Friday, 6 September 2013

Tunataka Katiba ya mwafaka, siyo jeuri na kiburi

Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa siku mbili mfululizo umekuwa shubiri bungeni.
Juzi wabunge wote wa kambi ya upinzani kutoka vyama vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi walitoka bungeni kuonyesha kutokufurahishwa kwao na uamuzi wa kukataliwa kwa pendekezo la kuuondoa kwanza bungeni ili kutoa fursa kwa wadau wa Zanzibar kutoa maoni yao.

Jana ilikuwa ni tafrani tena baada ya pendekezo la kutaka kuondolewa bungeni kwa muswada huo kukataliwa baada ya kupigwa kura hali iliyoishia kiti cha spika kuamuru Kiongozi wa Kambi Rasmi Bungeni, Freeman Mbowe, kutoka nje kwa madai kuwa alikataa kutii kiti.

Hali iliyoonekana bungeni haikuwa nzuri kwa vigezo vyovyote vile.

Muswada huu umekuwa na mwelekeo unaovunja maelewano, mshikamano na kuna kila dalili kwamba wabunge wa kambi ya upinzani wanaamini kwamba serikali inatumia nguvu zake hasa kwa kujiegemeza kwenye wingi wa wabunge wake kuupitisha muswada huo.

Tangu jana asubuhi kulikuwa na dalili kwamba baadhi ya wabunge hawakuwa radhi muswada huo ujadiliwe katika mkutano wa sasa na badala yake walikuwa wanaomba uondolewe bungeni ili kufanya mashauriano.

Swali aliloulizwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwake, kama hakuona ni busara kwa serikali kuondoa muswada huo bungeni, ilikuwa ni kielelezo kingine cha kuonyesha kwamba bado kulikuwa na mwako mkubwa wa kisiasa kwamba mambo hayakuwa yamekaa sawa juu ya muswada huo.

Kimsingi muswada huu ni sehemu ya mchakato wa kuandika katiba mpya ambayo inatarajiwa kwamba ifikapo mwaka 2015 itakuwa tayari ili itumike kwenye uchaguzi mkuu wa rais na wabunge.

Hadi sasa Tume ya Katiba imekwisha kupokea maoni ya wananchi juu ya katiba wanayoitaka, imetayarisha rasimu ya katiba, imeunda mabaraza ya katiba, na yatari mjadala wa mabaraza umemalizika juu ya rasimu husika na mapendekezo yamewasilishwa kwa Tume.

Hata hivyo, pamoja na hatua zozote zilizopigwa hadi sasa juu ya mchakato wa katiba mpya, safari bado ni ndefu na ngumu. Ugumu wa safari hii unajikita kwenye jambo muhimu kubwa, maelewano ya kisiasa.

Kwamba ni kwa kiwango gani wadau wote kwa ujumla wao, iwe ndani ya bunge, nje ya bunge, ndani ya  baraza la wawakilishi, kwenye vyama vya hisari na kila mwenye kuitakia nchi hii mema na anayeweza kuwa na maoni juu ya  mchakato huu, wamehusika katika kuandaa sheria ambayo mwisho wa siku itawapatia katiba nzuri ambayo ni sheria mama.

Kwa upeo wetu, kazi ya kutunga katiba kwa mataifa mengi imekuwa ya mgogoro mkubwa sana. Yapo mataifa mengi ya Afrika ambayo yaliishia kusambaratishana kwa sababu tu ya kushindwa kuendesha vema mchakato wa katiba.

Kwa Tanzania kumekuwa na mwanzo mzuri. Awali kulikuwa na kishindo kilichosababisha rasimu ya awali ya sheria ya kuundwa kwa Tume ya Katiba kuamsha taharuki kubwa. Hali ilitulizwa kwa mazungumzo na kuingiza ndani ya muswada yale yote yaliodhaniwa kuwa na umuhimu wa kuzingatia maslahi mapana ya kitaifa.

Lakini pia kuna wakati Rais Jakaya Kikwete kwa hekima zake, aliamua kusikiliza kilio cha baadhi ya vyama vya siasa hata pale sheria ilipopitishwa kwa msukumo tu wa wingi wa wabunge wa chama tawala, bila kuzingatia maslahi mapana ya kitaifa.

Rais aliita makundi ya vyama vya siasa Ikulu na kupokea mawazo na mapendekezo yao ambayo yalizaa marekebisho ya sheria ya kuundwa kwa Tume ya Marekebisho ya Katiba.

Umauzi wa Rais Kikwete ulifikiwa bila kujali kwamba waliokuwa wamepitisha muswada husika walikuwa ni wabunge wa chama chake tena wakiwa wengi ndani ya bunge.

Hakung’ng’ana tu na hoja ya wingi wa wabunge wake. Hakubweteka tu kwa kuwa ana wabunge zaidi ya theluthi mbili wanaotokana na chama chake, ila  alisukumbwa na  hoja ya kutaka kuona makubaliano ya pamoja yanafikiwa katika machakato wa katiba mpya.

Kila sauti na hoja yenye nguvu inasikika, inazingatiwa kwa kuwa katiba ni maafikiano ya kitaifa kuliko dhana tu ya wengi wape.

Ni kwa msingi huu sisi tunasema kuwa mijadala ya kisiasa katika kutengeneza sheria katika mchakato mzima kuelekea kupatikana kwa katiba mpya, ni lazima dhana ya makubaliano ya kitaifa itawale akili za wale wote wanaodhani kwamba leo wako salama sana kwa sababu tu wanatokana na upande wa chama kinachounda serikali.

Ni vema ikaeleweka kwamba katiba ni zaidi ya vyama vya siasa. Ni zaidi ya uanachama wa chama cha siasa; ni misingi wa haki, uhuru na wajibu katika taifa.

Wapo wabunge wengi ndani ya bunge la sasa ambao awali hawakuwa wanachama wa vyama ambavyo vimewapa uwakilishi. Lakini, katiba ni ile ile, wakiwa chama tawala, wakiwa upinzani na vinginevyo.

Tunaasa kwamba hasira, jeuri, kiburi na unazi havitatupa katiba mpya inayokidhi vizazi vya sasa ni vijavyo. Tuwe makini.
CHANZO: NIPASHE

Tusipokuwa makini tofauti hizi zitaiua EAC


Sasa ni bayana kwamba tofauti zilizopo miongoni mwa baadhi ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), zimeanza kukuzwa, huku wachambuzi wa masuala ya kidiplomasia wakionya kwamba tofauti hizo zisipotatuliwa haraka jumuiya hiyo itasambaratika na kubaki historia.

Sote tunatambua kwamba tofauti hizo zilianza baada ya Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania kumshauri Rais Paul Kagame kuzungumza na FDLR ambao ni waasi wa nchi hiyo wanaohusishwa na mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.
Rais Kikwete pia alimshauri Rais wa Uganda, Yoweri Museveni kuzungumza na waasi wa nchi hiyo ADF, akisema hatua hiyo italeta amani ya kudumu katika ukanda mzima wa Maziwa Makuu.
Kwa bahati mbaya Rais Kagame alikasirishwa na ushauri huo. Alisema ushauri wa Rais Kikwete yalikuwa matusi kwa Rwanda na kusema nchi hiyo haiwezi kamwe kuzungumza na watu waliofanya mauaji ya kimbari.
Kiongozi huyo alitoa kauli zisizokubalika kidiplomasia dhidi ya Rais Kikwete ambaye aliamua kuzipuuza, ingawa baadhi ya vyombo vya habari nchini Rwanda vimeendeleza vita ya maneno.
Tunashawishika kusema kwamba Rais Museveni kwa kukaa kimya aliukubali ushauri wa Rais Kikwete au alifanya hivyo tu ili kuepusha kukua kwa mgogoro huo. Wapo wanaosema Rais Kikwete alitoa ushauri huo kwa nia njema, lakini wakosoaji wake wanasema pamoja na nia yake hiyo kuwa ya dhati kabisa, angeutoa faragha kwa Rais Kagame au katika vikao mwafaka vya EAC badala ya kufanya hivyo katika kikao cha Umoja wa Afrika (AU), kilichofanyika Addis Ababa, wakisema huko hapakuwa pahala pake.
Hilo hakika ndilo chimbuko la mgogoro tunaoushuhudia hivi sasa ambao tunadhani umekuzwa kupita kiasi tukitilia maanani matukio ambayo yamekuwa yakitokea katika siku za hivi karibuni. Hata hivyo, zipo tetesi pia kwamba Rwanda haikufurahishwa na kitendo cha Tanzania kukubali kupeleka wanajeshi wake nchini DRC kuungana na kikosi cha Umoja wa Mataifa (UN), kulinda amani nchini humo kwa lengo la kuwanyang’anya silaha waasi wa M23 wenye asili ya Rwanda.
Tumelazimika kuandika hayo yote ili kuweka kumbukumbu sahihi za mtiririko wa mgogoro huo ambao baadhi ya watu walidhani ungeziingiza nchi hizo mbili jirani katika vita.
Hivi sasa umefanyika mkakati wa kuitenga Tanzania kiuchumi ambapo juzi marais wa Kenya, Uganda na Rwanda waliungana kuzindua upanuzi wa Bandari ya Mombasa inayokusudiwa kutumiwa na nchi hizo kupakua na kusafirisha mizigo. Mkakati huo ulizinduliwa na marais wa nchi hizo mjini Entebbe hivi karibuni ambapo Tanzania haikualikwa kama ambavyo haikualikwa juzi wakati wa uzinduzi huo.
Tofauti zinazoendelea kujitokeza hakika sio ishara njema kwa mustakabali wa EAC. Siku chache zilizopita uliibuka mzozo miongoni mwa wabunge wa EAC jijini Arusha ambapo wabunge wa Uganda, Kenya na Rwanda walisababisha kikao cha Bunge kuvunjika ili kumshinikiza Spika aruhusu kujadiliwa kwa hoja ya vikao vya Bunge kufanyika kwa mzunguko katika nchi wanachama badala ya Tanzania pekee.
Wabunge wa Tanzania nao walifanya hivyo siku iliyofuata wakipinga hatua ya wabunge hao kutaka kumshinikiza Spika kukubali hoja hiyo kinyume na Kanuni za Bunge.
Kwa mwenendo huo sisi tunadhani kuna ajenda ya siri iliyofichwa chini ya zulia. EAC inachungulia kifo. Zinahitajika busara kuinusuru. Vinginevyo, historia ya EAC ya mwaka 1977 itajirudia.

Ghasia kubwa zalipuka kupinga muswada

Dodoma. Jana, Bingwa wa Dunia wa uzani wa kati (super middle), unaotambuliwa na Shirikisho la Ngumi Duniani (WBF), Francis Cheka alitembelea Bunge baada ya kutwaa taji hilo karibuni na jana hiyohiyo, Bunge hilo lilishuhudia ngumi kavukavu katika vurugu kubwa pengine kuliko zote zilizowahi kutokea katika ukumbi wake.
Katika masumbwi hayo yasiyo rasmi, Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ anadaiwa kumpiga kichwa Askari wa Bunge na kumchania sare na kung’oa kipaza sauti.
Mbilinyi jana alisema alikuwa anatafutwa na polisi huku akisema hilo limemshangaza akidai kwamba yeye ndiye aliyeshambuliwa na askari huyo.
Vurugu hizo zilitokea baada ya Naibu Spika, Job Ndugai kuamuru kutolewa nje kwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
Katika vurugu hizo Mbilinyi alibebwa juujuu na polisi hadi nje ya ukumbi huku akiwa hana viatu.
Pamoja na tafrani hiyo, Ndugai alisema wakati akihitimisha kikao cha Bunge kipindi cha asubuhi kuwa amewasamehe wabunge wote waliohusika na kosa hilo la utovu wa nidhamu na kuwaruhusu kurejea kipindi cha jioni kuendelea na Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Hata hivyo, wabunge wote CUF, NCCR-Mageuzi na Chadema ambao baada ya tukio hilo walitoka nje ya ukumbi, hawakurejea na baadaye walitoa msimamo wa pamoja wakisema hawatashiriki katika mjadala huo.
Msimamo huo ulitolewa na Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Mbunge wa CUF, Habib Mnyaa.
Mbowe alisema wameamua kususia majadiliano hayo kuonyesha msimamo wao wa kupinga kupitisha mambo yasiyo na masilahi kwa nchi.
“Hatuko tayari kushiriki katika uchakachuaji wa Katiba... Matumizi ya nguvu ya polisi kamwe hayatatupatia Katiba nzuri,” alisema. Alisema kambi rasmi ya upinzani inalaani vikali kitendo cha Ndugai kuruhusu Bunge kunajisiwa kwa kuruhusu polisi kuingia ndani kinyume na kanuni.
Mnyaa alisema kitendo cha wadau wa Zanzibar kutoshirikishwa katika kutoa maoni yao katika muswada huo wa marekebisho ni dharau kubwa.
Mbatia alisema Tanzania haiwezi kuingia Uchaguzi Mkuu wa 2015 kwa kutumia Katiba ya sasa kwa sababu tayari kuna mgongano wa kikatiba kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu alimtaka Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Kuu, (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi kutoa ushahidi kama Rais aliteua wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kulingana na mapendekezo ya taasisi zao.Kuanza kwa tafrani
Sakata hilo lilianza saa 6:45 mchana muda mfupi baada ya kukamilika kwa kura kuamua kama Bunge liahirishwe au la kutokana na hoja iliyotolewa na Mbunge wa Mkoani (CUF), Ali Hamisi Seif (CUF). Waliotaka liahirishwe walipata kura 59 na waliokataa 159.
Baada ya Ndugai kutangaza matokeo hayo na kutaka shughuli za Bunge ziendelee, Mbowe aliposimama na kusema ana hoja Naibu Spika alimwamuru akae chini.
Baada ya Mbowe kusisitiza ana hoja na kumwomba Spika amsikilize ndipo Ndugai alipomwamuru atoke nje na alipokaidi alisema:” Naomba askari wote waliopo katika mazingira haya (ya Bunge) waingie ndani ya ukumbi wa Bunge”.
Baada ya kitambo kifupi, Mbowe akiwa bado amesimama alitoa maagizo atolewe nje: “Kiongozi wa upinzani atolewe nje.”
Polisi waliingia ndani ya Ukumbi wa Bunge lakini Wabunge wa Kambi ya Upinzani kwa umoja wao, walimzinga Mbowe asifikiwe na askari hao.
Baada ya kuona polisi wanaelekea kushindwa, Ndugai alitoa maagizo mengine: “Askari hamjaletwa humu ndani kufanya majadiliano mnatakiwa kuhakikisha kiongozi wa upinzani anatolewa nje”.
Alisema yeye ndiye anayeendesha kikao hicho hivyo lazima Mbowe atolewe nje.
Hapo ndipo wabunge hao wa upinzani walipoanza kuimba: “Hatutaki kuburuzwa hatutaki kuburuzwa… hatutaki kuonewa,” huku wakiendelea kumzinga Mbowe.
“Askari wote mliopo humu ndani naomba mnisikilize… Sasa naagiza kwa mara ya mwisho... nasema kiongozi wa upinzani atolewe nje.”
Ngumi zarushwa
Baada ya kauli hiyo ya Ndugai, ndipo polisi walipotumia nguvu hasa kwa Mbilinyi na Mbunge wa Maswa Mashariki (Chadema), Silvester Kasulumbai.
Katika patashika hiyo, inadaiwa kwamba Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Moses Machali alipigwa ngumi ambayo ilimfanya apepesuke hadi sakafuni.
Kilichomponza Mbilinyi ni hatua yake ya kusogelea Siwa. Polisi waliokuwa karibu, walimbeba juujuu hadi nje ya ukumbi.
Wakati akitolewa nje ya ukumbi, alijaribu kujizuia kwa kushika kipaza sauti kinachotumiwa na upande wa upinzani hadi kikang’oka.
Mbunge wa Viti Maalumu (CUF), Mozza Abeid, alivuliwa hijabu katika vurumai hizo wakati polisi walipokuwa wakitumia nguvu ili kumfikia Mbowe.
Baada ya kuona hali inazidi kuwa mbaya, Mbowe aliamua kutoka nje huku akisindikizwa na polisi pamoja na wabunge wa vyama hivyo na alipofika nje ya ukumbi alipokewa na polisi wa kawaida waliomweka chini ya ulinzi kabla ya kumwachia baada ya ombi la Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini.
Kutokana na hali ya mambo kuwa tete, askari wa Bunge waliwaondoa wageni waliokuwa wamekaa katika kumbi za wageni wakiwamo wanafunzi wa shule mbalimbali za sekondari huku baadhi ya wabunge wa CCM waliokuwa na simu za kisasa za mkononi na kompyuta mpakato (Ipad) wakichukua picha za tukio zima.
Inadaiwa kwamba baada ya kutoka nje ya ukumbi, Mbilinyi alimtwanga ngumi mmoja wa askari waliomtoa kwa nguvu kabla ya kuamuliwa na wabunge na polisi.
Wakati wote huo, wafanyakazi wa Bunge na wageni walionekana wakiwa wamejikusanya katika makundi wakitafakari na kushangaa yaliyokuwa yakitokea.
 Balaa lilivyoanza
Akitumia Kanuni ya 69(1), Mbunge wa Mkoani (CUF), Ali Hamisi Seif, alitaka kuahirishwa kwa mjadala wa Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013 kutokana na ukweli kuwa Kamati ya Sheria, Katiba na Utawala ya Bunge ilipaswa kukusanya maoni ya wadau mbalimbali nchini ikiwamo upande wa Zanzibar jambo ambalo halikufanyika wakati wa maandalizi ya muswada huo.
“Ilipaswa sheria hii inapotaka kufanyiwa marekebisho iende tena kulekule Zanzibar lakini jambo la kusikitisha kamati inayohusika na masuala ya Katiba haikwenda. Mimi ni mjumbe wa kamati na tuliitwa Dar lakini ratiba waliyotupa haikuonyesha kama tungekwenda Zanzibar,” alisema. Mkosamali naye aliomba mwongozo kwa Spika, akisema kwa kuzingatia matakwa ya kiapo cha Spika au Naibu alipaswa kuendesha Bunge kwa haki bila upendeleo.
“Kanuni inasema Spika ama Naibu Spika ama Mwenyekiti ataendesha shughuli za Bunge kwa haki, uadilifu, bila chuki wala upendeleo wowote kwa kuongozwa na Katiba ya nchi,” alisema na kuongeza: “Kwa kuwa sisi tumekuweka hapo ili uendeshe Bunge kwa uadilifu, usiburuzwe na chama chako na uzingatie miongozo yote kwa wakati. Kwa nini usitumie mamlaka yako kuondoa muswada huu”?
Mbunge wa Peramiho (CCM), Jenister Mhagama aliomba mwongozo kwamba kwa kuwa bado kuna malalamiko basi waipe Serikali nafasi ya kuthibitisha kwamba majadiliano ya kamati yalikamilika.
Lissu katika kuomba mwongozo wake, alisema Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria, Katiba na Utawala, Pindi Chana alilidanganya Bunge alipowasilisha maoni ya kamati kwamba wadau wa muswada huo walishirikishwa jambo ambalo alisema si kweli.
Lissu alisema hakuna Mzanzibari aliyefika mbele ya kamati hiyo kutoa maoni kuhusu muswada wowote.
Hata hivyo, Chana alijibu akisema wadau wa Zanzibar walitoa maoni yao na kukabidhi nyaraka mbalimbali kwa Spika kuthibitisha kauli yake hiyo. Alivitaja vyama vya Jahazi Asilia na ADC kuwa vilihojiwa.
Kwa upande wake, Lukuvi alimshambulia Lissu kwa kauli yake ya juzi kwamba uteuzi wa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba uliofanywa na Rais Jakaya Kikwete ulikuwa na walakini. “Lissu alisema jana (juzi) kwamba wapo wadau ambao walisema ijapokuwa waliandikiwa barua ya kuwasilisha majina matatu kila moja ili Rais ateue mmoja lakini hakuna mjumbe aliyeteuliwa”.
Alitaja majina ya walioteuliwa kuwa ni Maria Kashonda (Tec), Jesca Mkuchu (CCT), Humphrey Polepole (Civil Society) na Profesa Palamagamba Kabudi (Kundi la Wasomi).
Lukuvi aliwataja wengine waliopendekezwa na taasisi zao na Rais kuwateua kuwa ni Mwamtumu Malale (Bakwata) na Dk Sengondo Mvungi (NCCR) na Profesa Mwesiga Baregu wa Chadema.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Fredrick Werema alisema katika mchakato wa muswada huo, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) iliwasilisha maoni yake mbele ya kamati.
Alisema Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi aliwasilisha kwa kamati mapendekezo ya SMZ, Mei mwaka huu na mapendekezo hayo ikiwamo uteuzi wa wajumbe 166 yalizingatiwa.
 Waacha muswada, wapiga vijembe
Baada ya kurejea katika kikao cha Bunge cha jioni jana, wabunge wa CCM waliopewa fursa ya kuchangia mjadala wa muswada huo walitumia muda mwingi kuwajadili wabunge wa kambi ya upinzani.

Monday, 29 July 2013

Utafiti:Sera ya uwekezaji madini hainufaishi jamii

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Uhasibu Arusha na Mchumi, Balozi Morwa alitoa mapendekezo hayo juzi, wakati akiwasilisha utafiti kuhusu wajibu wa kampuni kwa jamii(CSR),uliofanyika katika machimbo ya Tanzanite Mirerani, wilayani Simanjiro Mkoa wa Manyara.
Arusha. Serikali imeshauriwa kubadili sera ya uwekezaji nchini kwa kulazimisha kisheria kampuni za wawekezaji hasa wa Sekta ya Madini, kutekeleza miradi ya jamii inayozunguka maeneo yao ya uchimbaji badala ya suala hilo kuwa ni la hiari.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo cha Uhasibu Arusha na Mchumi, Balozi Morwa alitoa mapendekezo hayo juzi, wakati akiwasilisha utafiti kuhusu wajibu wa kampuni kwa jamii(CSR),uliofanyika katika machimbo ya Tanzanite Mirerani, wilayani Simanjiro Mkoa wa Manyara.
Morwa akiwasilisha utafiti huo ,ambao uliratibiwa na Mtandao wa Mashirika yasiyo ya kiserikali ya Mkoa wa Arusha kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Finnish NGO Platform, alisema wamebaini kuwa jamii zinazozunguka migodi ya Tanzanite hazinufaiki ipasavyo.
Morwa alisema utafiti huo, ulihoji watu 350 na nyaraka kukusanywa,wamebaini,wajibu wa kampuni ya wawekezaji kwa jamii ukiwa wa kisheria kama Ghana, utawanufaisha na ikishindika ifutwe na kampuni hizo zilipe kodi kubwa kama nchi nyingine.

Tume ya Uchaguzi itasababisha vurugu

Uchaguzi mdogo wa madiwani katika kata nne za Jimbo la Arusha Mjini ulifanyika juzi, ambapo Chadema kiliibuka mshindi katika kata zote nne za Themi, Kimandolu, Elerai na Kaloleni.
Kata hizo zilikuwa wazi tangu mwaka 2011 baada ya madiwani wake kutimuliwa uanachama na chama hicho kwa kwenda kinyume na msimamo wa chama chao kuhusu kutomtambua Meya wa Jiji la Arusha.
Kinyume na matarajio ya wengi, uchaguzi huo ulikuwa na idadi ndogo sana ya wapigakura kulinganisha na chaguzi zilizopita, kwani kati ya wapigakura zaidi ya 60,000 waliojiandikisha ni 11,042 tu waliojitokeza kupiga kura.
Kwa mfano, Kata ya Elerai inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya wapigakura 23,885 lakini waliojitokeza kupiga kura juzi ni 3,824 tu.
Takwimu hizo zinaibua maswali magumu, hasa kuhusu hali inayoendelea kujitokeza ya kudidimia kwa demokrasia nchini.
Takwimu hizo zinatoa tahadhari ya kishindo kwamba huko tuendako sio salama na kwamba nchi yetu inakabiliwa na maangamizi makubwa iwapo Serikali haitaweka mazingira ya kuwawezesha wananchi kushiriki katika chaguzi mbalimbali pasipo kuhofia maisha yao.
Kutojitokeza kwa idadi kubwa ya wananchi kupiga kura katika uchaguzi wa Arusha juzi kumehusishwa na hofu iliyotokana na bomu lililorushwa katika mkutano wa kufunga kampeni za udiwani za Chadema mwezi uliopita ambapo watu wanne walikufa na wengine 60 kujeruhiwa, hivyo kusababisha kuahirishwa kwa uchaguzi katika kata hizo hadi juzi.
Lakini pia utendaji mbovu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Tec), katika chaguzi mbalimbali, ukiwamo wa juzi jijini Arusha pia umedhihirisha kwamba huko tuendako hapatakuwa salama iwapo tume hiyo haitafanyiwa mabadiliko makubwa.
Tunalazimika kusema hapa kwamba yafaa tutumie fursa tuliyonayo hivi sasa ya kuandika Katiba mpya kuhakikisha kwamba Katiba hiyo inatuzawadia Tume ya Taifa ya Uchaguzi iliyo huru na yenye uwezo wa kufanya kazi kwa ufanisi wa hali ya juu.
Uchaguzi wa juzi jijini Arusha umedhihirisha ulegelege na udhaifu mkubwa uliopo katika Tume hiyo. Pamoja na kuwa na uzoefu wa kutosha katika kusimamia chaguzi mbalimbali, Tume hiyo haionyeshi kubadilika wala kuwa na dira na mwelekeo wa kuiwezesha kwenda na wakati kuhakikisha chaguzi zinafanyika kwa mujibu wa sheria.
Kama tulivyoshuhudia katika uchaguzi wa Arusha juzi, kasoro ambazo zingeweza kuzuilika zimeendelea kujitokeza na nyingi zimekuwa zikijirudia kutokana na watendaji wa taasisi hiyo nyeti kufanya kazi kwa mazoea tu.
Pamoja na wananchi kuwa na shahada halali za kupigia kura na majina yao kubandikwa katika mbao za matangazo, baadhi yao walizuiwa kupiga kura kutokana na Daftari la Wapigakura kutokuwa na majina, maelezo na picha zao.
Baadhi ya majina ya wapigakura yalitokea zaidi ya mara moja wakiwa na namba tofauti, huku wataalamu wa mifumo ya kompyuta wakisuasua kurekebisha matatizo yaliyojitokeza.
Matatizo hayo, ikiwa ni pamoja na Tume kushindwa kuhakiki Daftari la Wapigakura mara kwa mara ni viashiria vya vurugu katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, kwani wananchi hawatakubali kuondoka vituoni pasipo kupiga kura kwa uzembe tu wa Tume hiyo.
Hii pengine inadhihirisha kwamba haitaweza hata kutumia teknolojia ya kisasa kuhesabu kura mwaka 2015. Matokeo yake ni vurugu zitakazotokana na kasoro hizo.

Bajeti finyu kikwazo cha kupata haki mahakamani-Jaji mkuu Tz



Dar es Salaam. Jaji Mkuu wa Tanzania, Mohammed Chande Othman, amesema ni vigumu mahakama kama taasisi ikaweza kutoa haki kwa wakati kama haitaweza kujitosheleza kimapato.
Aliyasema hayo jana Dar es Salaam alipokuwa akizindua kitabu kilichoandikwa na Jaji Mkuu Mstaafu, Barnabas Samatta kiitwacho ‘Uhuru wa Mahakama’ na kuchapishwa na Kampuni ya Mkuki na Nyota.
“Uhuru wa kitaasisi ambao haujakamilika ni ule wa kifedha na kimiundombinu, bila huu kukamilika ni vigumu kila mwananchi kuweza kupata haki kwa wakati,” alisema Jaji Chande.
Alisema licha ya kuwa Serikali imekuwa ikijitahidi kuongeza bajeti ya mahakama, bado lengo halijafikiwa na kuwa ni vyema muhimili huo ukatengewa fedha za kutosheleza kuendesha shughuli zake.
Jaji Chande alisema kuwa, katika bajeti ya mwaka 2013/14 muhimili huo umetengewa Sh160 bilioni ingawa mahitaji yake halisi ni Sh300 bilioni.
Alisema pia kuwa,kitabu hicho kitawasaidia viongozi wengi ambao wamekuwa wakidhani kuwa mahakama ni chombo cha Serikali. “Wakisoma kitabu hiki wataelewa na wataachana na dhana hii,” alisema Jaji Chande.
Akizungumzia maudhui yaliyopo kwenye kitabu hicho kilichoandikwa kwa lugha ya Kiswahili, Jaji Chande alisema kuwa kimelenga kumsaidia mwananchi wa kawaida kuijua mahakama na pia watawala, vyama vya siasa na wanasheria watapata mwongozo makini.
Kwa upande wake Jaji Samatta alisema kuwa, mwanzoni kabisa wazo lake lilikuwa ni kuandika juu ya kesi ambazo zimewahi kutikisa nchini kwa upande wa Tanzania bara na Zanzibar.
Alisema, alikuja kuachana na wazo hilo baada ya kuona hapati baadhi ya vielelezo ambavyo vingemwezesha kuandika kitabu hicho.

Saturday, 20 July 2013

TENDWA HAMA CHOHOTE KITAKACHO ANZISHA KAMBI YA MAFUNZO YA KIJESHI TUNAKIFUTA

OFISI ya Msajili wa Vyama Vya Siasa nchini imevitaka vyama vya siasa kutii agizo la kutoanzisha kambi za mafunzo ya kulinda amani maarufu kwa jina la mgambo , huku ikisisitiza kwamba itachukua hatua za kisheria kwa chama chochote kitakachoiuka , ikiwemo kukifuta.

Aidha ofisi hiyo imesema kuwa Katiba ya nchi imempa jukumu kila mwananchi kulinda amani na usalama wa nchi, pia kujilinda yeye mwenyewe na mali zake kwa kutoa taarifa katika vyombo vya dola pale anaposikia au kuona mtu anataka kufanya au anafanya uhalifu au amemdhuru mtu.

Kauli hiyo imetolewa  jijini Dares Salaam na ofisi hiyo katika taarifa yake iliyoitoa kwa vyombo vya habari iliyotiwa saini na Rajab Juma kwa niaba ya Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa kufutia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutangaza hivi karibuni kinakusudia kuanzisha kambi za mafunzo ya kujilinda kwa vijana wake nchi nzima.

Alisema suala hilo lilitangazwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe na kuandikwa katika vyombo vya habari kabla ya chama hicho, kuwasiliana na taasisi husika ikiwemo ofisi hiyo ili kupata ushauri kuwa

Mbunge wa Bumbuli akataa kupokea mradi wa maji

lipangwa kujenga tanki lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita 135,000, lakini mkandarasi aliamua kujenga tangi lenye uwezo wa kuhifadhi lita 90,000 ili kuuunganisha na tanki la zamani lenye uwezo huohuo lakini mkandarasi hakuunganisha matanki hayo jambo ambalo ni kosa’’ alisema..

Tanga. Katika hatua inayoashiria kuchoshwa na utekelezaji usioridhisha wa miradi, Mbunge wa Jimbo la Bumbuli, wilayani Lushoto, January Makamba amekataa kuupokea mradi wa maji uliojengwa katika Halmashauri Mpya ya Bumbuli kutokana na kile alichokieleza kuwa umejengwa chini ya kiwango.
Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Bumbuli, Makamba, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia alisema kuwa mradi huo wenye thamani ya zaidi ya Sh400 milioni haukutekelezwa ipasavyo pamoja na kutengewa fedha nyingi na wahisani ambao ni Benki ya Dunia.
Mradi huo umepangiwa kuwanufaisha, wanakijiji katika vijiji vinne vya Bumbuli Mission, Bumbuli Kaya, Mboki na Kwamanolo na ulikuwa uanze kutoa huduma ya maji kuanzia Kijiji cha Kwamanolo.
“Ilipangwa kujenga tanki lenye uwezo wa kuhifadhi maji lita 135,000, lakini mkandarasi aliamua kujenga tangi lenye uwezo wa kuhifadhi lita 90,000 ili kuuunganisha na tanki la zamani lenye uwezo huohuo lakini mkandarasi hakuunganisha matanki hayo jambo ambalo ni kosa’’ alisema..
Alisema fedha zilizotumika na thamani halisi ya mradi ni tofauti na kwamba ni vigumu kwake kuamini kwamba mradi huo utatekelezwa kama ulivyokusudiwa awali.
Alisema ni afadhali asipokee kwanza mradi huo ili taratibu zingine za kuchunguza zifanyike kama ni kweli mradi huo utasambaza maji ya kutosha.

Masaibu haya ndiyo huwatokea wanawake ndani ya vyumba vya leba

Mwanahamisi Majube amelala katika kitanda cha hospitali moja ya umma (jina linahifadhiwa) ikiwa ni  saa chache  baada ya kufanyiwa upasuaji wa kujifungua.
Analia na kuugulia kwa uchungu, akilalamikia maumivu makali ya tumbo.
Kwa sababu hiyo, anamwita daktari akimweleza kuwa anahisi kuna kitu tumboni mwake na kinamuumiza mno,  lakini daktari anamjibu kuwa maumivu hayo yatatulia.
“Nisaidieni nitakufa kabla ya kumwona mtoto wangu, naumwa daktari, nakufa jamani,” anasema Mwanahamisi.
 Anapoendelea kuita, wakunga ndani ya wodi hiyo wanaibuka na kumjibu: “Acha kudeka, ulifikiri kuzaa ni kama kucheza kamari. Nyamaza, unawapigia kelele wenzako.”
Anaendelea kuita kwa zaidi ya saa lakini bila msaada wowote na baada ya kulia kwa muda mrefu, anatupa miguu huku na kule…ananyamaza, kisha anatulia. Kumbe… Mwanahamisi amekata roho!
 Mwanahamisi ni miongoni mwa wanawake wengi nchini ambao hukumbana na vifo vya kuepukika wakati wa kujifungua au muda mfupi baadaye.
Vifo hivyo, vingi vinasababishwa na uzembe wa madaktari, huduma dhaifu, ukosefu wa vifaa na sababu nyingine zinazozuilika wakati wa kujifungua.
 Pamoja na uchungu wa kujifungua anaoupata mwanamke, ukosefu wa vifaa tiba, maumivu mengine huyapata toka kwa baadhi ya  wahudumu wa afya.
 Hali hiyo imesababisha baadhi ya wanawake, hasa wale wanaojiweza kukimbilia katika hospitali binafsi ambapo wanapata huduma bora zaidi.
Hata hivyo, ni wanawake wachache nchini wenye uwezo huo na zaidi ya asilimia 80 wanategemea hospitali za Serikali ambazo  baadhi, ndizo zenye changamoto.
Katika mdahalo wa afya ya uzazi uliondaliwa na Dk Tausi Kida na Riziki Pansiano, wadau walikiri kuwa kuna matatizo mengi yaliyowakumba wanawake wakati wa kujifungua, kubwa likiwa rushwa na matusi.
Kwa mfano, wadau walieleza kuwa watoa huduma wengi, yaani wauguziwamelalamikiwa kuwa wanadai hongo ili waweze kutoa huduma kwa wagonjwa.
 Hii ni sababu mojawapo muhimu inayowafanya kinamama wasijifungue chini ya uangalizi wa wataalamu wa tiba kwenye vituo vyetu vya afya na hivyo kuwa kwenye hatari zaidi ya kupata matatizo wakati wanapojifungulia nyumbani.
“Niliwahi kushuhudia mama mjamzito kuachwa mapokezi mpaka kafariki bila hata kuhudumiwa. Ndugu wa dada huyu waliambiwa kuwa bila ya elfu 75 mgonjwa wenu hapati huduma kwa daktari. 
Kinamama hawa wakiendelea kuchangishana mmoja hadi mwingine wakifuata fedha hadi huko Morogoro, mwishowe baada ya saa karibu nane baada ya pesa kutopatikana mwenzetu akafariki.”
Wachangiaji pia walihusisha matatizo ya vifo na matusi na maneno ya kukatisha tamaa wanayoyatoa manesi kwa wajawazito.
 “Mama akiomba msaada utasikia mfuate huyo aliyekupatia mimba”. Alisema mchangiaji mmoja.
Maneno mengine yanayowatoka wauguzi ni kama vile usitusumbue hatupo kwa ajili yako hapa, mara unataka nijigawe ili nimhudumie huyu na wewe.
“Nimepata kumsikia nesi akisema kuwa huyu mwanamke asije akatulaza macho, anasema Dk. Salatiel Moyo, mchangiaji katika mjadala huo.
Takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa vifo vya uzazi Tanzania  ni 578 kati ya vifo 100,000 ambayo ni sawa na asilimia 18 ya vifo vyote vya wanawake wa kati ya miaka 15 hadi 49.
Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO), zinaeleza kuwa, asilimia 46 tu ya wanawake ndiyo husaidiwa na mtaalamu wa afya wakati wa kujifungua.
Faraja Mujuni, alimpoteza mtoto wake na kujikuta akiondolewa kizazi baada ya kupata uchungu pingamizi kwa muda mrefu.
“Kila nilipomwambia mkunga kuwa mtoto anatoka alikataa, kila nililomweleza alikuwa akiniangalia na kunifyonza, mwishowe, mtoto alifariki na mimi kuondolewa kizazi, kwani kilipasuka,” anasema Faraja.
Mwanamke mwingine, Anastazia Simwanza, mkazi wa Vingunguti jijini Dar es Salaam anasema alipofikishwa katika wodi ya wazazi, alikuta vitanda vimejaa, hivyo akaambiwa alale chini.
“Ilikuwa saa tisa usiku. Wakati huo uchungu ulikuwa ukiniuma kwa kasi, nikamwita nesi, lakini akaniambia bado kabisa mtoto hajashuka,”anasema Simwanza.
Simwanza anaeleza kuwa, baada  ya dakika kadhaa, chupa ilipasuka na mtoto akaanz saa kutoka, jambo lililosababisha ajifungue mwenyewe, bila msaada wa muuguzi na mtoto aliangukia chini sakafuni.
“Mwanangu alipata matatizo kwa sababu aliangukia sakafuni ndiyo maana hajatembea mpaka sasa wakati ana miaka sita,” anasema.
Paschal Msechu anaeleza jinsi yeye na mkewe mjamzito walivyotukanwana na wauguzi wakati mke wake alipokuwa akiugulia maumivu ya uchungu wa kujifungua.
“Kila nikijaribu kuwaeleza waliniambia niwaache wao wanajua kazi yao, walianza kumtukana mke wangu kwa sababu alikuwa hawezi kutembea, wakamrushia maneno mazito,” anasema Msechu.
 Si huyo tu, Yohana  Mwanga, anaeleza jinsi mke wake mpenzi alivyopoteza maisha kwa sababu  tu ya kukosa vifaa.
“Hatukuwa tumebeba vifaa vyote, wakati muuguzi ananiambia hayo, mke wangu alikuwa katika hali mbaya mno. Wakati natafuta hela za kununua, mke wangu alifariki kwa kukosa huduma.” Anasema Mwanga
 Mwanga, kwa masikitiko anasema: “Nimempoteza mke wangu kwa kukosa fedha tu, wala si kingine.”
Idadi kubwa ya vifo vya uzazi katika baadhi ya maeneo duniani inaonyesha ni kutokana na kukosekana kwa usawa katika upatikanaji wa huduma za afya, na inaonyesha pengo kati ya matajiri na maskini.
Karibu wote, vifo vya uzazi (asilimia 99 hutokea katika nchi zinazoendelea.
 Mhadhiri wa Chuo cha Wakunga katika Chuo Kikuu cha Sayansi ya  Tiba Muhimbili, Dk Sebalda Leshabari, anasema wakunga wenye tabia zinazolalamikiwa na wanawake wanafanya makosa kwani hawakufundishwa hivyo vyuoni mwao.
Hakuna mkunga anayefundishwa kuwa jeuri au kutukana, sisi tunawafundisha mawasiliano mazuri na mama mjamzito na ujuzi mwingine,’ anasema Dk Leshabari.
Anasema hata Chama cha Wakunga Tanzania (TMA) wakati wa makongamano hutoa elimu na kuwakumbusha wakunga kuhusu huduma nzuri kwa wajawazito.
“Hizo  shutuma  tunazisikia zote na tunawapa mifano wanafunzi wetu wasirudie  tabia hizo,” anasema
 Dk Leshabari pia anatoa angalizo zaidi na kusema mpaka sasa ni asilimia 61 tu ya wanawake Tanzania wanaojifungulia hospitali, je, wengine wanajifungulia wapi?  

Janjaweed wadaiwa kuhusika mauaji ya askari wa Tanzania

. Wakati miili ya wanajeshi saba wa Tanzania waliouawa nchini Sudan ikiwasili leo, taarifa zinadai kundi la Janjaweed ambalo linaungwa mkono na Serikali, linahusika katika mauaji hayo.
Wanajeshi hao wa Tanzania ambao ni sehemu ya Jeshi la Kulinda Amani la Umoja wa Mataifa (Unamid), waliuawa Julai 13 eneo la Kusini mwa Darfur.
Askari wengine 17 walijeruhiwa katika shambulio hilo na wanaendelea kupatiwa matibabu kwenye hospitali maalumu.
Taarifa za UN, zilieleza juzi kwamba ingawa kundi hilo halijatambuliwa rasmi, mashuhuda wamekuwa wakieleza mauaji hayo yamefanywa na kundi linaloungwa mkono na Serikali ya Sudan.
Kiongozi wa moja ya makundi ya wapiganaji la Sudan Liberation Movement (SLM), Minni Minnawi, ndiye aliyeibuka awali na kuwatuhumu mgambo wanaoungwa mkono na Serikali na kutaka ufanyike uchunguzi wa kimataifa.
Katika mahojiano yake na gazeti la Sudan Tribune alipokuwa akihudhuria mkutano wa majadiliano kuhusu namna ya kupata amani ya kudumu nchini Sudan uliofanyika mjini Geneva, Uswisi, Minnawi alikanusha tuhuma kwamba kundi lake linahusika na shambulio hilo.
Kiongozi huyo alikuwa akijibu tuhuma za Serikali ya Sudan kwamba, kundi lake ndilo lililohusika na shambulio hilo.
“Tuna uhakika shambulio lililofanywa dhidi ya walinzi wa amani wa Unamid liliandaliwa na kutekelezwa na Janjaweed, tuko tayari kutoa ushirikiano kwa chombo maalumu cha kimataifa kitakachoundwa kufanya uchunguzi kuhusu tukio hili,” alisema.
Alisema wanamgambo wa Janjaweed hivi sasa wanakabiliwa na ukata wa hali ya juu na ukosefu wa vifaa, kwa sababu Serikali haina tena uwezo wa kuwafadhili hivyo wameamua kufanya matukio ya uporaji kukidhi mahitaji yao.
Wanajeshi saba waliuawa kwenye shambulio lililotokea Julai 13 huko Khor Abeche, Nyala nchini Sudan wakati walinda amani.
Wakati huohuo, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limesema miili ya wanajeshi hao itawasili leo kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, (Terminal one) saa 9:00 alasiri.
“Baada ya kuwasili miili hiyo itapelekwa Hospitali ya Kuu ya Jeshi, Lugalo. Baada ya maandalizi, miili hiyo itaagwa rasmi kwa heshima zote Jumatatu kuanzia saa 3:00 asubuhi viwanja vya Wizara ya Ulinzi, Upanga, Dar es Salaam,” inasema sehemu ya taarifa hiyo.

Katika hatua nyingine, Msemaji wa Katibu Mkuu wa UN, Martin Nesirky, alisema walinda amani hao waliwekewa mtego wakiwa katika majukumu yao ya msingi ya kulinda amani. Alisema UN imeanza kufanya uchunguzi wake binafsi na kuitaka Serikali ya Sudan kuwasaka wahusika ili wawajibishwe.