Thursday, 19 June 2014

Tuliteleza mikataba ya madini, sasa tusonge mbele-2

Madini na maisha ya wananchi
Haiingii akilini kuona kampuni za kigeni zinazochimba madini Tanzania zinawekeza nchi za nje, huku wananchi wa Tanzania wakiendelea kuwa maskini.
Nafahamu kuwa mimi siyo mwandishi wa kwanza kuandika suala la madini Tanzania, lakini haimaanishi kwamba tufunge mdomo au tutupe kalamu zetu.
Madini ni miongoni mwa rasilimali zenye thamani kubwa, hivyo kama zitawekewa sheria na usimamizi mzuri, taifa linaweza kunufaika sana kimaendeleo.
Tanzania tunazalisha madini ya aina nyingi kama dhahabu, almasi, rubi, tanzanite, ulanga nk.
Katika uzalishaji huo, kuna baadhi ya migodi inamilikiwa na wachimbaji wadogo wazalendo na mingine inamilikiwa na wachimbaji wakubwa hususani kampuni za kigeni na mingine inamilikiwa kwa ubia baina ya wageni na wazawa au mengine ya wazawa.
Ulinzi wa madini yetu
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ibara ya 27 ibara ndogo ya 1 inaeleza kuwa kila mwanachi ana jukumu la kulinda mali ya nchi ikiwa ni pamoja na madini. Hii ndiyo kusema kwamba kwa kuacha madini kuchimbwa kiholela, wananchi na Serikali yenyewe haijitendei haki. Madini ni mali ya yote inapaswa kuwanufaisha wote.
Madini katika pato la taifa
Hivi karibuni kuna michango mbalimbali inaendelea bungeni kuijadili bajeti, hatujaelezwa kwa kina mapato yanayotokana na madini, miaka yote tumeendelea kuwa tegemezi.
Wasomi wanaongezeka, ajira haziongezeki, deni la taifa nalo linazidi kupanda. Tuna rasilimali nyingi zikiwamo madini, lakini ni kama yametushinda kujinufaisha, sasa tunakimbilia sekta ya gesi. Rais wa Botswana, Festus Mogae tarehe 7, Juni, 2006 alisema: “Kwa watu wetu, kila almasi inayouzwa inawakilisha chakula mezani, mazingira mazuri ya kuishi, afya bora, maji safi, barabara kuunganisha jamii zetu na vingi zaidi.”
Kasoro za sheria za madini Tanzania
Sheria inayosimamia madini Tanzania ni Sheria ya Madini ya mwaka 2010 Na.14 pamoja na kanuni zake mbalimbali zinazohusu mazingira zilitolewa na gazeti la Serikali Na. 403 la tarehe 5/11/2010 inayohusu kanuni za mazingira.
Sheria hizo zinahitaji kupitiwa upya kwa sababu ya kasoro zake kadhaa zinazoonekana.
Moja ya kasoro hizo ni kwamba katika maombi ya kupewa leseni za uchimbaji madini kama watu wana sifa sawa za kupewa, wanaangalia nani wa kwanza kuomba, kama wameomba siku moja wataangalia mazingira husika.
Tunahitaji kufanya mabadiliko na sheria hiyo kutamka kuwa utaifa ndiyo kitu cha msingi cha kuangalia.
Tumeona wiki iliyopita mjini Dodoma, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete alikuwa akizindua kampeni ya Uzalendo, mambo haya ya uzalendo yasambae katika sekta zote mpaka za madini.
Mbili, waziri ana mamlaka makubwa sana kwenye sheria hii ya madini, anasaini mikataba kwa niaba ya Watanzania; kifungu cha 15 cha sheria ya madini ya mwaka 2010 kinamruhusu waziri husika kuamua kugawa maeneo ya uchimbaji kwa zabuni au kawaida.
Madaraka ni makubwa sana ukizingatia na unyeti wa sekta. Kumpa mtu madaraka makubwa kiasi hicho ni kuweka mwanya wa rushwa. Tatu, kamishna wa madini kwa mujibu wa kifungu cha 19 cha sheria no. 14 ya mwaka 2010 ya madini huteuliwa na Rais tu. Hii ni nafasi nyeti inatakiwa kuwa ya wazi na ya kiushindani, Watanzania waombe nafasi hiyo, mwenye uwezo mkubwa ndiyo apewe nafasi.
Kifungu cha 18 (2) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 kinakataza mtu yeyote zaidi ya mmiliki halali wa leseni ya madini, kumiliki, kusafirisha au kuuza madini, jambo kama hili pia linapaswa kuangaliwa, kwa sababu kwa namna moja ama nyingine kinazuia watu wengine kujiingiza kwenye biashara hii.
Kifungu cha 18 (3) kinakataza mtu yeyote kusafirisha nje ya nchi madini au sampuli za madini bila kuwa na leseni ya madini, kibali cha kusafirisha madini nje ya nchi na uthibitisho wa malipo ya mrabaha. Sheria kama hii inapaswa kuangaliwa, kwani angeweza kuruhusiwa tu yeyote ili mradi awe anafuata taratibu nyingine za biashara.
Kwa mujibu wa Kifungu cha 18 (4) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, mtu yeyote atakayekiuka sheria kuhusiana na umiliki na biashara ya madini akipatikana na hatia atatozwa faini ya kiasi kisichozidi Sh10 milioni au kifungo kisichozidi miaka mitatu, au adhabu zote mbili.
Kwa kampuni, adhabu iliyopo kwa mujibu wa sheria kwa kosa hilo ni kulipa faini isiyozidi Sh50 milioni. Wataalamu wa madini wanabainisha kuwa faini iliyowekwa na sheria na adhabu yake ni ndogo sana ukilinganisha na thamani ya madini.
Kifungu cha 6 (4) cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010, kinampa mamlaka kamishna wa madini kutaifisha madini yaliyopatikana kinyume cha sheria, pamoja na vifaa vilivyotumika kuzalisha madini hayo. Sheria ilipaswa kueleza zaidi juu ya uhifadhi na uuzaji wa madini hayo.
Tano, sheria ya madini kifungu cha 25 (1) inaeleza kuwa ripoti inayotolewa na wamiliki wa haki miliki za migodi ni siri, kwa nini ripoti iwe siri? Kwa nini isiwekwe wazi mfano kwenye tovuti ya wizara na kufanya kila mwananchi ajionee kinachoendelea kwenye rasilimali ya nchi yao. Mikataba ni siri, ripoti kutoka kwa wamiliki nayo ni siri. Waswahili wanasema “halali haina siri, haramu ndiyo ina siri.”
Hizi ni baadhi ya kasoro kwenye sheria ya madini. Haya mambo yawekwe wazi kila mmoja ajue kinachoendelea.
Maeneo ya migodi yatangazwe wazi, kila mtu agombanie kwa ushindani ulio sawa. Maeneo ya madini yaianishwe na yatangazwe, watu wagombanie kwa usawa, kipaumbele wapewe wazawa wenye sifa na uwezo, tusiwabeze Watanzania juu ya hili.
Kwa mfano kwa sasa tunataka kujikita kwenye kuchimba urani, lakini imefahamika kuwa madini hayo ya urani yana hatari kubwa kwa binadamu kutokana na kuwa na mionzi yenye madhara. Lazima tujifunze kutoka kwenye uchimbaji wa madini mengine kama dhahabu, almasi, Tanzanite na chokaa, ambao ulisababisha wananchi kupata magonjwa ya ngozi, saratani, uchafuzi wa maji na vifo vya mifugo na wanyama wengine wa porini na majini.
Kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na 403 la tarehe 5/11/2010 kanuni ya 7 na 8 zinakataza uchafuzi wa mazingira, lakini kanuni ya tisa inasema ukifanya kosa la uchafuzi faini haitazidi milioni moja au kifungo kisichozidi miezi sita, najiuliza hiyo adhabu kweli inaonyesha nia ya dhati ya kulinda mazingira kweli?
Jibu jepesi, hapana, tutunze mazingira yetu, madini yana thamani sana lakini hata mazingira yetu yana thamani kubwa sana.
Kwa kifupi, baada ya mikataba hiyo kutomnufaisha mwananchi, Serikali haina budi kuangalia mapungufu hayo katika sheria na kuyafanyia kazi ili madini na rasilimali nyingine ziwe na usimamizi thabiti na wenye manufaa kwa kila Mtanzania.

Kesi tano za mabilioni Uswisi zachunguzwa

Dar es Salaam. Tanzania imeomba msaada kwa taasisi iitwayo International Centre for Asset Recovery – ICAR (Kituo cha Kimataifa cha Urejeshaji Mali) ya Uswisi kuchunguza kesi tano zinazohusu watu na taasisi zinazotuhumiwa kuficha mabilioni ya fedha nchini humo.
Itakumbukwa kuwa baada ya kuibuka kwa sakata la mabilioni hayo ya Uswisi, Serikali iliunda kikosi kazi chini ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Fredrick Werema kulifanyia kazi.
Gazeti hili lilifuatilia suala hilo hadi Uswisi na kubaini kuanza kwa uchunguzi huo, huku fedha nyingi zikitajwa kwamba zinatokana na vitendo vya rushwa.
Akizungumza na mwandishi wetu mjini Bern, Uswisi hivi karibuni, Mtafiti wa Sheria wa ICAR, Andrew Dornbierer alisema: “Tuna makubaliano na Serikali ya Tanzania hasa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), tunachunguza kwa kina kesi za rushwa na utoroshwaji wa fedha, hivyo tuko katika ukusanyaji wa taarifa. Siwezi kukupa mifano ya moja kwa moja kwa sababu bado tunazifanyia kazi na tunadhibitiwa katika utoaji wa taarifa.”
Mkurugenzi wa ICAR, Gretta Fenner Zinkernagel alithibitisha uwepo wa kesi hizo za Tanzania.
“Ni kweli tumeombwa na Serikali ya Tanzania kusaidia kuchunguza baadhi ya kesi… zilikuwa zimeshachunguzwa lakini kutokana na uwezo wao mdogo tunawasaidia. Kwa harakaharaka naweza kusema tunazo kesi tano hivi… ni kesi za watu binafsi na taasisi na zinahusu masuala ya fedha. Hatuwezi kutaja majina kwa sababu tunakatazwa kabisa na mkataba wetu na taasisi tunazofanya nazo kazi.”
Licha ya kutotaja majina, Zinkernagel alisema wanaochunguzwa katika kesi hizo wanahusishwa na kampuni hewa zilizoanzishwa kwa lengo la kuchota fedha kisha kwenda kuzificha nje ya nchi.
“Kuna watu wenye masilahi binafsi na wamekuwa wakipokea rushwa au wamekuwa wakitumia mashirika kwa ubia au kampuni kivuli na ushirika mwingine wa kimataifa ili kusafirisha fedha kwenda kwenye kampuni fulani kwa lengo la kuzificha. Ni kampuni zinazotumiwa na wafanyabiashara kuhamisha fedha haramu na mwisho hujisafisha,” alisema.
Jaji Werema
Jaji Werema alikiri Tanzania kuiomba ICAR kufanya uchunguzi huo lakini akakataa katakata kutaja watu wala kampuni zinazofanyiwa uchunguzi.
“Hatuwezi kutaja majina ya watu waliofunguliwa kesi kwa sababu kwanza tutakuwa tumeingilia haki zao kisheria. Pili, tunaweza kuwataja lakini baadaye ikabainika kuwa si kweli, bali ni tuhuma tu na wakaja kutushtaki na tatu, tutakapowataja watu hao tuliowafungulia kesi tutaharibu upelelezi wetu.
“Katika kesi hizi, kisheria, tunafanya kazi zetu kwa utaratibu ili tusiharibu upelelezi na tupate mambo mengi. Mnadhani tumekaa kimya hatufuatilii lakini tunafanya kazi yetu. Siku ikifika mtaona na mtasikia.”
Balozi wa Uswisi nchini, Olivier Chave alisema watu au taasisi zilizoweka fedha nchini humo hawawezi kutajwa kwani ulinzi wa faragha za watu ni suala la kimataifa... “Sizungumzii tu akaunti za Tanzania, suala la kulinda faragha za watu ni la kimataifa. Ukiwa raia wa Uingereza, Ufaransa au Tanzania, huwezi kupata taarifa za maisha ya mtu binafsi. Kwa sababu wewe kama ni raia mwema, una haki ya kuwa na faragha yako.”
Taarifa za 2011 kutoka Uswisi zilionyesha kuwa kuna kiasi cha Sh327.9 bilioni zilizofichwa kwenye benki za nchi hiyo, lakini Ripoti mpya ya mwaka 2012 ya Benki za Uswisi inaonyesha kuwa fedha hizo zimepungua hadi Sh291.96 bilioni.
Akizungumzia kupungua kwa fedha hizo, Balozi Chave alisema: “Inawezekana ni kutokana na kelele za vyombo vya habari hasa Mwananchi, pengine wenye fedha wameamua kuzihamishia kwenye benki za nchi nyingine.”
Taarifa ya Global Financial Integrity ya 2013 inaonyesha kuwa utoroshaji haramu wa fedha kutoka Tanzania kati ya 2008 na 2011 umefikia jumla ya Dola za Marekani 2.935 bilioni (Sh4.2 trilioni) na inakadiriwa kuwa Watanzania wanamiliki utajiri wa Dola za Marekani 750 milioni (Sh1.23 trilioni) katika Visiwa vya Jersey.
Muda wa uchunguzi
Wakati Tanzania ikiwa imepeleka kesi hizo mbele ya taasisi hizo ndani ya mwaka mmoja, Zinkernagel alisema zinaweza kuchukua miaka mitano hadi 10 ili kufanikisha kurejesha fedha zilizofichwa.
“Tangu uchunguzi unaanza hadi fedha zirudishwe kwa nchi husika inaweza kuchukua hadi miaka 10. Sisi hatuna muda mrefu tangu tuanzishe taasisi hii, lakini tunafahamu baadhi ya kesi zimechukua hadi miaka 20. Hizi ni kesi za kimataifa, hivyo unaanza kufuatilia akaunti na mifumo ya taasisi nyingine… hiyo tu inaweza kuchukua hata miezi sita. Bado mtuhumiwa anaweza kukata rufaa. Ni kweli unataka mambo yaende haraka lakini pia huwezi kukiuka utawala wa sheria.”
Mbali na Tanzania, Zinkernagel alisema taasisi yake pia inashughulikia kesi za nchi nyingine 12 duniani na kwamba wamefanikiwa kukamata baadhi ya fedha na mali zilizoibwa katika baadhi ya nchi.
Alisema kazi hizo hufanywa bila malipo yoyote kwa kuwa taasisi hiyo hupata fedha kutoka serikali za Uswisi na Uingereza.
Changamoto
Akieleza changamoto zilizopo katika kupambana na uhalifu wa fedha haramu, Zinkernagel alisema ni ushirikiano hafifu kati ya nchi zinazoibiwa fedha na zile zinazoficha.
“Mamlaka za Uswisi zikigundua kuwapo kwa mali labda kama za Tanzania, wanaweza kuanzisha uchunguzi wao lakini ili kuhusisha uchunguzi na nchi husika watahitaji msaada kutoka nchi husika. Mamlaka ya Uswisi haiwezi kuendeleza kesi bila ushirikiano na mamlaka za Tanzania, kwa mfano. Hapo ndipo tunapokumbana na siasa nyingi pale tunaposhughulikia kesi kama hizo. Inakuwa vigumu kupata ushirikiano wa wanasiasa tunapouhitaji, hiyo ni changamoto kubwa.
“Changamoto nyingine, ni uwezo mdogo wa vyombo vya usalama vya Tanzania wa kushughulikia kesi za rushwa, matumizi mabaya ya fedha na madaraka. Ni kazi ngumu kufuatilia kesi kama hizo kwani unahitaji kuhusisha sekta mbalimbali. Changamoto hiyo ya utaalamu pia inaigusa Tanzania ndiyo maana haina uwezo wa kuchunguza kesi kama hizo.”
Kwa upande wa nchi zinazoficha fedha, Zinkernagel alisema kuna tatizo la kutoweka vikwazo kwa taasisi za fedha zinazotuhumiwa kuhifadhi fedha haramu.
Tanzania imetajwa kuwa nchi ya 13 kati 20 duniani kwa utoroshwaji wa fedha nje ya nchi.
Taarifa zilizopatikana kutoka katika mitandao mbalimbali ikiwamo Global Financial Integrity, Carl Smith, One Dola Bilioni na Taarifa ya Swiss,” zinaonyesha kuwa Tanzania hupoteza mabilioni ya fedha kila mwaka kutokana na biashara haramu ya uhamishaji wa fedha na misamaha ya kodi na mikataba mibovu.

Monday, 2 June 2014

Polisi wanolewa Uchaguzi Mkuu wa 2015

Dar es Salaam. Harakati za kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015 zimeanza. Polisi wameanza mafunzo yatakayowaongezea uwezo wa kusimamia uchaguzi huo.
Mafunzo hayo yanafadhiliwa na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), kupitia mradi wake wa Uwezeshaji wa Demokrasia (DEP).
Wakufunzi wanane kutoka Chuo cha Polisi cha Uingereza wanaendesha mafunzo kwa maofisa 88 wa polisi wa ngazi za juu na kati.
Akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo hayo, Naibu Kamishna wa Polisi, Simon Sirro alisema yamekuja wakati mwafaka wakati jeshi hilo likijiandaa kwa shughuli hiyo muhimu ya kitaifa.
Mafunzo hayo yanayofanyika Dar es Salaam na Zanzibar yanalenga kuwajengea uwezo makamanda wa polisi wa kupanga, kumudu na kuratibu kwa ufanisi hatua za kipolisi za matukio yanayotishia utulivu wa amani katika jamii.
Alisema katika kila kozi ambayo itaendeshwa kwa wiki mbili, itatoa mafunzo kwa maofisa hao ya kuheshimu haki za binadamu, utawala wa sheria na namna ya kudhibiti ghasia na baadaye kuwafundisha askari wote waliobaki. “Tunataka maofisa wetu wawe na ujuzi wa kutosha kusimamia wakati wa vurugu ili uchaguzi ujao uwe wa haki na amani. Wawe na uwezo mzuri wa kuwaelewesha wananchi juu ya kazi yao ili kuendeleza imani juu ya polisi nyakati kama hizo. Pia yatatusaidia kutambua namna gani tufanye kazi katika mazingira ya vurugu yenye watoto na wanawake.”
Alipoulizwa juu ya matumizi ya nguvu nyingi kwa raia, Sirro alisema wasingependa polisi kutumia nguvu hizo lakini mazingira husika hulazimisha hali hiyo kutokea.
“Ukiona tumetumia moshi… moshi… tumeona mazingira yameturuhusu kufanya hivyo. Askari polisi anapotumia moshi kukutawanya unasema nguvu kubwa… nashindwa kukuelewa. Kwa mfano, wewe una panga na mimi nina kirungu… unakuja kunipiga na panga hivi nikitumia kirungu kukupiga ili nikupeleke polisi kuna ubaya?
Mtaalamu wa masuala ya usimamizi wa uchaguzi wa UNDP nchini, William Hogan alisema taasisi yake inathamini uchaguzi mkuu, pia namna polisi wanavyotumika katika uchaguzi katika nchi za kidemokrasia. “Umakini wa polisi wakati wa usimamizi wa uchaguzi hususan katika kuheshimu haki za binadamu na utawala wa sheria ni moja ya vitu muhimu ambavyo hupima iwapo uchaguzi husika ulikuwa wa haki na wazi hivyo polisi wanahitajika kuongezewa uwezo,” alisema Hogan.
Alisema mafunzo hayo ni mwendelezo tu wa mafunzo kwa polisi kwani yalishafanyika 2010 na yalikuwa na mafanikio.
Alisema wanataka uchaguzi mkuu ujao uwe bora ulimwenguni kwa kuanzia na kuheshimu haki za binadamu na utawala wa sheria.

Rais wa Malawi ana msimamo mkali Ziwa Nyasa

Dar es Salaam. Wingu jeusi limeanza kutanda kuhusu hatima ya mzozo wa Ziwa Nyasa kutokana na msimamo wa hivi karibuni wa kiongozi wa Democratic Progressive Party (DPP), Peter Mutharika ambaye sasa ni Rais mpya wa Malawi.
Hiyo inatokana na msimamo wa Mutharika ambaye ni Profesa wa Sheria wa kupinga kuendelea kujadiliana na Tanzania kuhusu nani mwenye haki ya kumiliki ziwa hilo alioutoa wakati alipowatembelea wananchi wa Chipoko, kando ya ziwa hilo miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu ambao ulimwigiza madarakani.
Pamoja na kwamba mazingira ya msimamo huo yanaweza kutofautiana na hali halisi ya sasa, tofauti za kisiasa baina yake na mtangulizi wake, Joyce Banda zinaweza kuongeza msukumo mpya wa kutaka kutoendelea na mazungumzo ya mpaka wa ziwa hilo.
Akizungumza na wananchi hao, Profesa Mutharika aliwatoa wasiwasi na kuwataka kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwa maelezo kuwa ziwa hilo lipo kwenye himaya ya Malawi na kwamba kuendelea kujadiliana na Tanzania ni kupoteza muda.
“Hakuna haja ya kuendelea kujadiliana, Ziwa Malawi ni mali ya Malawi na litaendelea kuwa la Malawi daima,” alisema Mutharika ambaye pia amewahi kufundisha sheria Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Alimshutumu Banda na kudai alikuwa dhaifu kiasi cha kutoa fursa kwa Tanzania kutumia udhaifu huo kutaka kupora ziwa hilo.
“Ziwa hili letu ila Tanzania inatumia tu udhaifu wa Serikali iliyopo kwani wenyewe wanajua ndani ya mioyo yao kuwa hawana chochote katika ziwa hilo. Tutakaporejea serikalini mwakani haya mambo yote yasiyo na kichwa tutayamaliza. Nataka niwahakikishie kwamba tutapeleka meli zaidi kwenye ziwa hili ili kuinua shughuli zetu za kiuchumi na kutengeneza ajira kwa vijana wetu.”
Hata hivyo, wiki iliyopita Serikali ya Tanzania ilitoa msimamo wake kuhusu mzozo huo wa mpaka na kudaia kuwa itaendelea kujadiliana na Malawi.
Akizungumza bungeni wakati akiwasilisha Bajeti ya wizara yake, Waziri wa Mambo ya nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alisema Tanzania ilikuwa ikifuatilia kwa karibu uchaguzi wa Malawi na kwamba iko tayari kufanya kazi na serikali yoyote itakayoingia madarakani.

Mwanamke ‘apewa’ daraja la upadri

Michigan, Marekani. Mtandao wa wanaharakati wanaopigania wanawake kupewa daraja la upadri, umemtangaza mwanachama wake, Lillian Lewis (75), kuwa padri Mkatoliki.
Uamuzi huo ambao unauweka mtandao huo katika hatari ya kutengwa na Makao Makuu ya Kanisa Katoliki duniani (Vatican), umefanyika mwishoni mwa wiki baada ya mwanamke huyo kutangazwa kasisi wa kwanza nchini Marekani.
Alikuwa miongoni mwa wanawake wa kwanza kuhudhuria masomo ya tauhidi (theolojia) katika Chuo Kikuu cha Marquette miaka ya 1960.
Lewis alisema kashfa za karibuni kwenye kanisa hilo na kutengwa kwa baadhi ya watu ni moja ya mambo ambayo yamemchochea kufikiria kupanda kwenye mimbari na kuhubiri.
“Nimedhamiria kuonyesha njia kwa wengine kwamba wanawake tunayo nafasi kubwa ya kuongoza kanisa kama makasisi. Nina mabinti wanne. Hakuna hata mmoja ambaye anasali kwenye kanisa hilo (Katoliki),” Lewis aliliambia shirika la ABC News. “Wamekerwa na matukio ya siku za nyuma, kashfa ambazo zimeliandama kanisa … wanasema Ukatoliki umebakia kuwa wa kwangu, si wao.”
Sherehe za upadrisho wa Lewis zilizofanyika Jumamosi, zilihudhuriwa na wageni 200 kwenye eneo la nyumba yake. Miongoni mwao walikuwa ni viongozi wa dini isipokuwa wale wa Kanisa Katoliki. Lewis ni mwanachama wa mtandao wa Roman Catholic Womenpriests ambao ulianzishwa mwaka 2002 na umekuwa ukitaka ushirikishi, kumjua Kristo zaidi kwenye karne ya 21 … wenye mtazamo wa kumfuata Yesu kikamilifu kwa kuwahusisha wanawake kama mitume na watu sawa kama ilivyo katika Injili.
Maofisa wa Kanisa Katoliki, Jimbo la Michigan ambao hawakuhudhuria sherehe hizo walieleza kuwa waumini wake walioshiriki sherehe hizo batili nao watashughulikiwa.
Askofu Paul Bradley wa Jimbo Katoliki Kalamazoo, alitoa tamko kali kupitia mtandao wa WWMT-TV in Kalamazoo, Mich., akieleza kuwa yeyote aliyeshiriki shughuli hiyo hatambuliwi na Kanisa Katoliki.
Mbali ya kuonywa na jimbo hilo, Lewis alisema shughuli hiyo ilikuwa yenye mafanikio na alitarajia kuwa ingepingwa na Kanisa Katoliki. Hata hivyo, alisema licha ya kupewa daraja hilo, hafahamu jukumu ambalo atapewa na kanisa.
Alisema majirani zake na mwanawe wa kiume na mchumba wake, walimuunga mkono baada ya kutambua nafasi ya mwanamke kama kasisi na kusema yuko tayari kuwafungisha ndoa wapenzi hao.
Hilo ni pigo jipya kwa Kanisa Katoliki ambalo kwa siku za karibuni lina kilio cha kutaka mapadri waruhusiwe kuoa huku Papa Francis akieleza msimamo wake kuwa angependa kuendelea kuwa na mapadri waseja.

Lissu arusha kombora lingine kwa mawaziri

Dodoma. Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk Binilith Mahenge, jana walituhumiwa kutumia vibaya nafasi zao kwa kuweka fedha nyingi za miradi ya maji katika maeneo wanakotoka, huku sehemu zenye matatizo ya huduma hiyo zikitengewa fedha kiduchu.
Ilielezwa bungeni jana kuwa Profesa Maghembe ambaye ni Mbunge wa Mwanga, Kilimanjaro, wizara yake imetenga Sh1.4 bilioni kwa ajili ya miradi ya maji, ambazo ni zaidi ya mara saba ya Sh190 milioni zilizotengwa kwa ajili hiyo katika Wilaya ya Ikungi, Singida.
Akichangia Bajeti ya Wizara ya Maji jana, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu alihoji kile alichokiita upendeleo wa wazi katika ugawaji wa fedha za maji, unaoipa kipaumbele baadhi ya mikoa wanakotoka mawaziri.
Pia aliitaja Wilaya ya Makete, Njombe anakotokea Dk Mahenge ambaye amewahi kuwa Naibu Waziri wa Maji kuwa imetengewa Sh1.9 bilioni na kusema: “Upendeleo wa aina hii haufai kwa sababu utaleta matatizo na siyo haki hata kidogo.”
“Profesa Maghembe atueleze sababu za kutenga bajeti hii kwa upendeleo, huku mikoa isiyokuwa na vyanzo vya maji, mito ya kudumu na mabwawa ya maana imepewa bajeti kidogo ikilinganishwa na ile yenye mifumo mizuri ya maji,” alisema Lissu.
Alisema licha ya Profesa Maghembe katika hotuba yake kutaja mikoa ya Dodoma, Singida, Simiyu na Shinyanga kuwa inakabiliwa na upungufu wa maji, imetengewa kiasi kidogo cha fedha, huku mikoa inayopata mvua za kutosha na vyanzo vya uhakika vya maji ikitengewa mabilioni ya fedha.
“Dodoma imetengewa Sh7.2 bilioni, Singida Sh3.2 bilioni, Shinyanga Sh3.2 bilioni na Simiyu Sh2.8 bilioni, wakati mikoa yenye vyanzo vya maji na mvua za kutosha imetengewa fedha nyingi; mfano ni Tanga Sh10.7 bilioni, Kilimanjaro Sh6.3 bilioni, Mbeya Sh9.2 bilioni na Mtwara Sh7.5 bilioni,” alisema.
Lissu alisema hali hiyo inaweza kutafsiriwa kuwa mawaziri hao wanatumia mamlaka yao kujipendelea na kuhoji kama huo ndiyo utaratibu wa Serikali ya CCM... “Kama utaratibu wa mgawanyo wa fedha ndiyo huu sisi tunaotoka mikoa yenye ukame tutapataje maji?”
Jana Profesa Maghembe aliendelea kuwa katika wakati mgumu, baada ya kuandamwa na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika ambaye alimwita kuwa ni mzigo kutokana na kutokutolewa kwa fedha za miradi ya maji.
Mnyika alionyesha kushangazwa na wabunge wenzake kuunga mkono bajeti ya wizara hiyo, licha ya kuwa ndogo na fedha za miradi zimekuwa hazitolewi kama inavyotakiwa.
“Kwa kufanya hivi sidhani kama tunamsaidia Profesa Maghembe ambaye ni CCM. Fedha zilizotengwa mwaka jana kuisaidia wizara hii hazijatoka na za bajeti hii hazitatoka kwa kiwango cha kuwezesha utekelezaji. Namna bora ya kumsaidia ili viongozi wa CCM wasiendelee kumwita mzigo ni kuikataa bajeti hii ili Serikali irudi mezani na kujiuliza.”
Mnyika alisema kuwa hata ahadi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuwa Serikali itaongeza Sh80 bilioni kwa wizara hiyo kabla ya Mei 31 mwaka huu nayo haijatekelezwa na kusisitiza kuwa wabunge wakiipitisha bajeti hiyo watakuwa wameuziwa mbuzi kwenye gunia.
Alisema kuwa hata miradi ya maji jijini Dar es Salaam ambayo Profesa Maghembe aliahidi kuwa itakamilika mpaka sasa hakuna kilichofanyika.
Mbunge wa Mbozi Magharibi (Chadema), David Silinde alisema Profesa Maghembe amechota mabilioni ya fedha na kuyapeleka katika miradi ya maji kwenye jimbo lake la uchaguzi wakati maeneo mengine ameyaacha licha ya kuwa yana kipaumbele na kwamba anatumia miradi ya Serikali kujinufaisha kisiasa.
“Ukitaka takwimu zote ninazo hapa, idadi ya watu kwako ni wachache kuliko hata kwangu lakini kwa vipindi viwili mfululizo umekuwa ukijitengea mabilioni ya fedha, wewe ni mzigo kabisa,” alisema Silinde.
Mwandosya amtetea
Wakati akijibu hoja za wabunge, Profesa Maghembe hakugusia tuhuma hizo na badala yake Profesa Mwandosya alimtetea akisema miradi hiyo katika wilaya za Same, Mwanga na Korogwe ilianza wakati yeye (Mwandosya) akiwa Waziri wa Maji... “Si kweli kwamba Profesa Maghembe anapendelea jimbo lake kwa sababu hakuwa waziri wa wizara hiyo wakati mradi huo unaanzishwa. Wananchi wa Same, Mwanga, Korogwe na Simanjiro wana haki ya kupata maji kama wananchi wa sehemu nyingine yoyote. Mwacheni waziri atekeleze majukumu yake ili watu hawa wapate maji”.
Alisema mradi wa maji wa Same, Mwanga na Korogwe ni muhimu sana kwa sababu utakuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya watu 400,000 ambao hawapati maji kabisa.
Alisisitiza kuwa yuko tayari kubeba lawama juu ya mradi huo na si Profesa Maghembe, kwani waziri huyo anafanya kazi nzuri ya kutekeleza mradi huo ambao ulikuwapo hata kabla hajapelekwa katika wizara hiyo.

Tuesday, 20 May 2014

Wabunge wataka JK aunde tume ya elimu

Dodoma/Dar. Baadhi ya wabunge jana walichachamaa wakisema elimu nchini ipo mahututi na kumtaka Rais Jakaya Kikwete kuunda tume ya kudumu ya elimu itakayochunguza mfumo wa elimu nchini.
Wabunge hao walikuwa wakichangia hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa mwaka wa fedha 2014/2015 iliyowasilishwa na waziri wake, Dk Shukuru Kawambwa Jumamosi usiku.
Mbunge wa Longido (CCM), Lekule Laizer alipendekeza safari zote za wabunge na mawaziri nje ya nchi zifutwe na fedha zake zipelekwe kuboresha shule za kata.
Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia alizungumzia uduni wa vitabu na mitihani ya wanafunzi wa shule za msingi akisema inakosewa kutungwa.
“Nina mtihani wa majaribio wa darasa la saba ambao haufanyiki. Niliwahi kumpa profesa mmoja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambaye alitumia saa mbili na nusu bila kupata jibu lolote la kuandika. Mtihani wenyewe haufanyiki,” alisema Mbatia na kutoa ofa ya Sh10 milioni kwa profesa mwingine yeyote bungeni ambaye ataweza kufanya mtihani huo na kupata alama 100.
“Haya ni madudu ya kutisha. Mwaka jana nilivyotoa maoni yangu hapa na waziri akasema maoni yetu yamechukuliwa, alisema rasimu ya mwisho sera ya elimu imepelekwa Baraza la Mawaziri Machi 2013, lakini hadi sasa bado haijakamilika,” alisema na kuongeza kuwa hiyo ni dalili ya Bunge kutoheshimiwa.
Pia alizungumzia ripoti za kamati zilizoundwa kuchunguza elimu lakini hazikufanyiwa kazi na badala yake zikawekwa kwenye makabati.
“Tumwombe Rais aunde Tume ya Kudumu ya Elimu kwa sababu kwa hali inavyokwenda ni mbaya sana na napendekeza tume hii ishughulike na kudhibiti mambo yote yanayofanya kutetereka kwa ubora elimu nchini.
Mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba alisema elimu ya Tanzania iko mahututi na kuwaomba wabunge kuacha siasa katika elimu.
“Bajeti itapita lakini tunaua kizazi kijacho. Mheshimiwa mwenyekiti nenda darasa la kwanza mpaka la saba anayoyasema Mbatia yapo hata kama hatuyapendi lazima tuseme ukweli,” alisema.
Alisema ukienda katika vyuo vikuu ni majanga. “Kama unajiangalia wewe na familia yako, basi tunaliua Taifa. Nimefanya utafiti kwenye nchi 35, Tanzania ni nchi ya mwisho kwa ufaulu,” alisema na kuongeza kuwa nchi zote zilizoendelea kiuchumi, kiwango cha ufaulu ni juu ya asilimia 60.
Mbunge wa Ngara (CCM), Deogratias Ntukamazina alisema hakuna Wizara ya Elimu baada ya elimu ya sekondari na msingi kuondolewa
“Mbele ya Waziri Mkuu niseme kuwa sasa hatuna Wizara ya Elimu… na sasa wanaondoa elimu ya watu wazima, shule zote za mazoezi zimeondolewa.”
Mbunge wa viti maalumu (CUF), Magdalena Sakaya alisema anashangazwa na wizara kushusha madaraja ya ufaulu ambayo awali, kuanzia alama 34 ilikuwa ni daraja O lakini leo ni ufaulu.
“Kiukweli waziri aliyeko katika wizara hii ameshindwa kusaidia elimu nchini. Tangu ameshika wadhifa huo anazidi kubebwa. Kwa nini tunambeba mtu ambaye ameshindwa kusaidia elimu nchini?” alihoji.
Safari za nje
Laizer alitaka safari za mawaziri na wabunge nje ya nchi zifutwe na fedha hizo ziboreshe shule za kata ambako ndiko watoto wa maskini wanakosoma.
Alisema anashindwa kuunga mkono bajeti ya wizara hiyo wakati watoto wake wote katika jimbo lake wanafeli kutokana na shule za kata kutokuwa na walimu wa kutosha.
Akifanya majumuisho, Waziri Kawambwa alikiri deni la Sh61 bilioni la madai ya walimu, lakini akasema serikali imekuwa ikilipa.
Alisema kuanzia Agosti mwaka jana hadi Machi, jumla ya Sh16 bilioni zimelipwa na kwamba si kweli kwamba deni hilo limebakia kuwa Sh61 bilioni.

Sunday, 11 May 2014

Mbowe atangaza mawaziri kivuli

Dodoma. Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, ametangaza Baraza lake la mawaziri kivuli 28 na naibu mawaziri 12, na kufanya baraza lote kuwa na mawaziri 40.
Katika baraza hilo la mawaziri linalojumuisha wabunge wanaotokana na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), mawaziri 25 wanatoka Chadema, 11 wanatoka CUF na NCCR-Mageuzi ni wanne.
Mawaziri kivuli walioachwa katika baraza hilo ni Sylvester Kasulumbay (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi), Highness Kiwia (Viwanda na Biashara) na Rose Kamili (Kilimo, Chakula na Ushirika).
Wengine walioachwa na Mbowe akasisitiza kuachwa kwao siyo kwa sababu hawawezi kazi bali ni kutaka kuwa na baraza la mawaziri dogo ni Sabrina Sunga (Naibu Waziri Maji).
Katika Baraza hilo, nafasi ya mnadhimu mkuu wa upinzani Bungeni iliyokuwa ikishikiliwa na Tundu Lissu (Chadema) sasa itashikiliwa na Mbunge wa Tumbe, Rashid Abdalah kutoka chama cha CUF.
Akitangaza baraza hilo Bungeni mjini Dodoma jana, Mbowe alisema Wizara ya Katiba na Sheria imeongezewa majukumu ya Muungano na waziri wake atakuwa ni Lissu na naibu wake ni Abdalah.
Pia amemteua Mbunge wa kuteuliwa na Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa taifa wa NCCR-Mageuzi,  James Mbatia ambaye anakuwa Waziri wa Fedha wakati Naibu wake atakuwa Christina Lissu kutoka Chadema.
Mawaziri Ofisi ya Rais ni Profesa Kulikoyela Kahigi (Utawala Bora-Chadema), Vicent Nyerere (Utumishi-Chadema) na Esther Matiko (Mahusiano na Uratibu-Chadema).
Ofisi ya makamu wa Rais itakuwa na mawaziri wawili ambao ni mchungaji Israel Natse kutoka Chadema atakayeshughulika na Mazingira na Naibu wake atakuwa ni Assah Othman Hamad (CUF).
Mnadhimu wa Upinzani Bungeni ndiye atakayeshikilia pia nafasi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Mazingira.
Mawaziri katika ofisi ya Waziri mkuu ni Pauline Gekul (Uwekezaji na Uwezeshaji-Chadema), Rajabu Mohamed Mbaruku (Sera, Uratibu na Bunge-CUF) na David Silinde (Tamisemi-Chadema).
Wizara ya Chakula, Kilimo na Ushirika itashikiliwa na Meshack Opulukwa (Chadema), Wizara ya Nishati na Madini atakuwa John Mnyika Chadema na Naibu wake “atakuwa Raya Ibrahim (Chadema).

Kulingana na orodha hiyo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa itashikiliwa na Ezekiah Wenje (Chadema) na Naibu wake ni Rashid Abdalah  kutoka  CUF.
Mawaziri wengine na wizara zao kwenye mabano ni Felix Mkosamali (Ujenzi-NCCR-Mageuzi), Magdalena Sakaya (Maji-Cuf), na Moses Machali (Uchukuzi- NCCR- Mageuzi).
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaongozwa na Godbless Lema wa Chadema na Naibu wake ni Khatibu Said Haji wa CUF wakati Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi ni Halima Mdee wa Chadema.
Kwa mujibu wa orodha hiyo, Mbowe amemteua Rose Kamili Sukum kutoka Chadema kuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi wakati Naibu wake atakuwa ni Mkiwa Adam Kiwanga wa CUF.
Wizara ya Maliasili na Utalii itashikiliwa na mchungaji Peter Msigwa (Chadema), Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeenda kwa Joseph Selasini (Chadema) na naibu ni Rukia Ahmed Kassim (CUF).
Mbowe pia amemteua Masoud Abdalah Salim wa CUF kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa na Wizara ya Elimu itashikiliwa na Susan Lyimo  na Naibu wake ni Joshua Nasari wote toka Chadema.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeenda kwa Dk Gervas Mbassa na Naibu wake ni Conchesta Rwamlaza wote wa Chadema. David Kafulila (NCCR) ameteuliwa Waziri wa Viwanda na Biashara.
Katika baraza hilo la mawaziri, Injinia Habib Mnyaa wa CUF ameteuliwa kuwa Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia wakati Lucy Owenya kutoka Chadema akiteuliwa kuwa naibu wake.
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto imeenda kwa Baruan Salum Khalfan wa CUF na Naibu wake ni Subreena Sungura wa Chadema. Cecilia Paresso wa Chadema anakuwa Waziri wa Kazi na Ajira.
Wizara ya Habari, Vijana na Michezo imeendelea kushikiliwa na Joseph Mbilinyi wa Chadema.
Akizungumza na wanahabari, Mbowe alisema wakati katika Baraza la Mawaziri la Serikali ya CCM, wanaume ni 36 na wanawake 15, wao upinzani wanaume ni 26 na wanawake ni 14.
Hali kadhalika Mbowe alisema wakati Baraza zima la mawaziri la Serikali ya CCM likiwa na mawaziri kamili 28 na manaibu 22, wao Baraza lao Kivuli lina mawaziri kamili 28 na naibu mawaziri 12.
Alisema nafasi ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Ubungeni iliyokuwa ikishikiliwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe itantangazwa baadaye

Lugola: Serikali ya CCM inaendeshwa kisanii

Dodoma. Mbunge machachari wa Mwibara, Alphaxard Kangi Lugola, amedai kuwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo yeye ni mbunge wake, inaendeshwa kisanii.
Lugola ambaye katika Bunge lililopita aliwaongoza wabunge wenzake kuichachafya Serikali hadi mawaziri wanne kujiuzulu nyadhifa zao, jana aligeuka tena mwiba kwa Serikali ya CCM.
Akichangia hotuba ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Lugola alisema anashangaa Waziri mwenye dhamana, Christopher Chizza kuendelea kuwa waziri wakati hotuba yake imejaa blabla.
Pia alimgeukia naibu wa wizara hiyo, Godfrey Zambi na kumwambia kuwa amejisahau kwamba naye alikuwa akikaa kiti cha nyuma bungeni akipaza sauti, lakini baada ya kupata madaraka amewageuka na kushirikiana na waziri.
Akichangia kwa hisia kali, Lugola alihoji inakuwaje wakulima wanapelekewa pembejeo feki, dawa feki na skimu za umwagiliaji zinachakachuliwa na bado Chizza anaendelea kubaki ofisini kama Waziri.
“Waziri huyuhuyu ndiye anayezindua mbegu aina ya Chutoni ambayo haioti, bado ni Waziri. Waziri huyu huyu analipa ruzuku mbegu ya pamba isiyoota bado ni Waziri,” alisema Lugola.
Lugola alihoji kama Mchina aliyekuwa akijenga daraja la Kilombero alijiua kwa sababu tu ya kuhofia kupigwa risasi atakaporudi kwao, hata Waziri Chizza alipaswa awe ameiacha kazi hiyo.
“Simshauri waziri ajiue, lakini kwa vitendo vyote hivi waziri huyu angekuwa ameacha wizara hii na kupumzika na kufanya kazi nyingine mbadala,” alisema Lugola huku akipigiwa makofi.
Lugola alikumbushia Chizza alikuwa ni miongoni mwa mawaziri waliotajwa kuwa ni mizigo na kusema mambo yanayofanywa na wizara hiyo yatakigharimu Chama Cha Mapinduzi.
Mbunge huyo alibainisha kuwa, katika hotuba yake mwaka jana, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema Serikali iko kwenye mchakato wa kuanzisha mfuko wa kinga ya pamba ili kuwasaidia wakulima.
Hata hivyo, alisema katika hotuba ya Waziri Mkuu juzi, hakuna sehemu aliyozungumzia mfuko huo wala Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika katika hotuba yake ya mwaka huu, naye hajazungumzia mfuko huo.
“Hivi nchi hii tunaiendesha kwa usanii mpaka lini? Usanii juu ya usanii… Hatuwezi kuwadanganya wananchi kwa kiwango hiki. Itakuwaje mimi mbunge niunge mkono bajeti ya namna hii?” alihoji.

Alimgeukia Zambi na kumweleza kuwa aliwahi kumtahadharisha kuwa atakapokuja na bajeti yake ahakikishe anampa majibu ya asilimia 20 ya malipo waliyoahidiwa wakulima waliotumia mbegu ya chutoni.
“Uniambie asilimia 20 ya malipo ya wakulima ambayo waliahidiwa kwamba wakitumia chutoni walipwe kama sehemu ya malipo yao, lakini hili halimo kwenye bajeti,” alisema na kuongeza:
“Hakuna lolote humu ni blabla tu… Mheshimiwa Zambi wewe ulikuwa ‘backbencher’ (kiti cha nyuma) kama mimi ulikuwa unapiga muziki kama kasuku juu ya wizara hii, leo unashirikiana na waziri wako unakuja na vitu ambavyo havina majibu, maana yake nini?”
Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa (CCM), alisema wakati Zambi akiwa mbunge, alikuwa msitari wa mbele kupinga matumizi ya mbolea ya minjingu na kumtaka aeleze kama bado ana msimamo huo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda (Chadema), aliwashukia wakuu wa mikoa ya Simiyu na Geita kuwa ni chanzo cha tatizo kwa wakulima wa pamba.
Mbali na hilo, amemtaka Balozi wa Uingereza nchini ajitokeze kueleza misaada inayotolewa na nchi yake inavyotumiwa kwenye sekta ya pamba kwani imekuwa ni sehemu ya ubabaishaji kwa kuendeshwa semina zisizo na maana.
Shibuda alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akichangia maoni kwenye hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa mwaka 2014/15.
Aliwatuhumu wakuu hao kuwa walimpeleka Waziri Mkuu katika kampuni ya Kiotoni wakamdanganya kuwa mbegu hizo ni nzuri, lakini kumbe hazikuwa zimefanyiwa utafiti wa kina na kuwasababishia hasara kubwa wakulima.
Shibuda alisema mbegu za kiotoni zina udhalimu mkubwa na hazina tija yoyote kwa wakulima lakini kila siku wakuu wa mikoa na wilaya wanazipigia debe licha ya kuwa wanatambua kwamba wakulima wanaumizwa.
Magdalena Sakaya aliifananisha Serikali kuwa ni sawa na sikio la kufa kwa kuwa kila wakati imeshindwa kuwa na majibu ya ukombozi kwa wakulima wa Tanzania ambao ndio wapigakura wao.
Mbunge wa Kasulu, Moses Machali (NCCR-Mageuzi) aliwapongeza wabunge wa CCM wanaoonyesha ujasiri wa kuisema Serikali yao kuwa inaendesha mambo kisanii na hivyo kushindwa kuwaletea wananchi maendeleo.
“Serikali imekuwa ikidanganya katika kutatua matatizo ya wananchi ndiyo maana tunaona ni Serikali ya maigizo… Ukisoma hotuba ya bajeti hapa haijibu matatizo ya wananchi,” alisema.
Wakati wabunge hao wakiiponda bajeti hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imeitaka Serikali, kueleza ni lini na vipi wakulima walioathirika na mbegu feki watafidiwa.
Msemaji wa Kambi hiyo wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Rose Kamili, alisema tayari wakulima wameshapata hasara na bado wako wanaoendelea kuathirika na tatizo la mbegu kutoota.

Friday, 9 May 2014

Kafulila awalipua mawaziri akaunti ya Escrow

Dodoma. Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila jana aliibua tuhuma nzito bungeni akiwahusisha mawaziri wawili na Sh200 bilioni zilichotwa katika Akaunti ya Escrow, iliyokuwa inamilikiwa kwa pamoja kati ya Tanesco na Kampuni ya kufua umeme ya IPTL.
Katika tuhuma hizo, alimuunganisha pia Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na vigogo wengine, wakiwamo wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na wa Serikali, wote akiwataja tu kwa vyeo bila majina.
Mawaziri waliotajwa ni Waziri wa Nishati na Madini, Waziri wa Fedha na Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Ingawa Kafulila hakutaja kwa majina, Waziri wa Nishati ni Profesa Sospeter Muhongo, wa Fedha ni Saada Mkuya, Katibu Mkuu wa wizara hiyo (Nishati) ni Eliakim Maswi na AG ni Frederick Werema.
Kafulila alitoa tuhuma hizo bungeni alipokuwa akichangia hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2014/15.
Mbunge huyo alisema fedha zilizoibwa katika Akaunti ya Escrow ni nyingi kuliko zile zilizoibwa katika kashfa ya Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ya BoT mwaka 2005.
“Pamoja na hilo, Watanzania wamekuwa wakisikia kwenye vyombo vya habari kwamba Tanesco wakati ilipokuwa na mgogoro na IPTL walifika mahali wakafungua akaunti ya Escrow,” alisema.
Mbunge huyo alisema akaunti hiyo ilifunguliwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), mwaka 2004 na hadi jana, akaunti ile ilishafikia Dola za Marekani 122 milioni,” alisema Kafulila.
Alisema fedha hizo ziliwekwa kwa lengo maalumu kutokana na mgogoro uliokuwapo kati ya IPTL na Tanesco ili ziweze kusaidia malipo baada ya mgogoro kuisha katika Baraza la Usuluhishi wa Kibiashara la ISCID.
Alitaka jambo hilo liingie kwenye rekodi kwa kuwa linahusu BoT na vigogo akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Katibu wake na pia Waziri wa Fedha.
Alisema wakati Tanesco ikidaiwa madeni zaidi ya Sh400 bilioni, viongozi hao wameidhinisha kugawanywa kwa fedha hizo kihuni jambo alilosema halivumiliki hata kidogo.
Kafulila alisema fedha hizo zilichotwa na Kampuni ya PAP aliyosema ya “Singasinga na ya kitapeli” ambayo iliidhinishiwa kuchota fedha hizo kinyume na utaratibu.
Alisema fedha hizo hazikupaswa kuchukuliwa kwa kuwa kulifanyika udanganyifu mkubwa kwamba PAP ilikuwa imenunua IPTL wakati jambo hilo si la kweli.
Alisema IPTL ilikuwa na makubaliano ya kufanya kazi kwa kampuni mbili ambazo ni VIP Engineering ya Tanzania iliyokuwa na hisa asilimia 30 na Mecmer ambayo ilikuwa na asilimia 70 ya hisa.
Hata hivyo, alidai kuwa anao ushahidi kuwa PAP ilikuwa imenunua hisa za VIP na hakukuwa na vielelezo vya kununua Mecmer kwa kuwa kampuni hiyo tayari ilishapoteza uhalali wake kwa kuwa ilikuwa chini ya muflisi nchini Malaysia.
Aliliambia Bunge kuwa wakati wa uchukuaji wa fedha hizo kutoka BoT, ilipaswa kulipiwa kodi lakini zilichukuliwa kinyemela bila hata ya kulipiwa kodi.
Alisema TRA iliiandikia Hazina na nakala kwa BoT kwamba wakati wa kulipa fedha hizo lazima kodi ikatwe, lakini cha ajabu hilo halikufanyika licha ya kukumbushwa.
“Kwa mfano, tulimwita Gavana katika kikao chetu cha Kamati ya Uchumi pale Bagamoyo na alikiri kuwa alibanwa na viongozi wa juu kiasi cha kushindwa kufurukuta, kwa hali kama hiyo Naibu Spika unategemea nini?” alihoji.
Kafulila alisema, Gavana katika kikao hicho alikiri kuwa, kulikuwa na presha (shinikizo) ambazo asingeweza kuzizuia na kuwa alikuwa amejitahidi kwa kiasi kikubwa hadi kufikia alipofika.
Alisema ISCID lilitoa hukumu ndogo Februari, mwaka huu kuwa Tanesco na IPTL wakae pamoja na kupitia hesabu zao namna watakavyogawanya fedha hizo na walipewa siku 60 ambazo mwisho wake ulikuwa jana.
Aliituhumu Tanesco kuwa katika makubaliano hayo ilikataa kukaa meza moja na kufanya hesabu za namna ya kulipana jambo alilosema linaonyesha ilidhamiria kufanya hivyo.
“Kwa sababu wanajua kuwa fedha ile ilishaliwa na wajanja wachache, Mheshimiwa Waziri Mkuu, hili kwa vyovyote halikubaliki na halivumiliki kwa sababu Dola122 milioni ni zaidi ya Sh200 bilioni ambazo ni nyingi kuliko za EPA, lazima litoke na mtu.”
Alisema hayuko tayari kuona fedha hizo zikitafunwa bila ya utaratibu na akashangazwa kuona Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), akishindwa kuchukua hatua.
Akoleza moto jioni
Katika kikao cha jioni, Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu alimwita tena Kafulila kutoa ufafanuzi wa hoja yake aliyoitoa mchana, ambayo iliombewa mwongozo na Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina kwamba Gavana alishinikizwa kutoa fedha hizo.
Wakati wa mwongozo huo, Kafulila hakuwapo na ndiyo sababu ya Mwenyekiti kumpa nafasi ya kufuta kauli yake kuwa Gavana alishinikizwa. Hata hivyo, Kafulila alikazia akisema alishinikizwa kutoa fedha hizo.
“Gavana aliwahi kuniambia, mnanionea bure. Kulikuwa na presha kubwa sana kuhusu fedha hizi… ukweli ni kwamba IPTL inabadilishwa tu rangi na watendaji ni walewale.”
Baada ya Kafulila kuzungumza, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisimama na kusema: “Tuhuma dhidi ya Gavana wa Benki Kuu zinatolewa kwa kuwa hawezi kuingia bungeni kujitetea.
“Lakini Gavana tulimuuliza na akakanusha kuwa aliwahi kuyatamka hayo maneno na kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni atakuja kufafanua jambo hili kesho (leo) katika hotuba yake,” alisema Lukuvi.
Hata hivyo, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee alisimama kuomba mwongozo akisema: “Kamati ya Bunge iundwe ili tuchunguze fedha hizi za Escrow zimekwenda wapi? Kafulila ana ushahidi wa kutosha, kwa nini hamtaki athibitishe?
“Vikao vyote vya kamati vinawekewa kwenye kumbukumbu rasmi (hansard) ili kujua kama Gavana alitoa maneno hayo ama hakutoa, iundwe kamati ijulikane mbivu na mbichi na wezi wa fedha za Escrow tunao humu ndani ya Bunge.”