Wednesday, 27 February 2013

Pinda: Hatukukosea kuunda tume *Asema lengo ni kubaini kiini cha tatizo


WAZIRI Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, amesema tume iliyoiunda ili kuchunguza matokeo ya kidato cha nne yaliyotangazwa Februari 18 mwaka huu, itaanza kazi siku mbili au tatu zijazo.


Bw. Pinda aliyasema hayo Dar es salaam jana wakati akijibu maswali ya waandishi wa habari waliotaka kujua ni lini
tume hiyo itaanza kazi na kuongeza kuwa, pamoja na watu
kuipinga, Serikali haikukosea kuiunda ili ifanye uchunguzi
wa kina kubaini kiini cha tatizo.

“Yanayosemwa ni mengi...wapo wanaosema tatizo linajulikana, jambo ambalo si kweli hivyo lazima tume ichunguze ili kujua mkweli na muongo,” alisema Bw. Pinda.

Aliongeza kuwa, tume hiyo pia itachunguza maeneo mengine
yenye utata mkubwa ili kuona jambo hilo halitokei tena.

Hivi karibuni, Bw. Pinda aliunda tume itakayochunguza sababu
ya matokeo mabaya kwa wanafunzi wengi waliofanya mtihani
wa kidato cha nne mwaka 2012.

Asilimia 60 ya wanafunzi waliofanya mtihani huo walipata sifuri ambapo tume hiyo itajumuisha Chama cha Wamiliki wa Shule na Vyuo Binafsi, Chama cha Walimu nchini (CWT), Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii na Umoja wa Wakuu wa Shule za Sekondari nchin

Waziri Muhongo akataa chakula hotelini aenda kwa mamalishe



Nipelekeni mahali nitakapopata chakula cha Kitanzania, ili tuwe sawa na Watanzania wenye hali ya chini kwani hizi fedha tunazokwenda kula huko ni jasho lao.”

Arusha
WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amekataa chakula Hoteli ya Mount Meru na kwenda kula chakula cha Mamalishe.
Tukio hilo lililowashangaza watu 13 waliokuwa katika msafara wake lilitokea hivi karibu wakati

Profesa Muhongo alipokwenda Arusha kwenye mkutano wa wataalamu wa umeme wa nchi 11 za Afrika Mashariki, Kati na Kaskazini.

Waziri Muhongo aliandaliwa chakula hotelini hapo, lakini aliwashangaza wenyeji wake ambao ni Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na uongozi wa wizara yake.

Baada ya kufika katika mgahawa wa Pizza Point uliopo katikati ya mji wa Arusha, Waziri Muhongo aliagiza ugali na samaki kwa bei ya Sh7,000.

Tukio la waziri huyo kukataa kula chakula cha usiku katika hoteli hiyo ya kifahari, iliwashangaza hata wafanyakazi wa mgahawa huo baada ya kupata taarifa hiyo.
Ingawa haikufahamika mara moja sababu za waziri huyo kukataa kula katika hoteli hiyo kutokana na kuchukua uamuzi ghafla, lakini taarifa za ndani zinadai hakutaka kutumia fedha za walipa kodi kwa matumizi binafsi.

“Waziri aliandaliwa chakula katika Hoteli ya Mount Meru Arusha na mpaka tunatoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia), ilijulikana tunakwenda kwenye hoteli hiyo lakini chakushangaza alipofika karibu na geti la kuingia hapo, akabadili uamuzi na kuamuru apelekwe mahali atakapopata chakula cha Kitanzania, huku akisema haoni sababu ya kula vyakula vya bei mbaya wakati kuna Watanzania hawana umeme,” alisema ofisa mmoja wa wizara hiyo ambaye hakutaka kutajwa na kumkariri Waziri Muhongo:

“Nipelekeni mahali nitakapopata chakula cha Kitanzania, ili tuwe sawa na Watanzania wenye hali ya chini kwani hizi fedha tunazokwenda kula huko ni jasho lao.”

Hata hivyo, Profesa Muhongo anadaiwa kuruhusu maofisa waliokuwa kwenye msafara wake ambao wangependa kula Mount Meru kuwashusha, ili akitoka kwa mamalishe awapitie kwa sababu kila mtu ana uamuzi wake.

Msafara wa waziri huyo ulikuwa na watu 13 akiwamo Msaidizi wake na Meneja Mawasiliano wa Tanesco, Badra Masoud ambao wote walilazimika kula chakula katika banda la Pizza Point.

Mmiliki wa mgahawa huo, Grace Lyatuu alisema hakutarajia ujio wa waziri huyo na msafara wake, lakini baada ya kutambua kuwa ni Profesa Muhongo akamshukuru Mungu kwa kumfikisha hapo.

“Kwakweli ilikuwa ni usiku mgumu kwangu, kwani msafara ulikuwa mkubwa na wagafla, sikuwa na uhakika wa kupata vyakula vya kuwatosha lakini baada ya chakula kupatikana nikamshukuru Mungu kwani ilikuwa ni usiku na tulikuwa na maandalizi ya kufunga mgahawa,” alisema Lyatuu.

Profesa Muhongo alitumia Sh100,000 kwa chakula cha watu 13 na vinywaji na kuokoa zaidi ya Sh344,500.

Vigogo 10 wahusishwa mabilioni ya Uswisi


ZITTO ASISITIZA NYARAKA ZIPO, DK HOSEAH NDIYE ANAYEZIZUIA

VIGOGO 10 wametajwa kuhusika katika kashfa ya kuficha Sh303.7 bilioni katika benki mbalimbali nchini Uswisi.
Katika orodha hiyo inadaiwa kuwa yupo kiongozi mmoja mwandamizi mstaafu, maofisa watatu wastaafu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), mawaziri wastaafu ambao baadhi yao bado ni wabunge na aliyewahi kuwa kiongozi mwandamizi wa Benki Kuu Tanzania (BoT).
Majina hayo ambayo mwandishi wetu amefanikiwa kuyaona, yamo katika orodha ya mchunguzi mmoja wa kimataifa wa masuala ya ufisadi (jina tunalo).
Juzi, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe alimshukia Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hoseah akimtuhumu kuandika barua Uswisi akisema Tanzania haina masilahi na mabilioni ya fedha yaliyofichwa katika benki zilizopo nchini humo. Hata hivyo, Dk Hoseah alikanusha madai hayo akisema hajawahi kufanya hivyo.
Akizungumza jana Zitto alisisitiza kauli yake akisema: “Sijawahi kumsema Dk Hoseah kwa lolote, kwa nini leo nimsingizie? Yeye mwenyewe anajua ushirikiano niliompa wakati wabunge wanapinga yeye asichunguze malipo ya posho mara mbili kwa wabunge.”
“Nilisimama kidete kusema Takukuru wapo sahihi na mimi nilikwenda mwenyewe kwao kuhojiwa na kuagiza wajumbe wa kamati yangu (Kamati ya Bunge ya Mashirika ya Umma), waende kuhojiwa. Spika aliyestaafu (Samuel Sitta) akaizima kashfa ya wabunge kupokea posho mara mbilimbili. Mwulizeni amesahau? Sasa leo nimzushie ili iwe nini?.”
Alisema orodha ya Watanzania wenye fedha huko Uswisi, ipo na ameiona na nyaraka zinaweza kutolewa kwa taasisi za Serikali tu.
“Dk Hoseah kazuia nyaraka hizo. Akitaka nimwonyeshe mtu anayeweza kutoa nyaraka hizo, nipo tayari isipokuwa aahidi kuiweka wazi,” alisema Zitto.
Alisema katika orodha ambayo Waziri wa Fedha wa Ufaransa anayo, kuna Watanzania lakini akaituhumu Serikali akisema haitaki kufuata njia halali za kupata orodha hiyo kwa kuwa viongozi wengi na wafanyabiashara wakubwa wana akaunti katika benki za Uswisi.
Juni 26, mwaka huu gazeti hili lilichapisha habari kuhusu utoroshwaji wa fedha hizo na kueleza kuwa Polisi wa Kimataifa (Interpol) nchini kwa kushirikiana na Takukuru inachunguza suala hilo.
Kiasi hicho cha fedha kimedaiwa kuingizwa katika akaunti za Watanzania na kampuni moja ya uchimbaji mafuta na kampuni kadhaa za uchimbaji madini ambazo zinafanya kazi Tanzania.
Chanzo hicho kiliongeza kwamba kiasi hicho cha fedha kipo katika akaunti sita tofauti zinazomilikiwa na Watanzania wakiwamo wanasiasa wakubwa.
Hata hivyo, chanzo hicho kilieleza kuwa tangu akaunti hizo zifunguliwe, wamiliki wake halali hawajawahi kuingiza hata shilingi.
“Uchunguzi wetu unaonyesha kuwa fedha hizo zipo katika akaunti sita tofauti ambazo zinamilikiwa na wanasiasa wakubwa nchini na wenzetu wa Uswisi wameeleza fedha hizo zimeingizwa na kampuni kadhaa ambazo zinahusika na mafuta pamoja na madini hapa nchini,” kilidokeza chanzo hicho.
Kugundulika kwa kiasi hicho cha fedha katika benki za Uswisi ni kutokana na ripoti ya Benki ya Taifa ya Uswisi (SNB) iliyotolewa mwaka huu.

Urais 2015: Utafiti wa Synovate wapondwa,wadau wadai una ajenda ya siri: Huko tuseme ni kuiogopa Cadema??




BAADHI ya wasomi nchini wameuponda utafiti uliofanywa na Shirika la Synovate huku miongoni mwao wakienda mbali zaidi kwa kusema: “Ulikuwa na ajenda ya siri.”


Utafiti huo pia umepondwa na wanasiasa akiwamo Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba ambaye amesema haziamini tafiti zinazotolewa na Syonovate akidai hazina ukweli wowote.


Licha ya matokeo ya utafiti huo wa Desemba mwaka jana kuonyesha kushuka kwa asilimia 25 kwa umaarufu wa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa pamoja na chama chake, lakini unaweka wazi kwamba kiongozi huyu angechaguliwa kuwa Rais kama uchaguzi huo ungefanyika sasa.


Dk Slaa anaongoza kwa asilimia 17, akifuatiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.


Katika maoni yao, baadhi ya wasomi kutoka taasisi mbalimbali za elimu ya juu nchini walieleza wasiwasi wao kuhusu usahihi wa matokeo hayo na kuhoji mbinu zilizotumika wakisema inawezekana hazikuwa sahihi.
Mhadhiri wa Sayansi ya Siasa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Alexander Makulilo ameuponda akisema haukufuata misingi ya sayansi ya siasa.


Dk Makulilo alisema alifanya utafiti kwa kampuni zinazofanya tafiti kama hizo kati ya mwaka 2010 hadi 2011 na kugundua udhaifu mkubwa katika kampuni hizo.


“Kwanza wanakosea, kwa mfano wanaposema kuwa utafiti huu ni mwendelezo wa ule uliofanyika Desemba 5 hadi 18, 2011. Ukichunguza utakuta data hizo hazipo. Zilizopo ni za Mei 2 hadi 19, 2011.”


“Kwa kawaida uelewa wa wananchi wa vijijini ni mdogo ukilinganisha na mijini kwa sababu mijini kuna vyombo vya habari. Kwa mfano, ukiangalia swali la nani anafaa kuwa Rais, mwaka 2011 walisema Dk Wilbrod Slaa alikuwa na asilimia 42, lakini sasa ana asilimia 17.


Vijijini wengi bado wanaikubali CCM kutokana na uelewa mdogo, iweje Dk Slaa ambaye chama chake hakina wafuasi wengi vijijini ashinde?” alihoji.


“Utafiti wa Synovate una dosari kubwa kisayansi, hauonyeshi tarehe wala wapi umefanyika. Waliohojiwa wameonyeshwa umri wao, lakini hawaelezwi maoni yao kulingana na umri, jinsia, wanatoka vijijini na mijini. Nilipofanya utafiti wangu niliwafuata wakakimbia…” alisema Dk Makulilo.


Mhadhiri mwingine wa UDSM, Profesa Gaudence Mpangala alisema nyakati za kuelekea Uchaguzi Mkuu, tafiti nyingi hufanyika zikiwa na malengo ya kubeba watu au chama fulani.


Hata hivyo, alisema kilichofanywa na Synovate ni utafiti hivyo kwa kuwa yeye hajafanya utafiti ni vigumu kuupinga moja kwa moja... “Ila kwa mtizamo wa kawaida unatia shaka.”

Alisema kitendo cha utafiti huo kuonyesha kuwa CCM inakubalika zaidi kuliko Chadema kwa sababu kwa siku za karibuni chama hicho kimekuwa kikizungumzia zaidi mambo ya kitaifa, pia kunampa shaka.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (Sua), Dk Clavery Tungaraza alisema tafiti zinazofanywa na Synovate ni mara nyingi matokeo yake huwa hayaakisi uhalisia wa maisha.


Dk Tungaraza alisema utafiti wa Sayansi ya Jamii ndiyo wenye kuaminika zaidi kutokana na kutobadilikabadilika tofauti na tafiti za Synovate ambazo hutegemea mtu aliyehojiwa yuko katika hali gani kwa wakati huo.


Msomi huyo alieleza kushangazwa na tafiti za taasisi hiyo ambazo alidai kuwa mara nyingi hufanywa wakati nchi inapojiandaa kuingia kwenye uchaguzi akisema ingekuwa ni uungwana kama zingekuwa zinafanywa kila mwaka ili kujiridhisha na uhalali wa matokeo yake.


Mhadhiri Msaidizi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (Saut), Baraka Nafari alisema ana shaka na utafiti huo na kudai kwamba inawezekana umefanywa kwa lengo la kumsafisha mtu fulani.


Alisema kwa kawaida matokeo ya utafiti uliofuata kanuni na taratibu zote, unatakiwa mwingine akiufanya mara 100, apate majibu kama yale ya utafiti wa awali mara 95.


“Hiyo inaitwa confidence level, (namna ya kujiaminisha, kuwa na imani na majibu). Kwa mfano, wanasema Watanzania hawaoni kuwa rushwa ni tatizo, wakati ukweli kwetu sisi rushwa ni janga, kuna shirika moja la kimataifa lilitaja nchi zenye rushwa Tanzania ikawa kwenye nafasi za juu sana,” alisema.


Kutokana na hali hiyo, alisema utafiti huo unaonekana kama chumba maalumu cha kuwasafisha baadhi ya watu na vyama vyao badala ya kusimamia kwenye ukweli... “Nautilia shaka kama uliandikwa kwa kuzingatia vigezo na siyo kwa lengo mahususi.”


Mhadhiri wa Chuo cha Mipango Dodoma, Dk Mark Msaki alisema kinachomtatiza ni kutoainishwa njia zilizotumika katika kufanya utafiti huo.


“Sikatai wala kukubali utafiti huu, lakini kwa kuwa ni jukumu la taasisi hizo kufanya tafiti nchini, zitekeleze hayo kwa kuzingatia haki kwa Watanzania wote na si vinginevyo,” alisema.


Dk Msaki pia alisema haridhishwi na taasisi za kisayansi kujikita katika kutafiti nani ana nafasi gani katika kupata urais wa Tanzania, huku nchi ikikabiliwa na changamoto nyingi zinazogusa moja kwa moja maendeleo ya jamii.


Alisema anaamini kuwa kitendo cha taasisi hizo kuibuka na tafiti zinazohusu urais, huku Uchaguzi Mkuu ukiwa bado takriban miaka miwili, ni ishara taasisi hizo kuhusika moja kwa moja katika kugeuza siasa ya Tanzania mchezo wa mpira wa miguu.

Wanasiasa wang’aka
Profesa Lipumba alisema: “Kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2010, Synovate walitoa utafiti ulioonyesha kwamba asilimia 94 ya Watanzania wako tayari kupiga kura lakini baadaye Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ilitoa takwimu zake zilizoonyesha kuwa waliopiga kura walikuwa asilimia 42 tu.”


“Inawezekana hata hao waliotoa utafiti huo wakawa wanamtengenezea mtu fulani njia tu kwa mtindo wa kumpigia debe, binafsi siwaamini hasa baada ya makosa yale ya mwaka 2010.”
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema matokeo ya utafiti huo yanaacha maswali kwani hakuna maelezo yaliyotolewa kuhusu methodolojia na sampuli iliyotumika.
Alisema matokeo ya utafiti huo yanakinzana na ripoti nyingine za mwaka wa 2012 hasa ule wa Economic Intelligence Unit ambao unaonyesha kuwa Chadema kinazidi kupanda.


Katibu Mkuu wa NCCR Mageuzi, Sam Ruhuza alisema kati ya vinara tisa wa urais waliotajwa, hakuna hata mmoja anayeweza kuwa Rais wa Tanzania na kuongeza kuwa ushahidi wa hilo ni huko kupanda na kushuka kwa umaarufu wao kisiasa.


“Huko kushuka na kupanda, ni ishara kuwa hakuna Rais kati ya hao, haiwezekani mtu anayependwa na kuungwa mkono aporomoke kutoka asilimia 42 mpaka 17 na huu ni mwaka mmoja tu. Ikipita miaka miwili si wengine watabaki na asilimia moja au sifuri?”



RAILA ODINGA AMBWAGA UHURU KINYATTA KURA ZA MAONI

tr" style="text-align: left;" trbidi="on">

Matokeo ya utafiti wa Consumer Insight yanaonyesha kuwa Odinga hivi sasa anaungwa mkono na asilimia 46.8 ya wapigakura dhidi ya mwenzake, Kenyatta aliyepata asilimia 42.9. Mashabiki wa Mudavadi wamepungua kutoka asilimia 5.4 hadi 4.2.

WAGOMBEA urais wanaochuana vikali Kenya, Raila Odinga wa Muungano wa Cord na Uhuru Kenyatta wa Jubilee, wameendelea kukabana koo ikiwa ni siku tano kabla ya Uchaguzi Mkuu Jumatatu ijayo.

Tafiti tatu tofauti zilizodhaminiwa na Nation Media Group (NMG), ambazo matokeo yake yametoka jana, zimeonyesha kuwa wagombea hao wanatofautiana kwa asilimia zisizozidi 1.5, hali inayoonyesha kuwa lolote linaweza kutokea siku ya uchaguzi. Hata hivyo, Odinga ana nafasi zaidi katika uchaguzi wa marudio.

Matokeo yote hayo yamebainisha kuwa hakutakuwa na mshindi wa moja kwa moja, kwa kuwa wote hawatafikisha nusu ya kura zinazohitajika, huku utafiti ukibainisha kuwa katika mzunguko wa pili utakaofanyika ndani ya wiki tatu tangu kufanyika kwa uchaguzi wa awali, Odinga ana nafasi kubwa ya kushinda.

Matokeo ya Pollster Infotrack
Utafiti wa Kampuni ya Pollster Infotrack, unaonyesha kuwa kama uchaguzi ungefanyika leo, Odinga angeongoza kwa asilimia 46, Kenyatta angefuatia akiwa na asilimia 44.6, huku mgombea wa Amani, Musalia Mudavadi akiwafuata kwa mbali baada ya kupata asilimia 4.3.

Kwa mujibu wa matokeo hayo ya kura za mwisho za maoni, wote wawili, Odinga na Kenyatta wameongeza kura kwa asilimia moja kila mmoja, ikilinganishwa na matokeo ya wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa sheria za Kenya, si ruhusa kufanya wala kuchapisha kura za maoni siku tano kabla ya uchaguzi.

Kulingana na matokeo ya Infotrack Poll, Odinga anatazamiwa kushinda matokeo ya mzunguko wa pili kwa asilimia 49.2 huku mwenzake akiwa na asilimia 47.2.

Utafiti huo unaonyesha kuwa nusu ya wapiga kura wa Mudavadi watahamia kwa Odinga wakati Kenyatta atapata wale waliowapigia kura wagombea wengine, Martha Karua wa Narc, James Ole Kiyiapi (Restore and Build Kenya) na Peter Kenneth (Kenya National Social Congress).
Kwa upande wa makundi ya wagombea, Cord inaongoza kwa kuungwa mkono ikiwa na asilimia 45.8 ikifuatiwa na Jubilee (45.6%) na Amani ya Mudavadi ikiwa na asilimia 4.4.

Utafiti wa Consumer Insight
Matokeo ya utafiti wa Consumer Insight yanaonyesha kuwa Odinga hivi sasa anaungwa mkono na asilimia 46.8 ya wapigakura dhidi ya mwenzake, Kenyatta aliyepata asilimia 42.9. Mashabiki wa Mudavadi wamepungua kutoka asilimia 5.4 hadi 4.2.

Kampuni ya Consumer Insight imebaini kuwa iwapo uchaguzi utakwenda hadi marudio, Odinga atatangazwa mshindi kwa kufikisha asilimia 50.6 dhidi ya Kenyatta mwenye asilimia 46.3.
Utafiti huo wa Consumer Insight unaonyesha kuwa umaarufu wa Cord uko asilimia 47.8 wakati ule wa Jubilee ni asilimia 44.1.

Utafiti wa Strategic Pollster
Utafiti wa Strategic Pollster unaonyesha kuwa Odinga ataibuka mshindi kwa kupata asilimia 45.7 dhidi ya Kenyetta mwenye 43.8. Mudavadi bado ni wa tatu akiwa na asilimia 5.7.

Katika uchaguzi wa marudio, Strategic Pollster inasema Odinga ataibuka kidedea kwa asilimia 51.7 huku mwenzake Kenyetta akisimama kwenye asilimia 45.7.
Tafiti hizi zimetumia sampuli ya watu 2,600 wanaowakilisha wananchi 14,337,399 waliojiandikisha kupiga kura.

Wagombea urais walichuana vikali kwa mara ya pili juzi katika mdahalo, ambao ulikuwa fursa ya mwisho kupimwa na wapiga kura kabla ya uchaguzi utakaofanyika Jumatatu ijayo.
Kivuitu afariki dunia
Wakati huohuo, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Kenya (ECK), Jaji Samuel Kivuitu amefariki dunia, siku tano kabla ya Uchaguzi Mkuu.

Kivuitu (74) alifariki dunia saa nne usiku wa kuamkia jana katika Hospitali ya MP Shah ya Nairobi alikokuwa amepelekwa kutokana na mshtuko wa moyo.

Kivuitu anakumbukwa na mambo mawili makubwa na Watanzania. Matukio ya Uchaguzi Mkuu wa Kenya mwaka 2007 na pia kusoma Tanzania.

Alizua balaa Kenya baada ya kumtangaza katika mazingira ya kutatanisha Mwai Kibaki kama mshindi wa urais mwaka 2007 na kuzua vurugu za kikabila kutokana na mpinzani wake n Raila Odinga kuamini alipokonywa ushindi.

Alikuwa mmoja wa wanafunzi wa kwanza kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1961 na kumaliza mwaka 1965, akiwa katika Kitivo cha Sheria.

Familia ya marehemu Kivuitu imesema mazishi yatasubiri hadi Uchaguzi Mkuu umalizike Machi 4, mwaka huu

TCRA yafungia vituo viwili vya redio nchini

Felix
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano(TRCA)Walter Bugoya akitoa tamko la kuzifungia Redio Imani na Redio Kwa Neema kwa kipindi cha miezi 6 kutokana kutangaza matangazo yanayodaiwa kuwa ya kichochezi jijini Dar es Salaam jana.Kushoto ni Mkurungenzi wa Idara ya Habrio Maelezo Arthur Mwambene na Kaimu Mkurugenzi wav Utangazaji wa (TRCA)Andrew Kisaka.Picha na Fidellis
KAMATI ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa adhabu ya kuvifungia muda wa miezi sita vituo viwili vya redio za dini, Imani na Kwa Neema kwa kile kilichoelezwa ni kuendesha vipindi vya uchochezi.

Vilevile kamati hiyo imetoa adhabu ya faini ya Sh5 milioni kwa Kituo cha redio cha Clouds FM baada ya kubainika pia kukiuka taratibu za utangazaji kwa kurusha hewani kipindi kilichotafsiriwa kuwa ni cha uchochezi.


Kamati hiyo ya maudhui ilitangaza adhabu hizo jana jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari ikisisitiza kuwa lengo lao ni kuhakikisha kuwa vyombo vya habari vinazingatia maadili.


Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui ya TCRA,Walter Bugoya alisema TCRA imefikia hatua hiyo baada ya kuyafanyia uchunguzi wa kina malalamiko yaliyotolewa na wasikilizaji wa vituo hivyo vya redio.


Bugoya alisema redio hiyo ilitangazia wasikilizaji wake wasishiriki kwenye mkakati huo wa Sensa ya Taifa kwa kile walichodai kulingana na imani ya Kiislamu, wasingejua hatima ya mkakati huo.


Kuhusu Redio Kwa Neema inayorusha matangazo yake kutokea Geita, Bugoya alisema ilieneza uchochezi dhidi ya mtafaruku wa kidini uliozuka mkoani humo juu ya upande gani una haki ya kuchinja wanyama kwa ajili ya kitoweo.


Akizungumzia Kituo cha redio cha Clouds, Buyoga alisema kamati imeitaka kulipa fidia ya Sh5 milioni baada ya kubainika kuwa nacho kilienda kinyume cha maadili ya utangazaji kupitia kipindi chake cha Power Break Fast, cha Jicho la Ng’ombe walitoa kauli za uchochezi.

Tuesday, 26 February 2013

HILI SUALA LA UDINI LITATUFIKISHA WAPI NDUGU WATANZANIA?


HAKI YA KUCHINJA Waislamu, Wakristo wapigana mapanga *Mchungaji auawa kinyama, saba wajeruhiwa *Kisa ng'ombe, mbuzi waliochinjwa na Mkristo

SAKALA la nani mwenye haki ya kuchinja kati ya Wakristo na Waislamu, jana lilichukua sura mpya katika Kijiji cha Buselesele, Wilaya ya Chato, mkoani Geita baada ya kutokea vurugu kubwa
na kusababisha mauaji ya Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste,
Mathayo Kachila (48) na watu wengine saba kujeruhiwa.

Vurugu hizo zilitokea jana kijijini hapo kuanzia saa tatu asubuhi katika Soko Kuu la Buselesele, baada ya mtu mmoja ambaye inadaiwa ni Mkristo, kuchinja ngombe mmoja, mbuzi wawili.

Inadaiwa kuwa, Mchungaji Kachila alishambuliwa na kundi la Waislamu jirani na msikiti wakati akiwasindikiza wageni wake
baada ya vurugu hizo kupamba moto.

Akizungumzia tukio hilo, Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani humo, Paul Kasagabo, alithibitisha taarifa za kifo hicho na kuongeza kuwa, watu wengine saba walijeruhiwa vibaya kutokana na vurugu hizo.

“Chanzo cha vurugu ni mwananchi mmoja ambaye inadaiwa ni Mkristo aliyefahamika kwa jina moja la Obadia, kuchinja ngo'mbe mmoja, mbuzi wawili na nyama hizo kuuzwa katika bucha ambayo nje ilifungwa kitambaa chenye ujumbe unaosema 'Yesu tena bucha', ambayo anaimiliki hivyo hali hiyo iliwachukiza Waislamu.

“Katika vurugu hizi, bucha ya mtu anayelalamikiwa ilivunjwa pamoja na dula lililokuwa likitoa huduma ya M-Pesa na mwili
wa Mchungaji Kachila umehifadhiwa katika Hospitali ya
Wilaya ya Geita,” alisema.

Kamanda Kasagabo aliongeza kuwa, hadi sasa hakuna mtu ambaye amekamatwa kutokana na vurugu hizo ila jeshi hilo linaendelea kuwasaka wahusika ili waweze kufikishwa mahakamani.

Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Ernest Nkwabi, alithibitisha kupokelewa kwa mwili wa Mchungaji huyo hospitalini hapo na majeruhi saba.

“Tumepokea mwili mmoja wa marehemu na majeruhi saba ambao kati yao, wawili wamehamishiwa Hospitali ya Rufaa Bugando jijini Mwanza kwa matibabu zaidi kutokana na hali zao kuwa mbaya.

“Mwili wa marehemu una majeraha ya kukatwa na panga mara nne kichwani, mkono wa kushoto na kiganga chake chote kukatwa katwa hivyo kusababisha avuje damu nyingi,” alisema.

Aliwataja majeruhi waliopelekwa Hospitali ya Bugando kuwa ni Ramadhan Paschal (36), aliyejeruhiwa vibaya katika fuvu la kichwa upande wa mbele na Said Ntamopagafe (47) ambaye amejeruhiwa mguu wa kulia kwa kukatwa mapanga.

Alisema majeruhi wawili Vicent Raymond (18) na Yassin Rajab (56), bado wamelazwa hospitalini hapo wakiendelea na matibabu
na wengine wawili walitibiwa na kuruhusiwa.

Mkuu wa Wilaya ya Chato, Rodrick Mpogolo, alisema vurugu hizo zimedhibitiwa kijijini hapo na hali ya utulivu kurudi kama kawaida ambapo wananchi wanaendelea na shughuli zao bila hofu yoyote.
Share on linkedin Share on facebook Share on twitter Share on email More Sharing Services 0

CHADEMA wambana JK tatizo la udini


MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasi na Maendeleo (CHADEMA), ambaye pia ni Mbunge wa Mpanda Mjini, Bw. Said Arfi, ameitaka Serikali iwaeleze Watanzania kwanini inafumbia mambo tatizo la udini linaloendelea nchini.


Bw. Arfi aliyasema hayo mjini Dodoma jana katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Mwanga Bar, Kata ya
Uhuru na kusisitiza kuwa, tatizo hilo linaweza kuiweka nchi
mahali pabaya kwa siku za usoni.

Alisema Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali yake, bado haijachukua hatua zozote ili kuepusha machafuko yanayoweza
kutokea na kusababisha amani iliyopo kuwa historia.

“Awali Chama cha Wananchi CUF kilionekana cha Waislamu hivyo Wakristo wakakiogopa na kukimbia udini...hivi sasa CCM inadai CHADEMA ni chama cha Wakristo.

“Kutokana na propaganda hizi, tayari yameanza kutokea machafuko ambayo Wakristo na Waislamu wanapigana mapanga, tunamtaka Rais Kikwete alieleze Taifa kwanini chama chake kinasimamia
zaidi masuala ya udini,” alisema Bw. Arfi.


Aliongeza kuwa, baada ya mbinu za CCM kudai CHADEMA ni chama cha kikabila, sasa wameibuka na mbinu mpya wakidai
chama chao cha Wakristo jambo ambalio si kweli.

Alisema hivi sasa, CCM inatumia mamilioni ya fedha za wananchi katika mambo yasiyo na tija kwa jamii na Taifa badaya ya fedha hizo kuelekezwa katika sekta ya elimu ili kuongeza ufaulu wa
wanafunzi kwa lengo la kuongeza wataalamu.

“Tafiti mbalimbali zilizowahi kufanyika katika sekta ya elimu, zinasema uwekezaji mdogo katika sekta hii imechangia watoto wengi kuanza kidato cha kwanza wakiwa hawajui kusoma
wala kuandika lakini hakuna hatua zilizochukuliwa,” alisema.

Awali Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Mafunzo wa chama hicho Taifa, Bw. Benson Kigaila, aliwataka viongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kujiuzulu kutokana na matokeo mabaya ya wanafunzi waliomaliza kidato cha nne mwaka 2012.

Ole wenu mnaoona dini ni bora kuliko Mungu!

CHRISTIANS and Muslims in Tanzania can be partners in building a society shaped by the values taught by God: tolerance, justice, peace and concern for the poorest and the weakest.” Hiyo ni kauli ya kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani wakati huo, Baba Mtakatifu Yohane Paulo II aliyoitoa kwa Watanzania alipozuru nchini Septemba mwaka 1990.

Kwa tafsiri isiyo rasmi, ujumbe huu ulitaka kumaanisha kwamba, “Wakristu na Waislamu wa Tanzania wanaweza kuwa wadau katika kujenga jamii yenye maadili ya Kimungu; uvumilivu, haki, amani na kuwajali maskini na wanyonge.”

Nimelazimika kuanza na nukuu hii ili kuwaonyesha tu wafuasi wa kweli wa dini hizi jinsi walivyo na jukumu kubwa katika kuunda jamii yenye uvumilivu na mshikamano wa dhati ambao ndio msingi wa namna Mungu anavyotaka tuishi.

Kwa ufahamu mdogo nilionao kuhusu Uislamu (ninaweza kusahihishwa katika hili), ni kwamba jina tu lenyewe linamaanisha unyenyekevu na zaidi sana Uislamu ni dini ya amani na ukiwasikiliza baadhi ya wanazuoni wa Kiislamu wanasema Waislamu pia wamefundishwa namna ya kuishi na watu wasio wa dini yao kwa amani.

Na kwa kweli ziko baadhi ya hadithi zinashuhudia kuwa hata Mtume Mohamad (S.A.W) alipata msaada kwa namna moja ama nyingine kutoka kwa Wakristo na watu wengine wasio Waislamu, wakati anahamia Madina toka Makka.

Lakini pia katika Ukristu, upo msingi mmoja mkubwa wa imani yao, wanatakiwa wawapende jirani zao kama nafsi zao na zaidi sana wanatakiwa wawapende hata adui zao kwa sababu upendo ndiyo amri yao kuu.

Yako masimulizi katika Injili kwamba Bwana Yesu aliwaambia wale wote wanaomfuata na kuamini katika yeye kuwa wanaweza kuwa na uwezo hata wa kuhamisha milima, lakini kama wanatindikiwa na upendo ni kazi bure, utaona ni jinsi gani upendo ulivyo sehemu muhimu ya imani hii.

Bahati mbaya tuliyonayo katika jamii yetu kwa sasa, tumeanza kutumia dini hizi badala ya kuwa daraja la kutuunganisha, kutumia tofauti zetu kama njia ya kutuweka pamoja zaidi, sasa tunatumia tofauti za dini zetu kama sababu ya kuwa maadui na kujenga matabaka hasimu katika jamii yetu.

Kipo kitu kimoja ambacho viongozi na wafuasi wa imani hizi wanatakiwa watambue kuwa ni mpango wa Mungu wanayesema wanamwabudu, kutuumba tukiwa tunatofautiana.

Jinsi ambavyo tunatofautiana sura zetu na mawazo yetu ndivyo ambavyo tunatakiwa tutarajie tutatofautiana katika mitazamo ya mambo mbalimbali ikiwemo ya imani. Hili Mungu wanayemwabudu analijua na ndiyo maana kuna mbingu na jehanamu.

Sasa kama Mungu mwenye kuwaumba Binadamu hawa pamoja na uwezo wake wote usio na mipaka, lakini amewaacha binadamu hawa hawa waamue kuishi maisha watakayo kwa utashi wao binadamu mwingine ni nani mpaka atake watu wote waamini kama anavyoamini yeye?

Wataalamu wa elimu ya genetic wanatuambia kuwa ili kuwe na mtu ambaye anafanana na wewe kwa kila kitu, yaani sura, mawazo unayowaza wewe na yeye awaze hivyo na muwe na mtazamo unaofanana kwa kila kitu, ni lazima mzaliwe watoto laki tatu katika familia ya baba mmoja na mama mmoja, mtoto wa laki tatu na moja ndiye atakuwa anafanana kwa kila kitu na yule mzaliwa wa kwanza wa familia hiyo.

Hapa tunaweza kuona ni jinsi gani haiwezekani kutaka kufananisha mitazamo, kwa kuwa ni Mungu pekee na mwenye uwezo wa kila jambo chini na juu ya jua aliyeamua kutuwekea tofauti hizi na sisi hatuna namna wala uwezo wa kufanya vinginevyo, tunachoweza kufanya ni kutaka kuziishi tofauti hizo kwa manufaa yetu na kuifanya Tanzania iwe sehemu nzuri ya kuishi kila mmoja wetu apendavyo bila kuingilia uhuru wa mtu.

Kwa hakika ni uendawazimu na ujinga wa kiimani kutaka au hata kuthubutu tu kuwaza mikakati na mbinu za kuwafanya watu wote wawe Wakristu au Waislamu, hilo halitawezekana kwa sababu ni Mungu aliyedhamiria kutufaya tutofautiane namna hii, hizi tofauti zetu hatukuchagua wenyewe, tumejikuta kwa njia mbalimbali tuna mitazamo hiyo inayokinzana ambayo siyo lazima itufanye tupigane.

Dini hizi ni kama zinataka kuharibu taifa hili kama tu ambavyo dini zimeharibu mataifa mengine mengi yaliyotukuka kwa kuwa na amani na mshikamano na nguvu za kiuchumi.

Madai yanayoendelea sasa ya nani ana haki ya kuchinja kuliko mwingine, yanaweza kuwa ya msingi kulingana na imani za watu na hapa sitaki kuingia katika mtego wa kupuuza imani ya mtu, lakini hivi waumini hawa wamejiuliza ni kwa kiasi gani maisha ya mtu yana thamani kuliko hiyo nyama wanayogombania kuchinja?

Haiwezekani kwamba, Waislamu na Wakristu ambao hawazidi asilimia 50 ya Watanzania wote wanataka ndiyo wawe madereva wa nchi hii, wapo pia Watanzania wenye haki zao ambao wana haki ya kuishi kwa amani na hapa ndiyo wajibu wa Serikali unapoingia.

Katika hiki, Serikali haiwezi kukwepa wajibu wake katika damu za Watanzania zilizomwagika. Kwa sababu ni kweli kwamba, Serikali imetajwa legelege mno katika kusimamia mambo ya msingi ya taifa, hatimaye tumejikuta tunaliingiza taifa katika hali ambayo kama tukipuuzia kuchukua hatua za makusudi kulimaliza hili, tutaingia katika zama ambazo tunaweza tusitoke huko.

Tumeshindwa kuvumiliana kwa sababu ya vibaraka na uzembe wa Serikali kutotambua wajibu wake, ama imeamua kuupuuza kwa makusudi na sijui ni kwa maslahi ya nani.

Ole wetu tusipochukua hatua mujarabu kwa wakati na wananchi na wafuasi wa dini hizi wanaoshabikia mambo kama vile Yanga na Simba, wasifikiri hii ni ngoma ya kitoto.

Nchi hii ikilipuka wote tutakuwemo bila kujali nani anamwabudu nani kwa imani gani.

Yale tuliyozoea kuyaona kwenye mchakato wa Katiba, watu wanagombania kila mtu awe na mamlaka juu ya Katiba dhidi ya wenzao, hili nao lilikuwa Salamu ya jinsi gani tumefika hapa, kila jambo siku hizi tunahitaji kuliangalia kwa jicho la dini kwa manufaa ya dini zetu, hili halitatufikisha siyo tu tuendako kama taifa, bali hata wanaomwamini hawatafika kwa Mungu wao kwa mtindo huu.

Hili hata kwenye haki za kikatiba pia, hatuwezi kuwa waumini safi wa dini zetu kama tunapoandika Katiba kila mtu anataka imtambue yeye zaidi kuliko wengine, wako watoto wa mitaani, hawa wanatakiwa Waislamu na Wakristu wanaokwenda kutoa maoni kwenye Tume ya kuratibu maoni ya Katiba wawatetee.

Wako watoto wadogo wanaodhulumiwa haki, hawa hawawezi kusema kwenye Katiba, wakuwasemea ni sisi Waislamu na Wakristu tunaomjua Mungu kwa sababu Mungu kawaweka hawa katikati yetu ili aone sisi aliotujalia zaidi kuliko wao, tunatumia vipi neema hizo kwa manufaa ya wenzetu wasiojiweza.

Tuzifanye dini zetu ziwe sehemu ya kutupatanisha kwa msingi wa uvumilivu kwa sababu Mungu mwenyewe mwenye dini hizi tunazotumia kumwabudu ni mvumilivu kuliko tunavyoweza kufikiri.

Jaribu kujiuliza wewe unayetaka dini yako tu ndiyo iwe bora kuliko ya wengine, unadai huwezi kuvumilia wenye imani tofauti na wewe, hebu fikiria Mungu angekuwa siyo mvumilivu hata kwa nukta moja.

Wewe kiongozi wa dini unayehamasisha watu wa imani yako wawachukie na wasifungamane na wengine, jiulize kwa siku moja unawaza na kufanya mangapi ambayo Mungu angeamua kukushughulikia hapo hapo ungeweza kudumu kwa muda gani?

Mungu anavyotupenda tumezungukwa na mifano mingi sana ya jinsi dini na tofauti zozote za kijamii zimesababisha machafuko katika nchi za wenzetu, lakini sijui kwanini hatutaki kujifunza.

Migogoro inayozaa vita za kidini au za kikabila huwa inaanza namna hii kwa kukosa uvumilivu miongoni mwa wanajamii, tujue kwamba hata mbuyu ulipoanza kuchipua ardhini ulikuwa mdogo na dhaifu kama mchicha, lakini baada ya muda ukawa ulivyo.

Chokochoko za kidini tunaweza kuziona ndogo na zinafanywa na wapuuzi, hivyo haziwezi kutuletea madhara na mitafaruku katika jamii.

Tutakuwa tunajidanganya, tusipokuwa macho na kuchukua hatua sasa mambo yakishashika kasi sina hakika tutakimbilia wapi, lakini walau nina hakika na jambo moja kwamba, machafuko yakianza hakuna atakayebaki salama, si Muislamu au Mkristo.

Ole wao wanaoziona dini ni bora kuliko Mungu.

Katiba mpya ifute mfumo wa ‘Westminister’ - Kujenga Umoja na Utambulisho wa Kitaifa


WAKATI tunajadili utungaji wa Katiba mpya ya Tanzania, ni vizuri tukatafakari kwanza misingi itakayotuongoza katika kuandaa maudhui ya Katiba hiyo. Katika waraka huu napenda kutoa mawazo machache kuhusiana na suala hilo. Napendekeza misingi ifuatayo:

Kujenga umoja na utambulisho wa kitaifa, Kupanua uhuru na haki za msingi za raia, kupanua demokrasia, kuweka mfumo wa uwazi wa utawala na uongozi na kudhibiti ufisadi, kuimarisha uchumi na uzalishaji, kujenga umoja na ushirikiano wa kikanda na hatimaye umajumui wa Afrika nzima.

Kabla sijajadili misingi hiyo, nizungumzie kidogo suala la mchakato wa kuandaa Katiba. Katiba ni chombo chenye mamlaka juu ya kila mtu na kila chombo katika jamii.

Katiba lazima itawale mamlaka zote kuanzia kwa Rais hadi kwa balozi wa nyumba kumi na kuishia kwa mtu binafsi. Katiba sharti itawale asasi zote kuanzia Bunge hadi mahakama, polisi, asasi za kiraia na kidini, n.k.

Ndiyo maana haifai kwa Katiba kuamuliwa na vyama vya siasa ambavyo ni vikundi vyenye maslahi maalumu ndani ya Katiba hiyo.
Kujenga Umoja na Utambulisho wa Kitaifa
Katiba yoyote ile ya nchi huwa na jukumu la kujenga utaifa na utambulisho wa Taifa linalohusika na hivyo kuchunga na kulinda usalama na uzalendo wa Taifa hilo. Ndiyo maana Katiba za mataifa mengi hutaja mipaka ya nchi, Bendera ya Taifa, Wimbo wa Taifa, Lugha ya/za Taifa na lugha nyingine rasmi kama zipo.

Katiba za baadhi ya nchi hutaja hata hati za maandishi za lugha yao na vipengele muhimu vya utamaduni wa Taifa, kama vile dini, mila na kadhalika. Katiba ya sasa ya Tanzania inataja baadhi ya mambo haya lakini si yote. Kwa mfano haitaji Lugha ya Taifa!

Kujenga utambulisho na utaifa ni pamoja na kujenga umoja wa kitaifa kuweka misingi imara ya umoja inayokubalika kwa wananchi wote wa makundi na matabaka yote, kujenga uzalendo, mapenzi ya nchi na moyo wa kuwa tayari kuitetea na kuifia nchi ikibidi.

Ni wazi kwamba, suala la kuruhusu uraia wa nchi mbili au zaidi ambalo linapigiwa debe sana hivi sasa na baadhi ya watu, inabidi litazamwe kwa kuzingatia msingi huu wa uzalendo na maslahi ya Taifa: Mathalan, itakuwaje iwapo raia wa Marekani (au nchi nyingine), ambaye pia ni raia wa Tanzania, atatumwa na Rais wake wa Marekani na kupewa nyenzo zote kuja kututawala na kutekeleza matakwa ya nchi yake (ya Marekani) hapa kwetu? Utamzuiaje?

Hatusemi kwamba kiongozi asiyekuwa na uraia wa nchi ya kigeni hawezi kutumiwa na nchi hiyo kutekeleza maslahi yake katika nchi anayoiongoza. Tunawafahamu viongozi vibaraka wengi waliotumiwa hivyo. Tunachosema hapa ni kwamba, tusiwarahisishie maadui zetu mchakato wa kupata vibaraka miongoni mwetu.

Suala la utamaduni sharti lipewe uzito kikatiba, maana bila utamaduni hakuna Taifa na njia ya uhakika ya kumdhibiti na kumtawala mtu ni kumteka kitamaduni na kiakili.

Hapa suala la lugha sharti lipewe uzito unaostahiki; Lugha ya Taifa, Kiswahili ipewe nafasi muhimu kikatiba na lugha za kijamii na za kigeni tunazozihitaji zisisahaulike. Katiba itaje wazi kwamba Kiswahili ndiyo lugha ya Taifa na lugha rasmi ya kwanza na Kiingereza ni lugha rasmi ya pili.

Katiba ielekeze kwamba itatungwa sheria mahsusi itakayofafanua nafasi, dhima na matumizi ya lugha ya Taifa na lugha nyinginezo katika jamii.
Kupanua Uhuru na Haki za Raia
Katiba inapaswa kulinda uhuru na haki za raia ambazo ni pamoja na haki za kuishi, kuheshimiwa kama binadamu, kufanya kazi na kupata malipo ya haki kwa kazi hiyo, kupewa pensheni ya uzeeni, kujumuika, kusafiri, kuishi popote, kuabudu au kutokuabudu.

Haki za lugha na utamaduni pia zinahusika hapa. Na haki hizo lazima ziwe ni kwa raia wote bila kujali jinsi, kabila, rangi, dini, cheo, umri au nasaba.

Katiba ya sasa inatoa haki hizo kwa kiasi fulani. Katiba ijayo ingefaa isisitize na kufafanua zaidi haki hizi za msingi.
Kumtaja Mungu katika Katiba
Hapa tunaweza kueleza kuwa pendekezo la Jaji Mstaafu Barnabas Samatta, katika kongamano moja kuwa Katiba mpya itaje Mwenyezi Mungu halikubaliki kwa sababu linakwenda kinyume na uhuru wa kuabudu tunaouzungumzia.

Kwa kuwa Katiba tayari inatoa uhuru wa kuabudu, hakuna sababu ya kuufunga uhuru huo kwa kuuhusisha na imani fulani maalumu, zile zinazozingatia dhana ya Mungu. Ni vyema Katiba iendelee kutofungamana na imani ya dini yoyote.
Kupanua Demokrasia
Katika ulimwengu wa sasa na ujao, utawala wa kidemokrasia hauepukiki. Hivyo tunahitaji Katiba inayotambua haki na haja hiyo ya kujenga na kuimarisha demokrasia. Demokrasia tunayozungumzia hapa ni demokrasia pana inayojumuisha wananchi wote wa makundi yote. Hatuzungumzii demokrasia ya vyama vya siasa tu.

Katiba yetu ya sasa kwa kiasi kikubwa inajikita katika demokrasia ya vyama badala ya demokrasia ya Umma. Labda hili linahitaji ufafanuzi zaidi.

Miaka kadha iliyopita makundi mbalimbali ya wanasiasa, yalianza kufanya kampeni ya kutaka majimbo ya uchaguzi yaongezwe ili kuimarisha uwakilishi na demokrasia.

Tulishuhudia madiwani wa halmashauri mbalimbali, wakipitisha maazimio ya kuongeza majimbo ya udiwani na ubunge. Baadhi ya wabunge na vyama vyao vilevile walipendekeza majimbo mapya yaanzishwe.

Kampeni hiyo ilifanikiwa kwa kiasi fulani na majimbo mapya kadha yaliundwa, japo ilitolewa tahadhari kuwa jengo la sasa la Bunge mjini Dodoma halina nafasi ya kuongeza wabunge wengi. Msingi wa kampeni hii ni dhana potofu kuwa demokrasia maana yake ni kuwa na wawakilishi wengi wa vyama katika Bunge na mabaraza ya madiwani.

Mtazamo huu wa kimajimbo kuhusu uwakilishi unadaiwa kutokana na mfumo wa Westminister, yaani mfumo wa Bunge la Uingereza. Hii ni kweli kwa kiasi fulani tu.

Waingereza wana utaratibu wa uwakilishi wenye historia ya karne nyingi za mapambano ya kitabaka na kikatiba kati ya mamwinyi, mabwanyenye, watwana na wafanyakazi na kati ya ufalme wa England na falme za Wales, Scotland na Ireland, ambazo kwa pamoja zinaunda Ufalme wa Muungano wa Uingereza (UK).

Baada ya miaka mingi ya kupambana na kumwaga damu na baadhi ya viongozi na wafalme kukatwa vichwa, hatimaye Waingereza walikubaliana kuwa na Bunge lenye chemba au mabaraza mawili ili kuzingatia maslahi ya pande zote.

Mabaraza hayo ni lile la Mamwinyi (House of Lords) na lile la Makabwela (House of Commons). Wajumbe wa Baraza la Mamwinyi hawachaguliwi na wananchi na hujumuisha mamwinyi wenye kumiliki ardhi kubwa na viongozi wakuu wa Kanisa la Uingereza. Wajumbe wa Baraza la Makabwela huchaguliwa majimboni.

Mapambano ya kudai demokrasia nchini Uingereza, vilevile yaliibua vyama vikuu viwili, Conservative (chenye kuwakilisha maslahi ya mamwinyi na mabwanyenye) na kile cha Labour (ambacho awali kiliwakilisha maslahi ya matabaka ya wazalishaji wafanyakazi na vibarua.

Siku za karibuni, kimezuka chama kingine kikuu cha tatu, Liberal Democrats, ambacho kimetokana na muungano wa vyama vidogo viwili vya Liberal Party na Social Democratic Party, hicho ni chama cha kiliberali cha mrengo wa kati.

Vipo vyama vingine vidogo vidogo, lakini havina athari kubwa kiutawala. La muhimu kufahamu kuhusu mfumo huu wa Uingereza ni kwamba, vyama vyote vinavyoshika utawala huendeleza takriban sera zilezile za uchumi, utaifa na mambo ya nje na hakuna hata kimoja kwa sasa kinachowakilisha maslahi ya mnyonge.

Jingine la kukumbuka ni kwamba mfalme au malkia wa Uingereza, ni nguzo mojawapo ya Bunge la Uingereza kama alivyo Rais hapa kwetu.

Hivyo, madai ya kwamba Tanzania inafuata mfumo wa Westminister yana walakini maana hayasemi ukweli wote. Hata hivyo, kuna jambo moja la Westminister ambalo Tanzania na nchi nyingi za Jumuiya ya Madola zinaling’ang’ania, nalo ni uwakilishi na utawala kupitia katika vyama.

Huu ni utaratibu ulioletwa kwetu na nchi za Magharibi nasi tukaupokea na kuukubali bila kuusaili. Lakini je, utaratibu huu unahakikisha kuwapo kwa mfumo bora wa uwakilishi wa makundi yote ya wananchi?

Mugyabuso Mulokozi ni Profesa Mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.