Wednesday, 9 April 2014

Kamati kumi zaitesa CCM

Dodoma. Kura za awali katika Kamati 10 kati ya 12 za Bunge Maalumu la Katiba, zinakipa wakati mgumu Chama Cha Mapinduzi,(CCM) kutekeleza azma yake inayotajwa kuwa ni kufumua Rasimu ya Katiba, ili kuondoa mapendekezo ya Muundo wa serikali tatu, baada ya wajumbe wa Zanzibar kukwamisha upatikanaji theluthi mbili.
Kwa mujibu wa taarifa za kamati, ambazo tangu juzi zimeanza kutolewa katika sura ya kwanza na sita zinazungumzia Muundo wa Muungano, wajumbe kutoka Zanzibar kwa sasa ndiyo kikwazo kikubwa kwa CCM.
Hata hivyo, uamuzi ya mwisho kuhusu Muundo wa Serikali, kati ya mbili au tatu, unatarajiwa kujulikana Alhamisi wiki ijayo, wakati kamati zote zitakapowasilisha taarifa zao na kupigwa tena kura kwa wajumbe Tanzania Bara peke yao na Zanzibar peke yao.
Iwapo wajumbe wa Zanzibar wakiitetea kwa theluthi mbili kama sasa, mapendekezo ya muundo wa serikali tatu ndiyo yatakayopelekwa kwa wananchi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, baadhi ya wenyeviti wa kamati hizo, Stephen Wassira, Ummy Mwalimu, Anna Abdalah na Paul Kimili, walitaja moja ya vifungu ambavyo vimeshindwa kupata theluthi mbili kuwa ni ibara ya kwanza kifungu cha kwanza.
Akizungumza jana Wassira ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Namba Sita alisema kwamba katika kamati yake ibara hiyo imeshindwa kupata theluthi mbili, ili kuweza kufanyiwa marekebisho.
“Lakini huu siyo mwisho kama nilivyosema awali, tukirudi bungeni tutapiga kura kwa wajumbe wote na ndiyo itakuwa na uamuzi wa mwisho kama muundo wa Muungano utakuwa na Serikali tatu ama mbili, ambao utapelekwa kwa wananchi,” alisema Wassira.
Jussa, Lissu- tumeibana CCM
Jussa alisema: “Kwa taarifa za matokeo tulizonazo katika Kamati Namba 1, 2, 3, 4, 6, 10, 11 na 12 mapendekezo ya kubadilisha Rasimu katika ibara hizo mbili yamekwama. Kama CCM wakichakachua sura ya kwanza na sita, maana yake ni kwamba hapa hakuna Katiba, hakuna kura ya maoni na hakuna mwafaka.”
Vifungu hivi pia kwa mujibu wa wenyeviti wa kamati nyingine, isipokuwa kamati ya Tano, ambayo inaongozwa na Hamad Rashid, havikupata kura theluthi mbili na hivyo kubaki kama vilivyo kwenye rasimu.
Naye Lissu alisema kwa sasa CCM ndiyo inaweza kuanza mkakati wa kuvuruga Bunge kwani tayari wamejua hawana theluthi mbili ya Zanzibar ili kubadili Rasimu kama wanavyotaka.

Msekwa: Sitta ana lake jambo

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta kukiri kuchezewa kwa saini ya aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Msekwa amesema, ‘mzungumzaji huyo ana lake jambo’.
Sitta akizungumza na gazeti hili juzi mjini Dodoma alisema ni kweli kuna maneno katika hati hiyo ya sheria namba 22 ya 1964, iliyosainiwa na Nyerere na Msekwa, Aprili 25, 1964, yameongezwa.
Alifafanua kuwa saini ya Nyerere imeongezwa herufi ‘us’ kwa kompyuta na katika sehemu ya saini ya Msekwa kumeandikwa neno ‘Msekwa’ kwa kompyuta, jambo ambalo ni makosa. Sitta alisema walioongeza maneno hayo ni wafanyakazi wa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya kuona sehemu ya maandishi kwenye saini hizo hayasomeki, lakini walifanya makosa.
Msekwa akizungumza na gazeti hili jana alisema: “Saini iliyo katika hati original (halisi) ni ya kwangu mimi, lakini huyo anayesema zimechezewa muulizeni atakuwa na lake jambo. Kama kompyuta imekosea ni leo kwa kuwa kipindi hicho kompyuta hazikuwapo.”
Aliongeza: “Ana lengo gani la kutilia shaka, ana lengo gani la kusema imechakachuliwa, kinachotakiwa ni hati original ambayo iko ofisi ya Katibu wa Bunge itolewe, kwanini tuendelee kuandikia mate wakati wino upo?”
Maoni mengine
Mjumbe wa Bodi ya Kituo cha Taarifa kwa Wananchi Umma (TCIB), Hebron Mwakagenda alisema yote hayo yanatokea ni kuvuruga hoja iliyopo mezani.
Alisema kitendo cha kupoteza muda kuzungumzia suala la kuchezewa kwa saini halitakiwi kwani kama maudhui yake hayakuchezewa basi hoja ya muundo wa Muungano uamuliwe na wananchi wenyewe.
“Tusianze kupoteza muda kwa mambo ambayo hayapo cha msingi wananchi wenyewe waulizwe wanaupenda Muungano au la lakini tusianze kumtafuta mchawi kuwa saini zimechezewa wananchi waamue wenyewe kuhusu Muungano,” alisema Mwakagenda.
Sakata lilivyoanza
Utata huo ulianza wiki hii baada ya kamati za Bunge Maalumu la Katiba kuanza vikao vyake vya kujadili sura ya kwanza na ya sita ya Rasimu ya Katiba, zinazohusu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na muundo wake.
Hali hiyo ilitokana na kutopatikana kwa hati ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na ile ya Sheria ya Baraza la Mapinduzi ya kuridhia Mkataba wa Muungano.
Aprili 2 mwaka huu, Kamati namba 2 ilimwalika, Spika Mstaafu wa Bunge la Muungano, Pius Msekwa kutoa ufafanuzi kuhusu hati hizo, lakini uhalali wa saini zake uliibua malumbano makali. Msekwa aliitwa kutokana na kwamba ndiye aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika wakati huo.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Shamsi Vuai Nahodha, alithibitisha kutokea utata huo na kwamba walilazimika kumuita Msekwa ili kupata ufafanuzi wa masuala kadhaa na Msekwa alisema saini zilizopo katika hati hiyo ni ya kwake.
Nahodha alisema kwa maelezo ya Msekwa, inaonekana hati ya Muungano ipo Umoja wa Mataifa (UN), kwani kabla ya Muungano, Tanganyika ilikuwa na kiti chake UN na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar hali kadhalika.
Aliongeza kuwa baada ya UN kuomba uthibitisho wa Muungano, ndipo walipelekewa hati hiyo na kwamba haijawahi kurejeshwa.
Kwa upande wake Katibu wa Bunge la Katiba, Yahya Hamis Hamad alisema hati hiyo ipo Dar es Salaam na ni moja tu, hivyo siyo rahisi kuipeleka bungeni Dodoma.

Matumaini Katiba Mpya arijojo

Ikulu imeeleza kuwa imeshindwa kutimiza ahadi yake kwa taifa ya kulipatia Katiba Mpya ifikapo Aprili 26, 2014.
Katibu Mkuu Kiongozi (KMK), Balozi Ombeni Sefue alilieleza gazeti hili kuwa kwa hali ya mchakato huo ilivyo sasa, wameshindwa kufikia lengo hilo, lakini hawajakata tamaa kuhusu kupatikana Katiba Mpya ndani ya mwaka huu.
“Kweli matarajio ya awali yalikuwa hayo, lakini kama unavyoona hali ilivyo, ni vigumu kusema matarajio mengine, ingawa majadiliano yaliyofanywa mwaka huu ni lazima Katiba inayopendekezwa iwasilishwe kwa wananchi na mwakani tutakuwa na Katiba Mpya,” alieleza Balozi Sefue.
Katika hali isiyoeleweka Balozi Sefue alisisitiza msimamo wa awali wa Serikali kwamba Katiba itakayopatikana itatumika kwenye Uchaguzi Mkuu, unaotarajiwa kufanyika mwaka ujao.
Dk Slaa
Katibu Mkuu wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (Chadema), Dk. Willbroad Slaa, alisema hilo ni fundisho kwa Serikali kwamba kiburi na jeuri havitakiwi katika masuala yanayohusu umma.
Alisema muda huo wa kupatikana Katiba Mpya ulipotangazwa, walioanzisha kilio cha kudai Katiba Mpya nchini ambao aliwataja kuwa ni vyama vya upinzani vya siasa, taasisi mbalimbali za kijamii walipinga na kutoa ushauri kwa Serikali, lakini walipuuzwa.
Dk. Slaa alisema walipendekeza kwamba badala ya kupeleka mchakato wa Katiba mchakamchaka, warekebishe kwa mara ya 15 Katiba inayotumika, ili iende na wakati wa sasa ikiwamo Uchaguzi Mkuu ujao kwa lengo la kutoa muda wa kutosha kwa mchakato wa taifa kupata Katiba Mpya.
“Lakini walitukebehi na kututukana sana, sasa kiko wapi Aprili 26 hiyo hapo na Katiba haijapatikana na kusema itapatikana mwaka huu na kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu mwakani ni ndoto za mchana,” alieleza Dk. Slaa.
Dk. Slaa alisema tukio hilo liwe fundisho kwa Serikali, wawe wakweli, wanyoofu na wafahamu kuwa nje ya Serikali kuna watu makini na wanaojua vilivyo mchakato wa Katiba.
Alisema ana taarifa za Bunge Maalumu kuahirishwa Mei 9, 2014 ili kupisha Bunge la Bajeti. Hivyo mategemeo ya Katiba Mpya kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, yanatia shaka.
“Kwa akili ya kawaida tu isiyohitaji elimu ya chuo chochote, kutumia Katiba Mpya kwenye Uchaguzi Mkuu ujao ni jambo lisilowezekana kwa hiyo waache kutuletea matumaini yasiyokuwapo, sisi siyo watoto wadogo,” alieleza Dk. Slaa.
Kauli ya LHRC
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Helen Kijo Bisimba, alisema siyo tu Serikali imeshindwa kutimiza ahadi ya muda iliyojiwekea, bali hata mchakato wenyewe haueleweki.
Dk. Bisimba alisema kwa hali ilivyo, hawana hakika ya kupata Katiba na ikipatikana haitakidhi matakwa ya wananchi, kwa kuwa wanataka Katiba ya watu siyo ya kundi moja la watu.
“Mambo ya nchi hii tunayafahamu, inaweza ikapatikana kwa nguvu lakini wajue wananchi wataikataa na hata ikilazimishwa, haitakidhi mahitaji, itaweza kuathiri ustawi wa taifa,” alieleza Dk. Bisimba.
Alisema hilo waliliona mapema, wakataka kila hatua ya mchakato ipewe muda wa kutosha kabla ya hatua nyingine, ili wananchi waelimishwe lakini hawakusikilizwa.
Alisema kuwa katika mazingira hayohayo, Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilifanya kazi kubwa hadi kufanikisha maoni ya wananchi kupatikana na kutengeneza Rasimu ya kwanza na ya pili iliyowasilishwa bungeni Machi 18, 2014, lakini kwa jinsi Bunge Maalumu linavyoendeshwa, kuna kila dalili kwamba kazi hiyo itaharibiwa.
“Wakichezea Rasimu wajue wanachezea maoni ya wananchi, wanaoweza kuyakataa kupitia kura ya maoni na hivyo kusababishia taifa hasara isiyomithilika,” alieleza Dk. Bisimba.
Dk. Bisimba alisema mchakato huo umegharimu taifa fedha nyingi, muda mwingi, nguvu, akili, afya na hata uhai wa watu, hautakiwi kufanyiwa mzaha.
Alipotafutwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro ili kuzungumzia suala hilo jana hakupatikana, lakini Naibu Waziri wa wizara hiyo Angela Kairuki, alisema kuwa kwa hali ilivyo ni dhahiri haiwezekani kupata Katiba Mpya kwa muda huu tofauti na ilivyodhaniwa awali.
Hata hivyo, Kairuki alisema hawezi kuzungumzia hatua iliyofikiwa katika mchakato huo kwani mwenye mamlaka ya kuzungumzia ratiba ya Bunge Maalumu la Katiba ni mwenyekiti wake, Samuel Sitta.
“Hata hivyo tunachotakiwa kuzungumzia ni ubora wa kazi inayofanyika ili kufikia lengo la kupata Katiba itakayoongoza nchi kwa miaka 50 ijayo,” alisema Kairuki.

Thursday, 3 April 2014

Waathirika wa milipuko ya Osama Dar wafurahia fidia

Dar es Salaam. Baadhi ya wanafamilia wa waliopoteza ndugu kwenye shambulio la ugaidi katika Ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam mwaka 1998, wameelezea kufarijika kutokana na malipo ya fidia, licha ya kwamba hayawezi kurejesha uhai wa waliokufa.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti, ndugu hao walisema, licha ya mahakama nchini Marekani kuwapa fidia lakini pengo la jamaa zao halitazibika.
Wiki iliyopita, Mahakama Kuu ya Marekani, ilitoa amri ya kuwalipa fidia ya dola za Marekani 957 milioni (Sh1.555 trilioni) waathirika 23 wa shambulio hilo.
Jaji Thomas Bates katika hukumu yake alisema kati ya fedha hizo, Dola za Marekani 420 milioni (Sh670 bilioni) watapewa ndugu wa marehemu watano na waathirika wanne wa Tanzania wakati kitita kilichobaki kitakwenda kwa waathirika ambao ni Wamarekani.
Jaji Bates alisema Serikali za Iran na Sudan zitawajibika kulipa fidia hizo kutokana na kuhusika na mashambulio hayo mabaya kuwahi kutokea Afrika Mashariki.
Mmoja wa jamaa waliopoteza maisha katika tukio hilo, Kulwa Ramadhan alisema anasubiri kuletewa taarifa zaidi kuhusu taratibu za kupata fidia hiyo.
“Huwezi kuwa umeridhika na fidia kwa kuwa tumepoteza ndugu zetu lakini pia hata hicho kilichopatikana hatukukitarajia kupata,” alisema Ramadhan.
Alisema kuna baadhi ya jamaa wa marehemu watano hawakuingizwa kwenye idadi ya watakaopata fidia kutokana na kuchelewa kujiandikisha katika kesi hiyo.
“Baada ya tukio uongozi wa Ubalozi wa Marekani ulituambia tutoe taarifa zetu zote za mawasiliano na kwamba tusibadilishe namba za simu kwa ajili ya kuwasiliana kinachojiri.
“Lakini kuna baadhi ya jamaa walibadilisha namba zao na kufanya mawasiliano kuwa magumu hivyo kushindwa kuingizwa katika idadi ya wadai katika kesi hiyo,” alisema.
Ramadhan aliyempoteza pacha wake, Dotto Ramadhani alisema baadhi ya jamaa walijitokeza baadaye baada ya hatua muhimu za kesi kufanyika kitendo ambacho kiliwazuia kushiriki katika kesi.
Waathirika wengine
Naye Judith Mwila aliyempoteza mume wake kwenye tukio hilo, alisema anashukuru Ubalozi wa Marekani pamoja na mawakili waliowasaidia kufanikisha kesi hiyo.
“Binafsi nimepata taarifa kamili jana (juzi) kutoka kwenye gazeti la Mwananchi na sikutarajia kama tungeshinda kesi hiyo na tukapewa fidia ya fedha kiasi hicho. Hata hivyo tunaendelea kusubiri taarifa za mawakili wetu kuhusu taratibu zinazofuata kupata fedha hizo,” alisema.
Aliongeza kuwa iwapo atapata sehemu ya fedha hizo atashauriana na watoto wake jambo la kufanya ikiwamo kufanya biashara kubwa. Mwila ana watoto watatu alioachiwa na marehemu mume wake.
Alisema kuwa tangu mchakato wa kesi ulipoanza mwanzoni mwa mwaka 2001, Ubalozi wa Marekani na mawakili wao, walimpeleka Marekani mara mbili.
“Kesi hii imedumu muda mrefu. Mara ya kwanza nilikwenda 2001 kutoa ushahidi na mara ya mwisho ni 2010 na tangu wakati huo tulikuwa tukipewa tu taarifa juu ya maendeleo ya kesi,” alisema Mwila.
Kwa upande wake, Grace Paulo ambaye alifiwa na mumewe Elisha Paulo alisema: “Ninamshukuru Mungu kwa sisi kushinda kesi hii na hivyo tunasubiri mawasiliano na wahusika kufahamu jinsi ya kupata fedha hizo.
“Tumekuwa tukiishi kwa shida sana, hivyo hizo fedha zitatusaidia kujikwamua na matatizo yanayonikabili na mwanangu,” alisema Paulo ambaye aliachiwa mtoto mmoja aitwaye Mary Paulo.
Kwa mujibu wa waathirika hao, Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Misaada la Marekani (Usaid) liliwapa msaada wa kuwasomesha watoto pamoja na makazi ili kupunguza makali ya maisha.
Hata hivyo, wengi wao wanaendelea kufanya biashara ndogondogo kutokana na misaada hiyo kuwekwa katika eneo maalumu la ada za watoto.
“Kwa sasa ninafanya biashara ya kuuza nguo za mitumba na nilishaondoka Dar es Salaam mara tu baada ya msiba mwaka 1998 kutokana na maisha ya mjini kuwa magumu.
“Baadaye Ubalozi kupitia taasisi za kiraia walinitafuta hadi wilayani Mpwapwa ndipo waliponijengea nyumba ninayoishi sasa,” aliongeza Paulo anayeishi mkoani Dodoma.
Jamaa hao pia walisema kuwa gharama halisi za kesi hiyo hawazifahamu kutokana na kesi nzima kusimamiwa na Serikali ya Marekani na mawakili wao.
Hata hivyo, uhakika wa kupata fedha hizo unabaki mikononi mwa wakili wa jamaa hao, Thomas Fortune Fay ambaye baada ya hukumu hiyo alisema anafuatilia jinsi ya kupata fedha kwa Serikali za Sudan na Iran.
Alisema ataangalia jinsi ya kutaifisha baadhi ya mali za nchi hizo ili kupata fedha za kuwalipa waathirika hao.

Jaji Warioba aishangaa Serikali



Dodoma. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema waliokuwa wajumbe wa tume hiyo hawajawahi kudai malipo ya pensheni ya Sh200 milioni kama inavyodaiwa.
“Wajumbe wa Tume hawajatoa madai ya kulipwa shilingi milioni mia mbili. Hakuna mjumbe yeyote aliyetoa dai kama hilo na Serikali inajua,” alisema
Jaji Warioba katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, aliyoitoa kupitia Nyalali, Warioba and Mahalu Law Advocates ali ongeza:
“Nimeona taarifa iliyotolewa na Serikali kuhusu Tume ya Mabadiliko, nimeshangazwa na maudhui na lugha iliyotumika,” alisema Warioba akirejea taarifa iliyotolewa na Ikulu juzi ikieleza jinsi tume hiyo ilivyohitimisha kazi zake.
Wiki hii Jaji Warioba alikaririwa akilalamika jinsi yeye na makamishna wake walivyoondolewa ofisini na kunyang’anywa magari kwa haraka bila kusubiri siku waliyopanga kufanya makabidhiano, lakini Ikulu ilimjibu kwamba shughuli za Tume hiyo zilikoma siku ambayo Tume ilivunjwa.
Katika taarifa yake ya jana, Jaji Warioba alisema aliwasilisha Rasimu ya Katiba Machi 18 mwaka huu na Tume ilivunjwa Machi 19 wakati wajumbe wakiwa bado mjini Dodoma.
“Pamoja na lugha ya kejeli inayotumiwa na Serikali kuniita mnafiki, busara ya kawaida ilitakiwa kutumika kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani na kuandaa makabidhiano,” alisema.
Alisisitiza kuwa Serikali ilikuwa na wajibu wa kuwarejesha makwao wajumbe wa tume hiyo, hata kama muda wa kisheria wa kufanya kazi ulikuwa umepita.
“Niliwasilisha Rasimu Machi 18, 2014. Tume imevunjwa Machi 19, 2014 wakati wajumbe wako Dodoma. Pamoja na lugha ya kejeli iliyotumiwa na Serikali na kuniita mnafiki, busara ya kawaida ingeonyesha umuhimu wa Serikali kujipa muda wa kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani,” alisema Jaji Warioba na kuongeza:
“Hata kama sheria ilitaja muda wa kuvunja Tume bado ilikuwa ni wajibu Serikali kufanya mipango ya safari ya wajumbe baada ya kumaliza kazi. Sheria haikuizuia Serikali kufanya hilo. Huo ni wajibu wa Serikali na utaratibu wa kawaida unaotumiwa na Serikali kwa tume zote inazoziunda. Inaonekana Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliwekewa utaratibu tofauti. Kulikoni?”.

Friday, 28 March 2014

Siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili kikatiba

Katika maisha ya kawaida, binadamu ana msimamo wake na hata uamuzi  asiopenda ubadilike.
Katika medani ya siasa nchini msimamo wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kuhusu Muungano na muundo  unafahamika. Ni muundo wa kutaka  Serikali mbili ambao chama hicho unakipigania kwa udi na uvumba.
Hata hivyo, msimamo huo ni kinyume na mapendekezo au matakwa ya wengi kama ilivyoainishwa kwenye Rasimu ya Pili ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
 Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba ilikusanya maoni ya wananchi na ilipendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu.
Hivi karibuni akifungua Bunge Maalumu la Katiba, Rais Jakaya Kikwete akaunga mkono msimamo wa chama chake, jambo lililoibua mjadala unaoendelea hadi sasa.
Hoja ya Serikali mbili
Kwanini CCM wanataka Serikali mbili na siyo tatu au moja kama ilivyo maoni ya wananchi walio wengi kwa mujibu wa maelezo ya Tume ya Warioba? Makala haya yanachambua hoja hiyo.
 Profesa Bakar Mohammed ni Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anayesema msimamo wa CCM wa kudai Serikali mbili unatokana na hofu ya uhafidhina wa kuogopa mabadiliko.
Anasema viongozi wengi wa CCM wanasumbuliwa na hofu na woga wa mabadiliko na kwamba wanakuwa wagumu kuyakubali  yanapotaka kutokea.
“Kama mtu unaangalia madaraka zaidi, lazima kunakuwa na woga, na hii ni hulka ya binadamu kuwa na woga wa kuacha kile ulichokizoea… Lakini ukiangalia masilahi ya nchi na kuacha yale yanayokusukuma kusingekuwa na wasiwasi huu unaoonekana sasa,” anasema.
Anasema CCM inachofanya ni kuhakikisha haking’oki madarakani, huku viongozi wake wakiamini kuwa wana sifa za kuongoza na siyo wengineo.
Profesa Bakari anailinganisha hofu ya sasa ya CCM na ile waliyokuwa nayo viongozi wa chama hicho miaka ya 1990 zilipoanza vuguvugu za mabadiliko ya siasa za vyama vingi. Anasema CCM kiliendesha propaganda kuwa mfumo wa vyama vingi haukuwa na tija na ungeleta vita.
Hofu hiyo anasema ndiyo inayokifanya chama hicho kikongwe kuhofia kung’olewa madarakani.
 “Woga huo bado upo, wanaogopa pengine mfumo ukiwa wa Serikali tatu uwezekano wa wao kubaki madarakani utakuwa mdogo,” anafafanua.
Anaongeza kusema kuwa  hofu ya CCM siyo kwa ajili ya masilahi ya nchi,  badala yake inaonekana chama kinaangalia masilahi yake.
Ingekuwa vyema anasema kwa CCM  kueleza madhara yanayoweza kulikumba taifa ikiwa muundo wa Serikali tatu utapita.
 “Wanatoa hoja kuwa mfumo wa Serikali tatu unaweza kusambaratisha nchi, lakini hakuna uhakika kama mfumo huu uliopo nchi hauwezi kusambaratika,” anasema.
Hofu ya kuyumba na kuanguka
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk. Benson Bana anasema siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili inatokana na hofu ya kuyumba na kuanguka.
Anasema CCM kimekuwa madarakani na mfumo huo kwa miaka 50 na kwamba hofu yao ni kuwa ukiondoa Serikali mbili kinaweza kuyumba na kuachia madaraka.
Anasema misingi ya wanasiasa ni madaraka, na kwamba ukishayapata, huwezi kuyaachia kirahisi.
“Misingi ya wanasiasa ni madaraka… Kuyalinda, kuyahifadhi na kuyatumia madaraka yale kwa namna yoyote…Huwezi kuyaachia madaraka kirahisi. Utafanya ujanja, utatumia mbinu chafu  ili tu kuhakikisha unabaki madarakani, na hiki ndicho wanachofanya CCM,” anasema.
Dk. Bana anasema CCM kingeeleweka na kingekuwa na mwonekano mzuri zaidi endapo wangepigania kuwapo kwa Serikali moja.
“Wangekuwa wanataka muungano imara, endelevu na uliokomaa wangeelekeza katika Serikali moja…Lakini hawataki kwa sababu wanajua moja inaweza ikawanyima uongozi,” anasema.
Dk. Bana anasema ni vyema wananchi wakaelimishwa huu muungano una faida gani na wanafunzi shuleni katika elimu ya uraia waelezwe faida zake.
“Ingekuwa wazi tungejua nani anafaidika na nini, mikopo misaada, nani anachangia nini…Je zile sababu za waasisi za kuungana bado zipo sasa miaka 50 ya Muungano, ule woga kuwa Zanzibar itamezwa bado upo leo?” Anahoji.
Anaongeza kuwa ni vyema kwa watawala kutazama  mazingira ya sasa ya siasa zetu kwa kile anachoeleza kuwa hata Katiba ikipita ikakubali kuwapo wa Serikali mbili, bado wananchi watahoji mantiki ya muundo huo.
Msomi mwingine wa siasa, Dk. Alexander Makuliko  anasema hofu ya CCM ni kuwa ndio iliyouasisi Muungano wa Serikali mbili, hivyo  isingependa hali hiyo ibadilike.
Anaendelea kusema kuwa CCM imezoea mfumo huu na kuwa ikiukosa itaathirika, kwakuwa ni sera yake na imekuwa ikiitekeleza, lakini msimamo wa  wananchi ndiyo kitu cha msingi kuzingatiwa. Hoja zijengwe na zisikilizwe, ubabe hautakiwi, busara inahitajika zaidi.
Anasema pamoja na suala la  Serikali mbili kuwa  ni pimajoto ya  uhai wa CCM,  hata hivyo hoja zinazotolewa katika kutetea msimamo wao ni nzuri tu na zinazoeleweka vyema.
“Sioni kama wanang’ang’ania, lakini ukweli ni kuwa kila chama kina sera yake, na CCM kimeweka sera yake katika suala la Muungano wao wanasema ni Serikali mbili, na siyo tatu…kwamba tatu zitaongeza gharama na mengineyo, ni sababu za msingi kabisa,” anasema.
Anaongeza kuwa hoja zinazotolewa na chama tawala ni kubwa na siyo za kupuuzwa, lakini vilevile kero zinazotajwa kuhusu mfumo wa Muungano uliopo nazo zipo na zinaweza kutatuliwa katika mfumo uliopo.
“Unajua hivi vyama kila kimoja kinataka kuvutia kwake, hata bila rasimu ya Warioba…Ninashauri walete hoja, kisha watu wazipime hizo hoja, kwanini serikali mbili, na wale wa tatu tayari wameleta hoja na ushahidi, watu waachwe wapime,” anasema na kuongeza:
‘’Jambo la msingi kuzingatiwa ni kuwa mawazo ya wananchi wengi yataonekana wakati wa kura za maoni. Angalizo ni  kuhakikisha kuwa kura hiyo isije ikachakachuliwa.’’

.. Samuel Sitta awekwa mtegoni

Dodoma/Dar. Suala la ama kutumia kura ya siri au ya wazi kuamua ibara za Rasimu ya Katiba jana liliuteka upya mjadala wa Kanuni za Bunge la Katiba, huku ikielezwa kuwa limewekwa kama mtego kwa Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta katika kuwania urais.
Sitta ni mmoja wa wanasiasa wanaotajwa kuwa katika kinyang’anyiro cha urais katika uchaguzi mkuu ujao kupitia CCM, huku akikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa mahasimu wake kisiasa ndani ya chama hicho.
Mjumbe wa Bunge la Katiba, Godbless Lema alimtaka Sitta kuwa makini na maelekezo aliyodai mwenyekiti huyo anapewa katika uendeshaji wa Bunge na kudai pia kuwa, kuna kundi la watu wanaotaka urais katika Uchaguzi Mkuu 2015 wanaotaka kumkwamisha.
Akichangia hoja ya mapendekezo ya mabadiliko ya kanuni yaliyotaka kupitishwa mifumo miwili ya kura kwa wazi na siri, Lema ambaye ni Mbunge wa Arusha alisema kwa mazingira ambayo yanaendelea, Sitta anapaswa kuwa makini na watu wanaompatia maelekezo wakitaka aonekane hafai baadaye.
“Ni vyema ukawa makini na mapendekezo unayoletewa kwa sababu hao wote pamoja na wanachama wa chama chako wanajua kama utaliongoza vizuri Bunge hili, basi unaweza ukapata tiketi ya kugombea urais 2015 ndani ya chama chako, lakini ukishindwa watakudhihaki kuwa umeshindwa, hivyo hutaweza kuliongoza taifa,” alisema Lema huku Sitta aliyeonekana awali akitabasamu, alibadilika na kumtazama mbunge huyo kwa umakini.
Lema alisema miongoni mwa wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM na kamati nyingine za Bunge hilo, kuna watu ambao wanataka kugombea urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Katika mjadala huo, ilionekana wazi kuwa wajumbe bado wamegawanyika pande mbili – CCM wakionekana kuunga mkono kura ya wazi na upande wa upinzani wakipigia chapuo kura ya siri.
Miongoni mwa waliopigia debe kura ya siri ni John Mnyika aliyesema suala la upigaji kura ni la kikatiba ili kuhakikisha kila mjumbe anapiga kura yake bila kushurutishwa, kushinikizwa wala kupokea maelekezo kutoka kwa mtu au chombo chochote.
Wajumbe hao walikuwa wanajadili mapendekezo yaliyowasilishwa jana na Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge, Pandu Ameir Kificho, baada ya juzi kuzua mvutano uliosababisha Bunge hilo kuvunjika ili kusubiri maridhiano ya pande zinazopingana.
Mapendekezo ya Kanuni
Kificho alisema, mapendekezo hayo yamefikiwa kutokana na masharti ya kanuni ya 59 (1) na 87 (1) kwamba kanuni ya 38 (1) iweke utaratibu wa kupiga kura ama ya wazi au ya siri, ambao utatekelezwa na mwenyekiti kwa kushauriana na katibu.
Alisema wakati wa kupiga kura ya siri kila mjumbe atapiga kura ya ‘ndio’ au ‘hapana’  kwa kutumia karatasi ya kupigia kura itakayokuwa imeandaliwa na katibu kwa ajili ya hilo.
Mjumbe Michael Laizer alisema wamechoshwa  na malumbano juu ya kura za wazi au siri, hivyo iwapo kuna wajumbe ambao hawataki mapendekezo ya kamati waondoke.
Naye Ezekiel Olouch alisema utaratibu unaopendekezwa na kamati haujawahi kufanyika mahala popote duniani.
Alisema kura ya siri imekuwa ikitumika kuamua mambo ya msingi na kuepusha mpasuko katika jamii hasa katika masuala ambayo yanaweza kuligawa taifa.
Mohamed Raza alisema msimamo wake ni kupiga kura ya wazi kwani wengi wanajua msimamo wake ambao ametoka nao Zanzibar.
Joshua Nassari alisema anashangazwa kuona Taifa linarejeshwa katika karne ya 18 katika upigaji wa kura kwa kung’ang’ania kura ya wazi wakati wao wamechaguliwa kwa kura za siri.
“Mwenyekiti wewe tumekuchagua kwa siri wajumbe wote wamepatikana kwa siri, iweje leo kulazimisha kura ya wazi ili wajumbe wa CCM watakaopiga kura za siri wachukuliwe hatua,” alisema Nassari.

Tuhuma nzito bungeni,ni za rushwa dhidi ya Waziri Mkuu Pinda

Dar es Salaam. Hali ya hewa jana ilichafuka kwenye Bunge la Katiba baada ya mjumbe Ezekiel Wenje kuwatuhumu Waziri Mkuu Mizengo Pinda na baadhi ya mawaziri kuwa waliwahonga baadhi ya wajumbe wa kundi la 201.
Katika tuhuma hizo, Wenje alimtaja Waziri Profesa Jumanne Maghembe, Dk. Shukuru Kawambwa na Gaudensia Kabaka akisema kuwa walitoa rushwa ya vyakula, maji na vinywaji kwa wajumbe hao ili waunge mkono msimamo wa serikali mbili.
Kauli hiyo, iliyotolewa katika mjadala wa mabadiliko ya kanuni, ilisababisha mawaziri hao kunyanyuka kujibu tuhuma hizo, huku Wenje akisisitiza kuwa aliyoyasema ni kweli tupu.
Vilevile baadhi ya wajumbe wanaotoka katika kundi hilo walicharuka na kujaribu kujitetea huku mmojawapo akitishia kuwa iwapo Wenje asingeomba radhi, asingetoka ndani ya Bunge hilo.
Hoja ilipoanzia
Wenje, ambaye pia ni mbunge wa Nyamagana (Chadema), alianza kwa kueleza kwamba wapinzani “walilia” sana kuwa Bunge la Katiba lisingekuwa na usawa kutokana na Chama cha Mapinduzi kuwa na wajumbe wengi, ndipo ikaonekana wapatikane wajumbe wengine 201, lakini jambo la ajabu ni kwamba walioteuliwa katika kundi hilo asilimia 80 ni makada wa CCM akiwamo mzee maarufu ambaye ameingizwa kama mganga wa jadi.
Ingawa hakumtaja jina, Wenje alikuwa anamaanisha kada mkongwe wa CCM, Kingunge Ngombale-Mwiru aliyeteuliwa kupitia kundi la waganga wa jadi.
Kuhusu rushwa, Wenje alisema:“…Sasa kuna wajumbe wa kundi la 201 walipelekwa kwa Profesa Maghembe na Dk. Kawambwa wamepeana rushwa, vikao vingi vilifanyika usiku. Hii haikubaliki.”
Baada ya kauli hiyo ya Wenje, Profesa Maghembe alisimama ghafla huku akionekana kutaharuki, ambapo Makamu Mwenyekiti Samia Suluhu Hassan alimpa nafasi ya kujieleza.
Profesa Maghembe alikiri kuwakaribisha baadhi ya wajumbe wa kundi hilo, akieleza kwamba ilikuwa ni katika hali ya ukarimu uliozoeleka miongoni mwa jamii ya Kitanzania.
“Kuna kundi lipo hapa ambalo linafanya kazi ya kudhalilisha wenzao. Ni kweli niliwaalika kwa chakula wajumbe hao kwa taratibu za kawaida, lakini hakuna mbunge hapa anayeshindwa kujinunulia chakula, hakuna anayeweza kupewa rushwa.
“Kwa sababu hiyo ninaomba kiti chako kimtake mjumbe aliyewasilisha hoja hiyo aniombe radhi. Wenje aniombe radhi,” alisema Profesa Maghembe akiwa katika hali ya hasira, huku kukiwa na sauti za kuzomea na kushangilia kutoka kwa wajumbe.
Makamu mwenyekiti pia alifanya jitihada za kuwataka wajumbe kuwa wavumilivu, huku akitoa nafasi kwa Dk. Kawambwa kujieleza akisisitiza kwamba ni tuhuma nzito. 
Kawambwa alisema: “Ni kweli nilikutana nao; ni wajumbe ambao wanatoka kwenye taasisi zinazojihusisha na masuala ya elimu, lakini mbona wameshafanya mikutano yao mingine mingi ambayo mimi hawakuniita. Kama mtu akiwa hana hoja bora akae chini.”
Makamu Mwenyekiti alimtaka Wenje aombe radhi kutokana na kauli yake, lakini katika hali ya kushangaza mjumbe huyo alisisitiza kwamba Profesa Maghembe na Dk. Kawambwa wamekiri.
“Maghembe amekiri aliwaita wafugaji na wavuvi ndiyo waliokula chakula cha rushwa, pia wapo wengine walienda kwa Waziri Gaudensia Kabaka, kuna ushahidi mama mmoja siwezi kumtaja jina hapa alikwenda huko akafukuzwa, nitakupa jina lake mwenyekiti baadaye. Aliambiwa kwamba anatoa siri… hoja iliyojadiliwa huko ilikuwa ni kwamba msimamo ni wa serikali mbili… rushwa ya chakula, maji na bahasha walipewa,” alisema Wenje na kusababisha kulipuka kwa kelele zaidi.
Wenje aliongeza kuwa kuna wajumbe wengine walikwenda hadi kwa waziri mkuu ambako walikula, walikunywa hadi saa 7:00 usiku.
Alisema wengine walikwenda kwa Gaudensia Kabaka (Waziri wa Kazi na Ajira) na walikula na kunywa na kupewa bahasha.
Baada ya Wenje kukaa, baadhi ya wajumbe wa kundi la 201 walichachamaa wakitaka kutetea hadhi yao, akiwamo mjumbe kutoka kundi la wafugaji, Esther Juma aliyesema hawatendewi haki kama kundi kusema kwamba walihongwa.
Alisema yeye ana ng’ombe 3,000 na asingeweza kwenda kupokea rushwa ya chakula na kumtaka mbunge huyo kuwaomba radhi la sivyo asingetoka mlangoni.
Wakati mjadala huo ukiendelea, mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta aliyekuwa ametoka kwa udhuru, alirejea kimya kimya, na kumtaka Wenje kueleza iwapo anadhani kauli yake haikuwaudhi baadhi ya wajumbe.
Wenje alikiri kuwa ni kweli baadhi ya wajumbe wameudhika kutokana na ukweli aliosema dhidi yao na kuwaomba radhi kwa ukweli huo.
Kauli hiyo ilimfanya Sitta kutangaza kuwa anapeleka suala hilo kwenye Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge na uamuzi utakaotolewa atautangaza bungeni.

Tuesday, 25 March 2014

Baada ya matokeo Fanya uamuzi sahihi kujiendeleza kielimu

Wapo wanaofuata mkumbo wa kusoma mchepuo (combination) fulani kwa sababu marafiki zao wengi wameuchagua mchepuo huo. Aidha, wapo wanaolazimisha kusoma masomo magumu yaliyo nje ya uwezo wao kiakili.
Kwa mfano, unaweza kupata alama C katika mtihani wa Hisabati (Basic Mathematics), lakini alama hiyo siyo tiketi pekee ya kuchagua kusoma masomo yenye hesabu za kiwango cha juu (Advanced Mathematics).
Waliofeli nao?
Kama ilivyotangazwa na Baraza la Mitihani Tanzania, asilimia 78.91 ya wahitimu wamepata daraja la nne na sifuri. Ni dhahiri kuwa wanafunzi hawa hawana sifa ya kujiunga na kidato cha tano.
Hata hivyo, huo ndiyo uwe mwisho wa safari ya kusaka elimu kwa vile tu umefeli? Makala haya yanajaribu kutoa mapendekezo mbadala yanayoweza kutumiwa na wanafunzi ili kujiendeleza zaidi kielimu?
Kwanza ieleweke kutokuchaguliwa kidato cha tano au kufeli kidato cha nne si ishara mbaya maishani na wala haijawa sababu ya kuanza kuamini kuwa umeshafeli kimaisha.
Uzoefu unaonyesha hapa nchini kuna watu wengi baadhi yao leo ni maprofesa maarufu waliowahi kufeli katika madaraja fulani ya kielimu siku za nyuma, lakini kwa kuwa tu walikuwa na dhamira ya dhati na kutoa uamuzi sahihi, waliweza kujiendeleza na kufika kiwango hicho cha elimu kinachotamaniwa na kila mtu.
Nikupe siri moja ninayoifahamu kuhusu wasomi hawa, baadhi yao waliwahi kuwa walimu wangu pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hawa pamoja na wengine kuamua kuanza maisha ya familia au kikazi lakini walijiendeleza kupitia mfumo usio rasmi.
Unaweza kuihuisha ndoto yako ya kupata elimu kwa kurudia mitihani yako kwa mara nyingine. Mfumo wetu wa elimu unatoa fursa hiyo na ndiyo maana kuna utaratibu wa watahiniwa binafsi.
Rudi tena darasani. Kuna shule nyingi za sekondari zenye programu maalumu kwa ajili ya watu wanaorudia mitihani ya kidato cha nne tena kwa bei rahisi.
Zitafute shule hizi ila kuwa makini na vituo vinavyoitwa kwa Kiingereza ‘Tuition Centers’ ambavyo vingi vinajali masilahi kuliko ubora wa elimu.
Chunga jambo hili! Kuna mtindo wa wanafunzi wanaofeli kidato cha nne na kuamua kuingia kidato cha tano huku wakirudia mitihani yao. Hawa wanalazimika kusoma masomo ya mitihani wanayoirudia huku wakisoma pia masomo mapya ya kidato cha tano.
Huku ni kujidanganya, kwa mtindo huu, mwanafunzi husika hawezi kusoma kwa undani masomo ya kidato cha tano badala yake atakuwa anasoma ‘kimtego mtego’ ili afaulu tu mitihani ya ndani.
Fursa nyingine iliyopo kujiendeleza ni kusoma fani za ngazi ya cheti. Kusomea cheti siyo kuonekana mjinga, kwanza una uhakika wa kuajiriwa au kujiajiri. Kwa mtu mwenye ndoto ya kusoma zaidi, kipato cha ajira yako ndicho unachoweza kukitumia kujiendeleza zaidi.
Upo mfano mzuri wa walimu wa shule za msingi waliosomea ualimu kwa ngazi ya cheti. Wengi hujiendeleza kwa kurudia mitihani na hatimaye kufika vyuo vikuu.
Siyo ualimu pekee, kwa mujibu wa mfumo wa elimu nchini, kuna vyuo vingi vya kada ya kati vinavyotoa kozi za msingi kwa wahitimu wa kidato cha nne wakiwamo waliopata angalau daraja la nne.
Unachofanya ni kusomea cheti cha msingi kwa mwaka mmoja, kisha unaendelea kwa kusoma tena cheti cha juu kabla ya kupata fursa ya kusoma stashahada.
Kwa walio makini mlolongo huu wa elimu unaweza kukufikisha mbali. Unaweza kufika chuo kikuu kwa kutumia njia hii ya kusoma. Vipo vyuo vikuu vinavyowakubali wanafunzi hawa kwa sharti la kuwa vimesajiliwa na Baraza la Usimamizi wa Elimu ya Ufundi (NACTE).
Fursa nyingine inayotumiwa na baadhi ya wanafunzi wanaoishia kidato cha nne ni kusoma masomo ya ufundi katika vyuo vinavyosimamiwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA).
Wengi wamekuwa na mtazamo hasi na vyuo vya VETA wanasahau kuwa vyuo hivi vina msaada mkubwa kiajira na hata kujiendeleza zaidi kielimu.
Zaidi ya yote wigo wa mafunzo ya VETA umekua na kuhusisha mambo mengi ya kiufundi ya kisasa na yanayolipa kiajira iwe ajira binafsi au ajira rasmi. Kwa mfano, hivi sasa VETA inaendesha kozi katika sekta za madini, utalii, teknohama na nyinginezo muhimu zama za sasa.

Sitta ‘amkataa’ Warioba bungeni

Dodoma. Jaribio la kutaka kumrejesha bungeni Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba ili ajibu masuala yaliyoibuliwa na Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya kufungua Bunge limegonga mwamba.
Uamuzi wa kukataa ombi hilo ulitolewa jana na Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta wakati akijibu mwongozo ulioombwa na Mjumbe wa Bunge, Julius Mtatiro, akisema hadhani kama ni sahihi ombi hilo kutekelezwa.
Awali Mtatiro aliomba mwongozo kwa mwenyekiti, akitaka kujua iwapo kuna haja ya kumrejesha Jaji Warioba kutoa ufafanuzi juu ya baadhi ya hoja za Rais Kikwete ambazo zimekinzana na maoni ya wananchi yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba.
Mtatiro alisema: “Mtoa hoja mahususi alikuwa ni Jaji Warioba na Rais Kikwete alialikwa kama mgeni rasmi kufungua Bunge, lakini badala yake alikuja kujibu hotuba ya Warioba.
“Kwa sababu Rais alikaribishwa kama mgeni rasmi, lakini  alijibu  hoja za Warioba, je, hatuoni kama kuna haja ya kumrejesha mtoa hoja mahususi aje kujenga hoja  kutokana na alichosema Rais Kikwete?” alihoji Mtatiro ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CUF.
Katika ufafanuzi wake, Sitta alisema tayari amepokea kwa maandishi kutoka kwa baadhi ya wajumbe kuzungumzia suala hilo, jambo ambalo litafanyika lakini si kwa kumwita tena Jaji Warioba.
“Tunapenda kupata muda wa kuzungumzia  suala hili ili kuliweka sawa, hotuba zote mbili ambazo ni muhimu zitaandaliwa ili kupitiwa kuona kama malalamiko yanayotolewa yana hoja,” alisema Sitta.
Tangu Rais Kikwete ahutubie Bunge Ijumaa na kutoa hoja kinyume na mapendekezo ya Rasimu ya Katiba, hasa muundo wa Muungano, kumeibuka mijadala ya ama kuipinga au kuiunga mkono, huku wengine wakieleza kuwa imekiuka sheria.