Asema umehodhiwa na wanasiasa na kutahadharisha usipoangaliwa unaweza kuzaa machafuko.
Dodoma. Mwanazuoni na
Mwanasheria nguli, Profesa Issa Shivji ameuponda mchakato wa Katiba
Mpya kuwa umehodhiwa na wanasiasa na kutahadharisha kuwa usipoangaliwa
vizuri unaweza kusababisha machafuko.
Aliyasema hayo jana mjini hapa alipokuwa akitoa
mhadhara kwa Jumuiya ya Chuo Kikuu cha Dodoma, (Udom). Mhadhara huo
uliandaliwa kama sehemu ya mafunzo kwa ajili ya wanafunzi wanaojiandaa
kuhitimu masomo yao (Convocation ).
Profesa Shiviji ambaye alitumia saa 1.15 kutoa
mhadhara wake juu ya mchakato wa Katiba, alisema Bunge la Katiba lipo
juu ya Bunge la Kawaida.
Alisema katika historia ya Tanzania imewahi kuwa
na mabunge mawili yaliyoandaliwa kupata Katiba, lakini yote hayakuwa na
wabunge waliochaguliwa.
“Tukiangalia katika historia hatukuwahi kuwa na
Bunge la Katiba ambalo lilichaguliwa na wananchi. Safari hii tulikuwa na
nafasi ya kuwa na Bunge ambalo lilichaguliwa na wananchi lakini kwa
bahati mbaya hakuna nafasi ya kufanya hivyo ,”alisema.
Kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba,
wabunge wote 357 na Wawakilishi 81 watakuwa ni wabunge wa Bunge Maalumu
la Katiba huku mashirika yasiyo ya kiserikali yakipewa wawakilishi 20.
Wajumbe wengine ni vyama vya siasa vyenye usajili
wa kudumu 42, wawakilishi wa taasisi za elimu ya Juu 20, watu wenye
mahitaji maalumu (20), vyama vya wafanyakazi (20), wafugaji (10), wavuvi
(10), wakulima (20) na makundi mengine yenye mahitaji muhimu ni
wawakilishi (20).
Profesa Shivji alisema Bunge la Katiba litakuwa
na jumla ya wabunge 639, ambapo 438 asilimia 69 ya wabunge wa Bunge
hilo wanatokana na vyama vya siasa.
Alisema kati ya wabunge hao kutoka vyama vya siasa asilimia 52 ni Wana-CCM na asilimia 16 ni kutoka vyama vya upinzani.
“Katika wajumbe 42 watatokana na vyama vya
kisiasa, kwa hivi itafanya jumla ya wabunge la Katiba ambao watatokana
na vyama vya siasa kuwa ni asilimia 75;
“Kama hesabu zangu ni sahihi ama zinakaribia
wabunge wanaotokana na CCM watakuwa ni asilimia 63, wapinzani asilimia
27 na wasiokuwa na chama ni asilimia 10,”alisema.
Alisema kwa kuangalia idadi ya wajumbe wanaotokana na mashirika
yasiyo ya kiserikali wana uwiano sawa na wawakilishi wa mashirika ya
wavuja jasho yaani wakulima, wavuvi, wafugaji na wanazuoni.
Alihoji mashirika yasiyo ya kiserikali
yanawawakilisha kina nani katika Bunge hilo na mashirika hayo bila ya
aibu yamejigeuza kuwawakilisha wananchi wakati hiyo siyo sahihi kwa kuwa
hawahusiki na wananchi moja kwa moja.
“NGO’s zina nafasi ya wawakishi sawa, lakini si
wawakilishi wa wananchi hawakuchaguliwa na wananchi, wala hawawajibiki
kwa wananchi hali halisi wanawajibika zaidi kwa wafadhili, katika
sheria hii NGOs ndio wamepewa kipaumbele kana kwamba ni sawa na
wananchi,” alisema Shivji na kushangiliwa.
Kwa upande wa kura ya maoni, Profesa Shivji
alikikosoa kipengele katika sheria ya kura ya maoni ambayo inatarajiwa
kuletwa Bungeni katika mkutano wa 14 wa Bunge.
Alisema katika sheria hiyo inataka ili jambo likubaliwe ni lazima lipate kura za ndiyo asilimia 50 kwa kila upande muungano.
Alisema hilo litafanya watu wachache waamue kwa ajili ya walio wengi.
Alifafanua kuwa kwa mujibu wa sheria hiyo asilimia
50 inayotakiwa ni ya kura halali na wala si inayotokana na idadi ya
wapiga kura waliopo kisheria katika Bunge hilo.
Aidha, Profesa Shivji aliwataka wasomi wanapoona mambo yanaharibika kusema badala ya kusubiria mambo yaharibike ndipo waseme.
Alisema mchakato mrefu katika kupata Katiba ni muhimu sana na hautakiwi kuharakishwa.
“Jambo hili linatakiwa kuwa na muda wa kutosha
badala ya kuweka ratiba ya miezi, miaka, unatoa mwanya kwa matapeli wa
kisiasa kupenyeza na wanaweza kuleta vurugu kubwa sana,”alisema.
Alisema suala la kuwapa wataalamu kuandika Katiba bila ya kuwa na sheria ni kuwapa nafasi wanasiasa kuuvuruga.