Mgombea
urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa na Waziri Mkuu mstaafu,
Frederick Sumaye wakiwapungia wananchi wa mjini Ngombe walipokuwa
wakiwasili katika Uwanja wa National Housing mjini humo ulipofanyika
mkutano wa kampeni za mgombea huyo jana. Picha na Edwin Mjwahuzi
Ruvuma. Mgombea urais wa Chadema kwa mwamvuli wa vyama
vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa amesema
akiwa rais wa Awamu ya Tano atafuta maadui watatu ambao ni ujinga,
maradhi na umasikini waliodumu tangu nchi ipate uhuru mwaka 1961.
Akizungumza
katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika Uwanja wa Lembuka katika
Kijiji cha Madaba mkoani Ruvuma, Lowassa aliyekuwa akitumia staili ya
kuwauliza wananchi matatizo yanayowakibili na kisha kuwajibu
atakavyoyatatua, alisema tangu nchi ipate uhuru maisha ya Watanzania ni
duni na kuahidi kuwaondoa katika umasikini.
Wakati
Lowassa akisema hayo, Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye aliwataka
wananchi kuipa Chadema na Ukawa miaka mitano tu ili iweze kuwaletea
maedeleo na kama wakishindwa, warudi tena CCM.
“Jambo
kubwa ni kupiga kura na kuzilinda na ikiwezekana akina mama mpike
chakula kabisa nyumbani ili waume zenu wakifika nyumbani wajipakulie
wenyewe. Tusipoitoa CCM madarakani hatutaweza kuwatoa tena na lazima
wang’oke safari hii. Hata wana-CCM wenzangu nawashauri waondoke huko na
kujiunga na sisi. Ondokeni huko nyumba inawaka moto,” alisema Lowassa.
Katika
mkutano huo uliohudhuriwa na watu wachache ikilinganishwa na mikutano
mingine ya kampeni ya mgombea huyo wananchi hao walieleza kuwa
wanakabiliwa na ukosefu wa maji na umeme, migogoro ya ardhi, ada na
michango iliyokithiri katika shule pamoja na ushuru katika mazao.
“Tutamaliza tatizo la umeme ndani ya mwaka mmoja,
tutamaliza suala la kuporwa ardhi,” alisema Lowassa huku akiwahoji
wananchi wa kijiji hicho kwanini wakubali kuporwa ardhi.
Wananchi
hao walisema katika vituo vya afya wagonjwa wanaruhusiwa kurudi
majumbani kutokana na vituo hivyo kukosa maji sambamba na kutozwa ushuru
wa mazao usiokuwa na kichwa wala miguu.
Akizungumza
katika mkutaano huo, Waziri Mkuu mstaafu Frederick Sumaye alisema
maendeleo ya Tanzania hayafanani na rasilimali zilizopo nchini,
akiwataka wananchi kuyakubali mabadiliko ili kuepuka matatizo mengine.
“Nilikuwa
waziri mkuu kwa miaka 10 lakini nchi haikuwa na vita. Mkichagua
upinzani kutakuwa na amani kama kawaida,” alisema Sumaye huku akitolea
mfano yaliyotokea Masasi ambapo wananchi walichoma moto vituo vya polisi
na Halmashauri baada ya bodaboda kugongana na gari la polisi, “Hali
hiyo inatokana na wananchi kuchoka kuona viongozi waliowachagua
wananeema na wao wanaendelea kuwa masikini.”