Wednesday 20 May 2015

Ufisadi huu sasa kiama

Dodoma. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad amewasilisha ripoti tano za ukaguzi wa fedha kwa mwaka ulioishia Juni 30, 2014 akibainisha ufisadi wa zaidi ya Sh600 bilioni katika maeneo mbalimbali na matumizi ya fedha ambayo hayana maelezo ya kutosha.
Ukaguzi huo ulifanywa katika Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, mashirika ya umma, miradi ya maendeleo na ufanisi wa maeneo mbalimbali.
Ripoti hizo zinaonyesha jinsi watumishi hewa wa umma wanavyoendelea kulipwa mishahara, wakiwamo wa balozi za Tanzania waliostaafu, misamaha ya kodi na ukiukwaji wa ununuzi na matumizi yasiyoeleweka ya fedha katika Wizara ya Ujenzi na Kitengo cha Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu.
Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), Amina Mwidau na Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Rajab Mbaruk Mohamed walizichambua ripoti hizo na kueleza jinsi watumishi wa Serikali wanavyotafuna mabilioni ya fedha.
Akizungumzia ripoti hiyo katika mkutano wa pamoja na CAG, Mwidau alisema imeonyesha jinsi Sh285 bilioni za Kitengo cha Maafa zilivyotafunwa licha ya kuwa zilitengwa kwa ajili ya kufanya shughuli maalumu.
Kuhusu Wizara ya Ujenzi, alisema ililidanganya Bunge baada ya kueleza kuwa Sh262 bilioni zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara, kitu ambacho kimebainika kuwa siyo kweli.
“Ukaguzi unaonyesha kuwa fedha hizo zimetumika katika mambo mengine kabisa, yaani zimetumika tofauti na hakuna maelezo ya kuridhisha,” alisema Mwidau huku akifafanua kuwa wizara hiyo inadaiwa na makandarasi Sh800 bilioni.
Misamaha ya kodi
Profesa Assad alisema ofisi yake ilibaini kasoro katika mfumo wa ufuatiliaji wa misamaha ya kodi na kusababisha ukiukaji wa matumizi iliyotolewa kwa mafuta yanayotumika migodini.
Alisema mafuta yenye kodi ya Sh22.33 bilioni yaliyotakiwa kutumiwa na kampuni zilizosamehewa kodi, Geita Gold Mine na Resolute TZ Ltd, yalipelekwa kwa makandarasi wasiostahili msamaha na kusababisha hasara ya Sh22.33 bilioni,” alisema.
Alisema pia misamaha ya kodi kwa malengo tofauti na yaliyokusudiwa, ilitolewa na kusababisha upotevu wa Sh392.7 milioni katika Kampuni ya Kiliwarrior Expeditions Ltd ya Arusha iliyokuwa imesamehewa kodi Sh465.2 ili kuingiza magari 28.
Hata hivyo, alisema Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imefanikiwa kati ya hizo kukusanya Sh72.5 milioni.
Pia, alisema misamaha ya Sh53.4 milioni ilitolewa kwa Kampuni ya Kilemakyaro Mountain Lodge Limited kwa ajili ya mradi wa ujenzi na upanuzi hoteli katika Kijiji cha Changarawe wilayani Karatu, lakini kampuni iliagiza magari matatu kwa kutumia msamaha na mengine matano ‘kuchepushwa’.
“Hata hivyo, ukaguzi ulithibitisha ununuzi wa gari moja tu ya Hyundai Santa. Magari mengine matano aina ya BMW na Toyota Land Cruiser Prado hayakufahamika yalipo,” alisema. CAG aliishauri Serikali izibe mianya ya upotevu wa kodi kupitia misamaha ya kodi aliyobaini katika ukaguzi wa mwaka huu, ikiwa ni pamoja na kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa misamaha ya kodi iliyotolewa.
Mashine za EFD
Alisema katika ukaguzi wa malipo na matumizi  ya mashine za kielektroniki (EFD), ofisi yake ilibaini kuwa kampuni binafsi hazitumii mashine hizo za kutolea stakabadhi.
Alisema hali hiyo imesababisha malipo ya Sh4.4 bilioni kutokuwa na stakabadhi za kielektroniki kwa taasisi za Serikali Kuu na Sh4.6 bilioni kwa sampuli  22 ya mamlaka za serikali za mitaa.
“Katika suala hili, TRA ilitoza faini Sh440.8 milioni kwa wafanyabiashara ambao walishindwa kutumia mashine za EFD ambapo jumla ya Sh72 milioni zililipwa sawa na asilimia 16 na hivyo kufanya bakaa ya Sh369 milioni ambayo haikulipwa,” alisema.
Alisema pia ukaguzi ulibaini upungufu katika usimamizi wa matumizi ya fedha za Serikali kama vile, malipo yasiyokuwa na nyaraka. Upungufu mwingine ni hati za malipo ambazo hazikuwasilishwa kwa ukaguzi, fedha zilizotumika nje ya bajeti, matumizi yasiyokuwa na manufaa na malipo ambayo hayakuidhinishwa na maofisa masuuli.
Alishauri taasisi za Serikali zisiendelee kanunua vifaa na huduma kwa wafanyabiashara wasiotumia mashine za EFD kutoa stakabadhi ya kukiri kupokea fedha.
“Hii iende sambamba na kuhakikisha kuwa maofisa masuuli wanaimarisha mfumo wa udhibiti wa ndani ikiwa pamoja na kuimarisha ukaguzi kabla ya malipo,” alisema.
Mishahara hewa
Alisema fedha zilizolipwa kwa watumishi hewa wa Serikali Kuu ni Sh141.4 milioni, “Hali hii inaendelea licha ya kuwa Serikali imewekeza kwenye mfumo wa Lawson kama njia mojawapo ya kudhibiti hali hiyo,” alisema. Hata hivyo, alisema suala hilo linazidi kupungua ikilinganishwa na mwaka jana. Lakini alisema Sh1.01 bilioni katika halmashauri 36 zililipwa kama mishahara kwa watumishi waliotoroka kazini, waliofariki, waliostaafu na kufukuzwa kazi.
Alisema kutokana na watumishi hewa, Sh845 milioni za halmashauri zililipwa kama makato ya taasisi mbalimbali kama vile mifuko ya pensheni, taasisi za fedha, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na TRA kwa ajili ya wafanyakazi hao hewa.
Katika balozi
CAG pia ameeleza jinsi Serikali ilivyolipa Sh543.7 milioni kutokana na kuwalipa watumishi wa balozi za Tanzania waliostaafu, waliokuwa wakifanya kazi bila kuwa na mikataba kutokana na changamoto za malipo ya kurejeshwa nyumbani.
Watumishi hao ni wa balozi za Tanzania Kinshasa (DRC), Maputo (Msumbiji), Ottawa (Canada) na Washington DC (Marekani).
Ripoti hiyo inaonyesha tarehe ambazo watumishi hao walistaafu, lakini Serikali iliendelea kuwalipa huku wakiwa katika maeneo yao ya kazi, zikijumuisha kodi za majengo huku baadhi ya watumishi hao wakifanya kazi licha ya kuwa mikataba yao kumalizika.
Ufisadi Tanesco
Ripoti hiyo pia ilibaini kuwapo kwa ununuzi wa Sh3.2 bilioni uliofanywa na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), bila kuzingatia kiasi kilichotengwa kwenye bajeti ya Sh400 milioni.
“Katika zabuni nyingine, Tanesco iliingia mkataba wa Sh340 milioni ambayo ni zaidi ya bajeti iliyotengwa ya Sh154 milioni. Ukaguzi haukuweza kupata ushahidi wa kuwapo kwa marejeo ya bajeti kwa kiasi kilichotumika nje ya makisio,” alisema
Vyama vya siasa
Kuhusu ukaguzi wa vyama vya siasa, CAG alisema hadi kufikia Juni, 2013 vyama 21 wakati vinakaguliwa, ni 12 tu ndivyo vilivyowasilisha taarifa za hesabu.Alisema kati ya vyama 12, tisa havikuwasilisha taarifa za hesabu ambavyo ni UPDP, Tadea, UDP, Demokrasia Makini, Chausta, DP, Jahazi Asilia, AFP na CCK.
Alisema katika ukaguzi huo, ilibainika kuwa vyama sita vya siasa vilipata hati ya shaka ambavyo ni CCM, Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi, TLP na Chauma na vya vingine vilipata hati mbaya ambavyo ni NRD, UMD, ADC, APPT, NLD na SAU.
Alishauri Msajili wa Vyama vya Siasa akishirikiana na Mhasibu Mkuu wa Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA), waandae mwongozo wa aina ya muundo wa taarifa za fedha utakaotumiwa na vyama vyote vya siasa.
Bajeti
Kuhusu bajeti, alisema tathmini waliyofanya kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo, programu na shughuli nyingine za maendeleo katika baadhi ya halmashauri, imeonyesha kuwa hadi kufikia Juni 30, mwaka jana, halmashauri hizo zilikuwa na bakaa ya jumla ya Sh29.2 bilioni sawa na asilimia 28 ya jumla fedha zilizotolewa.
Alisema kubakia kwa kiasi kikubwa cha fedha bila kutumika katika utekelezaji wa miradi kunatokana na ucheleweshaji wa kutuma fedha katika halmashauri.
Deni la Serikali
Alisema hadi kufikia Juni 30, mwaka jana, deni la mifuko ya hifadhi ya jamii lilikuwa limefikia Sh1,699 milioni na Sh975.1 milioni zilipaswa kuwa zimereshwa, lakini hadi wakati wa kuandika ripoti hiyo zilikuwa bado hazijalipwa.
Alishauri mifuko na Serikali kuzingatia na kufuata mwongozo wa uwekezaji wa fedha za mifuko ambao pamoja na mambo mengine, unatoa ukomo wa aina za mali ambazo mifuko inaweza kuwekeza.

Monday 18 May 2015

UCHAGUZI UPINZANI 2015: Anna Mghwira, Mwenyekiti ACT- Wazalendo

Historia yake
Anna Mghwira ni Mwenyekiti wa kitaifa wa chama kipya cha siasa, ACT – Wazalendo. Alizaliwa Januari 23, 1959 katika hospitali ya Mkoa wa Singida, Kata ya Mungumaji, Kitongoji cha Irao Manispaa ya Singida Mjini. (Januari mwaka huu alitimiza miaka 56).
Baba mzazi wa Anna alikuwa diwani na kiongozi wa Tanu kabla ya CCM hadi mwaka 1985, mama yake alijishughulisha na kilimo na ufugaji na wazazi hawa kwa ujumla walipata watoto tisa, akiwamo Anna.
Mgwira alianza safari ya kielimu katika Shule ya Msingi Nyerere Road mwaka 1968 – 1974 akaendelea na sekondari kwenye Shule ya Ufundi Ihanja kati ya mwaka 1975 – 1978 kabla ya kuhitimisha masomo ya juu ya sekondari (kidato cha V na VI) Lutheran Junior Seminary kati ya mwaka 1979 – 1981.
Aliendelea na masomo ya chuo kikuu mwaka 1982 baada ya kujiunga Chuo Kikuu cha Thiolojia (Chuo Kikuu cha Tumaini) na kuhitimu Shahada ya Thiolojia mwaka 1986.
Mwaka huohuo, alijiunga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kusomea shahada ya Sheria.
Kati ya mwaka 1987 – 1998, aliendelea na shughuli za ujenzi wa Taifa, akifanya kazi ndani na nje ya nchi na kupata uzoefu mkubwa.
Safari ya elimu ya Mghwira ilikamilikia Chuo Kikuu cha Essex, Uingereza ambako alianza Shahada ya Uzamili ya Sheria (LLM) mwaka 1999 na kutunukiwa mwaka 2000.
Licha ya kuwa mwanasheria na mtheologia aliyebobea, pia amefanya kazi za maendeleo kwa muda mrefu na ana uzoefu katika uendeshaji wa Serikali za Mitaa, utumishi katika mashirika ya kimataifa, kitaifa na mashirika ya dini ambamo amejihusisha na masuala ya wanawake, watoto, wakimbizi, utawala na haki za binadamu.
Mghwira ana historia ya kupenda siasa, masuala ya jamii na michakato ya maendeleo kama inavyojidhihirisha katika maandiko yake mbalimbali katika majarida na magazeti ya hapa ndani ya nchi.
Alianza siasa tangu wakati wa Tanu akiwa mwanachama wa Umoja wa Vijana wa Tanu (Tanu Youth League) na aliwahi kushinda tuzo mbalimbali kutokana na ushiriki wa juu katika Tanu lakini baadaye ilipoanzishwa CCM alipunguza ushiriki wake ili ajipe muda katika masomo na baadaye ndoa na malezi ya watoto.
Kwa kipindi kirefu, hakuwa anajihusisha na siasa hadi alivyoamua kujiunga na Chadema mwaka 2009 ambako alishika nafasi mbili tu za uenyekiti wa baraza la wanawake  ngazi ya wilaya na katibu wa baraza la wanawake mkoa.
Machi mwaka huu alijiunga rasmi na ACT – Wazalendo na katika Mkutano Mkuu wa kwanza wa chama hicho, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kwanza wa ACT.
Aliolewa na Shedrack Maghwiya tangu mwaka 1982 na walibahatika kupata watoto watatu wa kiume: Fadhili, Peter na Elisha. Hata hivyo, kwa bahati mbaya, mumewe hivi sasa ni marehemu.
Mbio za ubunge
Mghwira alijitosa katika mbio za ubunge kwa mara ya kwanza Januari 2012 baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kutangaza uchaguzi mdogo katika Jimbo la Arumeru Mashariki baada ya kifo cha Solomon Sumari.
Alishiriki kura ya maoni ndani ya Chadema akihitaji kupewa ridhaa. Hata hivyo, chama hicho kilimpitisha Joshua Nassari (Josh) na Mghwira alikuwa na kazi ya kuendelea kumuunga mkono hadi ushindi ulipotangazwa kwa chama hicho.
Pia, amewahi kugombea ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki, kupitia Chadema japokuwa hakuchaguliwa kushikilia wadhifa huo.
Mbio za urais
Mghwira hajatangaza kuwa atagombea urais. Ila, tafiti kadhaa na maoni ya Watanzania zinaonyesha kuwa yeye ni miongoni mwa viongozi wa kisiasa ambao wamejipambanua hivi karibuni na kuonyesha uwezo mkubwa katika uwanja wa kisiasa na hivyo anapewa nafasi kubwa kuwa anaweza kupewa majukumu makubwa na anaweza kuyahimili.
Nguvu yake
Jambo la kwanza linalompa nguvu mwanamama huyu ni umahiri katika elimu. Yeye ni msomi nguli wa masuala ya sheria lakini ana shahada tatu za vyuo vikuu. Nchi yoyote ingependa pamoja na sifa nyingine, iongozwe na Rais ambaye elimu si kikwazo kwake. Kwa nchi kama Tanzania ambayo mfumo dume umewakandamiza wanawake kwa kipindi kirefu, Mghwira anakuwa mmoja wa wanawake wachache wenye uwezo mkubwa.
Kwa sababu Mghwira ni mwanamke imara na anayepambana kwa muda mrefu sasa. Kitendo tu cha yeye kuwa mwanamke ni baraka tosha kwa siasa za kisasa ambazo zinaanza kuchangamkia, kukubali na kutafuta mchango wa wanawake katika nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa. Jinsia yake inampa fursa ya kuendelea kuaminiwa zaidi katika jamii ambayo inazidi kupoteza imani na uaminifu wa wanaume.
Lakini nguvu ya tatu ya Mghwira ni uthubutu. Ameniambia kuwa hata alipoingia katika ndoa bado alithubutu kujiendeleza kielimu bila kuchoka. Alipambana na changamoto za ndoa na shule. Wanawake wengi huchagua kufanya jambo moja na kuacha mengine, yeye alikwenda nayo yote na kuyakamilisha salama. Uwezo na uthubutu huu vinamfanya kuwa mwanamama imara anayeweza kukabidhiwa uongozi wa taasisi kubwa.
Mghwira ni mtu wa kuhoji kila jambo, si mwanamama “Ndiyo Mzee”. Wakati natafuta maoni ya watu waliowahi kufanya naye kazi katika Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, mtendaji mmoja aliniambia kuwa ukimpa Mghwira kazi ya harakati iliyo kwenye maandishi, hataondoka kwako hadi umpe taarifa za kina za kila jambo na atakuhoji hadi utachoka.
Hata mtaalamu mshauri wa chama hicho Profesa Kitila Mkumbo ameniambia kuwa wakati wanafanya marekebisho ya katiba ya chama cha ACT walikabidhi kazi hiyo kwa jopo maalumu la wataalamu akiwemo Mghwira.
Profesa Kitila ananiambia kuwa kwa kiasi kikubwa katika timu hiyo, Mghwira ndiye aliyehoji na kutoa mapendekezo ya masuala mengi kuliko hata wataalamu wengine wa sheria ambao walikuwa wanaume.
Nilipojaribu kumfikia Mghwira kwa ajili ya kupata taarifa zake za kina na maisha binafsi, nilijikuta nashushiwa maswali matano mfululizo kiasi kwamba nilirudi kujipanga na kumtafuta tena. Huyu ni mwanasiasa wa kisasa ambaye anahoji kila jambo lililoko mbele yake, sifa hii wanaikosa wakuu wengi wa nchi.
Pamoja na kuwa na elimu kubwa, uzoefu wa kutosha wa kukaa nje ya nchi na kufanya kazi na taasisi za kitaifa na kimataifa, Mghwira ni mwanamama wa kawaida sana. Watu wa karibu naye wanamtaja hivyo. Si mtu wa kupoteza muda na mambo yasiyo na tija, anapenda kuandika makala za kuelimisha jamii, kufanya kazi na jamii na kujitolea na kujichanganya na wananchi wasio na uwezo na wenye kuhitaji msaada. Sifa zote hizi ni nguvu muhimu kwa binadamu yeyote ambaye anahitaji uongozi mkubwa wa nchi.
Udhaifu wake
Udhaifu mkubwa nilioubaini na hata kujulishwa na watu wa karibu naye ni kuwa yeye ni mwanasiasa mpole sana. Nimeambiwa kuwa ni mpole kupita kiasi na mara nyingi huwa anakuwa msikilizaji mzuri kabla hajaanza kuhoji mambo mfululizo. Moja ya sifa muhimu za Rais ajaye ni uwezo wa kuwa mpole na mkali kutegemeana na mazingira.
Kiwango cha upole cha mwanamama huyu kinazidi kiwango cha ukali alionao na naliona kama ni jambo linalopaswa kufanyiwa kazi kwa sababu Taifa letu lilipofikishwa, mara kadhaa nimesisitiza kuwa tunahitaji kiongozi anayeweza kumudu hali zote mbili.
Lakini udhaifu wa pili mkubwa wa Mghwira ni kutojijenga kisiasa ndani ya nchi. Katika siasa, bado namuona kama mchanga, hajakomaa na kuwa na uwezo mkubwa kiasi cha kujipa jina kubwa kwa jamii.
Mchango wake katika jamii ni mkubwa kwa sababu amewahi kusimamia masuala mengi ya kijamii na kisheria yanayoonekana, lakini ninachokisema hapa ni kuwa, chama chochote kile kina jukumu la kusimamisha kiongozi ambaye anajulikana katika tasnia za siasa. Kutojijenga na kuwa juu tokea alipokuwa Chadema nakuchukulia kama udhaifu ambao anahitaji kuufanyia kazi.
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Kama ACT - Wazalendo kitampitisha mwanamama huyu kuwa mgombea urais wa chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, sababu ya kwanza ya kufanya hivyo inaweza kuwa ni ile dhana ya kumpa mwanamke nafasi.
Chama anachotoka ndicho peke yake kimeweza kumpa mwanamke nafasi ya juu ya uongozi, nadhani pia bado chama hicho kinaweza kumpa jukumu kubwa zaidi ya hilo kwa sababu tayari kimeshajijengea misingi ya kuwajenga kina mama.
Lakini ikiwa Mghwira atapitishwa, uzoefu wake kimataifa na katika masuala ya haki za binadamu na kushughulika na masuala ya kijamii kunaweza kuwa moja ya sababu.
Mwanamama huyu amefanya kazi mbalimbali za kitaaluma na kijamii hapa Tanzania, Sweden, Marekani, Uingereza na nchi nyingine za Afrika. Amekuwa mwalimu wa vyuo vikuu hapa Tanzania na msimamizi wa miradi mbalimbali ya kitaifa ya mashirika ya ndani na nje ya nchi. Uwezo na uelewa wake vinampa fursa ya juu ya kuteuliwa kugombea urais na kuonyesha kuwa kina mama wanaweza ikiwa wanapewa fursa sawa na wanaume.
Nini kinaweza kumwangusha?
Dhana ileile ya kijinsia inayombeba, pia ndiyo inayoweza kumuangusha. Ikiwa ACT kitadhani kuwa vyama vingine washindani vitasimamisha wagombea wanaume imara ambao wanaungwa mkono na mfumo dume uliotawala nchi hii, chama hicho kinaweza kumuweka nje Mgwira na kutafuta mwanachama mwingine “mwanamume” ambaye atakuwa na fursa ya kupambana na wanaume wengine kutoka vyama vingine na kuangaliwa na jamii “ambayo kwa kiasi kikubwa bado inatawaliwa na wanaume”.
Lakini jambo la pili linaloweza kumwangusha ni ugeni wake katika masuala ya kisiasa. Kama nilivyoeleza, Mghwira hana uzoefu wa uongozi wa juu wa kisiasa katika vyama, nadhani nafasi aliyonayo ndani ya ACT - Wazalendo ndiyo inayompa uzoefu wa kwanza wa siasa za kitaifa.
Lakini uzoefu wa jumla unaonyesha kuwa vyama mbalimbali hapa Tanzania huteua wagombea urais wake miongoni mwa wanachama wazoefu au wale waliowahi kushika madaraka muhimu katika chama kwa muda mrefu. ACT ikipiga hesabu hizi inaweza kabisa kumuweka nje mwanamama huyu.
Asipochaguliwa (Mpango B)
Ikiwa hatapewa fursa ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama chake, anaweza kuwa na mipango mitatu mezani:
Mpango wa kwanza ni kugombea ubunge katika jimbo mojawapo Tanzania. Bahati nzuri nimejulishwa kuwa moja ya majimbo anayojipanga kugombea ni pale Singida. Ikiwa ndivyo basi, mpango huu unaweza kumfaa kwa maana ya kuzidi kujifunza na kupata uzoefu wa siasa za Tanzania kwa upana.
Lakini mpango wa pili ni kuendelea kufundisha vijana katika vyuo vikuu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri kwa wanafunzi na wa kisheria katika jamii. Katika masuala haya ana uzoefu mkubwa nayo na itakuwa tu ni kiasi cha kuendelea pale alipoishia.
Nadhani mpango wa tatu ni kuendelea kuongoza chama cha ACT - Wazalendo. Nimeambiwa kuwa uongozi (Uenyekiti wake) unapaswa kuisha Februari, 2020. Ikiwa ndivyo nadhani ana fursa njema ya kuendelea kufanya uongozi.
Hitimisho
Mgwira ni mwanasiasa na kiongozi wa chama kipya ambacho kimeanzishwa na wanachama wengi waliotoka Chadema. Safari yake kisiasa na hata ugombeaji wa nafasi nyingine kubwa za nchi kwa namna moja au nyingine, lazima utaathiriwa na ustawi au uzorotaji wa Chadema.
Ikiwa Chadema kitazidi kukubalika kwa Wwatanzania na kuwa chama kinachoimarika zaidi kuishinda ACT, ndiyo kusema kuwa yeye na wenzake watakuwa na wakati mgumu kujipambanua kisiasa na hivi ndivyo siasa za Afrika hutizamwa.
Pamoja na sintofahamu hizo, namuona Mgwira kama mmoja wanasiasa watulivu na wenye maono mapana katika Taifa hili. Kwa maneno yake yeye mwenyewe amenieleza kuwa “Natamani siku moja nchi hii iongozwe kwa misingi ya udugu na kusaidiana, kwa misingi ya malezi ya maadili bora kama alivyofanya Mwalimu Nyerere. Mimi nimekulia kwenye familia kubwa sana lakini wazazi wetu walitulea sote kama ndugu na tuliishi kwa furaha kubwa, nina ndoto kuwa Tanzania ijayo ipite katika njia hiyo.”
Ninachoweza kusema kwa sasa ni kumwombea mama huyu nguli wa upinzani na kumtakia safari njema katika nia zake za kisiasa ikiwamo hii ambayo ametajwa kwamba ana sifa za kuongoza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ni Mchambuzi wa Masuala ya Kisiasa na Kijamii; ana uzoefu mkubwa wa uongozi wa kisiasa hapa Tanzania. Ana Cheti cha Juu cha Sarufi na Lugha, Shahada ya Sanaa (B.A) katika Elimu (Lugha, Siasa na Utawala), Shahada ya Uzamili ya Utawala na Uongozi (M.A) na ni mwanafunzi wa fani ya sheria (LLB) – Anapatikana kupitia +255787536759.

Urais wawagonganisha NCCR-Mageuzi, Chadema

Dar es Salaam. Chama cha NCCR-Mageuzi kimeponda kauli ya Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu kwamba Katibu mkuu wa chama hicho kikuu cha upinzani, Dk Willibrod Slaa ndiye atakayekuwa mgombea urais kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Akiwa kwenye mkutano wa hadhara wa Chadema mjini Moshi, hivi karibuni, Lissu alikaririwa akieleza kuwa Dk Slaa, ndiye atakayepitishwa na Ukawa kugombea nafasi hiyo.
Lakini Mkuu wa Idara ya Kampeni na Uchaguzi wa NCCR-Mageuzi, Faustine Sungura aliliambia gazeti hili mwishoni mwa juma kuwa ni makosa kudhani kwamba Chadema ndicho chenye nafasi ya kusimamisha mgombea urais kupitia Ukawa, wakati bado mchakato wa kumpata mgombea haujafanyika.
Sungura ambaye pia ni miongoni mwa waasisi na mwanzilishi wa mageuzi nchini, alisema kati ya vyama vinne vilivyounda Ukawa, tayari Chadema imepewa majimbo mengi ya ubunge. “Fursa hiyo pekee imeshawapa uwezekano wa kutoa waziri mkuu kama upinzani utashinda”, alisema.
“Kwa kawaida chama chenye wabunge wengi ndicho kinachotoa waziri mkuu, sasa kwa namna yoyote Chadema ndiyo itakayotoa waziri mkuu, hivyo haiwezekani watoe na mgombea urais. Nawashauri wachague nafasi mojawapo,” alisema Sungura.
Sungura alisema kauli hiyo ya Lissu siyo sahihi na hailengi kujenga Ukawa, bali kuubomoa kwa kuwa haiwezekani chama kimoja kitoe rais, makamu wake na waziri mkuu. “Ni vizuri ikaeleweka mapema kwamba, haiwezekani chama kimoja kati ya vyama vinne washirika wa Ukawa, kikatoa mgombea urais, makamu na waziri mkuu,” alisema Sungura  na kuongeza:
“Kwa kuwa CUF kina nafasi kubwa ya kumtoa mgombea urais wa Zanzibar, vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema na NLD, kimoja kati ya vyama hivyo kitamtoa ama rais au waziri mkuu au spika wa Bunge, kinyume chake ni tamaa inayoweza kuua Ukawa.”
Kwa mujibu wa Sungura, mageuzi chanya hayawezi kuletwa kwa ubinafsi, bali nia ya dhati ya Ukawa katika kuyatafuta.

Asimamishwa kazi kwa kumtumia JK ‘meseji

Moshi. Mhasibu wa Hospitali ya Rufaa KCMC, Paul Mhumba amesimamishwa kazi kwa tuhuma za kutuma ujumbe wa simu ya mkononi (sms) kwa Rais Jakaya Kikwete.
Kuvuja kwa ujumbe huo na nambari ya simu iliyotuma, kumeibua hisia tofauti kuhusu usiri wa ofisi ya Rais katika kushughulikia malalamiko nyeti ya wananchi na kuwaweka njiapanda watoa habari za siri.
Mhumba, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Afya na Serikali Kuu (Tughe) Tawi la KCMC anadaiwa  na Menejimenti ya KCMC kuwa ndiye aliyetuma ujumbe huo.
Katika barua yake ya Mei 5, yenye kumbukumbu PF.4515/22, KCMC ilidai uchunguzi umebaini kuwa Mhumba ndiye mtumaji wa ujumbe huo.
“Uongozi umepokea taarifa iliyotumwa mwishoni mwa Aprili na mwanzoni mwa Mei mwaka huu kwa njia ya ujumbe wa simu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Jakaya Kikwete,” ilidai.
KCMC imedai katika barua hiyo, taarifa hiyo ya sms ilibeba ujumbe unaohusiana na matumizi mabaya ya fedha za hospitali hiyo unaofanywa na baadhi ya viongozi na Shirika la Msamaria Mwema (GSF).
Mbali na tuhuma hizo, lakini pia KCMC inadai taarifa hiyo ilimweleza Rais kuwa KCMC na GSF linalomiliki hospitali hiyo, zinajitosheleza kwa mapato, hivyo hakuna haja kwa Serikali kuendelea kuipatia ruzuku.
Pia, menejimenti imedai taarifa hiyo ilidai wafanyakazi wa KCMC wanatumikishwa kama watumwa, hivyo ni maombi yao (watumishi) Serikali ilegeze masharti ili ajira zao zichukuliwe na Serikali.
“Uchunguzi umeonyesha kuwa taarifa hiyo (kwa Rais), umeituma kwa kutumia simu ya kiganjani ambayo ulikabidhiwa kama mojawapo ya zana ya kuleta ufanisi katika majukumu yako,” imedai.
Mei 8, KCMC ilimwandikia barua Mhumba yenye kumbukumbu PF.4515/28 iliyotiwa saini na Profesa Raimos Olomi ikimjulisha kuwa amesimamishwa kazi kuanzia Mei 8 hadi Mei 14.
Katika barua hiyo, Profesa Olomi alidai menejimenti imepokea taarifa ya kutofanyika kwa kikao cha kamati ya nidhamu baada ya Mhumba kumkataa mwenyekiti kutokana na kukosa imani naye.
Pia, kikao hicho hakikufanyika baada ya Mhumba kuomba kamati hiyo iahirishwe kwa sababu mwakilishi wake hakuwapo na kikao kingine kupangwa Mei 15.
Hata hivyo, bado mhasibu huyo hajarejeshwa kazini na vikao vilikuwa vinaendelea kuhusu hatua za kinidhamu zinazostahili dhidi yake.
“Wakati hayo mambo mawili yanafanyiwa kazi, menejimenti imeamua kukusimamisha kazi. Kabla hujaondoka unatakiwa ukabidhi vitendea kazi pamoja na simu ya mkononi uliyokabidhiwa,” imedai.
Ofisa Uhusiano wa KCMC, Gabriel Chisseo alipoulizwa kuhusu sakata hilo alisema kwa nafasi yake, hawezi kulizungumzia.
Mhumba alipotafutwa wiki iliyopita, alikiri kusimamishwa kazi kwa tuhuma za kumtumia Rais ujumbe wa simu ya mkononi, ingawa alikanusha kuhusika.
“Maudhui hayo kama ni kweli yalitumwa, hayana matatizo. Nimeongea na katibu mkuu kumuuliza kama alipokea sms kutoka kwa Rais na kuwapa KCMC na namba ya mtumaji amekanusha,” alidai.
Hata hivyo, alidai yeye akiwa mwenyekiti wa Tughe, amekuwa akionekana kama adui pale anapojaribu kutetea masilahi ya watumishi, likiwamo suala la kutopandishwa daraja tangu mwaka 2007 hadi 2015.
“Ni kweli, watumishi hawajapandishwa madaraja tangu 2007. Sisi (Tughe) tumekuwa tukilipigania kwa sababu linachangia wastaafu kulipwa pensheni ndogo,” alisema.
“Mimi kama kiongozi wa wafanyakazi, niko tayari kupeleka ushahidi kwa mambo ambayo Tughe tumekuwa tukipambana nayo, ikiwamo mahali zilipo fedha za mashine ya CT-Scan,” alisema Mhumba.
Tawi la Tughe KCMC, limemwandikia barua katibu mkuu wa Tughe, ikiomba Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama aingilie kati suala hilo ili haki itendeke.
Gama alipoulizwa kuhusu suala hilo, alikiri kupigiwa simu na Mhumba akimueleza lakini alimshauri aziandikie mamlaka husika.
Gama alisema akiwa mwakilishi wa Rais mkoani Kilimanjaro, atachunguza nini kimetokea baada ya kupata malalamiko rasmi kutoka kwa Mhumba au Tughe yenyewe.