Monday, 29 July 2013

Bajeti finyu kikwazo cha kupata haki mahakamani-Jaji mkuu Tz



Dar es Salaam. Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohammed Chande Othman, amesema ni vigumu mahakama kama taasisi ikaweza kutoa haki kwa wakati kama haitaweza kujitosheleza kimapato.
Aliyasema hayo jana Dar es Salaam alipokuwa akizindua kitabu kilichoandikwa na Jaji Mkuu Mstaafu, Barnabas Samatta kiitwacho ‘Uhuru wa Mahakama’ na kuchapishwa na Kampuni ya Mkuki na Nyota.
“Uhuru wa kitaasisi ambao haujakamilika ni ule wa kifedha na kimiundombinu, bila huu kukamilika ni vigumu kila mwananchi kuweza kupata haki kwa wakati,” alisema Jaji Chande.
Alisema licha ya kuwa Serikali imekuwa ikijitahidi kuongeza bajeti ya mahakama, bado lengo halijafikiwa na kuwa ni vyema muhimili huo ukatengewa fedha za kutosheleza kuendesha shughuli zake.
Jaji Chande alisema kuwa, katika bajeti ya mwaka 2013/14 muhimili huo umetengewa Sh160 bilioni ingawa mahitaji yake halisi ni Sh300 bilioni.
Alisema pia kuwa,kitabu hicho kitawasaidia viongozi wengi ambao wamekuwa wakidhani kuwa mahakama ni chombo cha Serikali. “Wakisoma kitabu hiki wataelewa na wataachana na dhana hii,” alisema Jaji Chande.
Akizungumzia maudhui yaliyopo kwenye kitabu hicho kilichoandikwa kwa lugha ya Kiswahili, Jaji Chande alisema kuwa kimelenga kumsaidia mwananchi wa kawaida kuijua mahakama na pia watawala, vyama vya siasa na wanasheria watapata mwongozo makini.
Kwa upande wake Jaji Samatta alisema kuwa, mwanzoni kabisa wazo lake lilikuwa ni kuandika juu ya kesi ambazo zimewahi kutikisa nchini kwa upande wa Tanzania bara na Zanzibar.
Alisema, alikuja kuachana na wazo hilo baada ya kuona hapati baadhi ya vielelezo ambavyo vingemwezesha kuandika kitabu hicho.

Saturday, 20 July 2013

TENDWA HAMA CHOHOTE KITAKACHO ANZISHA KAMBI YA MAFUNZO YA KIJESHI TUNAKIFUTA

OFISI ya Msajili wa Vyama Vya Siasa nchini imevitaka vyama vya siasa kutii agizo la kutoanzisha kambi za mafunzo ya kulinda amani maarufu kwa jina la mgambo , huku ikisisitiza kwamba itachukua hatua za kisheria kwa chama chochote kitakachoiuka , ikiwemo kukifuta.

Aidha ofisi hiyo imesema kuwa Katiba ya nchi imempa jukumu kila mwananchi kulinda amani na usalama wa nchi, pia kujilinda yeye mwenyewe na mali zake kwa kutoa taarifa katika vyombo vya dola pale anaposikia au kuona mtu anataka kufanya au anafanya uhalifu au amemdhuru mtu.

Kauli hiyo imetolewa  jijini Dares Salaam na ofisi hiyo katika taarifa yake iliyoitoa kwa vyombo vya habari iliyotiwa saini na Rajab Juma kwa niaba ya Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa kufutia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutangaza hivi karibuni kinakusudia kuanzisha kambi za mafunzo ya kujilinda kwa vijana wake nchi nzima.

Alisema suala hilo lilitangazwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe na kuandikwa katika vyombo vya habari kabla ya chama hicho, kuwasiliana na taasisi husika ikiwemo ofisi hiyo ili kupata ushauri kuwa

Mbunge wa Bumbuli akataa kupokea mradi wa maji

lipangwa kujenga tanki lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita 135,000, lakini mkandarasi aliamua kujenga tangi lenye uwezo wa kuhifadhi lita 90,000 ili kuuunganisha na tanki la zamani lenye uwezo huohuo lakini mkandarasi hakuunganisha matanki hayo jambo ambalo ni kosa’’ alisema..

Tanga. Katika hatua inayoashiria kuchoshwa na utekelezaji usioridhisha wa miradi, Mbunge wa Jimbo la Bumbuli, wilayani Lushoto, January Makamba amekataa kuupokea mradi wa maji uliojengwa katika Halmashauri Mpya ya Bumbuli kutokana na kile alichokieleza kuwa umejengwa chini ya kiwango.
Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Bumbuli, Makamba, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia alisema kuwa mradi huo wenye thamani ya zaidi ya Sh400 milioni haukutekelezwa ipasavyo pamoja na kutengewa fedha nyingi na wahisani ambao ni Benki ya Dunia.
Mradi huo umepangiwa kuwanufaisha, wanakijiji katika vijiji vinne vya Bumbuli Mission, Bumbuli Kaya, Mboki na Kwamanolo na ulikuwa uanze kutoa huduma ya maji kuanzia Kijiji cha Kwamanolo.
“Ilipangwa kujenga tanki lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita 135,000, lakini mkandarasi aliamua kujenga tangi lenye uwezo wa kuhifadhi lita 90,000 ili kuuunganisha na tanki la zamani lenye uwezo huohuo lakini mkandarasi hakuunganisha matanki hayo jambo ambalo ni kosa’’ alisema..
Alisema fedha zilizotumika na thamani halisi ya mradi ni tofauti na kwamba ni vigumu kwake kuamini kwamba mradi huo utatekelezwa kama ulivyokusudiwa awali.
Alisema ni afadhali asipokee kwanza mradi huo ili taratibu zingine za kuchunguza zifanyike kama ni kweli mradi huo utasambaza maji ya kutosha.

Masaibu haya ndiyo huwatokea wanawake ndani ya vyumba vya leba

Mwanahamisi Majube amelala katika kitanda cha hospitali moja ya umma (jina linahifadhiwa) ikiwa ni  saa chache  baada ya kufanyiwa upasuaji wa kujifungua.
Analia na kuugulia kwa uchungu, akilalamikia maumivu makali ya tumbo.
Kwa sababu hiyo, anamwita daktari akimweleza kuwa anahisi kuna kitu tumboni mwake na kinamuumiza mno,  lakini daktari anamjibu kuwa maumivu hayo yatatulia.
“Nisaidieni nitakufa kabla ya kumwona mtoto wangu, naumwa daktari, nakufa jamani,” anasema Mwanahamisi.
 Anapoendelea kuita, wakunga ndani ya wodi hiyo wanaibuka na kumjibu: “Acha kudeka, ulifikiri kuzaa ni kama kucheza kamari. Nyamaza, unawapigia kelele wenzako.”
Anaendelea kuita kwa zaidi ya saa lakini bila msaada wowote na baada ya kulia kwa muda mrefu, anatupa miguu huku na kule…ananyamaza, kisha anatulia. Kumbe… Mwanahamisi amekata roho!
 Mwanahamisi ni miongoni mwa wanawake wengi nchini ambao hukumbana na vifo vya kuepukika wakati wa kujifungua au muda mfupi baadaye.
Vifo hivyo, vingi vinasababishwa na uzembe wa madaktari, huduma dhaifu, ukosefu wa vifaa na sababu nyingine zinazozuilika wakati wa kujifungua.
 Pamoja na uchungu wa kujifungua anaoupata mwanamke, ukosefu wa vifaa tiba, maumivu mengine huyapata toka kwa baadhi ya  wahudumu wa afya.
 Hali hiyo imesababisha baadhi ya wanawake, hasa wale wanaojiweza kukimbilia katika hospitali binafsi ambapo wanapata huduma bora zaidi.
Hata hivyo, ni wanawake wachache nchini wenye uwezo huo na zaidi ya asilimia 80 wanategemea hospitali za Serikali ambazo  baadhi, ndizo zenye changamoto.
Katika mdahalo wa afya ya uzazi uliondaliwa na Dk Tausi Kida na Riziki Pansiano, wadau walikiri kuwa kuna matatizo mengi yaliyowakumba wanawake wakati wa kujifungua, kubwa likiwa rushwa na matusi.
Kwa mfano, wadau walieleza kuwa watoa huduma wengi, yaani wauguziwamelalamikiwa kuwa wanadai hongo ili waweze kutoa huduma kwa wagonjwa.
 Hii ni sababu mojawapo muhimu inayowafanya kinamama wasijifungue chini ya uangalizi wa wataalamu wa tiba kwenye vituo vyetu vya afya na hivyo kuwa kwenye hatari zaidi ya kupata matatizo wakati wanapojifungulia nyumbani.
“Niliwahi kushuhudia mama mjamzito kuachwa mapokezi mpaka kafariki bila hata kuhudumiwa. Ndugu wa dada huyu waliambiwa kuwa bila ya elfu 75 mgonjwa wenu hapati huduma kwa daktari. 
Kinamama hawa wakiendelea kuchangishana mmoja hadi mwingine wakifuata fedha hadi huko Morogoro, mwishowe baada ya saa karibu nane baada ya pesa kutopatikana mwenzetu akafariki.”
Wachangiaji pia walihusisha matatizo ya vifo na matusi na maneno ya kukatisha tamaa wanayoyatoa manesi kwa wajawazito.
 “Mama akiomba msaada utasikia mfuate huyo aliyekupatia mimba”. Alisema mchangiaji mmoja.
Maneno mengine yanayowatoka wauguzi ni kama vile usitusumbue hatupo kwa ajili yako hapa, mara unataka nijigawe ili nimhudumie huyu na wewe.
“Nimepata kumsikia nesi akisema kuwa huyu mwanamke asije akatulaza macho, anasema Dk. Salatiel Moyo, mchangiaji katika mjadala huo.
Takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa vifo vya uzazi Tanzania  ni 578 kati ya vifo 100,000 ambayo ni sawa na asilimia 18 ya vifo vyote vya wanawake wa kati ya miaka 15 hadi 49.
Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO), zinaeleza kuwa, asilimia 46 tu ya wanawake ndiyo husaidiwa na mtaalamu wa afya wakati wa kujifungua.
Faraja Mujuni, alimpoteza mtoto wake na kujikuta akiondolewa kizazi baada ya kupata uchungu pingamizi kwa muda mrefu.
“Kila nilipomwambia mkunga kuwa mtoto anatoka alikataa, kila nililomweleza alikuwa akiniangalia na kunifyonza, mwishowe, mtoto alifariki na mimi kuondolewa kizazi, kwani kilipasuka,” anasema Faraja.
Mwanamke mwingine, Anastazia Simwanza, mkazi wa Vingunguti jijini Dar es Salaam anasema alipofikishwa katika wodi ya wazazi, alikuta vitanda vimejaa, hivyo akaambiwa alale chini.
“Ilikuwa saa tisa usiku. Wakati huo uchungu ulikuwa ukiniuma kwa kasi, nikamwita nesi, lakini akaniambia bado kabisa mtoto hajashuka,”anasema Simwanza.
Simwanza anaeleza kuwa, baada  ya dakika kadhaa, chupa ilipasuka na mtoto akaanz saa kutoka, jambo lililosababisha ajifungue mwenyewe, bila msaada wa muuguzi na mtoto aliangukia chini sakafuni.
“Mwanangu alipata matatizo kwa sababu aliangukia sakafuni ndiyo maana hajatembea mpaka sasa wakati ana miaka sita,” anasema.
Paschal Msechu anaeleza jinsi yeye na mkewe mjamzito walivyotukanwana na wauguzi wakati mke wake alipokuwa akiugulia maumivu ya uchungu wa kujifungua.
“Kila nikijaribu kuwaeleza waliniambia niwaache wao wanajua kazi yao, walianza kumtukana mke wangu kwa sababu alikuwa hawezi kutembea, wakamrushia maneno mazito,” anasema Msechu.
 Si huyo tu, Yohana  Mwanga, anaeleza jinsi mke wake mpenzi alivyopoteza maisha kwa sababu  tu ya kukosa vifaa.
“Hatukuwa tumebeba vifaa vyote, wakati muuguzi ananiambia hayo, mke wangu alikuwa katika hali mbaya mno. Wakati natafuta hela za kununua, mke wangu alifariki kwa kukosa huduma.” Anasema Mwanga
 Mwanga, kwa masikitiko anasema: “Nimempoteza mke wangu kwa kukosa fedha tu, wala si kingine.”
Idadi kubwa ya vifo vya uzazi katika baadhi ya maeneo duniani inaonyesha ni kutokana na kukosekana kwa usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, na inaonyesha pengo kati ya matajiri na maskini.
Karibu wote, vifo vya uzazi (asilimia 99 hutokea katika nchi zinazoendelea.
 Mhadhiri wa Chuo cha Wakunga katika Chuo Kikuu cha Sayansi ya  Tiba Muhimbili, Dk Sebalda Leshabari, anasema wakunga wenye tabia zinazolalamikiwa na wanawake wanafanya makosa kwani hawakufundishwa hivyo vyuoni mwao.
Hakuna mkunga anayefundishwa kuwa jeuri au kutukana, sisi tunawafundisha mawasiliano mazuri na mama mjamzito na ujuzi mwingine,’ anasema Dk Leshabari.
Anasema hata Chama cha Wakunga Tanzania (TMA) wakati wa makongamano hutoa elimu na kuwakumbusha wakunga kuhusu huduma nzuri kwa wajawazito.
“Hizo  shutuma  tunazisikia zote na tunawapa mifano wanafunzi wetu wasirudie  tabia hizo,” anasema
 Dk Leshabari pia anatoa angalizo zaidi na kusema mpaka sasa ni asilimia 61 tu ya wanawake Tanzania wanaojifungulia hospitali, je, wengine wanajifungulia wapi?  

Janjaweed wadaiwa kuhusika mauaji ya askari wa Tanzania

. Wakati miili ya wanajeshi saba wa Tanzania waliouawa nchini Sudan ikiwasili leo, taarifa zinadai kundi la Janjaweed ambalo linaungwa mkono na Serikali, linahusika katika mauaji hayo.
Wanajeshi hao wa Tanzania ambao ni sehemu ya Jeshi la Kulinda Amani la Umoja wa Mataifa (Unamid), waliuawa Julai 13 eneo la Kusini mwa Darfur.
Askari wengine 17 walijeruhiwa katika shambulio hilo na wanaendelea kupatiwa matibabu kwenye hospitali maalumu.
Taarifa za UN, zilieleza juzi kwamba ingawa kundi hilo halijatambuliwa rasmi, mashuhuda wamekuwa wakieleza mauaji hayo yamefanywa na kundi linaloungwa mkono na Serikali ya Sudan.
Kiongozi wa moja ya makundi ya wapiganaji la Sudan Liberation Movement (SLM), Minni Minnawi, ndiye aliyeibuka awali na kuwatuhumu mgambo wanaoungwa mkono na Serikali na kutaka ufanyike uchunguzi wa kimataifa.
Katika mahojiano yake na gazeti la Sudan Tribune alipokuwa akihudhuria mkutano wa majadiliano kuhusu namna ya kupata amani ya kudumu nchini Sudan uliofanyika mjini Geneva, Uswisi, Minnawi alikanusha tuhuma kwamba kundi lake linahusika na shambulio hilo.
Kiongozi huyo alikuwa akijibu tuhuma za Serikali ya Sudan kwamba, kundi lake ndilo lililohusika na shambulio hilo.
“Tuna uhakika shambulio lililofanywa dhidi ya walinzi wa amani wa Unamid liliandaliwa na kutekelezwa na Janjaweed, tuko tayari kutoa ushirikiano kwa chombo maalumu cha kimataifa kitakachoundwa kufanya uchunguzi kuhusu tukio hili,” alisema.
Alisema wanamgambo wa Janjaweed hivi sasa wanakabiliwa na ukata wa hali ya juu na ukosefu wa vifaa, kwa sababu Serikali haina tena uwezo wa kuwafadhili hivyo wameamua kufanya matukio ya uporaji kukidhi mahitaji yao.
Wanajeshi saba waliuawa kwenye shambulio lililotokea Julai 13 huko Khor Abeche, Nyala nchini Sudan wakati walinda amani.
Wakati huohuo, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limesema miili ya wanajeshi hao itawasili leo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, (Terminal one) saa 9:00 alasiri.
“Baada ya kuwasili miili hiyo itapelekwa Hospitali ya Kuu ya Jeshi, Lugalo. Baada ya maandalizi, miili hiyo itaagwa rasmi kwa heshima zote Jumatatu kuanzia saa 3:00 asubuhi viwanja vya Wizara ya Ulinzi, Upanga, Dar es Salaam,” inasema sehemu ya taarifa hiyo.

Katika hatua nyingine, Msemaji wa Katibu Mkuu wa UN, Martin Nesirky, alisema walinda amani hao waliwekewa mtego wakiwa katika majukumu yao ya msingi ya kulinda amani. Alisema UN imeanza kufanya uchunguzi wake binafsi na kuitaka Serikali ya Sudan kuwasaka wahusika ili wawajibishwe.

Sunday, 30 June 2013

Wengi wamtakia Mandela afya njema

Mamia ya watu wanaendelea kukusanyika nje ya hospitali alikolazwa Nelson Mandela mjini Pretoria Afrika Kusini. Inaarifiwa Mandela bado yuko hali mahututi.Wamekuwa wakimuimbia nyimbo na kumuombea nje ya hospitali. Wengine wamekusanyika katika iliyokuwa makaazi ya Mandela mtaani Soweto.
Watu wana wasiwasi kuhusu hali y mandela lakini pia wanataka kuonyesha wanavyojivunia kiongozi wao ambaye wanamuona kama baba wa taifa lao.
Mandela , rais wa kwanza mweusi Afrika Kusini, anaugua maradhi ya Mapafu.
Mamia ya wananchi walikesha kwa maombi maombi nje ya makaazi ya zamani ya aliyekuwa rais wa taifa hilo Nelson mtaani Soweto.
Rais Jacob Zuma amesema kuwa afya ya shujaa huyo aliyepigana dhidi ya ubaguzi wa rangi nchini humo inaendelea kuimarika.
Mandela aliye na umri wa miaka 94 amekuwa hospitalini akiuguwa ugonjwa wa maambukizi ya mapafu.
Awali mwanawe wa kike, Makaziwe alisema afya ya babake inaendelea kuwa njema.
Aidha Makaziwe amevikashifu vyombo vya habari kwa kukita kambi nje ya hospitali alikolazwa shujaa huyo akisema wanahabari wanapaswa kumheshimu babaake.
Rais Jacob Zuma alisema Alhamisi kuwa hali ya Mandela iliimarika lakini bado yuko hali mahututi.
"leo angalau yuko sawa kidogo kuliko nilivyomwacha jana usiku,'' alisema Rais Zuma baada ya kuongea na madakatari wanaomtibu Mandela.
Bwana Zuma alifutilia mbali safari yake ya Msumbiji ili kumtembelea Mandela hospitalini.
Wakati huohuo mwanawe Mandela Makaziwe alisema Mzee 'bado yupo' na kuwa anaweza kuhisi mtu akimgusa.

Akiondoka Rais Obama, karibu Malkia Elizabeth

Watu hao wanaondolewa maeneo yao huku ikielezwa kuwa zoezi hilo ni endelevu, viongozi wa Manispaa za jiji hilo nao wamekuwa wakitoa elimu juu ya usafi kwa wafanyabiashara wa hoteli pia.
  Acha hilo, katikati ya wiki hii nyakati za jioni lilikatiza gari katikati ya jiji hilo likipuliza dawa ya kuua mbu na kuwafanya watu waliokuwa wamesimama kando ya barabara wakisubiri usafiri kukohoa hovyo, kupiga chafya na kutafuta sehemu ya kujificha kukwepa adha hiyo.
  Hayo yote yanafanyika ili Rais Barack Obama wa Marekani atakapowasili nchini na msafara wake alione Jiji la Dar es Salaam likiwa safi na kila njia inafanywa kuhakikisha jiji hilo linakluwa safi. Duh, usafi kwa ajili ya ujio wa wageni tu? Aibu gani hii.   Natambua wazi kwamba ugeni mkubwa wa viongozi wa zaidi ya nchi 14 umekuja nchini kwa mkutano wa Majadaliano ya Kiuchumi, pamoja na ziara ya Rais Obama wa Marekani ni heshima kubwa kwa taifa letu.    Pia, natambua kwamba ugeni huu utakuwa na manufaa kwa wafanyabiashara wetu wa hoteli, migahawa, huduma za usafiri na hata wafanyabiashara ndogondogo kwani watapata fursa ya kuingiza kipato.
  Sina tatizo na ujio wa viongozi hao, lakini kinachonishangaza ni kuanza kwa  operesheni ya usafi uliyoshindikana miaka nenda rudi kwa sababu tu ya ujio wa viongozi hao, huku watendaji wakidai ni zoezi endelevu.   Nchi yetu inawajali wageni kuliko wenyeji, ipo tayari kuhakikisha wageni hawang’atwi na mbu, hawasumbuliwi na wafanyabiashara na ombamba waliotapakaa maeneo ya mjini wala kusikia harufu chafu ya takataka zilizotelekezwa katika maroli, aibu gani hii!
  Kila kukicha tumekuwa tukishuhudia takataka zikitapakaa maeneo mbalimbali ya jiji na karibu kila kona kuna chupa za maji yaliyotumika, mifuko ya plastiki na taka nyinginezo.
  Kama hiyo haitoshi, kuna matela yaliyojaa takataka, yametelekezwa katika sehemu mbalimbali za masoko au maeneo ya makazi ya watu.    Mifereji ya kupitisha majitaka, mingi imeziba, jambo ambalo husababisha maji yanayotokana na mvua kusambaza uchafu, unaobebwa kwenye maeneo ya makazi au barabarani.
  Taka hizi husambaa na kuziba njia za waenda kwa miguu, hivyo kuwapa watumiaji hao wa barabara ugumu wakati wanapotembea.
  Katika mitaa mbalimbali kuna madimbwi yaliyosahauliwa na mamlaka husika, madimbwi ambayo yanawasitiri mbu na kuwa mahala pao kuzaliana na kueneza magonjwa ikiwamo Malaria.
  Kwa miaka nenda rudi Jiji la Dar es Salaam, ambalo ndilo kioo cha taifa letu, limekuwa likiongoza kwa kuupalilia ugonjwa wa kipindupindu, ambao chanzo chake kikuu ni uchafu. Karibu kila mwaka uongozi wa Hospitali za Jiji hilo hupokea wagonjwa wa Kipindupindu.
  Operesheni hii ya usafi inayofanyika sasa ilitakiwa kuanza miaka mingi iliyopita, siyo tu katika usafi wa mazingira bali ingekwenda hadi katika kusimamia miundombinu na ujenzi holela wa makazi usiozingatia mipango miji kwani ujenzi huo husababisha uchafu kutokana na kukosekana kwa miundombinu ya maji taka.
  Takataka kila mahali, harufu za vinyesi, maji taka, magari mabovu, biashara kila kona hadi makaburini. Mitaro imefurika , chupa za mikojo na mifuko ya plastiki imezagaa hadi barabarani mingine ikiwa na kinyesi, hiyo ndiyo Dar es Salaam.
  Lakini hivi sasa, ujio wa wageni hawa umewaamsha wahusika, wanafanya usafi kila kona kuhakikisha kuwa mambo yanakwenda sawa na siyo ajabu kuona kila kitu kimelala baada ya viongozi hao kuondoka.
  Usafi katika Jiji la Dar es Salaam unahitaji utafiti wa kina na njia za kitaalamu zaidi katika kuhakikisha masuala ya usafi na mazingira yanafanikiwa.
Nasema hivi kwa sababu mipango na miundo mbinu ya miji huo ni ya zamani tangu enzi ya mkoloni ambapo idadi ya wakazi likuwa ndogo ukilinganishwa na sasa. Natambua kuwa jukumu la usafi ni la watu wote, ila kwa upande wa Serikali inatakiwa kuja na mikakati mipya na endelevu itakayolitoa jiji hili katika hali ya uchafu kwa kutumia fedha zitokanazo na ukusanyaji wa mapato kutoka katika vyanzo mbalimbali na  siyo kusubiri ujio wa viongozi.
Wafanyabiashara kupanga bidhaa, barabarani na mbele ya majengo ya Ofizi za Serikali, kushamiri kwa gereji bubu mitaani, kumbi za burudani zinazopiga muziki usiku kucha, ni moja ya kero zilizowashinda watendaji wa mamlaka husika.
Mamlaka husika zimeshindwa hata kudhibiti mfumuko wa vilabu vya pombe, kiasi kwamba hata shule za msingi na sekondari za jijini Dar es Salaam zimezungukwa na Baa na nyumba za kulala wageni.
Karibu Rais Obama kwani ujio wako umewakumbusha wahusika kulifanyia usafi Jiji la Dar es Salaam ikiwa ni baada ya muda mrefu kupita tangu wafanye hivyo, pengine watakumbuka tena kufanya usafi siku atakayokuja Malkia Elizabeth wa Uingereza.
 

 

 

SPORTS: FAINALI CONFEDERATIONS CUP BRAZIL VS SPAIN LEO USIKU

Mtanange wa kombe la mabara(Confederation cup) unaoendelea huko nchini Brazil leo utafikia tamati ambapo ni fainali kati ya Brazil na Spain . Kwa Brazil hii ni furaha kwao kuingia fainali kwani wana historia nzuri ya fainali kwenye mtanange huo na mara tano za mwisho kuingia fainali hawajapoteza mchezo. Kwa Spain hii ni changamoto kubwa hasa baada ya kupita kwa mikwaju ya penati na hali ya Brazil kutumia faida ya kuwa nyumbani . Hata hivyo kocha wa Brazil (Scolari) amesema amejiandaa vyema na mchezo huo, atawatumia wachezaji wake wazuri kupambana na Spain na dakika 90 zitaamua mshindi kati yao. Timu hizo mbili mara ya mwisho kucheza ni miaka 14 iliyopita ambapo walitoa suluhu ya 0 - 0.
Mtanange huo utapigwa usiku wa leo (Saa Sita Kamili Usiku- Saa za Afrika Mashariki)
Wakati vigogo hao wawili wakipambana kwenye fainali hiyo, Uruguay na Italy watakuwa wanashindania mshindi wa tatu.

Vijana msikubali kununuliwa-Sumaye

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye amewatahadharisha vijana kuwa wanaelekea kwenye uchaguzi mkuu wasikubali kupewa rushwa ya kanga, fulana na fedha na mtu yeyote anayetaka kuingia madarakani.
Akizungumza jana alipokuwa kwenye bonanza la michezo la kikundi cha Ukwamani Jogging kilichopo Kawe, alisema vijana wawe makini katika kuchagua mtu mwenye uwezo wa kuongoza ambaye atajali masilahi ya wananchi wake siyo kwa masilahi yake binafsi.
“Najiuliza kama ninajiamini nataka kugombea Kawe au Arusha au Sumbawanga kama ninafaa na wananchi wananiamini mimi ninafaa na wananchi wananihitaji kwa nini niwachochee kwa kanga au fedha ukiona hivyo huyo hawafai kuwaongoza,” alisema na kuongeza:
“Ukiona mtu anatoa kitu ili achaguliwe hafai kuwa kiongozi kwani uongozi ni mzigo,” alisema Sumaye.
Aliwashangaa watu wazima wanaochukua fedha na kuweka mfukoni kisha wanapita mitaani huku wakisema fulani anafaa kwa kuwa anatoa rushwa na fulani hafai kwa kuwa hatoi kitu chochote.
Sumaye alisema anayetoa fedha ili apewe kura huyo hafai kuwa kiongozi kwa sababu atakuwa anawatumikia watu wake waliompa fedha sio mwananchi ambaye alijitolea kumchagua kiongozi hiyo kwa kumpigia kula halali ili aweze kusaidia kumtatulia kero mbalimbali zinazomkabili.
Alisema kama kuna watu wanaumizwa kwa kuambiwa wanapokea au kutoa rushwa huku akiwa anaendelea na kufanya hivyo aache ili asiendelee kuumizwa na hilo.
Sumaye alisema nchi haiwezi kuwa na maendeleo kama viongozi wataendelea kudidimiza nchi kwa rushwa,ufisadi na kuingiza dawa za kulevya nchini.
Alisema viongozi wanaoleta dawa za kulevya kama ni nzuri wangezitumia lakini hawazitumii matokeo yake wanaoathirika ni vijana ambao wanategemewa kulijenga taifa hili.
“Hatuwezi kudidimiza jamii kwa kuwaletea dawa za kulevya ili watoto wa wenzao waharibikiwe kwa nini wasiwape au kutumia hao viongozi ili waathirike wao wenyewe?” alisema Sumaye.

Wamachinga: Ujio wa Rais Obama umetuletea njaa

Dar es Salaam. Wafanyabiashara waliokuwa wakifanya biashara katikati ya jiji na kuondolewa kutokana na ujio wa Rais wa Marekani, Barack Obama, wamelalamika kuwa sasa wanakabiliwa na maisha magumu.
Obama anatarajia kuwasili nchini kesho katika ziara ya kikazi ya siku mbili huku akiambatana na ujumbe wa watu wapatao 700.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Mwananchi Jumapili, wafanyabishara hao walisema kuondolewa huko kumewafanya kukosa kipato walichokuwa wakikipata hivyo kusababisha ugumu wa maisha.
Frank Mkama alilalamika: “Hapa Serikali isiseme kuwa wanafanya usafi wa jiji kwa kuwaondoa wafanyabiashara hii si kweli! Mbona hawakufanya zamani, hapa ni Obama ndiyo amesababisha sisi tukaondolewa.”
“Hivi sasa maisha yangu yamekuwa magumu. Kipato ambacho nilikuwa nakipata hapa na kula na familia yangu sasa sikipati.”
Naye, Elizabeth Makata alilalamika Serikali ilipaswa kuwaandaa wananchi kwa kuwaeleza ujio huo wa Obama watanufaika vipi na si kuwafanya waathirike kwa kuvunjiwa maeneo yao.
Alielezea wasiwasi kuwa huenda baada ya ziara hiyo wakashindwa kuendelea na biashara kwa kuwa watakuwa wamekula mitaji.
Kwa upande wake, Ramadhan Issa alisema ziara hiyo ya Rais Obama imeathri maisha yake kutokana na kuvunjiwa kibanda alichokuwa akifanyia biashara hivyo hajui hatima ya maisha yake.
Kadhalika Mwananchi Jumapili iliwashuhudia askari polisi wakionekana kuongezeka katikati ya jiji wakipita huko na kule kuhakikisha hali ya usalama inaimarika.
Pia hali ya usafi imeendelea kuimarika kutokana na ujio kutokana na juhudi zinazoendelea kufanywa kwa lengo la kusafisha mazingira.
Licha kwamba wafanyabiashara hao wameondolewa hivi karibuni baadhi yao wameanza kurejea kuendelea na shughuli zao kama kawaida.