Friday 28 March 2014

Siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili kikatiba

Katika maisha ya kawaida, binadamu ana msimamo wake na hata uamuzi  asiopenda ubadilike.
Katika medani ya siasa nchini msimamo wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kuhusu Muungano na muundo  unafahamika. Ni muundo wa kutaka  Serikali mbili ambao chama hicho unakipigania kwa udi na uvumba.
Hata hivyo, msimamo huo ni kinyume na mapendekezo au matakwa ya wengi kama ilivyoainishwa kwenye Rasimu ya Pili ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
 Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba ilikusanya maoni ya wananchi na ilipendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu.
Hivi karibuni akifungua Bunge Maalumu la Katiba, Rais Jakaya Kikwete akaunga mkono msimamo wa chama chake, jambo lililoibua mjadala unaoendelea hadi sasa.
Hoja ya Serikali mbili
Kwanini CCM wanataka Serikali mbili na siyo tatu au moja kama ilivyo maoni ya wananchi walio wengi kwa mujibu wa maelezo ya Tume ya Warioba? Makala haya yanachambua hoja hiyo.
 Profesa Bakar Mohammed ni Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anayesema msimamo wa CCM wa kudai Serikali mbili unatokana na hofu ya uhafidhina wa kuogopa mabadiliko.
Anasema viongozi wengi wa CCM wanasumbuliwa na hofu na woga wa mabadiliko na kwamba wanakuwa wagumu kuyakubali  yanapotaka kutokea.
“Kama mtu unaangalia madaraka zaidi, lazima kunakuwa na woga, na hii ni hulka ya binadamu kuwa na woga wa kuacha kile ulichokizoea… Lakini ukiangalia masilahi ya nchi na kuacha yale yanayokusukuma kusingekuwa na wasiwasi huu unaoonekana sasa,” anasema.
Anasema CCM inachofanya ni kuhakikisha haking’oki madarakani, huku viongozi wake wakiamini kuwa wana sifa za kuongoza na siyo wengineo.
Profesa Bakari anailinganisha hofu ya sasa ya CCM na ile waliyokuwa nayo viongozi wa chama hicho miaka ya 1990 zilipoanza vuguvugu za mabadiliko ya siasa za vyama vingi. Anasema CCM kiliendesha propaganda kuwa mfumo wa vyama vingi haukuwa na tija na ungeleta vita.
Hofu hiyo anasema ndiyo inayokifanya chama hicho kikongwe kuhofia kung’olewa madarakani.
 “Woga huo bado upo, wanaogopa pengine mfumo ukiwa wa Serikali tatu uwezekano wa wao kubaki madarakani utakuwa mdogo,” anafafanua.
Anaongeza kusema kuwa  hofu ya CCM siyo kwa ajili ya masilahi ya nchi,  badala yake inaonekana chama kinaangalia masilahi yake.
Ingekuwa vyema anasema kwa CCM  kueleza madhara yanayoweza kulikumba taifa ikiwa muundo wa Serikali tatu utapita.
 “Wanatoa hoja kuwa mfumo wa Serikali tatu unaweza kusambaratisha nchi, lakini hakuna uhakika kama mfumo huu uliopo nchi hauwezi kusambaratika,” anasema.
Hofu ya kuyumba na kuanguka
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk. Benson Bana anasema siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili inatokana na hofu ya kuyumba na kuanguka.
Anasema CCM kimekuwa madarakani na mfumo huo kwa miaka 50 na kwamba hofu yao ni kuwa ukiondoa Serikali mbili kinaweza kuyumba na kuachia madaraka.
Anasema misingi ya wanasiasa ni madaraka, na kwamba ukishayapata, huwezi kuyaachia kirahisi.
“Misingi ya wanasiasa ni madaraka… Kuyalinda, kuyahifadhi na kuyatumia madaraka yale kwa namna yoyote…Huwezi kuyaachia madaraka kirahisi. Utafanya ujanja, utatumia mbinu chafu  ili tu kuhakikisha unabaki madarakani, na hiki ndicho wanachofanya CCM,” anasema.
Dk. Bana anasema CCM kingeeleweka na kingekuwa na mwonekano mzuri zaidi endapo wangepigania kuwapo kwa Serikali moja.
“Wangekuwa wanataka muungano imara, endelevu na uliokomaa wangeelekeza katika Serikali moja…Lakini hawataki kwa sababu wanajua moja inaweza ikawanyima uongozi,” anasema.
Dk. Bana anasema ni vyema wananchi wakaelimishwa huu muungano una faida gani na wanafunzi shuleni katika elimu ya uraia waelezwe faida zake.
“Ingekuwa wazi tungejua nani anafaidika na nini, mikopo misaada, nani anachangia nini…Je zile sababu za waasisi za kuungana bado zipo sasa miaka 50 ya Muungano, ule woga kuwa Zanzibar itamezwa bado upo leo?” Anahoji.
Anaongeza kuwa ni vyema kwa watawala kutazama  mazingira ya sasa ya siasa zetu kwa kile anachoeleza kuwa hata Katiba ikipita ikakubali kuwapo wa Serikali mbili, bado wananchi watahoji mantiki ya muundo huo.
Msomi mwingine wa siasa, Dk. Alexander Makuliko  anasema hofu ya CCM ni kuwa ndio iliyouasisi Muungano wa Serikali mbili, hivyo  isingependa hali hiyo ibadilike.
Anaendelea kusema kuwa CCM imezoea mfumo huu na kuwa ikiukosa itaathirika, kwakuwa ni sera yake na imekuwa ikiitekeleza, lakini msimamo wa  wananchi ndiyo kitu cha msingi kuzingatiwa. Hoja zijengwe na zisikilizwe, ubabe hautakiwi, busara inahitajika zaidi.
Anasema pamoja na suala la  Serikali mbili kuwa  ni pimajoto ya  uhai wa CCM,  hata hivyo hoja zinazotolewa katika kutetea msimamo wao ni nzuri tu na zinazoeleweka vyema.
“Sioni kama wanang’ang’ania, lakini ukweli ni kuwa kila chama kina sera yake, na CCM kimeweka sera yake katika suala la Muungano wao wanasema ni Serikali mbili, na siyo tatu…kwamba tatu zitaongeza gharama na mengineyo, ni sababu za msingi kabisa,” anasema.
Anaongeza kuwa hoja zinazotolewa na chama tawala ni kubwa na siyo za kupuuzwa, lakini vilevile kero zinazotajwa kuhusu mfumo wa Muungano uliopo nazo zipo na zinaweza kutatuliwa katika mfumo uliopo.
“Unajua hivi vyama kila kimoja kinataka kuvutia kwake, hata bila rasimu ya Warioba…Ninashauri walete hoja, kisha watu wazipime hizo hoja, kwanini serikali mbili, na wale wa tatu tayari wameleta hoja na ushahidi, watu waachwe wapime,” anasema na kuongeza:
‘’Jambo la msingi kuzingatiwa ni kuwa mawazo ya wananchi wengi yataonekana wakati wa kura za maoni. Angalizo ni  kuhakikisha kuwa kura hiyo isije ikachakachuliwa.’’

.. Samuel Sitta awekwa mtegoni

Dodoma/Dar. Suala la ama kutumia kura ya siri au ya wazi kuamua ibara za Rasimu ya Katiba jana liliuteka upya mjadala wa Kanuni za Bunge la Katiba, huku ikielezwa kuwa limewekwa kama mtego kwa Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta katika kuwania urais.
Sitta ni mmoja wa wanasiasa wanaotajwa kuwa katika kinyang’anyiro cha urais katika uchaguzi mkuu ujao kupitia CCM, huku akikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa mahasimu wake kisiasa ndani ya chama hicho.
Mjumbe wa Bunge la Katiba, Godbless Lema alimtaka Sitta kuwa makini na maelekezo aliyodai mwenyekiti huyo anapewa katika uendeshaji wa Bunge na kudai pia kuwa, kuna kundi la watu wanaotaka urais katika Uchaguzi Mkuu 2015 wanaotaka kumkwamisha.
Akichangia hoja ya mapendekezo ya mabadiliko ya kanuni yaliyotaka kupitishwa mifumo miwili ya kura kwa wazi na siri, Lema ambaye ni Mbunge wa Arusha alisema kwa mazingira ambayo yanaendelea, Sitta anapaswa kuwa makini na watu wanaompatia maelekezo wakitaka aonekane hafai baadaye.
“Ni vyema ukawa makini na mapendekezo unayoletewa kwa sababu hao wote pamoja na wanachama wa chama chako wanajua kama utaliongoza vizuri Bunge hili, basi unaweza ukapata tiketi ya kugombea urais 2015 ndani ya chama chako, lakini ukishindwa watakudhihaki kuwa umeshindwa, hivyo hutaweza kuliongoza taifa,” alisema Lema huku Sitta aliyeonekana awali akitabasamu, alibadilika na kumtazama mbunge huyo kwa umakini.
Lema alisema miongoni mwa wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM na kamati nyingine za Bunge hilo, kuna watu ambao wanataka kugombea urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Katika mjadala huo, ilionekana wazi kuwa wajumbe bado wamegawanyika pande mbili – CCM wakionekana kuunga mkono kura ya wazi na upande wa upinzani wakipigia chapuo kura ya siri.
Miongoni mwa waliopigia debe kura ya siri ni John Mnyika aliyesema suala la upigaji kura ni la kikatiba ili kuhakikisha kila mjumbe anapiga kura yake bila kushurutishwa, kushinikizwa wala kupokea maelekezo kutoka kwa mtu au chombo chochote.
Wajumbe hao walikuwa wanajadili mapendekezo yaliyowasilishwa jana na Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge, Pandu Ameir Kificho, baada ya juzi kuzua mvutano uliosababisha Bunge hilo kuvunjika ili kusubiri maridhiano ya pande zinazopingana.
Mapendekezo ya Kanuni
Kificho alisema, mapendekezo hayo yamefikiwa kutokana na masharti ya kanuni ya 59 (1) na 87 (1) kwamba kanuni ya 38 (1) iweke utaratibu wa kupiga kura ama ya wazi au ya siri, ambao utatekelezwa na mwenyekiti kwa kushauriana na katibu.
Alisema wakati wa kupiga kura ya siri kila mjumbe atapiga kura ya ‘ndio’ au ‘hapana’  kwa kutumia karatasi ya kupigia kura itakayokuwa imeandaliwa na katibu kwa ajili ya hilo.
Mjumbe Michael Laizer alisema wamechoshwa  na malumbano juu ya kura za wazi au siri, hivyo iwapo kuna wajumbe ambao hawataki mapendekezo ya kamati waondoke.
Naye Ezekiel Olouch alisema utaratibu unaopendekezwa na kamati haujawahi kufanyika mahala popote duniani.
Alisema kura ya siri imekuwa ikitumika kuamua mambo ya msingi na kuepusha mpasuko katika jamii hasa katika masuala ambayo yanaweza kuligawa taifa.
Mohamed Raza alisema msimamo wake ni kupiga kura ya wazi kwani wengi wanajua msimamo wake ambao ametoka nao Zanzibar.
Joshua Nassari alisema anashangazwa kuona Taifa linarejeshwa katika karne ya 18 katika upigaji wa kura kwa kung’ang’ania kura ya wazi wakati wao wamechaguliwa kwa kura za siri.
“Mwenyekiti wewe tumekuchagua kwa siri wajumbe wote wamepatikana kwa siri, iweje leo kulazimisha kura ya wazi ili wajumbe wa CCM watakaopiga kura za siri wachukuliwe hatua,” alisema Nassari.

Tuhuma nzito bungeni,ni za rushwa dhidi ya Waziri Mkuu Pinda

Dar es Salaam. Hali ya hewa jana ilichafuka kwenye Bunge la Katiba baada ya mjumbe Ezekiel Wenje kuwatuhumu Waziri Mkuu Mizengo Pinda na baadhi ya mawaziri kuwa waliwahonga baadhi ya wajumbe wa kundi la 201.
Katika tuhuma hizo, Wenje alimtaja Waziri Profesa Jumanne Maghembe, Dk. Shukuru Kawambwa na Gaudensia Kabaka akisema kuwa walitoa rushwa ya vyakula, maji na vinywaji kwa wajumbe hao ili waunge mkono msimamo wa serikali mbili.
Kauli hiyo, iliyotolewa katika mjadala wa mabadiliko ya kanuni, ilisababisha mawaziri hao kunyanyuka kujibu tuhuma hizo, huku Wenje akisisitiza kuwa aliyoyasema ni kweli tupu.
Vilevile baadhi ya wajumbe wanaotoka katika kundi hilo walicharuka na kujaribu kujitetea huku mmojawapo akitishia kuwa iwapo Wenje asingeomba radhi, asingetoka ndani ya Bunge hilo.
Hoja ilipoanzia
Wenje, ambaye pia ni mbunge wa Nyamagana (Chadema), alianza kwa kueleza kwamba wapinzani “walilia” sana kuwa Bunge la Katiba lisingekuwa na usawa kutokana na Chama cha Mapinduzi kuwa na wajumbe wengi, ndipo ikaonekana wapatikane wajumbe wengine 201, lakini jambo la ajabu ni kwamba walioteuliwa katika kundi hilo asilimia 80 ni makada wa CCM akiwamo mzee maarufu ambaye ameingizwa kama mganga wa jadi.
Ingawa hakumtaja jina, Wenje alikuwa anamaanisha kada mkongwe wa CCM, Kingunge Ngombale-Mwiru aliyeteuliwa kupitia kundi la waganga wa jadi.
Kuhusu rushwa, Wenje alisema:“…Sasa kuna wajumbe wa kundi la 201 walipelekwa kwa Profesa Maghembe na Dk. Kawambwa wamepeana rushwa, vikao vingi vilifanyika usiku. Hii haikubaliki.”
Baada ya kauli hiyo ya Wenje, Profesa Maghembe alisimama ghafla huku akionekana kutaharuki, ambapo Makamu Mwenyekiti Samia Suluhu Hassan alimpa nafasi ya kujieleza.
Profesa Maghembe alikiri kuwakaribisha baadhi ya wajumbe wa kundi hilo, akieleza kwamba ilikuwa ni katika hali ya ukarimu uliozoeleka miongoni mwa jamii ya Kitanzania.
“Kuna kundi lipo hapa ambalo linafanya kazi ya kudhalilisha wenzao. Ni kweli niliwaalika kwa chakula wajumbe hao kwa taratibu za kawaida, lakini hakuna mbunge hapa anayeshindwa kujinunulia chakula, hakuna anayeweza kupewa rushwa.
“Kwa sababu hiyo ninaomba kiti chako kimtake mjumbe aliyewasilisha hoja hiyo aniombe radhi. Wenje aniombe radhi,” alisema Profesa Maghembe akiwa katika hali ya hasira, huku kukiwa na sauti za kuzomea na kushangilia kutoka kwa wajumbe.
Makamu mwenyekiti pia alifanya jitihada za kuwataka wajumbe kuwa wavumilivu, huku akitoa nafasi kwa Dk. Kawambwa kujieleza akisisitiza kwamba ni tuhuma nzito. 
Kawambwa alisema: “Ni kweli nilikutana nao; ni wajumbe ambao wanatoka kwenye taasisi zinazojihusisha na masuala ya elimu, lakini mbona wameshafanya mikutano yao mingine mingi ambayo mimi hawakuniita. Kama mtu akiwa hana hoja bora akae chini.”
Makamu Mwenyekiti alimtaka Wenje aombe radhi kutokana na kauli yake, lakini katika hali ya kushangaza mjumbe huyo alisisitiza kwamba Profesa Maghembe na Dk. Kawambwa wamekiri.
“Maghembe amekiri aliwaita wafugaji na wavuvi ndiyo waliokula chakula cha rushwa, pia wapo wengine walienda kwa Waziri Gaudensia Kabaka, kuna ushahidi mama mmoja siwezi kumtaja jina hapa alikwenda huko akafukuzwa, nitakupa jina lake mwenyekiti baadaye. Aliambiwa kwamba anatoa siri… hoja iliyojadiliwa huko ilikuwa ni kwamba msimamo ni wa serikali mbili… rushwa ya chakula, maji na bahasha walipewa,” alisema Wenje na kusababisha kulipuka kwa kelele zaidi.
Wenje aliongeza kuwa kuna wajumbe wengine walikwenda hadi kwa waziri mkuu ambako walikula, walikunywa hadi saa 7:00 usiku.
Alisema wengine walikwenda kwa Gaudensia Kabaka (Waziri wa Kazi na Ajira) na walikula na kunywa na kupewa bahasha.
Baada ya Wenje kukaa, baadhi ya wajumbe wa kundi la 201 walichachamaa wakitaka kutetea hadhi yao, akiwamo mjumbe kutoka kundi la wafugaji, Esther Juma aliyesema hawatendewi haki kama kundi kusema kwamba walihongwa.
Alisema yeye ana ng’ombe 3,000 na asingeweza kwenda kupokea rushwa ya chakula na kumtaka mbunge huyo kuwaomba radhi la sivyo asingetoka mlangoni.
Wakati mjadala huo ukiendelea, mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta aliyekuwa ametoka kwa udhuru, alirejea kimya kimya, na kumtaka Wenje kueleza iwapo anadhani kauli yake haikuwaudhi baadhi ya wajumbe.
Wenje alikiri kuwa ni kweli baadhi ya wajumbe wameudhika kutokana na ukweli aliosema dhidi yao na kuwaomba radhi kwa ukweli huo.
Kauli hiyo ilimfanya Sitta kutangaza kuwa anapeleka suala hilo kwenye Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge na uamuzi utakaotolewa atautangaza bungeni.

Tuesday 25 March 2014

Baada ya matokeo Fanya uamuzi sahihi kujiendeleza kielimu

Wapo wanaofuata mkumbo wa kusoma mchepuo (combination) fulani kwa sababu marafiki zao wengi wameuchagua mchepuo huo. Aidha, wapo wanaolazimisha kusoma masomo magumu yaliyo nje ya uwezo wao kiakili.
Kwa mfano, unaweza kupata alama C katika mtihani wa Hisabati (Basic Mathematics), lakini alama hiyo siyo tiketi pekee ya kuchagua kusoma masomo yenye hesabu za kiwango cha juu (Advanced Mathematics).
Waliofeli nao?
Kama ilivyotangazwa na Baraza la Mitihani Tanzania, asilimia 78.91 ya wahitimu wamepata daraja la nne na sifuri. Ni dhahiri kuwa wanafunzi hawa hawana sifa ya kujiunga na kidato cha tano.
Hata hivyo, huo ndiyo uwe mwisho wa safari ya kusaka elimu kwa vile tu umefeli? Makala haya yanajaribu kutoa mapendekezo mbadala yanayoweza kutumiwa na wanafunzi ili kujiendeleza zaidi kielimu?
Kwanza ieleweke kutokuchaguliwa kidato cha tano au kufeli kidato cha nne si ishara mbaya maishani na wala haijawa sababu ya kuanza kuamini kuwa umeshafeli kimaisha.
Uzoefu unaonyesha hapa nchini kuna watu wengi baadhi yao leo ni maprofesa maarufu waliowahi kufeli katika madaraja fulani ya kielimu siku za nyuma, lakini kwa kuwa tu walikuwa na dhamira ya dhati na kutoa uamuzi sahihi, waliweza kujiendeleza na kufika kiwango hicho cha elimu kinachotamaniwa na kila mtu.
Nikupe siri moja ninayoifahamu kuhusu wasomi hawa, baadhi yao waliwahi kuwa walimu wangu pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hawa pamoja na wengine kuamua kuanza maisha ya familia au kikazi lakini walijiendeleza kupitia mfumo usio rasmi.
Unaweza kuihuisha ndoto yako ya kupata elimu kwa kurudia mitihani yako kwa mara nyingine. Mfumo wetu wa elimu unatoa fursa hiyo na ndiyo maana kuna utaratibu wa watahiniwa binafsi.
Rudi tena darasani. Kuna shule nyingi za sekondari zenye programu maalumu kwa ajili ya watu wanaorudia mitihani ya kidato cha nne tena kwa bei rahisi.
Zitafute shule hizi ila kuwa makini na vituo vinavyoitwa kwa Kiingereza ‘Tuition Centers’ ambavyo vingi vinajali masilahi kuliko ubora wa elimu.
Chunga jambo hili! Kuna mtindo wa wanafunzi wanaofeli kidato cha nne na kuamua kuingia kidato cha tano huku wakirudia mitihani yao. Hawa wanalazimika kusoma masomo ya mitihani wanayoirudia huku wakisoma pia masomo mapya ya kidato cha tano.
Huku ni kujidanganya, kwa mtindo huu, mwanafunzi husika hawezi kusoma kwa undani masomo ya kidato cha tano badala yake atakuwa anasoma ‘kimtego mtego’ ili afaulu tu mitihani ya ndani.
Fursa nyingine iliyopo kujiendeleza ni kusoma fani za ngazi ya cheti. Kusomea cheti siyo kuonekana mjinga, kwanza una uhakika wa kuajiriwa au kujiajiri. Kwa mtu mwenye ndoto ya kusoma zaidi, kipato cha ajira yako ndicho unachoweza kukitumia kujiendeleza zaidi.
Upo mfano mzuri wa walimu wa shule za msingi waliosomea ualimu kwa ngazi ya cheti. Wengi hujiendeleza kwa kurudia mitihani na hatimaye kufika vyuo vikuu.
Siyo ualimu pekee, kwa mujibu wa mfumo wa elimu nchini, kuna vyuo vingi vya kada ya kati vinavyotoa kozi za msingi kwa wahitimu wa kidato cha nne wakiwamo waliopata angalau daraja la nne.
Unachofanya ni kusomea cheti cha msingi kwa mwaka mmoja, kisha unaendelea kwa kusoma tena cheti cha juu kabla ya kupata fursa ya kusoma stashahada.
Kwa walio makini mlolongo huu wa elimu unaweza kukufikisha mbali. Unaweza kufika chuo kikuu kwa kutumia njia hii ya kusoma. Vipo vyuo vikuu vinavyowakubali wanafunzi hawa kwa sharti la kuwa vimesajiliwa na Baraza la Usimamizi wa Elimu ya Ufundi (NACTE).
Fursa nyingine inayotumiwa na baadhi ya wanafunzi wanaoishia kidato cha nne ni kusoma masomo ya ufundi katika vyuo vinavyosimamiwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA).
Wengi wamekuwa na mtazamo hasi na vyuo vya VETA wanasahau kuwa vyuo hivi vina msaada mkubwa kiajira na hata kujiendeleza zaidi kielimu.
Zaidi ya yote wigo wa mafunzo ya VETA umekua na kuhusisha mambo mengi ya kiufundi ya kisasa na yanayolipa kiajira iwe ajira binafsi au ajira rasmi. Kwa mfano, hivi sasa VETA inaendesha kozi katika sekta za madini, utalii, teknohama na nyinginezo muhimu zama za sasa.

Sitta ‘amkataa’ Warioba bungeni

Dodoma. Jaribio la kutaka kumrejesha bungeni Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba ili ajibu masuala yaliyoibuliwa na Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya kufungua Bunge limegonga mwamba.
Uamuzi wa kukataa ombi hilo ulitolewa jana na Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta wakati akijibu mwongozo ulioombwa na Mjumbe wa Bunge, Julius Mtatiro, akisema hadhani kama ni sahihi ombi hilo kutekelezwa.
Awali Mtatiro aliomba mwongozo kwa mwenyekiti, akitaka kujua iwapo kuna haja ya kumrejesha Jaji Warioba kutoa ufafanuzi juu ya baadhi ya hoja za Rais Kikwete ambazo zimekinzana na maoni ya wananchi yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba.
Mtatiro alisema: “Mtoa hoja mahususi alikuwa ni Jaji Warioba na Rais Kikwete alialikwa kama mgeni rasmi kufungua Bunge, lakini badala yake alikuja kujibu hotuba ya Warioba.
“Kwa sababu Rais alikaribishwa kama mgeni rasmi, lakini  alijibu  hoja za Warioba, je, hatuoni kama kuna haja ya kumrejesha mtoa hoja mahususi aje kujenga hoja  kutokana na alichosema Rais Kikwete?” alihoji Mtatiro ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CUF.
Katika ufafanuzi wake, Sitta alisema tayari amepokea kwa maandishi kutoka kwa baadhi ya wajumbe kuzungumzia suala hilo, jambo ambalo litafanyika lakini si kwa kumwita tena Jaji Warioba.
“Tunapenda kupata muda wa kuzungumzia  suala hili ili kuliweka sawa, hotuba zote mbili ambazo ni muhimu zitaandaliwa ili kupitiwa kuona kama malalamiko yanayotolewa yana hoja,” alisema Sitta.
Tangu Rais Kikwete ahutubie Bunge Ijumaa na kutoa hoja kinyume na mapendekezo ya Rasimu ya Katiba, hasa muundo wa Muungano, kumeibuka mijadala ya ama kuipinga au kuiunga mkono, huku wengine wakieleza kuwa imekiuka sheria.

CCM yaliteka Bunge la Katiba

Dodoma. Sasa ni wazi kwamba serikali mbili zimeonyeshwa taa za kijani baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kukamata uongozi wa Bunge Maalumu la Katiba.
Jana kamati 14 za Bunge hilo ziliwachagua viongozi wake; Mwenyekiti na Makamu na 12 kati yake zilichukuliwa na wajumbe kutoka CCM, chama ambacho tayari kimeweka wazi msimamo wake kuunga mkono Muungano kuwa ni serikali mbili.
Miongoni mwa waliochaguliwa wenyeviti ni Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Sera na Uratibu), Steven Wassira na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Ummy Mwalimu ambao wamekuwa mstari wa mbele kupigia chapuo mfumo huo badala ya serikali tatu zinazopendekezwa kwenye Rasimu ya Katiba.
Wengine ni Mbunge wa Same Mashariki, Anna Kilango – Malecela, Naibu Spika wa Bunge la Muungano, Job Ndugai, Mbunge wa Viti Maalumu, Kidawa Khamid Salehe, Mbunge wa Kuteuliwa, Shamsi Vuai Nahodha na Mbunge wa Mlalo, Hassan Ngwilizi.
Wengine wa CCM ni Mbunge wa Viti Maalumu, Anna Abdallah na aliyewahi kuwa Waziri katika serikali zilizopita Paul Kimiti. Pia wamo Mbunge wa Wawi ambaye alifukuzwa uanachama na chama chake cha CUF, Hamad Rashid Mohamed na Mwenyekiti wa kundi la wajumbe 201 wa kuteuliwa na Rais, Francis Michael.
Katika uchaguzi wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge, aliyekuwa mwenyekiti wa Muda na Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho alichaguliwa mwenyekiti na makamu wake, Dk Susan Kolimba.
Kamati ya Uandishi wa Katiba ilimchagua Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge na makamu wake, Mgeni Hassan Juma. Kwa kupata nafasi hizo ni dhahiri kwamba ‘mapishi’ ya uendeshaji wa Bunge hilo yatafanywa na CCM kwani mwenyekiti wake Samuel Sitta na makamu mwenyekiti Samia Suluhu Hassan pia ni makada wa chama hicho.
Wenyeviti hao wataungana na Sitta pamoja na Hassan kuunda Kamati ya Uongozi ya Bunge Maalumu, ambayo ndiyo itakuwa na mamlaka ya kupanga ratiba na miongozo mbalimbali ya uendeshaji wa Bunge hilo.
Waliochaguliwa kuwa makamu wenyeviti ni Profesa Makame Mbarawa, Shamsa Mwangunga, Fatma Mussa Juma, Dk. Sira Ubwa Mamboya, Assumpter Mshama, Dk. Maua Daftari na Waride Bakar Jabu. Wengine ni Biubwa Yahya Othaman, William Ngeleja, Salimin Awadh Salimin, Yusuf Massauni na Thuwayba Kisasi.
Mbowe atimuliwa
Katika uchaguzi huo, mjumbe wa Bunge hilo, Freeman Mbowe alitimuliwa katika kamati alikokwenda kushiriki uchaguzi kwa madai kwamba hakuwa mjumbe.
Mbowe alisema kabla ya uchaguzi huo alimfuata Mwenyekiti Sitta kumwomba wafanye marekebisho katika kamati tatu za Bunge.
Alisema waliafikiana kuwa Godbless Lema aliyekuwa Kamati namba saba ahamieKamati namba mbili na AnnaMary Stella Mallac aliyekuwa Kamati namba mbili ahamie Kamati namba sita.
Alisema kwa makubaliano hayo yeye (Mbowe) alihamia Kamati namba saba akitokea Kamati namba sita.
“Nilivyoingia katika ukumbi wa Igada, wajumbe walianza kuguna mara wakaanza kuzozana wakitaka wajumbe ambao hawakuwamo kwenye orodha ya kamati hiyo kutoka nje,” alisema na kuongeza;
“Waliamua kuitana majina, lakini hawakuona jina langu wakanitaka nitoke nje, nikawaeleza makubaliano kati yangu na Mwenyekiti (Sitta) lakini hawakuafiki walisisitiza nitoke ndani ya ukumbi huo.”
Alisema hatua hiyo iliwafanya makatibu wasaidizi kuitwa na kuelezwa kilichotokea ambapo waliwasiliana na Katibu wa Bunge hilo, Yahaya Khamis Hemed ambaye aliwajibu kuwa bado hajapokea taarifa za mabadiliko hayo na kuwataka wasubiri awasiliane na Sitta.
“Wakati nikiendelea kusubiria
jibu, mmoja wa wajumbe aliendelea kupaza sauti akitaka niondolewe ili waweze kupiga kura,” alisema.
Alisema hali hiyo ilimfanya yeye na baadhi ya wajumbe kutoka vyama vya upinzani, akiwamo Profesa Abdallah Safari kususia uchaguzi huo na kuondoka.
Mbowe alisema baada ya muda walifuatwa na makatibu wakiwaomba samahani warudi ukumbini kwa sababu wamepokea maelezo kutoka kwa Sitta. Sitta alithibitisha tukio hilo, lakini alisema halikuathiri matokeo ya uchaguzi kwa sababu kuondoka kwao hakukuathiri akidi inayotakiwa.

Monday 24 March 2014

Ndugai: Taifa lina tatizo la mgawanyo wa rasilimali

Mbunge wa Kongwa na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai ameomba ushauri kwa Seneta Amos Wako wa Kenya kuhusu mgawanyo wa rasilimali za taifa.
Ombi hilo la Ndugai, ambaye ni mjumbe wa Bunge la Katiba, lilitokana na historia aliyoitoa seneta huyo wa Busia Mashariki nchini Kenya, iliyotokana na uzoefu alioipata katika Mchakato wa kuunda na kuandika katiba ya nchi hiyo.
Mwishoni mwa wiki, Seneta Wako alieleza bungeni kuwa changamoto zilizokuwa zikiikabili Kenya wakati ikiandika Katiba yake, ni pamoja na wananchi kulalamikia mfumo wa mgawanyo wa rasilimali.
“Kulikuwa na madai kwamba hakukuwa na usawa katika kugawa keki ya taifa, maeneo yenye viongozi yalidaiwa kupendelewa kwa kuwa na huduma nzuri za kijamii kuliko mengine,” alieleza Seneta Wako.
Ndugai alipopata nafasi ya kuuliza swali, alisema tatizo la mgawanyo wa rasilimali lililokuwako Kenya, lipo hata hapa nchini lipo kwa kiwango kikubwa.
“Mikoa mingi inalalamikia uduni wa huduma kwa jamii. Kwa uzoefu wako unashauri nini kifanyike kutatua changamoto hii,” aliuliza Ndugai.
Seneta Wako alisema mgawanyo wa madaraka na rasilimali za taifa nchini Kenya unaendelea kushughulikiwa kupitia Utawala wa Majimbo, ingawa aliasa kwamba kinachofaa kwa wengine haimaanishi kitafaa kwa Tanzania.
Alisisitiza kuwa ufumbuzi wa matatizo ya Watanzania utatokana na Watanzania wenyewe kwa sababu ndio wanaofahamu mila, desturi na mfumo mzima wa maisha yao.

Sunday 23 March 2014

Tanzania inahitaji watumishi wafanyakazi wa aina gani?

Mwanzo wa maendeleo ya kweli kwa nchi yoyote duniani kama historia
inavyodhirisha, ni pale watumishi na wafanyakazi wanapobadilika na kujitambua kutokana na kuwepo sera na mifumo ya usimamizi nautendaji kazi inayotambua nafasi, stahili au haki, wajibu na majukumu ya kila mtu katika kuchangia maendeleo ya nchi.
Kwa jumla, wataalamu wa nadharia na tasnia ya rasilimali watu wanasema
Kwamba, kazi kubwa ya wanaosimamia rasilimali watu ni kuhakikisha kila shughuli katika taasisi husika anapatikana mtu sahihi, mwenye elimu na ujuzi sahihi, wakati sahihi na atakayepewa kazi sahihi ili aifanye kwa usahihi pia.
Hata hivyo, rasilimali watu kama somo ni somo pana na katika miaka ya leo imeanza kuaminika kwamba kiongozi wa taasisi anayepwaya katika elimu na ujuzi wa rasilimali watu hawezi kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa kama ilivyo kwa yule aliyesheheni nidhamu na nadharia husika.
Kazi ya kusimamia au kuongoza rasilimali watu inaanzia na mipango, ugawanyaji kazi na wajibu, utafutaji watu kujaza nafasi zilizo wazi, mahojiano ya kutathmini sifa na uwezo wa mtu kama unaendana na jinsi alivyo na uchaguaji miongoni mwa walioomba kazi idadi ya watu wanaotakikana kwa kazi fulani.
Menejimenti ya rasilimali watu inajumuisha pia mambo ya ufuatiliaji wa utendaji kazi, uchukuaji wa hatua za kinidhamu, afya na usalama wa wafanyakazi pamoja na mikakati yote inayoihakikishia taasisi kuendelea hata kama waliopo kwa wakati huo wataondoka au kufa.
Kampuni au idara ya Serikali au taasisi iwayo kwa hiyo ina maana kwamba utendaji kazi wake na sifa yake aghalabu, utatokana na aina ya watu walioajiriwa. Ukiajiri watu wa ovyo na utendaji wa taasisi husika nao pia utakuwa ni wa ovyo. Ukiajiri watumishi au wafanyakazi wazuri basi uwezekano wa taasisi hiyo kuwa na utendaji mzuri nao ni mkubwa pia.
Hii inamaanisha nini? Inamaanisha kwamba wale wote waliopewa dhamana ya kuajiri wafanyakazi au watumishi wapya lazima wawe wanaojua kila linalopaswa kujulikana juu ya mbinu zote zinazotumika katika nadharia na utendaji kazi katika tasnia ya rasilimali watu ili kuhakikisha kwamba watumishi watarajiwa wote wanapepetwa kwa namna ambayo chuya au chafu wote unaondolewa na panabakia nafaka nzima na safi.
Hili linahitaji kwa kiasi kikubwa ugwiji katika masuala ya saikolojia na sosholojia. Elimu zinazoweza kuwang’amua watu walivyo na watakavyokuwa kwa kuangalia historia yao ya kimaisha na kikazi.
Polisi wanapolalamika kwamba wameajiri askari polisi ambao wanashirikiana na majambazi kuwaibia na kuwadhuru wananchi ilhali tunajua kazi ya polisi inatakiwa iwe nini, hapo kunaonyesha kuna walakini mkubwa katika namna wafanyakazi katika eneo husika awanavyochambuliwa na mwishowe kuajiriwa.
Mamlaka za kodi na mapato zinavyolalamika kuna wafanyakazi walioiva na kupevuka kwa rushwa, pia tatizo ni hilo hilo, yaani, jinsi watumishi wao wanavyopatikana na jinsi wanavyochujwa ili wabakie wale walio safi.
Benki na sekta ya fedha inapolalamika juu ya wizi kushamiri katika mabenki kwa ushirkiano kati ya wafanyakazi wa taasisi za kifedha na wafanyabiashara au hata wezi ni ishara kwamba kuna ajira mbovu katika sekta husika.
Tunapolalamika juu ya utendaji kazi katika hospitali, shuleni, vyuoni na kadhalika jambo hili pia huwa ni dalili ya kuwepo kwa walakini katika masuala ya haki na wajibu wa watumishi wahusika.
Tumalizie kwa kusema kwamba rasilimali watu ambayo nchi inabahatika kuwa nayo haitoki juu mbinguni. Rasilimali hiyo inatokana na jamii iliyopo katika nchi husika.
Hivyo ni vigumu kuona kama jamii yenyewe inajikita katika uongo, ubabaishaji, uzembe, ubinafsi, uvivu, umbeya, maneno bila vitendo, kula usichokipanda na ila za kila aina, ni kwa vipi jamii hiyo inaweza kuwa na wafanyakazi wanaohitaji kuiondoa jamii yao kutoka kwenye hatua ya chini kabisa kimaendeleo na kuipeleka kwenye hatua ya juu kabisa kimaendeleo!

Warioba:‘Tumemaliza kazi yetu’

Dodoma. Siku moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kuzindua Bunge na kuponda ripoti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Joseph Warioba amesema jukumu walilopewa kwa mujibu wa sheria wamelikamilisha na wanawaachia wananchi waamue.
Akizungumza na Mwananchi jana asubuhi, Jaji Warioba alisema alichokizungumza Rais Kikwete ni maoni yake na kwamba hawezi kuyajadili.
“Rais Kikwete alichozungumza ni maoni yake, kwa sasa sipendi kuyazungumzia hayo, ” Jaji Warioba alieleza.
Alisema wamemaliza jukumu walilopewa na kwamba sasa jukumu lote lipo mikononi mwa Bunge.
Jaji Warioba alisema Tume yake ilikusanya maoni kutoka kwa wananchi, mabaraza ya wilaya ya Katiba na Taasisi mbalimbali, wakatengeneza rasimu ambayo sasa wameikabidhi kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Jaji Warioba pia alikataa kuzungumzia zogo lililoibuka bungeni na kusababisha rasimu kuwasilishwa Jumatano, baada ya kikao cha Jumanne kuvunjika.
Hali hiyo ilitokana na UKAWA kudai muda wa saa 1:30 uliokuwa umepangwa Jaji Warioba ahutubie bungeni uongezwe na kanuni inayoelekeza Rais Jakaya Kikwete ahutubie kabla Jaji Warioba hajawasilisha rasimu izingatiwe, baada ya kutangazwa kuwa Rais angehutubia baada ya rasimu kuwasilishwa.
Profesa Baregu
Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Mwesiga Baregu alisema alitarajia Rais Kikwete angezindua Bunge Maalumu na siyo kutoa maagizo na vitisho kwa wajumbe.
Alisema hajui lengo la Rais kufanya alichofanya lakini ana hakika kwa kutoa ufafanuzi wa hoja zilizotokana na maoni ya wananchi ndani ya rasimu, ameingilia kazi za Tume na hivyo amevunja Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83 toleo la mwaka 2012), inayosema:
“21.-(b) atakayejifanya kuwa mjumbe wa Tume au Sekretarieti; au (c) atakayeendesha programu ya elimu juu ya mabadiliko ya katiba kinyume na masharti ya sheria hii, atakuwa ametenda kosa.
(3) atakayetiwa hatiani kwa kutenda kosa kinyume na Sheria hii, atawajibika kulipa faini isiyopungua Sh2,000,000 (milioni mbili) na isiyozidi Sh5,000,000 (milioni tano) au kifungo kwa muda usiopungua mwaka mmoja na usiozidi miaka mitatu au adhabu zote mbili.
Sheria hiyo inaendelea kuelekeza, (4) Hatua zozote zilizochukuliwa chini ya kifungu hiki hazitachukuliwa kuwa zimefikia ukomo na zitaendelea kuwa na nguvu ya kisheria hata baada ya Sheria hii kukoma kutumika.”
Profesa Baregu alisema sheria imezungumzia mtu yeyote, hajui kwa Rais inakuwaje.
“Sijui ameona Bunge halitoshi, haliwezi kung’amua mambo au limepungukiwa kiasi cha kushindwa kumudu majukumu yake? Sielewi ila amevunja sheria na amelivunjia Bunge hadhi yake kiasi kwamba hata kazi yake inaweza isiaminike,” alieleza.
Profesa Baregu alisema Rais Kikwete amejipa jukumu la kujibu na kujadili hoja za rasimu na hivyo kuwa sehemu ya Bunge Maalumu.
Alisema wakati wabunge wanahimizwa kutumia mfumo wa maafikiano katika kuamua mambo, Rais amewajengea msingi wa mgawanyiko na chuki, hali itakayoathiri mpango wa kulipatia taifa Katiba inayotokana na wananchi.
Profesa Baregu alitaja baadhi ya kauli za Rais Kikwete ambazo zinaweza kuathiri mchakato kuwa ni kujirudia kwa kauli; “Nyie ndiyo mnaotunga Katiba (Wabunge wa Bunge Maalumu) kazi imebaki kwenu.” na maelekezo kwamba serikali tatu zitapatikana, lakini labda baada ya yeye (Rais Kikwete) kuondoka madarakani.
Jaji Ramadhan
Jaji Ramadhani alisema wao Tume wamemaliza kazi yao na kwamba sasa wanawaachia wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi waamue.
“Tumemaliza kazi yetu na sasa tunawaachia wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi,” alisema.
Hata hivyo, alisema ikitokea wajumbe wa Bunge hilo wakihitaji ufafanuzi wa jambo lolote, yeye binafsi anaahidi kutoa ushirikiano.
Kuhusu hotuba ya Rais Kikwete bungeni juzi, alisema yeye alikuwa Arusha akishughulika na vikao vya Mahakama ya Kimataifa ya Haki za Binadamu na kwamba hakuwa amepata muda wa kuipitia na kuitafakari kwa kiwango cha kuizungumzia.
“Ninasoma na kuitazama kupitia vyombo vya habari na ninafahamu nyie wanahabari huwa mnalenga pale palipowakuna. Hivyo nikitulia na kupata hotuba halisi aliyotoa nikaitafakari; nitaizungumzia,” alieleza.
Rais Kikwete akizindua Bunge juzi mjini Dodoma, alisema rasimu ya pili iliyowasilishwa bungeni na Jaji Warioba ina makosa mengi ya kiuandishi.
Alisema ina mambo mengi, baadhi yalitakiwa kuwekwa kwenye Sheria.
“Mbolea, mbegu, pembejeo vyote vimewekwa humo, hata umri na haki ya mtoto kupewa jina vinawekwa humo, yakiwekwa yote kama yalivyo, serikali haitaweza kuyatekeleza itashtakiwa mahakamani kila wakati,” alieleza.
Rais Kikwete aliwataka wajumbe wa Bunge Maalumu kusoma neno kwa neno, mstari kwa mstari na kujiridhisha na mambo watakayoidhinisha yaingie kwenye Katiba itakayopendekezwa.
Alisema watakachoona kinafaa kurekebishwa, kuboreshwa au kufutwa wasisite kufanya hivyo kwa sababu inatakiwa Katiba bora, inayotekelezeka na ambayo haitalalamikiwa kiasi cha kulazimika kuibadilisha muda mfupi baada ya kupitishwa.
Huku akishangiliwa na baadhi ya wajumbe, alisema wakichagua Serikali tatu watatakiwa kuondoa mambo yote yanayoweza kukanganya utendaji wa Serikali za washirika na ile ya Muungano. Lakini wakichagua Serikali mbili, mengi yatatekelezeka.
Rais Kikwete alisema serikali zote mbili zimeamua kwa dhati kutumia fursa ya mchakato wa mabadiliko ya Katiba kutatua mambo matatu kati ya sita ambayo bado hayajatatuliwa kutoka kwenye orodha ya kero 31 za Muungano zilizoainishwa na Zanzib

Tuesday 18 March 2014

Bunge lachafuka, Warioba asimama bila kuwasilisha Rasimu ya Katiba

Dodoma. Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba jana jioni alisimama kwa dakika tatu mbele ya kipaza sauti lakini akashindwa kuwasilisha Rasimu ya Katiba kutokana na vurugu zilizojitokeza bungeni.
Vurugu hizo zilitokea muda mfupi baada ya Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta kumwalika kuwasilisha Rasimu ya Katiba kwa muda wa dakika 120.
Jaji Warioba alisimama kwenye mimbari ya Bunge saa 11:02 jioni tayari kuhutubia lakini kabla ya kufanya hivyo, wajumbe kadhaa walisimama na kuomba mwongozo wa mwenyekiti.
Waliosimama ni Profesa Ibrahimu Lipumba, James Mbatia, Freeman Mbowe na Tundu Lissu.
Hata hivyo, Sitta aliwanyima fursa akisema: “Hakuna mwongozo hapa, naomba Mwenyekiti uendelee, waheshimiwa wabunge hakuna mwongozo naomba Mwenyekiti uendelee kwa ajili ya hansard.”
Kauli hiyo ilionekana kuchafua hali ya hewa kwani Jaji Warioba alipowasha kipaza sauti tayari kuanza kuhutubia, baadhi ya wajumbe walianza kupiga kelele, wengine makofi na kugonga meza hivyo kumfanya ashindwe kufanya kazi hiyo ya uwasilishaji.
Waliokuwa mstari wa mbele kupinga Jaji Warioba kuwasilisha Rasimu ya Katiba kwa sehemu kubwa walikuwa ni wajumbe wanaounda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Jaji Warioba akiwa anatafakari mbele ya mimbari, Sitta aliwasha kipaza sauti na kumtaka aendelee kuwasilisha Rasimu ya Katiba ... “Endelea Mwenyekiti, endelea kwa ajili ya kumbukumbu rasmi (hansard).”
Lissu akisikika akijibu kauli hiyo akisema: “Fuata kanuni mwenyekiti... fuata kanuni mwenyekiti,… huku akipiga kelele na kugonga meza na wakati huo Profesa Lipumba akiwa amewasha kipaza sauti chake kutaka kuzungumza huku naye akiendelea kupiga meza kwa nguvu.
Wengine waliosimama ni Mchungaji Christopher Mtikila, Ezekiel Oluoch, Philimon Ndesamburo, Moses Machali na Mchungaji Peter Msigwa.
Dakika tatu zilikatika huku kukiwa hakuna dalili za hali kutulia na kuona hivyo, Jaji Warioba aliamua kuondoka kwenye mimbari na kuketi kimya akiwa na Makamu Mwenyekiti wake Jaji Augustino Ramadhani.
Baada ya hapo, Sitta alisimama na kuwasha kipaza sauti na kusema: “Waheshimiwa wajumbe, katika mazingira haya tuliyonayo, naomba kutangaza kuwa nasitisha shughuli za Bunge hadi hapo tutakapotangaziwa tena.”
Licha ya kauli hiyo, baadhi ya wajumbe waliendelea kupaza sauti zao wakisema kwamba walikuwa wanaburuzwa.
Wakati hayo yakitokea, kikosi cha askari wa Bunge kiliingia ndani ya ukumbi na kusimama katika lango kuu hali iliyoonekana kuwa ni kuchukua hadhari endapo hali ya usalama ingechafuka.
Baada ya tamko la kuahirisha mkutano, askari hao waliingia moja kwa moja hadi alipokuwa ameketi Jaji Warioba na kumsindikiza hadi nje na jitihada za waandishi wa habari kumfuata ili kupata maoni yake hazikufanikiwa.
Kilichofuata baada ya hali hiyo ni kurushiana maneno kwa baadhi ya wajumbe akiwamo Dk Ave Maria Semakafu ambaye nusura azipige kavukavu na mjumbe mwingine ambaye jina halikuweza kupatikana mara moja.
Hata hivyo, baadhi ya wajumbe akiwamo Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais (Utumishi), Celina Kombani waliamulia ugomvi huo kabla ya kuwa mkubwa.
Wajumbe walionekana kukaa katika vikundi ndani ya Bunge huku wakijadiliana juu ya kilichotokea wakati Sitta, Katibu wa Bunge, Yahaya Khamis Hamad na msaidizi wake, Dk Thomas Kashililah wakiwa katika kikao cha faragha.
Baada ya kujadiliana kwa nusu saa, Hamad akiwa ameongozana na Dk Kashililah, alirejea katika ukumbi wa Bunge na kuwataka wajumbe kutawanyika hadi hapo watakapojulishwa.
Hali hiyo iliibua kelele kutoka kwa wajumbe wakitaka kujua iwapo waondoke katika maeneo ya Bunge au la. Hamad alisisitiza kwamba warejee nyumbani hadi hapo watakapojulishwa.

Sunday 16 March 2014

Tunahitaji kubadilika ili kuondoa umaskini

Nakumbuka nilipokuwa bado kijana katika mkoa nilioishi kulikuwa na matajiri kadhaa ambao sisi tuliwaona wametuzidi. Wengine walikuwa jamaa zetu, hivyo kuwafahamu kwa karibu zaidi namna walivyokuwa wakiendesha maisha yao na namna walivyokuwa wakifurahia maisha yao ya kutokukosa vitu vidogo vidogo.
Sehemu kubwa zaidi ya matajiri hao sasa hawapo tena katika hali hiyo ya kuwa navyo. Wengi wao sasa ni wahitaji, wakiishi maisha ya kubangaiza. Tukiwaacha wao hata sisi wengine japo siyo matajiri, lakini huenda tumewahi kushika ‘vipesa’ wakati fulani, lakini pesa hizo zikashindwa kabisa kubadilisha maisha yetu.
Hali hii inahitaji kujitafakari kwani haina maana kuzungumzia nchi kujitoa katika umaskini wakati watu wake hawana mpango wa kujitoa katika umaskini huo. Tujiulize, inakuwaje tunaendelea kuwa maskini hata pale ambapo tunapata fursa ya kuwa na fedha?
Majibu kwa swali hili yapo mengi, lakini leo tuangalie yale yanayoendeana na tabia.
Wengi wetu tuna tabia ya kutokuweka akiba. Tabia hii wanayo wakulima, wafanyakazi hata wafanyabiashara. Mtu akibarikiwa kuwa na ziada ya pesa, basi badala ya kufikiria namna pesa hizo zitakavyozalisha zaidi, pesa hizo zitatafutiwa matumizi zaidi.
Matumizi hayo mara nyingi siyo ya kuzipeleka kwenye eneo la uwekezaji ili mtu apate faida zaidi bali ni kwenye eneo la ulaji. Kwetu sisi pesa zaidi maana yake ni sherehe zaidi, ununuzi zaidi na mbwembwe nyingine nyingi zisizokuwa na tija. Mwishowe ziada yote iliyopatikana inayeyuka na kumrudisha mtu katika hali ile ile aliyokuwa nayo kabla ya fedha kumtembelea.
Hakika hii inahuzunisha; hebu fikiria leo mtu anawakaribisha kwenye sherehe ya ubatizo wa mwanawe ambayo inakuwa kubwa kuliko hata ya Tanzania kufikisha miaka 50, halafu kesho mtu huyo huyo anakugongea na kukuomba au kukukopa fedha ya kununulia unga wa ugali.
Yanatupata haya kwa sababu fedha inatuwasha pale inapokuwa mikononi mwetu. Wakati wenzetu wanachambua faida na hasara watakazozipata kwa kuwekeza katika miradi mbalimbali, sisi tunachambua kicheko tutakachokuwa nacho katika matanuzi ambayo hata kuyapanga hatupangi bali yanakuja hapo hapo baada ya kupata fedha.
Siamini kama kweli mtu alipanga kuwajengea vimada nyumba bora za kuishi halafu yeye na familia yake wakakosa sehemu ya kuishi. Naamini fedha zilipokuwa mkononi zilimtia upofu na zilimharibu akili yake, hata akatenda hayo. Tumewasikia wale waliopata ufahamu baada ya kufilisika na wakataka kuzimiliki nyumba hizo bila mafanikio.
Wao wanateseka kwa kukosa makazi, lakini wale waliowapa starehe za muda wanaishi katika nyumba za kifahari. Hata kama makazi yapo hizo fedha si zingewekezwa kwenye maeneo yanayozalisha fedha zaidi?
Uzalishaji huo si ungemwezesha sasa mtu kuishi uzee wake mwema? Uzee ambao mtu angekuwa anatumia muda mwingi sasa kuwaombea na kuwabariki watoto wake, badala ya kila siku kuwalaani kwa madai kwamba hawamjali.
Tabia nyingine inayotuvuruga sana ni ya kujionyesha. Katika kujionyesha huko mtu ananunua au anajenga, hata kile ambacho hana sababu nacho. Mtu alikuwa na friji yake inayomtosha kwa matumizi ya nyumbani kwake leo fedha imemtembelea basi atakwenda kununua friji kubwa, utafikiri anataka kuweka kuku wa kuuza.
Friji hiyo kubwa inaishia kuwekwa maji, atajenga nyumba kubwa zaidi yenye ghorofa mbili, halafu vyumba vingine vinaishia kuwa makazi ya mende. Inasikitisha sana pale watu wanapokuwa wamezeeka halafu nyumba hiyo ipo mahali ambapo familia haiwezi hata kubadilisha matumizi ya nyumba hizo yaani badala ya kuishi, labda wafanye hoteli au wapangishe.
Utakuta mtu kaishiwa kabisa, lakini hajui jinsi ya kuitumia nyumba hiyo ambayo kwa sasa inatumika kwa asilimia 10 tu. Ukijiuliza kwa nini mtu aliwekeza kwenye jumba kama hilo, jibu utakalopata ni alitaka watu wajue kwamba naye ana fedha.
Tunahitaji kweli vitu vyote tunavyovinunua? Hakuna siku tunajutia viatu na nguo nyingi tulizozijaza katika nyumba zetu, ambazo kwa kuwa zimepitwa na wakati zimejaza makabati yetu na hatuna za kuzifanyia?
Hivi kweli mtu unakosa hata fedha ya kununulia dawa, lakini ndani ya nyumba una vitu chungu mzima ulivyovinunua kwa kujionyesha na sasa havikuzalishii chochote, hiyo kweli ni akili?
Tunapenda sana kuwaiga wazungu, nafikiri tuwaige pia tabia yao ya kupenda kuweka akiba kwa ajili ya kuwekeza au kwa ajili matumizi ya baadaye. Tujifunze pia kufanya vitu kwa kiasi, tuache tabia ya kujionyesha, kwani tabia hii inatufanya tusifikiri vizuri katika kuwekeza fedha tuzipatazo.
Tusipobadilika, tutaishia kama tulivyo; leo mtu anapigiwa makofi kwa kuvaa vizuri, kutembelea magari ya kifahari, kuishi kwenye nyumba ya kifahari na kufanya sherehe kubwa kubwa halafu baada ya muda mfupi, anakuwa omba omba au kopa kopa asiyerudisha fedha anazokopa.
Hii haikubaliki hata kidogo. Tujizoeshe tabia mbadala nayo ni ya kuweka akiba na kununua vitu kwa mahitaji siyo kwa fahari.

Sitta: Katiba inaruhusu kununua uongozi

Dodoma. Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta amesema kushamiri kwa vitendo vya watu wachache kujitajirisha na wengine kununua uongozi, kunatokana na Katiba ya sasa kutokuwa na meno ya kupambana na rushwa na ufisadi.
Amesema vitendo hivyo vitakoma kama nchi ikiwa na Katiba nzuri, itakayowezesha kutungwa kwa sheria nzuri zitakazowabana mafisadi na watoa rushwa.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake Dodoma juzi, Sitta alisema: “Siridhiki na Katiba ya sasa inavyoshughulikia rushwa na ufisadi. Katika nchi yetu inaonekana ni rahisi mtu kujitajirisha kwa kutumia cheo chake na baada ya hapo kununua uongozi. Katika nchi maskini jambo hili ni hatari kubwa.”
Aliongeza, “Katiba lazima ielekeze kwamba iko tofauti kati ya kufanya biashara na kuongoza watu. Haiwezekani ukawa na biashara kubwa zinazochukua zabuni za Serikali na ukaendelea kuwa kiongozi wa Serikali, nchi nyingi zimetenganisha mambo haya.”
Alisema rushwa ni hatari na inaweza kusababisha nchi kukosa amani, kwa sababu wananchi maskini watafika mahali hawataona uhalali wa maisha ya watu wanaowaongoza.
“Nimeipenda Rasimu ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, imeeleza wazi kuhusu suala la  uadilifu hivyo lazima zitungwe  sheria zitakazowabana watu kutokutumia madaraka yao vibaya,” alisema.
Sitta ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, alisema ni hatari kuwa na mfanyakazi wa Serikali mwenye kampuni binafsi ambayo inapewa tenda za Serikali.
“Sisemi kuwa watu wasiwe wafanyabiashara, mtu akiamua kuhudumia umma anatakiwa kuweka mali na biashara zake katika mfumo wa kuendesha biashara hiyo bila yeye kuwa mhusika wa moja kwa moja. Hivyo, ndivyo wanavyofanya mataifa kama Uingereza na Marekani,” alisema Sitta.
Alisema taarifa nyingi za maendeleo katika nchi za Afrika zinaeleza kuwa nchi za bara hilo zinakwama kupiga hatua kimaendeleo kwa sababu ya rushwa.
“Rushwa inajenga mtandao ambao unashuka hadi ngazi za chini. Watumishi wa chini wakiona mikataba mibovu inawanufaisha wakubwa nao hutafuta mianya katika maeneo yao. Ikiwa hivyo wanaopata shida ni wananchi wanyonge,” alisema na kuongeza;
“Sisi wakubwa tunaweza kutoa rushwa na tukaishi vizuri ila watu maskini kutoa rushwa ni ngumu. Elimu yetu siyo nzuri, huduma za afya nazo hivyo hivyo kutokana na kushamiri kwa rushwa,” alisisitiza.
Alisema ni ajabu kuona vitabu vyenye makosa vinatumika katika shule mbalimbali nchini na hata ukifuatilia unabaini kuwa aliyetoa vitabu hivyo alitoa rushwa Wizara ya Elimu.
“Asilimia 40 ya dawa tunazotumia hapa Tanzania ni ‘feki’. Yaani unaandikiwa dawa ambazo hazina maana katika matibabu. Hali hii ni matokeo ya kuwa na mfumo mbovu ambao unahitaji kubadilishwa. Katiba Mpya inatakiwa kuzungumzia kiundani suala la uadilifu, kuwe na sheria zitakazozuia mtu kujinufaisha kutokana na wadhifa wake,” alisema.
Alisema rushwa ikiwa tabia ndani ya nchi, uchumi unakwama kwa sababu mapato ya Serikali badala ya kwenda kutatua matatizo ya wananchi yanakwenda katika zabuni za ovyo na kutajirisha wachache ambao nao wana tabia ya kutorosha fedha nje ya nchi.
“Mnachangia mfumo wa mapato ya Serikali lakini fedha zinatoroshwa nje ya nchi. Katika Afrika misaada inayotoka nje ni kidogo kuliko fedha zinazotoroshwa kwa rushwa. Kuna faida gani kujisifia kuwa Waziri wa Fedha kasaini mikataba wakati rushwa inatoka zaidi kuliko fedha inayoingia?” alihoji Sitta.
Alisema Tanzania imeathirika na rushwa, huku akitolea mfano jinsi wakulima wanavyokuwa na madeni hewa yanayowafanya washindwe kuendesha shughuli zao.
“Ni hatari kuwa na vijana waliokata tamaa kwa sababu ya kutokuwapo ajira. Tatizo la ajira ni kutokukua haraka kwa uchumi. Uchumi wetu utaweza kukua kwa haraka na kupunguza umaskini kama hatutaingia mikataba mibovu na tutakomesha rushwa,” alisema.
Alisema nchi ambayo viongozi wake wanapokea rushwa ni lazima itapata wawekezaji uchwara kwa sababu wanajua hata wakiboronga hakuna wa kuwafanya jambo lolote.
“Kama ni barabara watajenga tu hata kwa kiwango cha chini kwa sababu wanajua hata ikiharibika wao watakuwa wameshalipwa fedha zao na aliyetoa zabuni naye atakuwa ameshachukua chake,” alisema

Risasi zinavyotumika kuua raia Tarime


Tarime. Katika Kijiji cha Gomsala, Tarime mkoani Mara yupo Matuma Marwa (22), ambaye hakuwahi kufikiria kwamba siku moja atakuwa mlemavu pamoja na kuwa kila binadamu aliye hai ni mlemavu mtarajiwa.
Marwa alipatwa na ulemavu wa mguu Oktoba 9, mwaka jana, baada ya kupigwa risasi na polisi kwenye paja.
“Tulikuwa tunaelekea shambani, tukasikia milio ya risasi ikielekezwa tuliko sisi, risasi moja ilinipata kwenye paja na tangu wakati ule hadi sasa mguu wangu hauko sawa,” alisema Marwa na kuongeza:
“Kazi yangu ni mkulima, ila kwa sasa nashindwa kulima kwa kuwa mguu bado unauma.”
Marwa ni miongoni mwa watu waliopatwa na madhila yatokanayo na vita ya rasilimali baina ya wananchi na wawekezaji.
Marwa anaishi katika kijiji kilicho kandokando ya mgodi wa dhahabu wa North Mara.
Mgodi wa North Mara unamilikiwa na Kampuni ya African Barrick Gold tangu 2006 ilipoununua kutoka kwa Kampuni ya Placer Dome Tanzania, iliyokuwa ikimilikiwa na Afrika Mashariki Gold Mines.
Taarifa rasmi kutoka katika vijiji vinavyozunguka mgodi huo, zinaonyesha kuwa, mbali na waliojeruhiwa na kupata ulemavu wa kudumu, pia wapo waliopoteza maisha kutokana na kupigwa risasi na polisi wanaolinda usalama katika migodi hiyo.
Matukio hayo na mengine ya unyanyasaji, yanawafanya wakazi wa maeneo haya kuchukulia uwepo wa madini ya dhahabu kama kero kwao na siyo neema au baraka kama ilivyotarajiwa.
Watu 24 wanadaiwa kwamba wamekwisha uawa kwa kupigwa risasi katika matukio, akiwamo mkazi wa Kijiji cha Nyangoto, Ryoba Maseke ambaye alipigwa risasi Julai 12, 2012.
Shangazi wa Maseke, Suzana Mwita anasema, marehemu alikuwa mwanafunzi wa kidato cha nne katika shule ya sekondari ya Mugumu, Serengeti na alifika kijijini kusalimia ndugu zake na hapo ndipo mauti yalipomkuta.
Mwaka huohuo, polisi pia wanadaiwa kwamba walimuua kwa risasi mkazi wa kijiji cha Kewanja, Kibwaba Ghati (23) katika tukio la Novemba 6, wakati wananchi wanaodaiwa kuvamia mgodi, walipokurupushwa na askari wa jeshi hilo.
Mama mzazi wa Ghati, Wankrugati Malembela alisema: “Mwanangu alikuwa akichunga ng’ombe, Polisi walikuwa wakiwakimbiza wavamizi na kupiga risasi ovyo, ndipo risasi mojawapo ilipompata kwenye paji la uso na kufariki pale pale”.
Aliongeza: “Polisi waliuchukua mwili wake na kuupeleka mgodini na kuupiga picha wakisema eti alikutwa huko.”
“Tumekuwa tukifuatilia suala hili polisi lakini wanasisitiza kuwa alikutwa mgodini.Tumekwenda Barrick lakini wanatuzungusha tu,” alisema Malembela.
Polisi wajitetea
Diwani wa Kata ya Kemambo, Wilson Mangure alisema tangu 2011 hadi Januari mwaka huu, watu 69 wameuawa kwa kupigwa risasi na polisi huku mamia wengine wakijeruhiwa.
“Bado tunakusanya taarifa, lakini mauaji bado yanaendelea. Mwaka huu wameuawa watu wanne katika matukio matatu tofauti,” alisema Mangure.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Tarime/Rorya, Justus Kamugisha alikiri kuwapo kwa vifo ambavyo alisema vinatokana na mapambano na wavamizi wa mgodi.
Hata hivyo alisema mauaji hayo siyo ya mfululizo. “Hakuna mfululizo wa mauaji…, sisi kazi yetu ni kulinda raia na mali zao na kulinda mwekezaji, hatuko hapa kuua watu. Tunapambana na wavamizi ambao wanaingia mgodini kuiba dhahabu na kuharibu mali,” alisema Kamanda Kamugisha na kuongeza:
“Ungekuja hapa ningekuonyesha jinsi wanavyoharibu… kuna dhana kwa wananchi hapa Tarime kuwa dhahabu iliyoko pale ni yao. Wanavamia mgodi wanapambana na polisi. Wapo baadhi ya polisi waliojeruhiwa vibaya.”
Kwa upande wake Kamishna wa Polisi wa Mafunzo na Operesheni, Paul Chagonja ambaye ameshatembelea eneo hilo mara kadhaa, alisema mauaji yanayotokea yana sababu maalumu:
“Polisi siyo wajinga, waue watu bila sababu, haiwezekani, lazima kuwe na sababu…, huo ni mgogoro wa muda mrefu mno na ninyi waandishi wa habari mnapaswa kuwa wazalendo katika suala hilo,” anasema Chagonja na kuongeza: “Pale kuna watu wakorofi wanaopambana na polisi na kuharibu mali.”
Matukio mengine 
Matukio hayo yanaendelea kutokea hadi sasa kwani Januari 6, mwaka huu, mkazi wa Kijiji cha Kewanja, Kimosi Leonard alipigwa risasi mguuni baada ya polisi kuvamia kijiji hicho kwa lengo la kukamata baadhi ya watu.
“Mimi nilikuwa napita na safari zangu tu, nikashangaa watu wanakimbia ovyo. Ndipo nilipojikuta nimepigwa risasi ya mguu,” alisema Leonard ambaye anatembea kwa kuchechemea.
Aliongeza: “Siwezi kwenda kulalamika polisi, maana ukifika huko ndiyo unaongezewa kesi nyingine ya kuvamia mgodi.”
Mwingine ni Weigama Range ambaye alisema watoto wake Fredrick (7) na Happiness (6) wamepata ulemavu baada ya kulipukiwa na mabomu ya machozi yaliyorushwa na polisi.
“Watoto wangu walikuwa wakisoma katika shule ya msingi ya Kewanja. Agosti 23, 2011 polisi walirusha mabomu hapo shuleni na wanafunzi walianza kukimbia ovyo, ndipo mtoto wangu Happiness alianguka na kupoteza fahamu. Hadi leo ana tatizo la kuanguka anguka. Fredrick naye alianguka na kung’oka meno matatu ya mbele,” alisema Weigama na kuongeza:
“Mwaka huu, Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Paul Chagonja alikuja kufanya mkutano hapa kijijini na nilimwonyesha watoto na fomu za polisi na aliahidi kunisaidia, lakini sijapata msaada wowote. Nimejaribu kufuatilia polisi na kwa mbunge wetu, lakini sijapata chochote.”
Mbunge wa Tarime, Nyambari Nyangwine alizungumzia hali ilivyo sasa: “Angalau kwa sasa hali inaendelea kuimarika, kuliko zamani hali ilikuwa mbaya zaidi. Hayo mauaji ni kweli yanatokea na lawama nazipeleka kwa Serikali. Siwalaumu Barrick kwa sababu polisi ndiyo wanaofanya mauaji.”
Uvamizi wa mgodi
Baadhi ya wananchi wanakiri kwamba wamekuwa wakivamia mgodi, lakini wanawakosoa polisi kwa kutumia risasi za moto kuwadhibiti.
Marwa Bina (30) ambaye alikiri kwamba aliwahi kufanya uvamizi, alisema wanalazimika kufanya hivyo kwa kuwa hawana ajira.
“Tunavamia pale ili tupate fedha za kujikimu, ila kwa sasa ulinzi umeimarishwa na hata wakikupiga risasi hupewi fidia,” alisema.
Mwingine ni Joshua Masyaga aliyekuwa mvamizi mgodini hapo ambaye alisema vijana wengi waliamini kwamba watafaidika na madini hayo hata kwa kuyaiba tu.
“Mimi nilikuwa mvamizi baada tu ya kumaliza kidato cha nne 2010. Ni kweli nilipata dhahabu na kuuza lakini ni maisha ya hatari mno. Nimeshuhudia rafiki zangu wengi wakiuawa kwa risasi.
Akifafanua jinsi biashara hiyo inavyofanyika, Masyaga alisema kulikuwa na mawakala wa madini ambao huwasiliana na wafanyakazi wa mgodi wanaotoa kifusi nje.
“Kuna matajiri wanaofanya mpango na wafanyakazi wa ndani na polisi nao hushirikishwa. Mawe yakishamwagwa nje wale matajiri hutuma vijana wao kuokota na wengine huvamia tu. Hao ndiyo hupigwa risasi na polisi,” alisema na kuongeza:
“Mawe yakishapatikana tunayapeleka kwa wasafishaji ambao huyasaga na kuyawekea zebaki ili kupata dhahabu ambayo huchukuliwa na matajiri. Hata hivyo siku hizi ulinzi umeimarishwa mno, hiyo biashara imekufa.”
Majibu ya Barrick
Meneja wa Mgodi wa North Mara, Gary Chapman alisema:
“Mara nyingi watu wanaouawa ni wale wanaopambana na polisi, vinginevyo tuna uhusiano ni mzuri na wanajamii na ndiyo maana tunafanya nao mikutano kujadili maendeleo na watu wanashukuru kwa huduma zetu.”
Aliongeza: “Kuna watu wanaovamia mgodi wetu. Kwa hiyo unapozungumzia migogoro kama hiyo, siyo kwa mgodi tu bali katika jumuiya nzima.”
Naye Ofisa Uhusiano na Mawasiliano ya Umma wa ABG, Nector Foya alisema kampuni hiyo inao mfuko wa maendeleo (The ABG Maendeleo Fund) ambao hutoa huduma kwa wanajamii wanaozunguka migodi yao.
“Tuna mfuko wa maendeleo ya jamii ambao unasaidia huduma kama vile elimu, maji na afya. Tumejenga shule, hospitali na miradi ya maji katika vijiji vinavyozunguka migodi yetu, ndiyo maana tunasema tunao uhusiano mzuri na wanajamii,” alisema.
Halmashauri Tarime
Wakati kukiwa na matukio yanayozua mvutano baina ya wawekezaji na wananchi, uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime unajivuna kwa kupata faida kutoka kwenye mgodi huo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Athuman Akalamu alisema tangu kampuni ya ABG ilipofika imekuwa ikijitanua, hivyo kuchukua maeneo ya vijiji vilivyo jirani, hali inayosababisha migogoro ya ardhi miongoni mwa wanavijiji kutokana na fidia iliyokuwa ikilipwa.
Alisema kutokana na migogoro hiyo, Serikali iliunda kikosi kazi kwa ajili ya kushughulikia malalamiko husika.
Kiongozi wa kikosi hicho Minja Jeremiah alisema: “Mwaka 2012 Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Steven Masele na aliyekuwa Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Charles Kitwanga walitembelea mgodi huu baada ya kampuni ya ABG kulalamika kuwa eneo lao halitoshi. Hivyo tathmini ilifanywa na kijiji cha Nyangoto kilitakiwa kutoa eneo”.
Hata hivyo alisema kutokana na hali hiyo, kuliibuka makundi matano ya watu.
“Kundi la kwanza lilipinga kabisa mpango huo, huku la pili likikubali ila kwa kulipwa kwanza fidia, la tatu lilikubali fidia lakini waliendeleza makazi yao, wengine wakakubali sehemu ya fidia na wengine walichukua fidia lakini hawakuhama.
Ndiyo maana kikosi hiki kiliundwa Aprili 2013,” alisema. Alisema tangu wakati huo, wameshafanya uthamini katika vijiji vya Kewanja na Nyakunguru na wanavijiji wameshapata kibali cha Mthamini Mkuu wa Serikali na wamelipwa fidia katika awamu nne.
Hata hivyo anasema wapo watu wapatao 4,000 waliofanyiwa tathmini lakini bado hawajalipwa.
Utatuzi wa migogoro
Katika kurejesha uhusiano mwema kati ya mgodi huo na wanajamii, Shirika la Search for Common Ground lenye makao yake makuu Dar es Salaam, sasa limejikita wilayani Tarime ili kutafuta suluhu.
Meneja Programuwa shirika hilo, Patricia Loreskar alisema kazi kubwa ya shirika hilo ni kujenga mazingira ya mawasiliano na mijadala kwenye mazingira yenye migogoro.
Naye Meneja wa mradi wilayani Tarime, Jacob Malikuza alisema njia wanazotumia ni pamoja na kufanya utafiti wa maisha ya wanajamii kabla ya kuanza kutoa mafunzo.
Kwa upande wake Mwanasheria wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia anasema wamekuwa wakifuatilia mgogoro katika eneo hilo na wamefungua kesi London, Uingereza ili kuishitaki African Barrick Gold kwa ukiukwaji wa haki za binadamu.
Taarifa zaidi zinaonyesha pia kampuni ya uwakili ya Leigh Day nayo inahusika katika kesi hiyo ikiwawakilisha baadhi ya wanavijiji wanaozunguka mgodi huo, kutokana na matumizi ya nguvu kupita kiasi.
Kesi hiyo iliyofunguliwa mwishoni mwa mwaka jana, ilipingwa na ABG wakitaka iendeshwe Tanzania, lakini walishindwa katika pingamizi lao.
“Huo mgogoro tumeufuatilia sana, hadi sasa tumeshafungua kesi Uingereza.Hatukufungulia Tanzania kwa sababu mahakama zetu zinachelewesha mno kesi na mara nyingine hazitufikishi kwenye kupata haki,” alisema Sungusia.
Hata hivyo Amani Mustafa ambaye ni mwanzilishi na Mkurugenzi wa taasisi ya Haki Madini alisema ni watu wachache mno wenye uelewa na masuala ya sheria hadi kufikia kufungua kesi.
“Watu wachache sana wanaweza kupeleka kesi mahakamani. Kwanza kuna mazingira ya kutishana na kutokuaminiana. Isitoshe wengi hawaoni kama mahakama ndiyo suluhisho la mambo yao. Kwa kifupi wamepoteza imani na Serikali na mfumo mzima wa mahakama. Wanachoamini haki inapatikana mikononi mwao,” alisema Mustafa na kuongeza:
“Kuna mambo mengi mno kwenye mgodi ule; mauaji, unyanyasaji wa kijinsia, uchafuzi wa maji, kutofuatwa kwa taratibu za kazi mgodini na hata vyama vya wafanyakazi vinalalamika”.
Akizungumzia mfumo wa kushughulikia malalamiko, Mustafa alisema kutoelimika kwa wanavijiji ndiyo sababu kubwa ya kukosa haki.
“Kungetakiwa kutolewe elimu ya sheria kwa wanavijiji na mwelimishaji asilipwe na Barrick. Kwa sasa kuna ukiukwaji wa maadili na Serikali haina muda, bali imejikita kwenye ukusanyaji wa kodi kuliko kuangalia haki za watu,” alisema Mustafa.

Friday 14 March 2014

MAONI: Serikali isiwasujudie waandishi wa nje

Jumanne iliyopita tulichapisha habari kuhusu ujio wa mwandishi wa Gazeti la Daily Mail la Uingereza, Martin Fletcher, ambaye aliandika habari katika toleo la gazeti hilo la Februari 9, mwaka huu kwamba Serikali ya Tanzania imeshindwa kukomesha mauaji ya tembo na faru ambao wako katika hatari ya kutoweka, akiwatuhumu baadhi ya maofisa wa Serikali na jamaa wa Rais kuwa sehemu ya mtandao mkubwa wa ujangili.
Ujio huo umewashangaza wengi, kwani pamoja na Serikali kukanusha kumwalika, mwandishi huyo amesema ziara yake nchini imetokana na mwaliko wa Serikali. Hata hivyo, sisi hatuoni kama kualikwa ama kutoalikwa na Serikali ni jambo linalostahili kujadiliwa kwa kuwa sera ya uhariri ya magazeti yenye hadhi kama Daily Mail inawaelekeza na kuwasisitizia waandishi kufuata maadili ya taaluma yao, ambayo ni kuandika ukweli hata kama ukweli huo utawauma watu waliowafadhili ama kuwawezesha kupata habari.
Hivyo, hatutazamii mwandishi Fletcher apindishe habari au aandike habari za kuifurahisha Serikali kwa sababu tu ya kufadhiliwa na kuruhusiwa kuingia katika sehemu nyeti ambazo hata waandishi wazawa na wazalendo wa hapa nchini hawaruhusiwi. Kwa kuzingatia utamaduni, maadili na weledi wa waandishi hao, utakuwa muujiza kama mwandishi huyo atakubali ‘kununuliwa’ au kufadhiliwa na Serikali ili taarifa atakazotoa baada ya ziara yake nchini ziisafishe kutokana na taarifa za awali kwamba haifanyi juhudi za kutosha kuwalinda wanyamapori.
Imeripotiwa kuwa mwandishi huyo pamoja na mpigapicha wake wamepewa mapokezi mazuri nchini na kuingizwa katika maeneo nyeti kama ghala za kuhifadhia shehena za meno ya tembo yanayokamatwa, huku wakiwaacha maofisa katika Wizara ya Maliasili na Utalii wakiwa vinywa wazi. Pia waliruhusiwa kupiga picha kinyume na utaratibu na baadaye wakapelekwa Hifadhi ya Selous kwa ndege ya Idara ya Wanyamapori.
Wizara ya Maliasili na Utalii imekiri kuwa ziara ya mwandishi huyo imetokana na uamuzi wake wa kuweka uwazi suala hilo na kwamba waandishi wengine wa BBC na CNN wameomba kufanya ziara kama hiyo.
Ni wazi kuwa uamuzi huo ni jitihada za  kujikwamua na lawama za serikali kushindwa kukomesha vitendo vya ujangili na ndio maana Rais Kikwete alikwenda katika vituo vya utangazaji vya BBC na CNN, wakati waziri husika alikutana na wahariri wa magazeti ya Daily Mail na Mail on Sunday kufafannua suala hilo.
Tumezungumzia ziara ya wageni hao kwa kirefu ili kuonyesha jinsi Serikali inavyowatetemekea waandishi wa nje na kuwapuuza wa ndani, kiasi cha  kutotaka kwa makusudi kutoa habari kwa waandishi wa ndani au kukutana nao kuzungumzia masuala muhimu ya nchi.
Tulitarajia viongozi wa juu wa serikali wangekutana na vyombo vya habari vya ndani na kutoa ufafanuzi wa kina wa suala hilo ili wananchi wapate picha halisi ya nini kilitokea kabla ya kwenda nalo kwa waandishi wa nje.
Lakini juhudi kubwa ilielekezwa katika kutoa ufafanuzi na ushirikiano kwa vyombo vya habari vya nje, akiwemo mwandishi huyo wa Uingereza. Vyombo vya habari vya ndani vitasaidia serikali pale tu itakapoamua kuwa ya uwazi na kutoa ushirikiano kwa waandishi hasa katika masuala muhimu na nyeti yanayohusu mustakabali wa  taifa hili. Serikali inajidhalilisha kwa kudhani inawajibika kwa nchi zinazotoa misaada badala ya wapigakura waliowapa uhalali wa kukaa madarakani.

Samuel Sitta: Kura ya siri

Dodoma. Mwenyekiti Mteule wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta amezungumzia uwezekano wa kutumia kura ya siri katika kuamua ibara nyeti katika Rasimu ya Katiba.
Sitta aliyechaguliwa juzi kushika wadhifa huo, alisema atashirikiana na kamati ya uongozi itakayoundwa ya wenyeviti wa Kamati 15 za Bunge hilo na kamati ya ushauriano kupata jawabu la suala hilo.
Akizungumza katika mahojiano maalumu nyumbani kwake mjini Dodoma juzi, Sitta alisema: “Unajua kuna baadhi ya vifungu na ibara za Rasimu ya Katiba ni vizuri vipigiwe kura ya wazi na vingine ambavyo ni nyeti zaidi vipigiwe kura ya siri.”
Alisema si vizuri vifungu vyote vipigiwe kura sawa, yaani si lazima zote ziwe za siri au ziwe za wazi.
Alitoa mfano wa ibara inayosema kutakuwa na Mahakama Kuu ya Tanzania na kusema: “Hatuwezi kushindana katika suala la kuwapo kwa Mahakama na ni wazi kuwa jambo hilo mnaweza kupiga kura ya wazi. Nasema hivyo kwa sababu Katiba yoyote lazima ionyeshe mihimili yote ambayo ni Bunge, Serikali na Mahakama.”
Sitta ambaye pia ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alishinda kiti hicho katika uchaguzi uliofanyika juzi kwa kura 487 kati ya 563 (sawa na asilimia 85).
Mbunge huyo wa Urambo Mashariki ambaye kaulimbiu yake ni ‘kasi na viwango’, alisema vifungu na ibara za Rasimu ya Katiba vinavyoweka misingi ya Katiba, ni vizuri vikapigiwa kura ya siri.
“Unajua tuna viongozi wa dini na halitakuwa jambo la busara kama tukizijua hisia zao. Kama wewe uko karibu na imamu au askofu halafu anapiga kura ya wazi ya kutaka Serikali tatu wakati wewe muumini unataka Serikali mbili ni wazi kuwa jambo hilo linaweza kuleta hisia tofauti na kuwanyima watu haki na uhuru wa kuamua,” alisema Sitta.
Alitoa mfano wa Sura ya Sita ya Rasimu ya Katiba inayozungumzia Serikali na muundo wa madaraka katika Jamhuri ya Muungano na kufafanua kuwa katika sura hiyo atapendekeza ipigiwe kura ya siri.
Kuhusu suala hilo la muundo wa Serikali alisema: “Kikubwa ni wajumbe kujenga hoja, hatuwezi kwenda na misimamo isiyobadilika kwa sababu tunataka maridhiano. Nitatenda haki na nitatoa muda mrefu zaidi kwa wajumbe kujadili sura ya kwanza na ya sita ambazo zina uzito mkubwa kuliko sura nyingine ambazo ni za maelezo tu. Mfano suala la haki za binadamu ambazo wote tunakubaliana nazo.”
Alisema wakati wa kujadili muundo wa Serikali ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ukifika, ataishauri kamati ya uongozi, kutenga muda wa ziada katika suala hilo na mengine yenye utata.
Mwenyekiti huyo alisema suala la upigaji kura linatakiwa kuamuliwa kwa busara na atatumia hekima zake na za wajumbe wa Bunge hilo, kutatua mgogoro wa kura ya siri au ya wazi.
Wakati wa kujadili rasimu ya kanuni za Bunge hilo, kulizuka mvutano mkali katika vifungu vya 37 na 38 vinavyozungumzia aina ya kura itakayopigwa wakati wa kufanya uamuzi na kulazimika kuviweka kando. CCM kimekuwa kikinadi kura ya wazi kikisema ni ya haki huku wapinzani wakitaka kura ya siri.
Hata hivyo, kamati ya muda iliyoandaa kanuni za Bunge hilo, ilipendekeza kuwa Bunge Maalumu ndilo litakaloamua aina ya kura itakayopigwa.
Akizungumzia suala hilo Sitta alisema: “Pamoja na kuwapo kwa hali hiyo, lazima ifikie wakati tuamue. Hatuwezi kuwa na kanuni ambazo hazielekezi namna ya kupiga kura kwa sababu upigaji wa kura unaweza kuanza kufanyika wiki ya kwanza tu baada ya kuanza kujadili Rasimu ya Katiba.”
Samia Makamu Mwenyekiti
Wakati huohuo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan jana alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Bunge hilo baada ya kumshinda mpinzani wake, Amina Abdallah Amour.
Akitangaza matokeo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi, Dk Thomas Kashililah alisema kati ya kura 523 zilizopigwa, Suluhu alipata kura 390 sawa na asilimia 74.6, Amina kura 126 sawa na asilimia 24.1. Kura saba ziliharibika.
Kukamilika kwa uchaguzi huo kunafungua milango kwa Yahya Hamad Hamis kuapishwa kuwa Katibu wa Bunge la Katika na Dk Thomas Kashililah kuwa Naibu Katibu kwa mujibu wa sheria.
Makatibu hao wataapishwa leo saa nne asubuhi na Rais Jakaya Kikwete katika Ikulu ndogo ya Dodoma. Baada ya kuapishwa, Katibu atawaapisha Sitta na Samia katika Ukumbi wa Bunge kuanzia saa 10 jioni leo.
Awali wakati wakijieleza Amina alizua gumzo baada ya kueleza kuwa licha ya kuwa na watoto watano, ameachika na kwa sasa hana mume.
“Mimi ni mama wa watoto watano, nina shahada ya uzamili ya masuala ya fedha, nina stashahada ya sheria na nimefanya kazi katika Benki ya Biashara kwa miaka 23 ila kwa bahati mbaya nimeachika,” alisema na kusababisha wajumbe kuangua kicheko.
Baada ya kuchaguliwa, Suluhu alisema: “Nitafanya naye (Sitta) kazi kwa ushirikiano na uadilifu mkubwa. Pia ninawaahidi wajumbe wote kuwa nitawapa ushirikiano.”
Mbowe amuonya Sitta
Wakati huohuo; Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amemtumia salamu za pongezi Sitta huku akimtaka kuachana na masilahi ya chama chake.
“Ningependa kutuma salamu kwa Samuel Sitta ambaye amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, nataka aelewe kuwa alichokabidhiwa ni majukumu si cheo,” alisema na kuongeza:
“Mamilioni ya Watanzania watakuwa wanamfuatilia na kumtazama kwa makini mno... maana wananchi kwa sasa wanajua mchakato wa Katiba Mpya umebeba matumaini ya Taifa lao kwa miaka 50 hadi 100 ijayo.

Thursday 13 March 2014

Serikali yaingilia kati ada vyuo vikuu

Dar es Salaam. Serikali imekunjua makucha yake katika kudhibiti ada zinazotozwa katika vyombo vya utoaji elimu chini.
Jana, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa alizindua rasmi mfumo mpya wa ulipaji ada katika vyuo vya elimu ya juu, huku akisema utasaidia kudhibiti viwango vya ada vinavyotozwa kwa wanafunzi.
Akizindua mfumo huo jijini Dar es Salaam, Dk. Kawambwa alisema Serikali imeanzisha mfumo huo unaotarajiwa kuanza kutumika mwaka huu katika vyuo vyote, kwa lengo la kudhibiti ada kulingana na fani zinazotolewa.
“Sasa natarajia nitapata usingizi wa kueleweka maana kelele za viwango vya ada zilikuwa ni kubwa, kila chuo kilikuwa na ada yake. Niliulizwa vigezo vinavyotumika kupanga sikuwa na jibu, lakini sasa nitakuwa na majibu tena yanayoeleweka,” alisema.
Suala la viwango vya ada katika shule na vyuo binafsi liliwahi kuzungumziwa kwa kina siku za nyuma, huku Rais Jakaya Kikwete na Waziri Kawambwa wakinukuliwa kwa nyakati tofauti kutaka taasisi za elimu kupunguza viwango vya elimu. Aprili 2013 akifungua Mkutano Mkuu Maalumu wa Chama cha Wamiliki na Mameneja wa Shule na Vyuo Visivyokuwa vya Serikali (Tamongsco) uliofanyika mkoani Mbeya, Rais Kikwete alisema: “Elimu ni huduma muhimu na haki kwa mtoto. Siyo vyema kugeuzwa kuwa biashara ya kuleta faida kubwa.’’
Aliongeza kuwa Serikali ilikuwa katika mchakato wa kutathmini ada zinazotozwa vyuoni na sekondari ili kupendekeza viwango halisi vinavyopaswa kutozwa.
Kwa sasa udadisi wa gazeti hili umebaini kuwa wanafunzi walioanza masomo katika mwaka wa fedha 2013/2014 wanatozwa ada kuanzia Sh360,000 kwa mwaka hadi Sh9,900,000.
Kwa mujibu wa Dk. Kawambwa, mfumo huu ambao baadaye utaendelea hadi shule za sekondari na msingi, umepatikana kupitia kikosi kazi cha wataalamu ambacho pamoja na majukumu mengine kilipewa kazi ya kutathmini gharama.
Dk. Kawambwa alisema moja ya faida ya utaratibu huo mpya ni kudhibiti taasisi zinazotoza ada kubwa kwa sababu za binafsi ikiwamo biashara.
Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Tumaini Makumira cha Dar es Salaam (Tudarco), Profesa Uswege Minga alisema endapo gharama hizo zitakuwa sawa, vyuo binafsi vitaathirika kwa sababu ni gharama kubwa kuendesha chuo kikuu.

Mbatia: Katiba itapatikana kwa maridhiano

Dodoma. Jina la mwanasiasa James  Mbatia si geni sana miongoni mwa Watanzania na amejizolea sifa ya kutanguliza masilahi ya taifa tangu mchakato wa kupata Katiba Mpya ulivyoanza.
Mbatia, ambaye alishiriki katika harakati za kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi miaka ya 1990,  mara nyingi amejitokeza kusaka mwafaka pale inapotokea sintofahamu kwenye vikao vya Bunge Maalumu la Katiba.
Busara aliyoitumia wakati wa upitishaji wa muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013, ndiyo aliyoirudia katika Bunge Maalumu la Katiba.
“Dalili za kutopatikana kwa Katiba Mpya zimeanza kuonekana, ni vizuri ikatumika busara na hekima katika kuvuka kikwazo hiki na njia pekee ni maridhiano,” alisema Mbatia, Septemba,  mwaka jana.
Mbatia aliyotoa maneno hayo baada ya wabunge wote kutoka kambi ya upinzani isipokuwa Mwenyekiti wa TLP, Augustino Mrema wa TLP kususia upitishaji wa muswada kupinga ubabe wa CCM.
“Sisi siyo tutakaoifanya Tanzania isitawalike bali CCM. Tunafanya haya kwa nia njema kabisa hatutaki damu ya Watanzania imwagike kwa jambo linaloepukika,” alisema Mbatia katika kipindi hicho.
Katika kipindi hiki cha Bunge la Katiba,  busara hiyo ndiyo imetumika ili kusawazisha mambo wakati yalipokuwa yanakwenda vibaya kwenye semina ya kujadili Rasimu ya Kanuni.
Bunge hilo lilikuwa katika hati hati ya kuvunjika katika siku za awali tu za utungaji wa Katiba pale lilipojikuta likiwa njia panda kuhusu kuamua aina ya kura itumike kuamua vifungu vya Rasimu.
Kwanini Mbatia anaamini falsafa ya Katiba ni tendo la maridhiano?
Katika mahojiano maalumu na gazeti hili, Mbatia anasema Katiba siku zote ni tendo la maridhiano na kutoa mfano wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.
 “Mwezi Aprili  22, mwaka 1964, Rais Nyerere (Julius) alikaa na Rais Karume (Abeid) wa Zanzibar wakakubaliana kuwa nchi hizi ziungane, hili lilikuwa tendo la maridhiano,” anasema Mbatia.
“Kwa hiyo Aprili 24, mwaka 1964 Bunge la Tanganyika lilikaa na kutunga sheria ya maridhiano hayo na baadaye Aprili 26, mwaka huo, Muungano ukazaa nchi inayoitwa Tanzania,” anasema Mbatia.
Kwa msingi huo, Mbatia ambaye pia ni Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, anasema siku zote maridhiano yanaanza kwanza na watu wakishaafikiana ndio wanayatungia sheria.
“Tuna mfano mwingine wa kujifunza kule Zanzibar,  Seif Shariff Hamad (Katibu Mkuu CUF) na Rais Amani Karume walijifungia Ikulu Novemba mwaka 2009 na wakafanya tendo la maridhiano,” anasema.
“Walikaa wao wawili tu wakaridhiana kuwa watafute mwafaka na baada ya kuridhiana Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, likaitwa na kufanya mabadiliko ya 10 ya Katiba ili kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa,”anasema Mbatia.
Mbatia anasema maridhiano hayo ndiyo yaliyowafanya Watanzania na watu wengi duniani washuhudie Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2010 ukifanyika  bila tone la damu ya Mzanzibari kumwagika.
“Tume ya Jaji Warioba (Joseph) imekusanya maoni ya Wanzania na kupendekeza muundo wa Serikali tatu kuwa ndiyo chaguo la Watanzania lakini leo CCM wanatilia shaka uadilifu wa Jaji Warioba.
“Nawashauri rafiki zangu wa CCM wasianze kuhoji leo uadilifu wa Jaji Warioba. Yeye na mzee Butiku (Joseph) ni wafuasi wa karibu sana wa Nyerere lakini wameheshimu maoni ya Watanzania,” anaonya Mbatia.
Mbatia anasema ni vizuri wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, wakaiboresha Rasimu ya Katiba na kwamba kama kuna hoja mpya za kujenga ziingizwe lakini si kwa vitisho na ubabe.
“Kulazimisha mambo yenye mwelekeo wa kupatikana kwa Katiba yenye masilahi mapana ya CCM, litakuwa jambo la kutowatendea haki Watanzania na hicho kitakuwa ndiyo chanzo cha machafuko,” anaeleza Mbatia.
Mbatia anasema ni katika msingi huo huo wa kutaka Tanzania isiingie kwenye machafuko, ndiyo maana alipendekeza kuundwa kwa Kamati ya Maridhiano baada ya kujitokeza kwa dalili mbaya.
“Tulikuwa tumekwama katika njiapanda…CCM wameng’ang’ania kura ya wazi wakati wanajua si matakwa ya kidemokrasia, sasa mimi nikaona hapana hebu turudi kwenye maridhiano,” anasema Mbatia.
Mbatia anasema kwa moyo huo huo wa maridhiano alioupendekeza, ndio ulisaidia kupatikana kwa mwafaka juu ya kanuni ya 37 na 38 ya Bunge Maalumu la Katiba na kuongeza;
“Bila kuundwa kwa kamati ya maridhiano nina hakika Bunge hili lingekuwa limeshasambaratika lakini bado ‘spirit’ (moyo) ipo na hali hii ndiyo tunataka iendelee kwa sababu bado tuna shughuli pevu.
Mbatia anasema kutaibuka mvutano katika vifungu hivyo pale watakapofikia hatua ya kupitisha ibara za Katiba na kuwataka CCM wasome alama za nyakati na kutazama matakwa ya Watanzania.
“CCM waelewe kuwa Watanzania wanatutazama, leo wanapolazimisha kura ya wazi kupitisha Katiba halafu tukienda kwenye kura ya maoni Katiba hiyo hiyo ipigiwe kura ya siri, hakuna atakayewaelewa.”
Mbatia aliongeza kusema; ”Hakuna ubishi kuwa mabadiliko ya 10 ya Zanzibar yalikiuka Katiba ya Muungano na Watanzania wanalifahamu hilo lakini hoja ya msingi hapa ni maridhiano.”
Mabadiliko hayo ndio yaliyotamka kuwa Zanzibar ni nchi yenye mipaka yake, ina Katiba yake, ina bendera yake na ina wimbo wake wa Taifa, kitendo kinachotafsiriwa kuwa ni uhaini kwa mujibu wa Katiba ya Muungano.
Mbatia ni nani hasa?
Mbatia ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kuteuliwa na Rais,  Mwenyekiti wa Taifa wa NCCR-Mageuzi na amesoma fani ya uhandisi wa majengo.

Mabilioni Uswisi yachotwa

Dar es Salaam. Mabilioni ya shilingi yaliyowekwa na Watanzania katika benki za Uswisi yameanza kuhamishwa kimyakimya.
Ripoti ya Benki za Uswisi ya 2012 inaonyesha kuwa fedha zinazotoka Tanzania zimepungua kwa karibu Sh.36.4 bilioni ikilinganishwa na zilizokuwapo 2011 nchini humo, lakini haielezi sababu ya kupungua kwake.
Taarifa za kuhamishwa kimyakimya kwa fedha hizo ambazo zinaaminika kuwekwa na Watanzania waliowahi kuwa katika utumishi wa umma, imekuja wakati ambao Serikali inasubiriwa kutoa taarifa yake kuhusu vigogo walioficha fedha nchini humo, ambazo zinaaminika walizipata kwa njia zisizo halali.
Awali, kiasi cha fedha kilichotajwa kufichwa katika benki hizo ni Sh.327.9 bilioni (Dola za Marekani 204.96 milioni), lakini taarifa mpya ya 2012 inaonyesha kuwa kiasi hicho kimepungua hadi Dola za Marekani 182.2 milioni (Sh.291.5 bilioni).
Kiasi hicho cha fedha kinaweza kujenga barabara ya lami yenye urefu wa kilomita 300 ambao ni sawa na kutoka Morogoro hadi Iringa.
Akizungumzia ripoti hiyo, Balozi wa Uswisi nchini, Olivier Chave alisema: “Hadi mwisho wa 2012, fedha zilizopo kutoka Tanzania zimebaki Faranga za Uswisi 160 milioni (Dola za Marekani 182.2 milioni) na siyo zile za awali ambazo ni Faranga za Uswisi 180 milioni (Dola za Marekani 327.9 milioni)……. hivyo ndiyo kusema kuwa fedha hizo zinapungua,” alisema Chave na kuongeza:
“Inawezekana ni kutokana na kelele za vyombo vya habari hasa Mwananchi, pengine wenye fedha wameamua kuzihamishia kwenye benki za nchi nyingine. Sisi Serikali ya Uswisi tunapochapisha ripoti kama hizi kuonyesha jumla ya fedha kwa nchi zote duniani, haimaanishi kuwa fedha zote hizo ni haramu.”
Alisema ni makosa kwa vyombo vya habari kuendelea kuonyesha kwamba ni Uswisi pekee kunakofichwa fedha chafu, kwani zipo nchi nyingine ambako watu wa mataifa mbalimbali huweka fedha zao ambazo zimepatikana kwa njia haramu.
Benki za Uswisi zimekuwa zikidaiwa kutumika kuficha fedha chafu kutoka maeneo mbalimbali duniani kutokana na usiri wake katika kutunza taarifa za wateja.
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa Kenya inaongoza kwa nchi za Afrika Mashariki kwa kuwa na kiasi kikubwa cha fedha ambacho ni karibu Sh.1.6 trilioni ikifuatiwa na Uganda Sh.376.7 bilioni, kisha Tanzania Sh.291.5 bilioni.
Rwanda ina Sh.55.1 bilioni na Burundi Sh.42.2 bilioni.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alipoulizwa jana kuhusiana na taarifa hizo mpya alisema suala hilo la fedha zilizopo Uswisi si la kuzungumza kwenye vyombo vya habari.

“Hili jambo ni jambo nyeti sana kwa sababu kazi tuliyopewa kuchunguza suala hili bado hatujamaliza, kwa hiyo kuanza kulizungumza kwenye vyombo vya habari kunaweza kuathiri kazi hii,” alisema Jaji Werema.
Aliwaomba Watanzania kuvuta subira juu ya jambo hilo akisema kamati yake inaendelea kufuatilia na taarifa itawasilishwa.

Bilionea Mmarekani akoleza vita dhidi ya ujangili

Dar es Salaam. Familia ya bilionea namba mbili nchini Marekani, Warren Buffett imeunga mkono juhudi za kupambana na ujangili nchini kwa kuchangia helikopta moja.
Familia ya Warren Buffett imeamua kutoa msaada huo kupitia Mfuko wa Howard Buffett Foundation, baada ya kuridhishwa na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali.
Helikopta hiyo itatumika kwa ajili ya kusaidia mapambano dhidi ya ujangili katika hifadhi za taifa na mapori ya akiba nchini.
Msaada huo ulikabidhiwa juzi kwa Rais Jakaya Kikwete na mtoto wa bilionea huyo, Howard Buffett, ambaye yuko nchini kwa mapumziko ya kitalii.
Akikabidhi mfano wa helkopta kwa Rais Kikwete, Buffett alisema amevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Tanzania katika kukabiliana na ujangili hususan wa tembo na faru.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alisema wamepokea kwa furaha ufadhili huo, ambapo utahusisha mafunzo kwa marubani wawili nchini Marekani ama Afrika Kusini kutokana na matakwa ya wizara.
“Wametuambia pesa ipo tayari ila ni jukumu letu sisi kama Serikali kuchagua aina ya helikopta tunayoitaka. Itakuwa na uwezo wa kubeba watu sita na kwa sasa tunaangalia kama tuchukue Bell ama Ecopter, wataalamu wanashughulikia,” alisema.

Daraja Kigamboni neema au balaa?

Pembezoni mwa Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Tanzania (Tec), ujenzi unaendelea wa barabara na daraja la kuunganisha Mji wa Kigamboni na Jiji la Dar es Salaam, eneo la Mkondo wa Kurasini. Ujenzi huo unafanywa na kampuni mbili kutoka nchini China.
Kampuni hizo ni; China Railway Jiangchang (T) Ltd na China Major Bridge, mradi ambao unatarajiwa kukamilika Januari 2015 ukigharimu dola 136 milioni za Marekani, fedha ambazo asilimia 60 zinatolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na kiwango kingine kinalipwa na serikali.
Ujenzi huo unafanyika ikiwa ni sehemu ya kuwaondolea kero ya Kivuko wakazi wapatao 679,291 sawa na asilimia 5.7 ya watu wote wa Dar es Salaam na idadi hiyo ni tofauti na mamia wengine ambao wanaenda eneo hilo kila siku kwa ajili ya shughuli tofauti zikiwamo za kiuchumi.
Eneo la Kigamboni ambalo limelengwa kuwa mji mpya wa kisasa, lina utajiri mkubwa wa mazao mbalimbali ya chakula, biashara kama vile mbogamboga, matunda, viazi vitamu, magimbi, nazi, korosho na mazao ya baharini wakiwamo samaki, mapambo ya majumbani na bidhaa nyingine.
Pia mji huo una hifadhi historia kwani maeneo ya Mbwamaji, Puna, Kimbiji, Pembamnazi, Buyuni na kwingineko kuna mabaki ya majengo ya kihistoria ambayo hata hivyo yanatoweka kutokana na utunzaji na harakati za ujenzi wa nyumba za kisasa.
Pia eneo hilo linasifika kwa kuwa na fukwe zenye mchanga wa kuvutia na mandhari nzuri za kupendeza hali ambayo inachangia kuwavutia watalii na wageni wengine wanaotembelea eneo hilo ambalo pia upande mwingine ina hazina kubwa ya jiwe la jasi ambalo hutumika kutengenezea saruji.
Kulingana na mkandarasi ambaye ni mbunifu wa mradi huo ambalo ni la kuning’inia (Cable-Stayed Bridge), lina urefu wa mita 680 na upana wa mita 27.5 na linatarajiwa kuwa mbadala wa Kivuko cha Kigamboni ambacho kina pantoni za Mv Kigamboni na Magogoni.
Ujenzi huo unakaribia kukamilika, lakini hadi sasa gharama za kulitumia daraja hilo kwa wananchi wa kawaida, wenye magari, baiskeli, mikokoteni na vyombo vingine bado hazijainishwa. Suala hilo linawaacha watu weni katika maswali mengi kuliko majibu.
Ingawa hakijatajwa kiwango kitakachokuwa kinatozwa kama ada na ushuru mwingine, lakini bado kuna utata iwapo mradi huo utakamilika kwa wakati kutokana na sababu nyingi ikiwa ni pamoja na ukweli kuwa mradi umefikia zaidi ya asilimia 50 ya ujenzi wake, lakini kuna utata iwapo ujenzi utakamilika kwa wakati.
Hali hiyo inatokana na ukweli kuwa hadi hivi sasa serikali haijatoa kiasi chochote kati ya asilimia 40 ya fedha ambazo wanatakiwa kuchangia ili kukamilisha mradi huo hali ambayo inadaiwa kukwamisha upatikanaji wa fedha za fidia kwa baadhi ya watu ambao wanaguswa na mradi.
Msimamizi wa mradi huo, Mhandisi Karimu Mataka wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), anakiri serikali kutokutoa fedha ambazo iliahidi hadi sasa, na hali hiyo imechangia mradi kushindwa kukamilika Januari mwakani kama ilivyokadirwa na badala yake sasa unatarajiwa kukamilika Juni mwakani.
John Ngoma maarufu kwa jina la Jitu,mkazi wa eneo la Kijibweni ambaye eneo lake limechukuliwa kwa ajili ya kutoa nafasi ya utekelezaji wa mradi huo anasema ni vizuri wakaelezwa kiasi cha fidia watakachopewa kabla ya uthamini kufanywa jambo ambalo linapingwa na mfumo mzima wa fidia.
Kulingana na taratibu na kanuni za fidia, zinafanyika kwanza, kisha ndio malipo hupangwa tofauti na wanavyotaka wakazi hao ambao wanataka waambiwe kwanza watalipwa nini.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Injinia Mussa Iyombe, alipotembelea kujionea maendeleo ya ujenzi wa daraja hilo, anasema lilitarajiwa kukamilika Januari mwaka 2015, lakini sasa itaenda hadi Juni na wakazi wa eneo hilo ambao anasema idadi yao haizidi watu wanne suala lao limefikishwa wizarani.
Anasema ujenzi wa daraja hilo ulitarajiwa kukamilika Januari mwakani, lakini kutokana na changamoto walizokutana nazo wahandisi chini ya bahari na kwa wananchi zimewafanya wachelewe na sasa wanatarajia kukamilisha kazi hiyo Julai mwakani.
Mhandishi anasema kuwa licha ya changamoto zote wakandarasi wamekuwa wakiendelea vizuri na kile ambacho kimefanyika hadi hivi sasa kinatoa matumaini kwa Watanzania kuwa mradi utakamilika kwa wakati hivyo kuwaondolea kero.
Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Vijibweni, Bahari Mohamed anasema kimsingi fedha za fidia kwa ajili ya watu hao ambao wamegoma kutoa nafasi kwa mradi zipo na iwapo wataridhia na kuvunja nyumba zao watalipwa na iwapo wataendelea na mgomo huenda nyumba hizo zikavunjwa kwa nguvu na fidia wataifuata wakitaka.
“Fedha zipo isipokuwa wamegoma watu watatu katika eneo ambako wamejenga nyumba, mmoja wao anamiliki kiwanja ambacho hakijaendelezwa,” anasema Mohamed.
Mohamed anasema daraja litakuwa na faida kiuchumi iwapo wakazi wake watalitumia vizuri na kuwekwa utaratibu wa kueleweka.
Anasema ingawa hajui watu watatozwa kiasi gani cha fedha wakati wa kuvuka, amedokezwa kwamba waenda kwa miguu watapita bure isipokuwa wale wenye vyombo vya usafiri kama vile pikipiki, magari na mikokoteni.
“Nasikia waenda kwa miguu itakuwa bure hilo halina uhakika kwani hadi sasa haijaelezwa gharama zake zitakuwa vipi,” anasema.
Mmoja wa wachukuzi wa abiria katika boti iitwayo Kilimanjaro katika eneo hilo, Idrissa Hussein anasema wao wataangalia upepo unavyoeenda kwani wamekuwa wakitoa huduma hiyo kwa kipindi kirefu tena katika mazingira magumu.
“Kama watatoza fedha watu kuvuka tutaangalia ni kiasi gani kama italipa tutaendelea na huduma kwa kiwango cha sasa au pungufu yake la sivyo tutaangalia jambo lingine la kufanya kwani mashine na vyombo bado ni mali yetu,” anasema.
Mkazi wa eneo hilo, Jonathan Ngosha anasema endapo daraja hilo litatumika kutoa huduma kwa wananchi, litakuwa ni msaada mkubwa kwao.
Lakini anasema Daraja la Kigamboni likitumiwa kama kitegauchumi, watu wengi wataendelea kutumia boti kuvuka kutoka Kigamboni hadi upande wa pili wa maeneo ya Kurasini.
Mkazi huyo anataka gharama za matumizi ya daraja hilo ziwe wazi kwa ajili ya kuwaandaa wakazi wa eneo hilo na sio kuwa kimya kama ilivyo sasa kwani hali hiyo inazua maswali mengi kuliko majibu.