Sunday, 16 March 2014

Sitta: Katiba inaruhusu kununua uongozi

Dodoma. Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta amesema kushamiri kwa vitendo vya watu wachache kujitajirisha na wengine kununua uongozi, kunatokana na Katiba ya sasa kutokuwa na meno ya kupambana na rushwa na ufisadi.
Amesema vitendo hivyo vitakoma kama nchi ikiwa na Katiba nzuri, itakayowezesha kutungwa kwa sheria nzuri zitakazowabana mafisadi na watoa rushwa.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake Dodoma juzi, Sitta alisema: “Siridhiki na Katiba ya sasa inavyoshughulikia rushwa na ufisadi. Katika nchi yetu inaonekana ni rahisi mtu kujitajirisha kwa kutumia cheo chake na baada ya hapo kununua uongozi. Katika nchi maskini jambo hili ni hatari kubwa.”
Aliongeza, “Katiba lazima ielekeze kwamba iko tofauti kati ya kufanya biashara na kuongoza watu. Haiwezekani ukawa na biashara kubwa zinazochukua zabuni za Serikali na ukaendelea kuwa kiongozi wa Serikali, nchi nyingi zimetenganisha mambo haya.”
Alisema rushwa ni hatari na inaweza kusababisha nchi kukosa amani, kwa sababu wananchi maskini watafika mahali hawataona uhalali wa maisha ya watu wanaowaongoza.
“Nimeipenda Rasimu ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, imeeleza wazi kuhusu suala la  uadilifu hivyo lazima zitungwe  sheria zitakazowabana watu kutokutumia madaraka yao vibaya,” alisema.
Sitta ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, alisema ni hatari kuwa na mfanyakazi wa Serikali mwenye kampuni binafsi ambayo inapewa tenda za Serikali.
“Sisemi kuwa watu wasiwe wafanyabiashara, mtu akiamua kuhudumia umma anatakiwa kuweka mali na biashara zake katika mfumo wa kuendesha biashara hiyo bila yeye kuwa mhusika wa moja kwa moja. Hivyo, ndivyo wanavyofanya mataifa kama Uingereza na Marekani,” alisema Sitta.
Alisema taarifa nyingi za maendeleo katika nchi za Afrika zinaeleza kuwa nchi za bara hilo zinakwama kupiga hatua kimaendeleo kwa sababu ya rushwa.
“Rushwa inajenga mtandao ambao unashuka hadi ngazi za chini. Watumishi wa chini wakiona mikataba mibovu inawanufaisha wakubwa nao hutafuta mianya katika maeneo yao. Ikiwa hivyo wanaopata shida ni wananchi wanyonge,” alisema na kuongeza;
“Sisi wakubwa tunaweza kutoa rushwa na tukaishi vizuri ila watu maskini kutoa rushwa ni ngumu. Elimu yetu siyo nzuri, huduma za afya nazo hivyo hivyo kutokana na kushamiri kwa rushwa,” alisisitiza.
Alisema ni ajabu kuona vitabu vyenye makosa vinatumika katika shule mbalimbali nchini na hata ukifuatilia unabaini kuwa aliyetoa vitabu hivyo alitoa rushwa Wizara ya Elimu.
“Asilimia 40 ya dawa tunazotumia hapa Tanzania ni ‘feki’. Yaani unaandikiwa dawa ambazo hazina maana katika matibabu. Hali hii ni matokeo ya kuwa na mfumo mbovu ambao unahitaji kubadilishwa. Katiba Mpya inatakiwa kuzungumzia kiundani suala la uadilifu, kuwe na sheria zitakazozuia mtu kujinufaisha kutokana na wadhifa wake,” alisema.
Alisema rushwa ikiwa tabia ndani ya nchi, uchumi unakwama kwa sababu mapato ya Serikali badala ya kwenda kutatua matatizo ya wananchi yanakwenda katika zabuni za ovyo na kutajirisha wachache ambao nao wana tabia ya kutorosha fedha nje ya nchi.
“Mnachangia mfumo wa mapato ya Serikali lakini fedha zinatoroshwa nje ya nchi. Katika Afrika misaada inayotoka nje ni kidogo kuliko fedha zinazotoroshwa kwa rushwa. Kuna faida gani kujisifia kuwa Waziri wa Fedha kasaini mikataba wakati rushwa inatoka zaidi kuliko fedha inayoingia?” alihoji Sitta.
Alisema Tanzania imeathirika na rushwa, huku akitolea mfano jinsi wakulima wanavyokuwa na madeni hewa yanayowafanya washindwe kuendesha shughuli zao.
“Ni hatari kuwa na vijana waliokata tamaa kwa sababu ya kutokuwapo ajira. Tatizo la ajira ni kutokukua haraka kwa uchumi. Uchumi wetu utaweza kukua kwa haraka na kupunguza umaskini kama hatutaingia mikataba mibovu na tutakomesha rushwa,” alisema.
Alisema nchi ambayo viongozi wake wanapokea rushwa ni lazima itapata wawekezaji uchwara kwa sababu wanajua hata wakiboronga hakuna wa kuwafanya jambo lolote.
“Kama ni barabara watajenga tu hata kwa kiwango cha chini kwa sababu wanajua hata ikiharibika wao watakuwa wameshalipwa fedha zao na aliyetoa zabuni naye atakuwa ameshachukua chake,” alisema

No comments: