Hata hivyo, Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk
Florence Turuka alisema siyo sahihi kusema kwamba Waziri Mkuu amevunja
sheria kwani ilikuwa ni lazima serikali ichukue hatua jumuishi kwa
kuwashirikisha wadau husika.
“Siyo sahihi kusema kuwa tunataka kuvunja sheria, sisi tumepokea
mapendekezo na tutayaangalia kabla ya kutoa ripoti. Wewe vuta subira
tu,” alisema Dk Turuka.
Dk Turuka alisema kamati iliyoundwa na Serikali
ikiwajumuisha wadau mbalimbali wa barabara ilikamilisha kazi yake
Desemba mwaka jana na kwamba hivi sasa Serikali inatafakari mapendekezo
yaliyotolewa.
“Kamati ilishamaliza kazi tangu Desemba mwaka
jana… tulipokea mapendekezo kwa sababu ile ilikuwa kamati jumuishi,
kulikuwa na watu wa Tatoa, Taboa na Wizara ya Ujenzi na wataalamu, na
sasa tunayafanyia kazi,” alisema Dk Turuka.
Baadhi ya barabara ambazo zilikuwa katika hali
nzuri hivi sasa zimeharibika vibaya chanzo kikiwa ni uzito wa magari ya
mizigo. Miongoni mwa hizo ni Barabara Kuu ya Morogoro - Dodoma kati ya
Kijiji cha Magubike na Mji wa Gairo pamoja na Barabara ya Dar es Salaam
ya Morogoro eneo la kati ya Mlandizi na Chalinze.
Hali hii ndiyo iliyomsukuma Waziri wa Ujenzi, Dk
John Magufuli kufuta waraka unaoruhusu magari ya mizigo kuzidisha uzito
na badala yake kutaka sheria inayotaka malori yanayozidisha uzito uliopo
ndani ya asilimia tano kupunguza mzigo, kupanga mzigo upya au kulipia
uzito uliozidi mara nne ya tozo ya kawaida, ifuatwe.
Uamuzi wa Dk Magufuli ulipingwa na wamiliki wa
magari makubwa ya mizigo na kuungwa mkono na wamiliki wa mabasi ya
abiria, hivyo Waziri Mkuu Pinda aliingilia kati na kuamuru utaratibu wa
awali uendelee, ilhali suala hilo likiwa linatafutiwa ufumbuzi wa
kudumu.
Hata hivyo, Pinda alitangaza uamuzi wa kusitishwa
kwa utekelezaji wa amri ya Dk Magufuli katika mkutano ambao hata hivyo
waziri huyo wa sekta husika hakuhudhuria. Wakati huo kulikuwa na tishio
la kusitishwa kwa usafirishaji nchi nzima kama amri hiyo
isingetenguliwa.
Chanzo cha habari ndani ya Wakala wa Barabara
Tanzania (Tanroads) kinasema: “Tatizo kuna viongozi wengi wenye malori
na mabasi ndiyo wanaokwaza utekelezaji wa sheria hiyo.”
Kiliongeza: “Utakuta mtu ana magari hadi 300 na
yote yanazidisha uzito kwenye barabara kwa kisingizio cha kusamehewa
asilimia tano, unadhani barabara zetu zitaishia wapi? Ndiyo maana Dk
Magufuli kwa uchungu aliamua kuweka msimamo”.
Takwimu za upimaji wa magari ambazo ziko kwenye
tovuti ya wakala huyo wa barabara nchini zinaonyesha kuwa licha ya
kuwepo nafuu katika sheria bado magari mengi yamekuwa yakizidisha uzito.
Mathalan 2011/12 magari 684,600 yalipimwa na kati
ya hayo, 167,310 sawa na asilimia 24.44 yalikutwa yakiwa yamezidisha
mizigo, huku mengine 8,856 sawa na asilimia 1.30 yalipitisha kiwango cha
asilimia tano.
Hata hivyo, inaelezwa katika taarifa hiyo kuwa, asilimia 98.67
ya magari yanayozidisha mizigo huwa katika kiwango cha uvumilivu wa
asilimia tano, hali inayoonyesha kuwa ama wanahamisha mizigo au upangaji
mbaya wa mzigo ule ule katika gari.
Kwa mwaka 2011/ 2012, Tanroads ilitoza fani ya
Sh865,408,344.20 ambapo Sh859,508,181.40 zilikusanywa. Kwa mwaka 2013,
magari 3,060,057 yalipimwa na kati ya hayo, 790,777 sawa na asilimia
25.84 yakiwa yamezidisha mizigo. Asilimia 1.62 yalikuwa ndani ya mstari
wa asilimia tano na kwa jumla adhabu ya Sh5,490,255,235 ilikusanywa.
Wadau wa usafirishaji
Mkurugenzi wa Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania
(Tatoa), Zacharia Hanspope alitetea mgomo wao huku akimtaka mwandishi
amtafute msemaji wao kwa maelezo zaidi. Hata hivyo, alipotafutwa msemaji
huyo, Elias Lukumay hakutaka kuzungumzia kwa undani suala hilo akisema
kuwa bado wako kwenye vikao na Serikali.
“Nisingependa kuzungumzia suala hilo kwa kuwa kwa sasa kuna vikao vinaendelea. Tutawajulisha tu,” alisema Lukumay.
Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (Taboa),
Mustafa Mwalongo alisema kwa sasa wanaendelea na vikao na Serikali,
lakini bado msimamo wao ni kutokubali kupima mabasi kwenye mizani.
“Tunaye mwakilishi wetu kwenye vikao na Serikali.
Unajua kuna kamati iliyoundwa na Wizara ya Ujenzi na nyingine iliundwa
na Waziri Mkuu,” alisema Mwalongo na kuongeza:
“Tumekuwa tukipinga hatua hiyo kwa muda mrefu.
Mwaka 2004 tulipeleka madai serikalini na 2005 wakati Rais Jakaya
Kikwete anaingia madarakani alitoa tamko la kutusitishia upimaji, lakini
Wizara ya Ujenzi haitaki,” alisisitiza Mwalongo.
Sheria ilipindishwaje?
Ruhusa inayovunja sheria hiyo, ilitolewa na
aliyekuwa Waziri wa Miundombinu, Basil Mramba 2006, hatua ambayo
iliwaudhi wafadhili kutoka Norway.
Katika barua yake aliyomwandikia Mwenyekiti wa Tatoa) wakati huo, S.A
Seif, Julai 19, 2006 kujibu maombi yao, Waziri Mramba aliagiza kuwa
gari lisionekane kuwa limezidisha uzito hata kama unazidi kiwango cha
asilimia tano iliyowekwa na sheria hiyo.
“Kwa hiyo nimeamua kwamba, ekseli haitahesabika
kuwa imezidisha kama mzigo huo utakuwa umepita kiwango cha kisheria
baada ya kutoa asilimia tano cha uvumilivu wa kusoma mzani na baada ya
kushuka hadi kilo 100,” imesema sehemu ya barua hiyo iliyosainiwa na
Mramba ambayo gazeti hili limeiona..
Hata hivyo, barua hiyo ilipelekwa tu kama nakala Tanroads jambo
linalodaiwa kumkera mkurugenzi wake. “Ofisa Mtendaji Mkuu wa Tanroads
wakati huo, Ado Abeid alitaka sheria hiyo irudishwe kama ilivyokuwa,
lakini Waziri Mramba alikataa,” kinasema chanzo cha habari.
Hatua hiyo ya kupindisha sheria inaelezwa kuwakera wafadhili wa barabara kutoka Norway, Kampuni ya Asborn Norwegian Public Roads Administration iliyokuwa ikishauri kuhusu udhibiti wa uzito na hivyo kujitoa tangu mwaka 2006 kwa kutoridhishwa na hatua hiyo.
Sehemu ya barua hiyo ya Novemba 18, 2006,
inasomeka: “Baadhi ya vipengele vilivyomo katika barua vinahusika na
vinatakiwa kufuatwa kama hatua muhimu za kuimarisha utendaji wa mizani,
kanuni na vitendea kazi.
“Hata hivyo, barua yako pia imezungumzia mambo ya
kufanya kuhusu udhibiti wa mzigo katika ekseli ambapo baadhi ya
vipengele vimeachwa. Hali hii itaathiri udhibiti kwa ujumla na
kusababisha vurugu na uharibifu utakaoathiri utendaji.”
Kwa mujibu wa chanzo hicho, baada ya barua hiyo na
kutokuwepo kwa dalili ya kurekebisha sheria hiyo, tangu wakati huo
kampuni hiyo ilijitoa kusaidia miradi ya barabara nchini.
Hata hivyo, uamuzi wa Mramba uliopata utetezi wa
Pinda alipokuwa akitengua amri ya Dk Magufuli akisema ilitokana na
malalamiko ya wadau.
“Lengo lake
ilikuwa ni kufidia matatizo ya upungufu wa mizani kutoweza kupima kwa
usahihi uzito wa magari yanayopimwa katika vituo mbalimbali vya mizani
nchini, lakini hivi sasa mizani yetu ni mizuri na ya kisasa,” alisema
Pinda na kuongeza:
“Lakini ikumbukwe kuwa agizo hilo lilikuwa kinyume
na Sheria ya Usalama Barabarani sura ya 168 toleo la 2002 na kanuni
zake za 2001, ambayo inazuia malori kuzidisha uzito. Mramba aliamua vile
ili kumaliza hali iliyokuwa imejitokeza wakati akiwa Wizara ya
Miundombinu”.
Chanzo kinaendelea kufafanua kuwa, baada ya Mramba
kuondoka katika wizara hiyo mwaka 2007, wizara hiyo pia iliongozwa na
mawaziri, Andrew Chenge na Dk Shukuru Kawambwa ambao pia hawakuwahi kuifanyika kazi sheria hiyo.
Matakwa ya sheria
Sheria Na. 30 ya 1973 na kanuni Namba 30 ya 2001
iliyotangazwa kwenye Gazeti la Serikali tangazo Namba 30 la Februari 9,
2001 ilianza kutumika Januari 24, 2001 inafafanua uzito wa magari
unaotakiwa.
Kipengele cha saba cha sheria hiyo kinaeleza
magari yote yenye uzito kuanzia tani 3.5 na kuendelea na aina ya makosa
ya uzidishaji uzito, ambapo kifungu cha 2, 3, 4 vinafafanua matumizi ya
uzito uliozidi asilimia tano.
Vifungu vya sheria hiyo vinasomeka ifuatavyo:
2. Kwa sababu ya usambazaji wa mzigo kwenye gari,
ekseli au fungu la ekseli litahesabika kuwa limezidi uzito kama mzigo
utazidi ukomo wa uzito unaoruhusiwa kisheria baada ya kuongeza asilimia
tano (5) ya uzito unaoruhusiwa, na kisha kuiweka hesabu ya mwisho
isomeke kwa wastani wa kilo mia moja za karibu.
3. Kwa kila ekseli yaweza kusafirisha kama ziada
ya uzito kiasi cha asilimia tano (5) ya uzito unaoruhusiwa. Hata hivyo,
kama mzigo wenye uzito wa ziada hautapakuliwa, tozo kwa uzito huo wa
ziada itakuwa mara nne zaidi ya tozo ya kawaida inayolipwa kwa uzito uliozidi.
Mzigo wote wenye uzito unaozidi asilimia tano (5)
utapakuliwa na kupakiwa kwenye gari jingine isipokuwa tu kama kibali
maalum kimetolewa.”
4. Kama gari limethibitishwa kwamba limebeba uzito zaidi ya ule unaoruhusiwa gari hilo halitaruhusiwa kuendelea na safari mpaka hapo mzigo uliozidi utakapohamishiwa kwenye gari lingine au kupangwa upya ili kila ekseli iwe na uzito unaotakiwa.
“Baada ya kushusha au kupagwa upya gari lazima
lipimwe upya tena kuhakikisha kuwa mzigo uliobebwa upo kwenye viwango
vinavyokubalika.”