Saturday, 18 January 2014

Siasa ina athari soko la muziki?

Katika ushabiki wa kisasa tunaweza kufikia hatua ya kuchapana makonde mpaka kupelekana mahakamani, lakini tunaposikia ‘Bit’ kabla ya mashairi, taratibu kila mtu utamwona anaanza kujiachia bila kujali amekutana na hasimu wake wa kisiasa.
Hatua hiyo inatokana na nguvu iliyopo ndani ya muziki hususan ule uliongia katika karne hii ya 21, kwa staili mpya za kubana pua(R&B) na kufoka foka(Hip Hop).
Hata hivyo wakati hali hiyo ikijitokeza, kumekuwa na mtazamo, dhana na hofu juu ya wasanii wanaojihusisha kwa karibu na shughuli za kisiasa kwamba wanaweza kupoteza nguvu katika soko lao kimuziki.
Baadhi ya mashabiki waliozungumza na Starehe, wanasema hatua hiyo inaweza kusababisha idadi kubwa ya vijana ambao ni mashabiki wa Bongo Fleva, huku wakiwa wamejikita zaidi katika ushabiki na mivutano ya kisiasa.
Kutokana na mtazamo huo kwa mashabiki, Starehe imefanikiwa pia kuzungumza na baadhi ya wasanii wahusika ambao wako kwenye siasa pamoja na mameneja ambao husimamia soko la muziki huo hapa nchini.
Akizungumza na Starehe siku chache baada ya mvutano wa mbunge wa Kigoma Kaskazin Zitto Kabwe na Chama chake, Sunday Mangu ambaye ni kiongozi wa kundi la wasanii kutoka Mkoa wa Kigoma (KAS), anasema ni hatari kwa msanii kujihusisha moja kwa moja katika mgogoro na ushabiki wa kisiasa.
“Msanii hutakiwi kuwa sehemu ya ushabiki ila hatukatazwi kutoa ‘sapoti’ za kisiasa. Kwa mfano Zitto tumekuwa naye bega kwa bega kwenye mgogoro huo kama kijana mwenzetu ambaye amekutana na changamoto katika nafasi yake ya kisiasa,” anasema na kuongeza;
“Endapo msanii atafanya hivyo anaweza kujitenga na kundi fulani kwenye jamii hatua ambayo siyo sahihi, msanii hana kundi wala hatakiwi kuwa kwenye itikadi zozote za ushabiki.
Hata hivyo kwa upande wake Profesa Jay anafafanua akisema kuwa msanii kutumiwa kwenye kampeni za kisiasa haimaanishi kuwa yeye ni sehemu ya chama kile.
Jay anasema kwa msanii ambaye anatumika tu kwenye kampeni za siasa haoni kama inaweza kuathiri kazi zake na kwamba anachoangalia ni maslahi ya kazi yake.
“Msanii anatumiwa kwa pesa huwezi kusikia msanii anafanya kampeni bila malipo, mimi sijawahi kufanya kampeni na siwezi kujua moja kwa moja zimewaathiri vipi lakini sijawahi kuona kama kuna msanii yeyote aliyetumika kisiasa na akaathirika kimuziki,” anasema Jay.
Hata hivyo Jay anaongeza kuwa msanii pia ni binadamu kama wengine ambao wana haki ya kuwa na hisia katika ushabiki wa mambo wanayoyapenda katika jamii.

Akitoa mfano, Jay anasema msanii kabla ya kuwa msanii inawezekana alikuwa ni shabiki wa Simba, hivyo hawezi kuacha ushabiki wake kwa sababu ya muziki, kutokana na hofu ya kuathiri soko lake kwa mashabiki wa Yanga.
“Msanii kuwa na Kadi ya CCM au Chadema siyo dhambi pia japokuwa inaweza kuwa mbaya zaidi pale atakapojiingiza zaidi kwenye ushabiki wa kisiasa, binafsi sioni kama kuna tatizo ila mashabiki wanapaswa kujua msanii anapofanya hivyo ni sehemu ya kazi yake,” anasema Jay.Mbali na Jay, Afande Sele anasisitiza kuwa athari zinaweza kujitokeza katika upande wa wadau wa muziki.
“Wadau wa muziki wanaweza kuwa wamegawanyika katika makundi ya kisiasa kwa hivyo msanii unaweza kuwa chama fulani wakati mdau ambaye anatakiwa ‘kukusapoti’ bila kujua kumbe ana hisia na chama kingine cha siasa. Kwa mazingira hayo msanii unaweza kukosa msaada kwake,” anasema Sele.
Sele anasema pamoja na hofu hiyo lakini hakuna shabiki yeyote ambaye anaweza kumsaliti msanii kutokana na itikadi za kisiasa.
Anaongeza kuwa shabiki ambaye anaweza kuwa na dhana ya kumsaliti msanii kwa sababu za kisiasa, atakuwa hajamtendea haki.
“Mimi hakuna ambaye hajui kwa sasa ni mwanachama wa Chadema, lakini bado ninapopanda jukwaani nashangiliwa na mashabiki wangu wote wakiwamo hata wa vyama vingine. Hapo siasa inakuwa pembeni kabisa,” anasema Sele na kuongeza;
Kinachofanya msanii aendelee kukubalika kwa mashabiki wa aina zote ni kutokana na aina ya mashairi na ubora wa kazi zake.
Anasema shabiki mwenye mapenzi ya dhati kwa msanii, hawezi kubadilishwa mtazamo na mapenzi yake kwa itikadi hizo za kisiasa na badala yake mapenzi yataongeza kutokana na mwendelezo wa harakati.
“Kama mashairi yangu yalikuwa ni kugusa ukweli halisi wa maisha na udhaifu wa viongozi, naamini kuingia kwenye siasa itakuwa ni ushawishi zaidi kwa watu wanaohitaji mabadiliko,” anasema Sele.
Mameneja wanasemaje?
Meneja maarufu wa kundi la Tip Top Connection, Diamond, Shaa na wasanii wengine kadhaa anayejulikana kwa jina la Babu Tale, kwanza anasema ifahamike wazi kuwa msanii hana dini wala chama chochote anachokitumikia kupitia muziki wake.
Tale anasema msanii ni kama mfanyakazi yeyote mwingine ambaye yuko tayari kufanya kazi kwa ajili ya kuangalia masilahi yake.
“Kesho unaweza kumwona amevaa tisheti za CCM, lakini baada ya siku kadhaa utamwona Chadema endapo watapanda dau zuri. Hilo ni jambo muhimu sana kwa mashabiki kuelewa kabla ya kuyumbishwa na dhana za kisiasa,” anasema Tale na kuongeza;
Katika uchaguzi wa mwaka 2010 alitumika kwenye kampeni za Rais Kikwete akiwa na wasanii wake mbalimbali anaowasimamia. “Tulikubaliana kufanya shoo zile kwa sababu za kimasilahi, inawezekana siku nyingine ukawaona wasanii hao hao wakapanda kwenye jukwaa za vyama vingine.
Kwa upande wake Meneja wa kundi la Wanaume family(TMK), Said Fela anaongeza akisema changamoto kubwa iliyopo ni mashabiki ambao hawaelewi nini ambacho msanii anazingatia katika kazi zake.
Anasema kinachojitokeza ni mtazamo usiosahihi kwa mashibiki na kutokuelewa kama msanii anaweza kufanya shoo yoyote kama sehemu ya kazi zake kimuziki.
“Mashabiki wetu siwezi kuwahukumu kwani hawana ubaguzi hata kidogo, hawawezi kubadilishwa mapenzi yao kwa msanii kwa sababu za kisiasa, hatujafikia hatua ya kuwa na siasa au mashabiki wa aina hiyo,” anasema Fela.
Akitoa mfano Fela anasema msanii wa Hip Hop, Joseph Mbilinyi ambaye kwa sasa ni mbunge wa Mbeya Mjini, bado hajaathiriwa na siasa katika soko lake la muziki.
“Kama wasanii kujihusisha na siasa ingekuwa na athari basi ‘Sugu’ leo hii asingeweza kufanya shoo ambayo inaweza kuchanganya mashabiki wa aina zote bila kujali itikadi za vyama vyao,” anasema Fela na kuongeza;
Kwa hivyo mimi nadhani huo ni mtazamo ambao siyo sahihi kabisa, muziki wetu bado haujawa na tatizo kama hilo na siamini kama linaweza kujitokeza katika siku za mbele.

No comments: