Dar es Salaam. Wasomi wameonyesha wasiwasi wao juu ya mazungumzo
kati ya Rais Jakaya Kikwete na vyama vya siasa vya upinzani vyenye
wabunge, kuhusu tofauti zilizojitokeza katika Muswada wa Sheria ya
Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.
Wasomi hao licha ya kuunga mkono mazungumzo,
wamesema wanasiasa wana kawaida ya kuwa na agenda za siri jambo ambalo
baadaye huzusha tena mzozo, huku wakirejea kwamba si mara ya kwanza kwa
Rais Kikwete kufanya mkutano wa aina hiyo.
Kauli hizo zimetokana na Rais Kikwete kukutana na
viongozi wa vyama vya siasa; CCM, Chadema, CUF, NCCR Mageuzi, TLP na UDP
kukubaliana kuweka pembeni tofauti za kiitikadi na kutanguliza masilahi
ya taifa katika mchakato wa kuandikwa kwa Katiba Mpya.
Mhadhiri Mstaafu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam
(UDSM), Dk Azavery Lwaitama alisema uamuzi wa Rais Kikwete ni mzuri
lakini unaweza ukawa umechezwa kwa karata ya kisiasa.
Alifafanua, “Inaweza kuwa karata ya kisiasa kwa
sababu bado Bunge lina wabunge wengi wa CCM, pia marekebisho
yatasimamiwa na Waziri wa Katiba na Sheria, (Mathias Chikawe) sijui
kutakuwa na jipya gani.”
Lwaitama alisema ili mambo yaende sawa, Rais
Kikwete anatakiwa kuhakikisha kuwa marekebisho hayo yatakayofanywa nje
ya Bunge, hayabadilishwi tena bungeni. “Ahakikishe kuwa wabunge
wanapitisha tu yale ambayo yamerekebishwa nje ya Bunge.”
Naye Profesa Gaudence Mpangala wa UDSM alisema:
“Tutajua kama hili jambo limetulia ama la, kama Bunge likipitisha
mapendekezo mapya, kama ikiwa hivyo mambo yatakwenda vizuri.”
Hata hivyo, Profesa Mpangala alionyesha wasiwasi
wake kama wabunge wataamua kuyapinga mabadiliko hayo, huku akishauri
itumike njia ambayo itawafanya wabunge kukubaliana na kile
kilichojadiliwa nje ya Bunge.
Alisema Katiba nzuri ni lazima itokane na mwafaka wa pamoja na kwamba nia ya Rais Kikwete inapaswa kuendelezwa hadi bungeni.
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Bashiru Ally
alisema: “Siku zote mtu asiyejua anapokwenda hawezi kupotea njia,
mchakato wa Katiba Mpya una mgongano wa mtazamo kuna maswali mengi
kuhusu mchakato huu kuwa wa kisiasa na kisheria.
Alisema kuwa mchakato huo sasa haujulikani
unaendeshwa kwa masilahi ya nani, kwa sababu kila malalamiko mengi
yanayotolewa yamebebwa na vyama vya siasa.
“Tupo njiapanda, binafsi sina imani kubwa na mchakato huu, vyama vimeweka masilahi yao zaidi mbele,” alisema Bashiru.
Aliyekuwa Mbunge wa Monduli na Mkuu wa wilaya, Lepilal Ole
Moloimet alisema mtindo wa Rais Kikwete wa kuzungumza na wapinzani ni
mzuri kwa sababu unasaidia kuweka mazingira ya utulivu na maelewano
nchini.
Alisema utaratibu huo ni mzuri katika kuondoa
manung’uniko, hasa kwa wale ambao hawaridhiki na hali halisi ya mambo
yanavyokwenda nchini.
Naye Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape
Nnauye alisema atakuwa kwenye mazingira mazuri ya kuchambua mpango wa
Rais Kikwete kukutana na vyama vya upinzani, pindi mchakato ukikamilika.
“Bado ni mapema sana. Mazungumzo bado
hayajamalizika. Tusubiri yamalizike ndipo nitakapokuwa na nafasi nzuri
ya kuyazungumzia,” alisema Nape.
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Ntatiro alisema kwamba wanatarajia kutoa taarifa kuhusu mazungumzo hayo na Rais Kikwete.
Alisema mpaka sasa chama hicho bado hakina uhakika
kama kweli kilichoandikwa kwenye vyombo vya habari jana ndicho
kilichoafikiwa kwenye mazungumzo hayo.
Kwa upande wake Chadema kupitia kwa Ofisa wake wa Habari, Tumaini Makene nao walisema watatoa taarifa yao baadaye.
Makubaliano ya mkutano
Taarifa ya Ikulu juzi, ilisema Rais Kikwete na
viongozi hao walikubaliana vyama vyote vyenye mawazo, maoni na
mapendekezo ya kuboresha sheria hiyo, viwasilishe mapendekezo yao haraka
serikalini ili itafutwe namna ya kuyashirikisha katika marekebisho ya
sheria hiyo.
Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni
Wenyeviti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, Chadema, Freeman Mbowe,
NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula.
Katika hoja zao, wapinzani wanataka kuangaliwa upya kwa idadi ya wabunge wa Bunge Maalumu la Katiba, utaratibu wa
kupitisha Katiba Mpya kwenye Bunge Maalumu wakisisitiza kwamba kuwapo haki sawa kwa kila upande wa Muungano
Hoja nyingine ni ukomo wa Tume ya Mabaraza ya Katiba ambapo
viongozi hao walipendekeza kwa rais kuwa tume iendelee kuwapo hadi
Katiba Mpya itakapopatikana badala ya kuvunjwa mapema kabla ya Katiba
Mpya.
Hoja nyingine kuingizwa kwa mambo ambayo hayakujadiliwa wala kupitishwa na Bunge kwenye muswada huo, wakitoa mfano wa
kifungu kipya kinachompa Katibu wa Bunge na yule
wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, mamlaka ya kusimamia mchakato wa
kumchagua mwenyekiti wa muda wa Bunge.
Walisema pendekezo hilo ni jipya na kwamba halikuwepo kwenye muswada uliotolewa maoni na wadau.
No comments:
Post a Comment