Idadi ya watu waliofariki Tanzania yaongezeka
Idadi ya watu waliofariki dunia baada ya
mlipuko wa bomu katika mkutano wa Chadema imeongezeka baada ya mtoto
Fahad Jamal (7) ambaye hali yake ilikuwa mbaya na kulazwa chumba cha
wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) katika Hospitali ya Selian,
kuaga dunia juzi saa saba mchana hospitalini hapo.
Kwa mujibu wa Kaimu Mganga Mkuu wa
Hospitali hiyo, Dk Paul Kisanga mtoto huyo alifariki dunia wakati timu
ya madaktari kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MOI) na Hospitali ya
Jeshi ya Lugalo, Dar es Salaam wakijitahidi kila hali kuokoa maisha
yake.
Kifo hicho kinaongeza idadi ya marehemu
na kuwa wanne baada ya vifo vya Amiri Ally (7), Judith Moshi (25) ambaye
ni Katibu wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA) Kata ya Sokon One
jijini hapa na Ramadhan Juma (15).
Dk Kisanga alisema hospitali hiyo juzi
ilipokea majeruhi wengine 17 wa mabomu ya kutoa machozi katika eneo la
Soweto wakati polisi wakitawanya wafuasi wa Chadema.
Alisema majeruhi 14 wamelazwa huku
watatu wakitibiwa na kuruhusiwa ambapo pia Mbunge wa Arumeru Mashariki,
Joshua Nassari aliyekuwa amelazwa hapo kutokana na kuumia shingoni
aliruhusiwa na hali yake inaendelea vizuri.
Mganga Mkuu alaani Naye Mganga Mkuu wa
Hospitali ya Mkoa wa Mount Meru, Dk Frida Mokiti, amelaani vitendo vya
uvunjifu wa amani na vitisho vya wafuasi wa Chadema, ambavyo
vilisababisha kuvunjwa kwa mlango wa gari la wagonjwa na kuvunja lango
kuu la kuingilia hospitalini hapo.
Alisema katika tukio hilo la bomu,
wafuasi hao wa Chadema, walitishia madaktari na wauguzi wa zamu na
kutaka kuchoma moto majengo ya hospitali hiyo, wakishinikiza kutibiwa
haraka kwa majeruhi wa bomu.
Aliongeza kuwa hospitali haikupata
taarifa mapema ya mlipuko huo na hivyo kuchelewa kupeleka gari la
wagonjwa kwenye eneo la tukio ili kutoa msaada na kilichotokea ni
wafuasi wa chama hicho wakiwa na majeruhi walifika hospitalini na kuanza
vitisho na kufanya fujo zikiwamo kutishia kuchoma moto magari na
majengo ya hospitali hiyo.
Alisema hospitali hiyo haibagui wagonjwa
wala haitoi huduma kwa itikadi au imani ya mgonjwa bali kazi yake ni
kuhudumia watu wote bila ubaguzi.
Dk Mokiti, aliishukuru Wizara ya
Maliasili na Utaliii kwa misaada ya vifaa vyenye thamani ya Sh milioni
120 kwa hospitali zote tatu za Mount Meru, Selian na St Elizabeth.
Alisema pia wamepokea madaktari bingwa
kutoka Hospitali ya Moi Kenya, ambao wameongeza nguvu ya kuhudumia
majeruhi wa mlipuko huo. Wakati huo huo, kitendo cha wanasiasa
kunyoosheana vidole kuhusu tukio hilo la bomu kimeshutumiwa kuwa
kinaweza kuathiri upatikanaji wa wahusika sahihi.
Watu wa kada mbalimbali waliozungumza na
gazeti hili, walisema shutuma na mvurugano miongoni mwa wanasiasa,
vitasababisha Serikali kujikita katika kutatua mifarakano hiyo badala ya
kutafuta mbaya wa Watanzania.
Utalii Naibu Waziri wa Maliasili na
Utalii, Lazaro Nyalandu akizungumza na vyombo vya habari jijini hapa
kuhusu sekta ya utalii kuathirika na milipuko ya mabomu Arusha au safari
za watalii kusimama, alisema hali ya usalama Tanzania hususan Arusha ni
nzuri na kuomba watalii kuendelea kuja nchini kuona vivutio vya utalii.
Alisema Tanzania kuna amani na ndiyo
maana hata Rais wa Marekani, Barack Obama anatarajia kuja nchini na
kuongeza kuwa kutokana na amani iliyopo milango ya utalii imezidi
kufunguka, kwani hivi sasa watalii kutoka Japan, China, Uturuki na
sehemu mbalimbali duniani wanakuja kuangalia vivutio hivyo.
Aliongeza kuwa amani ni muhimu kwa
Tanzania hususan Arusha ambalo ndio mlango wa sekta ya utalii na
kuwasihi viongozi wa vyama vya kisiasa kuhakikisha wanalinda amani
nchini kwani endapo itapotea waathirika wengi wakiwamo wadau wa sekta ya
utalii, hoteli, wauzaji mboga na wengine wataathirika kimapato na
uchumi kudorora.
Katika hatua nyingine, wananchi wa
Arusha na viunga vyake, wanaendelea na shughuli zao za kila siku huku
wengine mapema jana asubuhi walifika eneo la Soweto kuangalia vitu
walivyokuwa wameangusha juzi.
Mwandishi wa habari hizi, alishuhudia
baadhi wakiwapa watoto wa mitaani Sh 500 hadi Sh 1,000 ili kuwasaidia
kuangalia kama simu, pochi na vitambulisho vyao kama vipo; wengine
walivipata lakini wengine hawakuambulia kitu.
Imeandikwa na Veronica Mheta, Gloria Tesha, Shadrack Sagati na Prisca Libaga
Mizengo Pinda, Nasema wapigwe tu!!!!!
Mizengo Pinda, Nasema wapigwe tu!!!!!
Dodoma/Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Mizengo
Pinda ameagiza vyombo vya dola kuwashughulikia kwa kuwapiga wale
watakaokataa kutii amri wakati wakifanya vitendo vya uvunjifu wa amani.
Akizungumza katika Kipindi cha Maswali ya Papo kwa
Hapo kwa Waziri Mkuu, bungeni Dodoma jana, Pinda alisema watu
wanapokaidi wanajitakia matatizo na vyombo vya dola.
Alisema hayo alipokuwa akijibu swali la nyongeza
la Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu aliyeuliza:
“Serikali ipo tayari kiasi gani kubainisha na kuchukua hatua stahiki,
badala ya kusakama makundi fulani, tujue chanzo halisi cha vurugu hizi
na matatizo haya na jinsi gani vyombo vya dola vinavyoshughulikia kwa
sababu yapo malalamiko katika baadhi ya maeneo kama Mtwara kwamba
wananchi wanapigwa na vyombo vya dola?”
Waziri Mkuu alijibu: “Ni lilelile nililosema...
mwishowe unaona anasema vyombo vya dola vinapiga watu. Ukifanya fujo,
umeambiwa usifanye hiki, ukaamua kukaidi, utapigwa tu... hamna namna
nyingine, maana wote tukubaliane kwamba nchi hii tunaiendesha kwa
misingi ya kisheria.
“Sasa kama wewe umekaidi, hutaki unaona kwamba ni
imara zaidi... wewe ndiyo jeuri zaidi watakupiga tu.... Mimi nasema
muwapige tu, kwa sababu hakuna namna nyingine... maana tumechoka.”
Pinda alisema Serikali imedhamiria kurejesha amani
nchini ikiwamo mkoani Mtwara na kuwataka Watanzania waiache Serikali
ifanye kazi hiyo. Alisema Serikali ina orodha ya watu wanaosemekana kuwa
ni vyanzo vya vurugu na matatizo yaliyotokea Mtwara na kushangaa wale
wanaopinga kukamatwa kwao.
“Lazima tuwakamate na kama katika kuwakamata
watafanya jeuri, jeuri, watapigwa tu kabla ya kupelekwa tunapotakiwa
kuwapeleka, kwa sababu hatuwezi kuendelea na hali hii, mkadhani kwamba
tutafika tunapokwenda. Nami nasema vyombo vya dola vijipange imara
vihakikishe vinadhibiti hali hii,” alisema.
Hata hivyo, jibu hilo lilipata upinzani wakati
Mbunge wa Konde (CUF), Khatibu Said Haji alipomwuliza Waziri Mkuu: “Hapo
awali umetoa kauli nzito ya kuliambia taifa hili kwamba wale raia wote,
ambao watakaokuwa wakaidi wapigwe tu na watapigwa tu; naomba ninukuu
Katika Ibara ya 13 na Kifungu cha 6B cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
“Ni marufuku kwa mtu yeyote aliyeshtakiwa kwa kosa
la jinai kuteswa kama mtu mwenye kosa, mpaka itakapothibitika anayo
hatia kwa kutenda kosa hilo.
“Pia ibara hiyohiyo Kifungu cha 6 E; kinasema ni
marufuku kwa mtu yoyote, kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu
zinazoweza kumdhalilisha. Kwa kauli yako uliyoitoa huoni kwamba umevunja
Katiba?” Akijibu swali hilo, Pinda alisema ni lazima kutofautisha kati
ya mtu aliyekwishakamatwa na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria...
“Mimi ninayemzungumza hapa ni mtu yule ambaye ameamua kufanya vitendo
hajakamatwa na ndiyo maana nilikwambia usiandamane... hapa mahali
hutakiwi kwenda wewe ukaamua kutumia mabavu kwa sababu mko wengi, ndiyo
maana nikasema, hawa watu tutashughulika nao hivyohivyo.”
Mbunge huyo hakuridhishwa na majibu hayo na kumtaka Waziri Mkuu kuyafuta.
Hata hivyo, Spika wa Bunge, Anne Makinda
aliingilia katika na kumweleza mbunge huyo kuwa kila mtu alikuwa
amemwelewa Waziri Mkuu na hakukuwa na haja ya kuendelea na hoja hiyo.
Kabla ya swali lake la nyongeza, Mangungu aliuliza: “Ukisikiliza
nyimbo nyingi za taifa katika Afrika zinasema hekima, umoja na amani
ndiyo ngao zetu. Je, hali ambayo imejitokeza katika nchi yetu na
matatizo yaliyojitokeza Arusha na maeneo mengine kama Mtwara. Nini tamko
la Serikali?
Waziri Mkuu alijibu: “Swali lililoulizwa na
Mheshimiwa Mangungu ni jambo linalotugusa sisi wote. Suala la amani,
ulinzi, utulivu ndiyo hasa tunu ya kila nchi ingependa kuwa nayo. Ni
kweli hivi karibuni kumejitokeza vurugu za hapa na pale kwa hiyo
angependa tuwaeleze Watanzania kama Serikali tunafikiria tufanye nini.
Alisema ipo haja ya jukumu hilo kuachwa kwa
viongozi wa kisiasa bila ya kujali itikadi zao... “Yako mambo ambayo
lazima tukubali kwamba ni jukumu letu sisi wote na kila mmoja lazima
azungumze lugha moja.
Ninyi wote ni mashahidi. Chadema waliposhinda
hapa, wao walikuja waziwazi, wakasema tutahakikisha nchi hii
haitawaliki. Sasa, inawezekana pengine ndiyo mwendelezo wa utekelezaji
wa kauli hizo.
“La pili ni upande wa Serikali, lazima tuhakikishe
kwamba wale wote ambao kwa kweli wanajaribu kuvunja amani kwa namna
yoyote ile, kazi kubwa tuliyonayo ni kubanana, kupambana kwelikweli kwa
njia zozote zile zinazoonekana zinastahili.
“Sasa mimi ninaomba sana Watanzania, maana kila
juhudi zinapoonekana zinaelekea huko, unapata watu wengine wanajitokeza,
unajua...unajua. Acheni Serikali itimize wajibu wake kwa sababu jambo
hili ni la msingi, lazima tulilinde kwa nguvu zetu zote.
“Rai yangu kwa Watanzania kila mmoja ajue kwamba
siku tukiingia katika vurugu, hakuna mshindi. Wote tutaumia, sasa wote
tuhakikishe hili jambo tunalisimamia vizuri.”
Chadema waja juu
Akizungumzia kauli hiyo, Mkurugenzi Habari na
Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema: “Kauli ya Pinda inakiuka Katiba
ya nchi na imethibitisha kwamba matumizi mabaya ya vyombo vya dola na
kusababisha mauaji ya raia yana baraka za Serikali.”
Alisema kauli ya Pinda kama ilivyokuwa ya Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi
zinatoa mwelekeo kwamba mauaji ya Arusha yana baraka za Serikali.
Wanasheria wakerwa
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za
Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema Waziri Mkuu hakustahili
kutoa kauli kama hiyo.
Alisema Pinda hapaswi kuwa na jazba, bali anatakiwa kuwa na
busara na kuzungumza kwa kuzingatia sheria za nchi badala ya kutoa
matamshi ambayo siyo mwafaka kwa nchi inayoongozwa kwa kufuata sheria na
taratibu.
Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS),
Francis Stola alisema kauli hiyo ya Waziri Mkuu, mbali ya kwenda kinyume
cha Katiba na sheria ya nchi, inaweza kuhatarisha amani.
Stola alisema matumizi ya nguvu kupita kiasi kudhibiti hali yoyote korofi hayaruhusiwi.
Bongo Star Search kusajili zaidi 50,000
Kampuni ya simu za mikononi ya Zantel, imezindua msimu mpya wa
shindano la kuimba la Epiq Bongo Star Search, mwaka huu ikiwa imejipanga
kuwapa vijana wengi zaidi fursa ya kuonyesha na kuendeleza vipaji vyao.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Benchmark
Production, Rita Paulsen msimu huu wa saba toka shindano hilo lianzishwe
mwaka 2006, kuna vitu vingi vipya ikiwamo ongezeko la jaji mmoja ambaye
ni mdau wa muziki kutoka mkoa husika.
Naye Afisa Biashara mkuu wa Zantel, Sajid Khan
alisema uzinduzi huo ni furaha kwa kampuni hiyo kwani unaashiria
ufunguzi wa milango ya kuwasaidia vijana wengi wa Kitanzania kutimiza
ndoto zao.
“Mwaka jana pekee Epiq BSS ilifanikiwa kusaili
vijana zaidi ya elfu hamsini, jambo ambalo linaloonyesha kuna uhitaji wa
kuwekeza zaidi katika kuwaendeleza vijana’ alisema Khan.
Katika kuwapa fursa vijana ambao hawatafikiwa na
majaji, Zantel kwa kushirikiana na Push Mobile watafungua laini za
kurekodi kwa simu.
No comments:
Post a Comment