Saturday, 13 September 2014

Uwekezaji ulivyoua Mji wa Mirerani-2

Sheikh Mohammed anasema serikali ndio inawanyanyasa wananchi wake kwa kupitisha sheria ambazo zinawazuia kunufaika na rasilimali za taifa lao ambazo Mungu amewapa.
“Wachimbaji wadogo wamepewa migodi yenye ukubwa wa mita 50 kwa 50 lakini mchimbaji mmoja mkubwa amepewa eneo kubwa zaidi ya eka tano halafu inapitishwa sheria ya kuchimba kwenda chini jambo ambalo haliwezekani huku ni kuwazuia wachimbaji wadogo kupata madini” alisema.
Alisema kwa sasa shughuli nyingi za msikiti huo zimesimama kwani wananchi wa Mirerani hawana fedha za kutoa sadaka tofauti na miaka ya nyuma ambapo sadaka ziliwezesha ujenzi wa msikiti huo, shule na kuwa na miradi.
Padri Aloyce Kitomali wa Kanisa la Katoliki Mirerani, alisema kanisa hilo lilikuwa na uwezo wa kukusanya sadaka katika ibada moja zaidi ya milioni moja lakini sasa hata Sh500, 000 hazipatikani kwani waumini hawana fedha.
Anasema miradi mingi ya kanisa hilo, sasa imezorota kwani wananchi wengi wanategemea madini ya tanzanite ambayo sasa hayapatikani na inasemekana anayepata ni mwekezaji.
“Wananchi hapa wengi wana hali ngumu ya maisha tofauti ya miaka ya nyuma kwani uchumi wao ulitegemea sana madini ya Tanzanite” alisema.
Osca Gunewe ambaye ni Katibu wa Bodi ya shule ya Kanisa la Pentekoste, anasema uchumi wa mji wa Mirerani unategemea madini ya Tanzanite hivyo kwa hali iliyopo sasa ni muhimu Serikali kuwasaidia wakazi wa mji huo.
Gunewe ambaye aliwahi kuwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Mirerani, anasema ingewezekana kuwasaidia watu wa Mirerani hata kwa kutolewa ajira kwa vijana wa Mirerani katika migodi ya mwekezaji.
Anasema lakini kampuni hiyo, haiajiri vijana wa Mirerani na hivyo sasa wapo mitaani tu kwani hata migodi ya wachimbaji wadogo mingi imesimama na ambayo inaendelea na kazi, inachukua vijana wachache sana.
Omar Awadhi alikuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mirerani miaka 10 iliyopita, anasema, maisha ya Mirerani sasa yamebadilika na hata uchangiaji shughuli za maendeleo umepungua sana. Anasema Mirerani licha ya utajiri wote, haina hata huduma ya maji safi, kwani ndoo moja inauzwa kati ya Sh400 na 500.
Awadhi anasema maji hayo yanatolewa Wilaya ya Hai Mkoa wa Kilimanjaro kitu ambacho siyo sahihi kulingana na utajiri wa tanzanite ambayo inapatikana Mirerani pekee duniani.
“Tatizo hapa ni mwekezaji kama madini haya yangechimbwa na wachimbaji wadogo pekee hali isingekuwa hivi, kwani watu wengi wangepata madini japo kidogo kidogo lakini yangeendelea kuujenga Mji wa Mirerani na hata mikoa ya jirani,” anasema.
Robo tatu ya migodi ya wachimbaji wadogo imesimama
Mayala Raurenti ni Ofisa Madini, Mirerani. Anakiri uchimbaji wa madini hayo kuzorota kwa wachimbaji wadogo, lakini anasema chanzo ni mahitaji makubwa ya teknolojia.
Raurenti anasema madini katika maeneo ya kitalii B na D vinavyomilikiwa na wachimbaji wadogo tofauti na miaka ya nyuma sasa yapo mbali na hivyo kuhitaji teknolojia za kisasa.
Hivi sasa wachimbaji wadogo, wamepungua kutokana na upatikanaji madini kuwa mgumu na kuanza kutumia mashine badala ya watu katika kupandisha michanga juu ya mgodi na hata kuchimba.
Mihayo Franeis ni Ofisa wa Miamba (jiolojist) katika machimbo ya Tanzanite Mirerani. Anasema kati ya migodi zaidi ya 400 ya wachimbaji wadogo ni migodi 120 tu ndiyo inachimbwa kila siku.
Anasema hali hiyo, ,imesababisha kupungua sana kwa wachimbaji wadogo kwani pia migodi hiyo, ambayo awali ilikuwa inawafanyakazi zaidi ya 4,000 sasa hawafiki 500.
“Mgodi ambao ulikuwa na wachimbaji wadogo 100 sasa wapo 15 hii inatokana na matumizi ya teknolojia za kisasa katika uchimbaji,” anasema.
Anasema hata mamia ya vijana ambao walikuwa wamejiajiri kuchambua michanga na kupata dhahabu sasa hawapo na ndio sababu watu wamepungua sana Mirerani. Anasema kitalu B kina migodi 183 na kitalu D kina migodi 368 lakini ambayo inachimbwa kila siku si zaidi ya migodi 120 hivyo ndio sababu mji kama wa Mirerani uliokuwa unategemea madini hayo umebadilika.
Hata hivyo, anakiri licha ya migodi kuwa michache inayochimbwa bado upatikanaji madini siyo kama zamani kwa kuwa miamba ipo mbali zaidi kwa migodi mingi.
“Ni kweli migodi mingi ya wachimbaji wadogo haipati madini, tatizo ni kuwa maeneo mengi yamechimbwa tayari na sasa madini yapo chini zaidi hivyo gharama za uchimbaji ni kubwa,” anasema.
Akizungumzia malalamiko ya wachimbaji kuwa madini mengi yapo eneo la mwekezaji alisema siyo sahihi kwani madini yote yapo kwenye miamba katika eneo la Mirerani lakini kwa maeneo ya wachimbaji wadogo yapo chini zaidi.
Serikali sasa yalia kukosa kodi Mirerani.
Martha Umbulla ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro. Anakiri hali ngumu ya maisha Mirerani lakini anasema hata kodi kutoka katika madini hayo, wilaya hiyo hainufaiki kwa sasa.
“Wakazi wa Mirerani wanategemea madini, sasa hayapatikani hivyo uchangiaji maendeleo siyo mzuri lakini Serikali tungeweza kupata hata kodi kutoka kwa wachimbaji hasa mwekezaji lakini hatupati,” anasema.
Anafafanua kuwa kodi ya mapato ya madini hayo, wachimbaji wanalipa Arusha kutokana na mji wa Mirerani kutokuwa na ofisi za Mamlaka ya kodi (TRA).
Alisema Serikali inafanyia kazi matatizo ya Mirerani ili kuona wananchi wataishi vipi na kutokwama shughuli mbali mbali za kiuchumi. Huu ndiyo mji wa Mirerani ambao sasa upo hoi na wananchi wanalia kila kona baada ya kushindwa kunufaika na madini ya Tanzanite.

No comments: