Saturday 29 August 2015

Lowassa: Wanawake nguzo ya mabadiliko

 
 
Mke wa Mgombea wa Urais wa Chadema, Mama Regina Lowassa akiwasalimia wanawake  walioshindwa kuingia katika ukumbi uliopo katika Jengo LAPF Kijitonyama baada ya ukumbi huo kufurika, wakati wa mkutano wa Mgombea Urais, Edward Lowassa alipokuwa akizungumza na wanawake wa Dar es Salaam, jana. Picha na Edwin Mjwahuzi
Dar es Salaam. Mgombea urais wa Ukawa, Edward Lowassa amesema mabadiliko katika Taifa hili ni jambo la lazima na linalohitaji nguvu ya wanawake ili kulifanikisha kwa maendeleo ya Watanzania wote.
Lowassa alisema hayo jana kwenye mkutano wa uzinduzi wa kampeni za wanawake, ulioandaliwa na Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha) na kutumia nafasi hiyo kuomba kura kwa wanawake na kuwataka wamtafutie kura kwa watu wengine.
Alisema anaamini kuwa wanawake katika umoja wao, ndiyo nguzo kubwa ya mabadiliko na wakiamua kufanya hivyo hakuna wa kupinga. Alisema wanawake wanakabiliwa na shida mbalimbali ambazo zinahitaji mabadiliko ya kimfumo.
“Nimekuwa mbunge kwa zaidi ya miaka 30, nina uzoefu kwamba mwanamke akisema anakupa kura anakupa kweli. Wanawake mtanipa kura zenu?” Lowassa aliwauliza wanawake waliohudhuria kwenye mkutano huo nao kwa pamoja walijibu “umepataaa”
Alisema anakusudia kuleta maendeleo kwa kasi kubwa ambayo hakuna anayeweza kufikia akitaka ifike mahali Watanzania waache woga wa kutafuta mabadiliko ya kweli.
Lowassa aliwataka wanachama wengine wa CCM kujiunga na upinzani kwa madai kwamba ndiko yalipo mabadiliko ya kweli. Aliendelea kunukuu kauli ya Mwalimu Julius Nyerere aliyowahi kuisema mwaka 1995, kwamba: “Wananchi wanataka mabadiliko, wasipoyapata ndani ya CCM watayatafuta nje ya CCM.”
Aliongeza: “Hawa wenzangu wa CCM waje Ukawa. Huku hakuna noma, waje tu wajiunge na gurudumu la mabadiliko,” alisema Lowassa huku akishangiliwa na wanawake waliohudhuria katika mkutano huo.
Awali, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alizindua salamu mpya itakayotumika katika kampeni zake nchi nzima. Alisema salamu hiyo inaambatana na ishara ya kuzungusha mikono kumaanisha mabadiliko.
“Lowassa amekuwa chachu ya mabadiliko nchini na ametuunganisha wote licha ya tofauti zetu, sasa napendekeza salamu mpya tutakayoitumia kwenye kampeni, nikisema Lowassa, mnazungusha mikono yenu kumaanisha mabadiliko,” Mbowe alielekeza na salamu hiyo ilianza kutumika papo hapo.
Alisema katika utafiti wake, amebaini kuwa wanawake wengi wamekuwa hawafiki kwenye mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa kwa sababu ya kusukumwa, kukanyagwa na kudhalilishwa kijinsia, hali aliyosema sasa itabadilishwa.
Alisema kuanzia sasa watatenga maeneo maalumu ya kukaa wanawake kwenye mikutano yao yote ya hadhara kuanzia siku ya uzinduzi wa kampeni zao kesho katika Viwanja vya Jangwani.
“Kuja kwa Lowassa ni mpango wa Mungu. Alitoka alikotoka na kuja kuwaunganisha wanawake, wasichana, wanaume na vijana nchi nzima. Hatuna budi kumuunga mkono ili atuletee mabadiliko tunayoyahitaji,” alisema Mbowe.
Regina Lowassa alonga
Mke wa mgombea urais wa Ukawa, Regina Lowassa ambaye hotuba yake ilikuwa ikikatishwa mara kwa mara na shangwe za wanawake, alitumia muda huo kuwaombea kura wagombea urais wa Tanzania Bara na Zanzibar.
Mama Lowassa alibainisha changamoto mbalimbali zinazowakabili wanawake nchini ikiwamo mfumo mbaya wa elimu ambao haumuandai mwanafunzi kujitegemea na kukosekana kwa huduma bora za afya kwa wajawazito.
Alisema Tanzania bado iko nyuma kiuchumi kwa sababu Serikali imeshindwa kutengeneza mazingira wezeshi kwa wanawake ili wanufaike na rasilimali zilizopo.
Mwenyekiti wa NCCR – Mageuzi, James Mbatia alisema wanawake ni wengi wana nguvu kubwa ya kuamua nani awe rais, hivyo kuwataka kumpa kura mgombea wa Ukawa ili akalijenge Taifa.
Ilivyokuwa
Licha ya ratiba ya mkutano huo kuonyesha ungeanza saa 8.00 mchana, wanawake wengi walifika kuanza saa tano asubuhi na kutumia muda mwingi kuimba nyimbo za kumsifu Lowassa nje ya Jengo la LAPF.
Baadhi ya watu walisikika wakiimba; “Kama siyo Kikwete, Lowassa tungempata wapi?” huku wengine wakisema “CCM siyo chama, kingekuwa chama Lowassa asingehama.”
Ilipofika saa nane mchana, idadi ya watu iliongezeka kiasi kwamba walinzi waliokuwa wakilinda lango la kuingilia ukumbini walilazimika kutumia nguvu ya ziada kuwazuia waliokuwa wanataka kuingia ndani.
Kutokana na idadi ya watu kuendelea kuongezeka, ilimbidi mshereheshaji kuomba vijana wa ulinzi wa Red Brigade kusaidia kuwazuia watu waliokuwa wanataka kuingia ndani wakati ukumbi umeshajaa.
Walinzi walilazimika kufunga milango na kutangaza kuwa Lowassa na viongozi alioambatana nao watazungumza na watu walio nje ya ukumbi kwanza, ndipo waingie ndani ili wote wasikie anataka kuwaambia nini.
Hata baada ya kuzungumza nao, wafuasi hao wa Ukawa waliendelea kufuatilia mkutano huo kupitia televisheni zilizofungwa nje ya ukumbi huo.
Waimbaji wa nyimbo za injili, Bahati Bukuku na Jeni Miso, walikuwa kivutio kwa wafuasi hao kutokana na nyimbo walizoiimba za kutaka mabadiliko huku msanii wa filamu Jackline Wolper akimzawadia Lowassa keki ya siku ya kuzaliwa. Lowassa alizaliwa Agosti 26, 1953.
Wanachama walonga
Mkazi Kitunda, Magdalena William (41) alisema amefika eneo la kongamano kuanzia saa 2.30 asubuhi ili asikose nafasi ya kuona kila kinachofanywa na kuamuliwa kwa ajili yao.
Zakia Haule (37), mkazi wa Magomeni, alisema hakuenda kwenye shughuli zake ili kuungana na wenzake kuleta mabadiliko kwa pamoja. Akiwa mwenye furaha na kujiamini, alisema amejipanga kuipigia kura Ukawa.
Mkazi wa Tabata, Siwatu Mussa (42) aliyefika saa nane mchana na kushindwa kuingia ukumbini alisema: “Nitakaa hadi nimuone anatoka, najipanga kwa ajili ya Jangwani naona nitakuwa wa kwanza, siku hiyo sitaki kupitwa na kitu.”
Tofauti na inavyokuwa watu wanapoingia mpirani, zinapobaki dakika nne au tano kuanza kuondoka, jana hakuna aliyefanya hivyo hadi Lowassa alipomaliza kuzungumza.
Imeandikwa na Peter Elias, Goodluck Eliona na Kalunde Jamal

Ukawa waanza kazi Jangwani leo

“Tutakuwa live (kusikika na kuonekana moja kwa moja kutoka Jangwani) katika redio nne na televisheni nne. Hatuwezi kutaja ni redio gani, lakini wananchi wawe makini na kuzingatia uwezekano wa wao kupata matangazo hayo kuanzia saa 9:00 alasiri mpaka saa 12:00 jioni,” Tumaini Makene.
Dar es Salaam. Mgombea urais wa Chadema na Ukawa, Edward Lowassa, ambaye leo atazindua kampeni zake kwenye viwanja vya Jangwani, jana aliamua kufunguka dhidi ya vitendo vya Jeshi la Polisi kupiga wananchi, akisema havikubaliki kwa kuwa vifaa vinavyotumika vinanunuliwa na kodi wanazokatwa.
Lowassa, ambaye anagombea urais chini ya mwavuli wa vyama vinne-Chadema, NLD, CUF na NCCR-Mageuzi, anazindua kampeni hizo baada ya kukabiliana na vizingiti kadhaa vilivyowekwa na taasisi za Serikali kuanzia wakati anatafuta wadhamini hadi sakata la kibali cha kutumia eneo hilo leo.
Akizungumza jana wakati wa majumuisho ya ziara zake fupi za jijini Dar es Salaam ambazo pia zilikatishwa na mazuio kutoka Jeshi la Polisi na Wizara ya Afya, Lowassa alisema vitendo hivyo vinaweza kuifanya Serikali ishtakiwe iwapo kutatokea vurugu. “Haiwezekani hela za walipakodi zitumike na polisi kupiga mabomu ya machozi. Tutawapeleka The Hague (Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Kihalifu),” alisema Lowassa wakati akiongea na makundi mbalimbali kwenye Hoteli ya Lamada jana.
Lowassa pia alisema kuna watu wanazusha kuwa akiingia madarakani atawafukuza Watanzania wenye asili ya Asia, jambo ambalo alisema si la kweli na hawezi kufanya hivyo kwa kuwa yeye si rais wa zamani wa Uganda, Idi Amini.
Katika makundi hayo, kulikuwa na wasanii zaidi ya 60 wa muziki wa kizazi kipya na waigizaji filamu, wengi wao wakiwa ni wale ambao hawajaonekana kwenye mikutano ya kisiasa tangu kuanza kwa harakati za uchaguzi.
Mkutano wa leo unafanyika baada ya Chadema kukataliwa na Serikali kutumia Uwanja wa Taifa, wenye uwezo wa kuchukua watu 60,000, na baadaye Ofisi ya Manispaa ya Wilaya ya Ilala kukatalia viwanja vya Jangwani kwa madai kuwa vilishakodiwa na CCM kwa siku tatu mfululizo kwa ajili ya matamasha ya wasanii.
Hata hivyo, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) iliingilia kati na chama hicho kikuu cha upinzani kuruhusiwa kutumia viwanja hivyo maarufu kwa michezo na mikutano mikubwa ya kidini na kisiasa.
Vyama vilivyo katika Ukawa vimepania kufanya mkutano mkubwa jijini Dar es Salaam kabla ya Lowassa kwenda Iringa kuanza rasmi kampeni za mikoani, na mgombea mwenza, Juma Haji Duni kuelekea Lindi na Mtwara.
“Tumekamilisha maandalizi kwa asilimia 90,” alisema Tumaini Makene, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano wa Chadema, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mkutano huo wa leo wa uzinduzi.
 “Tutakuwa live (kusikika na kuonekana moja kwa moja kutoka Jangwani) katika redio nne na televisheni nne. Hatuwezi kutaja ni redio gani, lakini wananchi wawe makini na kuzingatia uwezekano wa wao kupata matangazo hayo kuanzia saa 9:00 alasiri mpaka saa 12:00 jioni,” alisema Makene.
Alisema baada ya kumalizika kwa mkutano huo wa uzinduzi, Lowassa ataanza kampeni katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kwa kuanzia Mkoa wa Iringa ambako alikusanya wanachama wengi waliomdhamini wakati alipokuwa akiwania urais kwa tiketi ya CCM kabla ya kuhamia Chadema.
Lowassa anatarajiwa kutumia mkusanyiko wa leo kuanza kumwaga sera za chama hicho na Ukawa baada ya kushindwa kufanya hivyo kwenye mikutano ya awali kuepuka kukiuka sheria inayokataza kuanza kampeni mapema.
Katika taarifa yake ya jana, Jeshi la Polisi lilisema limejiandaa vizuri kuhakikisha kunakuwa na usalama kwenye viwanja hivyo na askari wake watalizunguka eneo hilo.
“Watu wanaruhusiwa kuja katika makundi madogo madogo kwa kutumia vyombo vya usafiri kama vile mabasi, magari madogo, pikipiki, watembea kwa miguu au baiskeli na si kusubiriana katika makundi makubwa yanayoashiria taswira ya maandamano,” inasema taarifa ya Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
Mkutano wa leo utahudhuriwa pia na Duni, ambaye amepitishwa kuwa mgombea mwenza wa Lowassa baada ya Chadema kufikia makubaliano maalumu ya yeye kuhamia chama hicho akitokea CUF chini ya mpango wa ushirikiano wa Ukawa wa kujiandaa kushika dola.
Wengine wanaotarajiwa kuhudhuria mkutano wa leo ni Seif Sharif Hamad, anayegombea urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CUF, Twaha Taslima (Kaimu Mwenyekiti wa CUF), Freeman Mbowe (Mwenyekiti wa Chadema), James Mbatia (Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi), na Emmanuel Makaidi (Mwenyekiti wa NLD). Mkutano wa leo umetanguliwa na matukio mengi ya kusigana baina ya Chadema na vyombo vya Serikali. Awali Chadema iliomba kufanyia mkutano huo kwenye Uwanja wa Taifa kutokana na idadi kubwa inayomfuata Lowassa kila aendako, lakini Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ilimkatalia kwa madai kuwa imeona kwa sasa uwanja huo ubakie kwa shughuli za kimichezo tu.
Baadaye Lowassa alifanya ziara fupi jijini Dar es Salaam, akianza kwa kupanda basi la daladala kutoka Gongo la Mboto hadi Chanika na siku iliyofuata alitembelea maeneo ya Tandale kabla ya Jeshi la Polisi kupiga marufuku safari zake likisema zinasababisha foleni zisizo na umuhimu kutokana na kuibuka kwa misafara kila anakokwenda.
Mbunge huyo wa Monduli pia alipanga kutembelea hospitali tatu za wilaya za Dar es Salaam, lakini Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii ikatangaza kuzuia ziara hizo, ikidai zingesumbua wagonjwa, kitu ambacho Chadema imekipinga ikitoa mfano wa mgombea mwenza wa CCM, Samia Suluhu kutembelea hospitali mjini Moshi bila ya kubughudhiwa na vyombo vya dola.
Wakati Chadema na Ukawa wakijiandaa kwa mkutano wa leo, Ofisa Utamaduni wa Wilaya ya Ilala aliwaambia waandishi wa habari kuwa chama hicho kisingeweza kutumia viwanja vya Jangwani kwa kuwa vimeshachukuliwa na CCM. Hata hivyo suala hilo lilimalizwa juzi. Kutokana na msigano huo, NEC imewaagiza wakurugenzi wote wa wilaya, ambao pia ni wakurugenzi wasaidizi wa uchaguzi kuhakikisha shughuli za kampeni zinapewa kipaumbele wakati huu wa kuelekea Uchaguzi Mkuu.
Juzi Chadema ilikwepa vikwazo hivyo vya Serikali baada ya kuandaa mkutano wa ndani na wanawake wa makundi mbalimbali jijini Dar es Salaam uliofanyika katika jengo la Millennium Towers ambao ulihudhuriwa na wanawake kutoka katika kila kada. Katika mkutano huo, Mbowe aliwaomba wakazi wa Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi leo kwenye viwanja vya Jangwani kumsikiliza mgombea wa urais wa Chadema (Ukawa).
“Tunaomba Watanzania waje kwa mamilioni sio kwa maelfu,” alisema Mbowe kwenye mkutano huo na kuwaahidi wanawake wote watakaofika Jangwani kuwa wataandaliwa eneo maalumu ambalo litakuwa na ulinzi ili kuwawezesha kufuatilia matukio bila usumbufu.
Mkutano huo unafanyika katika eneo hilo ikiwa ni siku sita tangu mgombea wa CCM, Dk John Magufuli kuzindua kampeni zake kwenye viwanja hivyo akiwa ameambatana na Rais Jakaya Kikwete, marais wa zamani, Benjamin Mkapa na Ali Hassan Mwinyi na makada wengine wa CCM.
19 wapata dhamana
Wakati kampeni za Chadema zikianza leo, wafuasi 19 wa chama hicho waliokuwa wakikabiliwa na mashtaka mawili ya kufanya mkusanyiko na maandamano wameachiwa huru baada ya kukamilisha masharti ya dhamana.
Wafuasi hao, ambao ni pamoja na wanafunzi na wafanyabiashara, walikaa Segerea kwa  siku tatu kutokana  na kushindwa kukamilisha masharti ya dhamana.

Sunday 23 August 2015

Treni ya Mwakyembe kurejea tena

Miezi kadhaa baada treni ya kubeba abiria jijini Dar es Salaam kusitisha safari zake kutokana na ubovu, imeelezwa kuwa hali hiyo ni kutokana na uchakavu wa injini.
Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Reli Tanzania, Charles Ndenge alisema treni hiyo imekuwa ikiharibika mara kwa mara, kutokana na injini zake kutumika kwa muda mrefu, huku treni hiyo ikifanya kazi tofauti na ilivyoundwa.
Elizabeth Edward
Dar es Salaam. Miezi kadhaa baada treni ya kubeba abiria jijini Dar es Salaam kusitisha safari zake kutokana na ubovu, imeelezwa kuwa hali hiyo ni kutokana na uchakavu wa injini.
Mkuu wa Masoko wa Kampuni ya Reli Tanzania, Charles Ndenge alisema treni hiyo imekuwa ikiharibika mara kwa mara, kutokana na injini zake kutumika kwa muda mrefu, huku treni hiyo ikifanya kazi tofauti na ilivyoundwa.
“Treni hii ilitengenezwa kwa safari za mbali, hata hivyo imeshafanya kazi kwa muda mrefu na injini zake zimechoka ndiyo maana zinafanyiwa marekebisho niwahakikishie watumiaji huduma ya usafiri itarejea kama kawaida” alisema Ndenge.
Alifafanua mpaka sasa matengenezo yamefika katika hatua nzuri na wiki mbili zijazo huduma hiyo itaanza kufanya kazi tena.
Ili kuepukana na adha ya kusitishwa kwa huduma hiyo mara kwa mara, Ndenga alisema kwamba kunahitajika treni iliyotengenezwa maalumu kwa ajili ya safari za mjini.
“Usafiri wa treni kwa safari fupi unaweza kuwa imara endapo kutakuwa na treni zilizotengenezwa maalumu kwa ajili ya kazi hiyo mikakati ambayo inaendelea, lakini hatuwezi kuizungumzia kwa sasa”alisema.
Aliweka wazi kwamba matengenezo ya injini hizo yanaendelea na wiki mbili zijazo huduma hiyo ya usafiri inaweza kurejea.
Kusitishwa kwa huduma hiyo ya usafiri kumeleta kero kubwa kwa wakazi wa Dar es Salaam, ambao wamekuwa wakitegemea njia kukabiliana na changamoto ya foleni hasa nyakati za asubuhi na jioni.
Wakizungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti, baadhi wa watumiaji wa usafiri huo walidai kuwa kukosekana kwa treni kumesababisha kuathirika kwa shughuli zao za kiuchumi kutokana na kutumia muda mwingi kwenye foleni.
“Treni ilikuwa inasaidia sana, lakini sasa hivi tunalazimika kupoteza muda mwingi kwenye foleni za daladala, hivyo tunaomba wahusika waliangalie suala hili kwa umakini zaidi usafiri wetu walala hoi urejee”alisema Erick Kivambala mkazi wa Ubungo Jasmine Ally mkazi wa Tabata alisema kukosekana kwa usafiri huo, kumeleta changamoto kubwa kwa wanafunzi ambao wamekuwa wakipata wakati mgumu kwenye daladaa kutokana na kusumbuliwa makondakta.
“Ingawa hata watu wazima tumeathirika lakini wanafunzi ndiyo wameathirika zaidi, maana treni ndiyo ilikuwa inawabeba bila matatizo yoyote, siku hizi unawakuta kwenye vituo vya daladala wakikunjana mashati na makondakta”alisema.
Kwa upande wake Ofisa Habari Mkuu Wizara ya Uchukuzi, William Budoya Ndenge alikiri kuwepo kwa kadhia hiyo na kueleza kuwa treni maalum kwa ajili ya safari za mjini zinahitajika kukabiliana na changamoto za usafiri katika maeneo hayo.
“Ili usafiri huu uwe wa uhakika ni lazima ziwepo treni ambazo zimetengenezwa maalum kwa ajili ya kutoa huduma za usafiri maeneo ya mijini,”alisema.
Kuhusiana na madai ya kuwepo kwa mvutano kati ya TRL na Wizara ya Uchukuzi katika suala la uendeshaji wa treni hiyo, Budoya alisema jambo hilo halina ukweli na wamekuwa wakishirikiana bega kwa bega kuhakikisha huduma hiyo inarejea.
“Sisi tunatunga sera na TRL ni waendeshaji tunatambua fika kwamba treni hili ni mkombozi kwa wakazi wengi wa Dar es Salaam, ndiyo maana tunaweka nguvu zote kuhakikisha linarejea”alisema Budoya

Unachopaswa kufanya siku ya uchaguzi



Dar es Salaam. Tanzania inaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu, Oktoba 25, mwaka huu. Baadhi ya wananchi hasa vijana waliofikisha miaka 18 hivi karibuni hawajawahi kushiriki kwenye uchaguzi wowote na uchaguzi huu ni wa kwanza kwao.

Saa 1: Wananchi wanatakiwa kufika vituoni kuanzia saa moja asubuhi wakiwa na vitambulisho vyao vya kupigia kura.
04:Jambo la nne, mwananchi akimaliza kupiga kura aende nyumbani kusubiri matokeo kutangazwa.
53:Kwa mujibu wa kifungu cha 53 cha Sheria ya Uchaguzi, wagombea urais na wagombea wenza wanayo haki ya kutumia vituo vya redio na televisheni vya Serikali wakati wa muda rasmi wa kampeni.
Peter Elias, Mwananchi
Dar es Salaam. Tanzania inaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu, Oktoba 25, mwaka huu. Baadhi ya wananchi hasa vijana waliofikisha miaka 18 hivi karibuni hawajawahi kushiriki kwenye uchaguzi wowote na uchaguzi huu ni wa kwanza kwao.
Vijana hawa na watu wengine, wanahitaji kujifunza au kukumbushwa juu ya mambo ya kufanya siku ya uchaguzi ili kufanya zoezi la upigaji kura kuwa lenye mafanikio na kuepusha uvunjifu wa sheria unaoweza kumweka mtu matatani.
Kwa bahati mbaya, elimu kwa mpigakura haitolewi mara kwa mara kwa wananchi mpaka nyakati za uchaguzi. Hata wakati huo ukifika, baadhi ya watu hasa wale wa hali ya chini, hawafikiwi na elimu hiyo.
Elimu kwa mpiga kura bado inahitajika ili kila mwananchi afahamu haki na wajibu wake katika mchakato mzima wa uchaguzi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ndiyo yenye jukumu la kutoa elimu hiyo kwa kushirikiana na wadau wengine.
Hata hivyo, zoezi hili linakabiliwa na changamoto ya uhaba wa rasilimali za kufanikisha utoaji wa elimu kwa wapigakura. Vilevile, hakuna chombo maalumu cha kuratibu na kusimamia utoaji wa elimu ya uraia.
Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva anasema changamoto kubwa wanayokabiliana nayo ni pamoja na uhaba wa Asasi za kiraia zinazotoa elimu kwa wapigakura na kuwafikia wananchi wote nchi nzima.
Jaji Lubuva anasema Tume imejipanga vizuri kuhakikisha kwamba elimu inawafikia wapigakura nchi nzima. Anasema watatumia vyombo vya habari vikiwamo vinavyomilikiwa na taasisi za dini ili kuwafikia wananchi haraka zaidi.
Zingatia haya siku ya uchaguzi
Mkurugenzi wa uchaguzi – Nec, Kailima Kombwey anafafanua mambo muhimu ambayo mpigakura anatakiwa kufanya siku ya uchaguzi bila kuathiri masharti ya sheria za uchaguzi na kanuni zake.
Wahi kituoni
Anasema jambo la kwanzana la msingi ni  kuwahi asubuhi katika kituo cha kupigia kura. Kombey anasema wananchi wanatakiwa kufika vituoni kuanzia saa moja asubuhi wakiwa na vitambulisho vyao vya kupigia kura.
Anasema kila mpigakura anatakiwa kujua kituo atakachopigia kura na kuhakiki kama jina lake lipo kwenye orodha ya wapigakura kwenye kituo husika.
Panga foleni
Kombey anabainisha kuwa watu watapanga foleni kuingia chumba cha kupigia kura na vituo vitafungwa kuanzia saa 10 jioni. Anasema watakaokuwa kwenye mstari baada ya muda huo wataruhusiwa kuendelea kupiga kura mpaka watakapomaliza.
“Tunasisitiza wananchi wajitokeze kwa wingi ili wawachague viongozi wao. Kupiga kura ni jambo la muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu. Wasipojitokeza basi wasilaumu kiongozi atakayechaguliwa na wengine,” alisema Kombwey.
Mkurugenzi huyo anasema katika uchaguzi wa mwaka 2010, waliandikisha watu milioni 20 lakini waliojitokeza kupiga kura walikuwa chini ya milioni 10. Kwa hiyo, anasisitiza zaidi kujitokeza kupiga kura siku hiyo.
Usivae sare za chama
Jambo la pili, mpigakura asivae nguo yenye nembo au alama yoyote ya chama cha siasa kwenye kituo cha kupigia kura. Kufanya hivyo ni kukiuka taratibu za uchaguzi na mtuhumiwa anaweza kushitakiwa kwa kuhujumu mchakato wa upigaji kura.
Kombey anafananisha jambo hilo na akufanya kampeni siku ya kupiga kura, jambo ni kinyume na kanuni. Kwa hiyo, fulana, kofia, bendera au kanga au nguo yoyote inayovaliwa na chama chochote haitakiwi kwenye eneo la kupigia kura.
“Tunatoa muda wa kampeni ili wanasiasa na vyama vyao wajinadi kadri wanavyotaka lakini siku ya uchaguzi siyo siku ya kufanya kampeni, ni kinyume cha kanuni za uchaguzi,” anasema mkurugenzi huyo.
Anaendelea kubainisha kuwa Tume kupitia kifungu cha 124 (a) cha sheria ya taifa ya uchaguzi ya mwaka 1985 ilianda maadili ya uchaguzi ambayo yamefanyiwa mabadiliko madogo mwaka huu na kukubaliwa na vyama vyote.
Wahusika wakuu katika maadili haya ni Tume ya Uchaguzi, Serikali, wagombea na wanachama wote wa vyama vya siasa. Kombwey anasema wadau hawa kwa pamoja wana wajibu wa kufanya uchaguzi huru na wa haki.
Usilete ushabiki
Jambo la tatu, wapigakura wasilete ushabiki kwenye vituo vya kupigia kura. Mambo ya ushabiki ni pamoja na kuongelea matokeo ya uchaguzi kabla hayajatangazwa na mamlaka husika zilizokasimiwa jukumu hilo.
Mkurugenzi huyo anafafanua kwamba jambo hilo linajenga hisia tofauti miongoni mwa wapiga kura na linaweza kusababisha vurugu endapo matokeo yatakuwa kinyume chake. Anabainisha kuwa kura ni siri ya mpigakura mwenyewe.
“Sitarajii kuona watu wakitengeneza makundi ya kujadili mwenendo wa uchaguzi kwenye vituo. Hiyo ni sawa na kampeni siku ya uchaguzi, hatutaacha ufanyike kwa sababu utaharibu mchakato wa uchaguzi,” anasema.
Ukipiga kura nenda nyumbani
Jambo la nne, mwananchi akimaliza kupiga kura aende nyumbani kusubiri matokeo kutangazwa. Kuendelea kukaa kwenye vituo vya kupigia kura kunasababisha msongamano usio wa lazima.
Kombwey anasema hakuna haja ya kukaa kwenye vituo vya kupigia kura kwa ajili ya kulinda kura kwa sababu tayari mawakala wa vyama vya siasa wapo kwa ajili ya kuangalia mwenendo mzima wa uchaguzi.
“Ile dhana ya kutaka kulinda kura zisiibiwe ndiyo inayosababisha vurugu kwenye vituo. Hizo ni hisia tu, hakuna wa kuiba kura kwa sababu kuna mawakala wanaowakilisha vyama vyao,” anasema.
Tume ina jukumu la kutangaza matokeo
Anasema jukumu la kutangaza matokeo ya urais ni la Tume ya uchaguzi. Tume pia imekasimisha jukumu la kutangaza matokeo ngazi ya kata kwa msimamizi msaidizi wa kata na ngazi ya jimbo kwa msimamizi wa halmashauri.
Kombwey anasema kuna baadhi ya watu wanatishia kutangaza matokeo endapo Tume itachelewa kufanya hivyo. Anasisitiza kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha utaratibu kwa sababu hakuna mtu mwenye jukumu hilo zaidi ya Nec.
Anasema Nec imejipanga kutangaza  matokeo ya urais ndani ya siku tatu kwa sababu watatumia Mfumo wa Kusimamia Matokeo (RMS) ambao utawawezesha kupokea, kujumlisha na kutangaza matokeo.
Licha ya kutakiwa kisheria kutangaza matokeo hayo ndani ya siku saba, Nec imebainisha kwamba mfumo huo utasaidia kuongeza kasi ya ukusanyaji wa matokeo kutoka sehemu mbalimbli nchini.
Mabadiliko ya sheria
Jaji Lubuva anasema mabadiliko makubwa ya sheria ya uchaguzi yalifanyika mwaka 2010, mwaka huu sheria hiyo haijafanyiwa marekebisho isipokuwa kanuni za uchaguzi zimerekebishwa ili kuleta ufanisi katika uchaguzi ujao.

Sumaye ajitoa CCM, ajiunga Ukawa

Historia imeendelea kuandikwa katika siasa za Tanzania baada ya leo, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye kujitoa CCM na kujiunga na chama kimojawapo kinachounda Umoja wa Katiba ya Wananchi-(Ukawa).
Akitangaza uamuzi huo jijini Dar es Salaam leo katika mkutano na wanahabari Sumaye amesema chama alichojiunga miongoni mwa vinne (Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD) vinavyounda Ukawa kitajulikana baadaye.
Louis Kolumbia, Mwananchi Digital
Dar. Historia imeendelea kuandikwa katika siasa za Tanzania baada ya leo, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye kujitoa CCM na kujiunga na chama kimojawapo kinachounda Umoja wa Katiba ya Wananchi-(Ukawa).
Sumaye anakuwa Waziri Mkuu mstaafu wa pili kujiondoa chama tawala katika historia ya Tanzania, ambapo waziri mkuu wa kwanza kuhama CCM ni Edward Lowassa aliyejiunga Chadema miezi michache iliyopita.
Akitangaza uamuzi huo jijini Dar es Salaam leo katika mkutano na wanahabari Sumaye amesema chama alichojiunga miongoni mwa vinne (Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD) vinavyounda Ukawa kitajulikana baadaye.
Waziri Mkuu huyo aliyehudumu Uwaziri Mkuu miaka yote 10 ya utawala wa awamu ya tatu chini ya Rais mstaafu, Benjamin Mkapa amesema amejiunga Ukawa kwa kushirikiana na viongozi wa umoja huo awatumikie Watanzania kwa kasi kubwa baada ya uchaguzi kwa kuwa anaamini Ukawa utashinda.
Amesema kukithiri kwa rushwa ndani ya CCM na kuvurugwa kwa mchakato wa uchaguzi kumechangia wananchi kukata tamaa hali iliyochochea uungwaji mkono wa upinzani tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
“Na sasa kuzuia wimbi la mabadiliko ni kazi kubwa sana. Naamini Ukawa watashinda uchaguzi huu, CCM wamezubaa wakidhani watashinda wakati wananchi wamechoka, wanahitaji mabadiliko” alisema na kuongeza.
“Sijajiunga Ukawa kwa kuwa mgombea wake wa urais anatoka Kanda ya Kaskazini, wala kwa kuwa viongozi wengi waandamizi wanatokea huko la hasha bali kutaka kutoa uzoefu wangu nikishirishiana na Lowassa katika uongozi wa nchi, alisema na kudai dhana kwamba hakuna maisha ya kisiasa nje ya CCM imepitwa na wakati.