Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 19 tangu
kuanzishwa kwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) hivi
karibuni, Jaji Warioba alisema ataingia mitaani kuitetea Rasimu ya
Katiba iliyokuwa imebeba maoni ya wananchi.
Alisema kuwa Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba imeondoa mambo manne muhimu.
Hata hivyo, akizungumza jana na gazeti hili
alisema kuwa Katiba hiyo imeacha maswali mengi kuliko majibu hasa kwa
upande wa Zanzibar.
Sitta atakuwa na kibarua kingine cha kujisafisha
mbele ya wananchi ambao alikaririwa akisema kuwa wamekuwa wakimtumia
meseji za matusi za ya 50 kila siku.
Kwa nyakati tofauti wananchi wasiojulikana
wamekuwa wakiandika meseji za matusi kwenye mitandano na simu kwa kile
wanachosema kuwa Sitta amelazimisha maoni ya CCM yatawale Bunge.
Baadhi ya wananchi waliohojiwa kuhusu mwenendo wa
Bunge hilo, waliwalaumu wajumbe wa Bunge waliokuwa wakisema walipiga
kuwa kwa niaba ya wananchi kwenye majimbo yao.
Walihoji ni lini wajumbe hao ambao ni wabunge wao
walikwenda kuwauliza iwapo wanataka kupiga kura ya hapana au ndiyo dhidi
ya Katiba iliyopendekezwa?
‘Mimi nimesikia tu mbunge wetu (anamtaja) amesema
wananchi wake wamechagua kura ya ndiyo. Ni nani alimtuma kwenda kuwa
tunataka Katiba hiyo wakati maoni yetu tulitoa tofauti, “ Yohana Change
mkazi wa Vwawa, Mbozi.
Mwanaidi Suleiman alisema haelewi nini
kilichotokea bungeni, kwa kuwa matarajio aliyokuwa nayo kuhusu Katiba
yameyeyuka baada ya kusikia mambo mengi yamekataliwa.
“Nafuu kama wangeondoa mambo mengine, lakini siyo
serikali tatu na uraia wa nchi mbili. Mimi hayo niliyaona makubwa sana,
kama hayapo sasa Katiba itahusu nini?” alihoji Mwanaidi.
Chadema na wanachama wake.
Hali ya hewa ndani ya Chadema ilichafuka baada
ya Sitta kusema kuwa kuna wajumbe wawili wa Umoja wa Katiba ya Wananchi
(Ukawa) kutoka Zanzibar walikubali kupiga kura kinyume na msimamo wa
vyama vyao.
Sitta alisema kuwa kati ya wajumbe hao, mmoja alikubali kupiga kura na kusema yuko tayari hata kufukuzwa na chama chake.
“Sasa wale wanaotumia mbinu za ovyoovyo ili
mchakato huu usikamilike wanapoteza muda, maana ukizuia maji huku,
yanaelekea kwenye mkondo mwingine,” alisema Sitta.
Taarifa hizo zilionekana kuwalenga wabunge wa Viti
Maalumu, Maryam Msabaha na Mwanamrisho Abama ambao kwa nyakati tofauti
walithibitishwa kutafutwa ili apige kura.
“Kweli nimesumbuliwa sana na watu ambao siwezi
kuwataja na wananitaka nipige kura na wengine walifika mpaka nyumbani
lakini mimi siwezi kushiriki maana nikifanya hivyo dhamiri yangu
itanishtaki,” alisema Msabaha.
Naye Abama alisema kuwa alikuwa amepewa ilani na
viongozi wake kwamba anatafutwa ili akapige kura, hivyo aliamua kukaa
ndani kukwepa mtego huo.
Kauli hizo mbili tofauti zinauachia Ukawa maswali
magumu yanayohitaji majibu ili kubaini iwapo kuna usaliti wowote
umefanyika au la.
Wabunge wengine ambao wanaweza kukukumbana na
matatizo ndani ya chama hicho ni Mbunge John Shibuda (Maswa Mashariki),
Said Arfi (Mpanda Mjini) ambao walikiuka uamuzi wa Ukawa kutoshiriki
Bunge hilo.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa jana
alisema kuwa suala la wasaliti wa chama linatarajiwa kuzungumzwa kwenye
vikao vya ndani.
“Siwezi kulitolea uamuzi suala hilo, baada ya
kumaliza uchanguzi sasa litazungumzwa ndani ya vikao vya chama na
kutolewa uamuzi,” alisema Dk Slaa.
Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro
alisema kuwa Sitta alipaswa kuwataja wajumbe kutoka Ukawa waliokubali
kupiga kura, lakini hakufanya hivyo.
“Juzi amechukua kura zao na hawataji ni kina nani
wala walipiga kura kwa njia gani. Hata akijiongezea hizo kula mbili feki
bado BMK upande wa Zanzibar wanabakiwa na kura 145 tu na siyo 146,”
alisema Mtatilo.
Wanananchi waikataa rasimu
Naye Joseph Lyimo kutoka Manyara,
amesema kuwa baadhi ya wakazi wa mkoani humo, wamesema Bunge la Katiba
limepitisha rasimu ya Katiba bila maridhiano kwa baadhi ya wajumbe hivyo
kusababisha hofu ya kupatikana kwa katiba mpya itakayokidhi matakwa ya
wananchi.
Wakizungumza jana na mwandishi wa habari hizi,
wananchi hao walidai kuwa rasimu hiyo iliyopitishwa bungeni juzi
haikukidhi maoni yaliyotolewa kwenye tume ya Warioba kwani ibara 28
zimefutwa na kuwapo ibara mpya 42.
Mkazi wa mji mdogo wa Mirerani, Abdalah Mtengeti
alisema kwenye Tume ya Warioba wananchi walipendekeza mbunge awe na
ukomo wa madarakani kwa miaka 15, lakini sasa wabunge hao wameridhia
asiwe na mwisho wa utawala.
“Wananchi hawawezi tena kumwajibisha mbunge
waliyemchagua wao wenyewe kama walivyopendekeza awali pia hakuna ukomo
wa mbunge tena hivyo atatawala hadi mwenyewe aseme sigombei tena,”
alisema Mtengeti.
Mwenyekiti wa Bavicha Mkoa wa Manyara, Frank
Oleleshwa alisema rasimu hiyo ya wabunge haikujali maoni ya wananchi
kwani walipendekeza kufutwa kwa vyeo vya wakuu wa mikoa na wilaya
lakini, wabunge wameridhia.
“Pia wananchi walipendekeza kuwepo na Serikali
tatu ikiwamo kurudisha Tanganyika ili kuwapo na usawa wa nchi, lakini
wabunge wamegoma hilo na kuridhia Rais wa Zanzibar awe makamu wa pili wa
Rais,” alisema Oleleshwa.
CCM, CUF Zanzibar
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui na
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai walipozungumza na
gazeti hili kwa nyakati tofauti visiwani humo, Mazrui alisema kwamba
mambo yaliyopitishwa na Bunge la Katiba katika rasimu hiyo yanagongana
na Katiba ya Zanzibar iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010 ikiwamo suala
la mamlaka ya ugawaji mikoa aliyopewa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa
kushauriana na Rais wa Zanzibar.
Alisema Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano
utekelezaji wake utakuwa mgumu kwa baadhi ya mambo Zanzibar mpaka Katiba
ya Zanzibar ifanyiwe tena marekebisho na kabla ya kufanyika hivyo
lazima kuitishwe kura ya maoni kwa wananchi.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar,
Vuai Ali Vuai alisema kwamba kama viongozi wote watafanya kazi kwa
kuzingatia sheria na katiba, Serikali ya Umoja wa Kitaifa(SUK)
haitoyumba kwa sababu hakuna mshindi wala mshindwa baada ya rasimu ya
katiba kupitishwa.
“Matokeo ya kura ya rasimu ya katiba, ni ushindi
wa wazanzibari wote na watanzania kwa ujumla, na hakuna mshindi wala
mshindwa” alisema Vuai ambaye pia alikuwa mjumbe wa bunge maalum la
katiba.