Mbunge wa Kongwa na Naibu Spika wa Bunge,
Job Ndugai ameomba ushauri kwa Seneta Amos Wako wa Kenya kuhusu
mgawanyo wa rasilimali za taifa.
Ombi hilo la Ndugai, ambaye ni mjumbe wa Bunge la
Katiba, lilitokana na historia aliyoitoa seneta huyo wa Busia Mashariki
nchini Kenya, iliyotokana na uzoefu alioipata katika Mchakato wa kuunda
na kuandika katiba ya nchi hiyo.
Mwishoni mwa wiki, Seneta Wako alieleza bungeni
kuwa changamoto zilizokuwa zikiikabili Kenya wakati ikiandika Katiba
yake, ni pamoja na wananchi kulalamikia mfumo wa mgawanyo wa rasilimali.
“Kulikuwa na madai kwamba hakukuwa na usawa katika
kugawa keki ya taifa, maeneo yenye viongozi yalidaiwa kupendelewa kwa
kuwa na huduma nzuri za kijamii kuliko mengine,” alieleza Seneta Wako.
Ndugai alipopata nafasi ya kuuliza swali, alisema
tatizo la mgawanyo wa rasilimali lililokuwako Kenya, lipo hata hapa
nchini lipo kwa kiwango kikubwa.
“Mikoa mingi inalalamikia uduni wa huduma kwa
jamii. Kwa uzoefu wako unashauri nini kifanyike kutatua changamoto hii,”
aliuliza Ndugai.
Seneta Wako alisema mgawanyo wa madaraka na
rasilimali za taifa nchini Kenya unaendelea kushughulikiwa kupitia
Utawala wa Majimbo, ingawa aliasa kwamba kinachofaa kwa wengine
haimaanishi kitafaa kwa Tanzania.
Alisisitiza kuwa ufumbuzi wa matatizo ya
Watanzania utatokana na Watanzania wenyewe kwa sababu ndio wanaofahamu
mila, desturi na mfumo mzima wa maisha yao.

No comments:
Post a Comment