Saturday 20 April 2013

Trafiki: Vigogo serikalini wanatuvuruga


Kamanda Mpinga aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake, ambapo alibainisha kuwa vigogo hao wamekuwa wakiingilia utendaji kazi wa askari wake hasa wanapokamatwa ndugu zao kwa kukiuka sheria.


Dar es Salaam. Kamanda wa Kikosi cha Usalama wa barabarani, Mohamed Mpinga amefunguka kwa kueleza anavyokwazwa na baadhi ya viongozi wa juu wa Serikali, wanavyokwamisha utendaji kazi wa askari wake.  
Kamanda Mpinga aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake, ambapo alibainisha kuwa vigogo hao wamekuwa wakiingilia utendaji kazi wa askari wake hasa wanapokamatwa ndugu zao kwa kukiuka sheria.
“Wapo wengi ambao husababisha Sheria za Usalama Barabarani kuvunjwa kwa makusudi na ndugu, jamaa au rafiki zao kwa kuwa watu hao mara wanapokamatwa, huwasiliana na vigogo hao kwa njia ya simu ambapo vigogo hao huanza kuwatisha askari wangu, pamoja na kuwalazimisha kutowachukulia hatua, “ alisema Mpinga.
Aliongeza:” Kwa kutambua hilo ndugu, jamaa na marafiki wa vigogo hao, wamekuwa wakikiuka sheria husika kusudi. Yaani mtu amegonga, unakuta kigogo anapiga simu kwamba asifunguliwe mashtaka, kwa kweli ni vyema kuongoza nchi kwa msingi wa sheria,” alisema Kamanda Mpinga huku akikunja uso kuonyesha kukerwa na jambo hilo.
Mpinga alisema hali hiyo ndiyo imesababisha nidhamu wanayopaswa kuwa nayo madereva barabarani kushuka hata kuamua kujiunga kwenye misafara ya viongozi mbalimbali, wakiwa na imani kwamba, hawawezi kuchukuliwa hatua kwa kuwa watakingiwa kifua na vigogo hao.
“ Nimewaeleza trafiki wote kuwa makini zaidi kwenye misafara, kwa sababu siku hizi hali imebadilika. Wawe wanajiangalia jinsi wanavyosimamia au kuongoza misafara wakizingatia na usalama wa maisha yao kwa jumla,” alisema Kamanda Mpinga.
“Hata hivyo, napenda kuwahakikishia kwamba nitasimamia sheria katika utendaji wangu wa kazi, simu ikipigwa kwangu sitoi ushirikiano wa aina hiyo. Nawasihi viongozi wenye tabia hizo waache kuingilia utendaji kazi wa askari, mtu anapita taa nyekundu inawaka akikamatwa lazima alipe faini,” alisema.
Aidha, alizungumzia kuhusu tuhuma zilizokuwa zikielekezwa kwa askari wake za kuwa na vitabu bandia vya kuandika adhabu, ambapo alieleza kuwa jambo hilo halina ukweli, huku akieleza kwamba vitabu vinavyotumika vilichapwa vingi mwaka 2011.
“Nimesikia tuhuma hizi, lakini nawahakikishia wananchi kwamba hazina ukweli kwa sababu baada ya kusikia nilifuatilia nikabaini hofu yao inatokana na mwaka kwa kuwa vitabu vingi vina GN 2057 2011 vilitolewa makao makuu ya polisi,” alifafanua Kamanda Mpinga.

Chadema wamtangazia vita Spika Makinda

Wabunge waliofukuzwa na Naibu Spika, Job Ndugai juzi ni pamoja na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, Mbunge wa Ilemela, Highness Kiwia, Mbunge wa Nyamagana, Ezekiah Wenje na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema.


Dodoma. Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe amesema kuwa watakata rufaa katika Kamati ya Kanuni ya Bunge dhidi ya mwongozo wa Spika uliobariki adhabu ya kuwatimua kwa siku tano wabunge sita wa Chadema kwa kudharau mamlaka ya Spika.
Akitoa mwongozo wake jana, Spika Anne Makinda alibariki wabunge hao kutimuliwa akisema kuwa Kanuni za Bunge zilikiukwa.
Wabunge waliofukuzwa na Naibu Spika, Job Ndugai juzi ni pamoja na Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, Mbunge wa Ilemela, Highness Kiwia, Mbunge wa Nyamagana, Ezekiah Wenje na Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema.
Juzi Mbowe aliomba mwongozo wa Spika kwa kutumia Kanuni ya 68 (7), akimtaka Spika aeleze naibu wake (Ndugai) alitumia kanuni gani ya Bunge, kuwasimamisha siku tano wabunge sita wa Chadema wasihudhurie vikao vya Bunge vinavyoendelea.
Mwongozo wa Makinda
Akitoa mwongozo huo jana, Spika Anne Makinda alisema kuwa kitendo kilichotokea hakiwezi kupuuzwa na wala kuvumiliwa na Bunge, pamoja na wananchi kwa kuwa ni utovu wa nidhamu ya Bunge na wananchi kwa jumla.
Alisema: “Kanuni ya 2(2) na 5(1), inampa mamlaka Spika ya kuleta amani bungeni.
Kanuni ya 2(2) inaeleza: “Iwapo jambo au shughuli yoyote haikuwekewa masharti katika kanuni hizi, Spika ataamua utaratibu wa kufuata katika jambo au shughuli hiyo, kwa kuzingatia Katiba, Sheria nyingine za nchi, kanuni nyingine zilizopo, maamuzi ya awali ya maspika wa Bunge na mila na desturi za uendeshaji bora wa shughuli za Bunge na uamuzi huo utaingizwa katika kitabu cha maamuzi ili kuongoza mwenendo wa baadaye wa uendeshaji wa shughuli za Bunge.”
Kanuni ya 5(1) inaeleza: “Katika kutekeleza majukumu yake yaliyotajwa katika Ibara ya 84 ya Katiba, Spika ataongozwa na kanuni hizi na pale ambapo kanuni hazikutoa mwongozo, basi Spika atafanya kazi kwa kuzingatia Katiba, Sheria nyingine za nchi, kanuni nyingine zilizopo, maamuzi ya awali ya maspika wa Bunge pamoja na mila na desturi za mabunge mengine yenye utaratibu wa kibunge unaofanana na utaratibu wa bunge la Tanzania.”
Makinda alisema kwa kutumia kanuni hizo mbili anakubaliana na uamuzi uliotolewa na Ndugai na kwamba suala hilo litaingizwa kwenye kitabu cha uamuzi wa Spika.
“Natumia Kanuni ya 2(2) na 5(1) kusema kuwa uamuzi uliofanywa na Ndugai ni halali na itaingizwa kwenye kitabu cha maamuzi ya Spika,” alisema Spika Makinda.
Kauli ya Mbowe
Mbowe jana alilieleza gazeti hili kuwa uamuzi wa Spika ulijielekeza katika jambo lisilo na kanuni inayolisimamia, tofauti na lile la kudharau mamlaka ya kiti cha Spika, lililotolewa maelekezo na Kanuni ya 74 (1).
Kanuni hiyo inasema: “Spika anaweza kutaja jina la mbunge kwamba amedharau mamlaka ya Spika na kisha kupeleka jina hilo kwenye Kamati ya Maadili na Madaraka ya Bunge; ikiwa kwa maneno au vitendo mbunge huyo anaonyesha dharau kwa mamlaka ya Spika; au Mbunge huyo atafanya kitendo chochote cha makusudi cha kudharau shughuli ya Bunge au mbunge yeyote anayeongoza shughuli hiyo.”

Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema alisema kuwa majibu ya Spika ni ya bahati mbaya kwa sababu yameonyesha mwendelezo wa kupuuza Kanuni za Bunge.
Akieleza kiini cha tatizo, Mbowe alisema kuwa ni kuyumba kwa kiti, upendeleo wa wazi, kupanga mikakati na CCM na kumpuuza Mnadhimu wa Chadema. Alisema nidhamu bungeni haitapatikana kwa kuwatimua wabunge na kwamba wapo tayari kwa hilo, hata kama wataisha wote, hadi pale Kiti cha Spika kitakapoacha upendeleo.
“Tutaliheshimu Bunge kama taasisi huru, lakini si lilivyo sasa kama taasisi ya CCM,” alisema Mbowe na kufafanua kuwa: “..Nje ya Bunge wote tunaheshimiana, lakini mambo yanakuwa tofauti bungeni kwa sababu ya Kiti cha Spika kutotenda haki.”
Alifafanua kuwa katika tukio zima, mbali na kupuuza kanuni, adhabu yenyewe ilitolewa nje ya utaratibu, ikiwa ni pamoja na kuruhusu askari wasiokuwa na sare kuingia bungeni.
“Bungeni pale kukiwa na siwa ni mahali patakatifu, lakini Naibu Spika ‘alipaniki’ akaruhusu watu wakatoka kusikojulikana bila sare na huo ni ukiukwaji wa taratibu,” alisema na kuongeza:
“Pale hata Makamu wa Rais ili aruhusiwe kuingia, lazima kanuni itenguliwe, watumishi wa Bunge na askari wanaoruhusiwa ndani, lazima wawe na sare maalumu, lakini mara hii Kiti cha Spika kimeruhusu watu wasiohusika kuingia.”
Alisema kwamba, Ndugai aliyaacha kando mambo ya msingi, akabakia kusema Tundu Lissu amesimama mara nyingi na kusahau kuwa mbunge huyo ni Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani, hivyo anaweza kusimama mara nyingi kadri ya mahitaji.
Alifafanua kuwa siku ya kufukuzwa kwa wabunge hao, Lissu alikuwa akitaka kuweka sawa kauli isiyokuwa sahihi ya Mwigulu Nchemba kuwa Dk Slaa hakufanya mkutano wa hadhara Singida wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka 2010, badala yake alifanya mkutano wa ndani ya viongozi wa dini.
Katika hatua nyingine, Frederick Katulanda, anaripoti kutoka Mwanza kuwa, wabunge watano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) waliosimamishwa kuhudhuria vikao vitano vya Bunge watafanya ziara katika mikoa mitano kwa ajili ya kuwaeleza wapigakura wa majimbo yao hali ya Bunge na upendeleo wa Spika wa Bunge , wanaoamini umesababisha wao kutimuliwa.
Akielezea ziara yao katika majimbo yao Mbunge wa Nyamagana, Ezekiah Wenje alisema kuwa wamefikia uamuzi huo ili kuwaeleza wananchi uonevu ndani ya Bunge na jinsi Spika na naibu wake wanavyoshindwa kusimamia kanuni kwa sababu ya kuwalinda CCM na Serikali.
Wenje alisema kwamba ratiba yao itaanzia katika Mkoa wa Mwanza, ambapo watafanya mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Sahara na kwamba wabunge wote watano watakuwapo kueleza yaliyowakuta bungeni.

Darasa la saba sasa kujiunga vyuo vikuu



Udahili huo utakaoanza mwaka huu wa masomo 2013/14, utakuwa ukiwahusisha wale ambao elimu yao imeishia darasa la saba na kuendelea, lakini walikosa sifa ya kuendelea na masomo kwa ngazi ya chuo kikuu.

Dar es Salaam. Tume ya Vyuo Vikuu Nchini (TCU), imepanga kuanza kuwadahili wanafunzi wa kujiunga na masomo ya vyuo vikuu kwa kutumia uzoefu wao.
Udahili huo utakaoanza mwaka huu wa masomo 2013/14, utakuwa ukiwahusisha wale ambao elimu yao imeishia darasa la saba na kuendelea, lakini walikosa sifa ya kuendelea na masomo kwa ngazi ya chuo kikuu.
Kupitia utaratibu huo mpya, mtahiniwa atajiunga na Chuo Kikuu kulingana na fani atakayoiomba na atatakiwa kufanya mitihani mitatu na kufaulu kwa wastani wa daraja B.
Mkurugenzi wa Ithibati na Ubora wa Elimu ya Juu kutoka TCU, Dk Savinus Maronga aliliambia gazeti hili kuwa baada ya kuona kuna watu wengi wanaopenda kuendelea na masomo ya elimu ya juu, lakini wameshindwa kutokana na kutokuwa na vigezo, TCU imeamua kuanzisha mitihani hiyo maalumu.
Alisema kuwa mfumo huo unaojulikana kama ‘Recognition of Prior Learning’ (RPL), utamwezesha mwombaji kudahiliwa vyuoni kupitia tume hiyo kama wanavyofanya watahiniwa wengine.
Sifa zinazotakiwa
Kuhusu sifa za kujiunga, Dk Maronga alisema kuwa mwombaji anatakiwa kuwa na umri kuanzia miaka 25 na kuendelea, sambamba na kuwa na elimu isiyopungua darasa la saba.
“Mwombaji anatakiwa kuwa na nia ya kujiunga na elimu ya chuo kikuu na uzoefu wa kile ambacho anakusudia kukisoma.
Awe na uwezo wa kuandika na kusoma Lugha ya Kiingereza, ambayo ndiyo inayotumika kufundishia vyuoni,”alisema Dk Maronga na kuongeza:
“Kuna watu wameishia darasa la saba, lakini wamefanya kazi katika eneo moja, mfano karani wa mahakama, mwandishi wa habari kwa muda mrefu. Hivyo mfumo huu utawawezesha kuendelea na masomo bila tatizo.”
Vigezo
Mkurugenzi huyo alisema, kutakuwa na mitihani ya masomo matatu, ambayo mtahiniwa ili apate nafasi ya kuendelea na masomo ni lazima afaulu kwa wastani wa daraja B.
Alisema daraja la kwanza linaloanza na alama A ni 75-100, daraja B+ ni 60-75, B ni 50-59, C ni 40-49, D ni 35-39 na daraja E ni 0-34.
“Katika mitihani mitatu atakayoifanya, atatakiwa kupata wastani wa daraja ‘B’ na somo husika la fani yake atatakiwa kupata alama B ili kuwa na vigezo vya kupata cheti kitakachomwezesha kuendelea na masomo yake,”alisema Dk Maronga.

Alibainisha kuwa mitihani itakayokuwa ikitumika kudahili watahiniwa itakuwa ni wa somo la Kiingereza na Hisabati utakaokuwa na alama 30.
Mtihani wa Pili utakuwa na alama 30 ambao ni mtihani wa Maarifa na wa tatu utakuwa na alama 40, utakaokuwa ukitokana na fani husika ya mwombaji.
“Mfano mtahimiwa anataka kusomea sheria au uandishi wa habari, atatakiwa kufaulu kwa asilimia 50 somo husika, hivyo endapo atakosa kupata asilimia 50 ya somo lake hatapata cheti kitakachomwezesha kuendelea na elimu ya juu,”alisema Dk Marango na kuongeza:
“Cheti tutakachompatia mtahiniwa kitakuwa halali kwa kipindi cha miaka mitatu na baada ya hapo mwombaji atatakiwa kufanya upya mitihani hiyo.”
Viambatanisho
Kutokana na maelezo ya TCU, mwombaji anatakiwa kuambatanisha cheti cha kuzaliwa au hati ya kusafiria,wasifu wake pamoja na vyeti vya ushiriki mzuri kutoka sehemu anayofanyia kazi.
Vingine ni nakala za vyeti vya taaluma, picha ndogo ‘passport size, nakala za vyeti vya taaluma za masomo ya hapo awali, ripoti ya tathmini ya utendaji kazi wake kazini kwa walioajiriwa kutoka kwa mwajiri na nakala ya kozi za awali alizokwishafanya.
Vituo vya Mitihani
Mkurugenzi huyo alisema mitihani itafanyika kati ya Mei na Juni mwaka huu katika vituo vinne vilivyoandaliwa katika vyuo.
Alisema kuwa chini ya mfumo huo Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), kitahusika na masuala ya Elimu huku Chuo Kikuu Tumaini Makumira cha Dar es Salaam (TUMADARCo) kikihusika na Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma.
Chuo cha Kilimo Sokoine (SUA), kitahusika na Kilimo na Wanyamapori wakati Chuo Kikuu cha Mzumbe (MU) kitahusika na masuala ya usimamizi na utawala,uhasibu, sheria na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT).
“Kwa kuwa ndiyo tunaanza, tumeamua kutenga vituo vinne, lakini mwakani tunatarajia kuongeza viwe vingi ili kukidhi mahitaji ya wananchi walio wengi,”anasema Dk Maronga.

Monday 15 April 2013

Raila, Kalonzo waenda Ikulu kwa Rais Uhuru










Lengo ni kufahamiana na kujadiliana kuhusu masuala ya nchi ya Kenya.
Nairobi. Vigogo wa Muungano wa Demokrasia na Mageuzi (Cord) wa Kenya, Raila Odinga na Kalonzo Musyoka wamerudi kutoka nchini Afrika Kusini na kumtembelea Rais Uhuru Kenyatta.
Ujio huo wa Odinga kwa mujibu wa msemaji wake, Dennis Onyango lengo lilikuwa  kufahamiana na kujadiliana masuala muhimu ya nchi.
Katika maongezi yao na Rais Kenyatta viongozi hao wa Muungano wa Cord walisema kwamba watahudhuria sherehe za kufunguliwa kwa Bunge la 11 nchini humo.
Akidhibitisha mbele ya waandishi wa habari taarifa za kuhudhuria sherehe hizo za kufunguliwa kwa Bunge hilo kwa viongozi hao Onyango alisema kwamba hayo ni makubaliano kati ya Uhuru na viongozi hao.
Alisema viongozi hao pia walijadiliana kuhusu namna  ya kukabili masuala yatakayowasilishwa bungeni kwa mtazamo wa kuridhiana.
Kwa sasa Muungano wa Jubilee unaounda serikali unamiliki mabunge yote mawili, huku maspika Justin Muturi na Ekwe Ethuro wa Bunge la Taifa na  la seneti mtawalia wakiwa wa Jubilee. Kwa hivyo, inatarajiwa kwamba ingawa Muungano wa Cord utakuwa upinzani kwa Serikali, hautakuwa na uwezo wa kupinga masuala muhimu.
Kwa upande wake Rais Kenyatta na Naibu wake  William Ruto waliahidi kuhakikisha kwamba upinzani unakua wa maana katika mabunge yote mawili na kwa Serikali kwa jumla.
“Walisema ni hamu yao kuona vyama vidogo vya upinzani vikitekeleza jukumu lao la kuiangalia Serikali ii isikiuke mipaka katika utendakazi wake,” alisema  Onyango.
Odinga alienda katika eneo Bunge la Khwisero kaunti ya Kakamega, ambapo alimwambia Rais Kenyatta asinunue wabunge wa Cord kuunga mkono upande wa Serikali.

Sh1 bilioni za kuzika viongozi zawakera wabunge




 Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola akichangia mjadala wa  Hotuba ya makadirio ya fedha katika Ofisi ya Waziri Mkuu,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa mwaka wa fedha 2013/14 ambapo alitamka kutounga mkono makadirio hayo. Picha na Edwin Mjwahuzi 

Ni zilizotangazwa kutengwa kupitia Hotuba ya  Waziri Mkuu.
Dodoma. Serikali ya Rais Jakaya Kikwete imelaumiwa kwa kutenga Sh1 bilioni kwa ajili ya maziko ya viongozi huku Watanzania wengi wakilia na umaskini mkubwa.
Shutuma hizo zilitolewa mwishoni mwa wiki bungeni kwa nyakati tofauti wabunge akiwamo wa  Viti Maalumu Lucy Owenya (Chadema) na Kangi Lugola (Mwibara-CCM) wakati wakichangia hotuba ya makadirio ya bajeti katika Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2013/14.
Katika mchango wake Owenya alisema inatia aibu kuona kiasi kikubwa cha fedha kikitengwa kwa ajili ya maandalizi ya kuzika viongozi huku mambo muhimu na ambayo ni kipaumbele yakiachwa.
“Ni aibu na fedheha kubwa, hivi mmetenga kiasi hicho kwani mnajua nani atakufa na lini atakufa ndio maana mnajiandaa kumzika,” alihoji Owenya.
Mbunge huyo alikwenda mbele zaidi na kueleza kuwa Serikali imeshindwa kufikiri na hasa namna ya kuwaondolea umasikini na tabu wanazopata wananchi wake lakini inawaza habari za watu wanaojiandaa kufa.
Vile vile katika mchango wake Lugola ambaye alisema asingeunga mkono hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu, alihoji sababu za kutengwa kwa fedha hizo bila kujua nani atakufa lini.
Mbali na hilo, Owenya pia aliilaumu Ofisi ya Waziri kwa kushindwa kutumia mbinu mbadala za kuzuia matumizi makubwa ya fedha za walipa kodi zinazotumiwa na wakuu wa mikoa kwa ajili ya kwenda Dodoma kufuatilia hotuba ya Waziri Mkuu.
Alimtaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuwatimua wakuu wa mikoa ili warudi mikoani kwao ili kuokoa fedha za walipa kodi zinazoteketea katika misafara yao mjini Dodoma.

Sunday 14 April 2013

Spika asipuuze ushauri wa CAG



SPIKA wa Bunge, Anne Makinda hivi karibuni alizifanyia mabadiliko kamati za kudumu za Bunge, huku Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ikiunganishwa na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC).
Ikumbukwe kuwa kamati hizi za uangalizi wa mashirika ya umma ziliundwa wakati wa uongozi wa Spika Samuel Sitta na kuwapa wapinzani waziongoze.
Kwa kipindi chote cha uhai wa kamati hizo, kwa kweli zilijitahidi kufanya kazi ya kufuatilia kwa ukaribu fedha za serikali ambazo zimekuwa zikifujwa hovyo bila utaratibu wa wazi.
Katika hatua ambayo haikutarajiwa, Spika Makinda alibadili utaratibu wa mtangulizi wake Sitta na hivyo akazivunja baadhi ya kamati na kuunda nyingine huku akiziunganisha POAC na PAC.
Lengo la Sitta lilikuwa ni kuongeza uwajibikaji wa serikali na ndiyo maana Bunge liliridhia kamati hizo tatu yaani Kamati ya Mashirika ya Umma (POAC), Kamati ya Serikali za Mitaa (LAAC) na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) ziongozwe na upinzani.
Uamuzi wa Spika Makinda kuziunganisha kamati za POAC na PAC umelalamikiwa na wengi akiwemo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovic Uttouh wakidai kila moja ilikuwa na majukumu makubwa ambayo hata hivyo hawakuyakamilisha, hivyo kuziunganisha ni kuwatishwa majukumu wajumbe wake.
Hata hivyo, wapo wanaoutazama uamuzi huo kama msukumo wa kisiasa wa Serikali ya CCM kujaribu kukibana chama kikuu cha upinzani bungeni na hivyo kutengeneza utaratibu huo kuwapunguzia madaraka.
Hivi karibuni CAG ameweka bayana kuwa kamati mpya ya PAC inahitaji muujiza wa Mungu kukamilisha kazi zake. Kwamba haiwezi kufikia nusu ya kazi zake za mwaka.
Alisema kabla ya kamati hizo kuunganishwa, POAC ilikuwa na mzigo mzito na sasa umeongezwa, ambapo katika hali ya kawaida itashindwa kufanya kazi ya kuisimamia serikali.
Hatupaswi kupuuza ushauri wa CAG. Huyu ni mtaalamu anayejua masuala ya fedha yalivyo na ugumu wake, hivyo kupendekeza kwake Kamati ya POAC irejeshwe kuna mantiki.
Ni wazi kuwa Spika wa Bunge alikurupuka pasipo kusikiliza mawazo ya wabunge katika uundwaji wa kamati mpya, vinginevyo kusingekuwa na manung’uniko haya tunayoyasikia leo.
Kosa hili la kuifuta kamati muhimu kama POAC kwa malengo ya kisiasa tu, ni tafsiri kwamba viongozi wetu hawajali maslahi ya watu na taifa kwa ujumla.
Tunaamini kuwa Spika wa Bunge kwa mamlaka aliyonayo ataufanyia kazi ushauri wa CAG kwa manufaa ya taifa letu ili kuokoa fedha za umma zisipotee holela.

Saturday 13 April 2013

Muuza dawa za kulevya aliyeishia kukatwa mkono, mguu



Hata baada ya kuhamia Uswis bado maisha yanaendelea kuwa magumu.Alijikuta akiandamwa na majanga zaidi.
Mbembele anaendelea na simulizi yake, anasema mwishoni mwa mwaka 1999 alifanikiwa kuhamia nchini Uswizi, alijiandikisha kama mkimbizi kutoka Msumbiji.
Hali ilivyokuwa nchini Uswizi
“Nilivyofika Uswizi, nilipelekwa moja kwa moja kwenye kambi ya wakimbizi iliyokuwapo jimbo la Debendorf katika Jiji la Zurich, nilijitambulisha kama John ‘Chuma’ Fernando kutoka Msumbiji.
Alipokelewa vizuri na maofisa wa uhamiaji na kupewa chumba kilichokuwa na mahitaji muhimu ya maisha ya mtu wa kawaida.
“Nilianza maisha mapya katika kambi hiyo, nilikutana na wazamiaji wengi kutoka nchi za Afrika mashariki na kati kama Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Demokrasia ya Kongo,” anasema na kuongeza.
“Maisha yalikuwa mazuri kwa sababu tulikuwa tunapewa kiasi cha dola 600 kila mwezi pamoja na mahitaji na huduma nyingine kama za michezo na cha kufurahisha zaidi tulikuwa huru kufanya mambo yetu”.
“Baada ya maisha ya miaka mitatu kambini pale ilitokea kampeni ya kuwarudisha watu waliokuwa na mazingira mazuri nchini mwao kutokana na kuporomoka kwa uchumi katika nchi za Ulaya”
“Kiongozi wa kambi yetu ‘Shefa’ alisikia taarifa halisi za uraia wangu kuwa ni Mtanzania na akaamua kufikisha taarifa hizo kwa maofisa wa uhamiaji ambao walinipeleka kwa Balozi wa Msumbiji kwa mahojiano,” anabainisha na kuongeza;“Nilifikishwa kwa Balozi wa Msumbiji, nilifanya naye mahojiano kuhusu uraia wangu, baadaye alinishtukia kutokana na kutokuongea vizuri kireno”
Anasema baada kushtukiwa na balozi alimueleza kuwa yeye ni Mmakonde wa Msumbiji ambaye hakubahatika kwenda shule ndiyo maana hakuweza kuongea Kireno kwa Ufasaha.
“Nilimwambia natokea Mweda mji wa Msumbiji unaopakana na Tanzania ambapo watu wake walikuwa wanaongea Kimakonde mchanganyiko na Kireno kama mimi”
Mbembele anaongea kwa kuonyesha ushujaa wa kumshinda balozi katika maongezi kwa kumdanganya “Balozi alinibembeleza nirudi msumbiji lakini nilikataa kwa kudai kuwa sababu nilizoondokea kule bado hazikutatuliwa”.
“Baada ya maongezi, balozi alishindwa kutafuta sababu ya kuniruidisha Msumbiji hivyo nikaendelea na maisha ya ukimbizi pale Dubendorf,”anasimulia kuwa wakati akishangilia ushindi wa kumdanganya balozi kumbe alikuwa ameshawekwa katika kitabu cha watu watukutu na wenye makosa.
Matukio ya ushirikina na jaribio la kutolewa sadaka
Baada ya kushinda jaribio la kurudishwa nyumbani Mbembele anasema chuki ilizidi baina yake na baadhi ya raia wa Kenya waliokuwapo kambini hapo na kumtengenezea mazingira magumu ya kuishi.
“Nilikosa rafiki, nilihisi kila mtu ni adui yangu. Sikuwa na chakufanya zaidi ya kumuomba Mungu na kuendelea na maisha kwa kuwa raia wengi walikuwa wanarudishwa makwao kwa wingi”.

Anasema siku moja akiwa matembezini alikutana na wazungu watatu ambao walikuwa wanaelekea katika sherehe kubwa ya utamaduni wa Waswizi ambayo hujumuisha toleo la sadaka ya damu ya binadamu.
“Kule Uswizi tarehe 1 Agosti kila mwaka huazimishwa sherehe ya nchi nzima, baadhi ya wenyeji husherekea na kutoa sadaka ya damu kwa miungu na mizimu yao,” anabainisha Mbembele na kuongeza;
“Wale watu watatu walinibembeleza tukashirikiane nao katika sherehe hizo mpaka nikakubali kuandamana nao huku tukitembea taratibu kuelekea katika msitu mkali uliopo ndani ya milima iliyopo pembezoni mwa mji”
Huku akionyesha dalili za kusisitiza uwepo wa uchawi uliopitiliza huko Uswizi, Mbembele anasema “Wanasema Tanzania kuna uchawi, aaah uchawi Ulaya bwana”
“Tulipoingia katikati ya poli tukielekea katika viwanja maalumu vya sherehe hizo, mtu mmoja kati ya wale watatu alibadilika ghafla akawa kama sokwe mkubwa mwenye meno ya kutisha kiasi cha kunitisha na kufanya niishiwe nguvu” anasema na kuongeza kuwa jambo hilo lilimtisha mno na kumkosesha raha.

KONA YA SHERIA:Unachotakiwa kufahamu kuhusu ndoa kisheria



Kutokana na sheria ya ndoa ya Mwaka 1971, ndoa inatafsiriwa kuwa ni muungano wa hiari baina ya mwanaume na mwanamke, muungano unaokusudiwa kudumu kwa muda wote wa maisha yao.
Kutokana na tafsiri hiyo kuna mambo makuu matatu yanayotiliwa mkazo na tafsiri hiyo. Kwanza muungano huo lazima uwe wa hiari yaani usitokane na kushurutishwa ama na mzazi au mtu yeyote yule.
Ikiwa wawili hao watakuwa wamelazimishwa kufunga ndoa, basi ndoa hiyo haitakuwa ndoa kwa mujibu wa tafsiri ya ndoa katika sheria ya ndoa ya mwaka 1971.
Wapo ambao wakati mwingine unaweza kuona kwa mfano mzazi au mlezi anamlazimisha kuoana na fulani kwa sababu zake, ndoa kama hiyo kisheria sio haki na mwenye kulazimishwa anaweza kuamua akipenda kuachana na aina hiyo ya ndoa. Jambo la msingi ni kuhakikisha anayelalamika anakuwa ana ushahidi kwa kile ambacho analalamikia, kwa mfano anaweza kueleza namna alivyolazimishwa.
Ni kweli inawezekana fulani anafaa kuwa na mwanao, kisheria inashauriwa kutomlazimisha, badala yake lililo la msingi ni kushauri, kisha mtu mwenyewe aamue.
Pili ndoa lazima iwe muungano wa watu wawili na ni lazima watu hao wawe wa jinsia mbili tofauti yaani mwanaume na mwanamke. Kwa maana hiyo ndoa ya watu wa jinsia moja yaani mwanaume na mwanaume au mwanamke na mwanamke haitambuliki katika sheria ya ndoa ya mwaka 1971.
Siku hizi kuna watu wameanza kuja na mambo ya ndoa za jinsia moja, hizo ni aina ya ndoa ambazo kwa mujibu wa sheria za Tanzania hazikubaliki.
Tatu ni uhusiano huo uwe wenye kukusudiwa kudumu kwa muda wote. Lengo la kufunga ndoa ni ndoa hiyo idumu kwa kwa kipindi chote cha maisha ya wanandoa. Ndio kusema kwamba hakuna ndoa za mikataba, ya kusema labda mtaishi kwa muda fulani, kwa mfano mwaka mmoja.
Ndoa inayofungwa ikiwa na lengo ya kuvunjwa baada ya kipindi fulani si ndoa halali kwa mujibu wa sheria ya ndoa ya mwaka 1971.
Ndoa itavunjwa ikiwa kutabainika/kutajitokeza mambo yanayoweza kupelekea ndoa kuvunjika kama inavyobainishwa kwenye sheria ya ndoa na si vinginevyo.
Kuna baadhi ya watu ambao wamekuwa wakikaa tu bila kuangalia namna gani wanaweza kuzingatia sheria za ndoa.Kwa mfano wapo watu ambao wamekuwa wakiishi tu, huku wao wakifikiri kwamba kuishi kwao kunatosha kuifanya ifahamike kama ndoa.
Kisheria ni kwamba kuna taratibu zake za kuzingatiwa ili watu wafahamike kama wanandoa.Kukubali kuishi tu bila kuzingatia taratibu za kisheria kunaondoa maana halisi ya ndoa hasa kwa mfano watu wenyewe wanapokuwa hawako tayari kuzifuata taratibu hizo.
Aina Za Ndoa
Kutokana na sheria ya ndoa ya mwaka 1971, ndoa zimemegawanyika katika aina mbili ambazo ndoa ya mke mmoja ambapo huhusisha mume mmoja na mke mmoja.
Aina ya pili ni ndoa ya wake wengi ambayo mume mmoja anakuwa na wake zaidi ya mmoja, waweza kuwa wawili ama zaidi kulingana na vile ambayo wahusika wenyewe wataona inafaa au kulingana na imani zao za dini, hata hivyo ni lazima kuwepo na makubaliano.

Chadema yatishia kujitoa mchakato wa Katiba Mpya

Dodoma na Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitajitoa katika mchakato wa Katiba Mpya endapo mambo muhimu mawili hayatapatiwa ufumbuzi hadi kufikia Aprili 30, mwaka huu.

Wakati Chadema wakisema hayo, Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), limesema uchaguzi wa wajumbe wa Mabaraza ya Katiba uliomalizika siku tatu zilizopita katika maeneo mbalimbali nchini haukuwa huru na ni batili, huku likipendekeza urudiwe katika maeneo yote yaliyokumbwa na kasoro.

Katika hoja zake, Chadema kimesema kinataka kufutwa kwa uteuzi/uchaguzi wa wajumbe wa Mabaraza ya Wilaya ya Katiba uliofanywa na Kamati za Maendeleo za Kata na badala yake wajumbe wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya wachaguliwe moja kwa moja na wananchi wa Kata husika bila kuchujwa na Kamati za Maendeleo za Kata (WDC).
Msimamo huo ulitolewa na Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe wakati akisoma hotuba yake ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2013/14 huku akiitaka Serikali kuwasilisha muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba ili maeneo kadhaa yafanyiwe marekebisho.

“Katika Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Katiba tunataka marekebisho ya vifungu vyote vinavyohusu uwakilishi katika Bunge Maalumu la Katiba wa taasisi zilizoainishwa katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba,” alisema Mbowe na kuongeza:
“Pia vifungu vyote vinavyohusu ushiriki wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutoka Zanzibar katika mijadala inayohusu mambo yasiyokuwa ya Muungano.”

Jukwaa la Katiba
Kwa upande wake, Jukwaa la Katiba limesema Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatakiwa kubadili mwenendo wake kuanzia katika utaratibu wa kuwapata wajumbe hao hadi uundwaji wa Bunge la Katiba na wananchi kupiga kura za maoni. Limesema isiporekebisha utaratibu huo, litakwenda mahakamani kusitisha mchakato mzima wa Katiba.

Kumalizika kwa uchaguzi huo kunaashiria kuanza kwa mabaraza ya Katiba Mei mwaka huu, ambayo yatakuwa yakijadili rasimu ya Katiba ambayo imetokana na maoni mbalimbali yaliyotolewa na wananchi.

Mwenyekiti wa Jukata, Deus Kibamba alisema uchaguzi huo ulikuwa na kasoro zaidi ya 15, ambazo ni itikadi za vyama na udini, rushwa, uchakachuaji, upendeleo, ubaguzi wa makundi ya watu wenye ulemavu na kukosekana kwa mwongozo timilifu wa uchaguzi huo.

Baadhi ya mikoa iliyokumbwa na kasoro hizo ni Dar es Salaam, Arusha, Mara, Singida na Dodoma. “Pia kulikuwa na vurugu katika uchaguzi huu, kukataliwa kwa barua za maombi za baadhi ya waombaji, kutokuwa na tarehe rasmi ya uchaguzi, uandikishaji bandia wa wapigakura, kukosekana kwa orodha ya majina ya wagombea katika mitaa na vijiji.”

Je hii ndiyo njia ya kujenga ajira kwa vijana wanaomaliza vyuo vikuu?

Serikali imekataa ushauri wa wabunge na kusema kuwa itaendelea kuwaajiri wastaafu mbalimbali nchini hadi hapo soko la ajira litakapojitosheleza.
Mbali na hilo, jana Serikali ilitangaza bungeni kuwa kazi za wakuu wa mikoa siyo ajira rasmi, bali ni ajira za kisiasa ambazo hazipaswi kuhesabiwa.
Akijibu swali bungeni jana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma) Celina Kombani, alikiri kuwa bado Serikali inaendelea kutoa ajira kwa watu ambao wamestaafu na kuwa itaendelea kufanya hivyo kwa siku za usoni.
Alikuwa akijibu swali la Vicent Nyerere (Musoma-Chadema) ambaye alitaka kujua Serikali ina mpango gani wa kusitisha kutoa mikataba kwa wastaafu ili wahitimu wanaotoka vyuoni wapate ajira na kujenga nchi yao.
Mbunge huyo pia alihoji nafasi za wakuu wa mikoa nchini ambao wengi hufanya kazi wakiwa katika umri mkubwa, huku baadhi wakiwa wamestaafu utumishi wa umma. Waziri alisema ni kweli kuwa wako wataalamu wengi wanaohitimu vyuo vikuu hapa nchini ambao wanahitaji kuingia katika soko la ajira, lakini hupatiwa ajira kulingana na uwezo na bajeti ya Serikali.
Kuhusu wastaafu kuendelea kupewa ajira, alisema “Hilo linatokana na utaalamu walionao ambao ni vigumu kuziba nafasi zao kwa kipindi cha haraka.”
Kombani alizitaja kada ambazo Serikali inatoa mikataba kwa wastaafu kuwa ni walimu, waganga, wahandisi na wahadhiri wa vyuo ambao

Tuesday 9 April 2013

Hatua za dharura kutumika kudhibiti dawa za kulevya Zanzibar













Zanzibar. Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema Serikali italazimika kuchukua hatua za dharura katika kukabiliana na wafanyabiashara wa dawa za kulevya nchini.
Alisema wafanyabiashara hao wamekuwa wakiwatumia vijana kwa ajili ya kununua na kusambaza dawa za kulevya, bila ya kuzingatia athari zitokanazo na biashara hiyo haramu ambayo pia huzorotesha maendeleo ya kiuchumi kwa taifa.
Maalim Seif alieleza jhayo jana ana katika hafla ya ufunguzi wa kampeni ya kupunguza matumizi ya dawa za kulevya na athari zake shuleni, iliyofanyika Shule ya Sekondari ya Lumumba.
Alisema hatua za dharura ni lazima zitumike katika kuwashughulikia wafanyabiashara hao, vyenginevyo taifa litaendelea kuangamia kutokana na matumizi makubwa ya dawa za kulevya.
Alifahamisha kuwa wafanyabiashara wa dawa za kulevya wamekuwa wakijali zaidi maslahi yao, na kuamua kuwatumia vijana kuendeleza biashara na matumizi ya dawa hizo, jambo ambalo halikubaliki kwa mustakbali wa Zanzibar.
Aliwahadharisha vijana kuwa makini na wafanyabiashara hao na kutokubali kutumiwa katika biashara hiyo. Ufunguzi wa kampeni hiyo iliyoandaliwa na “Sober Houses” chini ya ufadhili wa Hoteli ya “Double Tree Tanzania”, ulikwenda sambamba na uzinduzi wa chapisho maalum la kitabu ambacho kitatumika kufundishia shulen

Serikali yarudisha viboko shuleni





Kadhalika alisema Serikali imepiga marufuku matumizi ya simu za mikononi kwa sababu baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakizitumia vibaya jambo ambalo linawarudisha nyuma kimasomo.



Mpoki Bukuku, MWananchi
Serikali imesema itarudisha adhabu ya viboko kwa wanafunzi shuleni ili kujenga nidhamu na kujituma.Akizungumza Dar es Salaam jana wakati akizindua tovuti ya www.shledirect.co.tz inayowezesha wanafunzi kujisomea kwa njia ya mtandao, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo ilisema kuondolewa kwa adhabu ya viboko shuleni kumewafanya wanafunzi wengi kukosa nidhamu na wakati mwingine kujifanyia mambo kienyeji.

“Wasipotandikwa mambo hayaendi, nilipokuwa mwalimu mkuu nilikuwa nawatandika kweli ndiyo maana shule yangu ilikuwa ikiongoza Mkoa wa Mbeya hivihivi hawaendi...” alisema huku akishangiliwa na wageni waalikwa.

Alisema watoto wa siku hizi wamekuwa wakitumia vibaya teknolojia ambayo ingeweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika masomo yao... “Tovuti kama hiyo ingewasaidia kwa masomo, lakini wao wanakimbilia kwenye facebook na mambo mengine yasiyofaa.”

Aliyalaumu mashirika yasiyo ya kiserikali na haki za binadamu ambayo yamekuwa yakipigania kuondolewa kwa adhabu hiyo shuleni na kusababisha kushuka kwa nidhamu kwa kiasi kikubwa.

Kadhalika alisema Serikali imepiga marufuku matumizi ya simu za mikononi kwa sababu baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakizitumia vibaya jambo ambalo linawarudisha nyuma kimasomo.
“Simu tunazipiga marufuku, mwalimu akimkuta mwanafunzi na simu amnyang’anye ndizo zinatuharibia taifa letu.”

Aliwapongeza wabunifu wa mtandao huo akisema ni wazalendo kwani wamekuwa msaada katika jitihada za Serikali kukuza elimu nchini.

“Watu wanapiga kelele Mulugo na Kawambwa wajiuzulu, hata tukijiuzulu haitasaidia, bali kila Mtanzania atoe mchango wake katika elimu ili kuweza kuiendeleza.”
Mwanzilishi wa tovuti hiyo, Faraja Nyalandu alisema itakuwa na manufaa kwa wanafunzi wa Tanzania kwani masomo yanayotolewa yanaandaliwa na walimu wazoefu wenye shahada hivyo wanafunzi watakapoitumia watapata manufaa makubwa.

Maoni ya wadau
Akizungumzia hatua hiyo ya Serikali, Waziri Kivuli wa Elimu Mafunzo ya Ufundi, Suzan Lyimo aliitaka iache kuangalia mambo madogo ambayo yanachangia kwa kiasi kidogo tu kudorora kwa elimu na kuacha mambo makubwa.

“Kuna mambo makubwa zaidi yaliyotufikisha hapa tulipo, hii ni sawa na kushughulika na matawi na kuacha mizizi. Lazima tuangalie suala hili kwa upana zaidi, kuna ripoti nyingi na nzito hazijafanyiwa kazi mpaka sasa badala yake Serikali inaibuka na kuanza kutangaza vitu vidogo kama hivyo, wafanyie kazi kwanza ripoti ambazo zilitumia pesa nyingi za walipakodi kwani nyingi zina mapendekezo mazuri.”

Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Mpwapwa, Rukonge Mwero alisema uzuri wa adhabu ya viboko ni kwamba haipotezi muda”

Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Helen Kijo Bisimba alisema adhabu ya viboko haina maana katika kipindi hiki akisema wanafunzi wanapaswa kupewa adhabu ambazo zinawafundisha kama zile za kufanya usafi na kazi mbalimbali.

“Viboko havifundishi zaidi ya kumpatia mwanafunzi maumivu na kusababisha aichukie shule. Waelimishwe kwa kuelekezwa lakini wakiendelea kukiuka, wapewe adhabu za kufanya kazi mbalimbali.

Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Gratian Mukoba alisema walimu hawapati faida yoyote kuwachapa au kutowachapa viboko wanafunzi.
  “Hawa viongozi kila kukicha wanazungumza mambo yasiyo na maana, badala ya kuzungumzia masilahi ya walimu wanazungumza kuhusu viboko, hatuelewi wakiamka kesho watasema nini,” alisema Mukoba.

Monday 8 April 2013

Uhuru! Uhuru! Kesho ‘hakunaga’ Kenya


















Kesho kuapishwa akiwa ameshikiwa biblia na mke wake kama ilivyokuwa kwa Obama
Nderemo ,shamra shamra ,na vifijo za kuapishwa kwa Rais wa awamu vya nne nchini Kenya  zitasikika kesho katika Uwanja wa mpira wa Arap Moi.
Kesho Rais mteule wa Kenya,  Uhuru Kenyatta anatarajiwa kuapishwa baada ya kushinda uchaguzi mkuu wa nchi hiyo uliofanyika Machi 4 mwaka huu.
Uhuru anachukua nchi hiyo akiwa ni rais wa nne ambapo awali alitanguliwa na baba yake mzazi   Jomo Kenyatta aliyeongoza kuanzia mwaka 1964 mpaka 1978, kisha akafuata mzee Arap Moi  na Mwai Kibaki.
Kuapishwa kwa Rais huyo kulichelewa kutokana na kufunguliwa kwa kesi na mpinzani wake  Raila Odinga ambaye alipinga matokeo hayo kwa kubaini kulikuwa na udanganyifu.
Lakini hata hivyo pingamizi hilo halikufua dafu kwani mahakama ilimuidhinisha Kenyatta kuwa ndiye mshindi halali nchini humo.
Baada ya mahakama ya juu kutoa uamuzi huo ,kwa upande wake Raila Odinga alikubali yaishe kwa kusema kwamba alishatoa ahadi ya kukubaliana na uamuzi wa mahakama.
Uhuru alishatamka wiki iliyopita  kwamba wakati wa kuapishwa hataapa kwa kuinua Biblia bali atasaidiwa na mkewe kama alivyoapishwa Rais Obama wa Marekani.
Akidhibitisha hilo Mkuu wa Majeshi ya Kenya (KDF) Jenerali Julius Karangi alisema  kuwa Kenyatta aliomba kwamba mkewe Margaret Kenyatta amshikie Biblia atakapokuwa akiapishwa.
“Hili ni ombi la rais mteule na itakuwa vyema tukubali ombi lake katika siku hii ya kihistoria,” alisema Jenerali Karangi.
Kenyatta ataweka  tu mkono wake wa kushoto juu ya Biblia ikishikiliwa na mkewe, katika kile anachotaja hatua ya kuachana na mtindo wa awali wa kuapisha marais wa Kenya wakiinua Biblia.
Kesho  Rais Mwai Kibaki atamkabidhi katiba Mpya Kenyatta, ambayo ilianza kutumika mnamo Agosti 2010. Mtindo huu utakuwa wa kwanza tangu nchi hiyo kupata Uhuru.
Sherehe hiyo itafanyika katika Uwanja wa Michezo wa Moi Kasarani, ambapo pia Naibu wa Rais William Ruto ataapishwa.
Shughuli hiyo inatarajiwa kumalizika saa 7.45. Kamati ya Mamlaka ya Ofisi ya Rais tayari ina ratiba ya mpangilio wa shughuli hiyo.
Utaratibu uliowekwa ni kwamba  wageni watasimama  pindi Rais Kibaki anayeondoka madarakani atakaowasili, pia itapigwa  saluti na mizinga 21.
Kenyatta atapambwa kwa vifaa vya mamlaka ambavyo ni pamoja na Mkuu wa Nakshi (CGH), pia atapokea mkuki, ngao na katiba.
Zana hizo zinaashiria mamlaka; kwa mfano Katiba inasimamia Kenya na watu wake, mkuki unasimamia Amiri Jeshi Mkuu ilhali CGH ni heshima kubwa zaidi Kenya.
Mkuki huo ni ule ule uliopitishwa kutoka kwa Hayati Mzee Jomo Kenyatta hadi kwa Rais Mstaafu Daniel Moi, kisha kwa Rais Kibaki na sasa atakabishiwa  Kenyatta.

Kalonzo aaga kwa sherehe
Wakati kesho Uhuru akijiandaa kuapishwa kuwa Rais mpya wa nchi hiyo, Makamu wa Rais anayeondoka madarakani Kalonzo Musyoka aliandaa sherehe kubwa nyumbani kwake kwa lengo la kuwaaga wafanyakazi wenzake.
Wafanyakazi hao wakiongozwa na wakuu wa idara mbali mbali waliandaliwa chakula maridadi kabisa kikisindikizwa kwa hotuba  zenye kuvutia za kumsifia kiongozi huyo.
Kiongozi huyo alisifiwa  kutokana na uongozi wake bora katika wizara hiyo na akiwa msaidizi mkuu wa rais.
Kwenye hotuba yake makamu wa Rais  huyo aliyeandamana na mkewe Pauline Kalonzo, aliwapongeza wafanyakazi wote wa wizara hiyo kutokana na ushirikiano wao akisema kwamba kujitolea kwao kutoa huduma kuliiletea sifa wizara hiyo.

Tuesday 2 April 2013

Maghorofa 100 Dar feki, Serikali ina kigugumizi

 Kwanini Serikali haichukui hatua kwa majengo hayo 100 yaliyobainika kuwa hayajajengwa kwa kuzingatia viwango? Wenye akili timamu wanaweza kuendelea kujiuliza maswali mengi zaidi na kujibu wanavyoweza.


Dar es Salaam.
Kuporomoka jengo lililopo Mtaa wa Indira Gandhi Jijini Dar es Salaam, huenda ikawa mwanzo tu wa kuporomoka majengo mengine zaidi hasa kufuatia matokeo ya tume iliyoundwa mwaka 2006 iliyobaini zaidi ya majengo 100 Jijini Dar es Salaam yamejengwa bila kuzingatia viwango.
Kwanini Serikali haichukui hatua kwa majengo hayo 100 yaliyobainika kuwa hayajajengwa kwa kuzingatia viwango? Wenye akili timamu wanaweza kuendelea kujiuliza maswali mengi zaidi na kujibu wanavyoweza.
Wapo wanaoweza kusema rushwa ndio inasababisha mambo mengi kutofanyiwa kazi kwa ufasaha, lakini mbele ya sheria utaombwa utoe ushahidi, hapo bila shaka patafanya wengi kubadili maneno kwamba aaah labda Serikali inaendelea kufanya mchakato, mpango mkakati, mkakati yakinifu nk dhidi ya majengo hayo.
Kubomoa jengo lenye ghorofa 16 au hata chini au zaidi ya hapo baada ya kulibaini halijazingatia viwango, ni lazima uwe na uso mgumu. Baadhi ya wananchi wanasema wenye majengo bila shaka hawawezi kutulia wakisubiri sheria ifanye inachotakiwa kufanya, hapo ndipo ugumu unapoanzia.
Pinda analo na kujibu
Baadhi ya watu wanafikiri kuondolewa madarakani kwa viongozi walio katika wizara husika na sakata hili akiwemo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye ofisi yake ilichunguza na kubaini maghorofa zaidi 100 kuwa ni feki, kunaweza kuwa ni mojawapo ya mambo muhimu kwa sasa.
Mke na watoto wafukiwa
Licha kwamba jengo hilo liliporomoka saa 2.30 asubuhi, baadhi ya watu waliofukiwa na kifusi cha jengo hilo walikuwa wakiwasiliana na jamaa zao kwa njia ya simu na wengine wakipiga kelele za kuomba msaada.
Idd Baka ambaye alikuwa akiwasiliana na mkewe ambaye aliegesha gari huku ndani kukiwa na watoto wake wawili alikwenda dukani kununua bidhaa, mara jengo hilo likaporomoka, alikuwa akiwasiliana nae hadi majira ya mchana simu ya mke wake haikuwa inapatikana.
Vifaa duni
Ni dhahiri kwamba endapo kungekuwapo na vifaa vya kutosha katika zoezi la uokoaji lingewezaa kufanikiwa kwa  muda mfupi na kwa kiasi kikubwa hivyo kuwapata majeruhi wakiwa hai.  
Katapila latumika
Cha  ajabu na aibu kwa taifa kutokuwa tayari kwa kuwa na vifaa vya kuokolea kwani tangu saa 2:30 hadi ilipofika saa 4.30 ndipo lilipatikana katapila moja ambalo nalo halikuwa na tija kutokana na kuwapo kwa uwezekano wa kuwakandamiza au kuwajeruhi zaidi  watu waliofukiwa na kifusi hicho.
Kutokana na kutokuwepo na vifaa vya kukatia nongo waokoaji iliwachukua takribani dakika 15 kukata nondo zilizokuwa zimemkandamiza.
Umati wa watu ulivamia kifusi na kuanza kukisomba kwa mikono  ili hali jambo hili lilikuwa kama mchezo wa kuigiza ambao umegharimu uhai wa watu zaidi ya 35 pamoja na kuharibu magari yaliyobondwa na kuwa kama chapati takribani matano.
Mashuhuda
Ali Mparang’ombe mmoja wa mafundi wa jengo hilo anasema kudondoka kwa jengo hilo ni mtiririko wa majengo mengine kutokuwa katika viwango vinavyotakiwa.


“Ndugu yangu mimi ni fundi nilikuwa nimeingia ndani, lakini nilitoka kwenda upande wa pili kutafuta chai kwani leo (Ijumaa iliyopita) ni sikukuu mama lishe hawakuwepo wengi hapa”anasimulia Mparang’ombe na kuongeza:
“Ndipo kwa kule nilisikia kishindo kikubwa, kuja kuangalia ni jengo nililotoka takribani dakika 15 tu limeanguka, nimepoteza watu muhimu sana ambao tulikuwa tukifanya sote kazi, sasa sijui itakuwaje”.
Mparang’ombe anasema jengo hilo lilikuwa likijengwa chini ya viwango kwani katika ndoo 12 za mchanga walikuwa wakichanganya saruji mfuko mmoja.
Majengo mengi feki
“Hapa kama kama ndoo 12 mfuko mmoja wa saruji unategemea nini, na ni majengo mengi hapa mjini ambayo yamejengwa kwa aina hii, hivyo ni kudra za Mwenyezi  Mungu zinahitajika”anasema Mparang’ombe.
“Jengo hili lilipofika ghorofa ya 12 lilisimamishwa kujengwa na ghorofa ya 15 lilisimamishwa tena lakini hatujui alikuwa anatumia njia gani hadi akawa anaruhusiwa kuendelea na ujenzi,” anasema.
Kibali cha jengo lililoanguka
Naibu Meya wa Halmashauri ya Ilala, Kheri Kessy alisema mwaka 2007 walitoa kibali kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kushirikiana na ‘Aliraza Investment Limited’ kujenga jengo la ghorofa 10.
Alipotakiwa kueleza kwa nini hawakuchukua hatua baada ya kuendelea kujengwa hadi kufikia ghorofa zaidi ya 10,  alisema hawahusiki, ila kuna taasisi zingine za Serikali zinazosimamia majengo zinatakiwa kuulizwa.
Matokeo ya tume yanapuuzwa
Mwaka 2006 Tume iliyoundwa na aliyekuwa Waziri Mkuu Edward Lowassa ilibaini kuwa zaidi ya maghorofa 100 yaliyopo jijini Dar es Salaam yalikuwa chini ya viwango.
Idadi hiyo ni tone tu la maghorofa yaliyo chini ya viwango nchi nzima ambayo bila shaka kuyabomoa ugumu unakuja pale wamiliki wake kuwa vigogo na wafanyabiashara mashuhuri.
Hali kadhalika akiwa bungeni wakati wa majumuisho ya Ofisi yake Bungeni mwaka 2008/09, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alisema ofisi yake ingechukua hatua za makusudi dhidi ya majengo ili kuzuia vifo kama hivi visivyo vya lazima. Kufumbia macho mambo ndiko leo kumesababisha watu zaidi ya 35 kuuawa, achilia mbali mali zingine yakiwemo magari.

Jamii:Kwanini Tanzania haiendelei haraka

Ombaomba wa India wanafanya jambo kukushawishi kumsaidia.Kwa mfano nikiwa katika mitaa ya New Delhi, nilikutana na ombaomba, walianza kunichezea muziki na michezo mingine, kabla ya kunisogelea na kuomba

 
New Delhi, India. Hivi karibuni nilikuwa nchini India, ni baada ya kuwa nimechaguliwa kati ya waandishi pekee wawili kutoka Tanzania, kuungana na waandishi wengine 16 kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa ajili ya mafunzo na pia kuripoti mkutano baina ya India na nchi za Afrika, uliofanyika Jijini New Delhi.
Zaidi ya New Delhi, nilitembelea pia miji mingine kama vile Noida, Agra, Mumbai na kadhalika. Ninachoweza kusema ni kuwa kuna mambo mengi ambayo Tanzania inapaswa kujifunza kutoka India. India ni taifa linalokua haraka, wapo ombaomba lakini hata ukizungumza nao unakuta ‘wanafikiri  tofauti’ na sisi;wana tofauti kubwa na wa hapa nchini.
Tofauti ya ombaomba wa Tanzania na India
Ombaomba wa India wanafanya jambo kukushawishi kumsaidia.Kwa mfano nikiwa katika mitaa ya New Delhi, nilikutana na ombaomba, walianza kunichezea muziki na michezo mingine, kabla ya kunisogelea na kuomba.
Mtoto mwenye mmoja mwenye umri wa miaka nane hivi, alijichora uso kama paka usoni, hakika utatamani kumwangia maana anachekesha. Japo si wote wanaofanya kitu kabla ya kuomba, wengi ni wabunifu.
Hata nilipotembelea katika miji mingine, ikiwemo Mumbai bado niliendelea kubaini ubunifu wa watu hawa, kule nilikutana kwa mfano na dada mmoja aliniita akanifunga ua mkono wa kulia, nikawa nafikiri ni kama ‘karibu mgeni’…kule alikuwa ni ombaomba, baadae alianza kuniomba fedha.Haina maana kwamba ombaomba ni kazi nzuri, ninachotaka kukieleza hapa ni kwamba ni kuonyesha namna gani wenzetu wana ubunifu.
Hata wafanyakazi nchini, unakuta wengi sawa wanakuwa ofisini lakini wapo ambao ni wazembe, wengine wako bize na mitandao ya kijamii, badala ya kufanya mambo ya maana, mwisho wa mwezi ndio wa kwanza kuuliza kama mshahara umeshatoka au bado.
Baadhi ya wanandoa, ni mafisadi, anatumia fedha kuhonga, kulewa badala ya kuimarisha nyumba yake. Ulioa au kuolewa kwanini kama unashindwa kutulia na familia yako? Wengi wazuri wa kulalamika wanapata fedha ndogo, je unakitumiaje kidogo unachokipata?
Wengine wanahonga zaidi kuliko kufanya maendeleo, japo wachumi wanashauri kwamba ukitaka kuwa na maendeleo hakikisha angalau unaweka akiba asilimia 15 ya kipato chako, ili mwisho wa mwaka ufanyie kitu fulani kikubwa.
Wapo wanaoweza kuuliza aaah kipato chenyewe kidogo nitaweza kuwekeza hiyo asilimia 15? Jiulize je, kipato chako kingepungua au mwajiri wako angepunguza mshahara kwa asilimia 15 ungefanyaje?
Kama ungeishi, maana yake ni kwamba unapaswa kuishi na kufumbia macho hiyo asilimia 15 kwa kuiweka akiba ili hatimaye mwisho wa siku ufungue mradi au kuendeleza shughuli zako, hii ndio siri muhimu ya kufanikiwa katika maisha.Fanya kama hiyo asilimia 15 haiko, tafuta njia zingine za kuishi.
Mojawapo ya sababu ya kutokua haraka kwa maendeleo hapa nchini, ni tatizo la ubunifu na uwezo wa kuthubutu.Wengi wa Watanzania ni maarufu wa kulalamika, badala ya kuchukua hatua.Muda mwingi unapotea.
Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma India na Tanzania
Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi na Watumishi wa Umma Tanzania ina maswali mengi hasa namna inavyofanya kazi zake. Ni kama iko tu kufurahisha wakubwa, sio kusaidia kweli taifa, ndivyo watu wengi wanavyoona.
Kwa mfano mwisho wa viongozi kujaza fomu za kueleza mali zao na kuzirudisha kwenye sekretarieti hiyo ilikuwa Disemba 31 mwaka jana. Hata hivyo wale ambao hawajatangaza mali, hakuna hatua za kisheria wanazochukuliwa.