Saturday, 18 January 2014

Nzuri kuitamka, tamu kuisikiliza

Bado tunazungumzia habari za mwaka mpya mpaka labda tutakapoingia mwezi wa pili. Mwaka mpya, mambo mapya au siyo?
Mwaka mpya umeanza, kila mtu sasa anazungumzia mipango yake kwa mwaka huu, huku wengine wakiwa na viporo vya mwaka jana, hata hivyo siyo ishu kwa kuwa huu ni mwaka mwingine na una mambo yake.
Ni mipango mizuri kuitamka na mitamu kuisikiliza, lakini je, huu ni uhalisia au tunatekeleza wajibu wetu kwa kuwa ndiyo maongezi yaliyotawala vinywa vyetu mwezi huu.
“Ninataka kubadilika, mwaka huu pombe no, situmii pesa ovyo, lazima nijenge, nitapunguza uzito, naacha sigara n.k,” hii ni baadhi tu ya misemo inayotawala mwezi huu.
Ni mitamu kweli kweli kuitamka na hata usikilizapo huleta raha. Kwa mhusika huenda inampa picha nzuri mbeleni kwani ikifanikiwa itakuwa bao la kisigino.
Cha kujiuliza hapa hivi ni kweli lazima tusubiri Januari mosi kuanza kutafuta mabadiliko katika maisha yetu, yaani ninaweza kuwa mtu tofauti Desemba 31, halafu nikaamka Januari mosi na kuwa mwingine.
Usiku wa mwaka mpya unalala ukiwa njwii kwa ulevi wa pombe, lakini ukiwa na matarajio ya kuacha ulevi kesho yake.
Kama ulikuwa hufahamu basi huu ndiyo ukweli, ni asilimia nane tu ya watu wote duniani ndio hufanikiwa kwa kutegemea mwaka mpya kubadilika, wengine wakijitahidi sana ni wiki moja tu baada ya hapo wanarudia maisha yao ya zamani.
Ni kujidanganya kudhani kuwa ifikapo tarehe fulani, unaweza kuiondoa tabia iliyojizoesha kwa miaka mingi.
Kisaikolojia unapojipangia tarehe za kubadilika katika kitu fulani, unakuwa unajiwekea ugumu kwani inatakiwa pale unapogundua tatizo uanze kulifanyia kazi na si kulipangia tarehe.
Maneno matupu hayavunji mfupa. Kupanga nitafanya hivi siku fulani ni sawa na usemi huo kwani hayo ni maneno matupu.
Kwa wenye tabia hii ni rahisi kusahau ulijipangia nini mara itakapingia Februari, pengine utaanza kuikumbuka mipango yako pale watu watakapoanza kuzungumza habari za mwaka kwisha.
Ikishafika Oktoba au Novemba kauli za ‘mwaka umeisha huu’ huanza kutawala maongezi yetu, hapo ndipo unaweza kukumbuka ulichojipangia kwa mwaka huu, lakini kwa kuwa ni mtu wa mwaka mpya basi utaona isiwe shida nitaaanza tena mwakani.
Kama unatamani mabadiliko basi usisubiri mwaka mpya, unapogundua kitu ndani yako ambacho ungependa kibadilike basi kifanyie kazi mara moja.
Mabadiliko hayaji mara moja bali kwa hatua ndogondogo, chukua hatua pale unapoona unapaswa kuanza.
Kuna matatizo mengine unapoyachelewesha ndipo yanapokuwa makubwa zaidi, badala ya kutumia muda mfupi kuyatatua unaweza kujikuta unatumia nguvu na pesa nyingi.
Mwaka mpya uwe wa kusherehekea sikukuu na mfanikio ambayo kwa uchache umeyafanikisha. Usisubiri mwaka mpya kuanza kufanya kitu fulani.

No comments: