Dar es Salaam. Zaidi ya nusu ya Watanzania wamekata tamaa ya
maisha, badala yake wanafikiri hali zao zitakuwa bora miaka kumi ijayo,
kwa mujibu wa ripoti ya taasisi ya Twaweza pamoja na Jumuiya ya
Maendeleo ya Kitaifa (SID).
Kutokana na kukata tama, wananchi wa maeneo
mbalimbali wamepoteza hata hamu ya kutumia haki zao za msingi, kama
kushiriki katika kuchagua viongozi wao wa ngazio mbalimbali, kwa mujibu
wa utafiti huo.
Utafiti huo uliofanywa katika maeneo mbalimbali ya
Tanzania Bara mwezi Agosti mwaka huu kwa kuhoji watu 1,408 unaonyesha
kwamba Watanzania wanaamini kuwa maisha yao yatakuwa bora mwaka 2015.
Matokeo ya utafiti huo uliopewa jina la ‘Tanzania
Ifikapo Mwaka 2025: Je, Watanzania Wana Matarajio Gani na Maisha Yao ya
Baadaye?, yamebainisha kuwa kwa kuangalia nchi kwa jumla, wananchi
wawili kati ya watatu wanaamini kuwa Tanzania itakuwa mahali pazuri pa
kuishi baada ya miaka 10 ijayo.
“Wananchi wa makundi yote bila kujali hali zao za
kiuchumi, wanaamini hivyo. Wananchi wenye kipato kikubwa, asilimia 64 na
wananchi maskini asilimia 68 wana matumaini na siku zijazo. Watanzania
wana matumaini na akiba tuliyonayo kwa ajili ya nchi,” inaeleza taarifa
ya matokeo ya utafiti huo.
“Baadhi ya wananchi bado wana wasiwasi na karibu
mwananchi mmoja kati ya watano anahofia maisha yake yatakuwa mabaya
zaidi mwaka 2025 kuliko yalivyo leo, na wapo wengine wanaodhani nchi
itakuwa mahali pabaya pa kuishi mwaka 2025.
“Kuna baadhi ya tofauti kati ya matajiri na
maskini, mwananchi mmoja kati ya wanne katika kundi la matajiri na mmoja
kati ya watano katika kundi la maskini hawana matumaini ya siku
zijazo.”
Utafiti huo unaendelea kueleza kuwa, wananchi tisa
kati ya 10 wanaamini kuwa viongozi (asilimia 54) au wananchi (asilimia
37) watakuwa na udhibiti zaidi wa maamuzi ya nchi yao, lakini linapokuja
suala la maisha yao wenyewe, wananchi wanaamini jitihada zao wenyewe
kuwa ndizo zitazobadilisha maisha yao.
Wananchi sita kati ya kumi, wanafikiri kuwa wao
wenyewe ndio w enye ushawishi zaidi juu ya hatma yao ya baadaye wakati
mwananchi mmoja kati ya watano anaamini kuwa Serikali itakuwa na
ushawishi mkubwa juu ya ustawi wa maisha yao ya baadaye.
Hata hivyo, katika utafiti huo, hakuna hata
mwananchi mmoja wa mjini aliyetaja Serikali kama ina ushawishi muhimu.
Mbali na wao wenyewe, wahojiwa wa mijini walitaja familia zao na
marafiki au wenzao kuwa wenye ushawishi kuhusu ya maisha yao ya baadaye.
Akizungumzia matokeo ya utafiti huo, mkurugenzi wa
SID, Aidan Eyakuze alisema: “Watanzania kwa kiasi kikubwa wana
matumaini na maisha yao binafsi ya baadaye, hasa ikilinganishwa na
wenzao kutoka nchi zenye maendeleo makubwa kiuchumi, Marekani na Ulaya.
“Matumaini haya na mtazamo chanya ni mtaji mkubwa.
Vinaimarisha uwezo wa nchi kusonga mbele kwa kujiamini na pia inaweka
mzigo kwa kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa tunafikia malengo ya
mafanikio kwa nchi yetu.”
Kwa upande wake, mkurugenzi mkuu wa Twaweza, Rakesh Rajani,
alisema: “Katika kipindi cha mabadiliko muhimu ya kitaifa na ya
kimataifa, wananchi wa matabaka yote kiuchumi, maeneo na jinsia zote,
wana matumaini ya kile kilichopo siku za baadaye nchini Tanzania.
“Changamoto kwa Serikali, wasomi wa ndani pamoja
na wananchi wenyewe, ni kuhakikisha kuwa matumaini haya yanaendelezwa
kupitia utungaji sera na utekelezaji wenye ufanisi, kuhimiza maendeleo
yenye usawa na kujenga mshikamano wa kijamii, ili matarajio ya wananchi
ya maisha bora siku zijazo yafikiwe.”
Akiwasilisha matokeo ya utafiti huo, Mtafiri Elvis
Mushi wa Twaweza alisema mtazamo huo ni tofauti kabisa na ule wa nchi
za Marekani na Ulaya ambapo karibu wananchi saba kati ya kumi ambao ni
asilimia 65, wanafikiri kuwa watoto wao watakuwa na hali mbaya zaidi
kifedha kuliko walivyo wao sasa.
Hata hivyo, Mtafiti kutoka SID, Edmund Matotay
alisema utafiti walioufanya na kulinganisha na nchi nyingine za Afrika
Mashariki unaonyesha kwamba uchumi wa Tanzania unakua kwa kasi nzuri
zaidi kwa sasa kuliko nchi nyingine, huku sekta ya huduma ikishika kasi
zaidi ya sekta za uzalishaji na kilimo.

No comments:
Post a Comment