Habari za kimataifa

 Bush kuwasili nchini Tanzania
Idadi ya watu waliofariki dunia baada ya mlipuko wa bomu katika mkutano wa Chadema imeongezeka baada ya mtoto Fahad Jamal (7) ambaye hali yake ilikuwa mbaya na kulazwa chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) katika Hospitali ya Selian, kuaga  dunia juzi saa saba mchana hospitalini hapo.
Kwa mujibu wa Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, Dk Paul Kisanga mtoto huyo alifariki dunia wakati timu ya madaktari kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MOI) na Hospitali ya Jeshi ya Lugalo, Dar es Salaam wakijitahidi kila hali kuokoa maisha yake.
Kifo hicho kinaongeza idadi ya marehemu na kuwa wanne baada ya vifo vya Amiri Ally (7), Judith Moshi (25) ambaye ni Katibu wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) Kata ya Sokon One jijini hapa na Ramadhan Juma (15).
Dk Kisanga alisema hospitali hiyo juzi ilipokea majeruhi wengine 17 wa mabomu ya kutoa machozi katika eneo la Soweto wakati polisi wakitawanya wafuasi wa Chadema.
Alisema majeruhi 14 wamelazwa huku watatu wakitibiwa na kuruhusiwa ambapo pia Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari aliyekuwa amelazwa hapo kutokana na kuumia shingoni aliruhusiwa na hali yake inaendelea vizuri.
Mganga Mkuu alaani Naye Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Mount Meru, Dk Frida Mokiti, amelaani vitendo vya uvunjifu wa amani na vitisho vya wafuasi wa Chadema, ambavyo vilisababisha kuvunjwa kwa mlango wa gari la wagonjwa na kuvunja lango kuu la kuingilia hospitalini hapo.
Alisema katika tukio hilo la bomu, wafuasi hao wa Chadema, walitishia madaktari na wauguzi wa zamu na kutaka kuchoma moto majengo ya hospitali hiyo, wakishinikiza kutibiwa haraka kwa majeruhi wa bomu.
Aliongeza kuwa hospitali haikupata taarifa mapema ya mlipuko huo na hivyo kuchelewa kupeleka gari la wagonjwa kwenye eneo la tukio ili kutoa msaada na kilichotokea ni wafuasi wa chama hicho wakiwa na majeruhi walifika hospitalini na kuanza vitisho na kufanya fujo zikiwamo kutishia kuchoma moto magari na majengo ya hospitali hiyo.
Alisema hospitali hiyo haibagui wagonjwa wala haitoi huduma kwa itikadi au imani ya mgonjwa bali kazi yake ni kuhudumia watu wote bila ubaguzi.
Dk Mokiti, aliishukuru Wizara ya Maliasili na Utaliii kwa misaada ya vifaa vyenye thamani ya Sh milioni 120 kwa hospitali zote tatu za Mount Meru, Selian na St Elizabeth.
Alisema pia wamepokea madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Moi Kenya, ambao wameongeza nguvu ya kuhudumia majeruhi wa mlipuko huo. Wakati huo huo, kitendo cha wanasiasa kunyoosheana vidole kuhusu tukio hilo la bomu kimeshutumiwa kuwa kinaweza kuathiri upatikanaji wa wahusika sahihi.
Watu wa kada mbalimbali waliozungumza na gazeti hili, walisema shutuma na mvurugano miongoni mwa wanasiasa, vitasababisha Serikali kujikita katika kutatua mifarakano hiyo badala ya kutafuta mbaya wa Watanzania.
Utalii Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu akizungumza na vyombo vya habari jijini hapa kuhusu sekta ya utalii kuathirika na milipuko ya mabomu Arusha au safari za watalii kusimama, alisema hali ya usalama Tanzania hususan Arusha ni nzuri na kuomba watalii kuendelea kuja nchini kuona vivutio vya utalii.
Alisema Tanzania kuna amani na ndiyo maana hata Rais wa Marekani, Barack Obama anatarajia kuja nchini na kuongeza kuwa kutokana na amani iliyopo milango ya utalii imezidi kufunguka, kwani hivi sasa watalii kutoka Japan, China, Uturuki na sehemu mbalimbali duniani wanakuja kuangalia vivutio hivyo.
Aliongeza kuwa amani ni muhimu kwa Tanzania hususan Arusha ambalo ndio mlango wa sekta ya utalii na kuwasihi viongozi wa vyama vya kisiasa kuhakikisha wanalinda amani nchini kwani endapo itapotea waathirika wengi wakiwamo wadau wa sekta ya utalii, hoteli, wauzaji mboga na wengine wataathirika kimapato na uchumi kudorora.
Katika hatua nyingine, wananchi wa Arusha na viunga vyake, wanaendelea na shughuli zao za kila siku huku wengine mapema jana asubuhi walifika eneo la Soweto kuangalia vitu walivyokuwa wameangusha juzi.
Mwandishi wa habari hizi, alishuhudia baadhi wakiwapa watoto wa mitaani Sh 500 hadi Sh 1,000 ili kuwasaidia kuangalia kama simu, pochi na vitambulisho vyao kama vipo; wengine walivipata lakini wengine hawakuambulia kitu.
Imeandikwa na Veronica Mheta, Gloria Tesha, Shadrack Sagati na Prisca Libaga
Share/Bookmark

No comments: