Wednesday 23 October 2013

Mshahara wa mwajiriwa wa wananchi unakuwaje siri


Share

Dar es Salaam. Ni ajabu kusikia kauli ya Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe kuhusu mishahara wanayolipwa Rais na Waziri Mkuu inazusha mjadala mkubwa.
Zitto akiwa wilayani Igunga hivi karibuni, alijitoa mhanga na kutangaza viwango alivyodai  kuwa ni mishahara ya rais na waziri mkuu kwa mwezi, huku akihoji iweje viwango viwe siri na visikatwe kodi.
Baadhi ya watu wamepinga hatua hiyo wakisema mshahara wa mtu ni siri yake. Waliopinga ni pamoja na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai na Waziri wa Nchi Katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya utumishi wa Umma, Celina Kombani akisema kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Sawa, inaweza kuwapo sheria inayozuia jambo hilo, lakini kwanini itungwe sheria ya namna hiyo?
Kwa upande wangu naunga mkono mishahara hiyo kuwa wazi. Nakubali kwamba mshahara wa mtu ni siri yake, lakini kwa viongozi wa umma kama rais na waziri mkuu, mishahara yao haipaswi kuwa siri, ndiyo maana nchi nyingi duniani zikiwemo Marekani, Ufaransa, Kenya na Afrika Kusini, mishahara ya viongozi kama huwekwa wazi.
Ifahamike kuwa rais ni kiongozi anayechaguliwa na wananchi, wao ndiyo wanaompa ajira ya kuwatumikia. Iweje mwajiri asijue anacholipwa mtumishi wake?
Kwenye nchi zilizoendelea kidemokrasia kama vile Marekani na nchi za Ulaya, masilahi na utendaji wa rais na waziri mkuu na viongozi wengine ni ya kikatiba.
Wananchi wanajua wazi kabisa, rais wanayemchagua watamlipa kiasi gani, Katiba inamwelekeza rais ateue mawaziri wangapi na watendaji wa Serikali kwa idadi maalumu.
Cha ajabu huku kwetu, rais anaamua kufanya atakavyo – anaweza hata kuteua mawaziri idadi anayoitaka na asiulizwe, mambo yanafanywa kwa siri ndiyo maana hata mikataba ya madini na uwekezaji mwingine ni siri.
Siri hizi za nini kama sisi wananchi ndiyo tumeichagua Serikali yetu wenyewe?
Hoja nyingine ni kuhusu mshahara wa rais kutokatwa kodi. Rais ni mtumishi wa umma namba moja na mlezi wa watumishi hata wa sekta binafsi.
Kwa muda mrefu wafanyakazi wamekuwa wakilalamikia kiwango cha asilimia 15 cha kodi wanayokatwa katika mishahara ndiyo ikashushwa hadi asilimia 14, hata hivyo bado ni mzigo.
Lakini rais atauonaje mzigo huo ikiwa yeye hakatwi kodi? Rais kwa mujibu wa Zitto analipwa wastani wa Sh32 milioni kwa mwezi bila kukatwa kodi, ana marupurupu ya safari za ndani na nje ya nchi na posho nyinginezo.
Kwa maana nyingine rais anaweza asiuguse kabisa mshahara wake kwa posho hizo, lakini bado akistaafu analipwa pensheni na atatunzwa na Serikali maisha yake yote.
Tuna viongozi wa Serikali wangapi wanaolipwa hivi, tuna marais wastaafu na mawaziri wakuu wangapi wanaofaidi kiinua mgongo cha Serikali huku idadi kubwa ya Watanzania ikiteseka katika lindi la umasikini na mlolongo wa kodi?

No comments: