Monday, 29 July 2013

Bajeti finyu kikwazo cha kupata haki mahakamani-Jaji mkuu Tz



Dar es Salaam. Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohammed Chande Othman, amesema ni vigumu mahakama kama taasisi ikaweza kutoa haki kwa wakati kama haitaweza kujitosheleza kimapato.
Aliyasema hayo jana Dar es Salaam alipokuwa akizindua kitabu kilichoandikwa na Jaji Mkuu Mstaafu, Barnabas Samatta kiitwacho ‘Uhuru wa Mahakama’ na kuchapishwa na Kampuni ya Mkuki na Nyota.
“Uhuru wa kitaasisi ambao haujakamilika ni ule wa kifedha na kimiundombinu, bila huu kukamilika ni vigumu kila mwananchi kuweza kupata haki kwa wakati,” alisema Jaji Chande.
Alisema licha ya kuwa Serikali imekuwa ikijitahidi kuongeza bajeti ya mahakama, bado lengo halijafikiwa na kuwa ni vyema muhimili huo ukatengewa fedha za kutosheleza kuendesha shughuli zake.
Jaji Chande alisema kuwa, katika bajeti ya mwaka 2013/14 muhimili huo umetengewa Sh160 bilioni ingawa mahitaji yake halisi ni Sh300 bilioni.
Alisema pia kuwa,kitabu hicho kitawasaidia viongozi wengi ambao wamekuwa wakidhani kuwa mahakama ni chombo cha Serikali. “Wakisoma kitabu hiki wataelewa na wataachana na dhana hii,” alisema Jaji Chande.
Akizungumzia maudhui yaliyopo kwenye kitabu hicho kilichoandikwa kwa lugha ya Kiswahili, Jaji Chande alisema kuwa kimelenga kumsaidia mwananchi wa kawaida kuijua mahakama na pia watawala, vyama vya siasa na wanasheria watapata mwongozo makini.
Kwa upande wake Jaji Samatta alisema kuwa, mwanzoni kabisa wazo lake lilikuwa ni kuandika juu ya kesi ambazo zimewahi kutikisa nchini kwa upande wa Tanzania bara na Zanzibar.
Alisema, alikuja kuachana na wazo hilo baada ya kuona hapati baadhi ya vielelezo ambavyo vingemwezesha kuandika kitabu hicho.

No comments: