Saturday, 20 June 2015

CCM imejali fedha za wagombea siyo demokrasia

Tangu Chama cha Mapinduzi (CCM) kilipofungua milango kwa makada wake wanaojiona wana sifa ya kuwania urais wakachukue fomu, wananchi wameshuhudia msururu mrefu wa makada hao wakitangaza nia kwenye mikutano ya hadhara na pili wakichukua fomu za udhamini.
Waliochukua fomu za udhamini hadi sasa wamefikia 38 na wanapita mikoani kutekeleza sharti la kudhaminiwa na wanachama 450 kutoka katika mikoa 15.
Upande mmoja ni jambo linalofurahisha kuona makada hao wakitumia haki yao ya kikatiba na kidemokrasia kushiriki katika mbio za kuwania urais. Pia kinadharia, ni jambo lenye afya kwamba kamati za uteuzi zitapata wigo mpana wa kuwachuja hadi kumpata anayefaa, kwa kuzingatia sifa zinazohitajika, kwa nafasi hiyo nyeti.
Upande wa pili, utitiri wa wagombea hao, ni ushahidi kwamba chama hakina tena mfumo wa kuandaa viongozi wake ila kinasubiri wazuke tu na kuifanyia sitihizai nafasi hiyo ya juu ya uongozi nchini.
CCM inajua kuwa nafasi ya urais ni nyeti lakini miongoni mwa waliotozwa Sh1 milioni na kupewa fomu ni wanaokosa sifa kabisa kama kada ambaye elimu yake ni ya msingi tu wakati kiwango cha elimu kinachohitajika ni shahada, na mwingine mwenye umri ulio chini ya miaka 40 inayotakiwa kikatiba.
Hata kama, makada hao wanatimiza haki yao kidemokrasia, CCM wanapokeaje fedha za fomu kutoka kwa makada ambao kimsingi hawana sifa ya urais? Hapa CCM imejali zaidi fedha na siyo demokrasia. Ikiwa katika jambo lililowazi kiasi hiki CCM imevurunda, si itavurugwa na utitiri wa wagombea hao wakati wa kumpata kada anayefaa kuwania urais?
Makada wengine waliopewa fomu ili waingie kwenye mchujo ni naibu mawaziri na mawaziri katika Serikali ya Awamu ya Nne; baadhi yao wameteuliwa hivi karibuni na hawajafanya kitu cha maana na wengine wamekuwa mizigo. Mbali ya hao, wapo waliotajwa wazi katika kashfa kubwa za ufisadi.
Hao wote wanapita mikoani kuomba udhamini wakiikosoa Serikali ilivyoshindwa kupambana na rushwa na kukusanya kodi na ilivyoshindwa kuboresha huduma za jamii kama elimu, afya na kuwapa ajira vijana. Baadhi yao wanajipigia debe kuwa hakuna mwingine anayefaa isipokuwa wao.
Vilevile, baadhi ya wagombea wanatumia wapambe kuhonga wanachama ili wafurike kwa wingi kudanganya umma kuwa wanadhaminiwa na wengi kwa madai wanapendwa; baadhi ya wagombea wamefanyiwa fujo hadi mmoja kupigwa na vijana wa tawi la ulinzi la chama hicho maarufu kama Green Guards.
Yanapofumbiwa macho, mambo haya ambayo yanakidhalilisha peupe chama hicho kikongwe tena na makada wake, ni ishara mbaya kuelekea kumpata mgombea atakayekuwa na uwezo wa kuunganisha kambi zinazopingana ndani ya chama, kujitenga na matajiri na kuongoza nchi kwa utulivu.
Tunapenda kuwakumbusha viongozi wa CCM kwamba wakati Mwalimu Julius Nyerere anastaafu alisema; “Bila CCM imara nchi itayumba.” Na kwa kuwasaidia wakati wa uteuzi wa mgombea urais mwaka 1995 alipendekeza wote waliotajwa katika vyombo vya habari kuwa wanahusika na kashfa za kisiasa au za rushwa waondolewe ili wabaki walio safi tu, na pia mgombea wa CCM asiwe mwenye kukumbatia matajiri.
Leo ni tofauti, tunachokiona ndani ya CCM kinatia shaka kwani licha ya utitiri huo mrefu wa wagombea urais tunadhani chama hicho kilipaswa kujua sifa za awali za wagombea wake kabla ya kuchukua fedha.Mathalani jambo la umri na elimu ni sifa ambazo zipo wazi, je kulikuwa na sababu gani ya kuchukua fedha kutoka kwa wagombea ambao tayari wanaonekana kukosa hata sifa za msingi kabisa.

Thursday, 18 June 2015

Prof Lipumba, Zitto DK Slaa, kuvaana kwenye mdahalo

Dar es Salaam. Umoja wa watendaji wakuu wa kampuni wa CEO RoundTable (CEOrt) umeandaa mdahalo wa kuzungumzia mbio za urais utakaowahusisha viongozi wa vyama vya upinzani, Profesa Ibrahim Lipumba, Dk Willibrod Slaa, Zitto Kabwe na Emmanuel Makaidi, lakini Chadema imesema itakuwa tayari kwa midahalo baada ya mchakato wa ndani kukamilika.
Kauli hiyo ya Chadema inaweza kuwa kikwazo kingine kwa CEOrt kuendesha midahalo hiyo baada ya wa kwanza uliokuwa uhusishe makada 10 wa CCM wanaoomba ridhaa ya chama hicho kuwania urais, kushindwa kufanyika kutokana na viongozi wa sekretarieti kutoa kauli tofauti siku moja kabla.
Kiongozi wa CEO, Ali Mufuruki alisema jana kuwa Dk Slaa, Profesa Lipumba, Makaidi na Zitto, ambaye ni kiongozi mkuu wa ACT-Wazalendo, wamethibitisha kushiriki kwenye mdahalo huo utakaofanyika kesho kuanzia saa 1:00 jioni jijini Dar es Salaam.
Lakini Dk Slaa aliiambia Mwananchi jana kuwa Chadema itakuwa tayari kushiriki kwenye midahalo baada ya kumaliza mchakato wa kupata mgombea wake na kukamilisha Ilani ya Uchaguzi, mambo ambayo alisema hupitishwa na vikao vya juu.
“Kamanda, sijui kama ni kongamano au mdahalo: 1. Chadema inaendeshwa kwa katiba, kanuni na taratibu zake. Hadi siku ya leo taratibu zetu hazijafikia kupata aspirants (watangazania),” alisema katibu huyo mkuu wa Chadema katika ujumbe wake mfupi wa simu.
“2. Kama kuna waliopata aspirants, Chadema bado mchakato wetu unaendelea. 3. Midahalo inafanywa kwa msingi wa ilani. Chadema ilani yetu haijafika bado mbele ya vikao vya maamuzi, yaani Baraza Kuu na Mkutano Mkuu. Hivyo tukienda mdahalo tutakuwa tunazungumzia ilani ipi?
“Hivyo tuko tayari kwa midahalo yote baada ya mchakato wetu wa ndani kukamilika.”
Mufuruku alikuwa ametuma taarifa hiyo kwenye ukurasa wake wa facebook na alipopigiwa simu na Mwananchi, alithibitisha kuwapo kwa mdahalo huo ambao alisema utaonyeshwa moja kwa moja na vituo vya televisheni, redio na intaneti.
Kuhusu ushiriki wa Zitto, ambaye atagombea ubunge wa Jimbo la Kigoma Mjini, Mufuruki alisema CEOrt imemualika kwa kuwa ni kiongozi wa chama ambacho kinaweza kusimamisha mgombea wa urais.
“Kushiriki si lazima uwe unachukua fomu za kugombea urais. Yeye ni kiongozi wa chama ana mawazo yanayoweza kutoa mchango kwenye mdahalo,” alisema Mufuruki.
CEOrt imepanga kufanya midahalo kadhaa mwezi huu na Juni 25 itaendesha mdahalo utakaoshirikisha wagombea kutoka CCM baada ya kada mmoja tu, Balozi Amina Salum Ali, kujitokeza kwenye mdahalo wa kwanza na hivyo kusababisha uahirishwe.
Profesa Lipumba, ambaye amechukua fomu za kuomba ridhaa ya CUF kupitishwa kugombea urais kwa mara ya tano iwapo jina lake litapitishwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), aliiambia Mwananchi jana kuwa atashiriki kwenye mdahalo huo, kama ilivyo kwa Makaidi ambaye amepitishwa na NLD kuwania nafasi hiyo.zi wa sekretarieti kutoa kauli tofauti siku moja kabla. NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na NLD vimepanga kusimamisha mgombea mmoja atakayeungwa mkono na vyama vyote, lakini kila chama kitalazimika kupata mgombea wake ambaye jina lake litapelekwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa ajili ya kupitishwa kabla ya kuteua mmoja ambaye atawakilisha vyama hivyo kwenye Uchaguzi Mkuu.
ridhaa ya chama hicho kuwania urais, kushindwa kufanyika kutokana na viongozi wa sekretarieti kutoa kauli tofauti siku moja kabla.
Kiongozi wa CEOrt, Ali Mufuruki alisema jana kuwa Dk Slaa, Profesa Lipumba, Makaidi na Zitto, ambaye ni kiongozi mkuu wa ACT-Wazalendo, wamethibitisha kushiriki kwenye mdahalo huo utakaofanyika kesho kuanzia saa 1:00 jioni jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, Dk Slaa aliliambia gazeti hili jana kuwa, Chadema itakuwa tayari kushiriki kwenye midahalo baada ya kumaliza mchakato wa kupata mgombea wake na kukamilisha ilani ya uchaguzi, mambo ambayo alisema hupitishwa na vikao vya juu.
“Kamanda, sijui kama ni kongamano au mdahalo: 1. Chadema inaendeshwa kwa katiba, kanuni na taratibu zake. Hadi siku ya leo taratibu zetu hazijafikia kupata aspirants (watangazania),” alisema katibu huyo mkuu wa Chadema katika ujumbe wake mfupi wa simu.
“2. Kama kuna waliopata aspirants (watiania), Chadema bado mchakato wetu unaendelea. 3. Midahalo inafanywa kwa msingi wa ilani. Chadema ilani yetu haijafika bado mbele ya vikao vya maamuzi, yaani Baraza Kuu na Mkutano Mkuu. Hivyo tukienda mdahalo tutakuwa tunazungumzia ilani ipi?
“Hivyo tuko tayari kwa midahalo yote baada ya mchakato wetu wa ndani kukamilika.”
Mufuruki alikuwa ametuma taarifa hiyo kwenye ukurasa wake wa facebook na alipopigiwa simu na Mwananchi, alithibitisha kuwapo kwa mdahalo huo ambao alisema utaonyeshwa moja kwa moja na vituo vya televisheni, redio na intaneti.
Kuhusu ushiriki wa Zitto, ambaye atagombea ubunge wa Jimbo la Kigoma Mjini, Mufuruki alisema CEOrt imemualika kwa kuwa ni kiongozi wa chama ambacho kinaweza kusimamisha mgombea wa urais.
“Kushiriki si lazima uwe unachukua fomu za kugombea urais. Yeye ni kiongozi wa chama ana mawazo yanayoweza kutoa mchango kwenye mdahalo,” alisema Mufuruki.
CEOrt imepanga kufanya midahalo kadhaa mwezi huu na Juni 25 itaendesha mdahalo utakaoshirikisha wagombea kutoka CCM baada ya kada mmoja, Balozi Amina Salum Ali, kujitokeza kwenye mdahalo wa kwanza na hivyo kusababisha uahirishwe.
Profesa Lipumba, ambaye amechukua fomu za kuomba ridhaa ya CUF kupitishwa kugombea urais kwa mara ya tano iwapo jina lake litapitishwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), aliiambia Mwananchi jana kuwa atashiriki kwenye mdahalo huo, kama ilivyo kwa Makaidi ambaye amepitishwa na NLD kuwania nafasi hiyo.
NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na NLD vimepanga kusimamisha mgombea mmoja atakayeungwa mkono na vyama vyote, lakini kila chama kitalazimika kupata mgombea wake ambaye jina lake litapelekwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa ajili ya kupitishwa kabla ya kuteua mmoja ambaye atawakilisha vyama hivyo kwenye Uchaguzi Mkuu.
Imeandikwa na Goodluck Eliona na Kelvin

Wema Sepetu sasa rasmi katika siasa

Dar es Salaam. Miss Tanzania 2006, Wema Sepetu (pichani kushoto akiwa na mama yake), ametangaza rasmi nia yake ya kutaka kugombea ubunge wa Viti Maalumu Singida Mjini, kupitia tiketi ya CCM.
Wema alisema kwa muda mrefu marehemu baba yake Balozi Issac Sepetu, alikuwa akimshauri aingie kwenye siasa na sasa ametimiza ndoto za wazazi wake.
Miaka mitano iliyopita, Wema anayekubalika na mashabiki wengi, aliwahi kuweka wazi kuwa yeye ni mkereketwa wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na mshabiki wa klabu ya soka ya Yanga na kwamba hiyo ndiyo sababu ya yeye kupendelea rangi za njano na kijani.
Akizungumza na kipindi cha redio cha Ala za Roho kwa njia ya simu, usiku wa kuamkia jana, Wema alisema yupo mkoani Singida kwa muda sasa akiendelea na kampeni ili kujitayarisha kuchukua fomu ifikapo Julai 15 mwaka huu.
Alisema anaamini nguvu za Mungu, Watanzania na watu wa Singida watamwamini na kumpa kura zao kwa kuwa sasa ni wakati wa vijana kujipambanua na kusaidia jamii yao.
“Nipo Singida kuhamasisha vijana wajitokeze kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Kupiga Kura, pia huku mimi ni nyumbani na nimejiandikisha tayari, ili ifikapo Julai 15 nichukue fomu. Ninachotafuta ni kuungwa mkono na Watanzania,” alisema Wema.
Alibainisha kuwa anajiamini na hakuna kitakachomshinda, kwani alipoingia katika mashindano ya ‘Miss Tanzania hakutegemea kama ataweza, lakini alifanikiwa, hata alipojitosa kwenye uigizaji akafanikiwa.
“Sasa naingia katika siasa, najua kwamba nitaweza. Mimi ni binadamu, nina mambo yangu, ila naamini hakuna linaloshindikana. Nitagombea ubunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Singida, Inshallah tuombe uzima,” alisema.
Wema alisema kwamba tayari ana kikundi chake cha kampeni akiwamo meneja wake Martin Kadinda sanjari na Petitman Wakuache.
“Nimeshafanya mengi kuhusu kujiandaa na uchaguzi hata kampeni, nilikuwa nazungumza na uongozi wangu ambao yupo Martin Kadinda pia yumo Petiman, huyu anahusika na kampeni yangu kwa hiyo Watanzania wajue tu kwamba nitachukua fomu ya kugombea ubunge wa Viti Maalumu na tutaona huko mbele itakavyokuwa kwa sababu hiki ni kinyang’anyiro,” alisema Wema.
Wema alisema kwamba kwa sasa ni kama anaingia kwenye mapambano yaliyo sawa na vita hivyo kuna kupata na kukosa.
“Lakini sifikirii kukosa kwa sababu mtu ukifikiri kukosa unajiweka kwenye ‘negative side’, lakini najua kwa nguvu za Watanzania na kwa nguvu za wananchi wa Singida, wataniamini na kunipa kura zao,”alisema.
Wema alifafanua kwamba licha ya kuungwa mkono na wanaume wengi mkoani humo, kinamama wa Singida pia wanamuunga mkono kwani wanamfahamu vizuri na sera zake wanazijua, hivyo ahofii kelele za watu wa pembeni.
“Nitaingia bungeni kwa ajili ya maslahi ya wananchi na kutetea haki za wananchi wangu, si kingine. Wamejitokeza watu wengi kwa ajili ya kugombea, kwa nini amejitokeza Wema Sepetu na watu wameanza kuzungumza mambo mengi?” alihoji.
Katika mahojiano hayo Diva alimuuliza Wema Sepetu kuhusu taarifa ya kuwa na uhusiano na rafiki wa kiume wa Linah alisema:
“Huwezi kuamini, habari hizo siyo za kweli kwa sababu tulikuwa tunafanyakazi naye tu, ila nimeshangazwa kuona kwa nini Linah ameenda hewani kwenye kipindi na kuzungumza hizo habari, naomba watu waelewe kwamba si kweli.”

Serikali yatangaza nafasi za kazi 1,100

Serikali kupitia Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma imetangaza nafasi za kazi 1,134 katika sekta mbalimbali za ofisi za umma.
Kwa mujibu wa Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Xavier Daudi nafasi hizo za kazi ambazo zinapatikana katika tovuti ya Sekretarieti ya Ajira ya www.ajira.go.tz ni kwa ajili ya waajiri mbalimbali wa ofisi za umma.
Katibu alifafanua kuwa nafasi 949 ni kwa ajili ya waajiri walioainishwa katika ofisi za wizara, halmashauri na nyingine 185 ni za taasisi na wakala mbalimbali za Serikali.
Aidha, amewataka waombaji wote wa fursa za ajira kufungua matangazo yote mawili ya kazi na kuzingatia masharti ya Matangazo yote kama yalivyo katika lugha ya Kiingereza na Kiswahili kabla ya kutuma maombi yao Aprili 9, 2013.
Daudi alifafanua kuwa waajiri ambao watatoa ajira hizo ni makatibu wakuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Fedha, Wizara ya Mambo ya Nje ya Nchi na Ushirikiano wa Kimataifa, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Wizara ya Maendeleo Jinsia na Watoto, Wizara ya Kazi na Ajira na Ofisa Mtendaji Mkuu Wakala wa Vipimo.
Wengine ni Makatibu wakuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Nishati na Madini, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Wizara ya Ardhi Nyumba na Makazi, Wizara ya Maji na Katibu Ofisi ya Rais Maadili.
Wengine ni Makatibu Tawala wa Mikoa ya Kagera, Iringa, Ruvuma, Mbeya, Mwanza, Shinyanga, Manyara, Dar es Salaam, Morogoro, Geita, Pwani, Mara, Kilimanjaro, Lindi, Singida, Tabora, Tanga, Katavi na Arusha; pamoja na wakurugenzi wa halmashauri za majiji na manispaa Mwanza, Iringa, Songea, Shinyanga, Morogoro, Singida, Kigoma/ Ujiji na Temeke.
Nafasi nyingine ni kwa ajili ya wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya Mufindi, Kyela, Rungwe, Mbeya, Chunya, Biharamulo, Bukoba, Muleba, Namtumbo, Songea, Morogoro, Makete, Mkuranga, Mbinga, Tunduru, Ukerewe, Sengerema, Ilemela, Busega, Maswa na Meatu.
Nyingine ni Wilaya za Shinyanga, Kishapu, Kilosa, Msalala, Rufiji, Rorya, Ruangwa, Lushoto, Mkinga, Mpanda, Monduli, Ngorongoro, Kigoma, Nachingwea, Rombo, Same, Singida, Urambo, Tabora, Babati, Mbulu, Simanjiro na Kiteto.
Pia zimo Wilaya za Handeni, Pangani, Kibondo, Chamwino Mtwara, Nanyumbu, Mpwapwa, Kongwa na Tandahimba pamoja na halmashauri za miji ya Njombe na Kibaha. Nafasi nyingine ni za Baraza la Kiswahili la Taifa (Bakita) na Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa).
Nafasi hizo zilizotangazwa zimegawanyika katika kada zifuatazo; Mchambuzi Mifumo ya Kompyuta daraja la II – (nafasi 10), Ofisa Vipimo II – nafasi 6, Mpima Ardhi, daraja la II (nafasi 26), Mhandisi daraja la II – Ufundi Umeme – Nafasi 9, Ofisa Mipango Miji daraja la II– nafasi 13 na Mhandisi daraja la II - Ujenzi (Nafasi 16).
Pia wanahitajika wahandisi daraja la II - Maji (Nafasi 13), Ofisa Misitu daraja la II (nafasi 7), Ofisa wa Sheria daraja la II – nafasi 3, Mtakwimu daraja la II – nafasi 8 na nyingine mbalimbali.

Mbowe ahukumiwa, utata wa sifa ya kugombea waibuka

Hai. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amehukumiwa kulipa faini ya Sh1 milioni au kwenda jela mwaka mmoja baada ya kupatikana na hatia ya kumshambulia mwangalizi wa Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Hai, Denis Mpelembwa. Mbowe, ambaye ni Mbunge wa Hai alilipa faini hiyo iliyochangwa chapchap na wabunge saba wa Chadema na wafuasi wa chama hicho waliokuwa mahakamani hapo.
Wabunge waliochanga fedha hizo ni, Mustafa Akuney wa Mbulu Lucy Owenya, Grace Kiwelu, Cecilia Pareso, Joyce Mukya, Rose Kalili na Paulin Gekul wote wa Viti Maalumu.
Utata wa kupoteza sifa ya kugombea
Hukumu hiyo iliibua mjadala mkali kwenye mitandao ya kijamii juu ya uwezekano wa kumzuia Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni kuwania tena ubunge au urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba.
Hata hivyo, Mwanasheria, Alex Mgongolwa akinukuu Katiba ya Tanzania Ibara ya 67 (1)(c); 67(2) (c na d) alisema hukumu hiyo haiwezi kumzuia kugombea ubunge kwa sababu hakwenda jela na kosa lake halihusu kukosa utovu wa uaminifu, kukwepa kodi wala kuvunja Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Suala hilo linafanana na lililotokea katika mchakato wa uteuzi wa wagombea urais mwaka 2005 wakati aliyekuwa mgombea urais wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila na mgombea mwenza wake, Saidi Soud Said walipowekewa pingamizi kutokana na kutumikia kifungo jela, Mtikila akitumikia mwaka mmoja kwa kosa la uchochezi, Said akitumikia chuo cha mafunzo kwa kosa la biashara ya vitambaa. Hata hivyo, pingamizi hilo lilitupwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame (marehemu) baada ya kusikiliza utetezi wa Mtikila na Said, kuwa makosa waliyofungwa kwayo hayakuwa ya kukwepa kodi, kukosa uaminifu wala kukiuka maadili ya viongozi wa umma.
Mashtaka
Mbowe alikuwa anakabiliwa na mashtaka ya kumfanyia shambulio la kawaida, mwangalizi wa ndani wa Uchaguzi Mkuu Oktoba 31, 2010, Nassir Yamin katika kituo cha kupigia kura kilichokuwa katika Zahanati ya Lambo.
Yamin alikuwa ni mwangalizi wa kutoka Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata).
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mpelembwa ambaye amehamishiwa Bukoba, alisema kitendo kilichofanywa na Mbowe hakikubaliki na kinapaswa kukemewa.
“Kitendo alichokifanya mshtakiwa akiwa Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema na Mbunge wa Jimbo la Hai ambaye alipaswa kuwa kioo cha jamii hakikubaliki na lazima kikemewe,” alisema.
“Kwa hiyo hukumu ya Mahakama ni kwamba atalipa faini ya Sh1,000,000 au akishindwa kulipa atakwenda magereza kwa mwaka mmoja,” alisema hakimu huyo.
Ushahidi
Akichambua ushahidi uliomtia Mbowe hatiani, Hakimu huyo alisema Mahakama imeegemea ushahidi wa shahidi wa kwanza, Yamin na shahidi wa pili John Mushi aliyekuwa msimamizi wa kituo.
Alisema ushahidi huo ulieleza kuwa siku hiyo Mbowe aliingia katika Kituo cha Zahanati ya Lambo katika Jimbo la Hai na kuuliza uhalali wa mlalamikaji kuwapo kituoni hapo.
Mashahidi hao waliiambia Mahakama kuwa walimuona Mbowe akimkunja na kumtoa nje kwa nguvu mwangalizi huyo wa ndani na baadaye mbunge huyo kuondoka katika kituo hicho.
Alisema ushahidi wa mashahidi hao uliungwa mkono na shahidi wa nne wa mashtaka, ambaye ni daktari wa Hospitali ya Wilaya ya Hai, aliyemtibu mlalamikaji na kujaza fomu PF3.
Alisema ushahidi wa daktari huyo unaonyesha kuwa mlalamikaji alikuwa na michubuko katika shavu lake moja na shingoni iliyotokana na kupigwa na kitu butu.
Hata hivyo, aliukataa ushahidi wa shahidi wa saba, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Shafii aliyekuwa mpelelezi mkuu kuwa Mbowe alikiri kufanya kosa hilo alipoandika maelezo ya onyo polisi.
Hakimu Mpelembwa alisema japokuwa upande wa mashtaka uliwasilisha maelezo hayo kama kielelezo lakini baada ya kuyapitia, hakuna mahali ambako Mbowe alikiri kufanya kosa hilo.
Utetezi wa Mbowe
Hakimu Mpelembwa alisema wakati akijitetea mahakamani, Mbowe alikanusha kufanya tukio hilo lakini alikiri kufika katika kituo hicho na kumtaka mwangalizi huyo kumwonyesha kitambulisho chake.
“Katika utetezi wake, mshtakiwa alikanusha kumpiga Nasir Yamin wala kumfanyia kitu chochote kibaya, bali alimwamuru atoke nje kwani hakuwamo kwenye orodha ya waangalizi iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.”
Hakimu huyo alisema, Mbowe alieleza kuwa hakuwahi kuitwa polisi, bali alikwenda mwenyewe baada ya kusikia kwenye vyombo vya habari kuwa amefunguliwa kesi ya aina hiyo.
Sababu za kutiwa hatiani
Hakimu Mpelembwa alifafanua dhana ya kosa la shambulio kuwa ni kitendo chochote chenye nia ya kudhuru mtu mwingine au hata kujaribu tu kumdhuru au kumtia hofu.
“Kwa maana nyingine ni kitendo cha kumtia mtu mwingine hofu na ili kosa hilo litimie ni lazima mshtakiwa awe na nia isiyo halali kisheria ya kutaka kutenda kosa nililolianisha,” alisema.
Hata hivyo, hakimu huyo alisema shahidi wa kwanza (Yamin) na wa Pili (msimamizi) waliiambia Mahakama kuwa mshtakiwa alimkunja na kumvuta nje mlalamikaji atoke nje ya kituo.
“Ushahidi wa Yamin na Mushi ni wa kuona kuwa mshtakiwa alimkunja na kumtoa nje mlalamikaji. Swali hapa ni je, kumvuta mtu na kumtoa nje kunapelekea kosa la shambulio?” alihoji.
Hakimu huyo alisema kwa tafsiri ya dhana nzima ya kosa la shambulio ni dhahiri kitendo alichokifanya mshtakiwa kinaangukia katika kosa hilo kwa mujibu wa sheria.
“Ushahidi wa shahidi wa kwanza na wa pili wa upande wa mashtaka unashabihiana na ushahidi wa daktari kwamba kulikuwa na michubuko. Kwa mantiki hiyo Mahakama inakubali ushahidi huo. Kutokana na Mahakama kukubali ushahidi wa mashahidi hao watatu, inakutia hatiani kwa kosa la shambulio kama ulivyoshtakiwa nalo.”
Mwendesha mashtaka, Inspekta Msaidizi wa Polisi, Feo Simon alisema ingawa hawana kumbukumbu ya makosa ya nyuma ya mshtakiwa, aliiomba itoe adhabu kali ili iwe fundisho kwake na kwa jamii.
Wakili wa Mbowe, Issa Rajabu aliyekuwa akisaidiana na Albert Msando, aliomba Mahakama impe adhabu ndogo mteja wake kwani hajawahi kutenda kosa lolote la jinai.
Hata hivyo, Hakimu Mpelembwa alisema kwa kutoa adhabu ya faini ya Sh1 milioni au kifungo cha mwaka mmoja jela amezingatia ombi la wakili wa Mbowe.
Baada ya hukumu
Hukumu hiyo iliyoanza saa sita mchana hadi saa 7.20 mchana, wafuasi wa Chadema waliokuwa wamefurika mahakamani hapo walitandika kanga chini na kuanza kuchangishana faini hiyo kazi ambayo ilisimamiwa na Kiwelu.
Wakati kazi hiyo ikiendelea, Mbowe aliendelea kushikiliwa ndani ya chumba cha Mahakama hadi wabunge hao walipokwenda Benki ya NMB, Tawi la Hai saa 7.40 mchana na kulipa faini hiyo na Mbowe kuachiwa saa nane mchana.
Mbowe azungumzia hukumu
Akizungumza nje ya chumba cha Mahakama hiyo, Mbowe aliwatoa hofu wanachama wa Chadema kwamba wasikatishwe tamaa na hukumu hiyo ambayo alisema alitegemea ingekuwa hivyo.
“Mnanipa pole ya nini? Kuna msiba hapa? Tupeane hongera. Sikutarajia cha tofauti na hiki kilichofanyika. Hakinivunji nguvu, bali kinaniimarisha katika mapambano,” alisema.
“Haki katika nchi hii itapiganiwa kwa watu wengine kuumia na wengine kuokoka. Nimesota mahakamani miaka mitano badala ya kufanya kazi ya wananchi. Hainivunji moyo,” alisema na kuongeza:
“Hainivunji moyo katika azma yangu ya kuikomboa nchi hii na ukombozi uko jirani. Mahakama ya nchi hii vimekuwa ni vyombo vya kutoa dhuluma kwa wananchi japo siyo mahakimu wote. Lakini iko siku Mahakama zitakuwa ni sehemu ya kutolea haki, kutenda haki na haki ionekane imetendeka. Mapambano yanaendelea na nawaomba msiwe wanyonge,” alisisitiza.
“Sitaki kuizungumzia Mahakama katika hatua ya sasa lakini ndani ya Mahakama kuna watu wanaotenda haki na ndani ya Mahakama kuna watu wasiotenda haki,” alisema Mbowe.
Alisema kesi hiyo haikustahili kuiendesha kwa miaka mitano na kwamba kodi za wananchi zinateketea pamoja na muda, akisema haiwezekani nchi ikaendeshwa katika utaratibu huo.
“Kama mimi mbunge, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, mtunga sheria wa nchi hii naweza kusoteshwa mahakamani miaka mitano, mwananchi wa kawaida atafanywaje?” alihoji Mbowe.

Hizi ndizo ndoto za waowania urais za kuiondoa nchi kwenye umaskini

Oktoba mwaka huu Watanzania wanatarajia kumpokea rais mpya wa awamu ya tano kwa imani kuwa atakata kiu kubwa ya watu wanaopenda kuona wanawekewa mazingira mazuri ya kuondokana na umaskini.
Uzoefu wa awamu nne zilizopita, umeonyesha kuwa pamoja na vyama vinavyowasimamisha wagombea kwenye kiti cha rais kuwa na sera zao, kila aliyengia alikuwa na aina yake ya mabadiliko katika uchumi nchi.
Anayeingia madarakani katika kipindi hiki, anaweza akawa ana majukumu makubwa zaidi kuliko wengine waliopita maana Watanzania wengi wana mambo mengi ambayo wanahisi yangetatuliwa, nchi itaingia kwa haraka kwenye mafanikio na kuondokana na umaskini uliokithiri.
Hadi sasa, Watanzania zaidi ya 30 wamejitokeza kupitia CCM na CUF, wakiwa na mawazo mbalimbali ya kutatua matatizo ya Watanzania kiuchumi, iwapo watapewa ridhaa ya kukalia kiti cha rais.
Yafuatayo ni sehemu ya maelezo ya baadhi yao ambao katika maelezo yao wanawahakikishia Watanzania watazifanya ndoto zao za maendeleo kuwa kweli.
Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa anasema akifanikiwa kuingia Ikulu atahakikisha analiondolea taifa sifa mbaya ya kuombaomba na kulifanya kuwa ‘mkoba wa neema’ katika Afrika. “Tunapaswa kuhakikisha kuwa ukuaji wa uchumi tunaouzungumzia unamnufaisha Mtanzania aliyeko mjini au kijijini na kwamba hali za Watanzania wa matabaka yote zinanyanyuka na kwamba wanaridhika na kuuona uhalisi wa ukuaji wa maendeleo tunayoyazungumzia,” anasema Lowassa.
Anasema anataka kuona ukuaji wa uchumi na ugunduzi wa utajiri unakwenda sambamba na uzalishaji wa ajira ili kuwawezesha Watanzania kukabiliana na changamoto za maisha yao.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe anasema akipewa ridhaa hiyo, atazishirikisha sekta binafsi na umma katika kuendesha uchumi na kuziwezesha kupata mitaji mikubwa.
Anasema ana mpango wa kuvifufua viwanda na kuboresha kilimo, ili mazao yanayozalishwa yanunuliwe hapahapa nchini.
“Hatutaki tena kusafirisha malighafi nje halafu tunaletewa bidhaa zilezile zilizosindikwa. Haya mapinduzi ya viwanda ni lazima, mara tu nikiingia Ikulu Oktoba mwaka huu,” anasema.
Anasema kasi ya kufanikisha maendeleo ya viwanda itachochewa na uwepo wa gesi asilia iliyovumbuliwa mikoa ya Kusini, itakayopunguza gharama za upatikanaji wa nishati ya umeme.
Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba anasema atahakikisha anakukuza uchumi kwa kuwa na serikali ya watu waadilifu. Anasema atahakikisha kuwa Serikali inaongozwa na falsafa ya uwezeshaji mpana kwa wananchi kisiasa, kiuchumi na kijamii. “Sitaunda serikali ya waporaji na wabinafsi. Nitaunda serikali yenye utu, inayowasikiliza watu, itakayotimiza wajibu wake bila chembe ya uonevu wala ulegevu. Nitaunda serikali ya mawaziri 18, ambayo haitakuwa na mtu hata mmoja anayetiliwa shaka uadilifu wake au uwezo wake,” anasema Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli.
Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina anasema anataka nafasi hiyo ya juu nchini ili akasimamia makusanyo ya kodi yatokanayo na rasilimali za taifa yanakuwa mara tatu. Anasema kuwa Tanzania ina uchumi mzuri lakini unaharibiwa na mfumo wa utawala uliopo. “Kwa sasa Taifa linakusanya Sh12 trilioni kwa mwaka, lakini mimi nitahakikisha makusanyo hayo yanaongezeka mara tatu ya hapo. Sasa makusanyo yanashindikana kutokana na kuwapo kwa mianya mingi ambayo inaruhusu wizi wa mali za umma,” anasema. Mpina anasema Tanzania siyo maskini ila umaskini uliopo unasababishwa na ubadhirifu wa fedha za umma, wizi, matumizi mabaya ya madaraka na mikataba mibovu inayofanywa na watu binafsi na serikali.
Mbunge wa Nzega, Hamis Kigwangala anaamini kuwa uchumi unajengwa kwa kuyapa umuhimu mambo makubwa matatu; huduma za jamii, elimu na maji. Anasema ataboresha miundombinu ya reli, barabara, bandari na viwanja vya ndege.
“Kazi ya kujenga uchumi na maendeleo ninaamini tunaiweza, tukiamua. Uwezo tunao, sababu tunazo na nia tunayo; sema tuna upungufu katika kuchukua hatua za kutenda,” anasema.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira anasema Tanzania inahitaji miundombinu mingi kuanzia vinu vya kufulia umeme hadi mifumo ya usambazaji maji safi na mawasiliano ya simu. “Utawala wangu utaweka kipaumbele cha hali ya juu mpanguo huo ili kuhakikisha uwapo wa miundombinu ya uhakika na gharama nafuu kwa ajili ya wazalishaji na walaji kuendana na ukuaji wa juu unaomfaidisha kila mmoja,” anasema.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu anasema ili kufanikiwa kiuchumi nchi, inahitaji rasilimali watu, hivyo ameahidi kutumia nguvu katika kufanikisha jambo hilo. Anasema anataka nchi ipige hatua kutoka hapa ilipo iende mbali zaidi kupitia sekta mbalimbali zikiwemo elimu na afya.
Waziri Nyalandu anaeleza atatumia nguvu kubwa kuwekeza katika rasilimali watu ambayo ni muhimu kama ilivyo kuongeza nguvu za kuwawezesha Watanzania kuwekeza katika jamii.
Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba anasema iwapo atachaguliwa kuingia Ikulu, atawavusha Watanzania kutoka katika hali ya uchumi mdogo uliopo hivi sasa na kuwaingia katika ulio wa kati. “Ninachoomba kutoka kwenu, mniamini na mniunge mkono katika hili, nitawavusha. Lakini tukumbuke kwamba kila mmoja lazima atimize wajibu wake katika utendaji kazi ili tufikie huko tunapotaka kufikia,” anasema Nchemba.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Forecast Entrepreneurship Limited, Boniphace Ndengo anasema Tanzania inaweza kufikia kiwango cha uchumi mzuri utakaoleta ustawi kwa wananchi wengi.
Ndengo anasema alianza biashara ya mghahawa mdogo Mtaa wa Uhuru mjini Musoma, lakini hivi sasa anaitwa mwekezaji hivyo kutokana na wingi wa rasilimali zilizopo nchini, anakusudia kujenga Tanzania kuwa kituo bora cha kimataifa cha utalii na kuifanya kuwa nchi ya uchumi wa kati.
Mjumbe wa Kudumu wa Umoja wa Mataifa (UN), Balozi Amina Salum Ally anasema atatokomeza rushwa kwa kuwa ni adui wa uchumi.
Amina anataja vipaumbele vyake kuwa ni pamoja na kuinua uchumi, kuongeza mapato, kupambana na rushwa, huduma za jamii kuondoa matabaka ya walionacho na wasionacho na kudhibiti mapato ili yaendane na matumizi.
Balozi Ally Karume anasema Tanzania ili iweze kujenga uchumi imara, inahitaji kiongozi mwenye mbinu na uwezo wa kupambana na rushwa na ufisadi kwa vile ndiyo adui wakubwa wa maendeleo yake.
“Uhuru wa kujituma ni muhimu sana kwa kila mtu. Siyo mtu anataka kuuza njugu wewe unamwambia huna leseni. Unamuuliza leseni kwani anataka kuendesha gari? Mtu akitaka kuendesha gari ndiyo mdai leseni, lakini siyo kuuza njugu lazima watu wapewe uhuru wa kujituma,” anasema Balozi Karume.
Mkurugenzi wa Kampuni ya Forecast Enterpreneurship, Boniphace Ndengo anasema adui mkubwa wa taifa ni rushwa na ujinga ambao ‘umezaa’ ufisadi, hivyo atakapoingia madarakani anapiga vita rushwa ili kukuza uchumi.
Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal anasema kwa kuwa yeye ni mwanasayansi atatumia taaluma hiyo kuleta maendeleo nchini. “Hakuna uamuzi uliokuwa sahihi zaidi ya uamuzi wa kisayansi. Mimi siku zote uamuzi wangu unafuata utaratibu huo, ndivyo nilivyolelewa na kufunzwa na nitaendelea kuongozwa kisayansi,” anasema.
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda anasema: “Nitahakikisha uchumi wa wanyonge unainuka. Kwa hiyo katika mpango wa miaka mingine mitano, tutajikita kwa wakulima, wafugaji na wavuvi. Tukifanya hivi umaskini utapungua kwa kiwango kikubwa na ajira zitapatikana.” Monica Mbega anasema akifanikiwa kuwa rais wa Tanzania atafanyia utafiti changamoto za awamu zilizopita na kuhakikisha anazitafutia suluhu ya kudumu.
Monica anasema pia atakabiliana na viashiria vya uvunjifu wa amani ambavyo vinatishia kuvuruga mipango ya maendeleo. Viashiria hivyo anavitaja kuwa ni uhasama, mauaji ya albino, wizi, ubaguzi wa dini na ukabila.
“Tutazungumzia upendo na umoja kuanzia ndani ya familia ndio kitovu kitakachosaidia kujenga amani. Amani itajengwa na upendo misamaha na umoja,” anasema.
Waziri wa Ofisi wa Rais (Kazi Maalumu) Profesa Mark Mwandosya anasema atakuza uchumi, ikiwa ni pamoja na kuanzisha kilimo cha kisasa, kuboresha pembejeo na miundombinu yote ya shughuli za kilimo.
Anasema atahakikisha vyombo vya kiuchumi kama Benki Kuu ya Tanzania (BoT), mifuko ya hifadhi inapewa uhuru zaidi wa kujisimamia na kwamba Serikali itakuwa mhimili wa uchumi ili kuwafanya Watanzania waone matunda ya kukua kwa uchumi. “Serikali itakuwa injini ya kukua Kwa uchumi kwa kuboresha mazingira ili sekta binafsi zifanye kazi kwa ufanisi na kulipa kodi nzuri kwa Serikali,’’ anasema.
Mbunge wa kuteuliwa, Profesa Sospeter Muhongo anasema ataondoa umaskini nchini kwa kutumia uchumi wa gesi. “Nitafuta umaskini kwa kutumia uchumi wa gesi ambao utakuwa unamilikiwa na Watanzania wenyewe. Gesi nimesomea kwa hiyo ninafahamu mambo haya vizuri. “Tena kutokana na juhudi zangu za kuhamasisha vijana wapelekwe nje kusoma masomo ya gesi, nategemea mwakani tutakuwa na wataalamu wengi zaidi watakaoweza kufanya kazi kwenye sekta hii.”
Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja anasema atapambana na mambo sita aliyoyaita maadui wakuu wa nchi, ambayo ni umaskini, ujinga, maradhi, rushwa, ufisadi na mmomonyoko wa maadili. “Maendeleo ya kweli ya nchi yetu hayawezi kuletwa na sekta ya umma peke yake, bali yataletwa kwa kushirikisha kikamilifu sekta binafsi. Ni muhimu rais wa awamu ya tano awe na weledi wa kutosha kuhusu utendaji wa sekta ya umma na binafsi,” anasema.

Sunday, 14 June 2015

Hali halisi ya nchi na rais tunaye mtaka, Taifa lifanye nini


Wengi mtakubaliana nami kwamba kinyang’anyiro cha kumtafuta mgombea urais kupitia Chama cha Mapinduzi kimekwenda kwenye kiwango kingine kabisa, na hasa ukizingatia mpaka sasa kuna makada zaidi ya 30 ambao wameonyesha nia ya kuomba ridhaa ya chama.
Wengi wamekuwa na maswali ya kiuchokozi hapa na pale kwamba unadhani wimbi hili kubwa la wagombea tafsiri yake ni nini? Nimejitahidi mara zote kusema kuna tafsiri zaidi ya moja, mosi ni uhalisia kwamba wana CCM wako huru kuweka mawazo yao hadharani, pili, demokrasia iko pana katika chama kwamba yeyote ambaye anaona anaenea katika nafasi basi anayo fursa ya kujitokeza na kutangaza nia na hatimaye kuomba kukubalika na chama.
Tatu, ni kwamba huenda watu hawajui maana hali ya tafsiri ya urais kama taasisi na Rais kama kiongozi mkuu wa nchi na majukumu yake, huenda watu wanauona urais kwa maana ya kusafiri kila pahala, kufungua miradi, kutoa hotuba, kutoa maelekezo, kupita kwenye msafara wakati wengine tunasubiri foleni, kutuma watu wakafanye kazi kana kwamba watu hawajui wanalopaswa kutenda.
Wengine wanadhani pia ukiwa Rais kazi ya kuwashughulikia wauza dawa za kulevya, kushughulikia wala rushwa na ufisadi ndio hasa itakuwa kazi yao, hawa nawaona wakitembea na pingu, bakora za mibungo na magereza yanayotembea ili kila watakaye mbaini basi watamfunga papo hapo, wapo watangaza nia ambao nikienda kwenye vichwa vya kwa kutafakari nawaona wakiwaza hivi.
Nne, ni kwamba huenda kuna watu wahuni pia, watu wasio na mapenzi mema na taifa hili, watu ambao wamegeuza nafasi ya urais bidhaa ya mnadani. Hawa wako pale kuhakikisha wanakuwa Rais, haijalishi sote tunajua urais mtu hupewa kama dhamana na wananchi, lakini wapo ambao tayari wameshajiona marais, hii ni kuwakosea wapigakura, na zaidi kukikosea heshima Chama cha Mapinduzi.
Hawa watu wa namna hii wao hawajali demokrasia kwa maana ya utawala wa watu kwa watu na watu wenyewe yaani kiingereza “democracy”, watu hawa ni genge la wajanja wachache ambao wanataka kushika madaraka ya nchi, maslahi yao ya msingi ni wao wenyewe kiingereza mtindo huu tunaita “mobocracy”.
Kisiasa- Tanzania iko Njiapanda
Wengi wanahoji dira ya Taifa hili ni ipi? Taifa halina dira, ninaposema hivi wengi mtasema kwamba mbona tunayo ile inaitwa “vision 2025”, ni kweli lakini ile ni dira ya Tanzania Bara pekee, na Tanzania Bara si Taifa, utaniambia pia “vision 2020” nakubali lakini hiyo inahusu Zanzibar pekee, sasa na mimi nitakuuliza je iko vision moja ambayo inazungumzia Taifa la Tanzania?
Kwanza nikitizama vision 2020 na 2025 utagundua bado hazina sifa ya kuwa Dira. Dira ni waraka ambao, Taifa kwa mwafaka limesema huko ndiko tunakotaka kwenda. Ukisoma vizuri hizi nyaraka mbili kila moja iko huru, nikimaanisha Ukisoma vision 2025 inazungumza kana kwamba Tanzania Bara ndio Jamhuri na Muungano na vivyo hivyo ukisoma vision 2020 unaona Zanzibar inajizungumza yenyewe kana kwamba ni huru. Kwangu mimi kitendo cha nchi moja kuwa na dira mbili na zisizosomana ni sawasawa kabisa na kuwa na ndege moja yenye marubani wawili wasio na uelewa wa pamoja wa wanakwenda wapi. Juzi juzi hapa kule nchini Ujerumani kitendo cha kuwa na marubani wawili wasio na uelewa wa pamoja ndege inapaswa kwenda wapi kilipelekea ajali mbaya kabisa, rubani mmoja anajua tunatakiwa kuwafikisha salama abiria wakati rubani mwingine ana mipango ya kutoa uhai wa abiria na yeye mwenyewe kwa kuigongesha kwa makusudi ndege kwenye milima.
Mzee Warioba alijaribu kututengenezea dira katika Rasimu ya Katiba Toleo la Pili, lakini Katiba Inayopendekezwa ikasema hata serikali isipofanya chochote katika utekelezaji wake isihojiwe kokote hata mahakamani na mtu yeyote asiwe na mamlaka ya kuhoji juu ya utekelezwaji wa dira hiyo, sasa hapo ni dira au kiini macho?
Taasisi za Mamlaka ya nchi hasa Bunge ni dhaifu, unakumbuka wakati wa Bunge Maalum wengi ya wabunge walitaka mikataba isipelekwe Bungeni, baada ya Bunge maalum wakazinduka wakataka mikataba ya TPDC, wakanyimwa, roho ikawauma sana hata wakatenda kinyume na mamlaka yao na kuelekeza Polisi iwakamate viongozi wa shirika la mafuta, walitenda kwa hasira, kiko wapi leo? Kitendo kile kikawafanya watake mikataba ipitie bungeni kupata ukubalifu, hawa ni wale wale ambao wengi wao walifuta masharti ya rasimu ya Warioba yaliyosema mikataba ya madini iridhiwe na bunge.
Wakati Bunge likiwa na mtanziko wa kimamlaka, hali iko dhahiri shahiri kwamba kuna upungufu wa utamaduni wa kidemokrasia (democratic culture), tumeacha kuwa watu wa majadiliano (dialogue), hatujengi hoja bali tunapiga makelele na kushutumiana wakati wote, Mwalimu Nyerere alipata kusema “argue, don’t shout”. Hatujengi muafaka, hatufanyi maridhiano, hatuna uelewa wa pamoja katika masuala ya msingi, hatuna uhimilivu (tolerance) lakini inaonekana tuna uhimilivu kwa mambo kama rushwa, ufisadi, mauaji ya albino na vikongwe n.k.
Tumeanza kushuhudia roho mbaya ya utengano (negative devisive force), ukabila, ukanda, udini, ubara na uzanzibari. Umeshuhudia hata watangaza nia tayari wameanza kujipanga kikanda hii ni hatari kwa ustawi wa umoja wa kitaifa.
Inaanza kuonekana uongozi si dhamana tena bali mali ya watu fulani. Utumishi wa umma unafanya kazi kwa woga. Maadili ya Taifa, binafsi na ya viongozi ni tatizo kubwa, hata pale Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi inapowafuatilia wale wanaokiuka miiko ya uongozi utagundua nguvu zake zina ukomo mkubwa.
Kuongezeka kwa vitendo vya rushwa, ufisadi na mmomonyoko wa maadili, angalia namna ambavyo watangaza nia wanatumia fedha nyingi, swali la kujiuliza ni fedha zao binafsi? Na kama si zao waliowapa wana maslahi gani na nafasi ambayo watangaza nia hawa wanaitafuta? Muungano wetu bado una changamoto nyingi, Serikali mbili hazieleweki, siyo tu kwenye Katiba ya 1977 bali hata kwenye Katiba Inayopendekezwa. Watu wa Tanzania Bara wanauona Muungano kama mzigo na watu wa Tanzania Zanzibar wanauona Muungano kama Kero. Kuvurugwa kwa mchakato wa kupata Katiba Mpya ni huzuni nyingine inayoongeza njia panda ya kisiasa
Kiuchumi- Tanzania njiapanda
Umma wa watanzania hauna mali za pamoja, tulibinafsisha kila kitu na mashirika ya umma yaliyosalia ni hohehahe, mfano ni shirika la ndege la Taifa “Air Tanzania”, Shirika la Reli (TRL) ni shida nyingine kubwa licha ya kwamba tuna ubia na watu wengine.
Tuna Shirika la Nyumba (NHC), hili linakimbia kwa kasi baada ya maboresho makubwa ya kiutendaji, lakini nawapa indhari kwamba uchumi wa Marekani ulianguka kwa uwekezaji usiotabirika katika makazi na nyumba, tuwe macho.
Sekta binafsi ni dhaifu, sekta binafsi imeingia katika huduma na si uzalishaji, tizama kampuni ambazo zinaonekana vinara ni makampuni ya simu.
Haya hayazalishi, haya yanatoa huduma na yanachukua fedha za Watanzania maskini zaidi kuliko hata faida ambayo tunanufaika nayo moja kwa moja kama wananchi maskini na wasio na ajira.
Angalia ongezeko kubwa la mabenki, unadhani wanufaikaji ni wakulima na wafanyabiashara ndogondogo ambao kwa kiasi kikubwa wanaangukia katika sifa za watu wasio kopesheka, Tuamke, benki ni nzuri lakini lazima tuwe na uchumi ambao unabeba watu wake.
Hakuna viwanda vya kutosha vya uzalishaji kunakopelekea tatizo la ajira na kupoteza fedha za kigeni (hakuna exports za kutosha), mchele wa mbeya na kwingineko tunao lakini tunaagiza, sukari ya kutoka Mtibwa, Kilombero na Kagera tunayo lakini tunaagiza, tunayo gesi lakini bado tunaagiza mafuta mazito. Halafu dola ya kimarekani ikifika zaidi ya shilingi 2000 tukiuliza tunaambiwa huko duniani dola imeimarika zaidi, kweli?
Sekta binafsi iliyo dhaifu haiwezi kusimamia demokrasia na kuhakikisha kwamba amani inaendelea kuwapo.
Na hapa niwaseme kidogo Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF) kwamba wameona Bunge Maalum lilivyoendeshwa na namna ambavyo Katiba Inayopendekezwa imedhoofisha maadili ya viongozi na kuvuruga Dira ya Taifa kwa kuiwekea vikwazo, lakini kwani umesikia wakikemea au wakishauri kitaalamu madhara ya kubomoa misingi ya maadili na uwajibikaji katika Katiba? Nawapa changamoto, na wao wajitafakari.
Mkazo haujawekwa katika uchumi wa kujitegemea unaozingatia ukuaji wa kilimo kinachotoa malighafi kwa ajili ya viwanda ambavyo vinachakata malighafi kuwa bidhaa zilizochakatwa au bidhaa kamili ambazo ziko tayari kurudi na kutumika katia sekta nyinginezo ikiwemo kilimo
Kukosekana kwa uchumi imara unaojitegemea kunazalisha watu masikini wengi zaidi katika Taifa letu. Tuna walipakodi wachache na tuna walaji wengi katika Taifa lakini pia mianya ya wanaokula zaidi yaw engine kinyume cha sheria ni wengi zaidi na kusababisha chakula wanachokusanya wachache wetu ama kinaliwa na wachache wetu kinyume na sheria na matokeo yake hakitoshelezi mahitaji yetu kama Taifa. Tunalo pia Tatizo la kuwa na vyanzo mbadala mbali na hivi vya sasa vya mapato ya Taifa na Serikali, na bado tunalo tatizo la kampuni za madini kutokutoa kodi ya mapato kutoka faida zao.
Wengi wanasema wanatoa kodi lakini ni kodi wanazokatwa wafanyakazi wao na sio kodi inayokatwa kutokana na shughuli za ushalishaji wa kampuni. Kwenye gesi ni eneo linguine ambalo ukiachia kwamba limegubikwa na sintofahamu juu ya namna mikataba yake imefungwa hasa katika ngazi ya utafutwaji wa gesi ni kizungumkuti kingine kinachotuweka kwenye njiapanda kama Taifa.
Rais tunayemtaka awamu ya tano
Tunataka Rais ambaye anajua tuko njia panda, ana ana uwezo na mamlaka ya kukemea kwasababu na yeye ni mwadilifu “moral authority”. Tunataka kiongozi ambaye anakubalika na jamii na jamii inamwona kama sehemu ya majibu ya changamoto zao. Hatutaki watu wajitembeze kwetu, tunajua tunataka Rais ambaye atasimamia masilahi yetu.
Leo karibu kila mtia nia, nasikia huyu kapata pesa kule, huyu kapata pale, huyu hela za wizi, huyu kapokea fedha chafu, huyu kachukua za watu wabaya na kadharika. Watanzania tuache ushabiki, tusimame na tuwe wamoja katika hili. Rais wetu akiletwa na watu maana yake si wetu ni wao. Tafakari

Zinakaribia siku za CCM kula gizani machungwa yaliyooza

Kuna kisa cha msafiri mmoja aliyeomba mahali pa kulala kwa mjumbe wa Serikali ya Mtaa ili kesho yake aendelee na safari yake. Alifika saa 5.00 usiku na kwa kuwa mjumbe alikuwa amekwisha kula, alichofanya ni kumwandalia msafiri huyo mahali pa kulala, basi.
Alishukuru. Mlo wake usiku ule ulikuwa machungwa sita aliyonunua njiani. Loo, alipokata la kwanza, lilikuwa limeoza, alitupa kwenye kona. Lahaula, alipochukua la pili, nalo lilikuwa limeoza. Balaa, kumbe yote yalikuwa vivyo hivyo.
Haraka aligundua kwamba kilichosababisha akaona machungwa kuwa yameoza ni kibatari, hivyo, alikizima, akachukua machungwa yale na kuanza kula gizani, akalala. Heri angelala na njaa kabisa maana kesho yake aliharisha sana njiani na kutapika; we acha tu!
Kisa hicho kinakaribia kujirudia ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho makada wake waliotangaza nia au kuchukua fomu za kuwania urais wanachafuana na kujiozesha. Akisimama huyu anasema yeye tu anafaa, akisimama yule anadai wengine wote bomu, sasa atapatikana wapi aliye bora?
Edward Lowasa alijizuia alipotangaza nia, lakini Charles Makongoro alimshona barabara Stephen Wasira. “Mzee Wasira alifanya kazi na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. Nyerere aliondoka yeye akabaki, bado yupo. Akaja Ali Hassan Mwinyi akaondoka, yeye yupo….na sasa huyu Mzee Wetu Jakaya Kikwete anaondoka, atamuaga yeye atabaki yupo!” Hebu jiulize, ikitokea ‘Bwana Yupo’ ameteuliwa itakuwaje?
Frederick Sumaye hakutafuna maneno, alisema; “Kama kuna mtu mwingine amekamilika kuliko mimi niambieni, nitampisha (katika mbio za urais).” Alishangiliwa na wafuasi wake huku wakimwambia; “Hakunaaaa.”
Bernard Membe aliwaambia wanaCCM mkoani Lindi; “Nimetafakari sana, nimeona ninatosha kwa nafasi hii nyeti…, nafasi adhimu na si ya mzaha japo naona wapo wanaofanya mzaha. Nimeangalia nikaona hakuna mwingine wa kufanana na mimi.” Halafua akadai, “Hata Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere huko aliko atafurahi endapo nitakuwa rais.” Yaani Nyerere afurahie Membe kuwa rais kuliko hata mtoto wake Makongoro?
Prof Sospeter Muhongo alisema; “Nafahamu... sidhani kama kuna mtu mwingine anafahamu kama mimi. Mkinipa ridhaa yenu wanaCCM, nitahakikisha tunatumia vyema fursa hizo kwa ajili ya manufaa ya uchumi wa Taifa hili….Mtu wa kufanya yote haya ndani ya CCM ni mimi, mnanijua vizuri…”
Samuel Sitta alijipigie debe kwa kusema; “Kwa kifupi ninao uelewa na uzoefu unaolingana na changamoto za kipindi kigumu cha miaka mitano ijayo yenye mwelekeo wa kutikisa misingi ya utawala wa nchi yetu… kwa uimara wangu wa uongozi, nitajumuisha nguvu na maarifa ya wananchi ili tuvuke salama na pia tutekeleze kazi za maendeleo kwa ufanisi na tija zaidi.”
Mwigulu Nchemba alisema; “Ahadi yangu kubwa kwenu ni kwamba nitawavusha. Nitawavusha wanaCCM wenzangu pamoja na Watanzania kwa ujumla… wakati ni sasa tunataka Taifa letu lifike kuwa nchi yenye uchumi wa kati.”
Kauli hizi zimetolewa kirejareja sana, lakini zitakuja kuwa na madhara makubwa mbele ya safari ndani na nje ya CCM kuwaaminisha wapigakura kwamba “chungwa teule” halijaoza kiviiile. Hapo watajitahidi kupiga msasa na kupinga methali isemayo “samaki mmoja akioza wote wameoza”.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati Kuu, Halmashauri Kuu ya Taifa na mkutano mkuu wa CCM walioshiriki mwezi huu, kuwaunga mkono makada wanaowapenda wawe marais, ndiyo mwezi ujao, watashiriki kumpitisha mmoja akapambane na wa Ukawa kutafuta tiketi ya kuishi Ikulu ya Magogoni, Dar es Salaam.
Nani akemee? Wazee wa kukemea walijazana Arusha, Butiama, Mwanza, Lindi, Mbeya na kwingineko kuwapiga ‘tafu’ watangazania.
Kingunge Ngombale-Mwiru, mmoja wa makada wenye hekima wanaotegemewa kutoa ushauri ndani ya CCM yuko katika Timu Lowasa. Siku Lowasa alipotangaza nia mjini Arusha, Kingunge alikuwapo na alitoboa siri ya Halmashauri Kuu akisema, Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Kikwete aliwataka wale wenye ugomvi kutafuta suluhu. Vyema. Je, yeye kuwa kwenye Timu Lowasa ni kusaidia suluhu ipatikane?
Lowasa mwenyewe yuko tayari kwa suluhu? Akijibu maswali ya wahariri kuhusu kutofautiana na wenzake alisema; “…Kama kuna mtu ambaye hanipendi ndani ya CCM, yeye ndiye ahame, siyo mimi.” Siku alipochukua fomu alisema, “Naamini katika ushindi na sina mpango wa kushindwa.” Waandishi wa habari walipomuuliza kama yupo tayari kushirikiana na wanasiasa wanaompinga sasa, aliwajibu; “Nitavuka daraja nitakapofika.” Mmh!
Ndiyo maana nasema zinakaribia siku za CCM kula gizani chungwa lililooza na kununua msasa ili kulitakatisha kabla ya kuliuza kwa wananchi.
0658 383 979

Wagombea waisuta Serikali kwa rushwa

Dar es Salaam. Makada wa CCM waliotangaza nia au kuchukua fomu za kuomba kupitishwa na chama hicho kuwania urais, wameeleza jinsi rushwa, ufisadi na udhaifu katika ukusanyaji kodi huku wakijinadi kuwa wao ndiyo wataondoa uovu huo iwapo watapitishwa kushika nafasi hiyo ya juu kisiasa.
Lakini hakuna hata mmoja aliyeiponda Serikali kwa kushindwa kudhibiti rushwa, ambayo baadhi walishasema kuwa imekithiri hata kwenye chama hicho tawala, huku mmoja akisema kuwa iwapo CCM itampitisha mlarushwa, atajiondoa.
Kati ya waliotangaza nia na kuchukua fomu, makada 11 ni mawaziri wa Serikali ya Awamu ya Nne wakiwamo mawaziri waandamizi walioshika nafasi za juu na waliofanya kazi katika awamu zote nne.
Pia wamo makada waliokuwamo kwenye Baraza la Mawaziri la Serikali ya Awamu ya Nne, lakini wakaondoka kwa sababu tofauti, huku kundi jingine likihusisha watendaji wakuu wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa.
Lakini bado tatizo hilo la rushwa limekuwa likitumiwa na makada hao wa CCM wanaowania urais wakati wakijinadi kwa wanachama wao kwamba watafumua mfumo uliopo, kusuka upya sheria na kuimarisha taasisi za fedha ili watuhumiwa wakubwa wa rushwa wafikishwe kortini na kufungwa, badala ya kuwakamata walarushwa wadogowadogo pekee.
Katika hotuba zao wakati wanatangaza nia mbele ya umati wa wafuasi wao na mbele ya waandishi wa habari baada ya kuchukua fomu, makada hao, mbali ya kueleza mikakati tofauti ya namna ya kuimarisha uchumi wamekosoa mfumo wa sheria kwamba unawalinda mafisadi wakubwa ambao hawakamatwi hadi kwa kibali maalumu.
Kwa mfano, akitangaza nia ya kuwania urais kijijini kwao Butiama, Charles Makongoro ambaye ni mtoto wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alisema anaomba kibali cha kuisaidia CCM ikomeshe rushwa, na atakapoingia madarakani, ili asiwaangushe Watanzania, anahitaji chama imara kisicho na shaka kama ilivyo sasa.
“Kosa la Rais Jakaya Kikwete ni kuwapenda sana marafiki zake. Kwa bahati mbaya, baadhi ya marafiki zake hao ni vibaka,” alisema Makongoro ambaye ni mbunge wa Afrika Mashariki.
Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe aliwaambia wafuasi wake mkoani Lindi kwamba ili kutekeleza utawala bora, hawezi kukaa kimya kuona rushwa, ubadhirifu, ufisadi vikichukua nafasi katika utawala wake.
“Ninawatumia salamu mapema, sitakuwa na kigugumizi kwa wanaotesa Watanzania. Nitahakikisha Watanzania wanachukia rushwa na kutakuwa na sheria kali dhidi ya mtoa na mpokeaji rushwa. Kama ni watumishi wa umma, watakwenda na maji...,” alisema mbunge huyo wa Mtama.
Ahadi ya kukomesha rushwa pia ilitolewa na Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta aliyesema kwamba anataka kulifanyia Taifa mambo matano, ikiwa ni pamoja na kutenganisha biashara na siasa na kusimamia maadili ya viongozi wa umma.
“Ili kukomesha tatizo la rushwa, hatuna budi kutunga sheria itakayotenganisha biashara na uongozi,” alisema Sitta kwenye Ikulu ya Wanyanyembe iliyopo Itetemia, Tabora.
Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba alisema akifika Ikulu, ili kupambana na rushwa, “nitafanya mabadiliko ya kisheria, kimfumo, kitaasisi na kijamii ikiwamo kuipa meno Takukuru kuwa na mamlaka kisheria ya kuwashtaki watuhumiwa wa rushwa moja kwa moja mahakamani”.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira alionyesha kukiri kuwa miongoni mwa makada waliojitokeza kuwania urais, wamo wenye kashfa za rushwa, lakini akajitenga nao kujionyesha kuwa hana doa hilo.
“Ili kukabiliana na changamoto hizi kubwa, itakuwa lazima kwa chama chetu kumteua mgombea ambaye hana historia ya kuhusishwa na ufisadi, iwe kwa kutuhumiwa tu au kuhusika kweli. Mgombea anayejua historia ya nchi yetu, pale ilipo na kule inakopaswa kuelekea,” alisema waziri huyo mkongwe na kuongeza:
“Kumbukeni sijatajwa katika kashfa kama za Escrow, EPA, Richmond na nyinginezo.”
Wasomi wawashangaa
Lakini kauli na ahadi hizo za makada hao wa CCM wanaotaka kuingia Ikulu zimewashangaza wachambuzi waliofuatwa na Mwananchi ili kutoa maoni yao kuhusu hoja za wagombea.
Mchambuzi wa masuala ya siasa kutoka Chuo Kikuu cha Ruaha (Rucu), Profesa Gaudence Mpangala alisema wengi waliotangaza nia ya kuwania urais wanatoka kwenye mfumo wa rushwa, hivyo itakuwa kazi ngumu kwao kuiondoa. “Tanzania imefikia ngazi ambayo rushwa imekuwa mfumo wa utawala. Ikifikia hatua hiyo kuindoa ni kazi kubwa kwa sababu kupiga vita mfumo si suala dogo, hawa watiania walishindwa huko serikalini, watawezaje sasa?” alihoji.
Alisema wengi kati ya wagombea hao wanatoka katika mfumo wa rushwa ambao wameujenga wenyewe, hivyo si kazi rahisi kuimaliza kwa sababu kuna kulindana na kustahimiliana.
“Kulindana ni utamaduni wa mfumo huo wa rushwa. Ndiyo wameujenga na walikuwa ndani ya mfumo, ndiyo maana wanashindwa kueleza watatumia mbinu gani
kuondoa mfumo huo,” alisema.
Alisema anahitajika mtu shupavu kuiondoa rushwa hapa nchini kwa sababu imeshaota mizizi kwenye mfumo wa utawala, na kwamba kusema tu wataimaliza hakuna ukweli wowote.
“Ufisadi unaofanywa na viongozi wa Serikali, vigogo na wanasiasa zina athari kubwa kwa uchumi wa nchi hii,” alisema Profesa Mpangala.
Mawazo hayo yanalingana na ya mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Hamad Salim ambaye alisema ni vigumu kwa wanaotaka kuwania urais kuimaliza rushwa kwa sababu wote wanafanya kazi katika mfumo uliojaa rushwa.
“Wao wenyewe wanaingia madarakani kupitia mfumo wa rushwa, sidhani kama wataweza kuung’ata mkono ambao unawalisha. Kama mchakato mzima wa kuingia madarakani kama vile kuchukua fomu, kupiga kura, kutafuta wadhamini wote umejaa rushwa, wataweza kuiondoa?” alihoji.
Alisema ahadi wanazozitoa watia nia ni vigumu kutekelezeka kwa sababu wanapambana na mfumo wao wenyewe na kazi ya kuumaliza ufisadi si ya mtu mmoja wala ya siku moja.
Salim alisema inashangaza baadhi ya watangazania kukusanya watu wanaowaunga mkono, kuandaa kampeni na kuandaa watu wa kuwashangilia.
Alisema watangazania hao wanatoa ahadi zao kama kampeni tu na wakiingia madarakani hawatafanya kazi kulingana na walichoahidi bali kwa kuangalia ilani ya CCM.
Mchambuzi wa masuala ya siasa wa UDSM, Dk Benson Bana aliwataka watangazania hao kuacha kutumia kigezo cha rushwa kama njia ya kupata kura na badala yake wazungumzie sera nyingine.
Dk Bana alisema Watanzania hawatamchagua kiongozi kwa sera zake za kutaka kuondoa rushwa kwani nao wanafahamu kuwa CCM imejaa rushwa.
“Watanzania hawamchagui mtu kwa kigezo cha kupambana na rushwa, hicho ni kimbelembele tu, waache kimbelembele,” alisema.
Dk Bana pia alisema watangazania hao waiache Takukuru ifanye kazi yake na wasiwadanganye wananchi kuwa wao ni mabingwa wa kupambana na tatizo hilo.
Lakini mkufunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha(IFM) kitivo cha kompyuta na mifumo ya hesabu, Dk Eliamani Sedoyeka aliliangalia tatizo la rushwa kuwa ni silka na hivyo ni vigumu kuthibitisha iwapo mgombea ana au hana tatizo hilo.
Dk Sedoyeka alisema kiongozi anayesema atapambana na rushwa anatakiwa kupimwa kwa rekodi yake ya uongozi kwa kuangaliwa iwapo aliweza kukemea, kuadhibu, au kukataa rushwa katika mazingira yoyote yale.
“Kwa mfano wapo watu wanajiweka karibu na matajiri, wanapewa fedha na matajiri za kufanya kampeni, je watakuja kulipa vipi hisani za matajiri watakapoingia madarakani? Hayo ndiyo mazingira,” alisema

Wednesday, 3 June 2015

Ukawa wawaponda waliotangaza nia CCM

Sumbawanga/Dar. Viongozi wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) wameponda tabia ya makada wa CCM wanaotangaza nia ya kugombea urais kufanya hafla zinazotumia fedha nyingi kwenye jambo dogo.
Viongozi hao wamesema vitendo hivyo vinaonyesha kuwa chama hicho tawala hakichukii ufisadi na hivyo hakiwezi kuwa na mgombea safi.
Makada hao wamelipia muda wa matangazo ya moja kwa moja kwenye vituo vya redio na televisheni, kufanya maandalilizi ya gharama kubwa kwenye sehemu walizotangazia nia, kuandaa vipeperushi na mabango ya thamani huku baadhi wakituhumiwa kusafirisha watu kutoka sehemu mbalimbali kuhudhuria hafla hizo.
Akihutubia wakazi wa Sumbawanga mkoani Rukwa, katibu mkuu wa Chadema, Dk Wilbroad Slaa alisema Serikali ya CCM ni kama ya watu wa ukoo mmoja wenye tabia zinazofanana.
Alisema Serikali imejaa tuhuma nyingi za rushwa na ufisadi na kwamba, kinachotakiwa ni kuinyima kura zote wakati wa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu.
Katibu huyo alisema wale wote wanaojitokeza kutangaza nia ni ‘mafisadi’ ndio maana wanatumia nguvu ya fedha kuwanunua Watanzania, jambo ambalo alisema ni kinyume cha maadili.
“Ni hatari sana kuwachagua viongozi kwa fedha, hawa wanataka kuliangamiza Taifa,” alisema.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema anashangaa chama kilichoasisiwa na mjamaa Mwalimu Julius Nyerere, vijana wake wanafanya sherehe kubwa kwenye jambo dogo.
“Hata mwanasiasa mkongwe Kingunge (ngombare Mwiru) anakwenda kuwa mpambe kwenye shughuli inayokiuka taratibu,” alisema na kuongeza kuwa hiyo ni ishara mbaya.
Mwenyekiti wa NLD, Emmanuel Makaidi alihoji wanaotumia fedha nyingi kwenye jambo dogo, watazirudishaje.
Alisema kama makada hao walifanya kazi halali, hawawezi kuwa na fedha zinazoweza kugharimia sherehe kubwa kama hizo.
Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema mfumo mbaya wa CCM ndio unaonyesha chama hicho hakichukii mafisadi.“Kama chama kingekuwa kinachukia ufisadi, kingeandaa utaratibu wake ili watu wote wanaotangaza nia wawe na nguvu sawa,” alisema Mbatia.