Sunday, 30 June 2013

Akiondoka Rais Obama, karibu Malkia Elizabeth

Watu hao wanaondolewa maeneo yao huku ikielezwa kuwa zoezi hilo ni endelevu, viongozi wa Manispaa za jiji hilo nao wamekuwa wakitoa elimu juu ya usafi kwa wafanyabiashara wa hoteli pia.
  Acha hilo, katikati ya wiki hii nyakati za jioni lilikatiza gari katikati ya jiji hilo likipuliza dawa ya kuua mbu na kuwafanya watu waliokuwa wamesimama kando ya barabara wakisubiri usafiri kukohoa hovyo, kupiga chafya na kutafuta sehemu ya kujificha kukwepa adha hiyo.
  Hayo yote yanafanyika ili Rais Barack Obama wa Marekani atakapowasili nchini na msafara wake alione Jiji la Dar es Salaam likiwa safi na kila njia inafanywa kuhakikisha jiji hilo linakluwa safi. Duh, usafi kwa ajili ya ujio wa wageni tu? Aibu gani hii.   Natambua wazi kwamba ugeni mkubwa wa viongozi wa zaidi ya nchi 14 umekuja nchini kwa mkutano wa Majadaliano ya Kiuchumi, pamoja na ziara ya Rais Obama wa Marekani ni heshima kubwa kwa taifa letu.    Pia, natambua kwamba ugeni huu utakuwa na manufaa kwa wafanyabiashara wetu wa hoteli, migahawa, huduma za usafiri na hata wafanyabiashara ndogondogo kwani watapata fursa ya kuingiza kipato.
  Sina tatizo na ujio wa viongozi hao, lakini kinachonishangaza ni kuanza kwa  operesheni ya usafi uliyoshindikana miaka nenda rudi kwa sababu tu ya ujio wa viongozi hao, huku watendaji wakidai ni zoezi endelevu.   Nchi yetu inawajali wageni kuliko wenyeji, ipo tayari kuhakikisha wageni hawang’atwi na mbu, hawasumbuliwi na wafanyabiashara na ombamba waliotapakaa maeneo ya mjini wala kusikia harufu chafu ya takataka zilizotelekezwa katika maroli, aibu gani hii!
  Kila kukicha tumekuwa tukishuhudia takataka zikitapakaa maeneo mbalimbali ya jiji na karibu kila kona kuna chupa za maji yaliyotumika, mifuko ya plastiki na taka nyinginezo.
  Kama hiyo haitoshi, kuna matela yaliyojaa takataka, yametelekezwa katika sehemu mbalimbali za masoko au maeneo ya makazi ya watu.    Mifereji ya kupitisha majitaka, mingi imeziba, jambo ambalo husababisha maji yanayotokana na mvua kusambaza uchafu, unaobebwa kwenye maeneo ya makazi au barabarani.
  Taka hizi husambaa na kuziba njia za waenda kwa miguu, hivyo kuwapa watumiaji hao wa barabara ugumu wakati wanapotembea.
  Katika mitaa mbalimbali kuna madimbwi yaliyosahauliwa na mamlaka husika, madimbwi ambayo yanawasitiri mbu na kuwa mahala pao kuzaliana na kueneza magonjwa ikiwamo Malaria.
  Kwa miaka nenda rudi Jiji la Dar es Salaam, ambalo ndilo kioo cha taifa letu, limekuwa likiongoza kwa kuupalilia ugonjwa wa kipindupindu, ambao chanzo chake kikuu ni uchafu. Karibu kila mwaka uongozi wa Hospitali za Jiji hilo hupokea wagonjwa wa Kipindupindu.
  Operesheni hii ya usafi inayofanyika sasa ilitakiwa kuanza miaka mingi iliyopita, siyo tu katika usafi wa mazingira bali ingekwenda hadi katika kusimamia miundombinu na ujenzi holela wa makazi usiozingatia mipango miji kwani ujenzi huo husababisha uchafu kutokana na kukosekana kwa miundombinu ya maji taka.
  Takataka kila mahali, harufu za vinyesi, maji taka, magari mabovu, biashara kila kona hadi makaburini. Mitaro imefurika , chupa za mikojo na mifuko ya plastiki imezagaa hadi barabarani mingine ikiwa na kinyesi, hiyo ndiyo Dar es Salaam.
  Lakini hivi sasa, ujio wa wageni hawa umewaamsha wahusika, wanafanya usafi kila kona kuhakikisha kuwa mambo yanakwenda sawa na siyo ajabu kuona kila kitu kimelala baada ya viongozi hao kuondoka.
  Usafi katika Jiji la Dar es Salaam unahitaji utafiti wa kina na njia za kitaalamu zaidi katika kuhakikisha masuala ya usafi na mazingira yanafanikiwa.
Nasema hivi kwa sababu mipango na miundo mbinu ya miji huo ni ya zamani tangu enzi ya mkoloni ambapo idadi ya wakazi likuwa ndogo ukilinganishwa na sasa. Natambua kuwa jukumu la usafi ni la watu wote, ila kwa upande wa Serikali inatakiwa kuja na mikakati mipya na endelevu itakayolitoa jiji hili katika hali ya uchafu kwa kutumia fedha zitokanazo na ukusanyaji wa mapato kutoka katika vyanzo mbalimbali na  siyo kusubiri ujio wa viongozi.
Wafanyabiashara kupanga bidhaa, barabarani na mbele ya majengo ya Ofizi za Serikali, kushamiri kwa gereji bubu mitaani, kumbi za burudani zinazopiga muziki usiku kucha, ni moja ya kero zilizowashinda watendaji wa mamlaka husika.
Mamlaka husika zimeshindwa hata kudhibiti mfumuko wa vilabu vya pombe, kiasi kwamba hata shule za msingi na sekondari za jijini Dar es Salaam zimezungukwa na Baa na nyumba za kulala wageni.
Karibu Rais Obama kwani ujio wako umewakumbusha wahusika kulifanyia usafi Jiji la Dar es Salaam ikiwa ni baada ya muda mrefu kupita tangu wafanye hivyo, pengine watakumbuka tena kufanya usafi siku atakayokuja Malkia Elizabeth wa Uingereza.
 

 

 

No comments: