Friday 27 March 2015

SHERIA: Sheria gharama za uchaguzi kung’ata zaidi

Dar es Salaam. Serikali inakusanya nguvu kuhakikisha Sheria ya Gharama za Uchaguzi ya mwaka 2010, inang’ata wagombea wote watakaojihusisha na rushwa katika harakati zao za kusaka uongozi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, watendaji kutoka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wamesema, utekelezaji wa sheria hiyo ulikuwa na changamoto nyingi katika uchaguzi uliopita mwaka 2010.
Msajili Msaidizi wa Vyama vya Siasa nchini, Sisty Nyahoza alisema katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, ofisi yake ilikumbana na  changamoto nyingi zilizofanya ishindwe kuisimamia sheria hiyo ipasavyo.
“Mwaka 2010 changamoto zilikuwa nyingi lakini tumejifunza. Uchaguzi wa mwaka huu tumeshajipanga, tunajua jinsi gani ya kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo, tunajua tunahitaji ushirikiano wa karibu wa wadau ili kuweza kufanikisha jambo hilo,” alisema Nyahoza.
Nyahoza alitaja wadau ambao ofisi hiyo inatarajia kushirikiana nao katika kuisimamia sheria hiyo kuwa ni pamoja na vyama vyote vya siasa, asasi za kijamii, waandishi wa habari na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
“Ushirikiano huu unaanza kuimarishwa kabla ya uchaguzi. tumebaini kwamba wadau hawa wanatakiwa kupatiwa mafunzo ya namna wanavyoweza kushiriki kufanikisha utekelezaji wa sheria hii, pia kutakuwa na simu maalumu za kuripoti matukio yatakayokuwa kinyume,” alisema. 
Kauli ya Takukuru 
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk Edward Hoseah alikiri kuwepo kwa mkakati wa kuunganisha nguvu hizo, licha ya kukabiliwa na changamoto ya rasilimaliwatu.
“Ni kweli hata sisi tumeona kuna umuhimu wa kushirikiana katika kufanikisha jambo hili, ingawa kuna changamoto ya rasilimali watu, tunaamini kazi zitafanyika kwa namna ambayo itadhihirisha dhana ya kuwapo kwa Takukuru,” alisema Dk Hoseah.
Dk Hoseah pia alitumia nafasi hiyo kuwaasa wananchi kuepuka kuuza haki zao za kuchagua viongozi bora kwa kudanganywa na zawadi za kanga, fulana, kofia na fedha. 
Sheria ikoje?
Ilitungwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano wake wa 18, uliofanyika Januari 2010. Sheria hiyo  imeweka utaratibu wa kusimamia na kuratibu mapato, matumizi  na gharama za kampeni na uchaguzi wa vyama vya  siasa na wagombea.
Sheria hiyo ilisainiwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete Machi 17, 2010 ili iweze kutumika katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, kwa lengo la   kukuza demokrasia ya mfumo wa vyama vingi nchini.
Madhumuni ya kuwekwa Sheria hii ya Gharama za Uchaguzi ni kujenga mazingira yatakayowezesha kuwapo kwa uwazi zaidi katika matumizi ya fedha zitakazotengwa kwa ajili ya kampeni, pamoja na kudhibiti vitendo vya rushwa ndani ya vyama vya siasa katika uteuzi wa mgombea na uchaguzi wenyewe kwa ujumla.
Sheria hii imegawanyika katika sehemu nane. Sehemu ya Kwanza inaweka masharti kuhusu mambo ya utangulizi ambayo ni jina, tarehe ya kuanza kutumika kwa sheria hii katika Tanzania Bara na Zanzibar  na vilevile inaweka tafsiri ya misamiati itakayotumika.
Sehemu ya pili inaorodhesha kazi za Msajili wa Vyama vya Siasa, ikiwemo mamlaka ya kusimamia na kukagua gharama za uchaguzi kwa vyama vya siasa  na mwenendo wa wasimamizi wa uchaguzi.
Sehemu ya  tatu inahusu masharti kuhusu fedha zitakazotumika kwa ajili ya uchaguzi, maana ya gharama za uchaguzi, uchaguzi ndani ya Vyama vya Siasa, gharama  ambazo vyama vya siasa vinapaswa kutumia wakati wa uchaguzi, masharti  kwa Vyama vya Siasa na wagombea kutoa taarifa kuhusu gharama zitakazotumika wakati wa uchaguzi.
Aidha, sehemu hii inatoa taarifa kuhusu michango au misaada inayotolewa na kupokewa na vyama vya siasa, kuzuia fedha kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kampeni za uchaguzi, matumizi ya gharama kwa vyama na taasisi za kiserikali  wakati wa kutoa elimu ya Kampeni na chaguzi za kisiasa.
Sehemu ya tano ya sheria hii inahusu masharti yanayokataza baadhi ya matumizi ya fedha kama gharama za kampeni na uchaguzi. Matumizi hayo ni yale yanayohusu  gharama kwa vitendo vinavyozuiwa  au kuwa haramu wakati wa kampeni na uchaguzi.
Sehemu ya sita ya sheria hii inapendekeza makosa ya  ujumla  pamoja na adhabu zinazoweza kutolewa kwa kukiuka masharti ya Sheria hii.
Sehemu ya saba inaweka masharti  kuhusu haki ya mgombea wa Ofisi ya Rais na Makamu wa Rais kutumia vyombo vya habari, wajibu wa Serikali na vyombo vya habari kumuwezesha kutumia  haki  hiyo.
Aidha, sehemu hii inaipa Serikali wajibu wa kutumia  vyombo vya ulinzi  na usalama ili kuhakikisha kwamba Vyama vya Siasa, wagombea wao na  wapiga kampeni wanafikia wapigakura bila ubaguzi wala  kupewa vitisho.
Sehemu ya nane ya sheria inafanya marekebisho katika Sheria ya vyama  vya siasa ili kuoanisha masharti  ya sheria hiyo. Marekebisho ya msingi ni kuongeza  kifungu cha 13A katika Sheria ya Vyama vya Siasa kwa lengo la kuweka utaratibu utakaowezesha Msajili wa Vyama vya Siasa kupata taarifa juu ya mgombea au chama cha siasa kinachojihusisha na vitendo vya ukiukaji wa masharti ya Sheria hii wakati wa kampeni za uchaguzi.

Urais Ukawa, hesabu zinalalia Chadema

Dar es Salaam. Wakati wenyeviti wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) pamoja na kamati zake za kitaalamu wanakutana Zanzibar kutafuta suluhu kuhusu mgawanyo nafasi za kugombea katika uchaguzi mkuu ujao, kuna uwezekano mkubwa vyama hivyo kuteua mgombea urais kutoka Chadema.
Tovuti hii inaweza kuripoti kwa uhakika kuwa uwezekano huo unatokana na vigezo vinavyotumiwa na vyama hivyo kusimamisha mgombea mmoja kwa kila jimbo na kwenye nafasi ya urais ambavyo vinaipa Chadema nafasi hiyo dhidi ya vyama vingine katika umoja huo ambavyo ni CUF, NCCR-Mageuzi na NLD.
Vigezo hivyo ni matokeo ya uchaguzi 2010, idadi ya madiwani kwa kila chama, matokeo ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa Desemba mwaka jana, mtandao wa chama nchini na nguvu ya mgombea iwapo Chadema kitamsimamisha katibu mkuu wake, Dk Willibrod Slaa kwa mara ya pili.
Taarifa zilizolifikia Mwananchi kutoka ndani ya kamati ya ufundi ya Ukawa zinasema pamoja na kuwapo mvutano katika baadhi majimbo Tanzania Bara, kwa upande wa Zanzibar hakuna tatizo hilo, jambo linaloipa CUF nafasi ya moja kwa moja kwenye ubunge, uwakilishi na hata urais wa visiwa hivyo.
Kwa mujibu wa habari hizo, nafasi nzuri ya CUF kupita moja kwa moja Zanzibar bila ushindani ndani ya Ukawa, inatoa fursa kwa upande wa Bara, kwa vyama vilivyosalia kupitishwa kuwania urais wa Muungano.
Hata hivyo, kwa vigezo vilivyotajwa hapo juu, Chadema ndiyo inakuwa na nafasi isiyo na kipingamizi kutokana na rekodi vyama vilivyosalia Bara.
Katika Uchaguzi Mkuu wa 2010, Chadema kilimsimamisha Dk Slaa na aliibuka wa pili baada ya Rais Jakaya Kikwete akiwa na kura 2,271,941 (asilimia 26.34) akifuatiwa na Profesa Ibrahim Lipumba aliyepata kura 695,667 (asilimia 8.06) na Hashim Rungwe wa NCCR-Mageuzi aliyepata kura 26,388 (asilimia 0.31). NLD haikusimamisha mgombea urais.
Kwa upande wa majimbo yaliyotokana na uchaguzi wa 2010, Chadema kiliongoza kikiwa na wabunge 24 (wote kutoka Bara), CUF 23 (wawili kutoka Bara, 21 Zanzibar) na NCCR-Mageuzi wanne (wote wa Bara).
Katika rekodi za uchaguzi wa mitaa zilitolewa na Tamisemi kabla ya chaguzi za marudio, Chadema ilipata mitaa 980, ikifuatiwa na CUF (mitaa 266), NCCR Mageuzi  (28)  na NLD mtaa mmoja. Kwa upande wa vijiji, Chadema kilishinda vijiji 1,754, CUF (516), NCCR-Mageuzi (67) na NLD vijiji viwili.
Hata kwa upande wa vitongoji Chadema kiliviongoza vyama hivyo kwa kupata vijiji 9,145 kikifuatiwa na CUF (2,561), NCCR-Mageuzi (339) na NLD vitongoji viwili.
Tayari NCCR-Mageuzi kimeonyesha nia ya kumteua Dk George Kahangwa kuwania urais wakati Mwenyekiti wa NLD, Dk Emmanuel Makaidi alikaririwa na gazeti hili hivi karibuni akisema kuwa chama chake kimekwishamteua kuwania urais, hivyo jina lake litapelekwa Ukawa kushindanishwa.
Mvutano mkali
Hali ikiwa hivyo, wajumbe wa Ukawa leo watakumbana na wakati mgumu wa kufikia maridhiano ya kugawana majimbo 19 kutokana na taarifa za kuwapo mvutano mkali wa pande zote za vyama husika.
Wanaokutana leo ni wenyeviti wa vyama, makamu wenyeviti, makatibu na wajumbe wa sekretarieti kutoka vyama hivyo.
Kabla ya kuanza kikao cha leo, jana asubuhi wajumbe 16 wa Kamati ya Ufundi walikutana na baadaye jioni wenyeviti wa umoja huo wakawa na kikao cha awali, ikiwa ni sehemu ya vikao vya hatua za kugawana maeneo ya kuwania ili kutoa ushindani na hatimaye ushindi dhidi ya CCM.
Chanzo cha habari kutoka ndani kimelieleza Mwananchi kuwa NLD nayo imeongeza mvutano ikihitaji majimbo matano.
Wiki iliyopita, gazeti hili liliandika kuwa Ukawa ilikuwa imekamilisha kazi ya ugawaji wa majimbo 170 lakini ukawapo mvutano katika majimbo 19 ambayo vyama zaidi ya kimoja vilikuwa vinayataka.
Majimbo hayo ni Segerea, Kinondoni, Kigamboni na Ukonga ya Dar es Salaam, Morogoro Mjini na mengine ya mikoa ya Mwanza, Shinyanga na Kagera.
“Mvutano ni kwamba, kuna vyama vinavyotaka uwakilishi tu wa majimbo hayo lakini kiukweli yanaweza kupotea bure tu endapo vitakabidhiwa. Wengine wanataka kuangalia zaidi ushawishi wa chama ndani ya jimbo husika ila wengine wanapinga, wakisema umoja huo hautakuwa na sababu kama watakosa uwakilishi,” kilieleza chanzo hicho.
“NLD wanahitaji majimbo matano, CUF na Chadema wanavutana zaidi, ila NCCR-Mageuzi wameonekana kushtushwa sana na hali hiyo,” kilisema chanzo kingine kutoka NCCR-Mageuzi.
Chanzo kingine kilieleza kuwa kamati ya wataalamu ilishakamilisha kazi yake ya uchambuzi wa majimbo hayo na kuwasilisha taarifa zake lakini kuna upinzani mkali ambao umeendelea kuibuliwa na wajumbe wa umoja huo.
“Kikao cha leo kinaashiria kuwa na mvutano, ninaamini kuna uwezekano wa kufikia mwafaka lakini ikishindikana kabisa kwa leo lazima vitaandaliwa vikao vingine,” kilieleza chanzo kingine.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Wataalamu, Benson Kigaila (Chadema) alisita kuweka wazi juu ya mvutano uliopo huku akibainisha kuwa maridhiano yatapatikana.
Kigaila alisema kikao cha leo kina nafasi kubwa ya kumaliza mvutano huo na kueleza Watanzania juu ya mwelekeo wa safari yao.
Kigaila ambaye pia ni Mkurugenzi wa Oganaizesheni ya Mafunzo na Usimamizi wa Kanda wa Chadema, alisema: “Kwa sasa siwezi kueleza chochote kwani vikao ndiyo vinafanyika kwa sasa, lakini naomba vikao vikishamalizika viongozi wetu watazunguza tu,” alisema.
Alipoulizwa juu ya NLD kuhitaji majimbo matano, Kigaila alikiri kuwa kweli wanataka mgawo wa majimbo lakini alikataa kutaja idadi yake.
“NLD wanayo haki kama vyama vingine, kwa nini wasipate? Watapata, lakini kuna taarifa sahihi zitakazoelezwa baada ya kikao cha leo.”
Jumanne wiki hii, Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Bara, Magdalena Sakaya alilieleza gazeti hili kuwa kikao hicho kitakuwa na ajenda ya kukusanya maoni na mapendekezo ya wanachama, kujadiliana kwa pamoja ili kufikia muafaka wa majimbo hayo.
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema katika hatua za kutafuta maridhiano ya majimbo hayo, vyama vyote vinapaswa kutambua kila nafasi ya chama kilichoshiriki kwenye makubaliano ya Ukawa.
“Tukifuata kanuni, nadhani kuna vyama ambavyo havitakuwa na nafasi Ukawa na haitakuwa na maana ya kuungana, kwa hivyo lazima busara itumike zaidi. Haiwezekani chama fulani kilazimishe kuchukua majimbo mengi kuliko kingine,” alisema Nyambabe.
Alipoulizwa kuhusu utata katika mgawanyo wa majimbo, Dk Slaa alisisitiza kumalizika kwa mvutano kutokana na busara za viongozi wa vyama hivyo.

Thursday 26 March 2015

Marufuku kuvuta sigara hadharani

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid amesisitiaza tamko la kupiga marufuku uvutaji wa sigara katika maeneo ya umma ili kuilinda jamii kutokana na madhara yatokanayo na moshi wa sigara.
Tamko la Waziri limekuja ikiwa ni siku moja tu baada ya maadhimisho ya Siku ya Kifua Kikuu Duniani, moja ya magonjwa yanayosababishwa na uvutaji wa tumbaku.
Agizo hilo limezingatia Sheria ya Usimamizi wa Bidhaa za Tumbaku, Sura ya 121 TL, ya mwaka 2003, Kipengele cha 12(1) ambacho kinakataza matumizi ya bidhaa hiyo katika maeneo ya umma.
“Agizo hili linawataka wananchi wanaotumia bidhaa za tumbaku, kupunguza au kuacha kabisa, pia linaijumuisha jamii yote kujua madhara ya matumizi ya tumbaku na umuhimu wa kuzuia uvutaji katika maeneo ya umma,” alisema Waziri katika tamko lake.
Uvutaji sigara ulianza kupigwa marufuku kwa mara ya kwanza mwaka 1575 na Kanisa la Katoliki lakini katika karne ya 20 harakati dhidi ya uvutaji sigara zilipamba moto kwa sababu za kiafya.
Sababu kubwa ya kupiga marufuku ni ukweli kwamba uvutaji sigara ni hiari wakati kuvuta pumzi ni lazima, hivyo mtu anayetumia kilevi hicho hana budi kukaa mbali ili kuepusha uwezekano wa kupata magonjwa kama ya moyo na saratani kwa wasiotumia na ambao kuvuta pumzi ni lazima.
Msemaji wa wizara hiyo, Nsachris Mwamaja alisema nia ya marufuku hiyo ni kuhakikisha wizara inatimiza kwa vitendo sheria hiyo ya bidhaa za tumbaku kwa kupiga marufuku na kuchukua hatua za kisheria. “Jamii itusaidie kutoa elimu katika hili, kuna suala la kujenga maeneo maalum ya kuvuta sigara na elimu kwa wale wanaovuta,” alisema.
Sheria ya usimamizi wa bidhaa za tumbaku ya mwaka 2003, inaeleza kuwa nia ni kuwalinda vijana wenye umri wa chini ya miaka 18 na wale wasiovuta wasishawishike kuvuta.
Kuwalinda wasiovuta wasipate madhara, kuifahamisha jamii juu ya madhara ya tumbaku na madhara ya kuvuta moshi wa sigara inayovutwa na mwingine na kuhakikisha jamii haina wavutaji sigara.
Maeneo ambayo yamepigwa marufuku kuvuta sigara yametajwa katika tamko hilo kuwa ni katika ofisi zote za serikali na taasisi zake, hospitali za umma, vyuo vikuu na shule za umma, vituo vya usafiri wa anga, mabasi, bandari na treni, bustani, fukwe na katika maeneo ya kupumzika ya umma.
Pia tamko hilo la wizara limekataza uvutaji wa sigara katika mikutano yote ya kiserikali.
“Wizara inawataka wale wote ambao wanataka kuacha kabisa kuvuta sigara, wawatafute wataalamu wa afya ili wapate ushauri wa kitaalamu,” alisema waziri katika tamko hilo.
Kadhalika, agizo hilo limewataka wafanyakazi wa sekta ya afya na watumishi wa umma kuhakikisha wanafanyia kazi na wanasimamia agizo hili.
“Tunataka kila mmoja ashiriki katika agizo hili la kuzuia bidhaa za tumbaku, sekta binafsi, asasi za kidini na wadau wengine wa afya watusaidie katika kufanikisha hili,” alisema Waziri
Wakati wizara ikitoa tamko hilo, Kampuni ya Sigara (TCCL) imekuwa moja ya kampuni zilizoongoza kwa kulipa kodi mwaka jana.

Tanesco haiwezi kukwepa lawama hizi

Leo katika gazeti hili tuna habari kuhusu vifo vya watu watatu ambao umauti wao unaelezwa kusababishwa na hitilafu ya umeme iliyoanzia kwenye nguzo ya Tanesco.
Ni tukio la kusikitisha kwa sababu miongoni mwa waliokufa ni wanafunzi wawili. Lakini huzuni inaongezeka pale inapobainika kuwa tukio hilo limechangiwa na uzembe wa Tanesco. Kwa mujibu wa Mjumbe wa Shina wa mtaa lilipotokea tukio, Kondo Namna, taarifa za hitilafu hiyo ziliripotiwa kituo cha Tanesco Kurasini tangu Agosti 2, 2014. Lakini tangu wakati huo hakuna matengenezo yaliyofanyika hadi vifo vilipotokea Jumapili.
Kwa mujibu wa Kondo pia zaidi ya nguzo saba zimeinamia kwenye nyumba za watu na wameshatoa taarifa Tanesco, lakini hadi wakati wa tukio hilo hakuna hatua zozote zilizochukuliwa. Lakini baada ya vifo hivyo shirika hilo lilikwenda kutoa pole kwa wafiwa na baadaye Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Mhandisi Felchesmi Mramba alisema jambo hilo linatakiwa lifanyiwe uchunguzi wa kina na hawezi kuwachukulia hatua wafanyakazi wanaodaiwa kuzembea.
Tunashindwa kumuelewa Mramba anataka uchunguzi wa kina wa nini, wakati ni ukweli kwamba wenye wajibu wao hawakuwajibika ipasavyo. Kuna mfululizo wa matukio mengi yanayotokana na uzembe wa wahusika kutokelekeza wajibu wao ipasavyo.
Aprili 2014 tarafa ya Mang’ula wilayani Kilombero mkoani Morogoro, mtoto Amon Ndawala mwenye umri wa miaka mitano, alikufa baada ya kugusa nyaya za umeme ambapo Tanesco walitaarifiwa lakini walipuuza kurekebisha hitilafu hadi kifo kilipotokea. Kabla ya tukio kuna taarifa kwamba wananchi kwa muda mrefu walilalamikia hatari ya miundombinu ya umeme katika eneo hilo, ikiwamo nyaya za shirika hilo kugusa juu ya paa za baadhi ya nyumba za watu huku nyingine zikigusana na miti ama kuning’inia njiani. Wananchi hao walidai kuwa wamekuwa wakitoa taarifa za mara kwa mara kwa viongozi wa shirika hilo kuhusiana na mazingira ya hatari ya miundombinu ya Tanesco, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa kurekebisha.
Agosti 2013 huko Mbalizi mkoani Mbeya, nyaya za umeme zilizokuwa zimening’inia mita moja kutoka usawa wa ardhi, zilisababisha kifo cha Neema Kipenya (26), baada ya kuteleza na kushika nyaya hizo kwa lengo la kujinusuru asianguke. Tukio hilo lilielezwa kusababishwa na uzembe wa kutoziondoa nyaya hizo na kuziacha hapo kwa miezi kadhaa.
Julai 2013 wilayani Hai mkoani Kilimanjaro eneo la Sadala, kijana aliyefahamika kwa jina la Valerian Mosha alikufa baada ya kunaswa na umeme uliotokana na kulegea kwa nguzo ya Tanesco na kusababisha nyaya zinazopitisha umeme kuwa kimo cha chini. Hayo ni matukio machache kati ya mengi ambayo yamesababisha vifo kutokana na uzembe wa wafanyakazi wa Tanesco, ama kwa makusudi au kwa sababu wanazozifahamu wenyewe.
Leo mkurugenzi wa Tanesco anaibuka na kusema hawezi kumchukulia hatua mfanyakazi wake, hadi uchunguzi wa kina ufanyike. Ni uchunguzi gani anaoutaka Mramba, zaidi ya taarifa zilizotolewa kuhusu dharura na kushindwa kufanyiwa kazi na watendaji wake?
Tunahoji kitengo cha dharura cha Tanesco kina kazi gani? Tabia ya wafanyakazi wa Tanesco ya kushindwa kutekeleza majukumu yao kwa wakati inatoka wapi? Ni nani wa kuwajibika kutokana na uhai wa Watanzania kupotea bila sababu? Kwa nini viongozi wa Tanesco wanashindwa kuwachukulia hatua wafanyakazi wazembe?

Utafiti: Hali ya uchumi ya mtu mmojammoja nchini ni mbaya kuliko ilivyokuwa miaka 10 iliyopita

Hivi karibuni, Taasisi ya Repoa ilitoa utafiti wake unaoonyesha kuwa hali ya kiuchumi ya wananchi inazidi kuwa mbaya ikilinganishwa na ilivyokuwa miaka 10 iliyopita.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa, licha ya pato la taifa kuendelea kuongezeka hadi kufikia asilimia saba, Watanzania wengi wanaamini kwamba hali ya uchumi nchini mbaya.
Utafiti huo wa Afrobarometer, awamu ya sita uliofanywa kati ya Agosti 26 na Septemba 29 mwaka jana, walihojiwa Watanzania 2,386 wa Tanzania Bara na Visiwani. Wananchi hao walisema kuwa hali ya maisha inazidi kuwa mbaya ikilinganishwa na ilivyokuwa mwaka 2003.
Akitoa ripoti ya utafiti huo, Dk Lucas Katera kutoka Repoa, anasema wananchi wanalalamika kuwa licha ya Serikali kusema kuwa uchumi ni mzuri na kwamba nchi inapiga hatua ikilinganishwa na ilivyokuwa, wanaona watu wachache tu ndiyo wanaonufaika na maendeleo hayo.
Akitoa mfano anasema mwaka 2003 asilimia 42 walisema hali ya uchumi ilikuwa mbaya, mwaka 2005 asilimia 38, utafiti uliofuata mwaka 2008 idadi ya wananchi iliongezeka na kufikia asilimia 57 huku mwaka jana walikuwa asilimia 67.
“Idadi ya wananchi wasioridhishwa na namna Serikali inavyotekeleza miradi ya huduma za kijamii imeongezeka. Wananchi wanne kati ya kumi hawafurahishwi na huduma ya maji inayotolewa,” anasema Dk Katera.
Mtafiti huyo anasema matokeo hayo yamebaini kuwa kuna uhusiano wa karibu kati ya hali mbaya ya kiuchumi na utoaji mbaya wa huduma za jamii.
“Wananchi saba kati ya kumi wanasema Serikali inafanya vibaya kwenye sekta ya maji na elimu jambo linalosababisha hali mbaya ya kichumi,” anasema.
Mtaalamu wa Sera na Bajeti, Gilead Teri anasema wananchi wanahoji juu ya sababu zinazofanya matumizi ya Serikali kutowekwa wazi. Wanapendekeza uwazi zaidi uongezwe kwenye masuala yanayohusu umma.
“Wengi wamekata tamaa, wanasema takwimu hizo haziendani na hali halisi ya kipato chao. Hapa Serikali inapaswa kuchukua hatua ikiwa ni pamoja na kuboresha huduma za jamii,” anasema.
Teri anasema kukithiri kwa rushwa ni moja ya changamoto zinazowafanya wananchi kutokuwa na imani na Serikali.
Mtaalamu wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Prosper Ngowi anasema uchumi unaweza kukua, lakini kama hakutakuwa na matumizi sahihi ya fedha za umma wananchi wataendelea kuona kasoro za kiuchumi.
Dk Ngowi anasema, kama tatizo ni watendaji Serikalini, kununua vitu vyenye thamani kubwa visivyomlenga mwananchi wa kawaida, moja kwa moja, kunawafanya wananchi kutoona faida ya ukuaji wa uchumi.
“Sekta binafsi ndizo zinazochangia ukuaji wa uchumi kwa kutoa asilimia fulani ya faida waliyoipata kwa jamii. Ni vigumu wananchi kujua kiasi kilichotolewa kutokana na muundo wa sheria za uwekezaji nchini,” anasema.
Hata hivyo, wakati tafiti kutoka mashirika binafsi zikionyesha kuwa hali ya uchumi imekuwa mbaya kuliko ilivyokuwa mwaka 2003, Serikali kwa upande wake imekuja na matokeo yanayotoa taarifa tofauti.
Msimamo wa Serikali
Serikali daima umekuwa ikishikilia msimamo tofauti na tafiti hizo. Wao wanaamini wananchi wananeemeka kupitia miradi mbalimbali wanayoiendesha.
Akitangaza matokeo ya kwanza ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) kwa mwaka 2013/14 Machi 13, mwaka huu, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda anasema ripoti ya mpango huo iliyotolewa na waangalizi kutoka nje ya nchi inaonyesha hali ya maisha kwa wananchi imeanza kuimarika.
Pinda anasema hali hiyo imeimarika kupitia sekta ya elimu iliyofanya vizuri zaidi kwa kupata asilimia 81, maji asilimia 80, Nishati asilimia 79, Kilimo asilimia 77, Uchukuzi asilimia 64 na Utafutaji Rasilimali Fedha asilimia 54.
Kwa matokeo hayo, anasema malengo ya BRN yanaonyesha dalili za kuleta ‘nuru’ katikati ya giza la umaskini linalowafunika wananchi wengi hasa waishio vijijini.
Waziri Mkuu anasema: “Kiu ya Watanzania kujiletea maendeleo endelevu imekuwa ni jambo lililochukuwa nafasi ya kipekee katika historia ya taifa letu.”
Akiwasilisha bungeni Hotuba ya mapendekezo ya Serikali kuhusu makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2014/15, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya anasema umaskini wa kipato unaendelea kupungua nchini huku uchumi ukikuwa kwa kiwango cha kuridhisha.
“Ukuaji huu umeongeza pato halisi la wastani la kila Mtanzania hadi kufikia Sh1,186,200 mwaka 2013 kutoka Sh1,025,038 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 14. “Umaskini wa kipato umeendelea kupungua ambapo kwa mujibu wa takwimu mpya za Utafiti wa Mapato na Matumizi katika Kaya Binafsi uliofanyika Mwaka 2012, umeonyesha kuwa umaskini wa kipato umepungua kwa wastani wa asilimia 6.2 kati ya mwaka 2007 na 2012 kutoka asilimia 34.4 hadi asilimia 28.2,” anasema Mkuya.
Vilevile, Waziri huyo anasema umaskini wa chakula umepungua kwa asilimia 2.1 kati ya mwaka 2007 na 2012 kutoka asilimia 11.8 hadi asilimia 9.7.
Mwandishi maarufu wa vitabu nchini Marekani, Mark Twain aliwahi kusema kuwa kufanikiwa katika maisha unahitaji vitu viwili; ujinga kidogo na ujasiri.
Anasema kuna wakati mwanadamu huhitaji kuwa mjinga kidogo ili aweze kufanya mambo anayoyaamini hata kama watu wote waliomzunguka wanampinga. Pia anahitaji ujasiri kufanya jambo ambalo wengine wanaliogopa.
Hata hivyo, ni wazi Watanzania wengi wanaamini kwamba kukua kwa uchumi wa nchi kunatokana na Serikali kuwabana kupita kiasi kwa kodi huku wafanyabiashara wakubwa na makundi machache wakineemeka zaidi kwa rasilimali za nchi.
Pato la Serikali linaongezeka lakini lile la wananchi walio wengi ni dogo ukilinganisha na gharama halisi za maisha.
Serikali inapaswa kuwa makini kubadili mwenendo huo. Hili litawezekana iwapo itawatumia wataalamu wake wa uchumi katika kuwashauri.

Miswada miwili ya habari kuwasilishwa ‘kimafia’ bungeni

Licha ya wadau wa habari kuwasilisha ombi kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda wakitaka miswada miwili ya habari ya mwaka 2015 iwasilishwe kwa mfumo wa kawaida, Serikali imeing’ang’ania huku ikisema itawasilishwa chini ya hati ya dharura Jumanne ijayo.
Miswada hiyo ni kati ya minne yenye ‘utata’ ambayo ilikuwa iwasilishwe bungeni leo na kesho, lakini jana ofisi ya Bunge ilitoa ratiba mpya inayoonyesha kuwa itawasilishwa wiki ijayo chini ya hati ya dharura, ikiwa ni kinyume na maombi ya wadau wa habari.
Kaimu Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu aliliambia gazeti hili jana kwamba Serikali inataka kufanya ubabe na imepanga kuiwasilisha Jumanne asubuhi licha ya wabunge kutojua nini kimeandikwa.
Miswada hiyo ni pamoja na ule wa Sheria ya Miamala ya Kielektroniki wa mwaka 2014, Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao wa mwaka 2015, Muswada wa Sheria ya Kupata Habari wa mwaka 2015 na Muswada wa Sheria ya Vyombo vya Habari.
Juzi, wadau hao walimwomba Spika Makinda atumie hekima kuishauri Serikali iiwasilishe katika mfumo wa kawaida miswada miwili ya habari, ili kutoa fursa kwa wananchi na wadau kutoa maoni kabla ya kupitishwa na kuwa sheria.
Imeelezwa kuwa Jumanne, Muswada utakaoanza kuwasilishwa bungeni ni ule wa Sheria ya Kupata Habari na utafuatiwa na wa Sheria ya Vyombo vya Habari.
“Tunajua kuwa miswada hii imelenga kuvifungia vyombo vya habari, maana huu ni mwaka wa uchaguzi. Wanachokifanya Serikali ni kuiwasilisha bungeni ‘kimafia’ tu. Sisi tutakachokifanya ni kuibana bungeni,” alisema Lissu.
Hata hivyo, alisema kutokana na wingi wa wabunge wa CCM, huenda miswada hiyo ikapitishwa, jambo alilodai kuwa litakuwa gumu kulizuia.
“Mpaka sasa hatujaipata miswada hii, kwa kweli jambo hili linatusikitisha maana hata katika kamati haijafika,” alisema Lissu.
Tangu mkutano wa 19 wa Bunge unaoendelea mjini hapa ulipoanza, kumekuwa na taarifa kuwa Serikali inakusudia kuwasilisha miswada hiyo chini ya hati ya dharura, lakini wadau wa habari wameendelea kuiomba ibadili msimamo huo kwani kufanya hivyo kutawanyima wananchi fursa ya kutoa maoni juu ya miswada hiyo kabla ya kuwa sheria.
Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel juzi alilieleza gazeti hili kuwa miswada hiyo hata ikiwasilishwa itakuwa vigumu kujadiliwa kutokana na muda uliopo, huku akishindwa kuthibitisha kama kweli itawasilishwa ama laa.
Alipotafutwa tena jana, Kaimua Katibu huyo wa Bunge, Joel kufafanua mabadiliko ya ratiba hiyo na kama miswada hiyo pamoja na hati ya dharura vimeshafikishwa katika ofisi ya Spika, hakupatikana.

JK, Nkurunziza wazindua treni za mizigo kwenda Burundi, Uganda na DR Congo

Rais Jakaya Kikwete na mwenzake Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi wamezindua safari za treni tatu za mizigo ‘block train’ kutoka Dar es Salaam kwenda Burundi, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Uzinduzi wa treni hizo zenye mabehewa 15 hadi 20 ulifanyika jana jijini Dar es Salaam muda mfupi baada ya Rais Kikwete kuzindua mkutano wa marais wanachama wa nchi zinazounda ukanda wa kati.
Marais waliohudhuria mkutano huo wa siku mbili ni Rais Yoweri Museven wa Uganda, Rais wa Kenya aliwakilishwa na Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo, Amina Mohamed, Rais wa DRC aliwakilishwa na Waziri wa Usafirishaji, Justine Kanumba huku Rais wa Rwanda, akiwakilishwa na Waziri wa Miundombinu wa nchi hiyo, James Musoni.
Akizindua treni hizo, Rais Kikwete alisema, “kuanzia sasa zitakuwa zikibeba mizigo ya nchi moja pekee yake kwa wakati mmoja, kama ni mizigo ya Burundi itakuwa Burundi tu vivyo hivyo kwa DRC na Uganda, kinyume na ilivyokuwa awali.
“Awali safari za treni za mizigo zilikuwa zikichukua wiki mbili kufikisha mizigo kwenye nchi husika, lakini sasa itakuwa inachukua siku mbili pekee,” alisema Rais Kikwete.
Kwa upande wake Rais Nkurunziza alisema Tanzania imefanya jambo la maana kuisaidia nchi yake ambayo ipo mbali na bahari. “Safari hizo zitasaidia kusafirisha mizigo mingi na kwa njia ya kwa haraka.”
Vikwazo vya usafirishaji
Awali akifungua mkutano wa Ukanda wa Kati wa Kibiashara jijini hapa, Rais Kikwete alisema Tanzania imeshapiga hatua kubwa katika kuhakikisha inaondoa vikwazo vyote vya usafirishaji mizigo kwenda nchi jirani, ikiwa ni pamoja na kupunguza idadi ya vizuizi barabarani.
“Tumeamua kupunguza vizuizi vya polisi barabarani kutoka 15 hadi vitatu na vituo vya mizani kutoka 10 hadi vitatu vitakavyojengwa vigwaza mkoani Pwani, Manyoni (Singida) na Nyakahura (Kagera),” alisema Rais Kikwete.
Alisema ni jukumu la nchi kuonyesha kuwajibika katika mradi huo kwa kuwa sehemu kubwa ya mradi ipo nchini, hivyo ni vyema kuhakikisha nchi jirani zinasafirisha mizigo yao kutoka bandari ya Dar es Salaam bila tatizo.
“Kama ambavyo nimesema inatuwezesha kukuza biashara za ndani na kimataifa na kukuza uchumi.”
Katika mradi huo, kilomita 2,707 za reli hiyo zipo Tanzania, barabara ni kilomita 2,406, pia bandari kubwa tatu za Dar es Salaam, Kigoma na Mwanza zipo Tanzania.
Kuhusu ufanisi wa bandari ya Dar es Salaam, Rais Kikwete alisema kuwa idadi ya mizigo inayosafirishwa imeongeka kutoka tani milioni 9.2 mwaka 2010 hadi tani milioni 14 mwaka 2014 na kufikia mwishoni mwa mwaka huu inatarajiwa kufikisha tani milioni 18.
“Idadi ya siku za kutoa mzigo bandarini zimepungua kutoka siku 21 hadi 9 na bado tunataka zipungue zaidi. Kuhusu wizi hakuna taarifa ya tukio lolote kwa miaka miwili sasa…pia Serikali ina mpango wa kujenga bandari mpya Bagamoyo itakayoweza kuhifadhi tani milioni 240 kwa mwaka,” alisema Rais Kikwete.
Kuhusu reli, alisema kuwa vichwa 13 vya treni vimeshanunuliwa na kati yake viwili viliwasili nchini wiki iliyopita. Vichwa vitano vinatarajiwa kuwasili mwezi ujao na vilivyobaki vitaletwa Mei mwaka huu. Pia mabehewa 274 yamenunuliwa kati yake 150 yaliwasili nchini Februari mwaka huu.
Hata hivyo, Rais Kikwete alisema pamoja na Tanzania kuingiza nchini mkongo wa mawasiliano ya intaneti, bado haijanufaika kiasi cha kutosha kwa kuwa baadhi ya wananchi wanautumia kwa ajili ya kutuma ujumbe na picha kwa njia ya mtandao wa kijami wa WhatsApp.
Rais Museveni aliyekuwa kivutio kwa watu wengi mkutanoni kutokana na muda mwingi kutoa matamshi ya utani, alisema sababu mbalimbali zinazokwamisha biashara kufanikiwa kuwa ni pamoja na ukosefu wa usalama, kutokuwapo kwa watendaji wenye ujuzi, kukosekana kwa soko na kukosekana kwa faida kuwa ndiyo sababu zinazoweza kukwamisha biashara kustawi.
Alisema ili mipango ya kibiashara inayopangwa na nchi hizo ifanikiwe lazima vikwazo vijulikane na kutafutiwa ufumbuzi mapema.
“Wataalamu wa uchumi wanasema gharama ya usafiri katika biashara inapaswa kuwa asilimia 40, mtaji asilimia 20, kazi asilimia 10, ukilitimba asilimia tano, lazima tujiulize kikwazo kipi kinatukwaza,” alisema Museven.
Alisema hakuna namna ujenzi wa reli unaweza kuepukika kwa kuwa barabara zinapitika mara kwa mara huku zikigharimu fedha nyingi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Amina Mohamed alisema miradi iliyoanzishwa chini ya mradi huo itachangia sehemu kubwa kuimarisha hali ya kiuchumi iliyokuwa imekwama katika baadhi ya miradi.

Friday 20 March 2015

Taifa njiapanda

Dar es Salaam. Wakati Taifa likijiandaa kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, yamebainika mambo matatu mazito ambayo yanaliweka njiapanda , hali inayosababisha viongozi na hata wananchi kubaki na maswali lukuki wakihoji hatma ya nchi yao.
Mambo hayo ambayo hadi sasa hayajulikani hatma yake ni Katiba Inayopendekezwa, Mahakama ya Kadhi na uboreshaji wa Daftari la Wapigakura kwa vifaa vya kielektroniki vya Biometric Voter Registration (BVR).
Mambo hayo yamekuwa  mjadala wa kitaifa kwa muda sasa, hoja kubwa ikiwa ni endapo matukio makubwa ya kitaifa – upigaji wa kura ya maoni kupitisha Katiba Mpya na Uchaguzi Mkuu wa Oktoba yatafanyika kwa mafanikio au yanaweza kukwama na kusababisha sintofahamu.
Uandikishaji BVR
Hoja kubwa katika eneo hili imekuwa ni iwapo kura ya maoni ya kupitisha Katiba itafanyika Aprili 30, mwaka huu kama ilivyopangwa, lakini Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian Lubuva mara kadhaa amesimamia msimamo wa Serikali kuwa uandikishaji unaendelea bila matatizo katika Mkoa wa Njombe kama ilivyopangwa.
Ukiacha upungufu unaosababisha shughuli hiyo kuchukua muda mrefu, Jaji Lubuva amekuwa akikwepa kuzungumzia madai kuwa Serikali haikutoa fedha za kutosha kufanikisha shughuli hiyo, lakini juzi alikiri kuwa Tume yake ilijaribu hata kuazima vifaa hivyo Kenya na Nigeria bila mafanikio.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amekaririwa na gazeti hili jana akisema hata bajeti ya mchakato huo ya Sh297 bilioni  iliyopangwa haipo kwa kuwa katika kasma ya tume zilikutwa Sh7.01 bilioni na fedha za maendeleo na fedha za tume hazikuonekana.
Profesa Lipumba alisema pia hata Sh144 bilioni za kura ya maoni zilizoelezwa na Tume hazikuonekana kwenye vitabu vya bajeti na kuwa BVR 250 zilizopo badala ya 8,000 zilizokusudiwa haziwezi kufua dafu.
Kuhusu muda uliosalia wa siku 42 kabla ya kura ya maoni, umeelezwa na wachambuzi kuwa hautoishi, ukilinganishwa na Kenya iliyokuwa na BVR 15,000 na ikaandikisha wapiga kura milioni 14 kwa siku kati ya 45 hadi 60.
Kutokana na hali hiyo, kinachosubiriwa na wananchi ni ama kuelezwa ni muujiza gani utafanyika hadi shughuli hiyo kukamilika na kura ya maoni kupigwa bila matatizo au kuahirisha kura hiyo hadi wakati au baada ya uchaguzi mkuu.
Mahakama ya Kadhi      
Saula jipya kabisa katika mjadala wa uanzishwaji wa Mahakama ya Kadhi inayotambuliwa na Serikali ni kesi iliyofunguliwa Mahakama Kuu na Mwenyekiti wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila akitaka mahakama itamke kuwa Mahakama ya Kadhi na masuala ya Jumuiya ya Kiislamu (OIC) ni haramu na itamke kuwa ulinzi na uhai na utu wa binadamu nchini hauwezi kubaguliwa na Uislamu.
Kesi hiyo iliyofunguliwa siku moja kabla ya Bunge kuanza mkutano wake wa 19 jana ambao pamoja na mambo mengine umepanga kujadili muswada wa marekebisho ya sheria mbalimbali, unaokusudia Mahakama ya Kadhi itambuliwe katika mfumo wa mahakama nchini, hali ambayo inaweza kubadili upepo katika chombo hicho cha kutunga sheria.
Hata hivyo, Mkurugenzi  wa Shughuli za Bunge, John Joel alisema hadi jana chombo hicho hakikuwa na taarifa yoyote kutoka mahakama kuhusu kesi ya Mahakama ya Kadhi.
Kwa siku za karibu suala la Mahakama ya Kadhi limeingia katika mjadala kutokana na ahadi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyoitoa bungeni kuwa Serikali ingeleta muswada huo ili kuitambua lakini isingewekwa katika Katiba Inayopendekezwa.
Katiba Inayopendekezwa
Katiba Inayopendekezwa ilipita katika misukosuko mingi na imeendelea kupingwa na baadhi ya makundi ya jamii, vyama vya siasa huku ikiungwa mkono na chama tawala na Serikali yake.
Huku ikiendelea kupigiwa chapuo kupitia vyombo vya habari, mikutano ya kisiasa ya chama tawala na baadhi ya makundi, vile vile imeendelea kupingwa na makundi mengine, jambo ambalo ni dhahiri limeacha mgawanyiko kitaifa.
Vyama vya upinzani chini ya umoja wao wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) wameweka msimamo wa kuendelea kuipinga na kujiweka kando katika mchakato wake, huku baadhi ya viongozi wa dini wakitoa matamko yanayoeleza msimamo wa kuipigia kura ya hapana Katiba hiyo.
Tamko la karibuni kabisa ni lile la Jukwaa la Wakristo lililotolewa na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT) lililoelekeza waumini kupiga kura ya Hapana kwa Katiba Inayopendekezwa.
Siku chache baada ya tamko hilo, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo aliibuka na kupingana na tamko hilo akisema waumini waachwe waamue wenyewe aina ya kura wanayoitaka, hivyo akaagiza tamko hilo lisambazwe na kusomwa makanisani ili waumini waamue wenyewe cha kufanya.
Hata hivyo, Ushirika wa Wachungaji wa Kipentekoste Tanzania (PPFT), umetoa kauli yake ukionya taasisi za kidini zinazotumia mwavuli wa dini kwa maslahi binafsi kuacha kuwaburuza katika suala la Katiba mpya.
Matamko hayo ya viongozi wa dini yameliweka Taifa kwenye kona na kuwaacha waumini wao na hata wananchi wengine wasijue washike lipi na waache lipi.
Kauli ya Serikali
Hata hivyo, akizungumzia matamko hayo, Kaimu Kiongozi wa Shughuli za Serikali bungeni jana, Samuel Sitta alisema mvutano uliopo kati ya Jukwaa la Wakristo Tanzania na Pengo kuhusu kuipigia kura ya “Hapana” Katiba Inayopendekezwa hauwezi kubadili msimamo wa Serikali kuhusu upigaji wa kura hiyo.
Sitta, ambaye pia ni Waziri wa Uchukuzi na aliyekuwa mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, alisema waumini waachwe wachague aina ya kura watakayopiga, kama viongozi hao wa dini wamegawanyika hamna namna ya kuwafanya wawe na kauli moja.
Maoni ya wadau
Kutokana na hoja hizo zinazolibana Taifa, waziri wa zamani wa mambo ya nje na mwanasiasa mkongwe nchini, Ibrahim Kaduma alisema: “Sikuwa natarajia kama ipo siku viongozi wetu watawadhihaki wananchi, kwani haiwezekani uwaambie kuwa kura ya maoni itafanyika Aprili 30, wakati uandikishaji unavyokwenda hauridhishi, hii ni kuwadhihaki tu.”
“Tumefanya makosa, turudi nyuma na tutumie uandikishaji kwa daftari letu, kisha tufanye uchaguzi na Kura ya Maoni, kwa kutumia BVR inahitaji mwaka mmoja au miwili zaidi kuhakikisha tunaandikisha watu wote.”
Alisema, “Tatizo Serikali haipo tayari kusikiliza ushauri kwani tulishasema huwezi kuandikisha watu wote kwa kipindi hiki kilichobaki, lakini haikusikia, hizo mashine zikimaliza kuandikisha zibaki hapo kwa ajili ya kuwaingiza watu wanaofikisha umri wa kuandikishwa na mchakato huu uwe endelevu, jambo ambalo sidhani kama litafanyika.”
Spika Mstaafu wa Bunge, Pius Msekwa alisema, “Kutojua ukweli ni adui mkubwa, wanazungumza Katiba hawajaisoma...kuzungumzia jambo ambalo hujui ukweli wake ni tatizo, tusizungumze jambo kama hulijui undani wake.”
Akizungumzia tamko la maaskofu alisema, “Kama Mkristo limenikwaza, sana lakini nilipata faraja na tamko la Kardinali Pengo. Kwanini  umnyime uhuru kupiga kura aipendayo, imenikwaza sana hii.”
“Usiwaelekeze jinsi ya kupiga kura kwani inajulikana na wanachotakiwa kukifanya ni kuwaelekeza kilichomo ndani ya Katiba hiyo na siyo kuwaeleza kwamba kapigeni kura ya hapana, hii siyo sahihi kwani ni watu wazima wanaweza kuamua wao wenyewe,” alisema Msekwa.
Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta), Gration Mukoba alisema nchi inapoelekea inahitajika mtabiri wa hali ya juu atakayetabiri Tanzania ya mwaka 2016 itakuwaje.
“BVR na vitambulisho vinavyotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) havina tofauti, lakini hawa Nida wana zaidi ya mwaka sasa na wakazi wa Dar es Salaam hawajapata wote, sasa kweli NEC watamaliza uandikishaji kabla ya Aprili 30, hii ni ndoto.”
Akizungumzia Mahakama ya Kadhi alisema, “Hivi leo tukiipitisha Mahakama ya Kadhi, kesho wanga nao watataka mahakama yao na makundi mengine yatajitokeza yakitaka mahakama yao...nchi iko katika wingu zito sana,” alisema Mkoba ambaye pia ni rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT).
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Ernest Mwasalwiba alisema, “Mahakama ya Kadhi ina mkanganyiko kwani elimu haijatolewa vya kutosha, mfano mtu asiyehusika nayo atafaidika nayo vipi, lakini kuna makundi yanapingana, nani atakayeiongoza, itatoa wapi fedha za kujiongoza haya yote yalitakiwa kutolewa ufafanuzi.”
Kuhusu BVR Dk Mwasalwiba alisema, “Muda uliobaki ndiyo unaolalamikiwa. Suala la kupiga kura ya maoni ni la wananchi, kwamba wapige au wasipige hilo lipo mikononi mwao.”
Aliongeza, “Haya matamko nisingeungana sana nayo kuwa upige kura ya hivi, lakini walichopaswa au wanachopaswa kukifanya viongozi wa dini na Serikali ni kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi kuhusu mchakato huu.”
Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk Billy Haonga alisema, “Uwezekano wa kura ya maoni kufanyika Aprili 30 ni mgumu kwani kama Njombe mpaka sasa hawajamaliza itakuwaje nchi nzima kumaliza kwa kipindi hicho.”
“Kinachotakiwa kufanyika sasa ni mawazo ya busara kutumika kura ya maoni iahirishwe na uandikishaji uendelee kwa umakini na inawezekana kabisa ukafanyika pamoja na uchaguzi mkuu siku hiyo hivyo kwani inawezekana kabisa.”

Nini kimejificha kuhusu Muswada wa Sheria ya Habari?

Tunawaunga mkono wabunge waliojitokeza kupinga kuwasilishwa kwa hati ya dharura muswada wa Sheria ya Kupata Habari wa mwaka 2015.
Wakizungumza bungeni juzi, baadhi ya wabunge waliihoji Serikali sababu ya kuharakisha kuwasilisha muswada huo kwa ajili ya kupitishwa kama sheria.
Si wabunge pekee, wadau wa sekta ya habari wanajiuliza kuhusu uharaka wa muswada huo ambao kimsingi si suala la jana au juzi. Ni suala la muda mrefu ambalo wadau wa habari wamekuwa wakilipigania.
Ikiwa muswada huu utawasilishwa kwa njia ya hati ya dharura, ina maana utasomwa kwa mara ya kwanza na kupitishwa vipengele vyote kwa siku moja. Hii ina maana kuwa si wadau wa habari wala watunga sheria wetu, watakaopata muda wa kutosha wa kuupitia muswada na kujiridhisha kuwa una kila sababu ya kuwa sheria kwa maendeleo ya sekta ya habari na wanahabari.
Aidha, wadau wa habari kama wataalamu wa sekta hiyo, watakosa fursa ya kuwaelewesha wabunge masuala mbalimbali yaliyomo katika muswada, ili hata wanapoupitia wawe na weledi wa kutosha wa kitu wanachotaka kukipitisha kuwa sheria rasmi.
Mchakato mzima wa suala hili umegubikwa na usiri ambao sisi tukiwa wadau wa habari, unatupa wasiwasi na hata kujiuliza una maana gani? Nini kimejificha nyuma ya usiri huu?
Tumesema hapo awali hili si suala la jana wala juzi, tumekuwa tukilipigania kwa muda mrefu. Kwa nini taratibu za kawaida za uwasilishaji wa miswada zisifuatwe ili wadau wote wajiridhishe kuwa sheria itakayotungwa itakuwa na tija na maendeleo kwa sekta yenyewe, wanahabari na Taifa kwa jumla?
Kinachotokea sasa kuhusu haraka na usiri ulioligubika suala hili, wadau wa habari hasa wanahabari wanaweza kusukumwa kuamini kuwa kuna dhamira isiyo njema kwao.
Hofu hii ya wanahabari imeshaanza kujidhihirisha katika mjadala bungeni, baada ya baadhi ya wabunge kufikia hatua ya kuinyooshea kidole Serikali kuwa pengine ina dhamira ya kutaka kuvikandamiza vyombo vya habari kupitia muswada huo.
Hatutaki kuamini kuwa Serikali yetu sikivu na inayoongoza kwa misingi ya kidemokrasia, inaweza kutunga kwa makusudi sheria inayolenga kuvibana vyombo vya habari. Na kama itakuwa hivyo, tunauliza ni kwa masilahi ya nani?
Tunawakumbusha viongozi na watendaji serikalini kuwa Tanzania ni nchi yetu sote, hakuna mtu mwenye haki ya kujiona yeye ni Mtanzania zaidi kuliko wengine au mzalendo kuliko wengine.
Tunatoa tanbihi hii kwa kuwa umejengeka utamaduni wa viongozi serikalini na hata wanasiasa kufikiri kuwa wao ni weledi wa kila kitu kuhusu maendeleo na ustawi wa Taifa hili.
Watu hawa wachache siku zote wanalazimisha maoni, mitazamo na fikra zao vitamalaki hata katika mazingira ambayo umma mpana unaona siyo sahihi tena kwa kuegemea katika hoja zenye mashiko.
Matokeo ya utamaduni huu wa wachache kujiona ndiyo wenye uwezo wa kufikiria kwa niaba ya wengine, tuliyaona wakati wa mchakato wa Bunge Maalumu la Katiba wakati wanasiasa walinyofoa mambo mengi yaliyopendekezwa na wananchi, wakapendekeza wanayoyataka wao. Mwishowe mchakato huo umegawanya nchi.
Na ndio maana tunasema muswada huu hauna udharura wowote, kwanini uwe siri? Urudishwe kwa wadau wauone ili kuzuia mgawanyiko mwingine.

Thursday 12 March 2015

Kiswahili dhidi ya Kiingereza au Kiswahili pamoja na Kiingereza?

Suala la matumizi ya lugha Tanzania limeleta ushindani mzito kati ya Kiswahili na Kiingereza.
Hoja ya watetezi wa Kiingereza inajumuisha pia madai kuwa kuendelea kutumia Kiswahili, ni kuwafanya Watanzania washindwe kushindana kiuchumi katika dunia ya leo.
Dunia ya leo ni dunia ya utandawazi ambapo mipaka baina ya mataifa inapuuzwa na watu wanaweza kuwekeza, kuajiriwa na kufanya biashara karibu popote duniani.
Kwa sababu hiyo Kiingereza kinawafungulia milango katika dunia ya utandawazi. Lakini tusije kusahau watu wengi kutoka nchi nyingi wanakitumia Kiingereza kama lugha ya kibiashara na mawasiliano na watu ambao hawajui lugha yao ya kitaifa. Watu hawa wakiwa katika nchi zao wanatumia lugha zao za taifa.
Mifano ni pamoja na Wajerumani, Wajapani, Wafaransa, Waitalia, Wachina, Warusi na wengineo.
Ninavyoona mimi ni kwamba uzito wa hoja ya wale wanaopendekeza Kiingereza iwe lugha ya kufundishia Tanzania, unatokana na hoja ya umuhimu wa lugha hiyo katika uchumi wa viwanda.
Msingi wa lugha ni fikra zinazoelezwa katika maneno ambayo yanadhihirisha mkakati wa mpango fulani. Endapo mchakato wa mpango hauridhiki katika kasi ya mwenendo wake, lugha inaweza kurekebisha na kuongoza kutokana na msingi wa lugha husika kuwa desturi za wote wanaohusika ambao wamekipa kipaumbele matumizi yake.
Changamoto iliyopo katika maendeleo ya matumizi ya Kiswahili ni kuendeleza fikra za Watanzania. Fikra zitakazoeleza vitendo endelevu ambavyo vitasukuma mbele uchumi wa Tanzania na kuboresha maisha ya Watanzania.
Tukumbuke moja ya maneno maridhawa ya Mwalimu Julius Nyerere aliyeahi kuandika kitabu akakipa jina la “We Must Run While They Walk. Alimaanisha Tukimbie wakati wenzetu wakitembea.
Hoja yangu ni lugha ipi inawasukuma Watanzania kukimbia kati ya Kiswahili na Kiingereza? Jibu la kimsingi ni zote hizo mbili. Uchaguzi uliopo ni wa njia. Kila lugha husika ina njia inayoweza kutumika kufikia malengo ya matumizi yake kwa ufanisi. Lakini pia tujiulize kama njia hiyo inajenga maadili ya kudumu nchini Tanzania?
Nashauri iwe njia ya kufuata au njia ya kuongoza ambayo itajenga utaifa Tanzania. Kiswahili kikiwa lugha ya chimbuko la Utanzania kinaweza kuongoza.
Kiingereza ni lugha ya uvamizi wa ardhi ya Afrika, haina budi iwe ya lugha ya pili. Wasichoelewa watu wengi ni kuwa Kiingereza kinaweza kusaidia katika dunia ya utandawazi, lakini hakina uwezo wa kujenga Utanzania.
Msingi wa uthibitisho wa hoja yangu nautolea mfano nchini Uingereza. Kwa nini Mfalme Henry VIII alikifanya Kiingereza kuwa lugha rasmi ya Uingereza akiipinga lugha ya Kilatini iliyotumiwa na jamaa wa mfalme, watu wa tabaka ya juu, matajiri, wasomi na wataalamu?
Kiingereza kilikuwa lugha ya sokoni, lugha ya kina yakhe, Ilikuwa lugha ya kuongea na watumishi na wahudumu nyumbani.
Kiswahili hata katika taaluma kinawezekana na kwa mfano, hakuna haja ya kutafsiri istilahi za sayansi, tiba au hesabu. Tukumbuke hata Kiingereza bado kinatumia istilahi za Kilatini katika fani hizi.
Wataalamu Waingereza waliendelea kutumia Kilatini katika fani hizo hata baada ya mapinduzi ya kilugha Uingereza.
Aidha, sioni haja kwa mfano tutohoe neno pressure na kuita presha, ilhali tunaweza kusema shinikizo
Pete Mhunzi ni Mmarekani mwenye asili ya Afrika na mpenzi wa Lugha ya Kiswahili

Mbatia aitupia lawama Serikali ajali ya Iringa

Dar es salaam. Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi taifa ,James Mbatia amesema kwamba  ajali  iliyotokea eneo la Mafinga Changalawe mkoani Iringa ilikuwa imepangwa na binadamu na wala sio mipango ya Mungu.
Akizungumza jijini leo Mbatia amesema ajali hiyo ilipangwa na watendaji wa serikali  kwa sababu ajali hiyo ilisababishwa na shimo kubwa ambalo limekaa kwa muda mrefu eneo hilo pasipo juhudi zozote za Serikali kulikarabati.
Mbatia amesema hawezi kukaa kimya ni lazima awasilishe suala hili  bungeni ili wahusika wachukuliwe hatua kwa kuacha shimo kubwa barabarani kwa muda mrefu bila kuliziba.
Amesema shimo hilo ambalo ndio hasa lilikuwa chanzo cha ajali hiyo ni la muda mrefu lakini viongozi wa serikali wanaliangalia tu bila kuchukua hatua ya kuliziba.
 ‘’Jamani  watanzania waliopoteza maisha kwenye ajali hiyo ni wengi na  ni aibu kwa taifa, ukizingatia chanzo cha ajali hiyo ni shimo la muda mrefu ambalo linaangaliwa na viongozi wetu kila siku bila kuliziba’’alisema Mbatia
Amesema ajali hudokeza kwa ujumla matokeo mabaya ambayo labda yangeweza kuepukwa au kukingwa ikiwa matukio yaliyosababisha ajali hiyo yangetambuliwa na kurekebishwa kabla ya tukio.
Amesema madereva wanaoendesha magari ya abiria wanatakiwa kupelekwa shule angalau kwa miezi sita ikiwa ni pamoja na kupimwa afya mara kwa mara.
Aidha ameitaka serikali kutoa tamko kuhusu ajali hiyo na sio kukaa kimya mpaka waanze kupigiwa makelele na wananchi kupitia vyombo vya habari.
Watu  zaidi ya 40  waliokuwa kwenye basi  la kampuni ya Majinjah Express lililokuwa likitokea Mbeya kwenda Dar es Salaam, walifariki papo hapo katika ajali hiyo iliyotokea jana wengine 23 wakijeruhiwa.

Wednesday 11 March 2015

Waziri Samuel Sitta azuia mabehewa 124 akihofia ufisadi

Dar es Salaam. Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta amezuia uingizaji wa mabehewa 124 ya mizigo yaliyobaki katika zabuni iliyofanywa na Kampuni ya Reli Tanzania (TRL), hadi pale uchunguzi wa tuhuma za ufisadi katika manunuzi hayo utakapokamilika.
Pamoja na hayo, Sitta alisema kuna hisia zimejitokeza kuwa huenda mabehewa hayo ni mitumba siyo mapya kama inavyodhaniwa.
Sitta aliwaeleza waandishi wa habari jana kuwa zabuni ilihusisha ununuzi wa mabehewa 274 na kwamba 150 tayari yalishaingia nchini, huku kukiwa na harufu ya ufisadi kuwa yalitengenezwa chini ya kiwango.
Mapema Aprili 2013, TRL iliipatia kampuni ya India iitwayo M/S Hindustan Engineering & Industrial Limited zabuni ya kutengenezea mabehewa ya mizigo kwa ajili ya Reli ya Kati. Serikali iliilipa kampuni hiyo Sh45.5 bilioni sawa na Sh166 milioni kwa kila behewa.
Hata hivyo, Sitta alisema kuwa Serikali ililipa asilimia 50 ya gharama zote za manunuzi na kwamba iwapo ikibainika udanganyifu wowote kampuni hiyo itawajibika.
“Nimekataza kabisa yale 124 yaliyobaki kule yasije. Nimeshawaagiza Reli kuwa yaliyopo kiwandani yanaendelea kutengenezwa au safarini hayaruhusiwi kuja kwa sasa mpaka tuweze kukwamua sakata hili.”
“Haiwezekani wakati tunachunguza 150 yaliyoingia tukayaruhusu yale 124 yaingie. Je, yakiwa na ubovu ule ule itakuwaje?” alihoji Sitta.
Alisema anaungana na aliyekuwa waziri wa wizara hiyo, Dk Harrison Mwakyembe kuwa mabehewa hayo ya mizigo yapo chini ya kiwango kutokana na kupinduka na kuacha reli mara kwa mara.
Alisema kiwango cha kuacha reli kwa mabehewa hayo siyo cha kawaida na ripoti ya Desemba mwaka jana ilionyesha kulikuwa na wastani wa upindukaji kila siku.
Kutokana na suala hilo kuwa kikwazo cha ufanisi kwa TRL, Sitta aliiagiza kamati ya uchunguzi wa sakata hilo (iliyoundwa na Dk Mwakyembe) kupitia Bodi ya Wakurugenzi ya TRL kukamilisha ripoti ifikapo Ijumaa wiki hii ili Serikali ijue la kufanya.
“Kuna mambo mengi tu ya kufanya kama kuvunja mkataba na mkandarasi, kumshtaki mhusika, kuangalia nani walienda kukagua na bado tukapata vibovu.
“Hii itatusaidia kujua hatua za kuchukua kiuwajibikaji kwa kuwa hivi sasa ni lazima mtu awajibike aidha kwa kufanya jambo kwa makusudi au kwa uzembe,”alisema Sitta. Alisema Idara ya Uhandisi katika wizara yake itasaidia kubaini nini kilitokea kiasi cha kuingiza nchini mabehewa yanayoleta hasara kubwa kwa taifa.
Kuhusu utendaji wa jumla wa TRL, Sitta alisema kwa sasa hali inaridhisha katika kampuni hiyo kiasi cha kuongeza mapato maradufu hadi kufikia Dola za Marekani 140 milioni (Sh252 bil) Desemba, 2014 kutoka Dola 38 milioni (Sh68.4 bil) Januari mwaka huo.
Alisema mabehewa mapya ya abiria yanatarajia kuanza kufanya kazi Aprili baada ya kukamilisha taratibu za Sumatra huku akibainisha kuwa hadi Julai mwaka huu watakuwa na vichwa 60 dhidi ya 107 vinavyohitajika.

Tuesday 10 March 2015

Mtoto mwingine akatwa kiganja Sumbawanga

Sumbawanga. Mtoto mwenye ulemavu wa ngozi ‘albino’ Baraka Cosmas (6) anayeishi na wazazi wake kijijini Kipeta, Bonde la Ziwa Rukwa wilayani Sumbawanga ameshambuliwa na kujeruhiwa vibaya kwa kukatwa kiganja cha mkono wake wa kulia na watu wasiojulikana kisha kutokomea nacho kusikojulikana.
Tukio hilo limetokea wakati Serikali ikiwa katika mkakati kabambe wa kupambana na mauaji ya albino na ikiwa ni wiki chache tu tangu mtoto mwingine Yohana Bahati aliyekuwa na umri wa mwaka mmoja kutekwa Februari 15, mwaka huu na kukutwa ameuawa katika eneo la Shilabela.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Jacob Mwaruanda alisema tukio hilo la kikatili lilitokea saa saba usiku wa kuamkia juzi.
Alisema wakati hayo yakitokea baba mzazi wa mtoto huyo inadaiwa alikuwa amelala katika nyumba ya mkewe mdogo kijijini humo.
Kamanda Mwaruanda alisema mtoto huyo amelazwa katika Kituo cha Afya cha Kamsamba wilayani Momba mkoani Mbeya kwa matibabu akiwa pamoja na mama mzazi.
Mwaruanda alisema, “Watu watatu majina yao yamehifadhiwa wanashikiliwa na polisi na uchunguzi zaidi kuhusiana na tukio hilo unaendelea ili kuwasaka wahusika na kiungo cha mtoto huyo.”
Mama mzazi Prisca Shaaban (28), alisema tukio hilo lilimkutana saa saba usiku, wakati akitaka kutoka nje kujisaidia.
“Nilikutana na mtu akifungua mlango, akanipiga ni kitu kichwani kisha nikazimia, nilipozinduka nikapiga kelele na majirani wakafika ndipo nilipogundua mtoto wangu amekatwa kiganja cha mkono wa kulia,” alisema mama mzazi.

Dk Slaa: Nalindwa na Mungu

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa amesema analindwa na Mungu na ndiyo maana chama hicho kimegundua mpango wa mlinzi wake kushawishiwa na maofisa usalama wa taifa ili kumwekea sumu katika chakula au maji.
Mlinzi huyo (jina tunalihifadhi kwa sasa) ambaye alikamatwa na kufikishwa katika kituo cha polisi cha Oysterbay juzi, pia anadaiwa kutumiwa na kigogo mmoja wa CCM kuiba siri za chama hicho.
Tayari polisi imeanza kuchunguza taarifa hizo na jana Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura aliliambia gazeti hili kuwa mtuhumiwa huyo ana haki kama watuhumiwa wengine wanaofikishwa polisi wakikabiliwa na kesi za jinai na kusisitiza kuwa; “Tuhuma zinazomkabili ni za kawaida na tunazichunguza.”
Akieleza alivyopokea taarifa hizo Dk Slaa alisema, “Ninalindwa na Mungu ndivyo ninavyoweza kusema. Chadema sisi huwa tunaanza na Mungu na kumaliza na Mungu. Ushahidi umewekwa wazi na hili ni jambo la kweli na limenigusa kwa kiasi kikubwa.”
Alisema baadhi ya mambo yaliyofanywa na mlinzi wake ameyaona kwa macho na kusisitiza kuwa njama zinazofanywa na wanaomtumia haziwezi kukiondoa chama hicho katika harakati zake za kila siku.
“Tupo makini ndiyo maana tumebaini yote. Tunawajua waliohusika na tupo makini katika kuwafuatilia. Kama Mungu yupo upande wetu tumuogope nani zaidi,” alisema.
Alisema Chadema ina safari ndefu hivyo ni lazima wana-Chadema kuvaa viatu ili kujikinga na vumbi na uchafu wa kila aina, akimaanisha kuwa chama hicho kinakumbana na vikwazo vingi.
Tuhuma dhidi ya mlinzi huyo zilitolewa juzi na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Mabere Marando kuwa wamebaini nyendo za mlinzi huyo na kuzifuatilia kwa ukaribu hadi kupata taarifa hizo alizosema ni ukweli mtupu.
Hili ni tukio la tatu kwa Chadema kudai kuna mipango ya kumfuatilia Dk Slaa, mara ya kwanza ilikuwa Februari 2009 alipobaini kutegewa vinasa sauti hotelini mkoani Dodoma na mkakati uliotajwa kuwa wa kuwaua yeye, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa Ubungo, John Mnyika.
Akieleza jinsi walivyombaini mlinzi huyo, Marando alisema pamoja na ushahidi wa mawasiliano ya simu, lakini pia mlinzi huyo alikiri kwa kinywa chake kutumiwa na maofisa hao ambao hakuwataja majina lakini alisema wako 22.
“Mlinzi alitueleza kwamba alikuwa akipewa fedha kwa ajili ya kutoa siri za vikao vya chama kupitia simu yake…kwa kuwa anaruhusiwa kuingia kwenye vikao vya chama hicho kama mlinzi amekuwa akitegesha simu yake ili kuwapa taarifa watu wa CCM `live’ ili wasikie kila kinachojadiliwa,” alidai Marando.
Marando aliyewahi kuwa ofisa wa usalama wa taifa na kuongeza kuwa wako mbioni kufikisha suala hilo polisi.
Mipango yenyewe
Akifafanua namna mipango hiyo ilivyofanywa, Marando alidai walibaini mlinzi huyo kutumiwa muda wa maongezi kwa nyakati tofauti wa jumla ya Sh7 milioni kwenye simu zake.
Marando alisema, “Kilichokuwa kinatokea ni kwamba kigogo wa CCM (anamtaja) na wenzake walikuwa wanasikia kila kinachozungumzwa kutoka kwenye vikao vya ndani vya Chadema kwa sababu ya mlinzi huyo.”
Kigogo huyo wa CCM hakupatikana juzi na jana kujibu tuhuma dhidi yake, lakini ofisa mmoja wa makao makuu alisema taarifa hizo zimewafikia na zitajibiwa kwa njia rasmi.
Kadhalika, Marando alisema walibaini kuwa mlinzi huyo amekuwa akizungumza kwa simu kwa saa mbili hadi tatu na maofisa usalama hao ili kuwapa taarifa mbalimbali za chama.
Marando alisema kwa miaka miwili mfululizo mlinzi huyo amekuwa na mawasiliano ya mara kwa mara na ofisa mmoja usalama wilayani Kinondoni ambaye ana uhusiano wa karibu na kigogo huyo wa CCM.

Wakulima wa kahawa kunufaika


Dar es Salaam. Wakulima wa kahawa nchini wataendelea kunufaika na zao hilo baada ya kuanzishwa kwa viwanda vya usindikaji.
Mkurugenzi Mtendaji Kampuni ya Chai Bora Kapila Ariyatilaka alisema hayo jana wakati wa uzinduzi wa bidhaa zitokanazo na kahawa.
Alisema wameingiza bidhaa mpya sokoni zitakazopanua wigo wa soko la kahawa na kuwanufaisha zaidi wakulima.
“Tumekuja kupanua wigo wa soko la kahawa, tuna mahitaji ya wastani wa tani 500 kwa mwezi, kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa zetu hususan ile ya Cafe Bora,” alisema na kuongeza:
“Lengo la kampuni ni kutosheleza mahitaji ya ndani pamoja na nchi za Afrika Mashariki.
Ariyatilaka alisema wakulima wa nyanya, pilipili na bidhaa nyingine pia wana fursa nzuri ya soko baada ya kampuni hiyo kuingia makubaliano ya kibiashara na Kampuni ya Dabaga iliyopo Iringa.
“Tunaangalia zaidi fursa ya masoko kwa bidhaa za mashambani kutokana na changamoto zinazowakabili wakulima, ndiyo maana tunashirikiana na Dabaga,” alisema.
Alisema iwapo bidhaa za Dabaga zitauzwa zaidi, mahitaji yataongezeka kwa wakulima wa nyanya Iringa na kwingineko.
“Tutakuwa tumewawezesha wakulima kuongeza kipato na pia Serikali itapata kodi zaidi kutokana na mauzo ,” alisema
Meneja wa Maendeleo ya Biashara wa Kampuni ya Chai Bora, Martin Ng’ethe alisema Tanzania inajivunia kuwa na aina zote za kahawa.
Alizitaja kuwa ni Arabika na Robusta tofauti na nchi nyingine zenye aina mmoja ya kahawa.

Zitto Kabwe avuliwa rasmi uanachama Chadema

Baada ya Mahakama Kuu Tanzania kanda ya Dar es Salaam leo kutupilia mbali kesi iliyokuwa imefunguliwa na Zito Kabwe dhidi ya Chama Cha Demokrasia na maendeleo (Chadema) ya kuhoji uhalali wa uanachama wake ndani ya chama hicho…
Habari zilizotufikia hivi punde zinaeleza kuwa Mwanasheria Mkuu wa Chama cha Demokrasia na maendeleo Tundu Lissu ametangaza kuvuliwa rasmi uanachama wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini Zitto Kabwe.
Akitangaza hatua hiyo ya kumvua uanachama,Lissu amesema kanuni na sharia za chama hicho ziko wazi na zinaelekeza kuwa endapo mwanachama yeyote atakishtaki chama hicho mahakamani na iwapo atashindwa atakuwa amejiondoa mwenyewe kwenye chama

Friday 6 March 2015

Viongozi kujiuzulu pekee haitoshi

Jana Profesa Sosperter Muhongo alitangaza kujiuzulu nafasi yake ya Waziri wa Nishati na Madini, akieleza kuwa anataka nchi isonge mbele kwa kuwa suala la kumtaka Rais amwondoe kutokana na kashfa ya uchotwaji fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow, limesababisha mambo mengi kukwama.
Profesa Muhongo amekuwa waziri wa pili kuondoka baada ya Profesa Anna Tibaijuka kuvuliwa uwaziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kutokana na kuingiziwa kwenye akaunti yake Sh1.6 bilioni na mmiliki wa zamani wa IPTL, fedha ambazo zinahusishwa na sakata la escrow.
Mbali na mawaziri hao, tayari Jaji Fredrick Werema amejiuzulu kazi yake ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, akieleza kuwa ushauri wake kuhusu fedha za escrow haukueleweka na kusababisha tafrani.
Pia, katibu mkuu wa wizara hiyo, Eliackim Maswi amesimamishwa kazi kupisha uchunguzi wa sakata hilo, wakati watumishi watano wa Tanesco, Benki Kuu (BoT) na Mamlaka ya Mapato (TRA) wamefikishwa mahakamani wakishtakiwa kwa kupokea rushwa inayohusu sakata hilo. Kashfa hii ni moja ya matukio mengi makubwa yaliyosababisha Rais kufanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri. Baadhi ya matukio hayo ni kashfa ya Richmond, CAG na Operesheni Tokomeza ambazo zilisababisha Rais kupangua baraza lake.
Ni jambo la kupongeza kwamba angalau hatua zimechukuliwa kwa kiwango fulani katika kushughulikia tatizo hilo lililohusu uchotwaji wa takriban Sh306 bilioni kutoka kwenye akaunti hiyo iliyokuwa BoT.
Kitu cha ajabu ni hii tabia inayoendelea kujengeka ya kuibuka kwa kashfa, mawaziri kujiuzulu, kuundwa kwa baraza jipya na baadaye mambo kuendelea kama kawaida kusubiri kashfa nyingine kuibuka bila ya hatu za dhati kuchukuliwa kudhibiti matukio kama hayo.
Jambo la ajabu ni kwamba kila kashfa inapoibuka, hutumika nguvu nyingi kuizua au kutetea viongozi wa Serikali hadi mambo yanapoonekana kuwa yamekuwa makubwa ndipo hatua zichukuliwe.
Tumeona katika kashfa ya escrow zilitumika nguvu nyingi kutetea wahusika hadi maji yalipozidi unga ndipo hatua zilipochukuliwa na kushughulikia wahusika. Kitu kibaya ni kwamba hadi wakati hatua zinaanza kuchukuliwa, tayari Serikali inakuwa imeshafuka na wananchi wameshaumia.
Mabadiliko ya Baraza la Mawaziri sasa yamekuwa ya kawaida kwa kuwa kila yanapofanyika hazichukuliwi hatua thabiti kuzuia kashfa zisitokee. Suala la fedha kuchotwa kwa fedha zinazokuwa BoT sasa linaonekana kuwa la kawaida kwa kuwa kashfa ya Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje lilipotokea, hakukuchukuliwa hatua madhubuti kuziba mianya kama hiyo kwenye taasisi hiyo nyeti ya fedha.
Tunadhani ni wakati mwafaka sasa kwa Serikali kuweka misingi imara ya uongozi itakayowabana viongozi wetu kujiingiza kwenye kashfa kama hizo. Misingi hiyo pia ihusishe hatua kali ambazo zinaweza kuchukuliwa kwa viongozi ambao wataingia kwenye kashfa hizo kwa makusudi au uzembe ili kuzuia wengine kufanya mambo ya aibu na yanayoumiza wananchi.
Pia, siyo ufahari kuwawajibisha viongozi wakati ufisadi umeshafanyika kama ilivyokuwa kwenye sakata la EPA na sasa escrow kwa kuwa fedha za walipa kodi zinakuwa zimeshachotwa. Ufisadi unatakiwa uzuiwe mapema kuliepusha Taifa kupoteza mabilioni ya fedha na wanaowajibishwa wachukuliwe hatua kwa kujaribu kula njama za ufisadi na siyo kuadhibiwa kwa kufanya ufisadi.
Kadri Serikali inavyoonekana kuweka mikakati ya kuwakingia kifua watu wanaotuhumiwa kwa ufisadi, ndivyo vitendo hivyo vinavyozidi. Serikali inatakiwa ionyeshe kuchukia ufisadi kwanzaNa ikichukia ufisadi, basi kujiuzulu wa kuwavua madaraka wahusika kutakuwa ni moja ya hatua za kuwashughulikia wahusika wote nah ii itasaidia kupunguza vitendo hivyo..

Magufuli: Mbowe kama malaika

Hai. Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli jana aliungana na viongozi wenzake wa Serikali kuwamwagia sifa viongozi wa vyama vya upinzani baada ya kumwelezea Mbunge wa Hai na Mwenyekiti Chadema, Freeman Mbowe kuwa ni mpigania maendeleo ya wananchi na kwamba alitakiwa awe malaika.
Dk Magufuli alimuelezea kiongozi huyo wa upinzani bungeni kuwa ni mtu ambaye anafuatilia maendeleo ya watu bila ya kujali itikadi zao.
Waziri huyo ameungana na Rais Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kusifu utendaji wa viongozi wa upinzani.
Februari 10, Rais Kikwete alisifu utendaji wa meya wa Manispaa ya Moshi, Jaffar Michael wa kuwaletea maendeleo wananchi, na siku 12 baadaye Waziri Pinda alimsifu mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa kwa kuwa kiongozi wa kwanza kuchangia vitanda 30 kwenye Hospitali ya Frelimo.
Jana, Dk Magufuli alimmwagia Mbowe sifa hizo katika mkutano wa hadhara baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya Kwasadala-Masama-Machame katika Jimbo la Hai inayojengwa kwa kiwango cha lami.
“(Mbowe)Unadhihirisha kwamba maendeleo hayana chama na kwa kweli tukienda hivi Tanzania itakuwa ni nchi ya kutolewa mfano. Sincerely (kwa dhati) nakupongeza Mbowe na Mungu akubariki,” alisema.
Kabla ya Dk Magufuli kutoa pongezi hizo, Mbowe aliwataka wanasiasa kutekeleza ahadi zao kwa vitendo kwa kuwa maendeleo hayana itikadi.
“Mimi naamini maendeleo hayana itikadi. Jambo jema likifanywa na chama chochote cha siasa ama kiongozi wa chama chochote au Mtanzania, kama ni jema anastahili kupongezwa,” alisema Mbowe.
“Hakuna aibu ya kukiri pale jambo jema linapofanyika. Ujenzi wa Barabara ya Kwasadala-Mula-Machame ni jambo jema,” alisisitiza Mbowe.
Hata hivyo, alitumia mkutano huo wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Masama kumuomba Dk Magufuli atoe maagizo ya kiserikali baada ya viongozi wawili wa CCM kutishia kuchoma moto greda lake.
“Nimenunua greda ili tusaidiane na Serikali, lakini juzi diwani na mwenyekiti wa kijiji walitishia kuchoma moto greda eti kwa sababu mbunge hajapewa kibali cha kuchimba barabara,” alilalamika.
Mbowe alisema vyama vya siasa ni lazima vifanye pamoja kazi ya kuwaletea wananchi maendeleo.
Akihutubia mkutano huo, Dk Magufuli alisema Mbowe ni kiongozi mpole na mstaarabu na ndiyo maana kila ombi lake analoliwasilisha serikalini kwa ajili ya wananchi wake haligongi mwamba.
“Utapata wapi mtu mpole kama huyu? Alimuomba Rais pale kwamba niongezee kilometa tatu, (Rais) akatoa siku ile ile,” alisema.
“Rais Kikwete ni mwenyekiti wa CCM, lakini ameleta barabara hapa kwa mwenyekiti wa Chadema. Huo ndiyo utanzania na haya ndiyo tunatakiwa viongozi tuige mfano.”
Waziri Dk Magufuli alisema Mbowe ni miongoni mwa wabunge wachache wa upinzani ambao hawamsumbui bungeni na anapokuwa na jambo, huwa wanatoka nje na kuteta.
“Wako wengine wanapigaga kelele, lakini wewe unakuja tunazungumza. Unasema ndugu yangu, brother (kaka). Mbowe weweee! Ulitakiwa uwe malaika,” alisema Dk Magufuli katika mkutano huo.
Hata hivyo, Dk Magufuli aligeukia siasa na kusema ustaarabu na upole alio nao Mbowe unatokana na malezi mazuri ya CCM kwa vile wazazi wake walikuwa wana-CCM na kwamba pongezi anazitoa kwa dhati. Alimpongeza Mbowe kwa kununua greda, akisema fedha hizo angeweza kuzitumia kwa shughuli nyingine lakini akaamua kulinunua ili kusaidia wananchi wak

Makongoro Nyerere afunguka urais

Dar es Salaam. Wakati CCM ikielekea katika kipindi kigumu cha kuamua mgombea wake wa urais kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, Makongoro Nyerere, ambaye ni mtoto wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, amezungumzia taarifa zilizoenea kwenye mitandao ya kijamii zikimtaja kuwa na mpango wa kuwania nafasi hiyo ya juu nchini.
CCM, ambayo imeshika nchi tangu kurejeshwa kwa siasa za vyama vingi, hujikuta katika wakati mgumu kila wakati inapotakiwa kutoa mgombea wa kurithi nafasi ya Rais aliye madarakani baada ya kuongoza vipindi viwili vya miaka mitano kila kimoja.
Tayari wanachama wanne wa chama hicho tawala wameshatangaza rasmi kuwania urais huku wengine sita wakifungiwa kwa makosa ya kudaiwa kuanza kampeni mapema, huku kukiwa na mlolongo wa watu wanaotajwa kuwa na mpango wa kujitokeza kuwania nafasi hiyo, akiwamo Makongoro, ambaye imeelezwa kuwa ameshauriwa kuchukua uamuzi huo kujaribu kukinusuru chama kutokana na makundi yanayoonekana kujitokeza katika mbio hizo.
“Mimi si mtabiri, siwezi kukwambia nitagombea au la, lakini uamuzi wangu utajulikana mara kipenga kitakapopulizwa na CCM,” alisema Makongoro ambaye ni ofisa wa zamani wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) na mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (Eala).
Vyanzo hivyo vya habari vimeeleza kuwa mkakati wa kuhakikisha Makongoro anakuwa rais, unaratibiwa na baadhi ya makada waliowahi kufanya kazi na Mwalimu Nyerere.
Mkakati huo pia unatajwa kuwa ulianza pale alipochaguliwa kuwa mbunge wa Eala. Tayari Waziri Mkuu Mizengo Pinda, January Makamba, ambaye ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Lazaro Nyalandu ambaye ni Waziri wa Maliasili na Utalii na Hamisi Kigwangala (mbunge) wametangaza nia ya kuomba ridhaa ya CCM kuwapitisha kuwania urais.
Hata hivyo, upinzani mkubwa unaonekana kuwa kwa vigogo ambao hawajatangaza nia hiyo na ambao wanatumikia adhabu ya kufungiwa kwa zaidi ya miezi 12 kutokana na kikiuka taratibu za chama hicho.
Miongoni mwa ambao hawajajitokeza ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ambaye wafuasi wake wamekuwa wakijitokeza katika siku za karibuni kueleza wazi msimamo wao kuwa ndio chaguo sahihi, na Bernard Membe, ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Pia yumo Waziri Mkuu wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Frederick Sumaye, Spika wa zamani wa Bunge, Samuel Sitta, Waziri wa Kilimo na Chakula, Steven Wasira na Naibu Waziri wa Fedha-Sera, Mwigulu Nchemba, ambaye alionywa na chama hicho dhidi ya safari zake mikoani zilizodaiwa kuwa na dalili za kampeni.
Kauli ya Makongoro
Akizungumza na gazeti hili, Makongoro hakuonyesha kukataa wala kukubali kuhusu uamuzi wa kugombea nafasi hiyo iliyoshikwa na baba yake kwa takribani miaka 25.
“Ninachoweza kutabiri kwa sasa ni iwapo nina njaa basi lazima nitakula au simba akitokea lazima nikimbie. Kama nina usingizi na kuna kitanda karibu lazima nitalala lakini mambo mengine siwezi kuyasemea,” alisema Makongoro ambaye aliwahi kuwa mbunge wa Arusha Mjini kwa tiketi ya chama cha NCCR-Mageuzi. Alisema anasubiri siku ambayo CCM itatangaza mchakato wa kuchukua fomu ndipo hatma yake itajulikana.
Makongoro ni nani
Makongoro ni mtoto wa tatu wa familia ya Hayati Nyerere na Januari 30 mwaka huu alitimiza miaka 56 tangu azaliwe. Alipata mafunzo ya uongozi wa kijeshi Monduli kati ya mwaka 1980 na 1982.
Luteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi alipata elimu ya sekondari ya juu na ya kawaida kwenye Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Tabora wakati elimu ya msingi alisomea katika shule tatu tofauti za Arusha, Bunge na Isike kati ya mwaka 1971 na 1978.
Mwaka 1995 Makongoro alihama CCM na kujiunga na NCCR Mageuzi na katika uchaguzi wa kwanza tangu kurejeshwa kwa siasa za vyama vingi, Makongoro alishinda ubunge wa Jimbo la Arusha Mjini, lakini hakumaliza kipindi chake kutokana na ubunge huo kupingwa mahakamani na hatimaye kutenguliwa.
Aprili 7, 2012 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilimchagua kuingia kwenye Bunge la Afrika Mashariki.
Maoni ya wachambuzi
Alipoulizwa kuhusu taarifa hizo, mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku alisema masuala ya urais wa Makongoro aulizwe mwenyewe.
“Sitaki kuulizwa kuhusu hilo, mimi si meneja wa kampeni wa hao watu. Nitoe kabisa katika hilo,” alisema Butiku, ambaye ni miongoni mwa watu waliofanya kazi na Mwalimu Nyerere wakati wa utawala wa awamu ya Kwanza.
Mwanasiasa mkongwe nchini, Kingunge Ngombale-Mwiru alisema hawezi kutoa maoni yoyote hadi pale Makongoro atakapoamua kutangaza nia ya kuwania nafasi hiyo.
Kwa upande wake, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Benson Bana alisema iwapo Makongoro anahitaji kuwa rais, basi angepata kwanza ushauri wa wazee kutoka Butiama.
“Kwangu mimi Makongoro hana sifa ya kuwa rais, kwani kuna vigezo gani vinavyoangaliwa? Angeomba ushauri kwanza hata kwa kina Butiku,” alisema Dk Bana.
Alisema kwa anavyofahamu, CCM huchagua viongozi wazalendo, wenye maadili na historia za kupendeza wala si viongozi kutokana na koo zao au umaarufu tu. Kadhalika Dk Bana alisema mchakato wa kumpata rais ajaye ni mgumu hivyo akaitaka CCM isikurupuke.
Mchambuzi wa masuala ya siasa, Profesa Gaudence Mpangala alisema haoni tatizo kwa mtoto huyo wa muasisi wa Taifa kwa kuwa ana sifa zote za uongozi na hana sifa ya ‘uchafu.’
“Ukizungumzia usafi wa viongozi, hana neno. Anaweza kuwa kiongozi mzuri tu na pia ana haki kikatiba,” alisema.
Profesa Mpangala alisema licha ya watu kukosoa kuwa watoto wa viongozi wa zamani wanatengenezwa kuwa viongozi, lakini kama mtu ana sifa basi hana budi kugombea.

Albino wapambana wakienda kwa Rais Kikwete

Dar es Salaam. Hali ya sintofahamu ilitokea jana baada ya wanachama wa Chama cha Albino Tanzania (Tas) kumshambulia kiongozi wao, Ernest Kimaya wakati wakiwa njiani kuelekea Ikulu ambako Rais Jakaya Kikwete aliwaita kwa mazungumzo.
Pembeni ya barabara inayopakana na Ikulu, karibu na jengo la Wizara ya Elimu wakati wakielekea kumuona Rais Kikwete, wanachama hao walianza kumshambulia Kimaya wakidai kuwa si kiongozi halali, lakini aliokolewa na maofisa usalama waliokuwapo katika tukio hilo.
Wanachama hao walitaka kushinikiza na wao kumwona Rais Jakaya Kikwete badala ya viongozi 15 ambao ndiyo waliotakiwa wamwone Rais na kuzungumza naye. Saa moja baadaye, viongozi hao wa Tas waliingia Ikulu kuonana na Rais Kikwete.
Wanachama hao walikuwa wakimtaka Kimaya aachie wadhifa wake kwa kuwa si kiongozi.
Kimaya alizomewa muda wote na kumvuta nguo na baadhi ya wanachama hao ambao walimtuhumu kuwa anajinufaisha na vifo vya albino vinavyozidi kutokea nchini.
Hata hivyo, Kimaya alishindwa kujizuia na kutaka kupigana na baadhi watu waliokuwa wakimzonga na kumtukana. Maofisa usalama walimchukua na kumwondoa eneo la tukio ili vurugu zisiendelee.
Baadhi ya wanachama wa Tas walisema viongozi wao wamejikusanya wenyewe kwenda Ikulu bila kuwashirikisha na kuwa hawafanyi mikutano ya mara kwa mara zaidi ya kuwaita kwenye maandamano.
Mmoja wa albino hao, Nuru Iddi alisema hawana imani na viongozi wao kwa sababu muda wao wa kuwepo madarakani uliisha tangu mwaka jana.
Alisisitiza kuwa tangu wakati huo hawajafanya uchaguzi wowote na viongozi wametulia ili waendelee kujinufaisha.
“Albino akiuawa kule Mwanza mimi ndiyo napata uchungu, siyo hawa viongozi... wao wanapokea michango mingi kutokana na vifo vya wenzetu lakini hawafanyi jambo lolote la maana kulinda maisha yetu,” alisema mwanachama huyo.
Iddi aliongeza kuwa wao ndiyo walitakiwa kuonana na Rais Kikwete ili wamueleze hali halisi na nini cha kufanya ili kulinda maisha yao.
Aliulaumu uongozi wa Tas kwa kutowashirikisha wao kama wanachama kutoa maoni ambayo yangewasilishwa kwa Rais.
Naye Mwalimu Matimbwa alisisitiza kuwa viongozi wao wako nje ya muda kikatiba. Alisema mwaka 2006 kulikuwa na kisa kimoja tu cha mauaji ya albino lakini mpaka sasa idadi imefikia 78. Aliushutumu uongozi wa Tas kutodhibiti ongezeko hilo la mauaji ya albino.
“Nasikia uchungu sana ninapoona wenzangu wanauawa lakini baadhi yetu wanajinufaisha na mauaji hayo. Hatuwezi kushinda vita hivi kama hatuna uongozi thabiti. Tunataka uchaguzi ufanyike haraka sana,” alisisitiza Matimbwa.
Matimbwa aliongeza kuwa katiba yao inataka uchaguzi ufanyike kila baada ya miaka mitano lakini uchaguzi huo haukufanyika mwaka jana.
Kimaya alikiri kuwa walitakiwa kufanya uchaguzi mwaka 2014, lakini walikubaliana na wanachama kuwa uongozi uliokuwepo madarakani kwa ngazi ya wilaya, mikoa na taifa uendelee na kazi.
“Sisi tupo madarakani kihalali kwa sababu wanachama wenyewe ndiyo walipendekeza kuwa tuendelee kuongoza. Hili ni kundi la wahuni tu, siyo wanachama wetu,” alisema kiongozi huyo kabla ya kushambuliwa na wanachama waliokuwa wakipiga kelele wakisema “hatumtambui, aachie kiti huyo”.
Kimaya alifafanua kuwa mara ya mwisho walifanya uchaguzi mwaka 2009, lakini mwaka jana walishindwa kufanya uchaguzi kwa sababu kulikuwa na mwingiliano wa mambo.
Rais Kikwete aliandaa chakula cha mchana na viongozi wa Tas, Ikulu jijini Dar es Salaam. viongozi wa Tas walipata nafasi ya kuongea naye juu ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi yanayoshika kasi nchini kwa sasa.