Tuesday, 25 March 2014

Baada ya matokeo Fanya uamuzi sahihi kujiendeleza kielimu

Wapo wanaofuata mkumbo wa kusoma mchepuo (combination) fulani kwa sababu marafiki zao wengi wameuchagua mchepuo huo. Aidha, wapo wanaolazimisha kusoma masomo magumu yaliyo nje ya uwezo wao kiakili.
Kwa mfano, unaweza kupata alama C katika mtihani wa Hisabati (Basic Mathematics), lakini alama hiyo siyo tiketi pekee ya kuchagua kusoma masomo yenye hesabu za kiwango cha juu (Advanced Mathematics).
Waliofeli nao?
Kama ilivyotangazwa na Baraza la Mitihani Tanzania, asilimia 78.91 ya wahitimu wamepata daraja la nne na sifuri. Ni dhahiri kuwa wanafunzi hawa hawana sifa ya kujiunga na kidato cha tano.
Hata hivyo, huo ndiyo uwe mwisho wa safari ya kusaka elimu kwa vile tu umefeli? Makala haya yanajaribu kutoa mapendekezo mbadala yanayoweza kutumiwa na wanafunzi ili kujiendeleza zaidi kielimu?
Kwanza ieleweke kutokuchaguliwa kidato cha tano au kufeli kidato cha nne si ishara mbaya maishani na wala haijawa sababu ya kuanza kuamini kuwa umeshafeli kimaisha.
Uzoefu unaonyesha hapa nchini kuna watu wengi baadhi yao leo ni maprofesa maarufu waliowahi kufeli katika madaraja fulani ya kielimu siku za nyuma, lakini kwa kuwa tu walikuwa na dhamira ya dhati na kutoa uamuzi sahihi, waliweza kujiendeleza na kufika kiwango hicho cha elimu kinachotamaniwa na kila mtu.
Nikupe siri moja ninayoifahamu kuhusu wasomi hawa, baadhi yao waliwahi kuwa walimu wangu pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Hawa pamoja na wengine kuamua kuanza maisha ya familia au kikazi lakini walijiendeleza kupitia mfumo usio rasmi.
Unaweza kuihuisha ndoto yako ya kupata elimu kwa kurudia mitihani yako kwa mara nyingine. Mfumo wetu wa elimu unatoa fursa hiyo na ndiyo maana kuna utaratibu wa watahiniwa binafsi.
Rudi tena darasani. Kuna shule nyingi za sekondari zenye programu maalumu kwa ajili ya watu wanaorudia mitihani ya kidato cha nne tena kwa bei rahisi.
Zitafute shule hizi ila kuwa makini na vituo vinavyoitwa kwa Kiingereza ‘Tuition Centers’ ambavyo vingi vinajali masilahi kuliko ubora wa elimu.
Chunga jambo hili! Kuna mtindo wa wanafunzi wanaofeli kidato cha nne na kuamua kuingia kidato cha tano huku wakirudia mitihani yao. Hawa wanalazimika kusoma masomo ya mitihani wanayoirudia huku wakisoma pia masomo mapya ya kidato cha tano.
Huku ni kujidanganya, kwa mtindo huu, mwanafunzi husika hawezi kusoma kwa undani masomo ya kidato cha tano badala yake atakuwa anasoma ‘kimtego mtego’ ili afaulu tu mitihani ya ndani.
Fursa nyingine iliyopo kujiendeleza ni kusoma fani za ngazi ya cheti. Kusomea cheti siyo kuonekana mjinga, kwanza una uhakika wa kuajiriwa au kujiajiri. Kwa mtu mwenye ndoto ya kusoma zaidi, kipato cha ajira yako ndicho unachoweza kukitumia kujiendeleza zaidi.
Upo mfano mzuri wa walimu wa shule za msingi waliosomea ualimu kwa ngazi ya cheti. Wengi hujiendeleza kwa kurudia mitihani na hatimaye kufika vyuo vikuu.
Siyo ualimu pekee, kwa mujibu wa mfumo wa elimu nchini, kuna vyuo vingi vya kada ya kati vinavyotoa kozi za msingi kwa wahitimu wa kidato cha nne wakiwamo waliopata angalau daraja la nne.
Unachofanya ni kusomea cheti cha msingi kwa mwaka mmoja, kisha unaendelea kwa kusoma tena cheti cha juu kabla ya kupata fursa ya kusoma stashahada.
Kwa walio makini mlolongo huu wa elimu unaweza kukufikisha mbali. Unaweza kufika chuo kikuu kwa kutumia njia hii ya kusoma. Vipo vyuo vikuu vinavyowakubali wanafunzi hawa kwa sharti la kuwa vimesajiliwa na Baraza la Usimamizi wa Elimu ya Ufundi (NACTE).
Fursa nyingine inayotumiwa na baadhi ya wanafunzi wanaoishia kidato cha nne ni kusoma masomo ya ufundi katika vyuo vinavyosimamiwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA).
Wengi wamekuwa na mtazamo hasi na vyuo vya VETA wanasahau kuwa vyuo hivi vina msaada mkubwa kiajira na hata kujiendeleza zaidi kielimu.
Zaidi ya yote wigo wa mafunzo ya VETA umekua na kuhusisha mambo mengi ya kiufundi ya kisasa na yanayolipa kiajira iwe ajira binafsi au ajira rasmi. Kwa mfano, hivi sasa VETA inaendesha kozi katika sekta za madini, utalii, teknohama na nyinginezo muhimu zama za sasa.

No comments: