Tuesday 28 January 2014

Kufungiwa umeme 27,000 alisema Waziri Muhongo



BEI ya kuunganisha umeme katika vijiji ambavyo bomba la gesi linapita kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam, imeshushwa zaidi na kuwa Sh 27,000. Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, ametangaza kuanzia mwaka huu wanavijiji ambako bomba la gesi linapita wataunganishiwa umeme kwa bei hiyo.
Profesa Muhongo alitangaza bei hiyo wakati wa uzinduzi wa upelekaji umeme katika Wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, ambao ulifanywa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda. Nanyumbu ni miongoni mwa wilaya tano za Mkoa wa Mtwara, lakini ndiyo pekee ambayo makao yake makuu yalikuwa hayajaunganishwa na umeme.
Profesa Muhongo alisema Wizara yake imefikia uamuzi huo baada ya agizo la Waziri Mkuu ambaye aliitaka iangalie namna wanakijiji hao watakavyofaidika na bomba hilo ambalo linapita katika makazi yao.
“Sasa napenda kutangaza, kwamba baada ya agizo hili la Waziri Mkuu, nimekaa na wataalamu wangu na tumeafikiana kuwa wanavijiji hawa ambako bomba la gesi linapita, waunganishiwe umeme kwa Sh 27,000 tu, duniani kote hakuna Serikali inayojali watu wake kama tulivyofanya sisi,” alisema Profesa Muhongo.
Juzi Pinda aliiagiza wizara hiyo kuhakikisha vijiji hivyo vinaunganishiwa umeme kwa bei rahisi, ili wananchi waone kuwa ni sehemu ya jamii inayofaidika na bomba hilo ambalo linatarajiwa kuwa ‘mwarobaini’ wa kumaliza tatizo la umeme nchini.
Pia Waziri Mkuu aliagiza Wizara hiyo kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), iangalie namna gani itahamasisha wanavijiji hao kwa kuwapa huduma zitakazowasaidia kuinua kipato chao; lakini pia kwa kujengea vijiji hivyo, huduma za jamii kama zahanati na shule.
Katika hotuba yake, pia Muhongo alisema Serikali inaendelea na juhudi za kupeleka umeme vijijini, ili angalau ifikapo mwaka 2015 asilimia 30 ya Watanzania wawe wamepewa huduma ya nishati hiyo. Kwa sasa ni asilimia 23 tu ya Watanzania ndio wanapata huduma hiyo.
Muhongo alisema ili kufikia lengo hilo, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limeagizwa mwaka huu liwafungie umeme wateja wapya wapatao 250,000 kutoka wateja 99,000 ambao wamefungiwa mwaka huu.
Pia alihadharisha wananchi wanaokwamisha miradi ya umeme vijijini kwa kudai fidia kuwa watasababisha lengo hilo lisifikiwe.
“Hivi kuna mtu hapa anadai fidia kutokana na mpango huu wa kuweka umeme hapa?” Alihoji Muhongo na kuongeza;
“Nashukuru kama hakuna mtu wa namna hiyo. “Kama mtajitokeza kudai fidia tutalazimika kusimamisha mradi huu ili tutafute fedha za kulipa fidia kwanza na fedha za umeme tutazipeleka sehemu nyingine,” alisema Muhongo.
Akitoa taarifa ya mradi huo wa umeme wilayani Nanyumbu, Meneja wa Kanda wa Tanesco, Mahenge Mgaya alisema kazi za kufikisha umeme makao makuu ya Wilaya ya Nanyumbu na vijiji vya jirani, zinahusisha ujenzi wa kilometa 139 za njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 kutoka Masasi hadi Mtambaswala.
Alisema gharama za mradi huo ni Sh bilioni 5.9 ikiwa ni pamoja na za ujenzi wa kilometa 50 za njia ya umeme wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transfoma 34 na kuunganisha wateja wapatao 780.
Pinda aliyezindua mradi huo alisema Serikali imedhamiria kuongeza idadi ya Watanzania wanaopata huduma ya umeme hasa vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

No comments: