Tuesday, 7 May 2013

Serikali yataja changamoto ugatuaji madaraka nchini


Imetaja sababu hizo kuwa ni ushiriki mdogo wa jamii kwenye shughuli za jamii na maendeleo, mahudhurio hafifu ya wananchi katika vikao vya uamuzi, ukusanyaji na usimamizi dhaifu wa mapato yake.



Dodoma. Serikali imekiri kukabiliwa na changamoto kubwa zinazoikabili katika kutekeleza sera ya ugatuaji madaraka kwa wananchi wake.
Imetaja sababu hizo kuwa ni ushiriki mdogo wa jamii kwenye shughuli za jamii na maendeleo, mahudhurio hafifu ya wananchi katika vikao vya uamuzi, ukusanyaji na usimamizi dhaifu wa mapato yake.
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri alisema ngazi ya mitaa na vijiji kumekuwa na tatizo kubwa la utunzaji wa vitabu vya hesabu, uandaaji taarifa za mapato na matumizi na taarifa za utekelezaji majukumu ya mitaa na vijiji.
Alikuwa akijibu swali la mbunge Viti Maalumu, Anastazia Wambura (CCM) ambaye alihoji Serikali inawezaje kuwahakikishia wananchi kwamba wenyeviti wa mtaa na vijiji wanajua wajibu wao kulingana na nafasi walizonazo.
Pia, mbunge huyo alitaka kujua Serikali jinsi inavyofuatilia fedha za uwezeshwaji na kujengewa uwezo, ambazo hutengwa kwa ajili ya kuwapa mafunzo viongozi hao ambazo hazifiki kwa wakati unaotakiwa.
Naibu Waziri alisema wenyeviti wa vijiji na mitaa wana wajibu wa kusimamia ulinzi na usalama maeneo yao, kuwakilisha wananchi katika vikao vya Kamati za Maendeleo ya Kata, wilaya na kuitisha na kuongoza mikutano.
“Kutokana na changamoto hizi, ni wazi kuwa upo umuhimu mkubwa wa kuendelea kuwajengea uwezo wenyeviti wa vijiji na mitaa na watendaji wao ili kuhakikisha wanajua majukumu yao ipasavyo,” alisisitiza Mwanri.
Mwanri alisema Serikali imekuwa ikipeleka asilimia 40 ya fedha za kujenga uwezo katika vijiji na mitaa, asilimia 50 ya fedha hizo hutumika kuwajengea uwezo viongozi hao.

No comments: