Mara nyingi tumekuwa tukishuhudia wasichana wengi hasa wakiwa
shuleni wakipata matatizo ya kuweweseka, kupiga kelele na
kuchanganyikiwa kiasi cha kushindwa kuendelea na masomo.
Ingawa watu wa jinsia zote, wakubwa kwa wadogo
wanaweza kupata tatizo hili, wanaoathirika zaidi ni wanawake hasa
wasichana wa umri kati ya miaka 12 na18.
Matukio ya wanafunzi kupagawa, kuweweseka na
kupiga kelele yametokea jijini Dar es Salaam katika shule kadhaa za
msingi. Agosti 2005, wanafunzi 24 wa Shule ya Msingi ya Uwanja wa Ndege
walipata tatizo hilo na Novemba 2006, wanafunzi 15 wa darasa la tano
katika Shule ya Msingi ya Mbuyuni.
Matukio kama yayo yametokea katika mikoa mingine
kama tukio la Machi 2007 kwenye Shule ya Msingi ya Lewa wilayani
Korogwe, Tanga, Mei 2008 lilipotokea kwa wanafunzi 50 na mwalimu wao
mkoani Dodoma na wanafunzi 30 wa Shule ya Msingi ya Mang’ula mkoani
Morogoro mwaka 2009.
Hali hii imekuwa ikipokewa kwa hisia tofauti na
watu mbalimbali katika jamii. Wengine huihusisha na imani za
kishirikina, kupagawa na pepo au kudhuriwa na mizimu.
Ingawa jamii ina maoni tofauti kuhusu tatizo hili,
wanasayansi wanaamini kuwa hali hii inatokana na matatizo ya afya ya
akili yanayojulikana kama hysteria.
Kihistoria ugonjwa huu ulianza zamani hata kabla
ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo. Jina la ugonjwa huu lilitokana na mawazo ya
madaktari wa zamani wa Kigiriki waliokuwa wanafikiria kwamba chanzo cha
ugonjwa huu ni matatizo katika mfuko au mji wa mimba wa mwanamke, ambao
kwa Kigiriki unaitwa hystera.
Madaktari wa Kigiriki walidhani kuwa huu ni
ugonjwa unaowapata wanawake pekee. Hii ilitokana na idadi kubwa ya
wagonjwa wa tatizo hili kuwa wanawake, na hata pale wanaume walipokuwa
na dalili za tatizo la hysteria ilidhaniwa kuwa wana tatizo jingine kwa vile hawakuwa na mfuko au mji wa mimba.
Dhana ya madaktari wa kipindi hicho juu ya ugonjwa
huu ilikuwa kwamba mfuko wa kizazi (mji wa mimba) unabana na kukauka
kutokana na kutokufanya ngono kwa muda mrefu au kuzidiwa na hamu ya
ngono. Matibabu ya enzi hizo yalihusisha kumtekenya mwanamke katika
sehemu zake za siri ili apate kumaliza hamu ya ngono, lakini matibabu
hayo yalikuwa hayatoi matokeo ya uponaji yaliyotarajiwa.
Hata hivyo, sayansi ya tiba ya binadamu imethibitisha kuwa hysteria ni ugonjwa wa akili unaotokana na msongo mkali wa mawazo na hisia.
Linaonekana ni tatizo zaidi la afya ya akili na kisaikolojia.
Tatizo hili hutokea pale mtu anapopata msongo wa
kihisia maishani zaidi ya vile alivyojiandaa au anavyoweza kukabiliana
nao. Mara nyingi msongo huu hutokana na hisia au mgogoro wa fikra,
kutokuwa na uhakika wa usalama katika siku za usoni, kutengwa na jamii
au kutosikilizwa kwa upendo. Tamaa kali ya kutaka kupendwa kuliko
kawaida isipotimizwa, pia huleta tatizo hili.
Wakati mwingine hisia na fikra hutokana na matatizo ya kawaida,
lakini akili huyakuza sana na mhusika akajiona hawezi kuyakabili, hafai
na hathaminiwi.
Mgonjwa anaweza kujilaumu na kupata hisia za
kupoteza ulinzi au kupata kumbukumbu isiyonyamazishwa ya tukio la
kinyama alilotendewa kama vile kubakwa, kunyanyaswa au ukatili wa
kijinsia.
Watu wanaopata ugonjwa wa hysteria huwa na matatizo ya kihisia ambayo mara nyingi hawapendi kuyazungumzia na kwa sababu hiyo, matatizo hayo huwaelemea sana.
Katika utafiti uliofanywa na Altamura AC na
wenzake nchini Malawi, iligundulika kuwa wanawake wengi, hasa wasichana
hupata msongo mkali sana wa mawazo, kujilaumu na kushuka sana moyo pale
wasiporidhishwa na hali ya maisha waliyo nayo.
Mwanasaikolojia Mareesa Dannielle wa New Zealand,
katika utafiti wake mwaka 2007, alibaini kuwa uongozi mbaya wa watu
unaweza kuchangia kwa namna moja ama nyingine kutokea kwa tatizo hilo.
Kaimu mganga mkuu wa Wilaya ya Ulanga, Eddy
Mjungu anasema: “Hii inaweza kuwa watoto kutolelewa vizuri, uhusiano wao
na wazazi, walimu na hata migogoro ya kimapenzi.”
Ugonjwa huu unaweza kumpata mtu mmoja pekee lakini
pia unaweza kusambaa kwa wengine katika kundi la watu wanaokabiliwa na
msongo wa kisaikolojia unaofanana na wanaokaa au kufanya kazi katika
mazingira yanayofanana.
Hysteria inayosambaa huanza na mtu mmoja
na anapoonyesha dalili, wengine nao huanza kujenga hofu na hisia za
kuathirika baada ya kumwona mwenzao.
Mara nyingi dalili za hysteria
inayosambaa hazionyeshi chanzo bayana na hazitafasiriki sawasawa lakini
zinaenea kwa haraka miongoni mwa walioona mgonjwa wa kwanza aliyepata
tatizo.
Hofu huongezeka zaidi na tatizo husambaa zaidi
pale linapoanza kuhusishwa na imani za kishirikina, mambo ya kimizimu na
kupagawa na majini au pepo wabaya.
Hofu huzidi pale timu ya wataalamu wa uchunguzi wa vyanzo vya magonjwa wanaposhindwa kubaini chanzo bayana cha tatizo.
Hysteria ingawa ni tatizo la afya ya
akili, pia hudhuru afya ya mwili kwa kiwango kikubwa. Hofu, woga na
wasiwasi husababisha mapigo ya moyo wa mgonjwa kwenda haraka, kutapika,
kupata kichefuchefu, mwili kuishiwa nguvu na maumivu ya kichwa.
Matatizo mengine ni pamoja na miguu kufa ganzi, kushindwa
kutembea, kupiga kelele au kucheka sana bila sababu za msingi na kupata
degedege.
Wagonjwa wengine hupoteza hamu ya chakula,
kutokupata choo kabisa au kuharisha na wengine hutokwa jasho jingi,
kutetemeka, kupumua kwa shida au kushindwa kupumua vizuri kiasi kwamba
hewa chafu ya ukaa haitolewi mwilini kwa kiwango cha kutosha.
No comments:
Post a Comment