Moshi. Mbunge wa Vunjo, Augustino Mrema (TLP) amesema amejiandaa
kuingia ‘vitani’ na Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia ambaye
ametangaza kuwania ubunge katika jimbo hilo, mwaka 2015.
“Siogopi mtu yeyote. Nimejiandaa vilivyo kwa
mpambano huu. Najivunia rekodi yangu nzuri ya utendaji wala sitishiki na
wananchi wangu nimewauliza wameniambia nisihofu,” alisema Mrema.
Kwa mujibu wa Mrema, anaamini rekodi yake nzuri ya
utendaji ndiyo itakayomuuza mwaka 2015 na kwamba, ni rekodi hiyo nzuri
ndiyo iliyowafanya wananchi wa jimbo hilo wakamchagua mwaka 2010.
“Umesahau nilikuwa mbunge wa Moshi Vijijini wakati
huo ikiwa ni pamoja na Vunjo? Rekodi yangu nilipokuwa naibu waziri mkuu
inajieleza. Yeye (Mbatia) aje nimejiandaa kwa mpambano,” alisema.
Juzi, Mbatia ambaye pia ni mbunge wa kuteuliwa,
alisema kwa sasa ameelemewa na maombi ya makundi mbalimbali ya jamii
yakimtaka agombee ubunge katika jimbo hilo mwakani.
“Nimefuatwa mara kadhaa na viongozi wa dini
wakiniomba nigombee tena 2015. Wapo wananchi wamenifuata hadi bungeni.
Simu yangu imejaa meseji nyingi za kuniomba,” alisema Mbatia.
Mbatia ambaye pia ni mwenyekiti mwenza wa Umoja wa
Katiba ya Wananchi (Ukawa), aliwahi pia kuwa mbunge wa kwanza wa jimbo
hilo chini ya mfumo wa vyama vingi mwaka 1995 hadi mwaka 2000.
“Hayo maombi ya wananchi siwezi kusema
nawakatalia, mimi ni nani nikatae kuwatumikia Watanzania wenzangu? Niko
tayari kuwatumikia ila wajue kwa sasa kuna mbunge,” alisema.
Mbatia aliongeza, “Natarajia kwenda Vunjo wakati
wowote kuanzia leo ili nitoe jibu rasmi mbele ya Wanavunjo. Nashukuru
kwa heshima hii waliyonipa. Naahidi sitawaangusha.”
Wiki iliyopita, baadhi ya wananchi waliodai
kuwawakilisha wenzao kutoka kata zote za jimbo hilo, walitoa tamko
lililosomwa na Mathew Temu wakimtaka Mbatia agombee ubunge kupitia vyama
vya NCCR, Chadema na CUF vinavyounda Ukawa. Katika tamko hilo, wananchi
hao walisema rekodi ya Mbatia alipokuwa mbunge haijawahi kuvunjwa.
No comments:
Post a Comment