Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete amewatuhumu baadhi ya
watendaji wa serikali yake kuwa ni kikwazo katika kufanikisha masuala
mbalimbali ya maendeleo kutokana na urasimu usiokuwa wa lazima katika
kutoa huduma kwa wananchi.
Akifungua kongamano la miaka 10 ya Tume ya
Utumishi wa Umma Dar es Salaam jana, Rais Kikwete alikemea na kulaumu
tabia ya baadhi ya watendaji hao wa Serikali ambao wamekuwa wakikwamisha
kwa makusudi kasi ya viongozi wa kisiasa ya kuleta maendeleo.
“Katika utendaji wa baadhi ya watendaji wakuu wa
Serikali limekuwa ni tatizo na wamekuwa wakikwamisha sana kasi ya
utekelezaji wa haraka wa malengo ya kisiasa,” alisema.
“Mara nyingine, viongozi wa kisiasa wamekuwa mbele
kimtazamo kuliko watumishi wa umma, hili limekuwa tatizo sana katika
utekelezaji wa malengo kwa haraka,” alisema Kikwete.
Alisema kumekuwa na malalamiko kwa makatibu wakuu
wa wizara kutoka kwa wawekezaji ambao huwachelewesha kwa makusudi kwa
visingizio vya kufuata utaratibu.
Alisema katika kufuatilia, amekuwa akilazimika
kuingilia utendaji wa baadhi ya wizara ili kuhakikisha mambo yanakwenda
na mara nyingine urasimu huo umekuwa ukifanywa kwa makusudi ili
kuwachosha wawekezaji na ‘kuwatoa upepo’ kwa manufaa binafsi.
“Haya ni malalamiko makubwa sana na yanatoa picha
mbaya kwa nchi yetu…watendaji wa namna hii ni lazima wabadilike,
ninahitaji kuona mabadiliko makubwa kwa kupitia Tume ya Utumishi ambayo
inatakiwa kukaa na hawa watumishi na kuwapa mafunzo ya kiutendaji
yanayoendana na mahitaji ya sasa,” alisema.
Abeza zawadi ya uprofesa
Akizungumzia utaratibu wa upandishwaji vyeo, Rais
Kikwete alisema ni muhimu weledi ukazingatiwa na utaratibu uliowekwa
ukaheshimiwa, kwamba lazima wafanyakazi wapandishwe vyeo na madaraja
ndani ya kipindi kilichowekwa, ambacho ni miaka mitatu.
Alisema kumekuwa na malalamiko kwa wafanyakazi
wengi wa Serikali kutopandishwa vyeo kwa muda mrefu na hata
wanapopandishwa vyeo mabadiliko ya mishahara kuendana na vyeo na
madaraja mapya hayafanyiki kwa wakati.
Alieleza kwamba utaratibu unaotumika katika vyuo
vikuu wa namna ya kuwapata wahadhiri wasaidizi, wahadhiri, maprofesa ni
wa wazi na ni mfano wa kuigwa kutokana na namna unavyofanyika, kwa kutoa
mafunzo kisha kuyathibitisha na kumpandisha mhusika daraja.
“Vyuo vikuu wana ngazi wanazotakiwa kuzipitia na
mafunzo maalumu hadi mtu anakuwa profesa. Siyo honorary professor
(uprofesa wa heshima) niliopewa mimi nilipokwenda China…walinishtukiza.
Nilifika pale wakanipiga na uprofesa, nikasema haya sasa makubwa!
(kicheko),” alisema.
Alisema matatizo ya upandishwaji vyeo yasipotatuliwa kwa wakati
ni tatizo kubwa kwa Serikali hasa unapokutana na vyama vya wafanyakazi
vyenye nguvu kama Chama cha Walimu na wanapofikia hatua ya kusema
wanagoma, unalazimika kuwaangukia.
Alisema suala la mtumishi kupandishwa cheo ni haki
yake ya msingi kazini hivyo hatarajii kusikia matatizo ya malalamiko ya
watumishi kutopanda vyeo kwa wakati.

No comments:
Post a Comment