Katika toleo la jana Waziri Mkuu mstaafu, John Malecela
alizungumzia historia yake katika siasa na mchakato wa Katiba Mpya.
Katika sehemu ya pili ya mahojiano na gazeti hili, anaeleza pamoja na
mambo mengine, ubinafsishaji, ajira na ushiriki wa wasomi kwenye siasa.
Swali: Kuna taarifa kwamba uliwahi kuwekwa ndani
kutokana na ushiriki wako katika harakati za ukombozi kupitia Tanu. Hili
likoje?
Malecela: Sikuwekwa ndani kwasababu ya harakati za
Tanu, hapana. Wakati narudi kutoka India baada ya kumaliza masomo yangu
ya shahada ya kwanza, nilipita njia ya Mombasa, kutoka Mombasa nikaja
Arusha. Arusha pale alikuwepo Nsilo Swai ambaye alikuwa mwalimu wangu
Mazengo halafu India tukasoma wote, kwa hiyo alikuwa pale kama Katibu
Mkuu wa Meru Cooperative Union. Nikaona nipite kwake nikae pale siku
mbili, tatu hivi, kutoka Arusha nikaja Dodoma. Nilipofika tu nikaitwa
kituo cha polisi. Nilipofika pale wakapekua mizigo yangu sasa wakanikuta
na kitabu kimoja cha George Padimo ambacho kilikuwa kinaitwa Pan
Africanism or Communism, wale wapekuzi kwa bahati mbaya hawakuwa Wazungu
walikuwa ni weusi wenzangu.
Basi wakasema huyu mtu ana chembe-chembe za
ukomunisti huyu ngoja tumweke ndani. Nililala mahabusu pale siku mbili
aliyekuja kunitoa alikuwa ni Mzungu. Wakati huo wa Waingereza kila siku
lazima mkuu wa polisi aende akaripoti kwa Mkuu wa Wilaya akieleza kwake
ana watu wangapi mahabusu na makosa yao.
Sasa alipokwenda kuripoti kwamba kwenye mahabusu
wana kijana ametoka India na wanafikiri kwamba ni mkomunisti, akawaambia
kwamba mleteni. Mkuu wa Wilaya huyo alikuwa anaitwa Eyas, nikaenda
ofisini kwake bahati yule Eyas alikuwa ni raia wa Ireland. Sasa
nilipofika ofisini kwake akaagiza chai tukawa tunakunywa, akasema
Waingereza hawa wabaya ndio maana sisi tunapigana nao we kijana angalia
usifanye ovyoovyo.
Wakati huo ulikuwa mwaka 1959. Basi akanihubiria
hapo, baada ya hapo akawaambia wale polisi ujinga huo, huyu hawezi kuwa
mkomunisti, huyu ni Mgogo mwacheni arudi kwao. Na kweli yule Mkuu wa
Wilaya alifurahi kuona kuwa mimi nimetoka kijijini huko akanipeleka
mpaka nyumbani Mvumi kwa gari yake.
Swali: Hapa tulipo kuna tatizo kubwa la ajira na wengi wamelizungumzia, wewe unalizungumzia vipi?
Malecela: Kwanza nataka muelewe huku tulikotoka
chama kilikuwa kinasema nini. Chama kilikuwa kinawakilisha siasa ya
ujamaa na kujitegemea ndio maana katika miongozo mingi ya Tanu na
baadaye Chama Cha Mapinduzi, ilikuwa kila siku inaomba watu wajiunge
pamoja katika vikundi ili kuzalisha. Nitawapa ushahidi wakati nikiwa
kwenye Baraza la Mawaziri.
Mara tu tulipopata uhuru Nsilo Swali alikuwa ndio
Waziri wa Mipango wakalizungumzia hilo la ajira ya vijana Dar es Salaam.
Wakasema si tunayo mashamba ya sukari Kilombero, basi wakachukua vijana
pale zaidi ya 3,000 wakakaa nao, nakumbuka walisindikizwa na treni la
kwenda Kidatu kuwapeleka vijana waende wakafanye kazi na walipewa
mishahara kama ya miezi miwili na vifaa vyote vya kwenda kukata miwa.
Hiyo yote ilikuwa ni nguvu za kuwapa vijana ajira.
Wakaenda kule miezi mitatu baadaye hakuna hata
mmoja aliyebaki. Niwape ushuhuda wa karibuni wakati Mama Kunambi
(Bernadetha, DC wa Dar es Salaam) aliwahi kuja na wazo lilelile, mimi
nikamwambia wazo hili huko nyuma tulijaribu, lakini baada ya miezi
mitatu wote wakawa wamerudi hapa. Kwanza tukapita kwenye mashamba ya
mkonge tukatafuta vibarua, sio ya wasomi hapana, ni ya vijana kufanya
kazi kwa mikono. Mama Kunambi akahesabu vijana wake 3,000, hizi rekodi
sijui kama Ilala wanazo, tukahangaika, tukawapeleka hawa vijana kwamba
waende wakafanye kazi huko na wao wakakubali.
Tukawapa mishahara miezi miwili kabla hata
hawajafika huko. Baada ya miezi mitatu minne wote wakawa wamesharudi Dar
es Salaam. Sijui kwa nini tukianza kusema ajira mimi nahisi mara
nyingine sisi Watanzania tunaanza kujiona Serikali yetu haifanyi
chochote, ndio maana tunakuwa na matatizo haya tunasahau hili ni tatizo
la ulimwengu mzima.
Ni kweli wenzetu walioendelea tatizo hili linakuwa
tofauti, kwa mfano Uingereza utakuta vijana wasiokuwa na ajira ni
wengi, lakini kule mara nyingine ni kwa sababu ya kuchagua kazi ambayo
ni sawa na huku ambako watu wanafikiri kuwa bado wanaweza kupata kazi ya
kufagia ofisini na siyo kwenda kukata mkonge.
Kwa hiyo hili tatizo la vijana tunalo, lakini sisi kama Tanzania
tunachotakiwa kufanya ni vitu viwili ambavyo kweli tuvifanye kwa juhudi
kubwa kabisa maana yake ndio urithi ambao baba wa taifa ametuachia wa
kukabiliana na matatizo yetu. Kama tunaweza kuboresha maisha ya vijijini
kweli huwezi kupata wamachinga Dar es Salaam. Jamani kwa sababu ninyi
ni watu wa habari naomba muende mkachunguze Dar es Salaam, muone hawa
watu wa Lushoto, Wasambaa nenda kahesabu hawa watu kama utamkuta Msambaa
Dar, hakuna, kwanini?
Mimi nimekwenda Lushoto unakuta kijana ana eka
yake ya nyanya, anailima vizuri kweli kweli na kiutaalamu. Ukiilima eka
moja vizuri, inakupa zaidi ya tani mia moja za nyanya na kule wanalima
mara tatu kwa mwaka.
Kwa hiyo kule Lushoto hupati vijana wa kuja kuwa wamachinga, hapana.
Swali: Viwanda vingi vilibinafsishwa haiwezi kuwa sababu ya tatizo la ajira?
Malecela: Mimi sisemi kuwa viwanda vingi
vimebinafsishwa ndio tatizo la ajira, hapana. Ninachosema kuna wakati
katika miaka ya 1970 Tanzania ilikuwa na viwanda vingi vya nguo. Kiwanda
cha Urafiki kilikuwa kimeajiri zaidi ya vijana 3,000, Ufi (Kiwanda cha
zana za kilimo) kiliajiri watu 1,000 na Tanita (cha kubangua korosho)
kiliajiri wafanyakazi 2,000.
Sasa vyote hivyo akaja mtu akutuambia ohhh
kuendeshwa na Serikali haifai, hivi vinatakiwa viende binafsi.
Tulivyosema hivyo viendeshwe na watu binafsi, Wahindi wakaja kwanza
wakapandisha bei ya korosho. Korosho kilo moja Sh800.
Viwanda vyetu vikakosa korosho kwa hiyo vikasimama
na hii imetokea juzi juzi hapa bei ya korosho imeanguka kutoka Sh800
kwa kilo hadi Sh120. Walipoona viwanda vimedorora havifanyi kazi na
vyama vya ushirika vimekufa kwa sababu vilikuwa vikiendeshwa na hii
biashara ya korosho, wakapunguza bei.
Nenda Morogoro yaani unajua vitu vingine tunasema
tu, lakini mimi ambaye niliona viwanda vikifanya kazi leo napita
Morogoro unaweza kuona ni mji unaokufa, lakini vilipokuwa vinafanya kazi
pita pale saa 10:00 jioni unaona watu wanatoka kule kwenye viwanda sasa
wanakuja mjini we mwenyewe unashangaa hivi hii ni Tanzania.
Kwa viwanda tukadanganywa ohh vitu vinavyoendeshwa
na serikali haviendi, vibinafsishwe tukasahau kwamba vingine watu wale
wanakuja na nia kabisa anakinunua kiwanda palepale anakifunga.
Nenda Mwanza mfano mzuri na huu ndio huwa
unanisikitisha kweli kweli, ukiwa unakwenda uwanja wa ndege mkono wako
wa kushoto utaona magofu makubwa, yale magofu yalikuwa majengo ya
kiwanda kikubwa cha ngozi.
Akaja mtu akabinafsisha akachukua mitambo yote kauza Kenya sasa ukienda pale unalikuta jumba tu tupu.
Swali. Kwa hiyo kwa kifupi ubinasfisishaji haukuwa kitu kizuri?
Malecela: Kwanza binafsi nisingependa kuhukumu kuhusu
ubinafsishaji. Mimi ninasema kila kitu mnapokifanya jamani mkifanye
hatua kwa hatua. Siku za nyuma tulikuwa hatuna haja ya kuleta hizi juisi
kutoka nje ya nchi, tulikuwa na kiwanda cha kutengeneza juisi ya
machungwa lakini hata kilivyokufa sijui. Tulikuwa na kiwanda cha betri
Matshushita. Unajua Matshushita kilivyokufa? Tajiri mmoja aliingiza
betri za matshushita kutoka Indonesia akauza, Matshushita wakaja
serikalini wakasema kama hivi tutafunga, wakafunga.
Barabara ya Pugu (Nyerere) ilikuwa mahali ambapo
ikifika jioni watu wanatoka kazini unaangalia unajua kweli tuna viwanda,
lakini vingi vimefungwa. Pale Dar es Salaam tulikuwa na viwanda vya
nguo tulikuwa na Sungura Textile, tulikuwa na Tasini, tulikuwa na kama
viwanda vinne vya kutengeneza nguo. Arusha General Tyre, tulikuwa na
viwanda viwili vya nguo hiki A-Z kilifikia wakati hadi kinatengeneza
nguo za ndani wakiziweka lebo ya mark Spencer, unatoka hapa unakwenda
kununua vest Uingereza kumbe inatengenezwa Arusha.
Swali: Kuna wimbi sasa kila mtu anagombea ubunge,
maprofesa, madaktari wanaacha kazi zao wanagombea ubunge. Unafikiri ni
kwanini?
Malecela: Nadhani hasa kwa wasomi mimi nasema
Mungu anisamehe kama ninawasingizia, wengi walifikiri nikiwa mbunge
nitakuwa waziri. Kwa huko nyuma maprofesa wachache walipata uwaziri
kweli. Walipoanza kuja kwa fujo na kwa wingi ikawa haiwezekani tena,
halafu wengine hata ufanisi wao ulikuwa mdogo.
Swali; Pamoja na hapo kuna wimbi hili la watoto wa viongozi nalo linakuja kwa kasi!
Malecela; Mimi nataka kuwaambia kwa kweli hilo la
kusema watoto wa wanasiasa mnawaonea. Unamkuta mzee yeye mfua vyuma,
anatengeneza visu amekaa na mfuko wake. Mtoto anakaa pembeni anaona baba
yake anapopuliza moto, anaona mpaka chuma kinavyokuwa chekundu.
Anamwona baba yake anavyokwenda kukigongagonga hadi kinakuwa kisu, ama
kama jembe na kadhalika.
Sasa mbona watoto wa walimu wakichukua ualimu
hatusemi? Watoto wa madereva wakiwa madereva hatusemi, ila watoto wa
viongozi wakiwa wanasiasa mnasema. Sisi tuna msemo kwamba; ukimwangalia
ng’ombe mguu wa mbele utakapokanyaga na huu wa nyuma utakuja kukanyaga
hapohapo.
Kwa hiyo hawa watoto wa wanasiasa bwana wakati
mwingine wanaongozana na baba anapokwenda mahali, mara nyingine haendi
kwa sababu anavutiwa na mkutano hapana, yeye anakwenda tu ili apande
gari la baba. Kwa hiyo anakwenda pale baba anahutubia pale anaona, sasa
watakuwa wajinga sana kama hawajifunzi. Kwa hiyo mimi nasema watoto wa
viongozi tuwahukumu kwa utendaji wao.
Kweli kama mtu akianza kutumia jina la baba yake ohh mimi mtoto wa fulaniatashindwa.
Swali: Unatoa ushauri gani kwenye hili wimbi la wasomi maprofesa na madaktari kukimbilia kwenye siasa?
Malecela: Mimi sina ushauri wowote. Ni kama nguo,
zilikuja watu wakaanza kulalamika jamani wasichana lakini baadaye ni
mtindo ulipita. Hata hivi sasa wengi watakwenda kwenye siasa lakini muda
ukifika watagundua kuwa kwenda kwenye siasa ni kupoteza muda.
Swali.Ukiwa Waziri Mkuu, ulikuwa ndio msimamizi wa
shughuli zote za Bunge. Kuna kipindi Bunge lilikuwa moto na hasa wakati
wa G 55 unaweza kulizungumzia hili?
Malecela: Siwezi kulizungumzia sana kwa sababu kipindi hicho
kilipita. Ni kweli kulikuwa na kundi la G 55 ambao walikuwa wanataka
Tanganyika. Katika Muungano Tanganyika nayo ionekane iwe Serikali ya
Tanganyika ya Zanzibar halafu Muungano. Ilikwenda ilivyokwenda lakini
mwisho ikaishia kwenye chama ambacho kilipeleka kwa wanachama basi mambo
yakamalizika.
Swali: Ukiwa Waziri Mkuu changamoto uliyoipata unaizungumziaje?
Malecela: Changamoto huwezi kuizungumzia kwa
sababu hizi ndizo zinazokujenga kwa wakati huo kwamba ukisikia jina
Malecela unalinganisha na hiki na hiki; vizuri na vibaya.
Swali: Ukiwa Waziri Mkuu, uliwahi kujionyesha
hadharani kuwa wewe ni mpenzi wa timu ya mpira ya Simba Sports Club,
uliwahi kukacha safari yako moja kwa ajili ya kwenda kushuhudia Simba
ikifanya vitu vyake uwanjani. Sijui kwa sasa hali yako ikoje kimichezo?
Malecela: Mechi zote ambazo nimewahi kuwa mgeni
rasmi Simba inacheza, ilishinda. Ngojeni niwape historia kidogo, mimi
wakati nikisoma Shule ya Sekondari Minaki, Dar es Salaam kulikuwa na
timu tatu. Kulikuwa na timu ya Wazungu, timu ya Wahindi, Magoha na
Waarabu na timu ya Waafrika.
Nendeni kwenye historia mchele walikuwa wanakula
Wahindi, Wasomali na wengine Mwafrika ulikuwa huruhusiwi kununua mchele
mpaka upate kibali. Sasa hata kama ukiwa mchezaji namna gani, timu ya
wazungu ilikuwa ikiitwa Sunderland sasa hata uwe nani ilimradi wewe ni
mweusi huwezi kuichezea timu hiyo.
Hii ya wahindi, magoha na waarabu ilikuwa ikiitwa Cosmo Club hata uwe nani huwezi kujiunga na kama sio wa jamii hizo.
Kwa watu weusi ilikuwa Yanga Africans, sasa wewe
hata utake kucheza mpira wa namna gani lazima ukawe Yanga. Kwa hiyo
hakukuwa na chaguo hivyo mtu ukiwa mpenzi wa mpira lazima tu uwe mwana
Yanga.
Kwa hiyo wazungu walipoanza kuondoka ile Sunderland ikaanza kupungukiwa nguvu wakajitahidi kujiunga na Cosmo.
Nao walipoanza kuondoka na kuhama ndio baadaye
wakaanza, jamani tuwachukue na wenzetu. Wakawachukua na waafrika na
mwenyekiti wa kwanza na ndio akaleta na jina la Simba alikuwa Amon
Nsekela. Karume alikuwa Yanga kwa sababu wakati ule hakuwa na chaguo.
Swali: Hadi sasa bado wewe ni shabiki wa Simba?
Malecela: Mimi napenda mpira mzuri tu. Kuna wakati
nilikuwa nafikiri hii vita ya Yanga na Simba ilikuwa inadumaza mpira.
Nilipokuwa Waziri wa Kilimo kwa kweli nilijitahidi nikaunda timu ikaenda
kucheza na hizi timu kubwa zikaenda droo. Baada ya hapo wachezaji wangu
wakachukuliwa mmoja mmoja na mtu wa kilimo akafanywa kuwa Mwenyekiti wa
Yanga na timu yetu ya Kilimo ikafa.
Swali Kuna jambo ambalo ungependa lifahamike kwa wananchi?
Malecela: Ningependa wananchi wafahamu kwamba
maendeleo ni hatua. Mimi nimekwenda Nigeria nimeendesha gari kutoka
Abuja kwa barabara mpaka Port Harcourt jamani, umaskini niliouona kule
ni wa kupindukia, huwezi kuulinganisha na wetu hata kidogo.
Mimi nilipokwenda kuripoti Tukuyu ilinichukua siku
mbili kufika. Siku ya kwanza niliondoka Dodoma na basi nikalala Iringa.
Kutoka pale kesho yake nikalala Mbeya ndio nikafika Tukuyu. Lakini sasa
ukitoka Dodoma saa 12:00 asubuhi Mbeya saa tisa umeshafika.
Hapa ilikuwa safari ya hapa (Dodoma) hadi Iringa
ilikuwa ni maili 240 ilikuwa ni ya kutwa nzima. Unaondoka hapa asubuhi
na mabasi haya ya Urafiki unafika kule jioni, lakini sasa hivi unaondoka
Iringa saa 12:00 asubuhi saa 4:00 asubuhi uko Dodoma.
Kinyago
Kinyago
Katika sebule ya Mzee Malecela mjini Dodoma
ameweka kinyango kikubwa mfano wa mti ambao umebeba watu wakiwa wamebeba
vitu mbalimbali.
Malecela anakizungumzia kinyago hicho kilimgharimu
sh 300,000 wakati akiwa Waziri Mkuu miaka ya tisini na kilichongwa kwa
muda wa miezi miwili.
Kama hiyo haitoshi anasema mchongaji wa kinyago
hicho ambaye sasa ni marehemu alikuwa akiifanya kazi hiyo tu kwa kipindi
cha miezi miwili ambapo ilimlazimu kumuwekea wafanyakazi kwa ajili ya
kumfulia, kumpikia na kumfanyia vitu vingine ili atumie muda mwingi
kuchonga kinyago hicho.
Anasema kinyago hicho kimetengenezwa kwa kutumia
shina la mti aina ya mpingo na hata kuingia katika sebule yake
ilimlazimu kuvunja moja ya dirisha kutokana na ukubwa wa kinyago hicho
ambacho ilishindikana kupita mlangoni.
Twende kwenye elimu, nimekuwa Chancellor (Mkuu wa
Chuo) wa Open University (Kikuu Huria) kwa miaka 20 tumekuwa na mikutano
ya ‘machancellors’. Bado Tanzania tuna vyuo vikuu vingi kuliko jirani
zetu Kenya, Uganda na sasa ukishakuwa kuliko Kenya na Uganda sembuse
Rwanda na Burundi. Hata Zambia, hata Msumbiji hawajafika hivyo mimi
nasema kuwa hili jambo la Watanzania kunung’unika kila siku kwamba
hatuna hiki hatujafanya hivi, ni kana kwamba hatujafanya maendeleo
nasikitika sana tunajitukana.
Wengine wanaosema hivyo hawajatoka waende wakaone
na mahali pengine palivyo. Nenda Horohoro mpaka wa Tanzania na Kenya,
ukija kwetu unaona watu, vijiji na nyumba za bati, palepale unapita
mpaka unaenda Kenya, utaona tofauti.
Ukiangalia ukubwa wa nchi ukichukua Kenya na
Uganda ukaziweka pamoja bado Tanzania ni kubwa kuliko nchi hizo kwa
zaidi ya maili 6,000. Kwa hiyo wenzetu wakijenga barabara ya lami zaidi
ya km 150 wameshafika kwenye mpaka wa nchi, lakini sisi kujenga barabara
kutoka Dar es Salaam hadi Tunduma ni zaidi ya Km 1000.
Nafikiri kwa nyinyi watu wa habari ukianza
kuzungumzia vitu vizuri ambavyo Serikali imefanya wataanza kutukana huyo
amekuwa CCM number two au CCM B .
Swali.Sasa hivi tunaona vyuo vyote vinatoa
shahada, hata vyuo vya kutoa vyeti au stashahada vinabadilishwa,
unalizungumziaje hili?
Malecela: Na hilo ni kosa kubwa sana unapokuwa na
mhandisi lazima huku chini uwe na watu wa kukuunga mkono, sasa hao ndio
tulikuwa tunawatoa mafundi, Mbeya, Dar Technical ni kweli ulivyosema.
CBE sasa imekuwa chuo kikuu. Chuo cha Mipango
kilijengwa kwa lengo la kusaidia maendeleo vijijini, malengo ya Mwalimu
(Nyerere) kila kijiji kiwe na mtu ambaye anaweza akasaidia mipango ya
maendeleo sasa ni chuo kikuu.
Mimi nilipokuwa India, nimeona mtu na shahada ya
uzamili lakini ni kondakta wa daladala, kwa nini? Kwa sababu Chuo Kikuu
cha Bombay kilikuwa kinapokea zaidi ya wanafunzi 60,000 kila mwaka.Ndio
nakwambia sasa tuna viwanda vya kutengeneza mabomu.
No comments:
Post a Comment