Saturday, 25 October 2014

Chadema walaani Meghji kuipigia kura Zanzibar

Sengerema. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitendo kilichofanywa na uongozi wa lililokuwa Bunge Maalumu la Katiba cha kumfanya Mjumbe wa Bunge hilo, Zakia Meghji kupiga kura kama Mzanzibar badala ya ‘Mtanzania Bara’ ni ‘uhuni’ unaotakiwa kuchukuliwa hatua na wananchi.
Hayo yalisemwa juzi na viongozi wa Mabaraza ya Wanawake na Vijana ya Chadema (Bawacha) na (Bavicha) katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi, Segerema mkoani Mwanza.
Kauli hiyo wameitoa ikiwa ni saa 48 baada ya gazeti hili kubainisha utata wa kura ya Meghji wakati wa kuipitisha Katiba inayopendekezwa kupiga kama mjumbe kutoka Zanzibar badala ya Tanzania bara kama alivyotakiwa.
Akihutubia mamia ya wananchi, Mwenyekiti mstaafu wa Bavicha, John Heche alisema, “Kilichofanywa na Sitta (Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta) cha kumbadilisha dakika za mwisho Meghji kuhalalisha Katiba yao ni uhuni ambao Watanzania wanatakiwa kuwawajibisha kupitia kura ya maoni.”
Aliongeza: “Hivi kweli inawezekanaje mtu katika vikao vyote awe anahesabika kama mjumbe kutoka Tanzania Bara halafu dakika za majeruhi baada ya kuona wanachokifanya hakitapata theluthi mbili, hususani Zanzibar wampeleke huko….”?
Huku akishangiliwa na umati huo, Heche alisema wajumbe wa CCM wameondoa tunu za taifa za uwazi na uadilifu baada ya kuona zimewabana.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Bawacha, Hawa Mwaifunga alisema wanawake wakiacha kutumika na CCM. hususani nyakati za chaguzi zinapokaribia wataifanya nchi hii iliyokosa maendeleo kwa miaka 52 baada ya uhuru kusonga mbele.
“Wanawake wenzangu nawaombeni mjitokeze kugombea nafasi mbalimbali lakini pia kujiandikisha katika daftari la wapiga kura na makazi ili muweze kushiriki kikamilifu katika chaguzi hizo,” alisema Mwaifunga
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Bawacha, Grace Tendega alisema,”Nawasihi wanawake wenzangu na vijana wenye sifa kwenda kujiandikisha ili kuweza kuwa na sifa ya kuchagua na kuchaguliwa...wanawake msiache kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwani tunaweza.”
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Bawacha, Kunti Yusuph alisema nchi hii imefika hapa kutokana na kuwakumbatia viongozi wasiotimiza wajibu wetu.
“Watanzania leo kupata huduma bora ni anasa, kuapata huduma za afya, elimu na maji navyo ni anasa hivyo tuchukue hatua kupitia uchaguzi wa serikaki za mitaa kubadili uongozi,” alisema Yusuph

Pinda atangaza rasmi kuwania urais

Dar es Salaam. Siyo tetesi tena. Sasa ni rasmi kwamba Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye amekuwa akitajwa kuwania urais amethibitisha wazi kuwa atagombea kiti hicho katika uchaguzi mkuu mwakani.
Alitoa uthibitisho huo juzi akiwa London, Uingereza ambako yuko katika shughuli za kikazi. Hatua hiyo inaondoa uvumi ambao umekuwapo kwa takriban miezi mitatu sasa kwamba naye tayari ameingia katika kinyang’anyiro hicho.
Pinda aliweka wazi nia ya kuelekea Ikulu akisisitiza kuwa hajatangaza rasmi lakini akasema kuwa ameanza harakati hizo ‘kimyakimya’. Alikuwa akijibu moja ya maswali aliyoulizwa katika Kipindi cha Dira ya Dunia kinachorushwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).
Alitamka rasmi kuwania nafasi hiyo baada ya kuulizwa kuwa anafikiri ni kiongozi gani anayefaa kurithi mikoba itakayoachwa na Rais Jakaya Kikwete.
“Mikoba ya Rais Kikwete inaweza kuchukuliwa na yeyote atakayeonekana mwisho wa safari kwa utaratibu wa chama na ndani ya Serikali .... kama anafaa. Waliojitokeza sasa ni wengi na mimi ninadhani ni vizuri,” alisema Pinda.
Alipoulizwa kama yupo miongoni mwa wengi alisema, “… umesikia kama nimo … basi tukubali hilo na yeye Waziri Mkuu yumo. Hao wote waliojitokeza pamoja na Waziri Mkuu aliyejitokeza ni katika jitihada za kusema hebu Watanzania nitazameni je, mnaona nafaa au hapana?”
“……..fanyeni hivyo kwa mwingine na mwingine, mwisho wa yote zile kura zitakazopatikana kwenye mkutano mkuu kama ni kutokana na chama kile kinachotawala na hatimaye Watanzania watakaojitokeza kupiga kura Oktoba kutokana na wagombea watakaojitokeza kutoka kwenye vyama mbalimbali huyo ndiye tutakayempata kama rais. Hivyo natangaza nia hiyo kimyakimya.”
Kiongozi huyo atakuwa wa pili kutangaza nia hiyo kupitia vyombo vya habari vya kimataifa, baada ya Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.
Alitangaza nia hiyo Julai 2, 2014, alipokuwa Uingereza katika mkutano wa sekta ya mawasiliano baada ya kuhojiwa kwenye kipindi hicho hicho cha Dira ya Dunia.
Urais CCM
Kuingia kwa Pinda katika mbio za urais kupitia CCM tayari kumebadili mwelekeo wa kinyang’anyiro cha nafasi hiyo kubwa ya uongozi nchini kutokana kuzigawa baadhi ya kambi za wagombea ambao walikuwa wakitajwa kwa muda mrefu kabla yake.
Wengine ambao wamekuwa wakitajwa kuwania nafasi hiyo kupitia CCM ni Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.
Wengine ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja na Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla.
Nguvu ya Pinda
Baadhi ya wapiga debe wa Pinda wakiongozwa na Mwenyekiti wa Mamlaka za Mitaa Tanzania (Alat), ambaye pia ni Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk Didas Masaburi, wamekuwa wakiweka kambi zao Dodoma kila kunapokuwa na vikao rasmi vya CCM ili kuwashawishi wajumbe wa vikao vya juu vya chama hicho wamuunge mkono.
Wakati wa vikao vya CC na NEC vya CCM vilivyomalizika wiki iliyopita mjini Dodoma, kundi la wafuasi wa Pinda likiongozwa na Dk Masaburi lilikuwa mjini humo kuendelea na jitihada za kusaka wafuasi.
Harakati hizo zinaweza kuwa ndiyo maana ya kauli ya Pinda pale aliposema kwamba tayari ametangaza ‘kimyakimya’ nia yake ya kugombea nafasi hiyo.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana anaunga mkono msimamo wa Pinda na wengine waliojitangaza katika chama chake huku akivilaumu vyama vya upinzani kwa wagombea wao kukaa kimya badala ya kujitokeza ili wananchi wawapime kama wa CCM wanavyofanya.
Kuhusu Pinda, Dk Bana alisema: “Ni mzoefu amekaa Ikulu muda mrefu na kwa wadhifa wake, si vibaya kujitangaza kwani anayejitangaza wananchi wanapata muda wa kumpima na chama pia kinampima tofauti na wale ambao hawajitangazi ambao ni hatari sana kwa kuwa wanapita chinichini kutoa rushwa.”
Kuhusu upinzani, alisema: “Sijui upinzani wana matatizo gani, ningefurahi kuona (Halima) Mdee, (John) Mnyika au (Willbrod) Dk Slaa wanajitokeza ili wananchi wawapime kwani Dk Slaa wa 2010 siyo Dk Slaa wa sasa. Wakijitokeza italeta uhai kwenye hizi harakati na wananchi watakuwa na nafasi nzuri ya kuwapima,” alisema na kuongeza: “Upinzani wanapokaa kimya wanatunyima fursa wananchi kuwapima.”
Manung’uniko
Tangu kuanza kwa tetesi kwamba Pinda ameingia katika kinyang’anyiro cha urais, kumekuwa na malalamiko ya chinichini dhidi yake kwamba amekuwa akicheza rafu kama ambazo ziliwafanya na makada wenzake wenye nia sawa na yake kufungiwa na Kamati Kuu ya CCM.
Itakumbukwa kwamba makada sita wa chama hicho ambao ni Sumaye, Lowassa, Membe, Makamba, Wasira na Ngeleja wanatumikia adhabu na wapo chini ya uangalizi wa chama hicho baada ya kutiwa hatiani kwa makosa ya kuanza kampeni za urais kabla ya muda kutangazwa.
Baadhi ya wagombea na makada wa CCM wamekuwa wakidai kuwa Pinda naye anacheza rafu hivyo kutaka ashughulikiwe, lakini wengine wamekwenda mbali zaidi na kuhoji ushiriki wake katika Kikao cha Kamati Kuu ambacho kilitoa adhabu hiyo ilhali akijua kwamba naye atakuja kugombea.
Makamba, Kigwangalla
Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Mbunge wa Nzega, Dk Hamisi Kikwangalla wamesema wanamkaribisha Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika mpambano wa kuwania safari ya kwenda Ikulu kupitia CCM.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, Makamba na Kigwangalla walionekana kutostushwa na uamuzi wa Pinda kuingia rasmi katika mbio hizo huku wakisema siyo tishio kwao.
Makamba kwa upande wake alisema hakuna cha ajabu kwa Pinda kuwania nafasi hiyo kwani 1995 alijitokeza Cleopa Msuya ambaye alikuwa pia waziri mkuu kupambana na mawaziri wengine kama Jakaya Kikwete na Edward Lowassa lakini alishindwa na Benjamin Mkapa ambaye alipitishwa.
Alisema pia mwaka 2005 alijitokeza Waziri Mkuu, Frederick Sumaye dhidi ya mawaziri wengine wadogo, lakini walimshinda.
“Mara zote hizo wagombea wengine walifanikiwa dhidi ya mawaziri wakuu. Nafasi za madaraka ya kiserikali hazina nafasi katika uteuzi wa wagombea ndani ya CCM,” alisema Makamba.
Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli alisema anamkaribisha ili wapimane ubavu lakini akasema ni muhimu kuanzia sasa hadi Mei mwakani, harakati hizo zisiathiri kazi za Serikali hasa ikizingatiwa kuwa Pinda ndiye msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali.
Dk Kigwangalla ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) inayosimamia Ofisi ya Waziri Mkuu alisema haogopi mgombea hata mmoja, hata akiwa na cheo kikubwa au kidogo kwake si tishio.
“Waziri Mkuu anakaribishwa kwenye mbio hizi na asifikiri zitakuwa rahisi kwani watu tumejipanga na tuna mikakati ya kushinda,” alisema Kigwangalla.
Hata hivyo, Dk Kikwangalla alisema kuingia kwa Pinda kunaweza kuharibu mchakato mzima kwenye chama kwa kuwa ni mmoja wa watu wanaotoa uamuzi hasa ikizingatiwa kuwa kwa nafasi yake, anaingia kwenye Kamati Kuu na Halmashauri Kuu.
“Waziri Mkuu yuko kwenye nafasi ya kutuchuja, hivyo ni kama kusema refa ameamua kucheza kitu ambacho ni tatizo. Kitendo cha kutaka uongozi katika nafasi kama yake kitaondoa usawa,” alisema Dk Kikwangalla.

Kura ya Maoni mkorogano

Dar es Salaam. Kitendo cha Serikali kutoa kauli tatu tofauti ndani ya wiki moja kuhusu tarehe ya Kura ya Maoni kupitisha Katiba Inayopendekezwa, kimeelezwa na watu wa kada mbalimbali nchini kuwa ni matokeo ya viongozi wa Serikali kukosa uongozi wa pamoja.
Wakizungumza na Mwananchi Jumamosi, wasomi, wanaharakati, viongozi wa dini na wanasiasa wamesema kauli hizo zinawachanganya Watanzania, kwamba mpaka sasa hakuna anayejua tarahe rasmi ya kufanyika Kura ya Maoni.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema alilieleza gazeti hili kuwa  kura hiyo ingefanyika Machi 30 mwakani na kwamba upigaji kura utatanguliwa na kampeni ambazo zitafanyika kwa siku 30, kuanzia mwanzoni mwa Machi ili kushawishi Katiba Inayopendekezwa iungwe mkono au kinyume chake kwa makundi yanayoipinga.
Siku moja baadaye, Rais Kikwete alipokutana na mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao katika Jamhuri ya Watu wa China alisema endapo mipango yote itakwenda kama inavyoandaliwa, Watanzania wataipigia kura ya maoni Katiba Inayopendekezwa Aprili mwakani.
Kauli ya Jaji Werema pia ilipingwa na Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), Jaji Damian Lubuva na kufafanua kuwa kura ya maoni haiwezi kufanyika Machi 30 mwakani kwa sababu kazi ya uandikishaji wa Daftari la Wapigakura haitakuwa imekamilika.
Utata umezidi kuongezeka baada ya jana katika mkutano wake na waandishi wa habari, Jaji Lubuva kusema kuwa Daftari la Kudumu la Wapigakura litakamilika Aprili 18 mwakani, huku taratibu zikieleza kwamba kura ya maoni itafanyika baada ya elimu kutolewa kwa wananchi na hutolewa kati ya miezi mitatu hadi sita.
Awali Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliwahi kukaririwa akisema kuwa Kura ya Maoni ifanyike kabla ya Uchaguzi Mkuu 2015, huku Rais Kikwete akikubaliana na viongozi wa vyama vya siasa kuwa kura ya maoni itafanyika baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti Mwalimu wa Idara ya Lugha za Kigeni na Isimu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Faraja Christoms alisema, “Hayo ni matokeo ya kukosekana kwa uwajibikaji wa pamoja. Sina hakika kama AG ndiye alipaswa kutaja tarehe ya kura ya maoni, yeye ni mshauri tu.”
Alisema kitendo cha kauli ya AG kutofautiana na iliyotolewa na rais ambaye amemteua ni ishara mbaya katika utendaji kazi wa Serikali.
“Wakati mwingine kauli kama hizi zinaweza kuwavunja moyo walioteuliwa. Nakumbuka Waziri Mkuu Pinda aliwahi kutoa kauli ya kupinga maelezo ya Waziri wa Ujenzi, Magufuli (John). Tafsiri ya kilichotokea ni kukosekana kwa uwajibikaji wa pamoja,” alisema.
Naye Katibu Mkuu  wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Dk Leonard Mtaita alisema kazi iliyobaki ni kuwahamasisha wananchi wakati wa kupiga kura ya maoni utakapofika  kwa maelezo kuwa kila mtu atapiga kura kutokana na anachokiamini.
Dk Mtaita alisisitiza pia kuboreshwa kwa Daftari la Wapigakura, akisema kuwa hilo ndilo litakuwa jambo la msingi ili kuwafanya Watanzania wote wenye sifa waweze kupiga kura, huku akiiomba Serikali kuhakikisha inasambaza nakala za kutosha za Katiba Inayopendekezwa.
Aliyekuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha St Augustine, Dk Charles Kitima alisema, Serikali kupuuza mawazo na malalamiko ya watu ni ishara mbaya, kufafanua kwamba Katiba Inayopendekezwa ina uhalali wa kisheria lakini inakosa uhalali wa kisiasa na ili kuokoa mvutano, maridhiano ni jambo la msingi.
“Wananchi wanaulalamikia mchakato wa Katiba, pamoja na mvutano unaoendelea, haya malalamiko ya wananchi si ya kufurahia hata kidogo. Jambo hili linatakiwa kupatiwa ufumbuzi,” alisema.
Aliongeza, “Rais ndiye anayetakiwa kutueleza msimamo wake ni nini juu ya suala hili. Je, na yeye atafuata masilahi ya CCM au atazungumza kama Rais. Kama maridhiano yatakosekana na Katiba hiyo ikapitishwa, haitadumu muda mrefu kwa sababu watawala wengine watakaokabidhiwa kijiti wataibadili Katiba hiyo.”
Mkurugenzi Mtendaji wa shirika lisilokuwa la kiserikali linalojihusisha na masuala ya kijamii, Fordia, Bubelwa Kaiza alisema tofauti za kauli za viongozi zinaonyesha kuwa mchakato wa kupata Katiba Mpya uliendeshwa katika taratibu zisizo sahihi, ndio maana hakuna kauli moja kuhusu siku ya kupiga kura ya maoni.
“Hayo ni majibu kwamba ndani ya serikali kuna mkanganyiko mkubwa kuhusu suala zima la Katiba Mpya. Hakuna msemaji sahihi, kila mtu anazungumza lake. Ndio maana hata katika Bunge Maalumu kila mtu alifanya lake, sheria zilibadilishwa bila kufuatwa kwa utaratibu,” alisema.
Alifafanua kuwa ni ngumu kwa kila jambo linalohusu Katiba kwenda vizuri kwa sasa kwa sababu mchakato uliharibika baada ya kuanza vikao vya Bunge Maalumu la Katiba.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), Deus Kibamba alisema elimu ya uraia inatakiwa kutolewa miezi mitatu hadi sita kabla ya kufanyika Kura ya Maoni, si siku 30 alizozitaja Jaji Werema.
“Huwezi kutoa elimu ya uraia kwa siku 30, mfano Zimbabwe walitumia miezi sita kutoa elimu ya uraia. Mchakato huu umeingiliwa na wajanja, si riziki tena, ni kama mtu aliyejifungua mtoto aliyekufa,” alisema.
Kibamba alisema Nec ilieleza kuwa kufikia Mei ndiyo itakuwa imemaliza kazi ya kuboresha Daftari la Wapigakura, kwamba kitendo cha Jaji Werema kueleza kuwa Kura ya Maoni itafanyika Machi mwakani, ni ishara ya ‘ukambale’.
“Waziri Mkuu (Pinda) alisema Katiba ipatikane kabla ya Uchaguzi Mkuu 2015, Rais Kikwete akakubaliana na TCD kuwa ni 2016, jana (juzi) Jaji Werema anatueleza kuwa ni Machi mwakani, tumsikilize nani?”
Alisema tarehe ya kura ya maoni kwa mujibu wa sheria inatakiwa kutangazwa na Rais si Mwanasheria Mkuu wa Serikali.  Kibamba alisisitiza kuwa Serikali bora ni ile inayojiendesha kwa uwajibikaji wa pamoja.
Rais mstaafu wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Felix Kibodya alisema, “Tamko la Serikali kwa jambo kama hilo huwa ni moja na si kila kiongozi kutoa tamko lake. Ndiyo maana tarehe ya  Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ilitolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, si mtu mwingine.”

Alisema huenda mkanganyiko ulioibuka juu ya tarehe rasmi ya kura ya maoni unatokana na nchi kutowahi kuendesha zoezi la upigaji wa kura hiyo.
“Sheria inaeleza wazi kuwa rais atatangaza tarehe rasmi siku 84 baada ya kukabidhiwa Katiba Inayopendekezwa. Ili muda usogezwe mbele ni lazima sheria ibadilishwe, nadhani hilo linaweza kufanyika katika kikao kijacho cha Bunge,” alisema.
Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania (TEC), Askofu Severini Niwemugizi  alisema  mchakato wa Katiba ni suala la kisheria na kisiasa, hivyo kama Rais alikutana na wanasiasa na kukubaliana, ingekuwa jambo jema kama makubaliano hayo yangezingatiwa.
 “Kama ni suala la sheria, sheria husika inabadilishwa lakini kama ni suala la makubaliano ya wanasiasa, pia lilitakiwa kuzingatiwa. Kwa sasa kuna mvutano mkali, sijui nini kitatokea,” alisema.
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk Willbrod Slaa alisema jambo hilo linatokana na viongozi wa Serikali kugawanyika huku akitolea mfano kauli ya Rais Kikwete kuwa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ungefanyika Februari mwakani, lakini baadaye Waziri Pinda akatangaza kuwa utafanyika Desemba 14 mwaka huu.
“Nchi inayokuwa na viongozi ambao kila mmoja anatoa kauli yake haiwezi kuwa na mshikamano. Wao hawana umoja halafu wanataka Watanzania kuwa na umoja, hilo litawezekana kweli?” alihoji Dk Slaa.
Aliongeza, “Hata kura ya maoni ikifanyika leo haina maana tena kwa sababu Katiba Inayopendekezwa imeondolewa mambo ya msingi yaliyotokana na maoni ya wananchi. Wanasema Katiba hii ni bora barani Afrika, sijui nani kawadanganya. Dk Slaa alisisitiza kuwa ili hali iwe shwari ni lazima kura ya maoni ifanyike wakati ambao Nec itakuwa imeliboresha Daftari la Wapigakura. “Watambue kuwa safari ya kudai Katiba Mpya ndiyo inaanza sasa kwa sababu Katiba Inayopendekezwa ni mali ya CCM, si Watanzania.”
Katibu Mkuu wa Taasisi ya Masheikh Wanazuoni wa Kiislamu Tanzania, Sheikh Khamis Mataka alisema, “Kama tunaamini kuwa Katiba Inayopendekezwa siyo nzuri, umefikia wakati wa kuwaachia wananchi wapige kura. Kama ni nzuri wataipitisha na kama hawaikubali wataikataa.”
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Ruaha, Profesa Gaudence Mpangala alisema, “Tangu mwanzo niliupinga mchakato wa Katiba na matokeo yake imezaliwa Katiba Inayopendekezwa isiyokuwa na maoni muhimu ya Watanzania. Sikubaliani na mchakato wa kura ya maoni.”
Profesa Mpangala alisema mchakato wa kupata Katiba Mpya unatakiwa kurudiwa mwaka 2016 kwa maelezo kuwa Katiba itakayopatikana haitakuwa na ridhaa kwa Watanzania.
Mwenyekiti wa Chama cha Ukombozi wa Umma (Chauma), Hashim Rungwe alisema, “Hayo ni matokeo ya nchi kuwa na sheria mbovu. Katiba yetu pamoja na sheria za nchi hii hazieleweki. Rais amepewa madaraka makubwa kiasi kwamba wengine wakitoa kauli hata kama wanaweza kufanya hivyo, kauli zao zinaonekana si kitu mbele ya kauli ya Rais.”

Saturday, 4 October 2014

Wanajeshi, polisi watwangana risasi

Tarime. Watu 12 wamejeruhiwa wakati wa mashambulizi ya kurushiana risasi baina ya askari wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) Kikosi 128 KJ cha Nyandoto na Polisi wa Kituo cha Stendi wilayani Tarime mkoani Mara.
Hatua hiyo imekuja wakati wanajeshi hao walipokuwa wakijaribu kumchukua askari mwenzao aliyekamatwa na Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani kwa kuendesha pikipiki bila kuwa na kofia ngumu.
Mashambulizi hayo ya kurushiana risasi na kutwangana ngumi na mateke yalitokea juzi saa 12 jioni katika Kituo cha Polisi Stendi.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime, Bernard Makonyo alisema amepokea majeruhi 10, kati ya hao wawili ni askari wa JWTZ, polisi saba na raia mmoja. Alisema majeruhi tisa wameruhusiwa na mwingine kupelekwa Hospitali ya Shirati kwa matibabu zaidi.
Dk Makonyo aliwataja waliojeruhiwa kuwa ni Aloyce Filbert (24) aliyepigwa risasi mguu wa kulia, Deodatus Dominic (26) aliyejeruhiwa puani na wote ni askari wa JWTZ.
Wengine ni askari polisi saba ambao ni Makoye Katula (26), Sylvester Michael (31), Salum Omary (44), Abdallah Halifa (24), Joel Msabila (25), Ally Juma (27) na Deogratius Tryphon (32) na raia Hamza Jumanne (33) aliyepigwa risasi mguu wa kushoto ambaye alipelekwa Hospitali ya Shitari, Rorya kwa matibabu.
Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya, Ndalama Salumu anadaiwa kujeruhiwa kwa kupigwa katika vurumai hizo huku mwananchi mwingine, David Kisaro (20) akijeruhiwa kwa bomu jichoni. Alitibiwa katika Zahanati ya Tarime.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Tarime/Rorya, Benedict Mambosasa alisema mwanajeshi aliyekamatwa alifanya makosa kwani baada ya kukamatwa na kuombwa kwenda kituo cha polisi, alikaidi.
Mambosasa alisema mwanajeshi huyo licha ya kukiuka taratibu, aliwatolea lugha za matusi polisi jambo lililowalazimu kumkamata kwa nguvu, ndipo wanajeshi wenzake walipoingilia kati na kusababisha kutokea kwa majibishano ya risasi za moto. Hata hivyo, alisema hakuna aliyejeruhiwa.
Alisema wanajeshi watatu ambao hawakutajwa majina, wamekamatwa na polisi kwa kuvunja utaratibu wa usalama.
Mkuu wa Wilaya ya Tarime, John Henjewele ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya, amelaani kitendo hicho cha kurushiana risasi za moto hewani akisema ni cha utovu wa nidhamu na maadili ya kazi ya jeshi na kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.
Alisema wananchi Tarime wameshangazwa kwa kitendo kilichofanywa na walinda usalama hao, wakisema si cha kinidhamu huku wakisema kilikwamisha shughuli zao kwa muda kwa kuhofia usalama wa maisha yao.
 Mkazi wa Tarime, Joseph Samson amesema kitendo hicho kimewashangaza sana wananchi.

KATIBA: Mtifuano wahamia uraiani

Dar es Salaam. Baada ya Bunge la Katiba juzi kufanikiwa kupata theluthi mbili ya wajumbe wa pande zote mbili za Muungano na kupitisha Katiba inayopendekezwa, sasa msuguano kuhusu Katiba unaonekana kuhamia uraiani.
Msuguano kuhusu Katiba hiyo unatarajiwa kuendelea mitaani, ndani ya vyama vya siasa na kwenye majukwaa kutokana na tofauti ya mitizamo iliyoibuka kuhusu Rasimu ya Katiba iliyopitishwa.
Ingawa matokeo ya kura za ushindi yalipokewa kwa furaha na wajumbe waliokuwapo bungeni kwa kucheza na kurusha vijembe kwa wapinzani, huenda kibarua kitakuwa kigumu kwa CCM itakapolazimika kupambana na wananchi, wanasiasa, wanaharakati na viongozi wa dini ‘waliojeruhiwa’ na mwenendo wa Bunge.
Bunge hilo liliendeshwa kwa upinzani mkali kutoka kwa makundi mbalimbali ya watu waliokuwa wakitaka lisimamishwe kwa madai kuwa limechakachua maoni yao kama yalivyopendekezwa kwenye Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni na Tume ya Jaji Joseph Warioba.
CCM na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar
CCM iliingia doa baada ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Othman Masoud Othman kuzua kizaazaa bungeni Jumatano wiki iliyopita kwa kupiga kura ya hapana katika ibara 22 kwenye Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa.
Mwanasheria huyo ambaye awali alijiondoa kwenye Kamati ya Uandishi kwa kutoridhishwa na mambo yalivyokuwa yanakwenda, alizomewa na baadhi ya wajumbe na kulazimika kutolewa ukumbini akiwa chini ya ulinzi wa askari wa Bunge.
Akizungumza na gazeti hili, Othman alisema kuwa alichofanya kilikuwa ni utashi wake kwa kuwa Serikali ilitamka kwenye Baraza la Wawakilishi na hata nje ya Baraza kuwa haikuwa na msimamo.
 “Kwa hiyo kama Serikali haikuwa na msimamo kwa maana ya upande, maana yake ni ipi pengine unisadie… nilipiga kura kwa kuzingatia utashi wangu na maoni yangu,” alinukuliwa Othman.
Ingawa Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Samuel Sitta alimtetea Othmani kwa kusema wajumbe hawakupiga kura kwa kutumia vyeo vyao, kwa namna wajumbe walivyoonyesha jazba imeonyesha kuwa CCM itapaswa kusafishwa taswira iliyochafuka.
Sitta na viongozi wa dini
Kwa upande mwingine, Sitta amejikuta akiingia kwenye ‘vita’ na viongozi wa dini, baada ya kuwataka waumini wa madhehebu mbalimbali kuupuza nyaraka zilizotolewa na viongozi hao kwa kuwa hazina utukufu wowote wa Mwenyezi Mungu.
Sitta alisema baadhi ya viongozi wa dini wanalenga kuliingiza taifa kwenye machafuko na kwamba yeye hatakuwa tayari kuvumilia hali hiyo.
Waraka huo ulitolewa kwa pamoja na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (FPCT) na Kanisa la Waadventista Wasabato (SDA).
Huku akiwa na waraka huo mkononi, Sitta alisema kuwa lugha iliyotumika haina staha na haikupaswa kutumiwa na watu wanaohubiri dini duniani.
Akizungumzia kauli ya Sitta, Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Methodius Kilaini alisema kauli ya Sitta inaonyesha kuwa amechoshwa na mwenendo wa Bunge la Katiba.
 “Sikutarajia kiongozi kama huyo kutoa kauli mbaya kama hiyo kwa Taifa zima. Sikutegemea mheshimiwa kama huyo kusema maneno kama hayo… Huenda ana stress (msongo wa mawazo). Hata ikiwa hivyo, hakupaswa kutoa kauli nzito kama hiyo. Anatakiwa kufahamu kuwa waraka huo umetoka kwa Wakristo wote hapa nchini,” alisema Askofu Kilaini.
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema-Bara, John Mnyika jana alisema kitendo cha Sitta na wenzake kushindwa hata kuelewa waraka wa viongozi wa dini na kuuita kuwa “hauna utukufu wa Mungu na wa kipuuzi”, ni wazi wamelewa madaraka wasaidiwe kwa kupumzishwa.
Hata hivyo, jana Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC) Father Raymond Saba, amesema bado wanaendelea kutafakari kauli ya Sitta na kwamba kwa sasa hawajatoa taarifa yoyote.
Akizungumzia kauli ya Sitta, Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Hamad Salim alisema kauli ya kiongozi huyo imeongeza mpasuko wa dini nchini hasa kuhusu mahakama ya kadhi.
“Viongozi wa dini wameipokea kauli ya Serikali kwa kuwa tu alisema ni kiongozi wa Serikali, lakini itatokea shida kama ahadi yao haitatekelezwa,” alisema Salim.
Sitta na Jaji Warioba
Sitta amejikuta kwenye vita ya maneno na Jaji Warioba huku kila mmoja akisisitiza kuwa anafanya kazi aliyotumwa na wananchi.
Akizungumza katika maadhimisho ya miaka 19 tangu kuanzishwa kwa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) hivi karibuni, Jaji Warioba alisema ataingia mitaani kuitetea Rasimu ya Katiba iliyokuwa imebeba maoni ya wananchi.
Alisema kuwa Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa na Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba imeondoa mambo manne muhimu.
Hata hivyo, akizungumza jana na gazeti hili alisema kuwa Katiba hiyo imeacha maswali mengi kuliko majibu hasa kwa upande wa Zanzibar.
Sitta alalamikia kutukanwa
Sitta atakuwa na kibarua kingine cha kujisafisha mbele ya wananchi ambao alikaririwa akisema kuwa wamekuwa wakimtumia meseji za matusi za ya 50 kila siku.
Kwa nyakati tofauti wananchi wasiojulikana wamekuwa wakiandika meseji za matusi kwenye mitandano na simu kwa kile wanachosema kuwa Sitta amelazimisha maoni ya CCM yatawale Bunge.
Wananchi wasubiri waelezo zaidi
Baadhi ya wananchi waliohojiwa kuhusu mwenendo wa Bunge hilo, waliwalaumu wajumbe wa Bunge waliokuwa wakisema walipiga kuwa kwa niaba ya wananchi kwenye majimbo yao.
Walihoji ni lini wajumbe hao ambao ni wabunge wao walikwenda kuwauliza iwapo wanataka kupiga kura ya hapana au ndiyo dhidi ya Katiba iliyopendekezwa?
‘Mimi nimesikia tu mbunge wetu (anamtaja) amesema wananchi wake wamechagua kura ya ndiyo. Ni nani alimtuma kwenda kuwa tunataka Katiba hiyo wakati maoni yetu tulitoa tofauti, “ Yohana Change mkazi wa Vwawa, Mbozi.
Mwanaidi Suleiman alisema haelewi nini kilichotokea bungeni, kwa kuwa matarajio aliyokuwa nayo kuhusu Katiba yameyeyuka baada ya kusikia mambo mengi yamekataliwa.
“Nafuu kama wangeondoa mambo mengine, lakini siyo serikali tatu na uraia wa nchi mbili. Mimi hayo niliyaona makubwa sana, kama hayapo sasa Katiba itahusu nini?” alihoji Mwanaidi.
Chadema na wanachama wake.

Hali ya hewa ndani ya Chadema ilichafuka baada ya Sitta kusema kuwa kuna wajumbe wawili wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kutoka Zanzibar walikubali kupiga kura kinyume na msimamo wa vyama vyao.
Sitta alisema kuwa kati ya wajumbe hao, mmoja alikubali kupiga kura na kusema yuko tayari hata kufukuzwa na chama chake.
“Sasa wale wanaotumia mbinu za ovyoovyo ili mchakato huu usikamilike wanapoteza muda, maana ukizuia maji huku, yanaelekea kwenye mkondo mwingine,” alisema Sitta.
Taarifa hizo zilionekana kuwalenga wabunge wa Viti Maalumu, Maryam Msabaha na Mwanamrisho Abama ambao kwa nyakati tofauti walithibitishwa kutafutwa ili apige kura.
“Kweli nimesumbuliwa sana na watu ambao siwezi kuwataja na wananitaka nipige kura na wengine walifika mpaka nyumbani lakini mimi siwezi kushiriki maana nikifanya hivyo dhamiri yangu itanishtaki,” alisema Msabaha.
Naye Abama alisema kuwa alikuwa amepewa ilani na viongozi wake kwamba anatafutwa ili akapige kura, hivyo aliamua kukaa ndani kukwepa mtego huo.
Kauli hizo mbili tofauti zinauachia Ukawa maswali magumu yanayohitaji majibu ili kubaini iwapo kuna usaliti wowote umefanyika au la.
Wabunge wengine ambao wanaweza kukukumbana na matatizo ndani ya chama hicho ni Mbunge John Shibuda (Maswa Mashariki), Said Arfi (Mpanda Mjini) ambao walikiuka uamuzi wa Ukawa kutoshiriki Bunge hilo.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa jana alisema kuwa suala la wasaliti wa chama linatarajiwa kuzungumzwa kwenye vikao vya ndani.
“Siwezi kulitolea uamuzi suala hilo, baada ya kumaliza uchanguzi sasa litazungumzwa ndani ya vikao vya chama na kutolewa uamuzi,” alisema Dk Slaa.
Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Julius Mtatiro alisema kuwa Sitta alipaswa kuwataja wajumbe kutoka Ukawa waliokubali kupiga kura, lakini hakufanya hivyo.
“Juzi amechukua kura zao na hawataji ni kina nani wala walipiga kura kwa njia gani. Hata akijiongezea hizo kula mbili feki bado BMK upande wa Zanzibar wanabakiwa na kura 145 tu na siyo 146,” alisema Mtatilo.
Wanananchi waikataa rasimu
Naye Joseph Lyimo kutoka Manyara, amesema kuwa baadhi ya wakazi wa mkoani humo, wamesema Bunge la Katiba limepitisha rasimu ya Katiba bila maridhiano kwa baadhi ya wajumbe hivyo kusababisha hofu ya kupatikana kwa katiba mpya itakayokidhi matakwa ya wananchi.
Wakizungumza jana na mwandishi wa habari hizi, wananchi hao walidai kuwa rasimu hiyo iliyopitishwa bungeni juzi haikukidhi maoni yaliyotolewa kwenye tume ya Warioba kwani ibara 28 zimefutwa na kuwapo ibara mpya 42.
Mkazi wa mji mdogo wa Mirerani, Abdalah Mtengeti alisema kwenye Tume ya Warioba wananchi walipendekeza mbunge awe na ukomo wa madarakani kwa miaka 15, lakini sasa wabunge hao wameridhia asiwe na mwisho wa utawala.
“Wananchi hawawezi tena kumwajibisha  mbunge waliyemchagua wao wenyewe kama walivyopendekeza awali pia hakuna ukomo wa mbunge tena hivyo atatawala hadi mwenyewe aseme sigombei tena,” alisema Mtengeti.
Mwenyekiti wa Bavicha Mkoa wa Manyara, Frank Oleleshwa alisema rasimu hiyo ya wabunge haikujali maoni ya wananchi kwani walipendekeza kufutwa kwa vyeo vya wakuu wa mikoa na wilaya lakini, wabunge wameridhia.
“Pia wananchi walipendekeza kuwepo na Serikali tatu ikiwamo kurudisha Tanganyika ili kuwapo na usawa wa nchi, lakini wabunge wamegoma hilo na kuridhia Rais wa Zanzibar awe makamu wa pili wa Rais,” alisema Oleleshwa.
CCM, CUF Zanzibar
 Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai walipozungumza na  gazeti hili kwa nyakati tofauti visiwani humo, Mazrui alisema kwamba mambo yaliyopitishwa na Bunge la Katiba katika rasimu hiyo yanagongana na Katiba ya Zanzibar iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2010 ikiwamo suala la mamlaka ya ugawaji mikoa aliyopewa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kushauriana na Rais wa Zanzibar.
Alisema Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano utekelezaji wake utakuwa mgumu kwa baadhi ya mambo Zanzibar mpaka Katiba ya Zanzibar ifanyiwe tena marekebisho na kabla ya kufanyika hivyo lazima kuitishwe kura ya maoni kwa wananchi.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema kwamba kama viongozi wote watafanya kazi kwa kuzingatia sheria na katiba, Serikali ya Umoja wa Kitaifa(SUK) haitoyumba kwa sababu hakuna mshindi wala mshindwa baada ya rasimu ya katiba kupitishwa.
“Matokeo ya kura ya rasimu ya katiba, ni ushindi wa wazanzibari wote na watanzania kwa ujumla, na hakuna mshindi wala mshindwa” alisema Vuai ambaye pia alikuwa mjumbe wa bunge maalum la katiba.

Warioba: Katiba bado ina maswali mengi

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Bunge Maalumu la Katiba kupitisha Katiba inayopendekezwa, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema Katiba hiyo bado ina maswali mengi kuliko majibu, hasa katika muungano na mgombea binafsi.
Amesema licha ya Zanzibar kuridhia mambo kadhaa kuwekwa katika orodha ya mambo ya muungano, hali inaweza kuwa tofauti ukifikia wakati wa Zanzibar kubadili Katiba yao ili kuwezesha utekelezaji wa mabadiliko hayo.
Juzi Bunge hilo lilipitisha Katiba inayopendekezwa kwa tofauti ya kura mbili na kuhitimisha kwa sasa mchakato wa kuandika Katiba hadi mwaka 2016 ambapo litafanyika zoezi la upigaji wa kura ya maoni.
Akizungumza na Mwananchi Jumamosi jana, Jaji  Warioba alisema, “Wasiwasi wangu ni juu ya muungano kwa sababu katika masharti ya mpito ni lazima Zanzibar ifanye marekebisho ya Katiba yake. Rasimu inayopendekezwa inasema Tanzania itakuwa nchi moja pamoja na madaraka ya rais kugawa nchi. Kwa maana hiyo lazima Katiba ya Zanzibar ibadilike.”
Alisema katika mambo ya muungano, Katiba inayopendekezwa imeliweka suala la kodi ambalo halikuwamo katika rasimu iliyotolewa na Tume ya Katiba, kusisitiza kuwa kitendo hicho hakitajibu swali la ‘Tanganyika kuvaa koti la Muungano’.
“Wameongeza kodi ya mapato, ushuru wa forodha  na bidhaa katika mambo ya muungano. Maana yake ni kwamba kodi yote inayokusanywa, ikiwamo ya kutoka Zanzibar itaingizwa kwenye mfuko wa muungano,”alisema.
Aliongeza, “Wakati huo huo Zanzibar imepewa uwezo wa kusimamia mambo yake yenyewe na ili iweze kulitekeleza hilo ni lazima iwe na vyanzo vyake vya mapato. Sasa watasimamiaje wakati mapato yote yanaingia kwenye mfuko wa muungano.”
Alisema ili suala hilo liweze kutekelezwa ni lazima Zanzibar ibadili Katiba yake na kusisitiza kuwa utakapofika wakati wa kubadili Katiba ya Zanzibar, jambo hilo linaweza kukwama.
“Sioni kama Wazanzibar watakubali suala hili. Kama mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar yatakwama, ni wazi kuwa Katiba inayopendekezwa haitatekelezeka. Mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar yanategemea maridhiano ya Wazanzibari wenyewe na kumbuka kuwa CUF na CCM wanavutana sana,” alisema Jaji Warioba.
Akifafanua hilo, alisema mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar lazima yapate theluthi mbili ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na kusisitiza kuwa kwa mvutano wa vyama hivyo viwili visiwani Zanzibar, itakuwa kazi ngumu kupitisha jambo hilo.
“Katiba ya Zanzibar isipobadilishwa kero za muungano zinazozungumzwa zitaendelea. Kazi iliyopo sasa ni kufikiria maridhiano kuhusu muungano, lazima tuhakikishe Zanzibar imekubali kubadili katiba yake na kuridhia mapato yake kuingizwa katika mfuko wa muungano,” alisema.
Aliongeza, “Kama ambavyo Tanzania Bara waliitegemea Zanzibar kupitisha Katiba inayopendekezwa, ni lazima pia ihakikishe kuwa Zanzibar inakubali kubadili Katiba yake.”
Kuhusu mgombea huru Jaji Warioba alisema, “Katiba inayopendekezwa imeweka masharti ya mgombea ubunge na kutaja sifa za ziada za mgombea huru ambazo ukizitazama kwa undani utabaini kuwa wanamkataa mgombea huru kistaarabu.”
Alisema sifa hizo za ziada walitakiwa kuwekewa na wagombea wengine, si mgombea huru pekee.
“Mfano ni kutoruhusu mtu kutoka katika chama cha siasa kisha  kugombea kama mgombea huru,” alisema.
Jaji Warioba aliyataja baadhi ya mambo ya msingi yalikuwamo katika rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kuingizwa tena katika Katiba inayopendekezwa kuwa ni malengo muhimu ya kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kimazingira.

Ukawa sasa waja na tuhuma nzito kuhusu kura

Dar es Salaam. Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) umeibua shutuma dhidi ya uongozi wa Bunge Maalumu la Katiba kwamba unawarubuni kwa fedha baadhi ya wajumbe wa umoja huo ili kuipigia kura Katiba inayopendekezwa.
Kamati ya Ufundi ya Ukawa, ilisema jana kuwa wajumbe wanaorubuniwa wapige kura ya ‘ndiyo’ kwa ahadi ya kupewa zaidi ya Sh500 milioni ni wa CUF na wengine wanne wa Chadema wanaotoka Zanzibar.
Hata hivyo, Katibu wa Bunge la Katiba, Yahya Khamis Hamad alikanusha madai hayo, akisema hajasikia kitu kama hicho na ndiyo kwanza alikuwa anasikia hilo kutoka kwa mwandishi wa habari hizi... “Hakuna kitu kama hicho, hilo jambo ndiyo nalisikia kutoka kwako.”
Kutokana na madai hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Ukawa, John Mnyika alisema kamati hiyo ilianza kikao cha siku mbili kuanzia jana kujadili hali hiyo na kutoa mapendekezo kwa uongozi wa juu wa umoja huo.
Licha ya Mnyika kukataa kutaja majina ya wajumbe waliorubuniwa, wajumbe wa Chadema wanaotokea Zanzibar ni Zeudi Abdallah ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti Baraza la Vijana Chadema (Bavicha), Maryam Msabaha, Mwanamrisho Abama na Raya Ibrahim. “Tumewataka wajumbe wetu wote kukusanya ushahidi na kuuwasilisha kwa viongozi wa Ukawa,” alisema Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Bara.
Aliongeza, “Chadema ina wajumbe wanne, watatu ni wabunge wa kawaida na mmoja wa kuteuliwa na Rais (Kundi la 201). Tumepata taarifa kutoka kwa wajumbe hao kwamba wanapigiwa simu na uongozi wa Bunge ukiwataka wasaini karatasi za kupigia kura ili uongozi wa Bunge uchakachue kura.
“Tumeanza kikao kujadili suala hili ila tumeamua kwanza tuueleze umma kupitia vyombo vya habari juu ya ‘uharamia’ unaofanywa na Bunge la Katiba linaloongozwa na Sitta (Samuel) na Makamu wake Samia (Suluhu Hassan).”
Ukiukaji kanuni
Akinukuu Kifungu cha 36 (3) cha Kanuni za Bunge la Katiba, Mnyika alisema si sahihi Sitta kutaka wajumbe waliopiga kura ya ‘hapana’ kuitwa katika Kamati ya Mashauriano na uamuzi huo ni kinyume na kanuni...
“Ni kama kuwatisha tu wajumbe.”
Kanuni hiyo inasema; “Endapo baada ya ibara ya Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa upya kupigiwa kura, theluthi mbili ya wajumbe wote kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya wajumbe wote kutoka Tanzania Zanzibar haikufikiwa, basi ibara hiyo itapelekwa kwenye Kamati ya Mashauriano ili kupata mwafaka.”
Sitta awataje
Mjumbe mwingine wa kamati hiyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fedha wa CUF, Joran Bashange alimtaka Sitta kutaja majina ya wajumbe wa CUF na Chadema waliopiga kura... “Tunamtaka awataje kwa majina maana ujanja wake na wenzake tumeshaujua na tuna ushahidi wote.”
Bashange alisema mpaka sasa hakuna mjumbe wa Bunge hilo ambaye ni mjumbe wa Ukawa aliyepiga kura kupitisha Katiba inayopendekezwa.
“Ndiyo maana walibadili kanuni ili kuruhusu wajumbe kupiga kura kwa faksi na baruapepe ili kufanya ‘uharamia’ wa kuiba kura,” alisema.

Friday, 19 September 2014

Mbowe ajisalimisha polisi, Shughuli zasimama

Dar es Salaam. Shughuli za kiserikali katika Wizara ya Mambo ya Ndani na ofisi jirani, jana zilisimama kwa siku nzima kutokana na hekaheka zilizoibuka baina ya polisi na wafuasi wa Chadema pale mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe alipojisalimisha polisi.
Hekaheka hizo ziliibuka kuanzia saa 5.10 asubuhi baada ya Mbowe akiongozana na wanasheria wa chama hicho, kufika katika ofisi za Makao Makuu ya Polisi ambako pia zipo ofisi za wizara hiyo kuhojiwa kuhusu kauli yake ya kuitisha maandamano nchi nzima kushinikiza kusitishwa kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Kabla ya Mbowe kuwasili, alifika Mkurugenzi wa Oganaizesheni ya Mafunzo na Usimamizi wa Kanda wa Chadema, Benson Kigaira na alipojitambulisha akakataliwa kuingia.
Baadaye waliwasili mawakili, Profesa Abdallah Safari na Mabere Marando ambao waliruhusiwa kuingia, kisha wakafuata Mbowe, John Mnyika na wanasheria wengine akiwamo John Malya na Peter Kibatala.
Wakati huo, Barabara ya Garden inayokatiza mbele ya wizara hiyo ilikuwa imefungwa na wafuasi wa Chadema walikuwa wamezuiliwa kwa mbali. Kila mwananchi aliyefika katika jengo hilo kupatiwa huduma, alijibiwa na askari waliokuwa na mbwa na silaha kuwa, “hakuna shughuli yoyote inayofanyika hadi kesho (leo)”.
Hali hiyo iliendelea hadi saa 9:10 alasiri baada ya Mbowe aliyehojiwa kwa saa mbili kuhusu tuhuma za uchochezi kuachiwa kwa dhamana.
Baada ya kuachiwa, Mbowe alisindikizwa kwa msafara wa magari manne ya polisi akielekea Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, ambako alipanda ndege kwenda Afrika Kusini kwa shughuli za kichama.
Ilivyokuwa
Ombi lililotolewa juzi na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Bara), John Mnyika kuwataka wanachama wa Chadema kujitokeza kumsindikiza Mbowe polisi, liliitikiwa kwani zaidi ya wanachama 100 walijitokeza katika ofisi hizo.
Walianza kukusanyika mmoja baada ya mwingine nje ya makao mkuu ya jeshi hilo kuanzia saa 4:30 asubuhi na kujichanganya katika kundi la waandishi wa habari, hali iliyosababisha askari polisi waliokuwa na bunduki na mabomu ya machozi kuwataka wanahabari wajitambulishe kwa kuonyesha vitambulisho ili wawatenge na wafuasi hao.
Licha ya juhudi hizo, hawakufanikiwa kuwatawanya wanachama hao ambao awali, walijieleza kuwa walikuwa wamefuata hati zao za kusafiria katika Ofisi za Uhamiaji zilizopo eneo hilo.
Hali ilibadilika baada ya Mbowe kufika katika ofisi hizo akiwa katika msafara wa magari matano huku ukiongozwa na Mnyika na wanachama hao kuanza kuimba nyimbo za chama hicho na kumsifu kiongozi wao.
Msafara huo ulizuiwa kwenye lango la ofisi hizo na askari wa FFU waliwazuia viongozi wengine, wakisema anayetakiwa kuingia ndani ni Mbowe na wanasheria wake pekee.
Baada ya gari la Mbowe kuingia, viongozi na baadhi ya wafuasi wa chama hicho nao walipenya kwa nguvu getini na kuingia ndani ya uzio huku wakisema ‘people’s power’ (nguvu ya umma). Kitendo hicho kiliwatibua FFU na kuanza kutumia nguvu kuwatoa nje, hali iliyozua vurugu kubwa.
Kutokana na mvutano huo, askari zaidi wa FFU waliokuwa katika Land Rover mbili wakiwa na mbwa waliongezeka na kuanza kuwashushia kipigo wafuasi hao huku wakiwataka kusimama umbali wa mita 100 kutoka lilipo jengo hilo.
Baada ya kutolewa ndani ya uzio baadhi ya wafuasi wa Chadema walikaa chini wakisema hawatafanya vurugu na wako tayari kuingia ndani wakiwa wamenyoosha mikono juu.
Katika kundi la wafuasi hao walikuwamo pia baadhi ya wabunge wa Chadema, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ (Mbeya Mjini), Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini) na Ezekiel Wenje (Nyamagana).
Wabunge waliofika baadaye na kuruhusiwa kuingia ndani ni Suzan Lyimo (Viti Maalumu) na Halima Mdee (Kawe).
Miongoni mwa walioathirika na hekaheka hizo ni wanahabari ambao pamoja na kuonyesha vitambulisho na kamera, baadhi yao walishushiwa kipigo na askari hao.
Katika kipigo hicho, mwandishi wa Habari wa Gazeti la Tanzania Daima, Josephat Isango na Mwandishi gazeti la Hoja, Shamimu Ausi walijeruhiwa. Isango alijeruhiwa mguuni na Ausi usoni karibu na jicho la kulia.
Wakati Isango alisema alivamiwa na askari wawili wa FFU na kwamba hata alipojitambulisha na kuwaonyesha kitambulisho waliendelea kumpiga, Ausi alisema alipigwa rungu usoni na akashangazwa na nguvu kubwa iliyotumika wakati awali, aliruhusiwa kusimama katika eneo alipokuwa akiendelea na kazi.
Baada ya vurugu hizo waandishi wa habari na wafuasi wa chama hicho walitakiwa kusimama katika makutano ya Barabara ya Ghana na Ohio umbali wa mita 100 kutoka yalipo makao makuu ya jeshi hilo kusubiri mahojiano yaishe.
Ilipofika saa 8.45, Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu alitoka nje ya ofisi hizo na kuzungumza na waandishi wa habari na wafuasi wa chama hicho.
Alisema mahojiano kati ya Mbowe na Jeshi la Polisi yalikwenda vizuri huku akiongozwa na wanasheria na kwamba polisi wamekubali kumpa dhamana lakini kabla hajaondoka, wafuasi wote wanatakiwa kuondoka eneo hilo bila maandamano.
“Polisi wanaomba mtawanyike, hawataki maandamano, wao watamsindikiza hadi makao makuu ya chama yaliyopo Kinondoni, mkifanya maandamano watatumia nguvu kuyazuia na hilo hawataki litokee. Nawaomba mtawanyike,” alisema Lissu.
Baada ya tangazo hilo, wafuasi hao kwa shingo upande, walikubali ushauri huo na kuondoka katika eneo hilo saa 9.00 alasiri.
Ilipofika saa 9.20 Mbowe alitoka katika ofisi hizo akisindikizwa na magari ya polisi aina ya Land Rover zilizojaa askari na baadaye ilielezwa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa aliyekuwa makao makuu ya chama hicho kuwa mwenyekiti huyo alikwenda moja kwa moja Uwanja wa Ndege kwa safari ya kikazi Afrika Kusini.
Mtikila azua gumzo
Wakati hekaheka zikiendelea, Mwenyekiti wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila alifika katika ofisi hizo saa 7.26 akiwa katika Bajaj lakini alizuiwa kuingia ndani na akaondoka.
Akizungumza na wanahabari, Mtikila alisema, “Ni lazima Watanganyika tuidai Tanganyika yetu kwa gharama yoyote, aluta continua.”
Makao Makuu
Baada ya kuondoka eneo hilo, wafuasi wa Chadema walikwenda katika ofisi za makao makuu ya chama hicho, Mtaa wa Ufipa, Kinondoni na kupewa maelekezo na Dk Slaa na Lissu.
Lissu alisema Mbowe anatuhumiwa kwa uchochezi kwa kauli yake kuhusu kufanyika maandamano nchi nzima, huku akisisitiza kuwa tuhuma alizopewa “ni za wizi wa kuku”.
“Mbowe aliposema kufanyika maandamano alikuwa na maana kuwa maandamano hayo yatafanyika baada ya Chadema kutoa taarifa, kauli yake haikuwa ya uchochezi hata kidogo,” alisema Lissu.
Aliongeza, “Kama polisi wakitueleza ni sheria ipi inakataza maandamano, sheria ipi inalazimisha wanaotaka kuandamana lazima wawe na kibali na sheria ipi inakataza watu kugoma, watakuwa na ruksa ya kumfunga Mbowe.”
Kwa upande wake, Dk Slaa alisema, “Mbowe baada ya kutoka polisi ameomba nimwagie kwa wanachama wa Chadema. Amekwenda Afrika Kusini katika mkutano wa chama. Safari yake ilikuwa imepangwa tangu juzi na ingeahirishwa kama angenyimwa dhamana leo.”Dk Slaa alimwagiza Kigaira kuhakikisha kuwa wanachama wawili wa chama hicho waliokamatwa na polisi wanaachiwa kwa dhamana. Zoezi la kufanya maandamano likifanyika kama hivi Taifa hili litabadilika,” alisema.

Saturday, 13 September 2014

Uwekezaji ulivyoua Mji wa Mirerani-2

Sheikh Mohammed anasema serikali ndio inawanyanyasa wananchi wake kwa kupitisha sheria ambazo zinawazuia kunufaika na rasilimali za taifa lao ambazo Mungu amewapa.
“Wachimbaji wadogo wamepewa migodi yenye ukubwa wa mita 50 kwa 50 lakini mchimbaji mmoja mkubwa amepewa eneo kubwa zaidi ya eka tano halafu inapitishwa sheria ya kuchimba kwenda chini jambo ambalo haliwezekani huku ni kuwazuia wachimbaji wadogo kupata madini” alisema.
Alisema kwa sasa shughuli nyingi za msikiti huo zimesimama kwani wananchi wa Mirerani hawana fedha za kutoa sadaka tofauti na miaka ya nyuma ambapo sadaka ziliwezesha ujenzi wa msikiti huo, shule na kuwa na miradi.
Padri Aloyce Kitomali wa Kanisa la Katoliki Mirerani, alisema kanisa hilo lilikuwa na uwezo wa kukusanya sadaka katika ibada moja zaidi ya milioni moja lakini sasa hata Sh500, 000 hazipatikani kwani waumini hawana fedha.
Anasema miradi mingi ya kanisa hilo, sasa imezorota kwani wananchi wengi wanategemea madini ya tanzanite ambayo sasa hayapatikani na inasemekana anayepata ni mwekezaji.
“Wananchi hapa wengi wana hali ngumu ya maisha tofauti ya miaka ya nyuma kwani uchumi wao ulitegemea sana madini ya Tanzanite” alisema.
Osca Gunewe ambaye ni Katibu wa Bodi ya shule ya Kanisa la Pentekoste, anasema uchumi wa mji wa Mirerani unategemea madini ya Tanzanite hivyo kwa hali iliyopo sasa ni muhimu Serikali kuwasaidia wakazi wa mji huo.
Gunewe ambaye aliwahi kuwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mirerani, anasema ingewezekana kuwasaidia watu wa Mirerani hata kwa kutolewa ajira kwa vijana wa Mirerani katika migodi ya mwekezaji.
Anasema lakini kampuni hiyo, haiajiri vijana wa Mirerani na hivyo sasa wapo mitaani tu kwani hata migodi ya wachimbaji wadogo mingi imesimama na ambayo inaendelea na kazi, inachukua vijana wachache sana.
Omar Awadhi alikuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mirerani miaka 10 iliyopita, anasema, maisha ya Mirerani sasa yamebadilika na hata uchangiaji shughuli za maendeleo umepungua sana. Anasema Mirerani licha ya utajiri wote, haina hata huduma ya maji safi, kwani ndoo moja inauzwa kati ya Sh400 na 500.
Awadhi anasema maji hayo yanatolewa Wilaya ya Hai Mkoa wa Kilimanjaro kitu ambacho siyo sahihi kulingana na utajiri wa tanzanite ambayo inapatikana Mirerani pekee duniani.
“Tatizo hapa ni mwekezaji kama madini haya yangechimbwa na wachimbaji wadogo pekee hali isingekuwa hivi, kwani watu wengi wangepata madini japo kidogo kidogo lakini yangeendelea kuujenga Mji wa Mirerani na hata mikoa ya jirani,” anasema.
Robo tatu ya migodi ya wachimbaji wadogo imesimama
Mayala Raurenti ni Ofisa Madini, Mirerani. Anakiri uchimbaji wa madini hayo kuzorota kwa wachimbaji wadogo, lakini anasema chanzo ni mahitaji makubwa ya teknolojia.
Raurenti anasema madini katika maeneo ya kitalii B na D vinavyomilikiwa na wachimbaji wadogo tofauti na miaka ya nyuma sasa yapo mbali na hivyo kuhitaji teknolojia za kisasa.
Hivi sasa wachimbaji wadogo, wamepungua kutokana na upatikanaji madini kuwa mgumu na kuanza kutumia mashine badala ya watu katika kupandisha michanga juu ya mgodi na hata kuchimba.
Mihayo Franeis ni Ofisa wa Miamba (jiolojist) katika machimbo ya Tanzanite Mirerani. Anasema kati ya migodi zaidi ya 400 ya wachimbaji wadogo ni migodi 120 tu ndiyo inachimbwa kila siku.
Anasema hali hiyo, ,imesababisha kupungua sana kwa wachimbaji wadogo kwani pia migodi hiyo, ambayo awali ilikuwa inawafanyakazi zaidi ya 4,000 sasa hawafiki 500.
“Mgodi ambao ulikuwa na wachimbaji wadogo 100 sasa wapo 15 hii inatokana na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchimbaji,” anasema.
Anasema hata mamia ya vijana ambao walikuwa wamejiajiri kuchambua michanga na kupata dhahabu sasa hawapo na ndio sababu watu wamepungua sana Mirerani. Anasema kitalu B kina migodi 183 na kitalu D kina migodi 368 lakini ambayo inachimbwa kila siku si zaidi ya migodi 120 hivyo ndio sababu mji kama wa Mirerani uliokuwa unategemea madini hayo umebadilika.
Hata hivyo, anakiri licha ya migodi kuwa michache inayochimbwa bado upatikanaji madini siyo kama zamani kwa kuwa miamba ipo mbali zaidi kwa migodi mingi.
“Ni kweli migodi mingi ya wachimbaji wadogo haipati madini, tatizo ni kuwa maeneo mengi yamechimbwa tayari na sasa madini yapo chini zaidi hivyo gharama za uchimbaji ni kubwa,” anasema.
Akizungumzia malalamiko ya wachimbaji kuwa madini mengi yapo eneo la mwekezaji alisema siyo sahihi kwani madini yote yapo kwenye miamba katika eneo la Mirerani lakini kwa maeneo ya wachimbaji wadogo yapo chini zaidi.
Serikali sasa yalia kukosa kodi Mirerani.
Martha Umbulla ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro. Anakiri hali ngumu ya maisha Mirerani lakini anasema hata kodi kutoka katika madini hayo, wilaya hiyo hainufaiki kwa sasa.
“Wakazi wa Mirerani wanategemea madini, sasa hayapatikani hivyo uchangiaji maendeleo siyo mzuri lakini Serikali tungeweza kupata hata kodi kutoka kwa wachimbaji hasa mwekezaji lakini hatupati,” anasema.
Anafafanua kuwa kodi ya mapato ya madini hayo, wachimbaji wanalipa Arusha kutokana na mji wa Mirerani kutokuwa na ofisi za Mamlaka ya kodi (TRA).
Alisema Serikali inafanyia kazi matatizo ya Mirerani ili kuona wananchi wataishi vipi na kutokwama shughuli mbali mbali za kiuchumi. Huu ndiyo mji wa Mirerani ambao sasa upo hoi na wananchi wanalia kila kona baada ya kushindwa kunufaika na madini ya Tanzanite.

Halima Mdee aibuka kidedea Bawacha

Dar es Salaam. Mbunge wa Kawe, Halima Mdee amechaguliwa kwa kishindo kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la Chadema (Bawacha) kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Suzan Lyimo.
Mkutano Mkuu wa Bawacha wa uchaguzi ulifanyika katika Ukumbi wa Mlimani City jijini hapa na ulianza juzi asubuhi na kuhitimishwa jana asubuhi.
Msimamizi wa uchaguzi huo, Arcado Ntagazwa akitangaza matokeo hayo jana alisema, Halima Mdee amepata kura 165 dhidi ya wapinzani wake sita ambao ni, Lilian Wasira kura (11), Chiku Abwao (15), Sophia Mwakagenda (18), Rebeka Magwisha (14) na Janeth Rither(35).
Kwa upande wa nafasi ya makamu mwenyekiti bara, Ntagazwa alimtangaza Hamida Abdalla aliyepata kura 125 dhidi ya Mariam Msabaha aliyejikusanyia kura 66 katika uchaguzi ulioingia ngwe ya pili baada ya kwanza kukosekana mshindi kutokana na kutofikisha asilimia 50 ya makamu mwenyekiti katika kura zilizopigwa. Naye Hawa Mwaifunga aliibuka mshindi wa nafasi ya makamu mwenyekiti bara kwa kupata kura 136 dhidi ya kura 99 alizopata Victoria Benedict katika uchaguzi uliorudiwa mara ya pili baada ya awali kushindwa kumpata mshindi.
Mdee ambaye pia ni Mbunge wa Kawe akizungumza mara baada ya kutangazwa mshindi jana asubuhi alianza kwa kuwashukuru wanawake wote waliompigia kura na hata wale ambao hawakumchagua kwani walitumia demokrasia yao.
“Wanawake tutaweza kusonga mbele kama tukipendana kwani uwezo, nguvu na nia tunazo, siri ya kuingia Ikulu mwaka 2015 ni kuwa na wanawake wengi ndani ya Bawacha lakini watakaokipigania chama,” alisema Mdee na kuongeza:
“Viongozi tuliochaguliwa tunatakiwa kushughulikia matatizo ya wanawake ili waweze kutuamini kwani taifa linatutegemea na tusiruhusu rushwa iwe kwetu.”
Kuhusu malengo ya Bawacha kwa siku za usoni Mdee alisema kwa kipindi cha miezi miwili watafanya operesheni kubwa nchi nzima ya kutoa elimu kwa wanawake waweze kujiunga na chama hicho ili kiweze kuwa na mizizi kuanzia ngazi za chini.
“Operesheni tutakayokwenda kuitangaza kuanza itakuwa kubwa, tutakwenda hadi ngazi za chini kabisa, tutawahamasisha wasichana wadogo ambao wamekuwa wakihofu kujiunga na vyama vya saisa hasa vya upinzani waweze kujiunga,” alisema Mdee.
Juzi viongozi wapya wa Baraza la Vijana la chama hicho (Bavicha) waliochaguliwa ni mwenyekiti, Paschal Patrobas, Makamu mwenyekiti bara, Patrick Ole Sosopi, Makamu mwenyekiti Zanzibar, Zuedi Abdullah.
Katibu Mkuu ni, Julius Mwita, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Omary Othuman Nassor na Naibu Katibu Mkuu Bara ni Getruda Ndebalema na mtunza hazina amekuwa Evelin Meena.