BEI ya kuunganisha umeme katika vijiji
ambavyo bomba la gesi linapita kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam,
imeshushwa zaidi na kuwa Sh 27,000. Waziri wa Nishati na Madini, Profesa
Sospeter Muhongo, ametangaza kuanzia mwaka huu wanavijiji ambako bomba
la gesi linapita wataunganishiwa umeme kwa bei hiyo.
Profesa Muhongo alitangaza bei hiyo
wakati wa uzinduzi wa upelekaji umeme katika Wilaya ya Nanyumbu mkoani
Mtwara, ambao ulifanywa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Nanyumbu ni
miongoni mwa wilaya tano za Mkoa wa Mtwara, lakini ndiyo pekee ambayo
makao yake makuu yalikuwa hayajaunganishwa na umeme.
Profesa Muhongo alisema Wizara yake
imefikia uamuzi huo baada ya agizo la Waziri Mkuu ambaye aliitaka
iangalie namna wanakijiji hao watakavyofaidika na bomba hilo ambalo
linapita katika makazi yao.
“Sasa napenda kutangaza, kwamba baada ya
agizo hili la Waziri Mkuu, nimekaa na wataalamu wangu na tumeafikiana
kuwa wanavijiji hawa ambako bomba la gesi linapita, waunganishiwe umeme
kwa Sh 27,000 tu, duniani kote hakuna Serikali inayojali watu wake kama
tulivyofanya sisi,” alisema Profesa Muhongo.
Juzi Pinda aliiagiza wizara hiyo
kuhakikisha vijiji hivyo vinaunganishiwa umeme kwa bei rahisi, ili
wananchi waone kuwa ni sehemu ya jamii inayofaidika na bomba hilo ambalo
linatarajiwa kuwa ‘mwarobaini’ wa kumaliza tatizo la umeme nchini.
Pia Waziri Mkuu aliagiza Wizara hiyo
kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), iangalie namna
gani itahamasisha wanavijiji hao kwa kuwapa huduma zitakazowasaidia
kuinua kipato chao; lakini pia kwa kujengea vijiji hivyo, huduma za
jamii kama zahanati na shule.
Katika hotuba yake, pia Muhongo alisema
Serikali inaendelea na juhudi za kupeleka umeme vijijini, ili angalau
ifikapo mwaka 2015 asilimia 30 ya Watanzania wawe wamepewa huduma ya
nishati hiyo. Kwa sasa ni asilimia 23 tu ya Watanzania ndio wanapata
huduma hiyo.
Muhongo alisema ili kufikia lengo hilo,
Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limeagizwa mwaka huu liwafungie
umeme wateja wapya wapatao 250,000 kutoka wateja 99,000 ambao
wamefungiwa mwaka huu.
Pia alihadharisha wananchi wanaokwamisha miradi ya umeme vijijini kwa kudai fidia kuwa watasababisha lengo hilo lisifikiwe.
“Hivi kuna mtu hapa anadai fidia kutokana na mpango huu wa kuweka umeme hapa?” Alihoji Muhongo na kuongeza;
“Nashukuru kama hakuna mtu wa namna
hiyo. “Kama mtajitokeza kudai fidia tutalazimika kusimamisha mradi huu
ili tutafute fedha za kulipa fidia kwanza na fedha za umeme tutazipeleka
sehemu nyingine,” alisema Muhongo.
Akitoa taarifa ya mradi huo wa umeme
wilayani Nanyumbu, Meneja wa Kanda wa Tanesco, Mahenge Mgaya alisema
kazi za kufikisha umeme makao makuu ya Wilaya ya Nanyumbu na vijiji vya
jirani, zinahusisha ujenzi wa kilometa 139 za njia ya umeme msongo wa
kilovoti 33 kutoka Masasi hadi Mtambaswala.
Alisema gharama za mradi huo ni Sh
bilioni 5.9 ikiwa ni pamoja na za ujenzi wa kilometa 50 za njia ya umeme
wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 34 na kuunganisha wateja wapatao
780.
Pinda aliyezindua mradi huo alisema
Serikali imedhamiria kuongeza idadi ya Watanzania wanaopata huduma ya
umeme hasa vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
No comments:
Post a Comment