Friday, 14 November 2014

Bunge likatae miswada inayominya uhuru wa habari

Serikali juzi iliwasilisha bungeni Muswada wa Sheria unaotishia uhuru wa vyombo vya habari, lakini ikauchomoa baadaye jioni baada ya kugundua kwamba umestukiwa na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.
Hatua hiyo ya Serikali ya kuwasilisha Muswada wa Sheria ya Takwimu unaoonekana kulenga kukwamisha vyombo vya habari katika kupata takwimu na kuzitumia katika habari na taarifa zinazotolewa kwa wananchi, imeonekana kwa wengi katika tasnia ya habari kama uthibitisho kwamba pengine Serikali haina dhamira ya kuona wananchi wanapata haki ya kupata habari.
Moja ya kifungu cha muswada huo kilicholalamikiwa na wabunge wengi ni Ibara ya 37 (4), ambacho kinaeleza kwamba wadau na vyombo vya habari vitakavyotoa takwimu bila kibali cha Ofisi ya Takwimu watakwenda jela miaka mitatu pamoja na faini ya Sh10 milioni au vyote kwa pamoja.
Inasikitisha kuona kwamba adhabu hiyo kubwa kupita kiasi imeungwa mkono na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara, ambayo iliwasilisha maoni yake bungeni juzi.
Adhabu ya kosa hilo awali ilikuwa kifungo cha mwaka mmoja, lakini katika hali ya kushangaza Kamati hiyo ilipendekeza iongezwe hadi miaka mitatu eti kuzuia tabia ya baadhi ya watu kutoa takwimu za uongo na kwa makusudi ili kupotosha jamii.
Hakuna anayepinga kuwapo umuhimu wa kuipa mamlaka zaidi na kuiwezesha Ofisi ya Taifa ya Takwimu kutekeleza majukumu yake ya kitakwimu kwa ufanisi, wala hakuna anayepinga uanzishwaji wa mfumo thabiti wa utoaji wa takwimu unaokusudia kuboresha na kuimarisha takwimu rasmi nchini.
Jambo hilo tumekuwa tukilisisitiza mara kwa mara na kwa kweli tunadhani Serikali imechelewa sana kuanza kuchukua hatua.
Hata hivyo, tunadhani Serikali inafanya makosa kudhani kwamba uchapishaji wa takwimu zisizo sahihi unatokana na watu kutaka kupotosha jamii na kuleta machafuko.
Ni kweli kwamba katika mazingira fulani takwimu zisizo sahihi zinaweza kusababisha vurugu, lakini pia lazima tukubali kwamba Serikali yenyewe ndiyo inapaswa kubeba lawama kwa uzagaaji wa takwimu zinazokinzana na zisizo sahihi.
Tangu tupate uhuru Serikali haijawahi siyo tu kuwa na utamaduni wa kuheshimu na kutunza takwimu, bali pia kuweka mazingira ya kuboresha ukusanyaji wa takwimu kwa kuweka mfumo thabiti na kuboresha Ofisi ya Taifa ya Takwimu.
Hivyo kama ni kupotosha takwimu, Serikali ndiyo imekuwa mpotoshaji namba moja. Hii imetokana na kutokuwapo mfumo wa kuainisha takwimu kutoka katika wizara, taasisi za Serikali, sekta ya umma na sekta binafsi kama inavyofanyika katika nchi nyingi duniani. Kwa mfano, hatudhani kama Serikali inazo takwimu sahihi kuhusu Deni la Taifa hivi sasa.
Tunachotaka kusema hapa ni kwamba muswada huo wa Sheria ya Takwimu uliochomolewa bungeni juzi ulilenga kuvibana vyombo vya habari na kuminya uhuru na haki ya wananchi kupata habari.
Kwa miaka minane sasa, Serikali imekuwa ikisuasua kupeleka bungeni Muswada wa Sheria ya Uhuru wa Habari na Vyombo vya Habari, hata baada ya kuihakikishia jumuiya ya kimataifa mara kwa mara kwamba muswada huo ungepelekwa bungeni.
Tunadhani Muswada wa Sheria wa Takwimu ni mwendelezo wa mkakati wa Serikali wa kuvibana vyombo vya habari. Bunge litafanya vyema kuukataa iwapo Serikali itaurudisha ukiwa na maudhui yaleyale yaliyoufanya uchomolewe bungeni juzi.

No comments: