala la kura ya maoni kuwa ndilo litakaloamua kuhusu kukubalika au kutokukubalika kwa katiba inayopendekezwa. Kamati inaunga mkono masharti haya kwa kuwa uamuzi wa wananchi ndiyo wa mwisho kuhusu jambo kubwa na nyeti kama la Katiba,” alisema Chana.
Wabunge Z’bar wapinga
Utaratibu wa kuwatumia masheha katika uandikishaji wa vitambulisho vya ukaazi Zanzibar umezua mjadala mkali bungeni baada ya wabunge wa CUF, kupinga kutumika katika kuwapata wapiga kura wa Katiba Mpya.
Akichangia Muswada wa Sheria ya Kura ya Maoni wa mwaka 2013, Mbunge wa Chakechake, Mussa Haji Kombo alitaka kufutwa kwa kipengele kinachotaka kutumika kwa Daftari la Wapiga Kura la Zanzibar katika kupiga kura za maoni kwa kuwa kitawanyima haki Watanzania ambao hawakuandikishwa kutokana na kunyimwa vitambulisho vya ukaazi na masheha.
“Msitugawe kwa kutubagua, leo hii mtu anayeandikishwa Tabora (katika daftari la wapiga kura) haulizwi kitambulisho cha ukaazi lakini wa Micheweni haandikishwi bila kuwa na kitambulisho cha ukaazi,” alisema. “Kuna danadana nyingi katika uandikishaji wa vitambulisho vya ukaazi lakini watoto wa miaka 12 wa wanachama wa CCM wameshapata vitambulisho… zoezi hili ni muhimu tutaliharibu kwa kufuata matakwa ya vyama,” alisema Riziki Omary Juma (Viti Maalumu).
Mbunge wa Mkoani, Ally Khamis Seif, alishauri kuanzishwa kwa daftari lingine la wapiga kura ambalo halitahusisha masharti ya kuwa na vitambulisho vya ukaazi ili kuwapa nafasi Wazanzibari wote kupiga kura katika mchakato huo.
“Kama mimi Sheha wangu wa Konde alininyima kitambulisho cha ukaazi kama ya Mbunge yamekuwa hayo je, Watanzania wa kawaida? Hili jambo litatuletea taabu katika maamuzi haya magumu tunayoyafanya, tuache kutumia daftari la wapiga kura la Zanzibar lile si daftari lile ni uchochezi litatuletea taabu,” aliongeza Mbunge wa Konde, Khatibu Said Haji.

Papa Francis adaiwa kutoroka Vatican usiku

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis amedaiwa kutoroka usiku Makao Vatican ili apate fursa ya kwenda kutoa misaada kwa walemavu na watu wasiojiweza.
Tetesi za Papa Francis kuwatembelea maskini hao usiku kwa kujificha zimekuja baada ya mahojiano yaliyofanywa na Askofu Mkuu, Konrad Krajewski ambaye kazi yake kubwa ni kukusanya fedha toka kwa wasamaria wema na kuwapelekea maskini.
Imeelezwa kuwa Askofu Krajewski amekuwa akiambatana na Papa Francis wakati mwingine na kwenda kuwapa misaada maskini maeneo ya vijiji, mjini Vatican.
Askofu Krajewski alisema tangu zamani alipokuwa Askofu Mkuu wa Jimbo la Buenos Aires, Papa Francis amekuwa akipenda kwenda mijini nyakati za usiku na kuwatembelea wenye shida mbalimbali.
“Amekuwa akionyesha dalili ya kupenda kunisindikiza kwenda kuwapa misaada maskini, pindi nikiondoka kwenda kufanya kazi hiyo,” alisema Padri Krajewski.
Hata hivyo, alipoulizwa iwapo Papa aliwahi kwenda naye nje ya mji kwa ajili hiyo, Askofu Krajewski, alisita kujibu swali hilo.
Wakati huohuo, gazeti la Huffington Post limeripoti kuwa walinzi wa Uswisi, wamethibitisha kuwa Papa amekuwa akizunguka maeneo mbalimbali usiku akiwa amevalia mavazi ya kawaida ya wachungaji na kuwapa misaada, wanaume na wanawake wenye shida mbalimbali.
Tangu kuteuliwa kwake, papa Francis amevipamba vichwa vya habari duniani baada ya kuonekana akijaribu kuvaa kofia za polisi wa zimamoto, kuwaruhusu vijana wadogo wa kiume kuibusu miguu yake na kuwapigia simu waumini wake na kuzungumza nao.
Hivi karibuni, aliripotiwa katika vyombo vya habari akiwabusu na kuwafariji waumini walemavu katika Kanisa la Mtakatifu Peter, huku taarifa nyingine zikionyesha kuwa ametuma fedha zake binafsi kwa wahamiaji na wanaohangaikia mafao yao.
Alipokuwa Askofu Mkuu wa Jimbo la Buenos Aires, Papa Francis alifahamika kwa kutoroka usiku na kuwatafuta watu, kuzungumza nao na wakati mwingine kuwanunulia chakula.
Mapapa wengine waliopita pia wametajwa kutoroka usiku, kwa mfano papa John wa X111 alikuwa na tabia ya kutoroka usiku na kwenda mitaa ya Rome kufurahia uzuri wa jiji hilo, wakati Papa Pius wa X11alivalia kama Mfaransa wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia na kwenda mipakani kuwasaidia Wayahudi wa Kirumi kisha kuwaweka katika sehemu salama.

JK asafisha vyombo vya dola Z’bar

Dar es Salaam. Katika kile kinachotafsiriwa kuwa ni kusafisha idara zilizopo ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Rais Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko katika Idara ya Uhamiaji baada ya kumteua Johari Masoud Sururu kuwa Kamishna mpya wa Zanzibar.
Uteuzi huo wa Rais Kikwete umekuja siku moja tangu alipomteua Kamishna wa Polisi, Hamdan Omari Makame kushika wadhifa huo Zanzibar huku aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo, Kamishna Mussa Ali Mussa akiteuliwa kushika wadhifa mpya wa Kamishna wa Polisi Jamii.
Taarifa iliyotolewa jana na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Isaac Nantanga ilieleza kuwa kutokana na uteuzi huo, aliyekuwa Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, Mwinchumu Hassan Salim atapangiwa kazi nyingine. Kabla ya uteuzi huo ambao umeanza Novemba 24 mwaka huu, Sururu alikuwa Mwambata wa Uhamiaji katika Ubalozi wa Tanzania, Abu Dhabi, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Agosti 28 mwaka huu baada ya kuongozana kwa matukio ya watu kukamatwa na dawa za kulevya na meno ya tembo katika viwanja vya ndege nchini, nje ya nchi na maeneo mbalimbali, Rais Kikwete alifanya mabadiliko katika idara hiyo kwa kumteua Sylvester Mwakinyule kuwa Kamishna Mkuu, Idara ya Uhamiaji.
Mwakinyule alichukua nafasi ya Magnus Ulungi ambaye ilielezwa kuwa atapangiwa kazi nyingine. Kabla ya uteuzi huo, Mwakinyule alikuwa Naibu Kamishna wa Uhamiaji na Mwambata wa Uhamiaji katika Ubalozi wa Tanzania, London, Uingereza.
Katika uteuzi wa juzi, Rais Kikwete alifanya mabadiliko katika idara nyingine ya wizara hiyo kwa kuwapandisha vyeo maofisa waandamizi wanne wa Jeshi la Polisi, pamoja na kufanya uteuzi wa nafasi za madaraka kutokana na mabadiliko ya muundo wa jeshi hilo. Waliopandishwa vyeo ni pamoja na Isaya Mungulu ambaye anakuwa Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Makosa ya Jinai (DCI) kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Robert Manumba ambaye amestaafu.
Awali, Mungulu alikuwa Mkuu wa Ufuatiliaji na Tathmini (CID) na baada ya Manumba kustaafu Novemba 11 mwaka huu, aliteuliwa kukaimu nafasi hiyo.
Maofisa wengine waliopandishwa vyeo kuwa Makamishna wa Polisi (CP) ni Ernest Mangu, Thobias Andengenye, Abdulrahaman Kaniki na Makame.
Rais Kikwete pia amempandisha cheo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Athuman Diwani kuwa Naibu Kamishna wa Polisi na kumteua kuwa Naibu DCI.
Walioteuliwa katika nafasi za madaraka ni Clodwig Mtweve (Kamishna wa Fedha na Utaratibu wa Ugavi na Usafirishaji wa Watu na Vitu (Logistics), Paul Chagonja (Kamishna wa Operesheni na Mafunzo).
Mangu (Mkurugenzi wa Usalama wa Jinai), Andengenye (Kamishna wa Utawala na Utumishi) na Kaniki (Uchunguzi wa Ushahidi wa Jinai).

Mandela afariki dunia

Mandela amekuwa akisumbuliwa na maradhi kwenye mapafu kwa muda mrefu, alilazwa na baadaye kuruhusiwa kutoka hospitali ambapo mauti yamemkuta akiwa nyumbani kwake mjini Pretoria.
RAIS wa kwanza wa Afrika Kusini na mpinga siasa za ubaguzi wa rangi, Nelson Mandela amefariki nchini humo akiwa na umri wa miaka 95.
Taarifa za kifo chake zimetangazwa na rais wa nchi hiyo, Jacob Zuma ambaye amesema Mandela amefariki majira ya saa 2.50 usiku wa Alhamisi kwa saa za Afrika Kusini.
Mandela amekuwa akisumbuliwa na maradhi kwenye mapafu kwa muda mrefu, alilazwa na baadaye kuruhusiwa kutoka hospitali ambapo mauti yamemkuta akiwa nyumbani kwake mjini Pretoria.
Tayari viongozi mbalimbali duaniani wameshaanza kutuma salamu za rambirambi kwa familia na taifa la Afrika Kusini.
Viongozi hao ni pamoja na Rais Barack Obama wa Marekani na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki-Moon.