Friday, 5 December 2014

RIPOTI: Watanzania wapoteza matumaini

Dar es Salaam. Zaidi ya nusu ya Watanzania wamekata tamaa ya maisha, badala yake wanafikiri hali zao zitakuwa bora miaka kumi ijayo, kwa mujibu wa ripoti ya taasisi ya Twaweza pamoja na Jumuiya ya Maendeleo ya Kitaifa (SID).
Kutokana na kukata tama, wananchi wa maeneo mbalimbali wamepoteza hata hamu ya kutumia haki zao za msingi, kama kushiriki katika kuchagua viongozi wao wa ngazio mbalimbali, kwa mujibu wa utafiti huo.
Utafiti huo uliofanywa katika maeneo mbalimbali ya Tanzania Bara mwezi Agosti mwaka huu kwa kuhoji watu 1,408 unaonyesha kwamba Watanzania wanaamini kuwa maisha yao yatakuwa bora mwaka 2015.
Matokeo ya utafiti huo uliopewa jina la ‘Tanzania Ifikapo Mwaka 2025: Je, Watanzania Wana Matarajio Gani na Maisha Yao ya Baadaye?, yamebainisha kuwa kwa kuangalia nchi kwa jumla, wananchi wawili kati ya watatu wanaamini kuwa Tanzania itakuwa mahali pazuri pa kuishi baada ya miaka 10 ijayo.
“Wananchi wa makundi yote bila kujali hali zao za kiuchumi, wanaamini hivyo. Wananchi wenye kipato kikubwa, asilimia 64 na wananchi maskini asilimia 68 wana matumaini na siku zijazo. Watanzania wana matumaini na akiba tuliyonayo kwa ajili ya nchi,” inaeleza taarifa ya matokeo ya utafiti huo.
“Baadhi ya wananchi bado wana wasiwasi na karibu mwananchi mmoja kati ya watano anahofia maisha yake yatakuwa mabaya zaidi mwaka 2025 kuliko yalivyo leo, na wapo wengine wanaodhani nchi itakuwa mahali pabaya pa kuishi mwaka 2025.
“Kuna baadhi ya tofauti kati ya matajiri na maskini, mwananchi mmoja kati ya wanne katika kundi la matajiri na mmoja kati ya watano katika kundi la maskini hawana matumaini ya siku zijazo.”
Utafiti huo unaendelea kueleza kuwa, wananchi tisa kati ya 10 wanaamini kuwa viongozi (asilimia 54) au wananchi (asilimia 37) watakuwa na udhibiti zaidi wa maamuzi ya nchi yao, lakini linapokuja suala la maisha yao wenyewe, wananchi wanaamini jitihada zao wenyewe kuwa ndizo zitazobadilisha maisha yao.
Wananchi sita kati ya kumi, wanafikiri kuwa wao wenyewe ndio w enye ushawishi zaidi juu ya hatma yao ya baadaye wakati mwananchi mmoja kati ya watano anaamini kuwa Serikali itakuwa na ushawishi mkubwa juu ya ustawi wa maisha yao ya baadaye.
Hata hivyo, katika utafiti huo, hakuna hata mwananchi mmoja wa mjini aliyetaja Serikali kama ina ushawishi muhimu. Mbali na wao wenyewe, wahojiwa wa mijini walitaja familia zao na marafiki au wenzao kuwa wenye ushawishi kuhusu ya maisha yao ya baadaye.
Akizungumzia matokeo ya utafiti huo, mkurugenzi wa SID, Aidan Eyakuze alisema: “Watanzania kwa kiasi kikubwa wana matumaini na maisha yao binafsi ya baadaye, hasa ikilinganishwa na wenzao kutoka nchi zenye maendeleo makubwa kiuchumi, Marekani na Ulaya.
“Matumaini haya na mtazamo chanya ni mtaji mkubwa. Vinaimarisha uwezo wa nchi kusonga mbele kwa kujiamini na pia inaweka mzigo kwa kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa tunafikia malengo ya mafanikio kwa nchi yetu.”
Kwa upande wake, mkurugenzi mkuu wa Twaweza, Rakesh Rajani, alisema: “Katika kipindi cha mabadiliko muhimu ya kitaifa na ya kimataifa, wananchi wa matabaka yote kiuchumi, maeneo na jinsia zote, wana matumaini ya kile kilichopo siku za baadaye nchini Tanzania.
“Changamoto kwa Serikali, wasomi wa ndani pamoja na wananchi wenyewe, ni kuhakikisha kuwa matumaini haya yanaendelezwa kupitia utungaji sera na utekelezaji wenye ufanisi, kuhimiza maendeleo yenye usawa na kujenga mshikamano wa kijamii, ili matarajio ya wananchi ya maisha bora siku zijazo yafikiwe.”
Akiwasilisha matokeo ya utafiti huo, Mtafiri Elvis Mushi wa Twaweza alisema mtazamo huo ni tofauti kabisa na ule wa nchi za Marekani na Ulaya ambapo karibu wananchi saba kati ya kumi ambao ni asilimia 65, wanafikiri kuwa watoto wao watakuwa na hali mbaya zaidi kifedha kuliko walivyo wao sasa.
Hata hivyo, Mtafiti kutoka SID, Edmund Matotay alisema utafiti walioufanya na kulinganisha na nchi nyingine za Afrika Mashariki unaonyesha kwamba uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi nzuri zaidi kwa sasa kuliko nchi nyingine, huku sekta ya huduma ikishika kasi zaidi ya sekta za uzalishaji na kilimo.

No comments: