Friday, 5 December 2014

Mbowe: Tutazuia uchaguzi wa Mitaa mahakamani ikiwa...

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema kama hali ya kuwaengua wagombea wa chama hicho katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa itaendelea kama ilivyo sasa, basi wataupinga uchaguzi huo mahakamani.
Mbowe alisema hayo jana katika mkutano wa hadhara wa operesheni mshikemshike mzizima uliofanyika Vijibweni Kigamboni.
“Tangu kampeni zianze kumekuwa na tabia ya kuengua wagombea wetu kiholela. Tumeshaweka angalizo mahakamani na kama hali ikiendelea hivyo tutaupinga uchaguzi mahakamani.”
Alisema baada ya kuibuka kwa tabia ya wagombea kuenguliwa aliwasiliana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akimsihi alitizame kwa kina suala hilo kwa sababu wagombea walienguliwa kimakosa.
“Alisema atalifanyia kazi lakini naona bado hali hiyo inaendelea na alisema atazungumza na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kuhusu jambo hili.
Nilipowasiliana naye mara ya pili alisema kama tunataka ushindi uchaguzi uwe wa haki. Kuona hivyo tumekwenda kutoa angalizo mahakamani,” alisema.
Aliongeza, “Tukutane katika uchaguzi na tuone nani ni bingwa kati ya CCM na Ukawa baada ya kutumia njia za mkato kama wao wanavyofanya.
Hata sisi hatutaki ushindi wa dezo ila wakitumia dola kutuyumbisha kamwe hatutokubali maana polisi wamekuwa wakitumika kama mawakala wa uchaguzi. Hilo halitakubalika.”
Aliwataka wananchi kutokaa mbali na vituo vya kupigia kura mara baada ya kuwachagua viongozi wanaowataka huku akisisitiza, “Msikubali kura zikahesabiwe sehemu nyingine watazichakachua.
Hata katika sheria za Uchaguzi hakuna sehemu inayosema baada ya kupiga kura, mpigakura anatakiwa kukaa umbali wa mita 100 kutoka katika kituo cha kupiga kura. Tumeweka mawakala nchi nzima kuhakikisha kila kitu kinakuwa sawa.”
Alisema hakuna dhambi mbaya kama wananchi kushindwa kuleta mapinduzi ndani ya nchi yao, hasa nchi kama Tanzania ambayo ina kila aina ya umasikini.

IPTL yazua Kizaazaa Mahakamani

Dar es Salaam. Kampuni za Pan Africa Power Solution Tanzania Limited (PAP) na Independent Power Tanzania Ltd (IPTL), zimewasilisha maombi ya kutaka Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato (TRA) akamatwe kwa kukiuka amri ya Bodi ya Rufaa za Kodi (TRAB) kwa kufuta Hati za Malipo ya Kodi za Mauzo ya Hisa (Capital Gain Certificate).
Kampuni hizo mbili, ambazo ziko kwenye mgogoro wa umiliki, ndizo zinahusika kwenye sakata la uchotwaji wa Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow iliyofunguliwa kuhifadhi fedha za malipo ya tozo ya kuuza umeme unaofuliwa na IPTL, kwa Shirika la Umeme (Tanesco), wakati wa kusubiri uamuzi wa mahakama katika kesi ya kupinga tozo hilo.
PAP, ambayo inadai imenunua hisa zote za IPTL, ndiyo iliyolipwa fedha zote zilizokuwa kwenye akaunti hiyo na kuamsha mjadala mkubwa bungeni ulioisha kwa Bunge kufikia uamuzi wa kuwawajibisha kisheria wote waliohusika, wakiwemo mawaziri.
Lakini uamuzi huo wa Bunge haukuwa tamati la sakata hilo baada ya kampuni hizo mbili kukata rufaa TRAB dhidi ya Kamishna wa TRA na Msajili wa Kampuni na Leseni (Brela) zikipinga kusudio la kufuta hati hizo.
Jana kampuni hizo mbili ziliwasilisha maombi ya hati ya kutaka Kamishna Mkuu wa TRA akamatwe, zikidai kuwa amepuuza amri hiyo iliyomzuia kutekeleza azma yake ya kufuta Hati za Malipo ya Kodi ya Mauzo ya Hisa.
Katika maombi hayo walalamikaji hao wanadai kuwa licha ya TRAB kutoa zuio hilo Novemba 26, 2014, Kamishna Mkuu wa TRA, ambaye ni mlalamikiwa wa kwanza, alitoa amri ya kuziondoa hati hizo siku iliyofuata, yaani Novemba 27, 2014, bila kujali amri hiyo.
Walalamikaji hao pia wanaiomba TRAB, baada ya kumkamata Kamishna Mkuu wa TRA, itoe amri afungwe kwa kudharau amri halali iliyotolewa na bodi na pia imwamuru akidhi matakwa ya amri ya TRAB ya Novemba 26.
Pia walalamikaji hao wanaiomba TRAB imwamuru mlalamikiwa huyo, kulipa gharama za uendeshaji wa shauri hilo pamoja na amri nyingine ambazo itaona kuwa zinafaa.
Maombi hayo ya PAP na IPTL ya hati ya kumkamata na kuamuru Kamishna Mkuu wa TRA afungwe yamepangwa kusikilizwa leo na Katibu wa TRAB, Respicius Mwijage.
Hati ya kiapo inayounga mkono maombi hayo inaeleza kuwa mlalamikiwa, akiwa ni raia wa Tanzania, siyo tu kwamba alipaswa kuwa mtiifu kwa mamlaka ya bodi hiyo, bali pia alipaswa kutekeleza sheria za nchi ambazo bodi hiyo ni sehemu yake.
Hati hiyo ya kiapo ya mkurugenzi wa operesheni wa IPTL, Parthiban Chandrasakaran, inaeleza kuwa kwa kitendo hicho cha kutotii amri ya bodi hiyo, mlalamikiwa amepoteza sifa ya kuwa mtumishi wa umma katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Pia inaelea kuwa kama bodi hiyo isipotumia mamlaka yake kukubali maombi hayo ya kutoa amri inayoombwa, basi walalamikaji watapata hasara isiyoweza kufidiwa.
Inafafanua hasara hizo kuwa ni pamoja na kodi nyingine ambazo tayari PAP wamelipa TRA kwa ajili ya kuendesha biashara.
Pia hati hiyo ya kiapo inafafanua kuwa kuondolewa kwa hati hizo kutahatarisha biashara ya walalamikaji ambayo wamekuwa wakiiendesha tangu walipota hati hizo.
Inaendelea kueleza kuwa kwa kuwa walalamikaji wako katika hatari ya kuvunja mkataba na Shirika la Umeme (Tanesco), na wadau wengine, jambo hilo litasabaisha vita ya kimahakama na hivyo kulipa fidia zisizo za msingi.
Hati hizo namba 004965600 na 0049657 zilitolewa na TRA Desemba 23, 2013, kwa ajili ya uuzaji wa hisa baina ya kampuni ya Mechmar Corporation (Malaysia) Berhard iliyokuwa ikimiliki asilimia 70 ya hisa za IPTL na Piper Links Investment Limited na kati ya Piper Link na PAP.
Hata hivyo baadaye, Novemba 19, 2014 TRA ilitoa taarifa ya siku sita kwa Brela ikionyesha kusudio la kuziondoa hati hizo kwa madai kuwa mkataba wa madai ya mauzo ya hisa hizo ulikuwa ni mkataba wa makubaliano ya uongo.
Wakati Huohuo Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema kitendo cha kushindwa kuwachukulia hatua wanaotuhumiwa kuchota Sh306 bilioni katika Akaunti ya Tegeta Escrow hadi sasa, ni ishara ya kuwa na Serikali dhaifu.
Mbowe, ambaye ni kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alisema viongozi waliotuhumiwa kwenye kashfa hiyo walitakiwa wawekwe kando kabla ya hatua zaidi.
“Leo (jana) ni siku ya tano na Rais Kikwete ameshindwa kutoa uamuzi wowote. Hii inaonyesha jinsi tulivyo na Serikali dhaifu,” alisema Mbowe wakati akihutubia mkutano wa kampeni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwenye Kata ya Vijibweni, Kigamboni.
“Hadi leo Waziri wa Ardhi, Profesa Anna Tibaijuka bado yupo ofisini na anasaini nyaraka mbalimbali za viwanja. Inakuwaje hadi leo wezi bado wapo ofisini?”
, kwanini wanalindwa?” alihoji.
“Wanapewa muda wa kukaa ofisini kujipanga ili hata Rais Kikwete atakapochukua uamuzi, wawe wamejipanga na kuchukua kidogo kilichokuwepo.”
Mbowe alisema sakata la Escrow lilitikisa nchi na kwamba kitendo cha watuhumiwa kutochukuliwa hatua hadi leo tafsiri yake ni kwamba viongozi wa Serikali wanalindana.

Sunday, 30 November 2014

Kama mnalitafuta joka basi huyu escrow ni yai tena moja tu!

Hatupaswi kufurahia kushughulika na matokeo bali uhodari wetu wa kuzuia mabalaa.
Kama ambavyo Watanzania wengi wiki hii na siku chache zinazokuja mijadala yao imegubikwa na sakata la Akaunti ya Escrow na tuhuma za ukwapuaji wa mabilioni ya pesa za Watanzania na mimi nitumie fursa hii kujadiliana nanyi kuhusu nafasi ya Katiba katika kuzuia ubadhirifu wa mali ya umma.
Kwa namna ninavyoona mambo yanakwenda Watanzania tusipokuwa makini tutakuwa watu wa matukio, watu wanaoendeshwa kwa matukio, kama tukikubali hali hiyo itakuwa jambo baya sana kwa taifa letu. Matukio kama haya huwa ni matokeo ya chanzo fulani, matukio haya huwa ni chanzo cha udhaifu wa mifumo yetu ya udhibiti pahala fulani. Kwa sababu haiwezekani jambo likishatokea ndio tuulizane ilikuwa kuwa vipi, nafuatilia mjadala wa Bunge ninaona kila anayezungumza ama anasema mtu au taasisi fulani alipaswa kujua.
Haya mambo hayakufanyika kwa kutumia mbinu za kijasusi, mbinu ambazo hutumia intelijensia ya hali ya juu kiasi kwamba hata kama ulikuwa mlinzi anayelinda lango lakini mtu akapita katika lango hilo pasina kuonekana. Jambo linaloendelea kujadiliwa bungeni wala halikutokea kwa kificho au kutumia intelijensia ya hali ya juu kufanya wanaotuhumiwa kutenda wasijulikane kwa namna yoyote, la hasha.
Hii inanipeleka katika hoja nyingine kwamba, unapoona katika nchi yenye utawala wa sheria, mchana kweupe mambo makubwa na ya kutisha hasa yale yenye nasaba na ubadhirifu wa mali ya umma yanafanyika mchana kweupe basi hatupaswi kusubiri kuona mawingu kujua mvua itanyesha.
Ninayaandika haya kwa maana ya kujifunza, hata kama tungepata Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wazuri kiasi gani, kama mifumo ya utawala wa nchi haijashonwa vema na kwa umadhubuti kikatiba kazi yao njema ingeishia katika jitihada zao za kibinadamu na kukosa usaidizi wa mifumo na taasisi za kikatiba. Binadamu kwa asili amekuwa kiumbe ambaye bila kujitungia kanuni huwa ni msumbufu kabisa, hata kama binadamu ni mwema kiasi gani, iwapo ataishi katika mazingira yasiyo na kanuni basi wema wake utakuwa hatarini kughiribika.
Katika ulimwengu wa leo utaratibu wa kuenenda katika jamii na Taifa lolote lile ni Katiba na sisi tumeamua kuandika Katiba Mpya na Bora. Ni Katiba Mpya na Bora ndiyo pekee inaweza kuwa silaha ya mwisho kuliangamiza joka ambalo limekuwa likitaga mayai kama vile Epa, Majengo ya Benki Kuu, Richmond na haya ni mayai ambayo tumeyaokota kweupe, bado hatuna hakika ya mayai ambayo joka ameyataga kwenye mashimo, vichakani na mayai ambayo joka huenda akayataga hivi karibuni tena. Sumu ya joka ni Katiba Mpya ambayo inatuwezesha wananchi kutumia mamlaka yetu kuiwajibisha Serikali, Bunge na Mahakama. Nchi ambazo zilipuuza kushughulika na joka kikatiba zimeishia kuwa mataifa yaliyoshindwa “failed states”. Tusikubali kufika huko.
Matukio ya escrow na Katiba
Nitumie pia fursa hii kutoa rai yangu kwa Watanzania kwamba, kuwa na Katiba Bora na inayotungwa na wananchi ndiyo mwarobaini wa kuziba mianya ya ubadhirifu katika Taifa letu. Kuwa na Katiba Bora ndiyo itakuwa salama yetu katika kuona wale tuliowapa dhamana wanawajibika haraka iwezekanavyo pindi tuhuma za ubadhirifu zinapotokea katika maeneo na mamlaka yao.
Sikiliza na usome pia, kwa namna ambavyo mjadala wa sakata hili umejipambanua katika Bunge letu la Jamhuri je, unadhani, viongozi wetu hawa watadiriki kwenda kutunga masharti makali na magumu ya kuwawajibisha viongozi wanafanya ubadhirifu wa mali ya umma, ilhali wao wenyewe ni viongozi wa umma wakati huo?
Nikuoneshe kidogo Rasimu ya Warioba ilisema hivi katika suala la Maadili na Miiko ya Viongozi na Watumishi wa Umma, akiwa katika kazi za ofisi au kazi binafsi au wakati amejumuika na watu wengine, atahakikisha kwamba mwenendo wake: hauruhusu kutokea mgongano wa masilahi kati ya masilahi binafsi na maslahi ya utumishi wa umma; hauhatarishi masilahi ya umma kwa ajili ya masilahi binafsi; au haushushi hadhi ya ofisi anayofanyia kazi. (2) Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (1), mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa sheria utakaowezesha Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji kusimamia utekelezaji wa masharti yanayohusu kanuni za uongozi wa umma. (3) Wadhifa wa “Kiongozi wa umma” kama ulivyotumika katika Sehemu hii utajumuisha viongozi wa kuchaguliwa (hii inamaanisha Rais, makamu wa rais, wabunge, madiwani n.k) na kuteuliwa (Mfano, mawaziri, manaibu waziri, makatibu wakuu na manaibu wao, wakurugenzi wa idara za Serikali n.k) kama watakavyoainishwa kwenye sheria za nchi.
Ibara hii pamoja na mambo mengine imefutiliwa mbali na Katiba Inayopendekezwa na zaidi ya yote masharti yake mahususi yakielekezwa kutungiwa sheria na Bunge. Hebu nikuulize tena, juzi ijumaa Bunge ilibidi liahirishwe baada ya wabunge kushindwa kutengeneza sentensi ya pendekezo la hatua za kuchukuliwa kwa wale ambayo wanatuhumiwa katika sakata la escrow, unadhani wabunge hawa watakaa na kutunga masharti mahususi na makali yatakayowabana na kuwawajibisha wao dhidi ya ubadhirifu ambao huenda baadhi yako wakaja kuufanya hapo baadaye? Jambo la kuhuzunisha zaidi hata ile Ibara ndogo ya 2 inayosema Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji kusimamia utekelezaji wa masharti yanayohusu kanuni za uongozi wa umma hakuna tena.
Yaani tunarudi kule kule ambako Secretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma isiyo na meno ambayo wananchi waliipigia kelele sana kwamba kuna tuhuma nyingi kuliko masuala yanayoshughulikiwa na sekretarieti hiyo na hasa hasa wananchi wakaweka msisitizo kwa wale watuhumiwa wakubwa wakubwa. 
Matukio ya escrow na maadili
Masharti mahususi yafuatayo kuanzia 203(2)(b)(e) hadi (o) yamefutwa kutoka katika Rasimu ya Warioba na hayamo katika Katiba Inayopendekezwa.
(2) Bila ya kuathiri masharti ya jumla ya ibara ndogo ya (1), majukumu mahususi ya Tume yatakuwa ni: (b) kufanya upekuzi kwa kushirikiana na taasisi nyingine; (e) kutoa ushauri juu ya masuala ya ubadhirifu wa fedha kwa mamlaka husika; (f) kufanya upekuzi kwa kiongozi wa umma anayepewa dhamana kabla ya kuingia madarakani; (g) kutoa elimu kwa umma kuhusu maadili na miiko ya viongoziwa umma; (h) kufanya uchunguzi kwa uamuzi yake yenyewe, au baada yakupokea malalamiko kutoka kwa mtu yeyote, kutokana nakutenda au kutokutenda kwa kiongozi wa umma au mtumishi (i) yeyote wa umma, au wakala wa Serikali, ikiwa kitendo kilichotendwa au kutokutendwa ni kinyume cha maadili ya umma; (j) kumwelekeza, baada ya kupata malalamiko au itakapoona inafaa, kiongozi wa umma au mtumishi wa umma, taasisi auwakala wa serikali au chombo chochote cha umma kufanya jambo lolote linalotakiwa na sheria, kuacha, kuzuia au kusahihisha utendaji mbaya au usiyo sahihi wa majukumu yake;
(k) kutoa ushauri kuhusu kuchukuliwa hatua kiongozi wa umma au mtumishi wa umma; (l) kumwelekeza kiongozi wa umma au mtumishi wa umma, kwa mujibu wa sheria za nchi, kutoa nyaraka zinazohusiana na matumizi ya ofisi, matumizi ya fedha au mali za umma, au kutoa taarifa ya matumizi mabaya kwa Tume, kwa hatua stahiki; (m) kuomba msaada au taarifa muhimu kutoka kwa mamlaka yoyote ya Serikali au binafsi katika kutekeleza wajibu wake,na kukagua kumbukumbu muhimu na nyaraka husika; (n) kwa kuzingatia sheria, kutangaza kwa umma, mambo yote yanayohusiana na uchunguzi uliofanywa na Tume, iwapo mazingira yanaruhusu; (o) kuchunguza jambo au mazingira yoyote yanayokiuka au kusababisha ukiukaji wa maadili.
Ninapofuatilia sakata hili sishangai sana kwanini masharti haya mahususi yameondolewa na badala yake Katiba Inayopendekezwa ikasema katika ibara yake ya 231(3) kwamba “Bunge litatunga sheria kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya Ibara hii”.
Mtu yeyote mwenye mapenzi mema na nchi yetu na anayependa kuona tunasifika kwa vivutio vya kitalii na siyo ufisadi kwa hakika atahakikisha Katiba Inayopendekezwa inaboreshwa na kurudisha masharti haya muhimu. Aidha, ikumbukwe kwamba ili Katiba Inayopendekezwa iboreshwe Sheria ya Kura ya Maoni inasema katika kifungu chake cha 35, kwamba Katiba Inayopendekezwa ikipata kura za “hapana” itakuwa ni fursa ya kuiboresha kabla haijapelekwa katika duru ya pili ya Kura ya Maoni.

Tumejifunza nini kutokana na kashfa hizi?

Tanzania imekumbwa na kashfa nyingi kubwa tangu ipate uhuru wake.
Kashfa hizi mbali ya kulitikisa taifa zimeliachia taifa maumivu makali ya upotevu wa fedha na kusababisha baadhi ya mawaziri na viongozi wa juu wa Serikali kung’olewa.
Kuanzia awamu ya kwanza ya Mwalimu Julius Nyerere aliyeiongoza nchi tangu mwaka 1961 ilipopata uhuru hadi 1986, Rais Ali Hassan Mwinyi (1986-1995), Rais Benjamin Mkapa (1995-2005) na Rais Jakaya Kikwete (2005-hadi sasa), kashfa zilizoitikisa nchini ni pamoja na Operesheni Uhujumu Uchumi, ufisadi katika Mfuko wa Kuwezesha Uagizaji Bidhaa kutoka Nje ya Nchi (Commodity Import Support – CIS) na Kashfa ya Rada.
Nyingine ni ufisadi Akaunti ya Epa, Kashfa ya Richmond, Operesheni Tokomeza Ujangili na hii ya sasa ya uchotaji mabilioni katika Akaunti ya Escrow.
Kwa hakika, kashfa hizi ni nyingi mno, ambazo zinatakiwa kutupa funzo la kudhibiti mianya ya kutokea kashfa nyingine.
Hata hivyo, inavyoonekana hatujajifunza kitu mbali ya kutokea kashfa hizo. Hii inadhihirishwa na jinsi kashfa ya escrow ilivyoshughulikiwa na Bunge letu.
Kama kuna kitendo cha aibu ambacho Bunge letu linakifanya mjini Dodoma ni kile kilichofanyika Ijumaa usiku cha baadhi ya wabunge na kiti cha Spika kuonyesha kuwalinda watuhumiwa wa kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow.
Ilikuwa inashangaza kuona baadhi ya wabunge ambao wananchi wamewapa dhamana ya kuwawakilisha katika chombo hicho kikuu cha uamuzi, wakijadili kashfa hiyo kwa itikadi za vyama.
Pia, lilichefua zaidi watu wengi waliokuwa wakishuhudia Bunge hilo kupitia redio na televisheni, baada ya baadhi ya wabunge kupendekeza adhabu nyepesi kwa watuhumiwa.
Ilikuwa kama mchezo wa kuingiza kuona mbunge akisema; “Mheshimiwa Spika mtuhumiwa huyu ni mtu mzuri hana ubaya wowote, hivyo naona asichukuliwe hatua.”
Wengine walilazimika kupotosha ukweli ilimradi kuwalinda watuhumiwa kwa madai kwamba fedha zilizochotwa kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow, siyo fedha za umma.
Wabunge wengine wakaenda mbali zaidi ya kueleza kuwa tuhuma za kuwapo wizi wa fedha hizo umeibuliwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe na wapinzani wenzake una lengo baya na Serikali.
Hata, wengine wakafikia mahali pa kusema kuwa wabunge wa CCM ambao watapitisha au kuunga mkono kuchukuliwa hatua kwa Waziri wa Nishati na Madini na watuhumiwa wengine basi siyo wana CCM.
Pia, jambo lingine la kushangaza ni kuona Spika Anne Makinda akimchagua kupendekeza adhabu anayostahili kuchukuliwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakimu Maswi baada ya kubainika kuwa alishindwa kuzuia au alizembea kuishauri Serikali kuhusu kuchotwa kwa fedha za escrow, Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge ambaye naye ni mmoja wa watuhumiwa wa sakata hilo.
Kwa ujumla mambo hayo yote yalivuruga mjadala mzima na kufikia mahali hata Spika Makinda kushindwa kufanya maamuzi yanayotakiwa.
Wabunge wa upinzani waliona wazi kuwa wabunge wa CCM walikuwa wakijaribu kuwalinda watuhumiwa kitu ambacho walikiona hakina tija kwa taifa.
Hali hiyo ndiyo iliyofanya baadhi ya wabunge wa upinzani kusimama na kuimba, kupinga kiti cha Spika kujaribu kuwalinda watuhumiwa.
Nini kimetufikisha hapo? Matukio ya ufisadi yanaongezeka nchini kutokana na Serikali kushindwa kuweka bayana hatua zinazopaswa kuchukuliwa watu wanapatikana na makosa hayo, ili iwe fundisho kwa wengine.
Kila mara wizi wa fedha za umma unapotokea, Serikali hupata kigugumizi kuwawajibisha wahusika, hatua inayowafanya watu wengi kuamini kushindwa kwao kunatokana na woga wa kutekeleza azma zao.
Hakuna uwajibikaji kama mtu kafanya jambo fulani, kuna kulindana sana, lakini kama wote wangechukuliwa hatua za wazi pengine ufisadi usingekuwa wa kiwango cha juu namna hii.
Nadhani kinachotakiwa kufanyika ni wenye dhamana ya kusimamia masilahi ya taifa, wanatakiwa kujitathmini upya.
Nasema wajitathimini upya kwa sababu haiwezekani kila mara nchi iingie katika kashfa ambazo tunaweza kuzizuia.
Kama hatua madhubuti zingeweza kuchukuliwa basi hakuna mtu ambaye angeweza kuingiza nchi katika aibu hii.
Kwa mfano kama waziri fulani angekuwa ameshafungwa miaka kumi jela kwa kuiibia serikali, naamini hakuna kiongozi wa serikali angekuwa na hamu ya kujiingiza katika ubadhirifu wa mali za umma. Kutokana na tabia ya kulindana ambayo ipo hivi sasa kila kiongozi anajua kuwa hata kama atapora mali ya umma sana sana akichukuliwa hatua itakuwa ni kuondolewa madarakani na yeye kubakia akiponda mali aliyoiba.

IPTL yazamisha mawaziri, AG, wabunge

Dodoma. Bunge limehitimisha mjadala wa Kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow kwa kupitisha maazimio manane, likiwamo la kuwawajibisha Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka.
Wengine waliowajibishwa pamoja na mawaziri hao ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) na kuwavua nyazifa zao wenyeviti watatu wa kamati za kudumu za Bunge.
Wenyeviti waliovuliwa nyadhifa zao ni Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Victor Mwambalaswa, Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala, William Ngeleja na Kamati ya Bajeti, Andrew Chenge. Viongozi hao wamevuliwa nyadhifa zao chini ya azimio la Bunge namba mbili.
Maazimio hayo mapya manane yalisomwa bungeni jana jioni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe.
Akizungumza bungeni Zitto alisema, mabilioni ya fedha yaliyotolewa kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow yametumika kuwapa kile kinachoonekana kuwa ni rushwa.
Zitto alisema baadhi ya watu waliochukua fedha hizo ni viongozi wa umma na maofisa wa Serikali kama mawaziri, majaji, wabunge, wenyeviti wa kamati za Bunge, wakuu wa taasisi za umma, viongozi wa dini, mawakili wa kujitegemea na watu binafsi.
“Vitendo vilivyofanywa na watu hawa vinaashiria uzembe na makosa mbalimbali ya jinai kama vile wizi, ubadhilifu kutakatisha fedha haramu, matumizi mabaya ya madaraka, rushwa na kupokea mali ya wizi,” alisema.
Alitaja azimio la kwanza la Bunge ni kulitaka Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na usalama vichukue hatua stahiki kwa mujibu wa sheria za nchi yetu.
Zitto alisema watu wote waliotajwa na taarifa maalumu ya kamati kuhusika na vitendo vyote vya kijinai kuhusiana na miamala ya Akaunti ya Escrow na watu wengine watakaogundulika kufuatia uchunguzi mbalimbali unaoendelea kuhusika katika vitendo hivyo vya jinai, watachukuliwa hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.
Azimio la tatu ni kuzitaka Kamati husika za kudumu za Bunge zichukue hatua za haraka na kwa vyovyote vile kabla ya mkutano wa 18 wa Bunge kuwavua nyazifa zao za wenyeviti wa kamati husika za Bunge. Zitto alitaja azimio la nne ni la kumuomba Rais auende Tume ya kijaji kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya Jaji Aloysius Mujulizi na Jaji Profesa Eudes Ruhangisa wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Alisema utaratibu wa kushughulikia nidhamu za majaji kwa mujibu wa Katiba unamtaka Rais kuunda Tume ya Uchunguzi ya Kijaji, kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya majaji.
Pia azimio la tano ni mamlaka husika za kifedha na za kiuchunguzi kuitaja Benki ya Stanbic na benki nyingine yoyote itakayogundulika kufuatia uchunguzi wa mamlaka za kiuchunguzi, kujihusisha na utakatishaji wa fedha zilizotolewa katika Akaunti ya Escrow, kuwa taasisi zenye shaka ya utakatishaji wa fedha haramu.
Azimio la sita alilitaja Zitto kuwa ni kuiomba Serikali iandae na kuwasilisha Muswada wa Marekebisho ya Sheria iliyounda Takukuru kwa lengo la kuanzisha taasisi mahususi itakayoshughulikia, kupambana na kudhibiti vitendo vya rushwa kubwa, ufisadi na hujuma za uchumi zinazotishia uhai wa taifa kiuchumi, kijamii na kisasa.
Alisema azimio la saba la Bunge ni kuitaka Serikali iangalie uwezekano wa kununua mitambo ya kufua umeme ya IPTL na kuimilikisha kwa Tanesco kwa lengo la kuokoa fedha za shirika hilo.
Katika azimio lake la nane Bunge liliazimia kwamba Serikali itekeleze azimio husika la Bunge mapema iwezekanavyo na kwa vyovyote vile kabla ya kumalizika kwa mkutano wa Bunge la Bajeti Serikali iwasilishe taarifa ya utekelezaji wa mapitio ya mikataba ya umeme.
Mbowe, Filikunjombe, Wassira
Wakichangia mapendekezo hayo mapya yaliyosomwa na Zitto, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe alisema wamekubaliana na mapendekezo hayo mapya manane yanayotosha kufikisha ujumbe.
Alisema ni muhimu viongozi wa Serikali wakalinda rasilimali za nchi kwa kutekeleza wajibu wao wakijua Watanzania wengi masikini wanawategemea wao kuwatoa kwenye umaskini.
“Niombe tu Waziri Mkuu awe mkali ili tusifike kwenye mshike mshike kama huu tuliofikia kwa sasa,” alisema Mbowe na kuongeza: “Waziri Mkuu uwe mkali kwa kweli.”
Mbunge wa Ludewa (CCM), Deo Filikunjombe ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) alilishukuru Bunge kwa kufanya kazi yake akieleza kuwa limeweka maslahi ya nchi kwa kushikana pamoja.
“Kumekuwa na makosa yamefanyika kwenye baadhi ya maeneo, hivyo hatua zimechukuliwa,” alisema Filikunjombe.
Alisema anafurahi kwamba hatua stahiki zimechukuliwa kwa waliohusika.
“Sasa hatua stahiki zitachukuliwa kwa kila mmoja kwa nafasi yake,” alisema.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu, Stephen Wasira alisema juzi hali ilikuwa mbaya, lakini wameweza kuridhiana kwa kuwa wote ni binadamu.
Alisema mtafaruku uliotokea umewafundisha kwamba wanaweza kukubaliana wakijadiliana.
“Kazi haikuwa rahisi, lakini tumeelewana na aliyosema Zitto ndiyo tuliyokubaliana kwa kuwa CCM haina sera ya kukubali jambo lolote ambalo linaminya maendeleo ya wananchi,” alisema.
Alisema Serikali ina wajibu wa kutekeleza maazimio ya Bunge hivyo yanayowagusa wenzao ndani ya Serikali watawajibika kwa kuwa ndiyo wajibu.
“Sasa hivi kila mhimili umeguswa hivyo tutatekeleza,” alisema Wasira.
Spika Anne Makinda aliwaonya wabunge kuachana na watu wenye fedha wanaotoa kwa lengo la kuwahonga, kwani zitawaweke pabaya kwa kuwa hawana kinga za makosa ya jinai.
Bunge laendelea jana asubuhi
Baada ya juzi Spika Makinda kuahirisha Bunge kwa kushindwa kufikia mwafaka, jana Bunge liliendelea asubuhi, lakini baada ya wabunge kuingia Spika alitangaza kuahirisha Bunge hadi saa tano asubuhi ili vyama vikafanye vikao kwa ajili ya kutafuta suluhu ni maneno gani yatumike katika mapendekezo ya Kamati ya PAC yanayotaka kuwang’oa vigogo wote wa Serikali wanaotuhumiwa kuhusika na sakata hilo.
Wakati Spika akitoa maelekezo hayo tayari asubuhi na mapema wabunge wa Kambi ya Upinzani walioungana wote walikuwa wameshakutana kwenye Ukumbi wa Msekwa kuweka msimamo kuhusu mapendekezo hayo.
Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini na Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema) Mchungaji Peter Msigwa walisema kuwa kikao chao kiliamua kuwa wasimamie mapendekezo yote yaliyopendekezwa na kamati kama yalivyo na lisibadilishwe hata moja.
Selasini alisema wabunge wa CCM wanachotaka kufanya ni kuwaokoa watuhumiwa, lakini wao wanaingia bungeni na msimamo mmoja wa kutaka mapendekezo yote ya PAC yapite kama yalivyo.
“Wakikataa tutamalizana pale ndani,” alisema Selasini huku Msigwa akisema, “Wanataka kutufanyia uhuni, sisi tunataka mapendekezo yote ya kamati yapite kama yalivyo.”
Wakati upinzani ukiwa na msimamo huo na kuendelea na shughuli zao Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alionekana akizunguka kuwaomba wabunge wa CCM waelekee White House (Makao Makuu ya CCM Dodoma) kwa ajili ya kikao chao.
Hata hivyo, wabunge wengine wa CCM walionekana kutojali kikao hicho huku wakiendelea mazungumzo na wabunge wa upinzani huku wakipongezana na wengine wakikandiana kutokana na jambo lililotokea juzi.
Bunge larejea saa tano na kuahirishwa
Kikao cha Bunge kilirejea jana saa tano baada ya kuahirishwa asubuhi na Spika alimpa nafasi Lukuvi ambaye alitoa hoja ya kuomba Bunge liridhie kuongeza muda wa saa moja kwa ajili ya pande zote mbili kufanya mashauriano na kurudi na kauli moja kama Bunge. “Nilikuwa naomba tuahirishe Bunge kwa saa moja ili tuendelee na mashauriano na kuja na kauli moja,” alisema Lukuvi.
Hoja hiyo ilipingwa na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika aliyesema kuwa haiwezekani wakatoka nje kwenda kwenye mashauriano ya kukubaliana na msimamo wa CCM na kusema ni kauli moja ya Bunge. “Haiwezekani tukatoka na kauli moja kwa kuweka msimamo wa misimamo ya kichama,” alisema Mnyika.
Lukuvi alisimama tena na kusema; “Tumeomba saa moja tuendelee na mashauriano ili tutoke pamoja na siyo suala la vyama hapa. Tunataka tushauriane kama Bunge.”
Baada ya Lukuvi kumaliza, Spika Makinda alisema anatoa muda hadi saa kumi jioni ili viongozi wa upinzani na CCM wakakae ili kushauriana jinsi gani ya kuweza kuja na maneno yanayofaa kwenye mapendekezo yanayofuatia.
Hoja hiyo ilionekana kupingwa na wabunge wakieleza kwamba saa kumi jioni ni mbali hivyo Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe alisimama na kusema kuwa masaa mawili yanatosha kwa mashauriano lakini siyo saa moja kama Serikali ilivyoomba.
Spika alimpa nafasi Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia ambaye yeye alipendekeza masaa matatu ili kamati ikae na kuona jinsi gani wataweza kufikia mashauriano yao.
Spika Makinda alisema ni lazima wabunge waelewe kwamba mabunge ya kisasa yakifikia katika hali kama ya jana na juzi, lazima wakutane pande zote na kufanya mashauriano.
“Tuwe Bunge la kisasa lazima tushauriane tunapofika kwenye suala kama hili na hivyo mkutane wote na kukubaliana. Hivyo tukubaliane wakija na kauli moja tunapitisha,” alisema Spika Makinda.
Mbunge wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole Sendeka aligomea kauli hiyo ya Spika na kueleza kuwa anakubali pande zote kutoa watu, lakini hakubaliani kwamba wakija na kauli moja ndiyo ipitishwe.
Kabla Ole Sendeka hajakaa Mbunge wa Nyamagana (Chadema), Ezekiel Wenje alisimama na kusema watu wapewe muda wa kushauriana, hivyo timu iundwe na ikae kwa muda mrefu ili wengine ambao hawatakuwa kwenye kamati hiyo wapate nafasi ya kutaarifiwa juu ya nini kinachoendelea
“Kwa hiyo Spika mimi nakubali turudi saa kumi ili hiyo timu ikakae na sisi kwenye vikao vyetu tupewe taarifa tukifika hapa baadaye tumalizane tu,” alisema Wenje na hoja yake iliungwa mkono na wabunge hivyo Spika Makinda akasema viongozi wote wakae na kuja na kauli moja.
Pia, akitaka Zitto awe na wawakilishi kwa kuwa ndiye mwenye hoja, lakini wale wanaotuhumiwa wasiingie kwenye kamati hiyo. Hivyo akaahirisha Bunge.
Bunge laahirishwa tena saa kumi
Bunge lilirejea tena saa kumi jioni na kuahirishwa baada ya Spika kupewa taarifa kwamba kamati iliyoteuliwa kwa ajili ya mashauriano haijamaliza kazi.
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenister Muhagama alisimama kwa upande wa CCM na kumweleza Spika kuwa corcus yao imeambiwa kwamba bado majadiliano yanaendelea.
“Spika sisi tulituma wawakilishi sita na mpaka sasa tumeambiwa kazi inaendelea lakini sijui kwa wenzetu imekuwaje lakini hadi sasa bado,” alisema Muhagama.
Spika Makinda alipokea taarifa hiyo na kuhoji upande wa upinzani una taarifa gani ambapo Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alisimama na kusema, “Na sisi tumeelezwa kwamba bado.”
Kwa kauli hiyo Spika Makinda aliamua kuahirisha Bunge hadi saa moja jioni na kuwaeleza wabunge kwamba suala hilo lazima limalizike ifikapo saa mbili na robo usiku.
Wabunge walitoka nje na kuendelea na shughuli zao huku wengine wakijikusanya vikundi vikundi wakijadiliana. Wengine waliamua kukaa Kanteen ya Bunge kusikiliza hotuba ya Rais Jakaya Kikwete ambaye amerejea nchini jana akitokea nchini Marekani alikokuwa kwa matibabu ya tezi dume.
Kilichotokea juzi usiku
Juzi Spika Makinda alilazimika kuahirisha Bunge kutokana na wabunge wa Kambi ya Upinzani kugoma kukubali marekebisho ya Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), Andrew Chenge kwamba uamuzi wa kumng’oa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo uachiwe mamlaka iliyomteua.
Chenge alifanya marekebisho akieleza pendekezo la kumng’oa Profesa Muhongo lisomeke kama lile la Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi ambalo Bunge lilipitisha kwamba: “Bunge linaazimia kulifikisha suala hili kwa mamlaka ya uteuzi kwa hatua zaidi.”
Kipengele hicho kilikataliwa na upinzani na kuamua kusimama wakitaka Profesa Muhongo achukuliwe hatua lakini CCM waligoma ndipo Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe aliposimama na kusema kuwa haiwezekani kamati imependekeza mambo halafu Bunge linataka kuwalinda watuhumiwa.
Mbowe alisema kama Bunge linaamua hivyo wao hawawezi kuwa upande wa uamuzi huo kauli iliyowanyanyua wabunge wote wa upinzani vitini kutaka waondoke, ingawa Spika alimsihi Mbowe kuwatuliza, ilishindikana na Spika kuamua kisitisha Bunge hadi jana.
Jitihada kubwa zilifanyika kuwasihi wabunge wa upinzani kutulia lakini walianza kupiga kelele wakieleza kuwa hawawezi kulinda wezi.
Spika Makinda kabla ya kuahirisha aliwaeleza wabunge kuwa anapata wakati mgumu kwa kuwa Bunge limekuwa likiingilia shughuli za mihimili mingine na kwamba tayari ana kesi mahakamani kutokana na kuelezwa kuingilia shughuli za mahakama hivyo aliwaomba wabunge waache kutoa maamuzi ambayo yanaingilia mhimili wa Serikali.
“Tayari mimi nina kesi huko katika mhimili mwingine sasa mnataka nigombane tena na Executive (Serikali) itakuwaje jamani naomba tutafute maneno ya kutokuingilia mhimili mwingine,” alisema Spika Makinda.
Maneno yake hayo yalionekana kupuuzwa na wabunge wa upinzani na wengine wa CCM huku wakipiga kelele kuwa ni lazima watuhumiwa waliohusika kwenye sakata la escrow washughulikiwe kama ilivyokuwa kwenye sakata la Operesheni Tokomeza Ujangili.

Wednesday, 26 November 2014

Majina Ya Waliokula Fedha Za Akaunti Ya Escrow Katika Ripoti Ya PAC Iliyosomwa Sasa Bungeni





Zitto: Upande wa viongozi wa kisiasa ambao waliingiziwa fedha katika akaunti zao binafsi ni; Mhe.
Andrew Chenge (Mb)
Zitto: Andrew Chenge aliingiziwa shilingi bilioni 1.6.
Zitto: Mhe. Anna Tibaijuka (Mb) na Waziri wa 62
Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi shilingi bilioni 1.6.
Zitto: Mhe.William Ngeleja (Mb) na ambaye alikuwa Waziri wa Nishati na Madini alipewa shilingi milioni 40.4
Zitto: Ndg. Daniel N. Yona ambaye alikuwa pia Waziri wa Nishati na Madini alipewa shilingi milioni 40.4.
Zitto: Ndg. Paul Kimiti ambaye ni Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Sumbawanga
alipewa shilingi milioni 40.4
Zitto: Dr. Enos S. Bukuku ambaye alikuwa Mjumbe wa Bodi ya TANESCO aliingiziwa shilingi milioni 161.7.
Zitto: Upande wa Majaji Prof. Eudes Ruhangisa, aliingiziwa milioni 404.25 na J.A.K Mujulizi aliingiziwa shilingi milioni 40.4
Zitto: kwa upande wa Watumishi wa umma,Ndg. Philip Saliboko ambaye alikuwa mtumishi wa RITA aliingiziwa
shilingi milioni 40.4
Zitto: Ndg. Emmanuel Daniel Ole Naiko ambaye
alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa (TIC) aliingiziwa shilingi milioni 40.4
Zitto: Ndg. Lucy L. Appollo ambaye ni Mtumishi wa TRA aliingiziwa shilingi milioni 80.8.
Zitto: Viongozi wa Madhehebu ya
Dini walioingiziwa fedha na Benki ya Mkombozi ni Askofu 63
Methodius Kilaini shilingi 80.9
Zitto: Askofu Eusebius Nzigirwa shilingi milioni 40.4 na Mchungaji Alphonce Twimann Ye Simon shilingi milioni 40.4.
Zitto: Watu walienda kugawana fedha kwenye Benki tajwa wakiwa na mifuko ya rambo, sandarusi,
mabox, magunia na lumbesa TegetaEscrow
Zitto: Bilioni 73.5
zilitolewa na kugawanywa kwa watu mbalimbali kinyume cha
Sheria ya Benki Kuu na Taasisi za Fedha ya 2006
Zitto: Taarifa
ya benki (bank statements) yenye majina na akaunti zote
zilizoingiziwa fedha zimeambatishwa.
Zitto: Kamati imebaini mawasiliano kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha

Friday, 14 November 2014

Bunge likatae miswada inayominya uhuru wa habari

Dar es Salaam Muungano wa vyama vya siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) huenda ukapata nafasi kubwa katika Uchaguzi Mkuu 2015, utafiti mpya wa Taasisi ya Twaweza umebanisha.
Utafiti huo umebainisha kuwa kuungana kwa vyama hivyo kutaongeza ushindani na kukitisha Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho kina ngome imara. Ukawa inaundwa na vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi, CUF na NLD.
Hata hivyo, takriban nusu ya Watanzania waliohojiwa katika utafiti huo uliowataka kubainisha iwapo upinzani ungesimamisha mgombea mmoja wangemchagua nani, walisema wangeichagua CCM na karibu theluthi moja wangemchagua mgombea wa upinzani iwapo watasimamisha mmoja.
Utafiti huo wa awamu ya 24 ulibainisha kuwa watu wawili kati ya 10 walikuwa tayari kumpigia mgombea badala ya chama wakati mmoja kati ya 10 akisema hajui angempigia nani iwapo upinzani ungemsimamisha mgombea mmoja 2015.
“Kundi lililosema kuwa wangemchagua mgombea wa upinzani lilipoulizwa kuwa nani anapaswa kuwa mgombea urais, watu wanne kati ya 10 (asilimia 41) walimtaja Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa.
“Majina mengine ya viongozi wa upinzani yaliyopata zaidi ya asilimia 10 ni Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kwa asilimia 14 na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akipata asilimia kumi na moja.
Viongozi wengine wa upinzani waliotajwa kuwa wangefaa kugombea urais ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe kwa asilimia sita huku Katibu Mkuu wa CUF ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Shariff Hamad, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, Mwenyekiti wa TLP, Augustino Mrema na Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, wakiambulia asilimia moja kila mmoja.
Pamoja na mapendekezo hayo, bado karibu kila watu wawili kati ya 10 (asilimia 21) walioulizwa swali hilo walisema hawajui ni nani anafaa kugombea urais kupitia upinzani, jambo ambalo linaweza kubadili matokeo hayo kwa urais katika dakika za mwisho.

Bunge likatae miswada inayominya uhuru wa habari

Serikali juzi iliwasilisha bungeni Muswada wa Sheria unaotishia uhuru wa vyombo vya habari, lakini ikauchomoa baadaye jioni baada ya kugundua kwamba umestukiwa na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.
Hatua hiyo ya Serikali ya kuwasilisha Muswada wa Sheria ya Takwimu unaoonekana kulenga kukwamisha vyombo vya habari katika kupata takwimu na kuzitumia katika habari na taarifa zinazotolewa kwa wananchi, imeonekana kwa wengi katika tasnia ya habari kama uthibitisho kwamba pengine Serikali haina dhamira ya kuona wananchi wanapata haki ya kupata habari.
Moja ya kifungu cha muswada huo kilicholalamikiwa na wabunge wengi ni Ibara ya 37 (4), ambacho kinaeleza kwamba wadau na vyombo vya habari vitakavyotoa takwimu bila kibali cha Ofisi ya Takwimu watakwenda jela miaka mitatu pamoja na faini ya Sh10 milioni au vyote kwa pamoja.
Inasikitisha kuona kwamba adhabu hiyo kubwa kupita kiasi imeungwa mkono na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara, ambayo iliwasilisha maoni yake bungeni juzi.
Adhabu ya kosa hilo awali ilikuwa kifungo cha mwaka mmoja, lakini katika hali ya kushangaza Kamati hiyo ilipendekeza iongezwe hadi miaka mitatu eti kuzuia tabia ya baadhi ya watu kutoa takwimu za uongo na kwa makusudi ili kupotosha jamii.
Hakuna anayepinga kuwapo umuhimu wa kuipa mamlaka zaidi na kuiwezesha Ofisi ya Taifa ya Takwimu kutekeleza majukumu yake ya kitakwimu kwa ufanisi, wala hakuna anayepinga uanzishwaji wa mfumo thabiti wa utoaji wa takwimu unaokusudia kuboresha na kuimarisha takwimu rasmi nchini.
Jambo hilo tumekuwa tukilisisitiza mara kwa mara na kwa kweli tunadhani Serikali imechelewa sana kuanza kuchukua hatua.
Hata hivyo, tunadhani Serikali inafanya makosa kudhani kwamba uchapishaji wa takwimu zisizo sahihi unatokana na watu kutaka kupotosha jamii na kuleta machafuko.
Ni kweli kwamba katika mazingira fulani takwimu zisizo sahihi zinaweza kusababisha vurugu, lakini pia lazima tukubali kwamba Serikali yenyewe ndiyo inapaswa kubeba lawama kwa uzagaaji wa takwimu zinazokinzana na zisizo sahihi.
Tangu tupate uhuru Serikali haijawahi siyo tu kuwa na utamaduni wa kuheshimu na kutunza takwimu, bali pia kuweka mazingira ya kuboresha ukusanyaji wa takwimu kwa kuweka mfumo thabiti na kuboresha Ofisi ya Taifa ya Takwimu.
Hivyo kama ni kupotosha takwimu, Serikali ndiyo imekuwa mpotoshaji namba moja. Hii imetokana na kutokuwapo mfumo wa kuainisha takwimu kutoka katika wizara, taasisi za Serikali, sekta ya umma na sekta binafsi kama inavyofanyika katika nchi nyingi duniani. Kwa mfano, hatudhani kama Serikali inazo takwimu sahihi kuhusu Deni la Taifa hivi sasa.
Tunachotaka kusema hapa ni kwamba muswada huo wa Sheria ya Takwimu uliochomolewa bungeni juzi ulilenga kuvibana vyombo vya habari na kuminya uhuru na haki ya wananchi kupata habari.
Kwa miaka minane sasa, Serikali imekuwa ikisuasua kupeleka bungeni Muswada wa Sheria ya Uhuru wa Habari na Vyombo vya Habari, hata baada ya kuihakikishia jumuiya ya kimataifa mara kwa mara kwamba muswada huo ungepelekwa bungeni.
Tunadhani Muswada wa Sheria wa Takwimu ni mwendelezo wa mkakati wa Serikali wa kuvibana vyombo vya habari. Bunge litafanya vyema kuukataa iwapo Serikali itaurudisha ukiwa na maudhui yaleyale yaliyoufanya uchomolewe bungeni juzi.

Mbowe amtaka Kikwete avunje Baraza la Mawaziri

Kigoma. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amemtaka Rais Jakaya Kikwete kulivunja Baraza la Mawaziri na kuunda jipya kutokana na tuhuma za ufisadi.
Katika taarifa yake aliyoitoa jana kwa vyombo vya habari baada ya mikutano yake katika mikoa ya Magharibi alisema ni lazima hatua hiyo kuchukuliwa ili kukabiliana na mafisadi ambao hakuwataja, vinginevyo alisema Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni anayoiongoza, itaanza maandalizi ya kuwasilisha bungeni, hoja ya kutokuwa na imani naye.
Alisema Serikali imekuwa ikishindwa kuchukua hatua za ufisadi ambazo zinawakabili watendaji wake: “Kambi ya Upinzani Bungeni inamtaka Rais Kikwete kumfukuza kazi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na mawaziri wake na kuunda Serikali mpya.”
Hivi karibuni, Mbowe alitoa tuhuma nzito kuhusu ufisadi katika ujenzi na bomba la gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam akisema kuna ufisadi umefanywa na vigogo wa Serikali wakiwamo baadhi ya mawaziri.
Alisema mradi huo ulitakiwa kugharimu Sh1.2 trilioni lakini vigogo hao wakaongeza kiasi kama hicho na sasa unagharimu Sh2.4 trilioni. Alitaka kuteuliwa kwa taasisi ya kimataifa ya ukaguzi ili kufahamu thamani halisi ya ujenzi wa bomba hilo.
Alisema kutokana na ufisadi huo na mwingine katika Akaunti ya Tegeta Escrow, ni dhahiri kuwa Baraza la Mawaziri limeshindwa kazi ya kumsaidia Rais.
Mbowe amnanga Zitto
Katika mkutano wa juzi mjini Kigoma, Mbowe alimzungumzia aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe akisema alimsaidia kuhakikisha anashinda ubunge wa Kigoma Kaskazini mwaka 2005 lakini akakosa shukrani.
Akihutubia mamia ya wakazi wa Kata ya Kalinzi iliyopo katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, Mbowe alisema hamchukii Zitto kama baadhi ya watu wanavyofikiri, bali mbunge huyo alikiuka maadili ya chama hicho akavuliwa uongozi.
“Nilimshauri Zitto Kabwe akagombee katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, lakini akaniambia kwamba hawezi kufanya hivyo kwa sababu hana fedha, nikampa fedha za kutosha, nikampa gari Toyota Hilux la kuzungukia katika jimbo na akawa mbunge.
Alisema gari hilo hajawahi kulirudisha hadi leo na yeye hakumuuliza kwa sababu alimchukulia kama ndugu yake... “Zitto ni kama mdogo wangu, amelala na kula nyumbani kwangu, nyumba yangu ilikuwa kama yake, nashangaa anakosa shukrani.”
Alisema kabla ya kugombea alimlipia nauli kutoka Ujerumani kurudi nchini kwa ajili ya kutafuta nafasi hiyo ya ubunge, hivyo anashangaa mtu wa aina hiyo amchukie kwa lipi.
Mbowe alisema Mkoa wa Kigoma umebahatika kuwa viongozi wa upinzani wenye uwezo lakini wamekuwa wakiwasaliti wananchi wa mkoa huo.
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Zanzibar), Salum Mwalimu alisema uchaguzi wa serikali ya vijiji, mitaa na vitongoji kiwe kipimo cha kuing’oa CCM kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
Aliwataka vijana kufanya uamuzi sahihi kwenye uchaguzi huo kwa kuvichagua vyama vinavyounda Ukawa kwa kuwa CCM imewatelekeza.
Zitto ajibu
Akizungumzia madai ya Mbowe, Zitto alisema ni utoto kwenda kumtangaza kwamba alimsaidia... “Yeye Mbowe anajua nilivyomsaidia pia lakini kwa kuwa nimelelewa kwa maadili mema na wazazi wangu siwezi kumtangaza. Ila muulizeni alikuwa na hali gani baada ya uchaguzi wa mwaka 2005 na nilimsaidia nini?
“Nimeshangazwa na tabia hiyo ya kusimanga tena kunisimanga kwetu, nyumbani kwetu. Hata hivyo, nimepuuza maana kwa vyovyote vile aliongea bila kufikiri.
“Anasema nilitaka kusaliti chama, aseme kwa ushahidi maana kutamka tu hakuna maana kitu hata kidogo.”
Alisema kiongozi mkubwa kama Mbowe anapaswa kujadili masuala ya Taifa na namna ya kutatua changamoto si, kusema watu na kuwasimanga.
“Nimeibadilisha Kigoma na kusimamia ujenzi wa miundombinu ya barabara, madaraja na viwanja vya ndege. Yeye kafanya nini Hai? Nimewezesha wakulima wangu kuwa na hifadhi ya jamii, bima ya afya na kukuza uzalishaji, yeye kafanya nini Hai?
Nimeibua hoja bungeni za maana ikiwamo kubadili sheria kwa manufaa ya nchi. Yeye kafanya nini bungeni tangu aingie, ametoa hoja gani binafsi, ametunga sheria gani binafsi?

Friday, 31 October 2014

Mkapa atoa ya moyoni rais 2015

Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa, amezungumzia mbio za kuwania urais wa 2015 kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), akitaja sifa za mtu anayepaswa kuteuliwa kuwa mgombea wake, ikiwamo ya kukubalika na kuuzika kwa jamii.

Amesema kukubalika na kuuzika kwa mtu katika siasa kunatokana na utendaji, haiba, wasifu na ushawishi wa mtu huyo ndani ya chama na serikalini na kwamba, umri siyo kigezo cha kuangaliwa ingawa siyo dhambi vijana wakajitokeza kujitosa katika kinyang’anyiro hicho.

Mkapa, ambaye anasifika kwa kuwa kiongozi jasiri na asiyemung’unya maneno, alisema hayo wakati akihojiwa na televisheni ya Citizen ya nchini Kenya, kwa njia ya simu.

Alikuwa akihojiwa juu ya kifo cha Rais wa Zambia, hayati Michael Satta, aliyefariki dunia, jijini London, nchini Uingereza Jumanne wiki hii.

Katika mahojiano hayo, Mkapa pia aliulizwa na mwandishi kuhusu Tanzania kutazamiwa kufanya uchaguzi mkuu mwakani huku mambo mengi yakisikika, hasa kwa wanaojitokeza kupitia CCM kutaka kuwania urais katika uchaguzi huo hadi wengine kufikia kuadhibiwa na chama.

Kabla ya kujibu, Mkapa alianza kwa kucheka na kisha akasema anachelea kupata jibu sahihi kuhusiana na swali aliloulizwa na mwandishi.


“…Ila niseme CCM ni chama kikongwe na kina hazina kubwa ya kutosha. Na Katiba ya chama chetu inaelezea kuhusu dhumuni la chama chetu, kubwa ikiwa ni kuhakikisha tunakamata dola, kuanzia serikali za mitaa mpaka serikali kuu. Sasa swali ni kwamba, dola inakamatwaje?” alihoji Mkapa.

Aliongeza: “Chama kama chama lazima muwe na mtu anayeuzika na kukubalika katika jamii kwa utendaji wake, haiba yake, wasifu wake (ndani ya chama na serikali).

“Lakini vile vile, ushawishi wake...Haya mambo ya umri na kadhalika, sisi hatukutazama wakati huo. Ila siyo dhambi vijana wakijitokeza. Maana yake hata wakati wangu, Rais wa sasa Mheshimiwa Kikwete na kina Lowassa walijitokeza. Na leo unaona Kikwete ndiye Rais.”


Alisema wakati wa utawala wake, viongozi wenzake wengi walihisi na kuamini kuwa hakuwa akimuunga mkono Rais Kikwete.

“Lakini mwandishi, nataka nikuhakikishie, hata kama mimi Ben Mkapa siko na Kikwete, mwisho wa siku wanachama ndiyo watakaosema wewe humtaki ila sisi tuachie huyo huyo...,” alisema Mkapa. 

Aliongeza: “Na hayo yalijitokeza mwaka 2005. Watu walimtaka Mheshimiwa Kikwete. Sasa mimi kuwa mwenyekiti wa chama hakunipi Mandate (mamlaka) ya kushindana na walio wengi. Na mliona (Kikwete) alishinda kwa asilimia kubwa kweli kweli”.

“Hivyo CCM ina taratibu zake na wanajua nani anafaa. Maana yake siasa hizi, tuhuma zingine za kipuuzi kweli kweli. Sasa mkiendekeza tuhuma, mwishowe mnakuta mnabaki bila chama. Na kwenye siasa mkianza kutuhumiana, hakuna wa kusimama...”

Alisema yeye binafsi, anaamini chama kitapata mtu safi, mwenye nguvu ya kukisaidia chama na serikali na kuendeleza yatakayoachwa na Rais Kikwete.

Mkapa alisema hakuna chama duniani kinachoona fulani atakivusha halafu kimwache na kusema kufanya hivyo, maana yake ni kukiua chama.

“Hivyo, hata sisi vyombo vyetu vya ndani vilikuwa vinatueleza kabisa kwamba, fulani yuko vizuri sana. Ila labda kuna aka katatizo. Sasa ako katatizo tunakafanyia kazi kwa maslahi ya chama na kwa maslahi ya huyo ajaye,” alisema Mkapa na kuongeza kuwa ana amini ndivyo ilivyo mpaka sasa.

Alisema tafiti zimefanyika na kwamba, anaamini wamesikika watu wakisema wanamtaka nani.

“Na wakati wangu mimi mgombea alikuwa ameshatungiwa nyimbo na watu mbalimbali wenye mapenzi naye. Hivyo, labda hata sasa yaweza kuwa hivyo...Waswahili walisema nyota njema huonekana asubuhi,” alisema Mkapa.

Aliongeza: “Nimalizie kama nilivyosema, ukongwe wa CCM na viongozi wake, naamini watapata mtu bora na mwenye nia njema na Taifa hili...”

Akijibu kuhusu wana CCM waliotajwa kwamba, anaamini yupo mmoja au wawili, ambao ameona wanaweza ama kufuata nyayo zake au za Mwinyi au za Mwalimu Nyerere au za Rais Kikwete, kwanza alianza kwa kucheka.

Baada ya kicheko, Mkapa alisema Tanzania kuna Kamati ya Maadili na kwamba, yeye na wenzake hivi sasa kikatiba ni wazee washauri, hivyo akasema vikao vya chama ndivyo vitakavyowaongoza na baada ya hapo, nao wanaenda na mtu huyo huyo.

Makada wa CCM waliowahi kutuhumiwa kuanza kampeni za kuwania urais mwaka 2015 kabla ya kuzuiwa na chama kupitia Kamati yake Ndogo ya Udhibiti na Nidhamu kujihusisha na suala hilo kwa miezi 12, huku mienendo yao ya kisiasa ikifuatiliwa, ni pamoja na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.

Wengine ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa; Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira.

Yumo pia aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, ambaye ni Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, pia hivi karibuni alikaririwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) akitangaza nia yake ya kuwania urais 2015. Mwingine aliyekwisha kutangaza nia ya kuwania urais mwakani ni Mbunge wa Nzega, Dk. Hamis Kigwangalla.

KUHUSU USHIRIKIANO WA VYAMA VYA UPINZANI (UKAWA)

Akijibu swali kuhusu ushirikiano uliosainiwa na vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD wa kusimamisha mgombea mmoja katika chaguzi, kuanzia ngazi ya serikali ya mtaa hadi urais kama ilivyokuwa kwa Kenya, Mkapa alisema bado hajajua
sera za vyama hivyo na namna makubaliano yao yalivyo.

Alisema pia bado hajaelewa kama inawezekana kuufananisha ushirikiano wa vyama hivyo na muungano wa Coard na Jubilee uliokuwapo nchini Kenya.

“Otherwise I'd like to wish them all the best (vinginevyo ningependa kuwatakia kila kheri),” alisema Mkapa na kumfanya mwandishi aangue kicheko.

KIFO CHA RAIS SATTA

Akimzungumzia hayati Rais Satta, Mkapa alisema hakuitwa “King Cobra” kimakosa, bali alistahili kutokana na uwezo aliokuwa nao ama wa kimaamuzi au wa kimsimamo.

“Nina hakika sana kwamba Wazambia na sisi kama Mataifa ya Afrika tutamkumbuka daima ndugu Satta. Satta daima alikuwa kwa ajili ya watu wake na Bara letu kwa jumla. Alisema na kusimamia kile alichokiamini kuwa ni cha kweli na chenye mafanikio, Satta ataendelea kuwa kiongozi mzuri daima,” alisema Mkapa.

Aliongeza: “Hivyo, maumivu yanayotukabili kwa kumpoteza Mzee Nyerere, Mzee Nkrumah, Mzee Mandela, Mzee Kenyatta ni sawa na yale yanayotukabili leo tunapomjadili Mheshimiwa Satta (Inatosha kusema kwamba tumempoteza shujaa mwingine katika Bara letu) Naitakia roho yake mapumziko ...”

Akijibu swali namna anavyoziona siasa za Afrika akiwa Rais mstaafu, Mkapa alisema ni kawaida na hana jambo kubwa la kusema japo kuna mengi yanatokea, ambayo mengine ni ya hovyo.

“Mathalan, Waafrika wazee wetu, walipigania sana ukombozi wetu. Ila nadhani wengi bado kuna watu wana matatizo na wanahitaji kukombolewa kifikra,” alisema Mkapa.

Aliongeza: “Maana yake kuna wenzetu wanatumika pasipo kujua na kusababishia nchi zao kuingia katika matatizo, kama vita na wengi wao wameanza kujuta”.
“Hivyo, ni lazma ifikie mahali watu waweze kujitambua na kujua ni yepi malengo mema kwa Bara letu ni yepi tunashinikizwa...” aliongeza kusema Mkapa.