Mwanzo wa maendeleo ya kweli kwa nchi yoyote duniani kama historia
inavyodhirisha, ni pale watumishi na wafanyakazi
wanapobadilika na kujitambua kutokana na kuwepo sera na mifumo ya
usimamizi nautendaji kazi inayotambua nafasi, stahili au haki, wajibu na
majukumu ya kila mtu katika kuchangia maendeleo ya nchi.
Kwa jumla, wataalamu wa nadharia na tasnia ya rasilimali watu wanasema
Kwamba, kazi kubwa ya wanaosimamia rasilimali watu
ni kuhakikisha kila shughuli katika taasisi husika anapatikana mtu
sahihi, mwenye elimu na ujuzi sahihi, wakati sahihi na atakayepewa kazi
sahihi ili aifanye kwa usahihi pia.
Hata hivyo, rasilimali watu kama somo ni somo pana
na katika miaka ya leo imeanza kuaminika kwamba kiongozi wa taasisi
anayepwaya katika elimu na ujuzi wa rasilimali watu hawezi kufanya kazi
kwa ufanisi mkubwa kama ilivyo kwa yule aliyesheheni nidhamu na nadharia
husika.
Kazi ya kusimamia au kuongoza rasilimali watu
inaanzia na mipango, ugawanyaji kazi na wajibu, utafutaji watu kujaza
nafasi zilizo wazi, mahojiano ya kutathmini sifa na uwezo wa mtu kama
unaendana na jinsi alivyo na uchaguaji miongoni mwa walioomba kazi idadi
ya watu wanaotakikana kwa kazi fulani.
Menejimenti ya rasilimali watu inajumuisha pia
mambo ya ufuatiliaji wa utendaji kazi, uchukuaji wa hatua za kinidhamu,
afya na usalama wa wafanyakazi pamoja na mikakati yote inayoihakikishia
taasisi kuendelea hata kama waliopo kwa wakati huo wataondoka au kufa.
Kampuni au idara ya Serikali au taasisi iwayo kwa
hiyo ina maana kwamba utendaji kazi wake na sifa yake aghalabu,
utatokana na aina ya watu walioajiriwa. Ukiajiri watu wa ovyo na
utendaji wa taasisi husika nao pia utakuwa ni wa ovyo. Ukiajiri
watumishi au wafanyakazi wazuri basi uwezekano wa taasisi hiyo kuwa na
utendaji mzuri nao ni mkubwa pia.
Hii inamaanisha nini? Inamaanisha kwamba wale wote
waliopewa dhamana ya kuajiri wafanyakazi au watumishi wapya lazima wawe
wanaojua kila linalopaswa kujulikana juu ya mbinu zote zinazotumika
katika nadharia na utendaji kazi katika tasnia ya rasilimali watu ili
kuhakikisha kwamba watumishi watarajiwa wote wanapepetwa kwa namna
ambayo chuya au chafu wote unaondolewa na panabakia nafaka nzima na
safi.
Hili linahitaji kwa kiasi kikubwa ugwiji katika
masuala ya saikolojia na sosholojia. Elimu zinazoweza kuwang’amua watu
walivyo na watakavyokuwa kwa kuangalia historia yao ya kimaisha na
kikazi.
Polisi wanapolalamika kwamba wameajiri askari
polisi ambao wanashirikiana na majambazi kuwaibia na kuwadhuru wananchi
ilhali tunajua kazi ya polisi inatakiwa iwe nini, hapo kunaonyesha kuna
walakini mkubwa katika namna wafanyakazi katika eneo husika
awanavyochambuliwa na mwishowe kuajiriwa.
Mamlaka za kodi na mapato zinavyolalamika kuna
wafanyakazi walioiva na kupevuka kwa rushwa, pia tatizo ni hilo hilo,
yaani, jinsi watumishi wao wanavyopatikana na jinsi wanavyochujwa ili
wabakie wale walio safi.
Benki na sekta ya fedha inapolalamika juu ya wizi kushamiri
katika mabenki kwa ushirkiano kati ya wafanyakazi wa taasisi za kifedha
na wafanyabiashara au hata wezi ni ishara kwamba kuna ajira mbovu katika
sekta husika.
Tunapolalamika juu ya utendaji kazi katika
hospitali, shuleni, vyuoni na kadhalika jambo hili pia huwa ni dalili ya
kuwepo kwa walakini katika masuala ya haki na wajibu wa watumishi
wahusika.
Tumalizie kwa kusema kwamba rasilimali watu ambayo
nchi inabahatika kuwa nayo haitoki juu mbinguni. Rasilimali hiyo
inatokana na jamii iliyopo katika nchi husika.
Hivyo ni vigumu kuona kama jamii yenyewe inajikita
katika uongo, ubabaishaji, uzembe, ubinafsi, uvivu, umbeya, maneno bila
vitendo, kula usichokipanda na ila za kila aina, ni kwa vipi jamii hiyo
inaweza kuwa na wafanyakazi wanaohitaji kuiondoa jamii yao kutoka
kwenye hatua ya chini kabisa kimaendeleo na kuipeleka kwenye hatua ya
juu kabisa kimaendeleo!

No comments:
Post a Comment