Monday, 24 March 2014

Ndugai: Taifa lina tatizo la mgawanyo wa rasilimali

Mbunge wa Kongwa na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai ameomba ushauri kwa Seneta Amos Wako wa Kenya kuhusu mgawanyo wa rasilimali za taifa.
Ombi hilo la Ndugai, ambaye ni mjumbe wa Bunge la Katiba, lilitokana na historia aliyoitoa seneta huyo wa Busia Mashariki nchini Kenya, iliyotokana na uzoefu alioipata katika Mchakato wa kuunda na kuandika katiba ya nchi hiyo.
Mwishoni mwa wiki, Seneta Wako alieleza bungeni kuwa changamoto zilizokuwa zikiikabili Kenya wakati ikiandika Katiba yake, ni pamoja na wananchi kulalamikia mfumo wa mgawanyo wa rasilimali.
“Kulikuwa na madai kwamba hakukuwa na usawa katika kugawa keki ya taifa, maeneo yenye viongozi yalidaiwa kupendelewa kwa kuwa na huduma nzuri za kijamii kuliko mengine,” alieleza Seneta Wako.
Ndugai alipopata nafasi ya kuuliza swali, alisema tatizo la mgawanyo wa rasilimali lililokuwako Kenya, lipo hata hapa nchini lipo kwa kiwango kikubwa.
“Mikoa mingi inalalamikia uduni wa huduma kwa jamii. Kwa uzoefu wako unashauri nini kifanyike kutatua changamoto hii,” aliuliza Ndugai.
Seneta Wako alisema mgawanyo wa madaraka na rasilimali za taifa nchini Kenya unaendelea kushughulikiwa kupitia Utawala wa Majimbo, ingawa aliasa kwamba kinachofaa kwa wengine haimaanishi kitafaa kwa Tanzania.
Alisisitiza kuwa ufumbuzi wa matatizo ya Watanzania utatokana na Watanzania wenyewe kwa sababu ndio wanaofahamu mila, desturi na mfumo mzima wa maisha yao.

No comments: