Sunday, 11 May 2014

Mbowe atangaza mawaziri kivuli

Dodoma. Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, ametangaza Baraza lake la mawaziri kivuli 28 na naibu mawaziri 12, na kufanya baraza lote kuwa na mawaziri 40.
Katika baraza hilo la mawaziri linalojumuisha wabunge wanaotokana na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), mawaziri 25 wanatoka Chadema, 11 wanatoka CUF na NCCR-Mageuzi ni wanne.
Mawaziri kivuli walioachwa katika baraza hilo ni Sylvester Kasulumbay (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi), Highness Kiwia (Viwanda na Biashara) na Rose Kamili (Kilimo, Chakula na Ushirika).
Wengine walioachwa na Mbowe akasisitiza kuachwa kwao siyo kwa sababu hawawezi kazi bali ni kutaka kuwa na baraza la mawaziri dogo ni Sabrina Sunga (Naibu Waziri Maji).
Katika Baraza hilo, nafasi ya mnadhimu mkuu wa upinzani Bungeni iliyokuwa ikishikiliwa na Tundu Lissu (Chadema) sasa itashikiliwa na Mbunge wa Tumbe, Rashid Abdalah kutoka chama cha CUF.
Akitangaza baraza hilo Bungeni mjini Dodoma jana, Mbowe alisema Wizara ya Katiba na Sheria imeongezewa majukumu ya Muungano na waziri wake atakuwa ni Lissu na naibu wake ni Abdalah.
Pia amemteua Mbunge wa kuteuliwa na Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa taifa wa NCCR-Mageuzi,  James Mbatia ambaye anakuwa Waziri wa Fedha wakati Naibu wake atakuwa Christina Lissu kutoka Chadema.
Mawaziri Ofisi ya Rais ni Profesa Kulikoyela Kahigi (Utawala Bora-Chadema), Vicent Nyerere (Utumishi-Chadema) na Esther Matiko (Mahusiano na Uratibu-Chadema).
Ofisi ya makamu wa Rais itakuwa na mawaziri wawili ambao ni mchungaji Israel Natse kutoka Chadema atakayeshughulika na Mazingira na Naibu wake atakuwa ni Assah Othman Hamad (CUF).
Mnadhimu wa Upinzani Bungeni ndiye atakayeshikilia pia nafasi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Mazingira.
Mawaziri katika ofisi ya Waziri mkuu ni Pauline Gekul (Uwekezaji na Uwezeshaji-Chadema), Rajabu Mohamed Mbaruku (Sera, Uratibu na Bunge-CUF) na David Silinde (Tamisemi-Chadema).
Wizara ya Chakula, Kilimo na Ushirika itashikiliwa na Meshack Opulukwa (Chadema), Wizara ya Nishati na Madini atakuwa John Mnyika Chadema na Naibu wake “atakuwa Raya Ibrahim (Chadema).

Kulingana na orodha hiyo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa itashikiliwa na Ezekiah Wenje (Chadema) na Naibu wake ni Rashid Abdalah  kutoka  CUF.
Mawaziri wengine na wizara zao kwenye mabano ni Felix Mkosamali (Ujenzi-NCCR-Mageuzi), Magdalena Sakaya (Maji-Cuf), na Moses Machali (Uchukuzi- NCCR- Mageuzi).
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaongozwa na Godbless Lema wa Chadema na Naibu wake ni Khatibu Said Haji wa CUF wakati Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi ni Halima Mdee wa Chadema.
Kwa mujibu wa orodha hiyo, Mbowe amemteua Rose Kamili Sukum kutoka Chadema kuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi wakati Naibu wake atakuwa ni Mkiwa Adam Kiwanga wa CUF.
Wizara ya Maliasili na Utalii itashikiliwa na mchungaji Peter Msigwa (Chadema), Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeenda kwa Joseph Selasini (Chadema) na naibu ni Rukia Ahmed Kassim (CUF).
Mbowe pia amemteua Masoud Abdalah Salim wa CUF kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa na Wizara ya Elimu itashikiliwa na Susan Lyimo  na Naibu wake ni Joshua Nasari wote toka Chadema.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeenda kwa Dk Gervas Mbassa na Naibu wake ni Conchesta Rwamlaza wote wa Chadema. David Kafulila (NCCR) ameteuliwa Waziri wa Viwanda na Biashara.
Katika baraza hilo la mawaziri, Injinia Habib Mnyaa wa CUF ameteuliwa kuwa Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia wakati Lucy Owenya kutoka Chadema akiteuliwa kuwa naibu wake.
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto imeenda kwa Baruan Salum Khalfan wa CUF na Naibu wake ni Subreena Sungura wa Chadema. Cecilia Paresso wa Chadema anakuwa Waziri wa Kazi na Ajira.
Wizara ya Habari, Vijana na Michezo imeendelea kushikiliwa na Joseph Mbilinyi wa Chadema.
Akizungumza na wanahabari, Mbowe alisema wakati katika Baraza la Mawaziri la Serikali ya CCM, wanaume ni 36 na wanawake 15, wao upinzani wanaume ni 26 na wanawake ni 14.
Hali kadhalika Mbowe alisema wakati Baraza zima la mawaziri la Serikali ya CCM likiwa na mawaziri kamili 28 na manaibu 22, wao Baraza lao Kivuli lina mawaziri kamili 28 na naibu mawaziri 12.
Alisema nafasi ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Ubungeni iliyokuwa ikishikiliwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe itantangazwa baadaye

Lugola: Serikali ya CCM inaendeshwa kisanii

Dodoma. Mbunge machachari wa Mwibara, Alphaxard Kangi Lugola, amedai kuwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo yeye ni mbunge wake, inaendeshwa kisanii.
Lugola ambaye katika Bunge lililopita aliwaongoza wabunge wenzake kuichachafya Serikali hadi mawaziri wanne kujiuzulu nyadhifa zao, jana aligeuka tena mwiba kwa Serikali ya CCM.
Akichangia hotuba ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Lugola alisema anashangaa Waziri mwenye dhamana, Christopher Chizza kuendelea kuwa waziri wakati hotuba yake imejaa blabla.
Pia alimgeukia naibu wa wizara hiyo, Godfrey Zambi na kumwambia kuwa amejisahau kwamba naye alikuwa akikaa kiti cha nyuma bungeni akipaza sauti, lakini baada ya kupata madaraka amewageuka na kushirikiana na waziri.
Akichangia kwa hisia kali, Lugola alihoji inakuwaje wakulima wanapelekewa pembejeo feki, dawa feki na skimu za umwagiliaji zinachakachuliwa na bado Chizza anaendelea kubaki ofisini kama Waziri.
“Waziri huyuhuyu ndiye anayezindua mbegu aina ya Chutoni ambayo haioti, bado ni Waziri. Waziri huyu huyu analipa ruzuku mbegu ya pamba isiyoota bado ni Waziri,” alisema Lugola.
Lugola alihoji kama Mchina aliyekuwa akijenga daraja la Kilombero alijiua kwa sababu tu ya kuhofia kupigwa risasi atakaporudi kwao, hata Waziri Chizza alipaswa awe ameiacha kazi hiyo.
“Simshauri waziri ajiue, lakini kwa vitendo vyote hivi waziri huyu angekuwa ameacha wizara hii na kupumzika na kufanya kazi nyingine mbadala,” alisema Lugola huku akipigiwa makofi.
Lugola alikumbushia Chizza alikuwa ni miongoni mwa mawaziri waliotajwa kuwa ni mizigo na kusema mambo yanayofanywa na wizara hiyo yatakigharimu Chama Cha Mapinduzi.
Mbunge huyo alibainisha kuwa, katika hotuba yake mwaka jana, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema Serikali iko kwenye mchakato wa kuanzisha mfuko wa kinga ya pamba ili kuwasaidia wakulima.
Hata hivyo, alisema katika hotuba ya Waziri Mkuu juzi, hakuna sehemu aliyozungumzia mfuko huo wala Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika katika hotuba yake ya mwaka huu, naye hajazungumzia mfuko huo.
“Hivi nchi hii tunaiendesha kwa usanii mpaka lini? Usanii juu ya usanii… Hatuwezi kuwadanganya wananchi kwa kiwango hiki. Itakuwaje mimi mbunge niunge mkono bajeti ya namna hii?” alihoji.

Alimgeukia Zambi na kumweleza kuwa aliwahi kumtahadharisha kuwa atakapokuja na bajeti yake ahakikishe anampa majibu ya asilimia 20 ya malipo waliyoahidiwa wakulima waliotumia mbegu ya chutoni.
“Uniambie asilimia 20 ya malipo ya wakulima ambayo waliahidiwa kwamba wakitumia chutoni walipwe kama sehemu ya malipo yao, lakini hili halimo kwenye bajeti,” alisema na kuongeza:
“Hakuna lolote humu ni blabla tu… Mheshimiwa Zambi wewe ulikuwa ‘backbencher’ (kiti cha nyuma) kama mimi ulikuwa unapiga muziki kama kasuku juu ya wizara hii, leo unashirikiana na waziri wako unakuja na vitu ambavyo havina majibu, maana yake nini?”
Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa (CCM), alisema wakati Zambi akiwa mbunge, alikuwa msitari wa mbele kupinga matumizi ya mbolea ya minjingu na kumtaka aeleze kama bado ana msimamo huo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda (Chadema), aliwashukia wakuu wa mikoa ya Simiyu na Geita kuwa ni chanzo cha tatizo kwa wakulima wa pamba.
Mbali na hilo, amemtaka Balozi wa Uingereza nchini ajitokeze kueleza misaada inayotolewa na nchi yake inavyotumiwa kwenye sekta ya pamba kwani imekuwa ni sehemu ya ubabaishaji kwa kuendeshwa semina zisizo na maana.
Shibuda alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akichangia maoni kwenye hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa mwaka 2014/15.
Aliwatuhumu wakuu hao kuwa walimpeleka Waziri Mkuu katika kampuni ya Kiotoni wakamdanganya kuwa mbegu hizo ni nzuri, lakini kumbe hazikuwa zimefanyiwa utafiti wa kina na kuwasababishia hasara kubwa wakulima.
Shibuda alisema mbegu za kiotoni zina udhalimu mkubwa na hazina tija yoyote kwa wakulima lakini kila siku wakuu wa mikoa na wilaya wanazipigia debe licha ya kuwa wanatambua kwamba wakulima wanaumizwa.
Magdalena Sakaya aliifananisha Serikali kuwa ni sawa na sikio la kufa kwa kuwa kila wakati imeshindwa kuwa na majibu ya ukombozi kwa wakulima wa Tanzania ambao ndio wapigakura wao.
Mbunge wa Kasulu, Moses Machali (NCCR-Mageuzi) aliwapongeza wabunge wa CCM wanaoonyesha ujasiri wa kuisema Serikali yao kuwa inaendesha mambo kisanii na hivyo kushindwa kuwaletea wananchi maendeleo.
“Serikali imekuwa ikidanganya katika kutatua matatizo ya wananchi ndiyo maana tunaona ni Serikali ya maigizo… Ukisoma hotuba ya bajeti hapa haijibu matatizo ya wananchi,” alisema.
Wakati wabunge hao wakiiponda bajeti hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imeitaka Serikali, kueleza ni lini na vipi wakulima walioathirika na mbegu feki watafidiwa.
Msemaji wa Kambi hiyo wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Rose Kamili, alisema tayari wakulima wameshapata hasara na bado wako wanaoendelea kuathirika na tatizo la mbegu kutoota.

Friday, 9 May 2014

Kafulila awalipua mawaziri akaunti ya Escrow

Dodoma. Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila jana aliibua tuhuma nzito bungeni akiwahusisha mawaziri wawili na Sh200 bilioni zilichotwa katika Akaunti ya Escrow, iliyokuwa inamilikiwa kwa pamoja kati ya Tanesco na Kampuni ya kufua umeme ya IPTL.
Katika tuhuma hizo, alimuunganisha pia Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na vigogo wengine, wakiwamo wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na wa Serikali, wote akiwataja tu kwa vyeo bila majina.
Mawaziri waliotajwa ni Waziri wa Nishati na Madini, Waziri wa Fedha na Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Ingawa Kafulila hakutaja kwa majina, Waziri wa Nishati ni Profesa Sospeter Muhongo, wa Fedha ni Saada Mkuya, Katibu Mkuu wa wizara hiyo (Nishati) ni Eliakim Maswi na AG ni Frederick Werema.
Kafulila alitoa tuhuma hizo bungeni alipokuwa akichangia hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2014/15.
Mbunge huyo alisema fedha zilizoibwa katika Akaunti ya Escrow ni nyingi kuliko zile zilizoibwa katika kashfa ya Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ya BoT mwaka 2005.
“Pamoja na hilo, Watanzania wamekuwa wakisikia kwenye vyombo vya habari kwamba Tanesco wakati ilipokuwa na mgogoro na IPTL walifika mahali wakafungua akaunti ya Escrow,” alisema.
Mbunge huyo alisema akaunti hiyo ilifunguliwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), mwaka 2004 na hadi jana, akaunti ile ilishafikia Dola za Marekani 122 milioni,” alisema Kafulila.
Alisema fedha hizo ziliwekwa kwa lengo maalumu kutokana na mgogoro uliokuwapo kati ya IPTL na Tanesco ili ziweze kusaidia malipo baada ya mgogoro kuisha katika Baraza la Usuluhishi wa Kibiashara la ISCID.
Alitaka jambo hilo liingie kwenye rekodi kwa kuwa linahusu BoT na vigogo akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Katibu wake na pia Waziri wa Fedha.
Alisema wakati Tanesco ikidaiwa madeni zaidi ya Sh400 bilioni, viongozi hao wameidhinisha kugawanywa kwa fedha hizo kihuni jambo alilosema halivumiliki hata kidogo.
Kafulila alisema fedha hizo zilichotwa na Kampuni ya PAP aliyosema ya “Singasinga na ya kitapeli” ambayo iliidhinishiwa kuchota fedha hizo kinyume na utaratibu.
Alisema fedha hizo hazikupaswa kuchukuliwa kwa kuwa kulifanyika udanganyifu mkubwa kwamba PAP ilikuwa imenunua IPTL wakati jambo hilo si la kweli.
Alisema IPTL ilikuwa na makubaliano ya kufanya kazi kwa kampuni mbili ambazo ni VIP Engineering ya Tanzania iliyokuwa na hisa asilimia 30 na Mecmer ambayo ilikuwa na asilimia 70 ya hisa.
Hata hivyo, alidai kuwa anao ushahidi kuwa PAP ilikuwa imenunua hisa za VIP na hakukuwa na vielelezo vya kununua Mecmer kwa kuwa kampuni hiyo tayari ilishapoteza uhalali wake kwa kuwa ilikuwa chini ya muflisi nchini Malaysia.
Aliliambia Bunge kuwa wakati wa uchukuaji wa fedha hizo kutoka BoT, ilipaswa kulipiwa kodi lakini zilichukuliwa kinyemela bila hata ya kulipiwa kodi.
Alisema TRA iliiandikia Hazina na nakala kwa BoT kwamba wakati wa kulipa fedha hizo lazima kodi ikatwe, lakini cha ajabu hilo halikufanyika licha ya kukumbushwa.
“Kwa mfano, tulimwita Gavana katika kikao chetu cha Kamati ya Uchumi pale Bagamoyo na alikiri kuwa alibanwa na viongozi wa juu kiasi cha kushindwa kufurukuta, kwa hali kama hiyo Naibu Spika unategemea nini?” alihoji.
Kafulila alisema, Gavana katika kikao hicho alikiri kuwa, kulikuwa na presha (shinikizo) ambazo asingeweza kuzizuia na kuwa alikuwa amejitahidi kwa kiasi kikubwa hadi kufikia alipofika.
Alisema ISCID lilitoa hukumu ndogo Februari, mwaka huu kuwa Tanesco na IPTL wakae pamoja na kupitia hesabu zao namna watakavyogawanya fedha hizo na walipewa siku 60 ambazo mwisho wake ulikuwa jana.
Aliituhumu Tanesco kuwa katika makubaliano hayo ilikataa kukaa meza moja na kufanya hesabu za namna ya kulipana jambo alilosema linaonyesha ilidhamiria kufanya hivyo.
“Kwa sababu wanajua kuwa fedha ile ilishaliwa na wajanja wachache, Mheshimiwa Waziri Mkuu, hili kwa vyovyote halikubaliki na halivumiliki kwa sababu Dola122 milioni ni zaidi ya Sh200 bilioni ambazo ni nyingi kuliko za EPA, lazima litoke na mtu.”
Alisema hayuko tayari kuona fedha hizo zikitafunwa bila ya utaratibu na akashangazwa kuona Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), akishindwa kuchukua hatua.
Akoleza moto jioni
Katika kikao cha jioni, Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu alimwita tena Kafulila kutoa ufafanuzi wa hoja yake aliyoitoa mchana, ambayo iliombewa mwongozo na Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina kwamba Gavana alishinikizwa kutoa fedha hizo.
Wakati wa mwongozo huo, Kafulila hakuwapo na ndiyo sababu ya Mwenyekiti kumpa nafasi ya kufuta kauli yake kuwa Gavana alishinikizwa. Hata hivyo, Kafulila alikazia akisema alishinikizwa kutoa fedha hizo.
“Gavana aliwahi kuniambia, mnanionea bure. Kulikuwa na presha kubwa sana kuhusu fedha hizi… ukweli ni kwamba IPTL inabadilishwa tu rangi na watendaji ni walewale.”
Baada ya Kafulila kuzungumza, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisimama na kusema: “Tuhuma dhidi ya Gavana wa Benki Kuu zinatolewa kwa kuwa hawezi kuingia bungeni kujitetea.
“Lakini Gavana tulimuuliza na akakanusha kuwa aliwahi kuyatamka hayo maneno na kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni atakuja kufafanua jambo hili kesho (leo) katika hotuba yake,” alisema Lukuvi.
Hata hivyo, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee alisimama kuomba mwongozo akisema: “Kamati ya Bunge iundwe ili tuchunguze fedha hizi za Escrow zimekwenda wapi? Kafulila ana ushahidi wa kutosha, kwa nini hamtaki athibitishe?
“Vikao vyote vya kamati vinawekewa kwenye kumbukumbu rasmi (hansard) ili kujua kama Gavana alitoa maneno hayo ama hakutoa, iundwe kamati ijulikane mbivu na mbichi na wezi wa fedha za Escrow tunao humu ndani ya Bunge.”

Wednesday, 9 April 2014

Kamati kumi zaitesa CCM

Dodoma. Kura za awali katika Kamati 10 kati ya 12 za Bunge Maalumu la Katiba, zinakipa wakati mgumu Chama Cha Mapinduzi,(CCM) kutekeleza azma yake inayotajwa kuwa ni kufumua Rasimu ya Katiba, ili kuondoa mapendekezo ya Muundo wa serikali tatu, baada ya wajumbe wa Zanzibar kukwamisha upatikanaji theluthi mbili.
Kwa mujibu wa taarifa za kamati, ambazo tangu juzi zimeanza kutolewa katika sura ya kwanza na sita zinazungumzia Muundo wa Muungano, wajumbe kutoka Zanzibar kwa sasa ndiyo kikwazo kikubwa kwa CCM.
Hata hivyo, uamuzi ya mwisho kuhusu Muundo wa Serikali, kati ya mbili au tatu, unatarajiwa kujulikana Alhamisi wiki ijayo, wakati kamati zote zitakapowasilisha taarifa zao na kupigwa tena kura kwa wajumbe Tanzania Bara peke yao na Zanzibar peke yao.
Iwapo wajumbe wa Zanzibar wakiitetea kwa theluthi mbili kama sasa, mapendekezo ya muundo wa serikali tatu ndiyo yatakayopelekwa kwa wananchi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, baadhi ya wenyeviti wa kamati hizo, Stephen Wassira, Ummy Mwalimu, Anna Abdalah na Paul Kimili, walitaja moja ya vifungu ambavyo vimeshindwa kupata theluthi mbili kuwa ni ibara ya kwanza kifungu cha kwanza.
Akizungumza jana Wassira ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Namba Sita alisema kwamba katika kamati yake ibara hiyo imeshindwa kupata theluthi mbili, ili kuweza kufanyiwa marekebisho.
“Lakini huu siyo mwisho kama nilivyosema awali, tukirudi bungeni tutapiga kura kwa wajumbe wote na ndiyo itakuwa na uamuzi wa mwisho kama muundo wa Muungano utakuwa na Serikali tatu ama mbili, ambao utapelekwa kwa wananchi,” alisema Wassira.
Jussa, Lissu- tumeibana CCM
Jussa alisema: “Kwa taarifa za matokeo tulizonazo katika Kamati Namba 1, 2, 3, 4, 6, 10, 11 na 12 mapendekezo ya kubadilisha Rasimu katika ibara hizo mbili yamekwama. Kama CCM wakichakachua sura ya kwanza na sita, maana yake ni kwamba hapa hakuna Katiba, hakuna kura ya maoni na hakuna mwafaka.”
Vifungu hivi pia kwa mujibu wa wenyeviti wa kamati nyingine, isipokuwa kamati ya Tano, ambayo inaongozwa na Hamad Rashid, havikupata kura theluthi mbili na hivyo kubaki kama vilivyo kwenye rasimu.
Naye Lissu alisema kwa sasa CCM ndiyo inaweza kuanza mkakati wa kuvuruga Bunge kwani tayari wamejua hawana theluthi mbili ya Zanzibar ili kubadili Rasimu kama wanavyotaka.

Msekwa: Sitta ana lake jambo

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta kukiri kuchezewa kwa saini ya aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Msekwa amesema, ‘mzungumzaji huyo ana lake jambo’.
Sitta akizungumza na gazeti hili juzi mjini Dodoma alisema ni kweli kuna maneno katika hati hiyo ya sheria namba 22 ya 1964, iliyosainiwa na Nyerere na Msekwa, Aprili 25, 1964, yameongezwa.
Alifafanua kuwa saini ya Nyerere imeongezwa herufi ‘us’ kwa kompyuta na katika sehemu ya saini ya Msekwa kumeandikwa neno ‘Msekwa’ kwa kompyuta, jambo ambalo ni makosa. Sitta alisema walioongeza maneno hayo ni wafanyakazi wa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya kuona sehemu ya maandishi kwenye saini hizo hayasomeki, lakini walifanya makosa.
Msekwa akizungumza na gazeti hili jana alisema: “Saini iliyo katika hati original (halisi) ni ya kwangu mimi, lakini huyo anayesema zimechezewa muulizeni atakuwa na lake jambo. Kama kompyuta imekosea ni leo kwa kuwa kipindi hicho kompyuta hazikuwapo.”
Aliongeza: “Ana lengo gani la kutilia shaka, ana lengo gani la kusema imechakachuliwa, kinachotakiwa ni hati original ambayo iko ofisi ya Katibu wa Bunge itolewe, kwanini tuendelee kuandikia mate wakati wino upo?”
Maoni mengine
Mjumbe wa Bodi ya Kituo cha Taarifa kwa Wananchi Umma (TCIB), Hebron Mwakagenda alisema yote hayo yanatokea ni kuvuruga hoja iliyopo mezani.
Alisema kitendo cha kupoteza muda kuzungumzia suala la kuchezewa kwa saini halitakiwi kwani kama maudhui yake hayakuchezewa basi hoja ya muundo wa Muungano uamuliwe na wananchi wenyewe.
“Tusianze kupoteza muda kwa mambo ambayo hayapo cha msingi wananchi wenyewe waulizwe wanaupenda Muungano au la lakini tusianze kumtafuta mchawi kuwa saini zimechezewa wananchi waamue wenyewe kuhusu Muungano,” alisema Mwakagenda.
Sakata lilivyoanza
Utata huo ulianza wiki hii baada ya kamati za Bunge Maalumu la Katiba kuanza vikao vyake vya kujadili sura ya kwanza na ya sita ya Rasimu ya Katiba, zinazohusu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na muundo wake.
Hali hiyo ilitokana na kutopatikana kwa hati ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na ile ya Sheria ya Baraza la Mapinduzi ya kuridhia Mkataba wa Muungano.
Aprili 2 mwaka huu, Kamati namba 2 ilimwalika, Spika Mstaafu wa Bunge la Muungano, Pius Msekwa kutoa ufafanuzi kuhusu hati hizo, lakini uhalali wa saini zake uliibua malumbano makali. Msekwa aliitwa kutokana na kwamba ndiye aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika wakati huo.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Shamsi Vuai Nahodha, alithibitisha kutokea utata huo na kwamba walilazimika kumuita Msekwa ili kupata ufafanuzi wa masuala kadhaa na Msekwa alisema saini zilizopo katika hati hiyo ni ya kwake.
Nahodha alisema kwa maelezo ya Msekwa, inaonekana hati ya Muungano ipo Umoja wa Mataifa (UN), kwani kabla ya Muungano, Tanganyika ilikuwa na kiti chake UN na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar hali kadhalika.
Aliongeza kuwa baada ya UN kuomba uthibitisho wa Muungano, ndipo walipelekewa hati hiyo na kwamba haijawahi kurejeshwa.
Kwa upande wake Katibu wa Bunge la Katiba, Yahya Hamis Hamad alisema hati hiyo ipo Dar es Salaam na ni moja tu, hivyo siyo rahisi kuipeleka bungeni Dodoma.

Matumaini Katiba Mpya arijojo

Ikulu imeeleza kuwa imeshindwa kutimiza ahadi yake kwa taifa ya kulipatia Katiba Mpya ifikapo Aprili 26, 2014.
Katibu Mkuu Kiongozi (KMK), Balozi Ombeni Sefue alilieleza gazeti hili kuwa kwa hali ya mchakato huo ilivyo sasa, wameshindwa kufikia lengo hilo, lakini hawajakata tamaa kuhusu kupatikana Katiba Mpya ndani ya mwaka huu.
“Kweli matarajio ya awali yalikuwa hayo, lakini kama unavyoona hali ilivyo, ni vigumu kusema matarajio mengine, ingawa majadiliano yaliyofanywa mwaka huu ni lazima Katiba inayopendekezwa iwasilishwe kwa wananchi na mwakani tutakuwa na Katiba Mpya,” alieleza Balozi Sefue.
Katika hali isiyoeleweka Balozi Sefue alisisitiza msimamo wa awali wa Serikali kwamba Katiba itakayopatikana itatumika kwenye Uchaguzi Mkuu, unaotarajiwa kufanyika mwaka ujao.
Dk Slaa
Katibu Mkuu wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (Chadema), Dk. Willbroad Slaa, alisema hilo ni fundisho kwa Serikali kwamba kiburi na jeuri havitakiwi katika masuala yanayohusu umma.
Alisema muda huo wa kupatikana Katiba Mpya ulipotangazwa, walioanzisha kilio cha kudai Katiba Mpya nchini ambao aliwataja kuwa ni vyama vya upinzani vya siasa, taasisi mbalimbali za kijamii walipinga na kutoa ushauri kwa Serikali, lakini walipuuzwa.
Dk. Slaa alisema walipendekeza kwamba badala ya kupeleka mchakato wa Katiba mchakamchaka, warekebishe kwa mara ya 15 Katiba inayotumika, ili iende na wakati wa sasa ikiwamo Uchaguzi Mkuu ujao kwa lengo la kutoa muda wa kutosha kwa mchakato wa taifa kupata Katiba Mpya.
“Lakini walitukebehi na kututukana sana, sasa kiko wapi Aprili 26 hiyo hapo na Katiba haijapatikana na kusema itapatikana mwaka huu na kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu mwakani ni ndoto za mchana,” alieleza Dk. Slaa.
Dk. Slaa alisema tukio hilo liwe fundisho kwa Serikali, wawe wakweli, wanyoofu na wafahamu kuwa nje ya Serikali kuna watu makini na wanaojua vilivyo mchakato wa Katiba.
Alisema ana taarifa za Bunge Maalumu kuahirishwa Mei 9, 2014 ili kupisha Bunge la Bajeti. Hivyo mategemeo ya Katiba Mpya kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, yanatia shaka.
“Kwa akili ya kawaida tu isiyohitaji elimu ya chuo chochote, kutumia Katiba Mpya kwenye Uchaguzi Mkuu ujao ni jambo lisilowezekana kwa hiyo waache kutuletea matumaini yasiyokuwapo, sisi siyo watoto wadogo,” alieleza Dk. Slaa.
Kauli ya LHRC
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Helen Kijo Bisimba, alisema siyo tu Serikali imeshindwa kutimiza ahadi ya muda iliyojiwekea, bali hata mchakato wenyewe haueleweki.
Dk. Bisimba alisema kwa hali ilivyo, hawana hakika ya kupata Katiba na ikipatikana haitakidhi matakwa ya wananchi, kwa kuwa wanataka Katiba ya watu siyo ya kundi moja la watu.
“Mambo ya nchi hii tunayafahamu, inaweza ikapatikana kwa nguvu lakini wajue wananchi wataikataa na hata ikilazimishwa, haitakidhi mahitaji, itaweza kuathiri ustawi wa taifa,” alieleza Dk. Bisimba.
Alisema hilo waliliona mapema, wakataka kila hatua ya mchakato ipewe muda wa kutosha kabla ya hatua nyingine, ili wananchi waelimishwe lakini hawakusikilizwa.
Alisema kuwa katika mazingira hayohayo, Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilifanya kazi kubwa hadi kufanikisha maoni ya wananchi kupatikana na kutengeneza Rasimu ya kwanza na ya pili iliyowasilishwa bungeni Machi 18, 2014, lakini kwa jinsi Bunge Maalumu linavyoendeshwa, kuna kila dalili kwamba kazi hiyo itaharibiwa.
“Wakichezea Rasimu wajue wanachezea maoni ya wananchi, wanaoweza kuyakataa kupitia kura ya maoni na hivyo kusababishia taifa hasara isiyomithilika,” alieleza Dk. Bisimba.
Dk. Bisimba alisema mchakato huo umegharimu taifa fedha nyingi, muda mwingi, nguvu, akili, afya na hata uhai wa watu, hautakiwi kufanyiwa mzaha.
Alipotafutwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro ili kuzungumzia suala hilo jana hakupatikana, lakini Naibu Waziri wa wizara hiyo Angela Kairuki, alisema kuwa kwa hali ilivyo ni dhahiri haiwezekani kupata Katiba Mpya kwa muda huu tofauti na ilivyodhaniwa awali.
Hata hivyo, Kairuki alisema hawezi kuzungumzia hatua iliyofikiwa katika mchakato huo kwani mwenye mamlaka ya kuzungumzia ratiba ya Bunge Maalumu la Katiba ni mwenyekiti wake, Samuel Sitta.
“Hata hivyo tunachotakiwa kuzungumzia ni ubora wa kazi inayofanyika ili kufikia lengo la kupata Katiba itakayoongoza nchi kwa miaka 50 ijayo,” alisema Kairuki.

Thursday, 3 April 2014

Waathirika wa milipuko ya Osama Dar wafurahia fidia

Dar es Salaam. Baadhi ya wanafamilia wa waliopoteza ndugu kwenye shambulio la ugaidi katika Ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam mwaka 1998, wameelezea kufarijika kutokana na malipo ya fidia, licha ya kwamba hayawezi kurejesha uhai wa waliokufa.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti, ndugu hao walisema, licha ya mahakama nchini Marekani kuwapa fidia lakini pengo la jamaa zao halitazibika.
Wiki iliyopita, Mahakama Kuu ya Marekani, ilitoa amri ya kuwalipa fidia ya dola za Marekani 957 milioni (Sh1.555 trilioni) waathirika 23 wa shambulio hilo.
Jaji Thomas Bates katika hukumu yake alisema kati ya fedha hizo, Dola za Marekani 420 milioni (Sh670 bilioni) watapewa ndugu wa marehemu watano na waathirika wanne wa Tanzania wakati kitita kilichobaki kitakwenda kwa waathirika ambao ni Wamarekani.
Jaji Bates alisema Serikali za Iran na Sudan zitawajibika kulipa fidia hizo kutokana na kuhusika na mashambulio hayo mabaya kuwahi kutokea Afrika Mashariki.
Mmoja wa jamaa waliopoteza maisha katika tukio hilo, Kulwa Ramadhan alisema anasubiri kuletewa taarifa zaidi kuhusu taratibu za kupata fidia hiyo.
“Huwezi kuwa umeridhika na fidia kwa kuwa tumepoteza ndugu zetu lakini pia hata hicho kilichopatikana hatukukitarajia kupata,” alisema Ramadhan.
Alisema kuna baadhi ya jamaa wa marehemu watano hawakuingizwa kwenye idadi ya watakaopata fidia kutokana na kuchelewa kujiandikisha katika kesi hiyo.
“Baada ya tukio uongozi wa Ubalozi wa Marekani ulituambia tutoe taarifa zetu zote za mawasiliano na kwamba tusibadilishe namba za simu kwa ajili ya kuwasiliana kinachojiri.
“Lakini kuna baadhi ya jamaa walibadilisha namba zao na kufanya mawasiliano kuwa magumu hivyo kushindwa kuingizwa katika idadi ya wadai katika kesi hiyo,” alisema.
Ramadhan aliyempoteza pacha wake, Dotto Ramadhani alisema baadhi ya jamaa walijitokeza baadaye baada ya hatua muhimu za kesi kufanyika kitendo ambacho kiliwazuia kushiriki katika kesi.
Waathirika wengine
Naye Judith Mwila aliyempoteza mume wake kwenye tukio hilo, alisema anashukuru Ubalozi wa Marekani pamoja na mawakili waliowasaidia kufanikisha kesi hiyo.
“Binafsi nimepata taarifa kamili jana (juzi) kutoka kwenye gazeti la Mwananchi na sikutarajia kama tungeshinda kesi hiyo na tukapewa fidia ya fedha kiasi hicho. Hata hivyo tunaendelea kusubiri taarifa za mawakili wetu kuhusu taratibu zinazofuata kupata fedha hizo,” alisema.
Aliongeza kuwa iwapo atapata sehemu ya fedha hizo atashauriana na watoto wake jambo la kufanya ikiwamo kufanya biashara kubwa. Mwila ana watoto watatu alioachiwa na marehemu mume wake.
Alisema kuwa tangu mchakato wa kesi ulipoanza mwanzoni mwa mwaka 2001, Ubalozi wa Marekani na mawakili wao, walimpeleka Marekani mara mbili.
“Kesi hii imedumu muda mrefu. Mara ya kwanza nilikwenda 2001 kutoa ushahidi na mara ya mwisho ni 2010 na tangu wakati huo tulikuwa tukipewa tu taarifa juu ya maendeleo ya kesi,” alisema Mwila.
Kwa upande wake, Grace Paulo ambaye alifiwa na mumewe Elisha Paulo alisema: “Ninamshukuru Mungu kwa sisi kushinda kesi hii na hivyo tunasubiri mawasiliano na wahusika kufahamu jinsi ya kupata fedha hizo.
“Tumekuwa tukiishi kwa shida sana, hivyo hizo fedha zitatusaidia kujikwamua na matatizo yanayonikabili na mwanangu,” alisema Paulo ambaye aliachiwa mtoto mmoja aitwaye Mary Paulo.
Kwa mujibu wa waathirika hao, Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Misaada la Marekani (Usaid) liliwapa msaada wa kuwasomesha watoto pamoja na makazi ili kupunguza makali ya maisha.
Hata hivyo, wengi wao wanaendelea kufanya biashara ndogondogo kutokana na misaada hiyo kuwekwa katika eneo maalumu la ada za watoto.
“Kwa sasa ninafanya biashara ya kuuza nguo za mitumba na nilishaondoka Dar es Salaam mara tu baada ya msiba mwaka 1998 kutokana na maisha ya mjini kuwa magumu.
“Baadaye Ubalozi kupitia taasisi za kiraia walinitafuta hadi wilayani Mpwapwa ndipo waliponijengea nyumba ninayoishi sasa,” aliongeza Paulo anayeishi mkoani Dodoma.
Jamaa hao pia walisema kuwa gharama halisi za kesi hiyo hawazifahamu kutokana na kesi nzima kusimamiwa na Serikali ya Marekani na mawakili wao.
Hata hivyo, uhakika wa kupata fedha hizo unabaki mikononi mwa wakili wa jamaa hao, Thomas Fortune Fay ambaye baada ya hukumu hiyo alisema anafuatilia jinsi ya kupata fedha kwa Serikali za Sudan na Iran.
Alisema ataangalia jinsi ya kutaifisha baadhi ya mali za nchi hizo ili kupata fedha za kuwalipa waathirika hao.

Jaji Warioba aishangaa Serikali



Dodoma. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema waliokuwa wajumbe wa tume hiyo hawajawahi kudai malipo ya pensheni ya Sh200 milioni kama inavyodaiwa.
“Wajumbe wa Tume hawajatoa madai ya kulipwa shilingi milioni mia mbili. Hakuna mjumbe yeyote aliyetoa dai kama hilo na Serikali inajua,” alisema
Jaji Warioba katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, aliyoitoa kupitia Nyalali, Warioba and Mahalu Law Advocates ali ongeza:
“Nimeona taarifa iliyotolewa na Serikali kuhusu Tume ya Mabadiliko, nimeshangazwa na maudhui na lugha iliyotumika,” alisema Warioba akirejea taarifa iliyotolewa na Ikulu juzi ikieleza jinsi tume hiyo ilivyohitimisha kazi zake.
Wiki hii Jaji Warioba alikaririwa akilalamika jinsi yeye na makamishna wake walivyoondolewa ofisini na kunyang’anywa magari kwa haraka bila kusubiri siku waliyopanga kufanya makabidhiano, lakini Ikulu ilimjibu kwamba shughuli za Tume hiyo zilikoma siku ambayo Tume ilivunjwa.
Katika taarifa yake ya jana, Jaji Warioba alisema aliwasilisha Rasimu ya Katiba Machi 18 mwaka huu na Tume ilivunjwa Machi 19 wakati wajumbe wakiwa bado mjini Dodoma.
“Pamoja na lugha ya kejeli inayotumiwa na Serikali kuniita mnafiki, busara ya kawaida ilitakiwa kutumika kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani na kuandaa makabidhiano,” alisema.
Alisisitiza kuwa Serikali ilikuwa na wajibu wa kuwarejesha makwao wajumbe wa tume hiyo, hata kama muda wa kisheria wa kufanya kazi ulikuwa umepita.
“Niliwasilisha Rasimu Machi 18, 2014. Tume imevunjwa Machi 19, 2014 wakati wajumbe wako Dodoma. Pamoja na lugha ya kejeli iliyotumiwa na Serikali na kuniita mnafiki, busara ya kawaida ingeonyesha umuhimu wa Serikali kujipa muda wa kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani,” alisema Jaji Warioba na kuongeza:
“Hata kama sheria ilitaja muda wa kuvunja Tume bado ilikuwa ni wajibu Serikali kufanya mipango ya safari ya wajumbe baada ya kumaliza kazi. Sheria haikuizuia Serikali kufanya hilo. Huo ni wajibu wa Serikali na utaratibu wa kawaida unaotumiwa na Serikali kwa tume zote inazoziunda. Inaonekana Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliwekewa utaratibu tofauti. Kulikoni?”.

Friday, 28 March 2014

Siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili kikatiba

Katika maisha ya kawaida, binadamu ana msimamo wake na hata uamuzi  asiopenda ubadilike.
Katika medani ya siasa nchini msimamo wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kuhusu Muungano na muundo  unafahamika. Ni muundo wa kutaka  Serikali mbili ambao chama hicho unakipigania kwa udi na uvumba.
Hata hivyo, msimamo huo ni kinyume na mapendekezo au matakwa ya wengi kama ilivyoainishwa kwenye Rasimu ya Pili ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
 Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba ilikusanya maoni ya wananchi na ilipendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu.
Hivi karibuni akifungua Bunge Maalumu la Katiba, Rais Jakaya Kikwete akaunga mkono msimamo wa chama chake, jambo lililoibua mjadala unaoendelea hadi sasa.
Hoja ya Serikali mbili
Kwanini CCM wanataka Serikali mbili na siyo tatu au moja kama ilivyo maoni ya wananchi walio wengi kwa mujibu wa maelezo ya Tume ya Warioba? Makala haya yanachambua hoja hiyo.
 Profesa Bakar Mohammed ni Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anayesema msimamo wa CCM wa kudai Serikali mbili unatokana na hofu ya uhafidhina wa kuogopa mabadiliko.
Anasema viongozi wengi wa CCM wanasumbuliwa na hofu na woga wa mabadiliko na kwamba wanakuwa wagumu kuyakubali  yanapotaka kutokea.
“Kama mtu unaangalia madaraka zaidi, lazima kunakuwa na woga, na hii ni hulka ya binadamu kuwa na woga wa kuacha kile ulichokizoea… Lakini ukiangalia masilahi ya nchi na kuacha yale yanayokusukuma kusingekuwa na wasiwasi huu unaoonekana sasa,” anasema.
Anasema CCM inachofanya ni kuhakikisha haking’oki madarakani, huku viongozi wake wakiamini kuwa wana sifa za kuongoza na siyo wengineo.
Profesa Bakari anailinganisha hofu ya sasa ya CCM na ile waliyokuwa nayo viongozi wa chama hicho miaka ya 1990 zilipoanza vuguvugu za mabadiliko ya siasa za vyama vingi. Anasema CCM kiliendesha propaganda kuwa mfumo wa vyama vingi haukuwa na tija na ungeleta vita.
Hofu hiyo anasema ndiyo inayokifanya chama hicho kikongwe kuhofia kung’olewa madarakani.
 “Woga huo bado upo, wanaogopa pengine mfumo ukiwa wa Serikali tatu uwezekano wa wao kubaki madarakani utakuwa mdogo,” anafafanua.
Anaongeza kusema kuwa  hofu ya CCM siyo kwa ajili ya masilahi ya nchi,  badala yake inaonekana chama kinaangalia masilahi yake.
Ingekuwa vyema anasema kwa CCM  kueleza madhara yanayoweza kulikumba taifa ikiwa muundo wa Serikali tatu utapita.
 “Wanatoa hoja kuwa mfumo wa Serikali tatu unaweza kusambaratisha nchi, lakini hakuna uhakika kama mfumo huu uliopo nchi hauwezi kusambaratika,” anasema.
Hofu ya kuyumba na kuanguka
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk. Benson Bana anasema siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili inatokana na hofu ya kuyumba na kuanguka.
Anasema CCM kimekuwa madarakani na mfumo huo kwa miaka 50 na kwamba hofu yao ni kuwa ukiondoa Serikali mbili kinaweza kuyumba na kuachia madaraka.
Anasema misingi ya wanasiasa ni madaraka, na kwamba ukishayapata, huwezi kuyaachia kirahisi.
“Misingi ya wanasiasa ni madaraka… Kuyalinda, kuyahifadhi na kuyatumia madaraka yale kwa namna yoyote…Huwezi kuyaachia madaraka kirahisi. Utafanya ujanja, utatumia mbinu chafu  ili tu kuhakikisha unabaki madarakani, na hiki ndicho wanachofanya CCM,” anasema.
Dk. Bana anasema CCM kingeeleweka na kingekuwa na mwonekano mzuri zaidi endapo wangepigania kuwapo kwa Serikali moja.
“Wangekuwa wanataka muungano imara, endelevu na uliokomaa wangeelekeza katika Serikali moja…Lakini hawataki kwa sababu wanajua moja inaweza ikawanyima uongozi,” anasema.
Dk. Bana anasema ni vyema wananchi wakaelimishwa huu muungano una faida gani na wanafunzi shuleni katika elimu ya uraia waelezwe faida zake.
“Ingekuwa wazi tungejua nani anafaidika na nini, mikopo misaada, nani anachangia nini…Je zile sababu za waasisi za kuungana bado zipo sasa miaka 50 ya Muungano, ule woga kuwa Zanzibar itamezwa bado upo leo?” Anahoji.
Anaongeza kuwa ni vyema kwa watawala kutazama  mazingira ya sasa ya siasa zetu kwa kile anachoeleza kuwa hata Katiba ikipita ikakubali kuwapo wa Serikali mbili, bado wananchi watahoji mantiki ya muundo huo.
Msomi mwingine wa siasa, Dk. Alexander Makuliko  anasema hofu ya CCM ni kuwa ndio iliyouasisi Muungano wa Serikali mbili, hivyo  isingependa hali hiyo ibadilike.
Anaendelea kusema kuwa CCM imezoea mfumo huu na kuwa ikiukosa itaathirika, kwakuwa ni sera yake na imekuwa ikiitekeleza, lakini msimamo wa  wananchi ndiyo kitu cha msingi kuzingatiwa. Hoja zijengwe na zisikilizwe, ubabe hautakiwi, busara inahitajika zaidi.
Anasema pamoja na suala la  Serikali mbili kuwa  ni pimajoto ya  uhai wa CCM,  hata hivyo hoja zinazotolewa katika kutetea msimamo wao ni nzuri tu na zinazoeleweka vyema.
“Sioni kama wanang’ang’ania, lakini ukweli ni kuwa kila chama kina sera yake, na CCM kimeweka sera yake katika suala la Muungano wao wanasema ni Serikali mbili, na siyo tatu…kwamba tatu zitaongeza gharama na mengineyo, ni sababu za msingi kabisa,” anasema.
Anaongeza kuwa hoja zinazotolewa na chama tawala ni kubwa na siyo za kupuuzwa, lakini vilevile kero zinazotajwa kuhusu mfumo wa Muungano uliopo nazo zipo na zinaweza kutatuliwa katika mfumo uliopo.
“Unajua hivi vyama kila kimoja kinataka kuvutia kwake, hata bila rasimu ya Warioba…Ninashauri walete hoja, kisha watu wazipime hizo hoja, kwanini serikali mbili, na wale wa tatu tayari wameleta hoja na ushahidi, watu waachwe wapime,” anasema na kuongeza:
‘’Jambo la msingi kuzingatiwa ni kuwa mawazo ya wananchi wengi yataonekana wakati wa kura za maoni. Angalizo ni  kuhakikisha kuwa kura hiyo isije ikachakachuliwa.’’

.. Samuel Sitta awekwa mtegoni

Dodoma/Dar. Suala la ama kutumia kura ya siri au ya wazi kuamua ibara za Rasimu ya Katiba jana liliuteka upya mjadala wa Kanuni za Bunge la Katiba, huku ikielezwa kuwa limewekwa kama mtego kwa Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta katika kuwania urais.
Sitta ni mmoja wa wanasiasa wanaotajwa kuwa katika kinyang’anyiro cha urais katika uchaguzi mkuu ujao kupitia CCM, huku akikabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa mahasimu wake kisiasa ndani ya chama hicho.
Mjumbe wa Bunge la Katiba, Godbless Lema alimtaka Sitta kuwa makini na maelekezo aliyodai mwenyekiti huyo anapewa katika uendeshaji wa Bunge na kudai pia kuwa, kuna kundi la watu wanaotaka urais katika Uchaguzi Mkuu 2015 wanaotaka kumkwamisha.
Akichangia hoja ya mapendekezo ya mabadiliko ya kanuni yaliyotaka kupitishwa mifumo miwili ya kura kwa wazi na siri, Lema ambaye ni Mbunge wa Arusha alisema kwa mazingira ambayo yanaendelea, Sitta anapaswa kuwa makini na watu wanaompatia maelekezo wakitaka aonekane hafai baadaye.
“Ni vyema ukawa makini na mapendekezo unayoletewa kwa sababu hao wote pamoja na wanachama wa chama chako wanajua kama utaliongoza vizuri Bunge hili, basi unaweza ukapata tiketi ya kugombea urais 2015 ndani ya chama chako, lakini ukishindwa watakudhihaki kuwa umeshindwa, hivyo hutaweza kuliongoza taifa,” alisema Lema huku Sitta aliyeonekana awali akitabasamu, alibadilika na kumtazama mbunge huyo kwa umakini.
Lema alisema miongoni mwa wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM na kamati nyingine za Bunge hilo, kuna watu ambao wanataka kugombea urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Katika mjadala huo, ilionekana wazi kuwa wajumbe bado wamegawanyika pande mbili – CCM wakionekana kuunga mkono kura ya wazi na upande wa upinzani wakipigia chapuo kura ya siri.
Miongoni mwa waliopigia debe kura ya siri ni John Mnyika aliyesema suala la upigaji kura ni la kikatiba ili kuhakikisha kila mjumbe anapiga kura yake bila kushurutishwa, kushinikizwa wala kupokea maelekezo kutoka kwa mtu au chombo chochote.
Wajumbe hao walikuwa wanajadili mapendekezo yaliyowasilishwa jana na Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge, Pandu Ameir Kificho, baada ya juzi kuzua mvutano uliosababisha Bunge hilo kuvunjika ili kusubiri maridhiano ya pande zinazopingana.
Mapendekezo ya Kanuni
Kificho alisema, mapendekezo hayo yamefikiwa kutokana na masharti ya kanuni ya 59 (1) na 87 (1) kwamba kanuni ya 38 (1) iweke utaratibu wa kupiga kura ama ya wazi au ya siri, ambao utatekelezwa na mwenyekiti kwa kushauriana na katibu.
Alisema wakati wa kupiga kura ya siri kila mjumbe atapiga kura ya ‘ndio’ au ‘hapana’  kwa kutumia karatasi ya kupigia kura itakayokuwa imeandaliwa na katibu kwa ajili ya hilo.
Mjumbe Michael Laizer alisema wamechoshwa  na malumbano juu ya kura za wazi au siri, hivyo iwapo kuna wajumbe ambao hawataki mapendekezo ya kamati waondoke.
Naye Ezekiel Olouch alisema utaratibu unaopendekezwa na kamati haujawahi kufanyika mahala popote duniani.
Alisema kura ya siri imekuwa ikitumika kuamua mambo ya msingi na kuepusha mpasuko katika jamii hasa katika masuala ambayo yanaweza kuligawa taifa.
Mohamed Raza alisema msimamo wake ni kupiga kura ya wazi kwani wengi wanajua msimamo wake ambao ametoka nao Zanzibar.
Joshua Nassari alisema anashangazwa kuona Taifa linarejeshwa katika karne ya 18 katika upigaji wa kura kwa kung’ang’ania kura ya wazi wakati wao wamechaguliwa kwa kura za siri.
“Mwenyekiti wewe tumekuchagua kwa siri wajumbe wote wamepatikana kwa siri, iweje leo kulazimisha kura ya wazi ili wajumbe wa CCM watakaopiga kura za siri wachukuliwe hatua,” alisema Nassari.