Friday, 31 October 2014

Mkapa atoa ya moyoni rais 2015

Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, amezungumzia mbio za kuwania urais wa 2015 kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), akitaja sifa za mtu anayepaswa kuteuliwa kuwa mgombea wake, ikiwamo ya kukubalika na kuuzika kwa jamii.

Amesema kukubalika na kuuzika kwa mtu katika siasa kunatokana na utendaji, haiba, wasifu na ushawishi wa mtu huyo ndani ya chama na serikalini na kwamba, umri siyo kigezo cha kuangaliwa ingawa siyo dhambi vijana wakajitokeza kujitosa katika kinyang’anyiro hicho.

Mkapa, ambaye anasifika kwa kuwa kiongozi jasiri na asiyemung’unya maneno, alisema hayo wakati akihojiwa na televisheni ya Citizen ya nchini Kenya, kwa njia ya simu.

Alikuwa akihojiwa juu ya kifo cha Rais wa Zambia, hayati Michael Satta, aliyefariki dunia, jijini London, nchini Uingereza Jumanne wiki hii.

Katika mahojiano hayo, Mkapa pia aliulizwa na mwandishi kuhusu Tanzania kutazamiwa kufanya uchaguzi mkuu mwakani huku mambo mengi yakisikika, hasa kwa wanaojitokeza kupitia CCM kutaka kuwania urais katika uchaguzi huo hadi wengine kufikia kuadhibiwa na chama.

Kabla ya kujibu, Mkapa alianza kwa kucheka na kisha akasema anachelea kupata jibu sahihi kuhusiana na swali aliloulizwa na mwandishi.


“…Ila niseme CCM ni chama kikongwe na kina hazina kubwa ya kutosha. Na Katiba ya chama chetu inaelezea kuhusu dhumuni la chama chetu, kubwa ikiwa ni kuhakikisha tunakamata dola, kuanzia serikali za mitaa mpaka serikali kuu. Sasa swali ni kwamba, dola inakamatwaje?” alihoji Mkapa.

Aliongeza: “Chama kama chama lazima muwe na mtu anayeuzika na kukubalika katika jamii kwa utendaji wake, haiba yake, wasifu wake (ndani ya chama na serikali).

“Lakini vile vile, ushawishi wake...Haya mambo ya umri na kadhalika, sisi hatukutazama wakati huo. Ila siyo dhambi vijana wakijitokeza. Maana yake hata wakati wangu, Rais wa sasa Mheshimiwa Kikwete na kina Lowassa walijitokeza. Na leo unaona Kikwete ndiye Rais.”


Alisema wakati wa utawala wake, viongozi wenzake wengi walihisi na kuamini kuwa hakuwa akimuunga mkono Rais Kikwete.

“Lakini mwandishi, nataka nikuhakikishie, hata kama mimi Ben Mkapa siko na Kikwete, mwisho wa siku wanachama ndiyo watakaosema wewe humtaki ila sisi tuachie huyo huyo...,” alisema Mkapa. 

Aliongeza: “Na hayo yalijitokeza mwaka 2005. Watu walimtaka Mheshimiwa Kikwete. Sasa mimi kuwa mwenyekiti wa chama hakunipi Mandate (mamlaka) ya kushindana na walio wengi. Na mliona (Kikwete) alishinda kwa asilimia kubwa kweli kweli”.

“Hivyo CCM ina taratibu zake na wanajua nani anafaa. Maana yake siasa hizi, tuhuma zingine za kipuuzi kweli kweli. Sasa mkiendekeza tuhuma, mwishowe mnakuta mnabaki bila chama. Na kwenye siasa mkianza kutuhumiana, hakuna wa kusimama...”

Alisema yeye binafsi, anaamini chama kitapata mtu safi, mwenye nguvu ya kukisaidia chama na serikali na kuendeleza yatakayoachwa na Rais Kikwete.

Mkapa alisema hakuna chama duniani kinachoona fulani atakivusha halafu kimwache na kusema kufanya hivyo, maana yake ni kukiua chama.

“Hivyo, hata sisi vyombo vyetu vya ndani vilikuwa vinatueleza kabisa kwamba, fulani yuko vizuri sana. Ila labda kuna aka katatizo. Sasa ako katatizo tunakafanyia kazi kwa maslahi ya chama na kwa maslahi ya huyo ajaye,” alisema Mkapa na kuongeza kuwa ana amini ndivyo ilivyo mpaka sasa.

Alisema tafiti zimefanyika na kwamba, anaamini wamesikika watu wakisema wanamtaka nani.

“Na wakati wangu mimi mgombea alikuwa ameshatungiwa nyimbo na watu mbalimbali wenye mapenzi naye. Hivyo, labda hata sasa yaweza kuwa hivyo...Waswahili walisema nyota njema huonekana asubuhi,” alisema Mkapa.

Aliongeza: “Nimalizie kama nilivyosema, ukongwe wa CCM na viongozi wake, naamini watapata mtu bora na mwenye nia njema na Taifa hili...”

Akijibu kuhusu wana CCM waliotajwa kwamba, anaamini yupo mmoja au wawili, ambao ameona wanaweza ama kufuata nyayo zake au za Mwinyi au za Mwalimu Nyerere au za Rais Kikwete, kwanza alianza kwa kucheka.

Baada ya kicheko, Mkapa alisema Tanzania kuna Kamati ya Maadili na kwamba, yeye na wenzake hivi sasa kikatiba ni wazee washauri, hivyo akasema vikao vya chama ndivyo vitakavyowaongoza na baada ya hapo, nao wanaenda na mtu huyo huyo.

Makada wa CCM waliowahi kutuhumiwa kuanza kampeni za kuwania urais mwaka 2015 kabla ya kuzuiwa na chama kupitia Kamati yake Ndogo ya Udhibiti na Nidhamu kujihusisha na suala hilo kwa miezi 12, huku mienendo yao ya kisiasa ikifuatiliwa, ni pamoja na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.

Wengine ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa; Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira.

Yumo pia aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, ambaye ni Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, pia hivi karibuni alikaririwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) akitangaza nia yake ya kuwania urais 2015. Mwingine aliyekwisha kutangaza nia ya kuwania urais mwakani ni Mbunge wa Nzega, Dk. Hamis Kigwangalla.

KUHUSU USHIRIKIANO WA VYAMA VYA UPINZANI (UKAWA)

Akijibu swali kuhusu ushirikiano uliosainiwa na vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD wa kusimamisha mgombea mmoja katika chaguzi, kuanzia ngazi ya serikali ya mtaa hadi urais kama ilivyokuwa kwa Kenya, Mkapa alisema bado hajajua
sera za vyama hivyo na namna makubaliano yao yalivyo.

Alisema pia bado hajaelewa kama inawezekana kuufananisha ushirikiano wa vyama hivyo na muungano wa Coard na Jubilee uliokuwapo nchini Kenya.

“Otherwise I'd like to wish them all the best (vinginevyo ningependa kuwatakia kila kheri),” alisema Mkapa na kumfanya mwandishi aangue kicheko.

KIFO CHA RAIS SATTA

Akimzungumzia hayati Rais Satta, Mkapa alisema hakuitwa “King Cobra” kimakosa, bali alistahili kutokana na uwezo aliokuwa nao ama wa kimaamuzi au wa kimsimamo.

“Nina hakika sana kwamba Wazambia na sisi kama Mataifa ya Afrika tutamkumbuka daima ndugu Satta. Satta daima alikuwa kwa ajili ya watu wake na Bara letu kwa jumla. Alisema na kusimamia kile alichokiamini kuwa ni cha kweli na chenye mafanikio, Satta ataendelea kuwa kiongozi mzuri daima,” alisema Mkapa.

Aliongeza: “Hivyo, maumivu yanayotukabili kwa kumpoteza Mzee Nyerere, Mzee Nkrumah, Mzee Mandela, Mzee Kenyatta ni sawa na yale yanayotukabili leo tunapomjadili Mheshimiwa Satta (Inatosha kusema kwamba tumempoteza shujaa mwingine katika Bara letu) Naitakia roho yake mapumziko ...”

Akijibu swali namna anavyoziona siasa za Afrika akiwa Rais mstaafu, Mkapa alisema ni kawaida na hana jambo kubwa la kusema japo kuna mengi yanatokea, ambayo mengine ni ya hovyo.

“Mathalan, Waafrika wazee wetu, walipigania sana ukombozi wetu. Ila nadhani wengi bado kuna watu wana matatizo na wanahitaji kukombolewa kifikra,” alisema Mkapa.

Aliongeza: “Maana yake kuna wenzetu wanatumika pasipo kujua na kusababishia nchi zao kuingia katika matatizo, kama vita na wengi wao wameanza kujuta”.
“Hivyo, ni lazma ifikie mahali watu waweze kujitambua na kujua ni yepi malengo mema kwa Bara letu ni yepi tunashinikizwa...” aliongeza kusema Mkapa.

Lowassa amuombea radhi Sitta kwa Kanisa

Wakati Katiba iliyopendekezwa na Bunge Maalum la Katiba (MBK) ikitarajia kuingia katika hatua ya kura ya maoni mwakani, Waziri Mkuu Mstaafu, Edward Lowassa, ameibuka na kuliomba radhi Kanisa Katoliki kufuatia mgongano iliyojitokeza kati ya kanisa hilo na baadhi ya viongozi serikali na wa Bunge hilo.

Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli, aliomba msamaha huo wakati akitoa salamu zake katika sherehe za maadhimisho ya miaka 50 ya Kanisa Katoliki Jimbo la Mahenge, mkoani Morogoro.

Alisema Kanisa Katoliki lina mchango mkubwa katika kudumisha amani na mshikamano nchini, hivyo mambo yaliyojitokeza yanapaswa kusamehewa.

“Najua hivi karibuni tumewaudhi, lakini mimi naomba mtusamehe bure tu, kama vile mzazi anavyomsamehe mtoto wake anapokosea,” alisema Lowassa na kuongeza kuwa Kanisa Katoliki ni muhimu katika maendeleo ya nchi.

Ingawa Lowassa hakueleza kwa undani tofauti zilizojitokeza kati ya Kanisa hilo na baadhi ya viongozi wa serikali, lakini  wakati BMK likiendelea, taasisi za dini zilisambaza waraka uliosainiwa na viongozi wake ukilikosoa Bunge hilo kwa mambo mbalimbali ikiwamo kuendelea kujadili rasimu bila maridhiano kutokana na wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kususia.

Kadhalika, viongozi wa madhahebu hayo ya Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Baraza la Kikiristo Tanzania (CCT) na Makanisa ya Pentekoste Tanzania (PCT), walilikosoa BMK kwa kupuuza maoni ya wananchi yaliyokuwa katika Rasimu iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Waraka huo ulisababisha aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, kujiweka katika wakati mgumu kwa kuzua mgogoro dhidi ya viongozi wa dini ya Kikristo, baada ya kuita waraka huo kuwa ni wa kipuuzi na wa hovyo hovyo.

Sitta ambaye alitoa kauli hiyo Oktoba Mosi mwaka huu, alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa waraka wa maaskofu una lugha ya Ukawa, ingawa maaskofu kwa upande wao waliueleza kuwa ni waraka wa kinabii, kwa ajili ya maslahi mapana ya nchi.

Sitta alitoa kauli ya kuuponda waraka huo bungeni alipokuwa akielezea mwenendo wa upigaji kura za kupitisha ibara na sura za rasimu ya katiba iliyopendekezwa kabla ya upigaji wa kura na wakati wa kutangaza matokeo, akisema watu wa Mungu kama maaskofu hawawezi kutoa waraka kama huo na kudai kuwa amekuwa akituhumiwa kwenye mitandao kwamba anadharau maaskofu.

“Nimalizie na viongozi wangu wa kiroho…mababa zangu maaskofu, natuhumiwa sana kwenye mablog kwamba nadharau maaskofu. Wakiwa na matendo kama hayo hao baadhi ya maaskofu itabidi tuendelee kuwadharau,” alisema na kuongeza:

“Ninao waraka huu ambao umelazimishwa kutumwa katika makanisa. Sioni utukufu wa Ukristo katika waraka huo. Huu waraka unamwamuru Rais airudishe Tume ya Mabadiliko ya Katiba.”

 Kuna Ukristo hapa?” alihoji na kuendelea: “Waraka huu unamlazimisha Rais asitishe mchakato wa Bunge Maalum…tangu lini watu wa kiroho wanatoa maagizo ya kisiasa? Hii sio haki hata kidogo…kuna Ukristo hapa? Waraka una lugha za wale Ukawa tuliowazoea.”

“Hivi kweli maaskofu wa Kikristo wanaweza kusema kwamba Wizara ya Katiba na Sheria irudishe tovuti ya Tume ya Jaji Warioba na kuirejeshea nyaraka zake zote ili wananchi wasome na kujifunza?” alihoji Sitta.

“Kwamba maoni ya wananchi hayawezi kufutwa na kudharauriwa na chama tawala, hivyo basi Bunge la Katiba lijadili na kuboresha tu rasimu ya katiba na si kubadilisha,” alisema Sitta.

“Waraka huu kwa shinikizo la maaskofu umesambazwa kwenye makanisa na kusomwa. Mimi nasema kama Mkristo, tukianza kuruhusu nchi yetu kutoa nyaraka hizi za kisiasa zisomwe makanisani kwa kudai huo ni msimamo wa maaskofu, basi nchi hii tutaipeleka kubaya.

“Na mini kama mtu mzima lazima nionye kuhusu tabia hii, ukizingatia nchi hii haina dini, hawa baadhi ya maaskofu ambao walikusanywa Dar es Salaam na makundi yale yale yanayohusishwa na Ukawa, kama wao ni wanachama wa siri wa vyama vya siasa vinavyochukia CCM wajitokeze waziwazi,” alisema Sitta.

Sitta aliendelea kunukuu waraka huo kwamba kuna askofu mmoja ameapa kwamba atawaelimisha waumini wake ili siku za usoni wawashughulikie viongozi kama mimi (Sitta). Nasema aendelee, lakini Mungu anaona yote yaliyo moyoni mwetu.”

Baada ya Sitta kutoa kauli hiyo, Askofu wa Jimbo la Katoliki la Bunda, Mhashamu Renatus Nkwande, alisema matamshi ya Sitta yanaonyesha anavyohangaika kualalisha kilicho haramu.

Alisema kitendo cha Sitta kuendesha BMK kwa kukejeli wajumbe wenzake walioondoka bungeni (Ukawa) na wajumbe walioandaa rasimu ya pili kwenye Tume ya Katiba Mpya chini ya Jaji Joseph Warioba, ni jambo la aibu ambalo halivumiliki, na ndiyo maana walitoa waraka wa kutokubaliana nacho.

“Kwa kweli Sitta ametutukana, ametafuta ubaya kwa viongozi wa dini, kwa kuwa tumesema ukweli ? Sisi tulikuwa tunatimiza wajibu wetu kwa Wakristo …tulizungumza kutokana na hitaji la wakati, na ulikuwa waraka wa unabii,” alisema.

Viongozi wengine wa kanisa Katoliki waliojibu kauli za Sitta ni Makamu Mwenyekiti wa TEC, Askofu Severine Niwemugizi na Askofu Msaidizi wa Jimbo la Bukoba, Dk. Methodius Kilaini, ambaye alinukuliwa akisema kuwa Sitta amelewa madaraka.

JK: Watendaji wakuu wananikwamisha

Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete amewatuhumu baadhi ya watendaji wa serikali yake kuwa ni kikwazo katika kufanikisha masuala mbalimbali ya maendeleo kutokana na urasimu usiokuwa wa lazima katika kutoa huduma kwa wananchi.
Akifungua kongamano la miaka 10 ya Tume ya Utumishi wa Umma Dar es Salaam jana, Rais Kikwete alikemea na kulaumu tabia ya baadhi ya watendaji hao wa Serikali ambao wamekuwa wakikwamisha kwa makusudi kasi ya viongozi wa kisiasa ya kuleta maendeleo.
“Katika utendaji wa baadhi ya watendaji wakuu wa Serikali limekuwa ni tatizo na wamekuwa wakikwamisha sana kasi ya utekelezaji wa haraka wa malengo ya kisiasa,” alisema.
“Mara nyingine, viongozi wa kisiasa wamekuwa mbele kimtazamo kuliko watumishi wa umma, hili limekuwa tatizo sana katika utekelezaji wa malengo kwa haraka,” alisema Kikwete.
Alisema kumekuwa na malalamiko kwa makatibu wakuu wa wizara kutoka kwa wawekezaji ambao huwachelewesha kwa makusudi kwa visingizio vya kufuata utaratibu.
Alisema katika kufuatilia, amekuwa akilazimika kuingilia utendaji wa baadhi ya wizara ili kuhakikisha mambo yanakwenda na mara nyingine urasimu huo umekuwa ukifanywa kwa makusudi ili kuwachosha wawekezaji na ‘kuwatoa upepo’ kwa manufaa binafsi.
“Haya ni malalamiko makubwa sana na yanatoa picha mbaya kwa nchi yetu…watendaji wa namna hii ni lazima wabadilike, ninahitaji kuona mabadiliko makubwa kwa kupitia Tume ya Utumishi ambayo inatakiwa kukaa na hawa watumishi na kuwapa mafunzo ya kiutendaji yanayoendana na mahitaji ya sasa,” alisema.
Abeza zawadi ya uprofesa
Akizungumzia utaratibu wa upandishwaji vyeo, Rais Kikwete alisema ni muhimu weledi ukazingatiwa na utaratibu uliowekwa ukaheshimiwa, kwamba lazima wafanyakazi wapandishwe vyeo na madaraja ndani ya kipindi kilichowekwa, ambacho ni miaka mitatu.
Alisema kumekuwa na malalamiko kwa wafanyakazi wengi wa Serikali kutopandishwa vyeo kwa muda mrefu na hata wanapopandishwa vyeo mabadiliko ya mishahara kuendana na vyeo na madaraja mapya hayafanyiki kwa wakati.
Alieleza kwamba utaratibu unaotumika katika vyuo vikuu wa namna ya kuwapata wahadhiri wasaidizi, wahadhiri, maprofesa ni wa wazi na ni mfano wa kuigwa kutokana na namna unavyofanyika, kwa kutoa mafunzo kisha kuyathibitisha na kumpandisha mhusika daraja.
“Vyuo vikuu wana ngazi wanazotakiwa kuzipitia na mafunzo maalumu hadi mtu anakuwa profesa. Siyo honorary professor (uprofesa wa heshima) niliopewa mimi nilipokwenda China…walinishtukiza. Nilifika pale wakanipiga na uprofesa, nikasema haya sasa makubwa! (kicheko),” alisema.
Alisema matatizo ya upandishwaji vyeo yasipotatuliwa kwa wakati ni tatizo kubwa kwa Serikali hasa unapokutana na vyama vya wafanyakazi vyenye nguvu kama Chama cha Walimu na wanapofikia hatua ya kusema wanagoma, unalazimika kuwaangukia.
Alisema suala la mtumishi kupandishwa cheo ni haki yake ya msingi kazini hivyo hatarajii kusikia matatizo ya malalamiko ya watumishi kutopanda vyeo kwa wakati.

Ukawa na dhana ya nguvu ya mnyonge au ‘zamu yetu kula’

Dar es Salaam. Kwa jumla, kuungana ni jambo jema kwani muungano huongeza nguvu. Muungano ni silaha ya mnyonge dhidi ya mwenye nguvu.
Ni kwa sababu hii, tumekuwa tukipigania umoja wa Afrika ili kujenga nguvu ya pamoja dhidi ya mabeberu wa mataifa ya Magharibi tukiamini kwamba bila nguvu moja mataifa ya Afrika hayataweza kuukabili ubeberu wa mataifa haya.
Tunao msemo maarufu usemao nguvu ya mnyonge ni umoja na hivi ndivyo waasisi wa mataifa ya Afrika walivyofanya katika kumfukuza mkoloni.
Bila kujali tofauti zao za kikabila na vinginevyo, wananchi wa Afrika waliunganisha nguvu na hatimaye pamoja na silaha zao duni, wakafanikiwa kumfukuza mkoloni katika ardhi ya Afrika.
Katika uwanja wa siasa, vyama vya siasa huungana kwa sababu mbalimbali lakini sababu tatu ni za msingi zaidi. Mosi, huungana pale ambako hakuna chama kinaibuka na ushindi wa moja kwa moja katika uchaguzi ulio na ushindani mkali.
Katika mazingira haya, inakuwa hakuna chama kinachoweza kuunda serikali imara peke yake bila kushirikisha kingine kwa sababu hakitaweza kupitisha sera au sheria yoyote bungeni.
Hivi ndivyo vyama vya Conservatives na Liberal Democrats vilivyoungana huko Uingereza baada ya vyama vikuu nchini humo vya Labour na Conservatives kushindwa kupata ushindi ambao ungekiwezesha chama kimojawapo kuunda serikali na kupitisha sera bungeni bila msukosuko mkubwa.
Hivi ni vyama ambavyo vina itikadi na msimamo tofauti kabisa kifalsafa na ilibidi viongozi wake wakae saa nyingi kukubaliana programu ya kutekeleza kabla hawajakubaliana kugawana nafasi za uongozi.
Kiongozi wa Liberal Democrats, Nick Cleggy alimshinikiza David Cameroon akubaliane na masharti ya kulegeza misimamo mikali ya chama chake kuhusu sera ya uhamiaji na hifadhi ya jamii kabla hajakubali kuingia naye ubia kuunda serikali.
Cameron amekiri mara kadhaa kwamba alilazimika kulegeza msimamo kuhusu sera mama za Conservatives ili kufanikisha kuwashawishi Liberal Democrats kuunda nao serikali vinginevyo Nick Cleggy angeunda serikali na Gordon Brown wa chama cha Labour.
Ni katika mazingira ya chama kimoja kushindwa kupata ushindi wa wazi ambayo yalivilazimisha vyama hasimu vya CUF na CCM kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) Zanzibar.
Pamoja na kwamba SUK iliundwa kama njia sahihi ya kuepusha shari na vita visiwani, msingi wa serikali hiyo ni ukweli kwamba hakuna chama chochote kati ya hivi viwili chenye uwezo wa kuunda serikali imara kwa sababu ushindi wa chama chochote huwa ni mwembamba. Hata hivyo, hatujui ni kwa kiwango gani vyama vya CUF na CCM huko Zanzibar vilikubaliana kutekeleza programu ya pamoja inayotokana na sera za vyama hivyo viwili.
Sababu ya pili ya vyama kuungana ni kuunganisha nguvu katika jitihada za kumwondoa adui anayefanana.
Kwa mfano, huko Zanzibar kabla ya mapinduzi ya mwaka 1964, vyama kadhaa viliungana katika jitihada za kuuondoa utawala wa Sultani uliokuwa unaendeshwa kibaguzi. Kwa hiyo, adui hapa alikuwa Sultani na ubaguzi wake wa rangi.
Sababu ya tatu ni pale vyama vinapounganisha nguvu ili kushinda uchaguzi kwa kutambua kwamba vikiingia kwenye uchaguzi kimoja, kimoja havitaweza kushinda kutokana na nguvu kubwa aliyonayo mshindani wao.
Hata hivyo, kushinda uchaguzi hakuwezi kutokana na kuunganisha nguvu ya kiuongozi pekee. Ni lazima kuunganisha pia nguvu ya kiitikadi, kifalsafa na kisera ili kuweza kujipambanua kwa wananchi.
Muungano wa kisera ni muhimu ili kuweza kutabirika tabia za wagombea watakapokuwa madarakani. Aidha, ni programu ya kisera inayoweza kuongoza kuchagua mgombea anayefaa zaidi kushika usukani wa utekelezaji wake baadaye.
Muungano wa vyama vinavyounda Ukawa umepokewa kwa shangwe kubwa. Furaha hii inatokana na msingi nilioueleza hapo awali kwamba wanyonge wakiungana hupata nguvu ya ajabu hata ya kuweza kuangusha milima.
Kwa hiyo, watu ambao wamekuwa wakisubiri utawala wa CCM kuanguka wanaamini kwamba kwa muungano huu angalau vyama vya upinzani vitafuta unyonge.
Nami naungana na Watanzania wengine kuwapongeza viongozi wa vyama ya Chadema, CUF, NCCR na NLD kwa ujasiri na uthubutu waliouchukua katika kujaribu kushirikiana katika chaguzi mbalimbali zijazo.
Lakini tunapowapongeza Ukawa, ni vizuri kutambua kwamba kuunganisha nguvu kama walivyofanya ni hatua moja tu inayopaswa kuanzisha hatua nyingi huko mbele. Hatua muhimu inayofuata sasa ni kujipambanua kwa wananchi kiitikadi, kifalsafa na kisera.
Kwa bahati viongozi wa sasa wa vyama vilivyoungana siyo watu wanaoamini katika mambo ya itikadi na falsafa.
Hawa ni viongozi ambao huitwa ‘wayakinifu’ (pragamatists). Myakinifu ni kiongozi anayeamini katika kinachowezekana leo na haongozwi na falsafa bayana ya kisiasa.
Kwa hiyo kiongozi yakinifu atambeba yeyote anayeona anafaa na huwezi kumuweka katika mrengo wowote kiitikadi. Kimsingi, hii ndiyo aina ya viongozi tulionao sasa tangu Mwalimu Julius Nyerere alipoondoka.
Ndiyo maana tumekuwa Taifa ambalo si la kijamaa, wala kiliberali wala kibepari. Tupotupo tu maadamu siku zinakwenda.
Pamoja na uyakinifu wao, bado naamini kwamba Ukawa watahitaji programu ya pamoja ya kisera. Hii ni hatua muhimu ili kutoa nafasi kwa wananchi kupima aina ya serikali watakayounda kama watashinda katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Bila msimamo yakinifu wa kisera, ni rahisi kutofautiana kwa sababu ya kukosa msingi wa kugawana madaraka. Bila sera yakinifu, utakapofika wakati wa kugawana nafasi za kugombea na hatimaye katika kuunda Serikali watalazimika kuzingatia sifa za kuchagulika na umaarufu badala ya sifa za kiuwezo.
Nakumbuka mwaka 2005 palipokuwa na jitihada za kuunda ushirikiano kama huu wa sasa, nilipewa jukumu la kufanya utafiti kujua nani alikuwa anakubalika zaidi katika Jimbo la Ubungo kati ya mgombea wa Chadema (John Mnyika) na mgombea wa CUF (marehemu mama Minja).
Niliandaa hojaji na nikaligawa katika kata zote za Jimbo la Ubungo kwa kutumia sampuli iliyopatikana kwa njia ya bahati nasibu. Matokeo yalionyesha kwamba Mnyika alikuwa anakubalika kwa mbali dhidi ya wagombea wengine wa upinzani.
Hata hivyo, katika kikao cha kujadili matokeo hayo, wawakilishi wa CUF waliyakataa na kunituhumu kwamba nilikuwa napendelea chama changu na huo ndiyo ukawa mwanzo wa ushirikiano kusuasua na hatimaye kusambaratika kabisa kabla ya kampeni kuanza.
Yote hii ni kwa sababu tuliwekeza zaidi kwenye kugawana wagombea lakini hatukuwekeza kabisa katika ushirikiano wa kisera.
Ninachojaribu kusema hapa ni kwamba, muungano wowote endelevu wa vyama vya siasa Tanzania, lazima uwe wa kuunganisha nguvu za wanyonge dhidi ya mabavu ya chama dola cha CCM.
Muungano wa namna hii lazima uwaunganishe kisera Watanzania na ndiyo unaopaswa kuwa msingi wa kugawana vyeo.

Lipumba: Kwanza CCM ing’oke, ruzuku baadaye

Dar es Salaam. Wakati Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi akisema suala la ruzuku na viti maalumu ni changamoto kwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema hicho si kipaumbele.
“Tunachokitaka ni kuunganisha nguvu zetu ili kuhakikisha tunaing’oa CCM madarakani kwanza, masuala mengine kuhusu ruzuku tutaweka utaratibu maalumu baadaye,” alisema.
Profesa Lipumba ambaye pia ni mwenyekiti mwenza wa Ukawa, alisema hayo Dar es Salaam jana alipokuwa akiwaeleza waandishi wa habari maazimio ya Baraza Kuu la Uongozi la Taifa la CUF lililokutana Jumatatu na Jumanne iliyopita.
“Wenzetu Kenya waliweza kuungana na kuhakikisha wanaking’oa chama tawala madarakani, lakini sasa kwa hapa mkiungana na kuwa chama kimoja ni lazima msajili chama chenu, sasa tunachokitaka ni kushirikiana tu kwanza,’’ alisema.
Alisema suala la ruzuku na uteuzi wa viti maalumu siyo lengo kuu la Ukawa inayoundwa na vyama vinne; CUF, Chadema, NCCR-Mageuzi na NLD kwa kuwa linajadilika. Alisema jambo la msingi hivi sasa ni ushirikiano wa amani.
Alisema kinachotakiwa kwa viongozi wa Ukawa ni kuaminiana kwanza ili kulinda muungano huo ambao alisema umeshaanza kukitikisa chama tawala, CCM.
Maazimio ya Baraza Kuu
Alisema Baraza hilo lilisisitiza umuhimu wa kuaminiana miongoni mwa vyama washirika katika ngazi zote ili kudumisha umoja huo na kufikia lengo la kuitoa CCM madarakani.
“Baraza limetaka uwepo utaratibu mzuri na wa wazi utakaoonyesha mambo ya msingi ambayo vyama vinavyounda Ukawa vimekubaliana. Utaratibu huu uwafikie viongozi wa ngazi zote za chama ili kuhakikisha jukwaa la Ukawa linatumika kwa lengo na dhamira iliyopo ndani ya hati ya makubaliano ambayo ni kuing’oa CCM madarakani,” alisema.
Kuhusu uchaguzi wa Serikali za Mitaa Profesa Lipumba alisema Baraza limetaka sheria irekebishwe ili uchaguzi wa diwani ufanyike pamoja na wa viongozi wa mitaa, vijiji na vitongoji kwa wakati mmoja, kwa vile diwani ndiye kiongozi mkuu wa kuchaguliwa wa kata.
Baraza hilo pia limetaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iratibu na kusimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa na utengenezwe utaratibu ambao utaifanya Tume hiyo kuwa huru kuwezesha chaguzi zote zijazo kufanyika kwa uhuru na haki.
“Taarifa za Tume zilieleza kuwa itaandikisha wapigakura mpaka kwenye ngazi ya vijiji na vitongoji, kwa hiyo uchaguzi wa Serikali za Mitaa usubiri mpaka daftari la kudumu la wapigakura likamilike na ndilo litumiwe kwenye uchaguzi huo,” alisema.
Akizungumzia Katiba Inayopendekezwa, Profesa Lipumba alisema Baraza Kuu la CUF, limesikitishwa kwa kiasi kikubwa na kitendo cha kupitishwa na kutangazwa kwa katiba hiyo na Bunge la Katiba lililoongozwa na Samuel Sitta akisema halikuzingatia sheria na taratibu za mabunge ya Jumuiya ya Madola.
“Ni ukweli usiofichika kwamba mchakato mzima wa kupitisha katiba haukuwa na mwafaka wa kisiasa, kanuni za uendeshaji wa bunge hilo zilikiukwa na Katiba yote inayopendekezwa haikupigiwa kura ya mwisho,” alisema
Profesa Lipumba alisema, katika vikao vya ushauriano na viongozi wa vyama vya siasa vinavyounda Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), Rais Jakaya Kikwete alikubaliana na viongozi hao kuwa mchakato wa kupata Katiba Mpya, hususan kura ya maoni uahirishwe mpaka baada ya Uchaguzi Mkuu 2015.
“Mwanasheria wa Serikali alitangaza kura ya maoni Machi 30, Rais akiwa China alisema Aprili, yaani tayari tarehe imeshatangazwa kabla hata ya daftari la wapigakura kukamilishwa,” alisema.
Alisema baraza hilo pia limesikitishwa na utaratibu unaofanywa na NEC juu ya uboreshaji wa Daftari la kudumu la Wapigakura akisema hadi sasa hatua za uandikishaji hazipo wazi na wadau wengi hawana taarifa za kutosha juu ya nini kinaendelea.
Alisema takwimu za Sensa ya Watu na Makazi 2012, zinaonyesha kuwa kuna vijana zaidi ya milioni 4.6 ambao watafikisha umri wa kuwa wapigakura kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 lakini bado hawajapewa fursa ya kuandikishwa huku wananchi wengi wakiwa wameshapoteza vitambulisho vya kupigia kura.
Alisema Juni, 19 mwaka huu, Nec, ilitangaza kufuta matumizi ya vitambulisho vya kupigia kura vya sasa na badala yake itatumia teknolojia mpya ya Biometric Voter Registration (BVR), ikiwa ni maboresho ya daftari la kudumu la wapiga kura na kwamba Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva alinukuliwa akisema katika Kura ya Maoni ya Katiba na Uchaguzi Mkuu, mpigakura atatumia kitambulisho kipya baada ya kuandikishwa upya katika mfumo huo na si vinginevyo.
Pia alisema Baraza Kuu linalaani vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu na sheria vinavyoendelea kufanywa na Serikali kwa kulitumia Jeshi la Polisi.
Alitoa mfano wa masheikh waliokamatwa Zanzibar na kuhamishiwa Dar es Salaam na kufunguliwa kesi akisema walijitokeza mbele ya Mahakama na kusema waziwazi kwamba wamefanyiwa mateso na vitendo vya kinyama lakini hakuna hatua zilizochukuliwa ikiwamo kupelekwa hospitali.
Kadhalika, alisema baraza hilo limepokea kwa mshangao taarifa za utoaji wa uraia unaofanywa na Serikali kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi. Alisema uamuzi wa kuwapa uraia wakimbizi katika majimbo yanayoongozwa na wabunge wa vyama vya upinzani ni mbinu ya kudhoofisha upinzani kwa kuwa wakimbizi wanaopewa uraia wanahamasishwa kuwa wachague chama tawala.
Kuhusu ardhi alisema: “Pamoja na Tanzania kuwa na ardhi ya kutosha kwa raia wake, ugawaji wa mapande makubwa ya ardhi kwa wawekezaji yataleta mtafaruku wa uvunjifu wa amani na kuwafanya raia wazawa kuwa maskini wa kudumu,’’ alisema Profesa Lipumba.
Kuhusu maradhi hatari ya ebola, Profesa Lipumba alisema Baraza Kuu limeitaka Serikali kuwa makini ili usiingie nchini akisema limesikitishwa na taarifa ya kwamba mpaka sasa nchi haina vifaa vya kuthibitisha kuwapo kwa vimelea vya ebola.

Monday, 27 October 2014

KNCU wamlaumu mrajisi wa vyama

Moshi. Chama Kikuu cha Wakulima wa Kahawa Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU), kimemjia juu mrajisi wa vyama hivyo nchini kwa kile ilichodai kukwamisha ustawi na maendeleo yake.
Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na mwenyekiti wa KNCU, Maynard Swai wakati akisoma hotuba yake katika mkutano mkuu maalumu ulioitishwa kwa shinikizo la mrajisi huyo, Dk Audax Rutabanzibwa.
Licha ya kupokea lawama hizo, Dk Rutabanzibwa aliyekuwa mwenyekiti katika mkutano huo hakuweza kujibu malalamiko yaliyoelekezwa kwake na mwenyekiti huyo.
Mwenyekiti huyo aliwaachia wajumbe wa mkutano huo kufanya uamuzi kwa njia ya kura kama bodi ya uongozi iendelee au ing’oke ambapo kura 83 zilikataa na 68 zikitaka ing’oke.
Swai alisema ofisi ya mrajisi huyo imekuwa kikwazo cha maendeleo kwa KNCU .
“Mfano, shamba la Garagagua lilitakiwa kuuzwa Mei 2014, wajumbe mlisharidhia lakini kutokana na ukiritimba wa ofisi ya mrajisi imekwama,” alisema Swai. Swai aliitaja mipango mingine kuwa ni ujenzi wa hosteli ya kisasa na hoteli kwenye eneo la makao makuu ya KNCU.
“Sina nia ya kuifundisha au kuikumbusha ofisi ya Mrajisi wajibu wake kiutendaji lakini ina wajibu wa kushauri na kusimamia ushirika ili uendelee kushamiri nchini kwa manufaa ya wanachama,”alisema.
Lakini Swai alisema hata tume mbalimbali za uchunguzi zilizotumwa KNCU katika kipindi kifupi cha miaka miwili na Mrajisi, hazijawahi kutoa mrejesho wa matokeo ya uchunguzi huo.
“Kifungu 57(1) cha sheria namba 6 ya Ushirika ya mwaka 2013 imeweka bayana kuwa ikiwa kuna uchunguzi au ukaguzi umefanywa dhidi ya chama cha Ushirika, Mrajisi atapaswa kutoa matokeo ya uchunguzi huo,”alisema Swai.
KNCU kimeshangazwa pia na hatua ya Mrajisi kutoamini ukaguzi uliofanywa na COASCO ambacho ni chombo cha Serikali kuhusu kiasi cha hasara ambayo KNCU ilipata wakati wa mdororo wa uchumi duniani mwaka 2008.
Katika hesabu hizo, KNCU ilionyesha kupata hasara ya zaidi ya Sh765 milioni wakati uhakiki uliofanywa na hazina ulionyesha KNCU kilipata hasara ya Sh250 milioni.
“Mrajisi aliagiza kufuatiliwa kwa tofauti hii huku akionesha kutokuwa na imani na hesabu zilizokaguliwa na COASCO jambo ambalo linashangaza kama Serikali haiwezi kuamini kazi iliyofanywa na chombo chake,” alisisitiza Swai.
Swai alisema tofauti hiyo ilifanyiwa kazi na KNCU na taarifa kurejeshwa kwa Mrajisi lakini hawajaona mawasiliano yoyote yanayoonyesha ufuatiliaji wa suala hilo hiyo inadhihirisha namna Mrajisi alivyoshindwa kuitetea KNCU.
Mwenyekiti huyo alipigilia msumari zaidi pale alipodai hata mkutano huo mkuu maalumu ulioitishwa na Mrajisi ni batili na unakiuka kifungu namba 55(9) cha sheria ya Ushirika.
“Sheria iko wazi kuwa hesabu zikishawasilishwa na kujadiliwa na kisha kupitishwa na mkutano mkuu, uamuzi wao (wajumbe) kuhusiana na hesabu hizo unakuwa wa mwisho,”alisema Swai.
Swai alisema ilikuwa ni batili kisheria, kwa Mrajisi kushinikiza kuitishwa kwa mkutano huo ili kujibu hoja za ukaguzi ambazo alidai hazikupatiwa majibu ya kutosha na KNCU wakati wenye mali walisharidhika na majibu hayo.

Kiwanda cha matrekta kujengwa Tanzania

Warsal, Poland. Kampuni ya Ursus ya Poland imesema ina mkakati wa kujenga kiwanda cha kutengeneza matrekta Tanzania kwa kushirikiana na kampuni ya Suma JKT.
Rais wa Bodi ya Ursus, Karol Zarajczyk alisema hayo jijini Warsaw jana wakati Waziri Mkuu Mizengo Pinda alipokutana na wafanyabiashara wenye nia ya kuwekeza Tanzania.
Zarajczyk alisema wanataka kujenga kiwanda hicho kwa kuwa wametambua Tanzania ina fursa ya kufungua milango ya kibiashara kwa nchi jirani za Afrika Mashariki na Kati.
Alisema lengo jingine la kampuni hiyo inayotengeneza matrekta ni kutoa mafunzo kwa wakulima ya jinsi ya kutunza matrekta hayo, ili waone umuhimu wake katika sekta ya kilimo.
“Barani Afrika tulianza kupeleka matrekta Ethiopia, Ghana na Guinea. Sasa hivi tumeamua kwenda Tanzania na Zambia.
“Nia yetu siyo kujenga tu kiwanda, bali pia kutoa huduma kwa wakulima juu ya uendeshaji na utunzaji wa matrekta hayo,” alisema.
Alisema wako tayari kutoa mafunzo kwa vijana wa Tanzania waliopo vyuoni ili waweze kuunganisha matrekta hayo, kuyafanyia ukarabati na kutengeneza vipuri vyake wakati kunapokuwa na ulazima wa kufanya hivyo.
“Tunapenda kujenga kiwanda mahali ambapo itakuwa rahisi kupata vijana wa kuajiriwa ili iwe rahisi kuwafundisha teknolojia tunayoitumia kutengeneza matrekta,” alisema.
Kwa upande wake, Pinda alisema atawasilisha maelezo hayo kwa waziri anayehusika na sekta hiyo ili mawasiliano rasmi ya kujenga kiwanda hicho yafanyike.

Chadema kujipima serikali za mitaa

Bukombe. Baraza la Wanawake la Chadema (Bawacha) limesema uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji utakaofanyika Desemba 14, mwaka huu, utatoa picha halisi ya uwezo wao wa kushika dola katika Uchaguzi Mkuu 2015.
Pia, Chadema imewaomba wananchi wote waliofikisha umri wa kupiga kura kujitokeza kujiandikisha katika daftari la makazi na daftari la kudumu la wapigakura wakati uandikishaji utakapoanza.
Halima Mdee, ambaye ni mwenyekiti wa Bawacha na mbunge wa Kawe, alisema hayo katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Kilimahewa wilayani Bukombe mkoani hapa.
Mdee alisema chama hicho kimejiandaa kuchukua dola mwakani, lakini hilo litafanikiwa ikiwa uchaguzi wa serikali za mitaa utatoa dira kamili ya ukombozi wa pili wa taifa.
“Watanzania, uchaguzi huu wa Desemba 14 ndiyo utatoa dira kamili… utakuwa ni uchaguzi muhimu kuliko hata huo wa mwakani wa madiwani, wabunge na urais kwani unapotaka kujenga nyumba madhubuti lazima uanzie msingi imara na ndiyo maana tunasema uchaguzi huu ni muhimu,” alisema.
“Wanawake wenzangu, acheni kuhongwa chumvi na kanga na CCM. Kama wameshindwa kuwaletea maendeleo kwa miaka 52 ya uhuru, ni maendeleo gani tena wanayotaka kuyaleta?” alihoji Mdee huku wananchi wakimjibu, “hakuna, hakuna… wameshindwa”.
Naye katibu mkuu wa baraza hilo, Grace Tendega alisema ifikapo Novemba 23, mwaka huu wananchi wajitokeze kujiandikisha katika daftari la makazi ili kuwawezesha kushiriki ipasavyo katika uchaguzi huo wa vijiji, vitongoji na mitaa.
“Tunawaomba wananchi ambao mmefikisha miaka 18 kujitokeza kwa wingi ili kuanza kuifuta CCM kuanzia ngazi ya chini kwa kuanzia huko ili mwakani wakati wa uchaguzi ujao, tuwe tumewaonyesha mlango wa kuondokea,” alisema Tendega.
Uchaguzi wa serikali za mitaa utafanyika Desemba 14, wakati Uchaguzi Mkuu utakuwa Oktoba mwakani.
kupigiwa kelele na CCM lakini hazina nguvu kutokana na kutodaiwa mahakamani kama hazitatolewa.
“Leo hii eti wanasema kuna haki za watoto, wazee, afya, wasanii lakini wanashindwa kusema kwamba haki hizo Ibala ya 20 (1)(2) zimefungwa kudaiwa makahakani…ikataeni pindi itakapokuja kupigiwa kura ya maoni kwani haina kitu na badala yake maoni yenu yametupwa kando,” alisema Mwaifunga

Upinzani waandika historia mpya

Dar es Salaam. Vyama vya upinzani vimeandika historia mpya tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, baada ya vyama vinne vya upinzani vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kutiliana saini makubaliano saba ya ushirikiano, kubwa ikiwa kusimamisha mgombea mmoja katika kila ngazi ya uchaguzi kuanzia sasa.
Tukio hilo lilifanywa na viongozi wakuu wa NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na NLD jana katika Viwanja vya Jangwani, Dar es Salaam na kuhudhuriwa na mamia ya wananchi, wakiwamo viongozi wa dini na taasisi mbalimbali.
Akisoma makubaliano hayo, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alianza kwa kueleza historia ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Katiba ya Tanganyika na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.
Alisema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ilitengenezwa kwa muundo wa chama kimoja cha siasa (CCM)... “ilifanyiwa marekebisho mwaka 1992 baada ya kuanza mfumo wa vyama vingi.
Mwaka 2011 tulianza mchakato wa kuandika Katiba Mpya, ilipatikana Rasimu ya Katiba iliyotokana na maoni ya wananchi lakini maoni hayo yameondolewa katika Katiba Inayopendekezwa.”
Alisema kitendo cha kuachwa kwa maoni ya wananchi yaliyokuwa katika Rasimu ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa ikiongozwa na Jaji Joseph Warioba, kimesababisha athari katika matukio muhimu ya kidemokrasia.
Akitaja makubaliano hayo, saba aliyosema yana lengo la kuzaa Tanzania Mpya, Dk Slaa alisema, “Jambo la kwanza ni kuhusisha sera za vyama vyetu na kuchukua yale yote yanayofanana ili tumwe na kauli zinazolingana na kufanana kwa Watanzania.”
Alisema jambo la pili ni kusimamisha wagombea wa pamoja kwenye ngazi zote za uchaguzi kuanzia Serikali za Mitaa, madiwani, wabunge, Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Rais wa Zanzibar na Rais wa Jamhuri ya Muungano.
Tatu, alisema utaratibu wa namna gani vyama vinavyounda Ukawa vitashirikiana katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na vijiji mwaka 2014 na Uchaguzi Mkuu 2015, utatolewa na vyama hivyo katika wakati muafaka na kusambazwa kwa viongozi wa vyama hivyo wa ngazi zote ili waweze kuutumia kama mwongozo na kufanyia kazi.
Nne, kushirikiana katika mchakato wa kuelimisha umma kuifahamu na kuipigia kura ya ‘hapana’ Katiba Inayopendekezwa ambayo haijazingatia maoni ya wananchi badala yake imezingatia masilahi ya kikundi kimoja cha watu ambacho ni CCM.
Tano, kujenga ushirikiano wa dhati katika mambo yote na hoja zote za kitaifa na zenye masilahi kwa Watanzania.
Sita, kuulinda Muungano bila kuwa na migongano ya masilahi kama ilivyo sasa na kama inavyojidhihirisha katika Katiba Inayopendekezwa.
Saba, “kuhimiza na kusimamia ushirikiano wa pamoja baina yetu na asasi na makundi mbalimbali ya Watanzania yenye nia ya dhati ya kulinda na kuenzi Muungano wetu bila kunyenyekea masilahi binafsi ya kikundi, kabila au itikadi.”
Dk Slaa alisema kwa uamuzi huo wa Ukawa ni wazi kuwa Watanzania watawaunga mkono huku akiwataka wajiandae kuwa na Tanzania Mpya.
Maalim Seif
Katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa CUF ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad alisema msimamo wa Ukawa ni msimamo wa Watanganyika na Wazanzibari, huku akiwataka wananchi kuipigia kura ya ‘hapana’ Katiba Inayopendekezwa na kuifananisha na takataka.
“Wamepiga kura kupitisha Katiba peke yao, wakaikubali peke yao, wakaitangaza peke yao. Eti wameikabidhi Katiba kwa Rais (Jakaya) Kikwete na Rais wa Zanzibar, sijui hawa viongozi wameikubali vipi hii Katiba, hakuna kitu pale,” alisema huku akishangiliwa na wananchi waliohudhuria tukio hilo.
Maalim Seif alisema theluthi mbili kutoka Zanzibar haikupatikana na Bunge hilo lilitumia ujanja wa kuongeza idadi ya wajumbe wawili kutoka Zanzibar, ambao hawakutakiwa kupiga kura kupitia upande huo wa Muungano.
Profesa Lipumba
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema: “Ukawa ina msingi wa uadilifu, uwazi na uwajibikaji na ndiyo kiboko ya kupambana na CCM. Kama mnataka rasilimali za nchi yenu kataeni Katiba Inayopendekezwa. Adui wa nchi hii ni mafisadi ndani ya CCM, lazima tuwe na mtandao wa mabadiliko nchi nzima. Vijana tufanye mazoezi ya viungo kwa ajili ya kupambana na mafisadi hawa.”
Aliwataka wananchi kuhakikisha kuwa wanajisajili katika daftari la Serikali za Mitaa ili kuwachagua viongozi wa vyama vinavyounda Ukawa... “Naanza kuona mwanga wa kuiondoa CCM madarakani. Tujenge ushirikiano kwa ajili ya nchi yetu.”
Mbowe
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema: “Yaliyotokea leo siyo mapenzi ya Lipumba, Mbowe, Mbatia, Makaidi wala Nyambabe, bali ni mapenzi ya Mungu. Kama kuna mmoja wetu aliyepo hapa anayeshuhudia tukio hili huku amenuna … dhoruba limtokee.”
Huku akishangiliwa na umati wa wafuasi wa Ukawa, Mbowe alisema ni mategemeo yake kuwa viongozi wote waliotia saini makubaliano hayo, walizungumza kutoka rohoni kwamba wanaungana na wana nia moja.
Aliwataka viongozi wa chama chake katika ngazi zote, kuhakikisha wanakubaliana na mapendekezo yanayotolewa na Ukawa na kwamba yeyote anayeona hataweza aondoke mapema.
“Katika chama chetu hakuna masilahi ya maana kuliko nchi yetu. Ni marufuku kiongozi wa Chadema kupuuza muungano wa Ukawa na kama yupo mwenye masilahi binafsi aanze safari mara moja,” alisema Mbowe.
Aliwaagiza viongozi wa taasisi zote za Chadema, Bawacha, Bavicha na Baraza la Wazee, kuhakikisha wanafanya kampeni za kuipinga Katiba Inayopendekezwa nchi nzima kuanzia Novemba Mosi. Aidha, aliwaomba viongozi wa Ukawa kuhamasisha viongozi wao kuipinga Katiba Inayopendekezwa.
Mbatia
Mbatia alisema Taifa limeandika historia mpya na kuwaomba viongozi wenzake ndani ya Ukawa kuaminiana ili Watanzania nao wawaamini kwa kuwa wanataka kuweka mbele masilahi ya taifa.
Kuhusu Katiba, Mbatia alisema ni maarifa, mwongozo na inayounda dola hivyo asiwepo wa kuifanyia mchezo. Alitaka Katiba Inayopendekezwa ikataliwe na wananchi kwa kuwa haisadifu sifa hizo.
“Ukawa wana utulivu wa ndani wa kuwatumikia Watanzania wote… tuache kuangalia masilahi binafsi. Wakishinda Chadema… mimi nikubali, akishinda CUF lazima nikubali, hata wakishinda NLD nao nitakubali lakini na NCCR tukishinda nao waone tumeshinda kusiwepo na kinyongo kwa kuwa wote tunapigania mama Tanzania,” alisema.
Makaidi
Mwenyekiti wa NLD, Dk Emmanuel Makaidi alisema umoja wa wananchi ndiyo utakaowapa nguvu viongozi wa Ukawa na kuongeza kuwa anaipenda Tanzania na anataka Zanzibar iwe na mamlaka kamili.
“Mungu siyo Athuman wala siyo wa John… Mungu alijua kupitia misukosuko hii ya Katiba, Ukawa tutaunganishwa. Bahati hii inaweza isitokee tena, wakati wa ukombozi ni sasa na utakapofika wakati wa kupigia kura ya maoni tuseme hapana, hapana, hapana na moto… moto mpaka CCM iungue,” alisema Dk Makaidi huku akishangiliwa kwa nguvu.

Saturday, 25 October 2014

Chadema walaani Meghji kuipigia kura Zanzibar

Sengerema. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitendo kilichofanywa na uongozi wa lililokuwa Bunge Maalumu la Katiba cha kumfanya Mjumbe wa Bunge hilo, Zakia Meghji kupiga kura kama Mzanzibar badala ya ‘Mtanzania Bara’ ni ‘uhuni’ unaotakiwa kuchukuliwa hatua na wananchi.
Hayo yalisemwa juzi na viongozi wa Mabaraza ya Wanawake na Vijana ya Chadema (Bawacha) na (Bavicha) katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi, Segerema mkoani Mwanza.
Kauli hiyo wameitoa ikiwa ni saa 48 baada ya gazeti hili kubainisha utata wa kura ya Meghji wakati wa kuipitisha Katiba inayopendekezwa kupiga kama mjumbe kutoka Zanzibar badala ya Tanzania bara kama alivyotakiwa.
Akihutubia mamia ya wananchi, Mwenyekiti mstaafu wa Bavicha, John Heche alisema, “Kilichofanywa na Sitta (Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta) cha kumbadilisha dakika za mwisho Meghji kuhalalisha Katiba yao ni uhuni ambao Watanzania wanatakiwa kuwawajibisha kupitia kura ya maoni.”
Aliongeza: “Hivi kweli inawezekanaje mtu katika vikao vyote awe anahesabika kama mjumbe kutoka Tanzania Bara halafu dakika za majeruhi baada ya kuona wanachokifanya hakitapata theluthi mbili, hususani Zanzibar wampeleke huko….”?
Huku akishangiliwa na umati huo, Heche alisema wajumbe wa CCM wameondoa tunu za taifa za uwazi na uadilifu baada ya kuona zimewabana.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Bawacha, Hawa Mwaifunga alisema wanawake wakiacha kutumika na CCM. hususani nyakati za chaguzi zinapokaribia wataifanya nchi hii iliyokosa maendeleo kwa miaka 52 baada ya uhuru kusonga mbele.
“Wanawake wenzangu nawaombeni mjitokeze kugombea nafasi mbalimbali lakini pia kujiandikisha katika daftari la wapiga kura na makazi ili muweze kushiriki kikamilifu katika chaguzi hizo,” alisema Mwaifunga
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Bawacha, Grace Tendega alisema,”Nawasihi wanawake wenzangu na vijana wenye sifa kwenda kujiandikisha ili kuweza kuwa na sifa ya kuchagua na kuchaguliwa...wanawake msiache kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwani tunaweza.”
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Bawacha, Kunti Yusuph alisema nchi hii imefika hapa kutokana na kuwakumbatia viongozi wasiotimiza wajibu wetu.
“Watanzania leo kupata huduma bora ni anasa, kuapata huduma za afya, elimu na maji navyo ni anasa hivyo tuchukue hatua kupitia uchaguzi wa serikaki za mitaa kubadili uongozi,” alisema Yusuph