Dar es Salaam. Kwa jumla, kuungana ni jambo jema kwani muungano
huongeza nguvu. Muungano ni silaha ya mnyonge dhidi ya mwenye nguvu.
Ni kwa sababu hii, tumekuwa tukipigania umoja wa
Afrika ili kujenga nguvu ya pamoja dhidi ya mabeberu wa mataifa ya
Magharibi tukiamini kwamba bila nguvu moja mataifa ya Afrika hayataweza
kuukabili ubeberu wa mataifa haya.
Tunao msemo maarufu usemao nguvu ya mnyonge ni
umoja na hivi ndivyo waasisi wa mataifa ya Afrika walivyofanya katika
kumfukuza mkoloni.
Bila kujali tofauti zao za kikabila na vinginevyo,
wananchi wa Afrika waliunganisha nguvu na hatimaye pamoja na silaha zao
duni, wakafanikiwa kumfukuza mkoloni katika ardhi ya Afrika.
Katika uwanja wa siasa, vyama vya siasa huungana
kwa sababu mbalimbali lakini sababu tatu ni za msingi zaidi. Mosi,
huungana pale ambako hakuna chama kinaibuka na ushindi wa moja kwa moja
katika uchaguzi ulio na ushindani mkali.
Katika mazingira haya, inakuwa hakuna chama
kinachoweza kuunda serikali imara peke yake bila kushirikisha kingine
kwa sababu hakitaweza kupitisha sera au sheria yoyote bungeni.
Hivi ndivyo vyama vya Conservatives na Liberal
Democrats vilivyoungana huko Uingereza baada ya vyama vikuu nchini humo
vya Labour na Conservatives kushindwa kupata ushindi ambao ungekiwezesha
chama kimojawapo kuunda serikali na kupitisha sera bungeni bila
msukosuko mkubwa.
Hivi ni vyama ambavyo vina itikadi na msimamo
tofauti kabisa kifalsafa na ilibidi viongozi wake wakae saa nyingi
kukubaliana programu ya kutekeleza kabla hawajakubaliana kugawana nafasi
za uongozi.
Kiongozi wa Liberal Democrats, Nick Cleggy
alimshinikiza David Cameroon akubaliane na masharti ya kulegeza misimamo
mikali ya chama chake kuhusu sera ya uhamiaji na hifadhi ya jamii kabla
hajakubali kuingia naye ubia kuunda serikali.
Cameron amekiri mara kadhaa kwamba alilazimika
kulegeza msimamo kuhusu sera mama za Conservatives ili kufanikisha
kuwashawishi Liberal Democrats kuunda nao serikali vinginevyo Nick
Cleggy angeunda serikali na Gordon Brown wa chama cha Labour.
Ni katika mazingira ya chama kimoja kushindwa
kupata ushindi wa wazi ambayo yalivilazimisha vyama hasimu vya CUF na
CCM kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) Zanzibar.
Pamoja na kwamba SUK iliundwa kama njia sahihi ya
kuepusha shari na vita visiwani, msingi wa serikali hiyo ni ukweli
kwamba hakuna chama chochote kati ya hivi viwili chenye uwezo wa kuunda
serikali imara kwa sababu ushindi wa chama chochote huwa ni mwembamba.
Hata hivyo, hatujui ni kwa kiwango gani vyama vya CUF na CCM huko
Zanzibar vilikubaliana kutekeleza programu ya pamoja inayotokana na sera
za vyama hivyo viwili.
Sababu ya pili ya vyama kuungana ni kuunganisha nguvu katika jitihada za kumwondoa adui anayefanana.
Kwa mfano, huko Zanzibar kabla ya mapinduzi ya
mwaka 1964, vyama kadhaa viliungana katika jitihada za kuuondoa utawala
wa Sultani uliokuwa unaendeshwa kibaguzi. Kwa hiyo, adui hapa alikuwa
Sultani na ubaguzi wake wa rangi.
Sababu ya tatu ni pale vyama vinapounganisha nguvu
ili kushinda uchaguzi kwa kutambua kwamba vikiingia kwenye uchaguzi
kimoja, kimoja havitaweza kushinda kutokana na nguvu kubwa aliyonayo
mshindani wao.
Hata hivyo, kushinda uchaguzi hakuwezi kutokana na
kuunganisha nguvu ya kiuongozi pekee. Ni lazima kuunganisha pia nguvu
ya kiitikadi, kifalsafa na kisera ili kuweza kujipambanua kwa wananchi.
Muungano wa kisera ni muhimu ili kuweza kutabirika
tabia za wagombea watakapokuwa madarakani. Aidha, ni programu ya kisera
inayoweza kuongoza kuchagua mgombea anayefaa zaidi kushika usukani wa
utekelezaji wake baadaye.
Muungano wa vyama vinavyounda Ukawa umepokewa kwa
shangwe kubwa. Furaha hii inatokana na msingi nilioueleza hapo awali
kwamba wanyonge wakiungana hupata nguvu ya ajabu hata ya kuweza
kuangusha milima.
Kwa hiyo, watu ambao wamekuwa wakisubiri utawala
wa CCM kuanguka wanaamini kwamba kwa muungano huu angalau vyama vya
upinzani vitafuta unyonge.
Nami naungana na Watanzania wengine kuwapongeza
viongozi wa vyama ya Chadema, CUF, NCCR na NLD kwa ujasiri na uthubutu
waliouchukua katika kujaribu kushirikiana katika chaguzi mbalimbali
zijazo.
Lakini tunapowapongeza Ukawa, ni vizuri kutambua
kwamba kuunganisha nguvu kama walivyofanya ni hatua moja tu inayopaswa
kuanzisha hatua nyingi huko mbele. Hatua muhimu inayofuata sasa ni
kujipambanua kwa wananchi kiitikadi, kifalsafa na kisera.
Kwa bahati viongozi wa sasa wa vyama vilivyoungana siyo watu wanaoamini katika mambo ya itikadi na falsafa.
Hawa ni viongozi ambao huitwa ‘wayakinifu’
(pragamatists). Myakinifu ni kiongozi anayeamini katika kinachowezekana
leo na haongozwi na falsafa bayana ya kisiasa.
Kwa hiyo kiongozi yakinifu atambeba yeyote
anayeona anafaa na huwezi kumuweka katika mrengo wowote kiitikadi.
Kimsingi, hii ndiyo aina ya viongozi tulionao sasa tangu Mwalimu Julius
Nyerere alipoondoka.
Ndiyo maana tumekuwa Taifa ambalo si la kijamaa, wala kiliberali wala kibepari. Tupotupo tu maadamu siku zinakwenda.
Pamoja na uyakinifu wao, bado naamini kwamba Ukawa
watahitaji programu ya pamoja ya kisera. Hii ni hatua muhimu ili kutoa
nafasi kwa wananchi kupima aina ya serikali watakayounda kama watashinda
katika Uchaguzi Mkuu ujao.
Bila msimamo yakinifu wa kisera, ni rahisi
kutofautiana kwa sababu ya kukosa msingi wa kugawana madaraka. Bila sera
yakinifu, utakapofika wakati wa kugawana nafasi za kugombea na hatimaye
katika kuunda Serikali watalazimika kuzingatia sifa za kuchagulika na
umaarufu badala ya sifa za kiuwezo.
Nakumbuka mwaka 2005 palipokuwa na jitihada za
kuunda ushirikiano kama huu wa sasa, nilipewa jukumu la kufanya utafiti
kujua nani alikuwa anakubalika zaidi katika Jimbo la Ubungo kati ya
mgombea wa Chadema (John Mnyika) na mgombea wa CUF (marehemu mama
Minja).
Niliandaa hojaji na nikaligawa katika kata zote za
Jimbo la Ubungo kwa kutumia sampuli iliyopatikana kwa njia ya bahati
nasibu. Matokeo yalionyesha kwamba Mnyika alikuwa anakubalika kwa mbali
dhidi ya wagombea wengine wa upinzani.
Hata hivyo, katika kikao cha kujadili matokeo
hayo, wawakilishi wa CUF waliyakataa na kunituhumu kwamba nilikuwa
napendelea chama changu na huo ndiyo ukawa mwanzo wa ushirikiano
kusuasua na hatimaye kusambaratika kabisa kabla ya kampeni kuanza.
Yote hii ni kwa sababu tuliwekeza zaidi kwenye kugawana wagombea lakini hatukuwekeza kabisa katika ushirikiano wa kisera.
Ninachojaribu kusema hapa ni kwamba, muungano
wowote endelevu wa vyama vya siasa Tanzania, lazima uwe wa kuunganisha
nguvu za wanyonge dhidi ya mabavu ya chama dola cha CCM.
Muungano wa namna hii lazima uwaunganishe kisera Watanzania na ndiyo unaopaswa kuwa msingi wa kugawana vyeo.

No comments:
Post a Comment