Dar es Salaam. Wakati safari ya kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu wa
Oktoba mwaka huu ikipamba moto, kumeibuka makundi ya watu yaliyofungia
akaunti katika mitandao ya kijamii yakiwaunga mkono baadhi ya wanasiasa
waliotangaza au wanaotajwa kuwa na nia ya kugombea urais ya
kuwashambulia washindani wao.
Kila kundi limejipatia wafuasi wengi ambao
wanaonyesha kumkubali mwanasiasa husika wanayedhani anafaa kuwa rais wa
Tanzania endapo atapitishwa na chama chake na kupigiwa kura na wananchi.
Hata hivyo, wasomi na wachambuzi wanaonya kuwa
pamoja na njia hii kuwa ya haraka kuwafikia wapigakura walio wengi ambao
ni vijana na wanawake, inatakiwa kutumika kwa uangalifu la sivyo
inaweza kusababisha machafuko.
Makundi yenyewe
Makundi hayo, mengi yakipatikana katika mitandao
ya Facebook, Twitter na WhatsApp yanafanya kazi ya kuwanadi wanasiasa na
kubainisha shughuli mbalimbali wanazozifanya kila siku wawapo katika
ziara zao za binafsi, za kiserikali au kichama katika maeneo mbalimbali
nchini.
Baadhi ya kurasa za makundi hayo zenye wafuasi
wengi ni pamoja na ule wa ‘Team Lowassa’, kundi linalomuunga mkono
Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa ambao hadi jana ulikuwa na wafuasi
46,124 ambao wanaweza kupata habari mbalimbali zinazomhusu kiongozi
huyo.
Hata hivyo, mbunge huyo ambaye pia aliwahi kuwa
waziri mkuu, hivi karibuni alikaririwa na gazeti hili akiikana moja ya
akaunti za Twitter iliyokuwa imechapisha taarifa zilizomkariri
akizungumzia suala la ufisadi wa escrow.
Akizungumzia kurasa hizo, Msaidizi wa Lowassa,
Abubakar Liongo alisema akaunti hizo zinatengenezwa na marafiki na
kusisitiza kwamba kiongozi huyo hahusiki nazo kwa namna yoyote.
“Hawa ni marafiki tu, huwezi kuwazuia kufanya
wanachotaka kufanya, sisi tumeshatoa taarifa kuwa hizi hatuhusiki nazo,”
alisema Liongo.
Kundi jingine linajitambulisha kama ‘Team Hamis
Kigwangalla’ linalomuunga mkono Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla na
mpaka kufikia jana lilikuwa na wafuasi 9,893. Hili ni kundi la pili
kuwa na wafuasi wengi katika mtandao wa Facebook baada ya lile la Team
Lowassa.
Ukurasa mwingine umeanzishwa na watu wanaomuunga
mkono Mbunge wa Bumbuli na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na
Teknolojia, January Makamba. Ukurasa huu umepewa jina ‘January Makamba –
The next President’ na hadi jana ulikuwa na wafuasi 7,075.
Wanasiasa wengine wanaohusishwa na mitandao hiyo
ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe
ambaye mbali na akaunti yake kwenye WhatsApp, ukurasa wa marafiki zake
kwenye Facebook wenye jina la ‘Bernard Membe Fans Page’ umefikisha
wafuasi 5,120.
Kundi la wafuasi wa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa
linafuatia. Kundi hilo lililoanzisha mtandao uliopewa jina ‘Dr Slaa Team
Winner – 2013/2015’ hadi jana lilikuwa na wafuasi 4,337.
Vilevile, lipo kundi jingine linalomuunga mkono
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira na
ambalo ukurasa wake uitwao ‘Wasira wa Watanzania (WWW)’ lina wafuasi
3,524.
Pia upo ukurasa wa “Marafiki wa Samwel Sitta’
katika Facebook wenye mashabiki 2,238 wanaomuunga mkono Waziri wa
Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta.
Katika mtandao wa Twitter, wanasiasa hao na
wengine hawako nyuma, karibu kila mmoja ana akaunti binafsi huku wafuasi
wao wakipata nafasi ya kusoma yale wanayoyaandika wakati wowote.
Miongoni mwa wanasiasa wenye wafuasi wengi ni
Zitto Kabwe ambaye watu 208,294 wanafuatilia hoja zake na wakati
mwingine kujibizana.
Anayefuata ni Makamba mwenye wafuasi 151,822,
Bernard Membe (45,889) na Dk Slaa (40,830). Lazaro Nyalandu aliyetangaza
wiki iliyopita kuingia katika mbio za kusaka urais, akaunti yake ya
Twitter inafuatiliwa na watu 36,726.
Wengine katika mkondo huo ni Dk Khamis Kigwangalla
(26,322), William Ngeleja (11,110), Anna Tibaijuka (8,053), Freeman
Mbowe (4,162), Asha-rose Migiro (4,736), Edward Lowassa (2,123), Stephen
Wasira (750) na Dk Emmanuel Nchimbi (515).
Ni dhahiri kuwa wanasiasa vijana ndiyo wanaotumia
zaidi mitandao ya kijamii na kuwa na wafuasi wengi ambao wengi wao pia
ni vijana.
Maoni ya wachambuzi
Baadhi ya wasomi nchini wameelezea kuwa si jambo
baya kutumia mitandao ya kijamii kujinadi kwa wananchi. Hata hivyo,
wameonyesha wasiwasi kwa jinsi inavyotumika na kuwa inaweza kusababisha
machafuko.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT),
Hamad Salim alisema kadri muda unavyokwenda, ndivyo jamii inavyobadilika
na mabadiliko haya yanahusisha pia matumizi ya mitandao ya kijamii.
Salim alisema vijana na wanawake ambao ndiyo idadi
kubwa ya wapiga kura, sasa wanatumia mitandao ya kijamii. Alisisitiza
kuwa hii ndiyo sababu pekee iliyowasukuma wanasiasa kuanza kutumia
mitandao ya kijamii.
“Mitandao hii inawasaidia wanasiasa kujitangaza kwa wananchi,
pia haina gharama kwao. Tulizoea kuona wanasiasa wakipita mitaani kutoa
zawadi na kujinadi kwa wananchi kipindi cha uchaguzi, sasa ni rahisi,”
alisema.
Hata hivyo, Salim alionya kuwa mitandao ya kijamii
isipodhibitiwa kikamilifu, inaweza kusababisha machafuko ya kisiasa
kama ilivyotokea katika nchi za Tunisia na Libya na kusababisha mapigano
ya wenyewe kwa wenyewe ambayo yanaendelea mpaka sasa.
“Tuliona pia wakati wa sakata la escrow, watu
walianza kuunda baraza la mawaziri mtandaoni kabla hata Rais hajasema
chochote. Sasa hii ni hatari, wakati mwingine inaweza kujenga chuki,”
alisema.
Alisema katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa
uliofanyika hivi karibuni, Ukawa hawakutumia nguvu kubwa kwa sababu
walishajenga ngome kwenye mitandao ya kijamii.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM),
Richard Mbunda alisema sasa hivi mitandao ya kijamii ni sehemu ya maisha
ya Watanzania. Hivyo, inakuwa rahisi kwa wanasiasa kuwafikia wengi
ndani ya muda mfupi kwa njia hiyo.
Alisema uzuri wa mitandao ya kijamii ni kuwa
wanasiasa wanapata nafasi ya kujitangaza na wananchi pia wanapata
kuwafahamu na kuwapima kama wanaweza kuongoza Taifa hili.
Aliuangana na Salim akisema kuwa Tanzania haina
udhibiti mzuri wa mitandao ya kijamii, jambo linaloweza kusababisha
chuki na mifarakano miongoni mwa wanajamii.
“Si kila linaloanzishwa ni jema asilimia 100,
wengine wanatumia mitandao ya kijamii kuwachafua wengine, hasa mahasimu
wao kisiasa,” alisema Mbunda na kuitaka Serikali kuwa na udhibiti wa
mitandao hiyo hasa wakati huu kuelekea Uchaguzi Mkuu.









