Pamoja na changamoto za viwango duni vya ubora, ufaulu hafifu,
uhaba wa miundombinu, mazingira yasiyoridhisha ya kujifunza na
kufundishia; sekta ya elimu imeendelea kukumbwa na matatizo ya miongozo
duni inayosababisha ikose mwelekeo.
Matatizo haya ni kama vile kuanzishwa kwa
utaratibu wa kuweka kivuli (OMR) kwa shule za msingi, kupanga upya
viwango vya alama za ufaulu elimu ya sekondari (angalia matokeo ya
kidato cha nne 2012).
Mengine ni kufutwa kwa daraja sifuri na kuanzishwa
kwa daraja la tano (dalili ya kuficha aibu ya ongezeko la daraja
sifuri), kurejeshwa na kubatilishwa tena kwa sharti la ufaulu kidato cha
pili na kuanza kutumika kwa viwango vipya vya ufaulu vilivyokataliwa na
Bunge mwaka 2013.
Kimsingi matatizo haya sehemu tu ya matukio yanayotoa picha ya mkanganyiko uliopo katika mfumo unaoongoza elimu.
Taswira inayojitokeza hapa ni kuwa serikali
inatumia nguvu nyingi kuipamba sura ya elimu kwa kurekebisha matokeo na
kurahisisha ufaulu huku kwa ndani imeficha udhaifu mkubwa katika
ufundishaji, ujifunzaji, usimamizi wa shule, uwajibikaji na ubovu wa
elimu inayotolewa.
Hakuna haja ya kulumbana, kila Mtanzania anaguswa
na hali ya kuporomoka kwa kiwango cha elimu nchini. Umefika wakati
Serikali ichukue hadhari na kuachana na tabia ya kupuuza ushauri
unaotolewa na wadau wa elimu wanaosisitiza mambo ya msingi ya kufanyia
kazi ili kuboresha elimu.
Kwa mfano, kufaulisha wanafunzi ambao
hawakufundishwa kikamilifu ni kutengeneza kansa nyingine ambayo
italitafuna taifa letu kwa miaka mingi ijayo. Huu si uzalendo.
Tukemee tabia ya serikali kufanya amuzi wa mzaha
katika elimu na kuitaka isikilize vilio vya wananchi na kuwataka
watendaji kutanguliza mbele maslahi ya taifa.
Tunaitaka serikali na wabunge kuzingatia mambo muhimu yafuatayo katika bajeti ya elimu ya mwaka 2014/15.
Masilahi ya walimu
Kwa mujibu wa Takwimu za Chama cha Walimu (CWT),
hadi kufikia Desemba 2013 madai ya walimu ambayo hayakulipwa yalifikia
Sh 61bilioni. Ombi la CWT kwa serikali kuongeza mishahara ya walimu kwa
asilimia 50 limekataliwa na walimu wameendelea kupuuzwa.
Wakati huohuo serikali inatumia asilimia 43 tu ya
fedha za mishahara ya watumishi wa umma kuwalipa walimu ambao idadi yao
ni asilimia 67 ya wafanyakazi wote wa umma. Lakini serikali ilitumia
asilimia 57 ya fungu la mishahara ya umma kuwalipa wafanyakazi wa sekta
nyingine ambao ni asilimia 33 tu ya watumishi wote wa umma.
Serikali kupitia Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk
Shukuru Kawambwa, imeahidi kuwa italipa madai haya ya walimu katika
mwaka wa fedha 2014/15.
Hata hivyo, tunakumbusha kuwa haya ni madai ya
muda mrefu na ahadi kama hizi zimekuwa zikitolewa mara kwa mara pasina
utekelezaji.
Serikali itambue msemo usemao; “Uzuri wa mfumo wa
elimu unategemea ubora wa walimu wake”. Kwa mantiki hii haina budi
kuwathamini walimu kama kweli inakusudia kuboresha elimu.
Walimu wamekata tamaa na tusipokuwa makini hali
hii itaambukizwa kwa watoto wetu, familia zao na hatimaye sehemu kubwa
ya jamii pia itakata tamaa.
Uwekezaji katika elimu
Katika makubaliano ya mpango wa Elimu Kwa Wote
(EFA - 1990), ambayo Tanzania imeridhia, iliazimiwa kuwa uwekezaji
katika elimu katika kila nchi mwanachama ufikie walau asilimia 20 ya
bajeti nzima au asilimia sita ya pato la nchi husika.
Hata hivyo, hali imekuwa tofauti katika nchi yetu.
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita uwekezaji umekuwa ukishuka
badala ya kuongezeka.
Kwa mfano, mwaka 2008/09 bajeti ya sekta ilifikia
asilimia 20, lakini ikashuka mpaka asilimiua 18 mwaka 2010/11. Na
baadaye mwaka 2013/14 ikashuka hadi asilimia 17.3.
Tunazidi kuikumbusha serikali katika kipindi hiki
wanachoelekea kupanga na kupitisha bajeti, izingatie makubaliano haya
ambayo kwa hiyari ilitia saini na kuridhia kuwa itajitahidi kupanga
walau asilimia 20 ya bajeti yake kuu katika sekta ya elimu.
Upungufu wa ruzuku shuleni
Tanzania iliporidhia kutekeleza mipango ya
maendeleo ya elimu ya msingi na sekondari, lengo lilikuwa kuziwezesha
shule za umma kuwa na uwezo wa kujiendesha na kusimamia utoaji wa elimu
katika kiwango kinachostahili.
Utoaji wa ruzuku (Sh 10,000 kwa wanafunzi wa
msingi na 25,000 kwa sekondari) ulikuwa sehemu ya maazimio ya
utekelezaji wa makubaliano hayo.
Jambo la ajabu ni kuwa, taarifa za utekelezaji wa mpango na
azimio hili la utoaji ruzuku zinaonyesha kuwa kiasi ambacho kimekuwa
kikifika shuleni ni pungufu ya kilichopangwa.
Mathalani, katika awamu ya kwanza ya mpango wa
elimu ya msingi, wastani wa Sh 6,497 tu ndizo zilizofika shuleni badala
ya Sh10,000, huku wastani wa Sh 5,500 tu ndio ukifika shuleni wakati wa
utekelezaji wa awamu ya pili.
Hali hii inaendelea hata katika utekelezaji wa
awamu ya tatu. Wastani wa kiwango kilichofika shuleni mwaka 2012/13 ni
Sh 3,580 badala ya Sh 10,000.
Hali hii inazikumba pia shule za sekondari ambazo
nazo zinapokea wastani wa Sh 16,384 badala ya 25, 000 kwa mwaka kwa kila
mwanafunzi.
Ikumbukwe tu hapa kuwa viwango hivi ni wastani tu
wa hali ya utoaji ruzuku shuleni, lakini katika hali halisi ziko shule
nyingi ambazo hupata chini ya wastani wa 1,500 kwa mwaka kwa kila
mwanafunzi.
Bajeti ya elimu ya awali
Kwa kutambua umuhimu wa elimu ya awali katika
makuzi na maendeleo ya mtoto kitaaluma na kijamii, serikali imeazimia
katika mipango yake mbalimbali kufanya uwekezaji stahili katika eneo
hili.
Sera ya Elimu ya 1995, mtaalaa wa elimu ya awali
wa 2007, Dira ya Taifa 2025, Mpango wa Maendeleo Elimu ya Msingi (MMEM),
Mkukuta ni miongoni mwa mipango ambayo inaakisi azimio la serikali
kukuza elimu ya awali.
Pamoja na maazimio haya serikali imeshindwa
kutekeleza kwa vitendo makubaliano haya. Mathalani uwiano kati ya
wanafunzi wa awali na darasa umebaki kuwa 1:115 badala ya 1:25, uwiano
kati ya mwanafunzi kwa mwalimu pia ni 1:124 badala ya 1:25. (BEST 2013).
Tutakumbuka kuwa elimu ya awali haikugusiwa kabisa
katika mpango wa ruzuku katika awamu ya kwanza ya Mpango wa Maendeleo
Elimu ya Msingi (MMEM ). Na hata ilipogusiwa katika awamu ya pili, fedha
kwa ajili ya ruzuku elimu ya awali hazikutoka kabisa.
Katika awamu ya tatu, elimu ya awali imejumuishwa
katika bajeti ya ruzuku kwa shule za msingi. Hata hivyo, taarifa za
utekelezaji mipango zinaonyesha fedha kwa ajili ya elimu ya awali
hazijumuishwi katika fedha ya ruzuku inayokwenda shuleni.
Kuimarisha ukaguzi
Hali ya ukaguzi bado ni mbaya, uwezo wa serikali kukagua shule
hauridhishi. Takribani asilimia 19.1 tu ya shule zote za msingi ndizo
zinazokaguliwa kwa mwaka na asilimia 21.4 kwa shule za sekondari.
Wizara husika ijitahidi kuongeza bajeti ya ukaguzi
wa shule angalau idara iweze kukagua asilimia 50 ya shule zote za
msingi na sekondari kwa mwaka.
Kama bajeti ya ukaguzi itaongezwa tuna imani shule
zetu zitakaguliwa. Hivyo viwango vya ubora vitafahamika, upungufu
utafanyiwa kazi ili hatimaye tuweze kuwa na elimu bora.
Wakati tukiitaka serikali kuongeza bajeti ya
ukaguzi, tunasisitiza pia umuhimu wa kuwa na Wakala ya Ukaguzi wa Elimu
kama zilivyo sekta nyingine. Hii ndio njia pekee na sahihi ya kuboresha
ufanisi katika suala la ukaguzi.
Mazungumzo ya mchakato huu yamekuwepo kwa taribani miaka mitatu sasa lakini mafanikio yake hayaonekani. Itaendelea wiki ijayo

No comments:
Post a Comment