Nakumbuka nilipokuwa bado kijana katika mkoa nilioishi kulikuwa
na matajiri kadhaa ambao sisi tuliwaona wametuzidi. Wengine walikuwa
jamaa zetu, hivyo kuwafahamu kwa karibu zaidi namna walivyokuwa
wakiendesha maisha yao na namna walivyokuwa wakifurahia maisha yao ya
kutokukosa vitu vidogo vidogo.
Sehemu kubwa zaidi ya matajiri hao sasa hawapo
tena katika hali hiyo ya kuwa navyo. Wengi wao sasa ni wahitaji,
wakiishi maisha ya kubangaiza. Tukiwaacha wao hata sisi wengine japo
siyo matajiri, lakini huenda tumewahi kushika ‘vipesa’ wakati fulani,
lakini pesa hizo zikashindwa kabisa kubadilisha maisha yetu.
Hali hii inahitaji kujitafakari kwani haina maana
kuzungumzia nchi kujitoa katika umaskini wakati watu wake hawana mpango
wa kujitoa katika umaskini huo. Tujiulize, inakuwaje tunaendelea kuwa
maskini hata pale ambapo tunapata fursa ya kuwa na fedha?
Majibu kwa swali hili yapo mengi, lakini leo tuangalie yale yanayoendeana na tabia.
Wengi wetu tuna tabia ya kutokuweka akiba. Tabia
hii wanayo wakulima, wafanyakazi hata wafanyabiashara. Mtu akibarikiwa
kuwa na ziada ya pesa, basi badala ya kufikiria namna pesa hizo
zitakavyozalisha zaidi, pesa hizo zitatafutiwa matumizi zaidi.
Matumizi hayo mara nyingi siyo ya kuzipeleka
kwenye eneo la uwekezaji ili mtu apate faida zaidi bali ni kwenye eneo
la ulaji. Kwetu sisi pesa zaidi maana yake ni sherehe zaidi, ununuzi
zaidi na mbwembwe nyingine nyingi zisizokuwa na tija. Mwishowe ziada
yote iliyopatikana inayeyuka na kumrudisha mtu katika hali ile ile
aliyokuwa nayo kabla ya fedha kumtembelea.
Hakika hii inahuzunisha; hebu fikiria leo mtu
anawakaribisha kwenye sherehe ya ubatizo wa mwanawe ambayo inakuwa kubwa
kuliko hata ya Tanzania kufikisha miaka 50, halafu kesho mtu huyo huyo
anakugongea na kukuomba au kukukopa fedha ya kununulia unga wa ugali.
Yanatupata haya kwa sababu fedha inatuwasha pale
inapokuwa mikononi mwetu. Wakati wenzetu wanachambua faida na hasara
watakazozipata kwa kuwekeza katika miradi mbalimbali, sisi tunachambua
kicheko tutakachokuwa nacho katika matanuzi ambayo hata kuyapanga
hatupangi bali yanakuja hapo hapo baada ya kupata fedha.
Siamini kama kweli mtu alipanga kuwajengea vimada
nyumba bora za kuishi halafu yeye na familia yake wakakosa sehemu ya
kuishi. Naamini fedha zilipokuwa mkononi zilimtia upofu na zilimharibu
akili yake, hata akatenda hayo. Tumewasikia wale waliopata ufahamu baada
ya kufilisika na wakataka kuzimiliki nyumba hizo bila mafanikio.
Wao wanateseka kwa kukosa makazi, lakini wale
waliowapa starehe za muda wanaishi katika nyumba za kifahari. Hata kama
makazi yapo hizo fedha si zingewekezwa kwenye maeneo yanayozalisha fedha
zaidi?
Uzalishaji huo si ungemwezesha sasa mtu kuishi
uzee wake mwema? Uzee ambao mtu angekuwa anatumia muda mwingi sasa
kuwaombea na kuwabariki watoto wake, badala ya kila siku kuwalaani kwa
madai kwamba hawamjali.
Tabia nyingine inayotuvuruga sana ni ya
kujionyesha. Katika kujionyesha huko mtu ananunua au anajenga, hata kile
ambacho hana sababu nacho. Mtu alikuwa na friji yake inayomtosha kwa
matumizi ya nyumbani kwake leo fedha imemtembelea basi atakwenda kununua
friji kubwa, utafikiri anataka kuweka kuku wa kuuza.
Friji hiyo kubwa inaishia kuwekwa maji, atajenga nyumba kubwa
zaidi yenye ghorofa mbili, halafu vyumba vingine vinaishia kuwa makazi
ya mende. Inasikitisha sana pale watu wanapokuwa wamezeeka halafu nyumba
hiyo ipo mahali ambapo familia haiwezi hata kubadilisha matumizi ya
nyumba hizo yaani badala ya kuishi, labda wafanye hoteli au wapangishe.
Utakuta mtu kaishiwa kabisa, lakini hajui jinsi ya
kuitumia nyumba hiyo ambayo kwa sasa inatumika kwa asilimia 10 tu.
Ukijiuliza kwa nini mtu aliwekeza kwenye jumba kama hilo, jibu
utakalopata ni alitaka watu wajue kwamba naye ana fedha.
Tunahitaji kweli vitu vyote tunavyovinunua? Hakuna
siku tunajutia viatu na nguo nyingi tulizozijaza katika nyumba zetu,
ambazo kwa kuwa zimepitwa na wakati zimejaza makabati yetu na hatuna za
kuzifanyia?
Hivi kweli mtu unakosa hata fedha ya kununulia
dawa, lakini ndani ya nyumba una vitu chungu mzima ulivyovinunua kwa
kujionyesha na sasa havikuzalishii chochote, hiyo kweli ni akili?
Tunapenda sana kuwaiga wazungu, nafikiri tuwaige
pia tabia yao ya kupenda kuweka akiba kwa ajili ya kuwekeza au kwa ajili
matumizi ya baadaye. Tujifunze pia kufanya vitu kwa kiasi, tuache tabia
ya kujionyesha, kwani tabia hii inatufanya tusifikiri vizuri katika
kuwekeza fedha tuzipatazo.
Tusipobadilika, tutaishia kama tulivyo; leo mtu
anapigiwa makofi kwa kuvaa vizuri, kutembelea magari ya kifahari, kuishi
kwenye nyumba ya kifahari na kufanya sherehe kubwa kubwa halafu baada
ya muda mfupi, anakuwa omba omba au kopa kopa asiyerudisha fedha
anazokopa.
Hii haikubaliki hata kidogo. Tujizoeshe tabia mbadala nayo ni ya kuweka akiba na kununua vitu kwa mahitaji siyo kwa fahari.

No comments:
Post a Comment