Monday, 2 June 2014

Lissu arusha kombora lingine kwa mawaziri

Dodoma. Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk Binilith Mahenge, jana walituhumiwa kutumia vibaya nafasi zao kwa kuweka fedha nyingi za miradi ya maji katika maeneo wanakotoka, huku sehemu zenye matatizo ya huduma hiyo zikitengewa fedha kiduchu.
Ilielezwa bungeni jana kuwa Profesa Maghembe ambaye ni Mbunge wa Mwanga, Kilimanjaro, wizara yake imetenga Sh1.4 bilioni kwa ajili ya miradi ya maji, ambazo ni zaidi ya mara saba ya Sh190 milioni zilizotengwa kwa ajili hiyo katika Wilaya ya Ikungi, Singida.
Akichangia Bajeti ya Wizara ya Maji jana, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu alihoji kile alichokiita upendeleo wa wazi katika ugawaji wa fedha za maji, unaoipa kipaumbele baadhi ya mikoa wanakotoka mawaziri.
Pia aliitaja Wilaya ya Makete, Njombe anakotokea Dk Mahenge ambaye amewahi kuwa Naibu Waziri wa Maji kuwa imetengewa Sh1.9 bilioni na kusema: “Upendeleo wa aina hii haufai kwa sababu utaleta matatizo na siyo haki hata kidogo.”
“Profesa Maghembe atueleze sababu za kutenga bajeti hii kwa upendeleo, huku mikoa isiyokuwa na vyanzo vya maji, mito ya kudumu na mabwawa ya maana imepewa bajeti kidogo ikilinganishwa na ile yenye mifumo mizuri ya maji,” alisema Lissu.
Alisema licha ya Profesa Maghembe katika hotuba yake kutaja mikoa ya Dodoma, Singida, Simiyu na Shinyanga kuwa inakabiliwa na upungufu wa maji, imetengewa kiasi kidogo cha fedha, huku mikoa inayopata mvua za kutosha na vyanzo vya uhakika vya maji ikitengewa mabilioni ya fedha.
“Dodoma imetengewa Sh7.2 bilioni, Singida Sh3.2 bilioni, Shinyanga Sh3.2 bilioni na Simiyu Sh2.8 bilioni, wakati mikoa yenye vyanzo vya maji na mvua za kutosha imetengewa fedha nyingi; mfano ni Tanga Sh10.7 bilioni, Kilimanjaro Sh6.3 bilioni, Mbeya Sh9.2 bilioni na Mtwara Sh7.5 bilioni,” alisema.
Lissu alisema hali hiyo inaweza kutafsiriwa kuwa mawaziri hao wanatumia mamlaka yao kujipendelea na kuhoji kama huo ndiyo utaratibu wa Serikali ya CCM... “Kama utaratibu wa mgawanyo wa fedha ndiyo huu sisi tunaotoka mikoa yenye ukame tutapataje maji?”
Jana Profesa Maghembe aliendelea kuwa katika wakati mgumu, baada ya kuandamwa na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika ambaye alimwita kuwa ni mzigo kutokana na kutokutolewa kwa fedha za miradi ya maji.
Mnyika alionyesha kushangazwa na wabunge wenzake kuunga mkono bajeti ya wizara hiyo, licha ya kuwa ndogo na fedha za miradi zimekuwa hazitolewi kama inavyotakiwa.
“Kwa kufanya hivi sidhani kama tunamsaidia Profesa Maghembe ambaye ni CCM. Fedha zilizotengwa mwaka jana kuisaidia wizara hii hazijatoka na za bajeti hii hazitatoka kwa kiwango cha kuwezesha utekelezaji. Namna bora ya kumsaidia ili viongozi wa CCM wasiendelee kumwita mzigo ni kuikataa bajeti hii ili Serikali irudi mezani na kujiuliza.”
Mnyika alisema kuwa hata ahadi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuwa Serikali itaongeza Sh80 bilioni kwa wizara hiyo kabla ya Mei 31 mwaka huu nayo haijatekelezwa na kusisitiza kuwa wabunge wakiipitisha bajeti hiyo watakuwa wameuziwa mbuzi kwenye gunia.
Alisema kuwa hata miradi ya maji jijini Dar es Salaam ambayo Profesa Maghembe aliahidi kuwa itakamilika mpaka sasa hakuna kilichofanyika.
Mbunge wa Mbozi Magharibi (Chadema), David Silinde alisema Profesa Maghembe amechota mabilioni ya fedha na kuyapeleka katika miradi ya maji kwenye jimbo lake la uchaguzi wakati maeneo mengine ameyaacha licha ya kuwa yana kipaumbele na kwamba anatumia miradi ya Serikali kujinufaisha kisiasa.
“Ukitaka takwimu zote ninazo hapa, idadi ya watu kwako ni wachache kuliko hata kwangu lakini kwa vipindi viwili mfululizo umekuwa ukijitengea mabilioni ya fedha, wewe ni mzigo kabisa,” alisema Silinde.
Mwandosya amtetea
Wakati akijibu hoja za wabunge, Profesa Maghembe hakugusia tuhuma hizo na badala yake Profesa Mwandosya alimtetea akisema miradi hiyo katika wilaya za Same, Mwanga na Korogwe ilianza wakati yeye (Mwandosya) akiwa Waziri wa Maji... “Si kweli kwamba Profesa Maghembe anapendelea jimbo lake kwa sababu hakuwa waziri wa wizara hiyo wakati mradi huo unaanzishwa. Wananchi wa Same, Mwanga, Korogwe na Simanjiro wana haki ya kupata maji kama wananchi wa sehemu nyingine yoyote. Mwacheni waziri atekeleze majukumu yake ili watu hawa wapate maji”.
Alisema mradi wa maji wa Same, Mwanga na Korogwe ni muhimu sana kwa sababu utakuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya watu 400,000 ambao hawapati maji kabisa.
Alisisitiza kuwa yuko tayari kubeba lawama juu ya mradi huo na si Profesa Maghembe, kwani waziri huyo anafanya kazi nzuri ya kutekeleza mradi huo ambao ulikuwapo hata kabla hajapelekwa katika wizara hiyo.

Tuesday, 20 May 2014

Wabunge wataka JK aunde tume ya elimu

Dodoma/Dar. Baadhi ya wabunge jana walichachamaa wakisema elimu nchini ipo mahututi na kumtaka Rais Jakaya Kikwete kuunda tume ya kudumu ya elimu itakayochunguza mfumo wa elimu nchini.
Wabunge hao walikuwa wakichangia hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa mwaka wa fedha 2014/2015 iliyowasilishwa na waziri wake, Dk Shukuru Kawambwa Jumamosi usiku.
Mbunge wa Longido (CCM), Lekule Laizer alipendekeza safari zote za wabunge na mawaziri nje ya nchi zifutwe na fedha zake zipelekwe kuboresha shule za kata.
Mbunge wa Kuteuliwa (NCCR-Mageuzi), James Mbatia alizungumzia uduni wa vitabu na mitihani ya wanafunzi wa shule za msingi akisema inakosewa kutungwa.
“Nina mtihani wa majaribio wa darasa la saba ambao haufanyiki. Niliwahi kumpa profesa mmoja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambaye alitumia saa mbili na nusu bila kupata jibu lolote la kuandika. Mtihani wenyewe haufanyiki,” alisema Mbatia na kutoa ofa ya Sh10 milioni kwa profesa mwingine yeyote bungeni ambaye ataweza kufanya mtihani huo na kupata alama 100.
“Haya ni madudu ya kutisha. Mwaka jana nilivyotoa maoni yangu hapa na waziri akasema maoni yetu yamechukuliwa, alisema rasimu ya mwisho sera ya elimu imepelekwa Baraza la Mawaziri Machi 2013, lakini hadi sasa bado haijakamilika,” alisema na kuongeza kuwa hiyo ni dalili ya Bunge kutoheshimiwa.
Pia alizungumzia ripoti za kamati zilizoundwa kuchunguza elimu lakini hazikufanyiwa kazi na badala yake zikawekwa kwenye makabati.
“Tumwombe Rais aunde Tume ya Kudumu ya Elimu kwa sababu kwa hali inavyokwenda ni mbaya sana na napendekeza tume hii ishughulike na kudhibiti mambo yote yanayofanya kutetereka kwa ubora elimu nchini.
Mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba alisema elimu ya Tanzania iko mahututi na kuwaomba wabunge kuacha siasa katika elimu.
“Bajeti itapita lakini tunaua kizazi kijacho. Mheshimiwa mwenyekiti nenda darasa la kwanza mpaka la saba anayoyasema Mbatia yapo hata kama hatuyapendi lazima tuseme ukweli,” alisema.
Alisema ukienda katika vyuo vikuu ni majanga. “Kama unajiangalia wewe na familia yako, basi tunaliua Taifa. Nimefanya utafiti kwenye nchi 35, Tanzania ni nchi ya mwisho kwa ufaulu,” alisema na kuongeza kuwa nchi zote zilizoendelea kiuchumi, kiwango cha ufaulu ni juu ya asilimia 60.
Mbunge wa Ngara (CCM), Deogratias Ntukamazina alisema hakuna Wizara ya Elimu baada ya elimu ya sekondari na msingi kuondolewa
“Mbele ya Waziri Mkuu niseme kuwa sasa hatuna Wizara ya Elimu… na sasa wanaondoa elimu ya watu wazima, shule zote za mazoezi zimeondolewa.”
Mbunge wa viti maalumu (CUF), Magdalena Sakaya alisema anashangazwa na wizara kushusha madaraja ya ufaulu ambayo awali, kuanzia alama 34 ilikuwa ni daraja O lakini leo ni ufaulu.
“Kiukweli waziri aliyeko katika wizara hii ameshindwa kusaidia elimu nchini. Tangu ameshika wadhifa huo anazidi kubebwa. Kwa nini tunambeba mtu ambaye ameshindwa kusaidia elimu nchini?” alihoji.
Safari za nje
Laizer alitaka safari za mawaziri na wabunge nje ya nchi zifutwe na fedha hizo ziboreshe shule za kata ambako ndiko watoto wa maskini wanakosoma.
Alisema anashindwa kuunga mkono bajeti ya wizara hiyo wakati watoto wake wote katika jimbo lake wanafeli kutokana na shule za kata kutokuwa na walimu wa kutosha.
Akifanya majumuisho, Waziri Kawambwa alikiri deni la Sh61 bilioni la madai ya walimu, lakini akasema serikali imekuwa ikilipa.
Alisema kuanzia Agosti mwaka jana hadi Machi, jumla ya Sh16 bilioni zimelipwa na kwamba si kweli kwamba deni hilo limebakia kuwa Sh61 bilioni.

Sunday, 11 May 2014

Mbowe atangaza mawaziri kivuli

Dodoma. Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, ametangaza Baraza lake la mawaziri kivuli 28 na naibu mawaziri 12, na kufanya baraza lote kuwa na mawaziri 40.
Katika baraza hilo la mawaziri linalojumuisha wabunge wanaotokana na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), mawaziri 25 wanatoka Chadema, 11 wanatoka CUF na NCCR-Mageuzi ni wanne.
Mawaziri kivuli walioachwa katika baraza hilo ni Sylvester Kasulumbay (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi), Highness Kiwia (Viwanda na Biashara) na Rose Kamili (Kilimo, Chakula na Ushirika).
Wengine walioachwa na Mbowe akasisitiza kuachwa kwao siyo kwa sababu hawawezi kazi bali ni kutaka kuwa na baraza la mawaziri dogo ni Sabrina Sunga (Naibu Waziri Maji).
Katika Baraza hilo, nafasi ya mnadhimu mkuu wa upinzani Bungeni iliyokuwa ikishikiliwa na Tundu Lissu (Chadema) sasa itashikiliwa na Mbunge wa Tumbe, Rashid Abdalah kutoka chama cha CUF.
Akitangaza baraza hilo Bungeni mjini Dodoma jana, Mbowe alisema Wizara ya Katiba na Sheria imeongezewa majukumu ya Muungano na waziri wake atakuwa ni Lissu na naibu wake ni Abdalah.
Pia amemteua Mbunge wa kuteuliwa na Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa taifa wa NCCR-Mageuzi,  James Mbatia ambaye anakuwa Waziri wa Fedha wakati Naibu wake atakuwa Christina Lissu kutoka Chadema.
Mawaziri Ofisi ya Rais ni Profesa Kulikoyela Kahigi (Utawala Bora-Chadema), Vicent Nyerere (Utumishi-Chadema) na Esther Matiko (Mahusiano na Uratibu-Chadema).
Ofisi ya makamu wa Rais itakuwa na mawaziri wawili ambao ni mchungaji Israel Natse kutoka Chadema atakayeshughulika na Mazingira na Naibu wake atakuwa ni Assah Othman Hamad (CUF).
Mnadhimu wa Upinzani Bungeni ndiye atakayeshikilia pia nafasi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Mazingira.
Mawaziri katika ofisi ya Waziri mkuu ni Pauline Gekul (Uwekezaji na Uwezeshaji-Chadema), Rajabu Mohamed Mbaruku (Sera, Uratibu na Bunge-CUF) na David Silinde (Tamisemi-Chadema).
Wizara ya Chakula, Kilimo na Ushirika itashikiliwa na Meshack Opulukwa (Chadema), Wizara ya Nishati na Madini atakuwa John Mnyika Chadema na Naibu wake “atakuwa Raya Ibrahim (Chadema).

Kulingana na orodha hiyo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa itashikiliwa na Ezekiah Wenje (Chadema) na Naibu wake ni Rashid Abdalah  kutoka  CUF.
Mawaziri wengine na wizara zao kwenye mabano ni Felix Mkosamali (Ujenzi-NCCR-Mageuzi), Magdalena Sakaya (Maji-Cuf), na Moses Machali (Uchukuzi- NCCR- Mageuzi).
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi itaongozwa na Godbless Lema wa Chadema na Naibu wake ni Khatibu Said Haji wa CUF wakati Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi ni Halima Mdee wa Chadema.
Kwa mujibu wa orodha hiyo, Mbowe amemteua Rose Kamili Sukum kutoka Chadema kuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi wakati Naibu wake atakuwa ni Mkiwa Adam Kiwanga wa CUF.
Wizara ya Maliasili na Utalii itashikiliwa na mchungaji Peter Msigwa (Chadema), Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki imeenda kwa Joseph Selasini (Chadema) na naibu ni Rukia Ahmed Kassim (CUF).
Mbowe pia amemteua Masoud Abdalah Salim wa CUF kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa na Wizara ya Elimu itashikiliwa na Susan Lyimo  na Naibu wake ni Joshua Nasari wote toka Chadema.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeenda kwa Dk Gervas Mbassa na Naibu wake ni Conchesta Rwamlaza wote wa Chadema. David Kafulila (NCCR) ameteuliwa Waziri wa Viwanda na Biashara.
Katika baraza hilo la mawaziri, Injinia Habib Mnyaa wa CUF ameteuliwa kuwa Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia wakati Lucy Owenya kutoka Chadema akiteuliwa kuwa naibu wake.
Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto imeenda kwa Baruan Salum Khalfan wa CUF na Naibu wake ni Subreena Sungura wa Chadema. Cecilia Paresso wa Chadema anakuwa Waziri wa Kazi na Ajira.
Wizara ya Habari, Vijana na Michezo imeendelea kushikiliwa na Joseph Mbilinyi wa Chadema.
Akizungumza na wanahabari, Mbowe alisema wakati katika Baraza la Mawaziri la Serikali ya CCM, wanaume ni 36 na wanawake 15, wao upinzani wanaume ni 26 na wanawake ni 14.
Hali kadhalika Mbowe alisema wakati Baraza zima la mawaziri la Serikali ya CCM likiwa na mawaziri kamili 28 na manaibu 22, wao Baraza lao Kivuli lina mawaziri kamili 28 na naibu mawaziri 12.
Alisema nafasi ya Naibu Kiongozi wa Upinzani Ubungeni iliyokuwa ikishikiliwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe itantangazwa baadaye

Lugola: Serikali ya CCM inaendeshwa kisanii

Dodoma. Mbunge machachari wa Mwibara, Alphaxard Kangi Lugola, amedai kuwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambayo yeye ni mbunge wake, inaendeshwa kisanii.
Lugola ambaye katika Bunge lililopita aliwaongoza wabunge wenzake kuichachafya Serikali hadi mawaziri wanne kujiuzulu nyadhifa zao, jana aligeuka tena mwiba kwa Serikali ya CCM.
Akichangia hotuba ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Lugola alisema anashangaa Waziri mwenye dhamana, Christopher Chizza kuendelea kuwa waziri wakati hotuba yake imejaa blabla.
Pia alimgeukia naibu wa wizara hiyo, Godfrey Zambi na kumwambia kuwa amejisahau kwamba naye alikuwa akikaa kiti cha nyuma bungeni akipaza sauti, lakini baada ya kupata madaraka amewageuka na kushirikiana na waziri.
Akichangia kwa hisia kali, Lugola alihoji inakuwaje wakulima wanapelekewa pembejeo feki, dawa feki na skimu za umwagiliaji zinachakachuliwa na bado Chizza anaendelea kubaki ofisini kama Waziri.
“Waziri huyuhuyu ndiye anayezindua mbegu aina ya Chutoni ambayo haioti, bado ni Waziri. Waziri huyu huyu analipa ruzuku mbegu ya pamba isiyoota bado ni Waziri,” alisema Lugola.
Lugola alihoji kama Mchina aliyekuwa akijenga daraja la Kilombero alijiua kwa sababu tu ya kuhofia kupigwa risasi atakaporudi kwao, hata Waziri Chizza alipaswa awe ameiacha kazi hiyo.
“Simshauri waziri ajiue, lakini kwa vitendo vyote hivi waziri huyu angekuwa ameacha wizara hii na kupumzika na kufanya kazi nyingine mbadala,” alisema Lugola huku akipigiwa makofi.
Lugola alikumbushia Chizza alikuwa ni miongoni mwa mawaziri waliotajwa kuwa ni mizigo na kusema mambo yanayofanywa na wizara hiyo yatakigharimu Chama Cha Mapinduzi.
Mbunge huyo alibainisha kuwa, katika hotuba yake mwaka jana, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema Serikali iko kwenye mchakato wa kuanzisha mfuko wa kinga ya pamba ili kuwasaidia wakulima.
Hata hivyo, alisema katika hotuba ya Waziri Mkuu juzi, hakuna sehemu aliyozungumzia mfuko huo wala Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika katika hotuba yake ya mwaka huu, naye hajazungumzia mfuko huo.
“Hivi nchi hii tunaiendesha kwa usanii mpaka lini? Usanii juu ya usanii… Hatuwezi kuwadanganya wananchi kwa kiwango hiki. Itakuwaje mimi mbunge niunge mkono bajeti ya namna hii?” alihoji.

Alimgeukia Zambi na kumweleza kuwa aliwahi kumtahadharisha kuwa atakapokuja na bajeti yake ahakikishe anampa majibu ya asilimia 20 ya malipo waliyoahidiwa wakulima waliotumia mbegu ya chutoni.
“Uniambie asilimia 20 ya malipo ya wakulima ambayo waliahidiwa kwamba wakitumia chutoni walipwe kama sehemu ya malipo yao, lakini hili halimo kwenye bajeti,” alisema na kuongeza:
“Hakuna lolote humu ni blabla tu… Mheshimiwa Zambi wewe ulikuwa ‘backbencher’ (kiti cha nyuma) kama mimi ulikuwa unapiga muziki kama kasuku juu ya wizara hii, leo unashirikiana na waziri wako unakuja na vitu ambavyo havina majibu, maana yake nini?”
Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa (CCM), alisema wakati Zambi akiwa mbunge, alikuwa msitari wa mbele kupinga matumizi ya mbolea ya minjingu na kumtaka aeleze kama bado ana msimamo huo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda (Chadema), aliwashukia wakuu wa mikoa ya Simiyu na Geita kuwa ni chanzo cha tatizo kwa wakulima wa pamba.
Mbali na hilo, amemtaka Balozi wa Uingereza nchini ajitokeze kueleza misaada inayotolewa na nchi yake inavyotumiwa kwenye sekta ya pamba kwani imekuwa ni sehemu ya ubabaishaji kwa kuendeshwa semina zisizo na maana.
Shibuda alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akichangia maoni kwenye hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwa mwaka 2014/15.
Aliwatuhumu wakuu hao kuwa walimpeleka Waziri Mkuu katika kampuni ya Kiotoni wakamdanganya kuwa mbegu hizo ni nzuri, lakini kumbe hazikuwa zimefanyiwa utafiti wa kina na kuwasababishia hasara kubwa wakulima.
Shibuda alisema mbegu za kiotoni zina udhalimu mkubwa na hazina tija yoyote kwa wakulima lakini kila siku wakuu wa mikoa na wilaya wanazipigia debe licha ya kuwa wanatambua kwamba wakulima wanaumizwa.
Magdalena Sakaya aliifananisha Serikali kuwa ni sawa na sikio la kufa kwa kuwa kila wakati imeshindwa kuwa na majibu ya ukombozi kwa wakulima wa Tanzania ambao ndio wapigakura wao.
Mbunge wa Kasulu, Moses Machali (NCCR-Mageuzi) aliwapongeza wabunge wa CCM wanaoonyesha ujasiri wa kuisema Serikali yao kuwa inaendesha mambo kisanii na hivyo kushindwa kuwaletea wananchi maendeleo.
“Serikali imekuwa ikidanganya katika kutatua matatizo ya wananchi ndiyo maana tunaona ni Serikali ya maigizo… Ukisoma hotuba ya bajeti hapa haijibu matatizo ya wananchi,” alisema.
Wakati wabunge hao wakiiponda bajeti hiyo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imeitaka Serikali, kueleza ni lini na vipi wakulima walioathirika na mbegu feki watafidiwa.
Msemaji wa Kambi hiyo wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Rose Kamili, alisema tayari wakulima wameshapata hasara na bado wako wanaoendelea kuathirika na tatizo la mbegu kutoota.

Friday, 9 May 2014

Kafulila awalipua mawaziri akaunti ya Escrow

Dodoma. Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila jana aliibua tuhuma nzito bungeni akiwahusisha mawaziri wawili na Sh200 bilioni zilichotwa katika Akaunti ya Escrow, iliyokuwa inamilikiwa kwa pamoja kati ya Tanesco na Kampuni ya kufua umeme ya IPTL.
Katika tuhuma hizo, alimuunganisha pia Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na vigogo wengine, wakiwamo wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na wa Serikali, wote akiwataja tu kwa vyeo bila majina.
Mawaziri waliotajwa ni Waziri wa Nishati na Madini, Waziri wa Fedha na Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Ingawa Kafulila hakutaja kwa majina, Waziri wa Nishati ni Profesa Sospeter Muhongo, wa Fedha ni Saada Mkuya, Katibu Mkuu wa wizara hiyo (Nishati) ni Eliakim Maswi na AG ni Frederick Werema.
Kafulila alitoa tuhuma hizo bungeni alipokuwa akichangia hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2014/15.
Mbunge huyo alisema fedha zilizoibwa katika Akaunti ya Escrow ni nyingi kuliko zile zilizoibwa katika kashfa ya Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ya BoT mwaka 2005.
“Pamoja na hilo, Watanzania wamekuwa wakisikia kwenye vyombo vya habari kwamba Tanesco wakati ilipokuwa na mgogoro na IPTL walifika mahali wakafungua akaunti ya Escrow,” alisema.
Mbunge huyo alisema akaunti hiyo ilifunguliwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), mwaka 2004 na hadi jana, akaunti ile ilishafikia Dola za Marekani 122 milioni,” alisema Kafulila.
Alisema fedha hizo ziliwekwa kwa lengo maalumu kutokana na mgogoro uliokuwapo kati ya IPTL na Tanesco ili ziweze kusaidia malipo baada ya mgogoro kuisha katika Baraza la Usuluhishi wa Kibiashara la ISCID.
Alitaka jambo hilo liingie kwenye rekodi kwa kuwa linahusu BoT na vigogo akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Waziri wa Nishati na Madini pamoja na Katibu wake na pia Waziri wa Fedha.
Alisema wakati Tanesco ikidaiwa madeni zaidi ya Sh400 bilioni, viongozi hao wameidhinisha kugawanywa kwa fedha hizo kihuni jambo alilosema halivumiliki hata kidogo.
Kafulila alisema fedha hizo zilichotwa na Kampuni ya PAP aliyosema ya “Singasinga na ya kitapeli” ambayo iliidhinishiwa kuchota fedha hizo kinyume na utaratibu.
Alisema fedha hizo hazikupaswa kuchukuliwa kwa kuwa kulifanyika udanganyifu mkubwa kwamba PAP ilikuwa imenunua IPTL wakati jambo hilo si la kweli.
Alisema IPTL ilikuwa na makubaliano ya kufanya kazi kwa kampuni mbili ambazo ni VIP Engineering ya Tanzania iliyokuwa na hisa asilimia 30 na Mecmer ambayo ilikuwa na asilimia 70 ya hisa.
Hata hivyo, alidai kuwa anao ushahidi kuwa PAP ilikuwa imenunua hisa za VIP na hakukuwa na vielelezo vya kununua Mecmer kwa kuwa kampuni hiyo tayari ilishapoteza uhalali wake kwa kuwa ilikuwa chini ya muflisi nchini Malaysia.
Aliliambia Bunge kuwa wakati wa uchukuaji wa fedha hizo kutoka BoT, ilipaswa kulipiwa kodi lakini zilichukuliwa kinyemela bila hata ya kulipiwa kodi.
Alisema TRA iliiandikia Hazina na nakala kwa BoT kwamba wakati wa kulipa fedha hizo lazima kodi ikatwe, lakini cha ajabu hilo halikufanyika licha ya kukumbushwa.
“Kwa mfano, tulimwita Gavana katika kikao chetu cha Kamati ya Uchumi pale Bagamoyo na alikiri kuwa alibanwa na viongozi wa juu kiasi cha kushindwa kufurukuta, kwa hali kama hiyo Naibu Spika unategemea nini?” alihoji.
Kafulila alisema, Gavana katika kikao hicho alikiri kuwa, kulikuwa na presha (shinikizo) ambazo asingeweza kuzizuia na kuwa alikuwa amejitahidi kwa kiasi kikubwa hadi kufikia alipofika.
Alisema ISCID lilitoa hukumu ndogo Februari, mwaka huu kuwa Tanesco na IPTL wakae pamoja na kupitia hesabu zao namna watakavyogawanya fedha hizo na walipewa siku 60 ambazo mwisho wake ulikuwa jana.
Aliituhumu Tanesco kuwa katika makubaliano hayo ilikataa kukaa meza moja na kufanya hesabu za namna ya kulipana jambo alilosema linaonyesha ilidhamiria kufanya hivyo.
“Kwa sababu wanajua kuwa fedha ile ilishaliwa na wajanja wachache, Mheshimiwa Waziri Mkuu, hili kwa vyovyote halikubaliki na halivumiliki kwa sababu Dola122 milioni ni zaidi ya Sh200 bilioni ambazo ni nyingi kuliko za EPA, lazima litoke na mtu.”
Alisema hayuko tayari kuona fedha hizo zikitafunwa bila ya utaratibu na akashangazwa kuona Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), akishindwa kuchukua hatua.
Akoleza moto jioni
Katika kikao cha jioni, Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu alimwita tena Kafulila kutoa ufafanuzi wa hoja yake aliyoitoa mchana, ambayo iliombewa mwongozo na Mbunge wa Kisesa (CCM), Luhaga Mpina kwamba Gavana alishinikizwa kutoa fedha hizo.
Wakati wa mwongozo huo, Kafulila hakuwapo na ndiyo sababu ya Mwenyekiti kumpa nafasi ya kufuta kauli yake kuwa Gavana alishinikizwa. Hata hivyo, Kafulila alikazia akisema alishinikizwa kutoa fedha hizo.
“Gavana aliwahi kuniambia, mnanionea bure. Kulikuwa na presha kubwa sana kuhusu fedha hizi… ukweli ni kwamba IPTL inabadilishwa tu rangi na watendaji ni walewale.”
Baada ya Kafulila kuzungumza, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisimama na kusema: “Tuhuma dhidi ya Gavana wa Benki Kuu zinatolewa kwa kuwa hawezi kuingia bungeni kujitetea.
“Lakini Gavana tulimuuliza na akakanusha kuwa aliwahi kuyatamka hayo maneno na kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni atakuja kufafanua jambo hili kesho (leo) katika hotuba yake,” alisema Lukuvi.
Hata hivyo, Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee alisimama kuomba mwongozo akisema: “Kamati ya Bunge iundwe ili tuchunguze fedha hizi za Escrow zimekwenda wapi? Kafulila ana ushahidi wa kutosha, kwa nini hamtaki athibitishe?
“Vikao vyote vya kamati vinawekewa kwenye kumbukumbu rasmi (hansard) ili kujua kama Gavana alitoa maneno hayo ama hakutoa, iundwe kamati ijulikane mbivu na mbichi na wezi wa fedha za Escrow tunao humu ndani ya Bunge.”

Wednesday, 9 April 2014

Kamati kumi zaitesa CCM

Dodoma. Kura za awali katika Kamati 10 kati ya 12 za Bunge Maalumu la Katiba, zinakipa wakati mgumu Chama Cha Mapinduzi,(CCM) kutekeleza azma yake inayotajwa kuwa ni kufumua Rasimu ya Katiba, ili kuondoa mapendekezo ya Muundo wa serikali tatu, baada ya wajumbe wa Zanzibar kukwamisha upatikanaji theluthi mbili.
Kwa mujibu wa taarifa za kamati, ambazo tangu juzi zimeanza kutolewa katika sura ya kwanza na sita zinazungumzia Muundo wa Muungano, wajumbe kutoka Zanzibar kwa sasa ndiyo kikwazo kikubwa kwa CCM.
Hata hivyo, uamuzi ya mwisho kuhusu Muundo wa Serikali, kati ya mbili au tatu, unatarajiwa kujulikana Alhamisi wiki ijayo, wakati kamati zote zitakapowasilisha taarifa zao na kupigwa tena kura kwa wajumbe Tanzania Bara peke yao na Zanzibar peke yao.
Iwapo wajumbe wa Zanzibar wakiitetea kwa theluthi mbili kama sasa, mapendekezo ya muundo wa serikali tatu ndiyo yatakayopelekwa kwa wananchi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, baadhi ya wenyeviti wa kamati hizo, Stephen Wassira, Ummy Mwalimu, Anna Abdalah na Paul Kimili, walitaja moja ya vifungu ambavyo vimeshindwa kupata theluthi mbili kuwa ni ibara ya kwanza kifungu cha kwanza.
Akizungumza jana Wassira ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati Namba Sita alisema kwamba katika kamati yake ibara hiyo imeshindwa kupata theluthi mbili, ili kuweza kufanyiwa marekebisho.
“Lakini huu siyo mwisho kama nilivyosema awali, tukirudi bungeni tutapiga kura kwa wajumbe wote na ndiyo itakuwa na uamuzi wa mwisho kama muundo wa Muungano utakuwa na Serikali tatu ama mbili, ambao utapelekwa kwa wananchi,” alisema Wassira.
Jussa, Lissu- tumeibana CCM
Jussa alisema: “Kwa taarifa za matokeo tulizonazo katika Kamati Namba 1, 2, 3, 4, 6, 10, 11 na 12 mapendekezo ya kubadilisha Rasimu katika ibara hizo mbili yamekwama. Kama CCM wakichakachua sura ya kwanza na sita, maana yake ni kwamba hapa hakuna Katiba, hakuna kura ya maoni na hakuna mwafaka.”
Vifungu hivi pia kwa mujibu wa wenyeviti wa kamati nyingine, isipokuwa kamati ya Tano, ambayo inaongozwa na Hamad Rashid, havikupata kura theluthi mbili na hivyo kubaki kama vilivyo kwenye rasimu.
Naye Lissu alisema kwa sasa CCM ndiyo inaweza kuanza mkakati wa kuvuruga Bunge kwani tayari wamejua hawana theluthi mbili ya Zanzibar ili kubadili Rasimu kama wanavyotaka.

Msekwa: Sitta ana lake jambo

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samwel Sitta kukiri kuchezewa kwa saini ya aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika, Pius Msekwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Msekwa amesema, ‘mzungumzaji huyo ana lake jambo’.
Sitta akizungumza na gazeti hili juzi mjini Dodoma alisema ni kweli kuna maneno katika hati hiyo ya sheria namba 22 ya 1964, iliyosainiwa na Nyerere na Msekwa, Aprili 25, 1964, yameongezwa.
Alifafanua kuwa saini ya Nyerere imeongezwa herufi ‘us’ kwa kompyuta na katika sehemu ya saini ya Msekwa kumeandikwa neno ‘Msekwa’ kwa kompyuta, jambo ambalo ni makosa. Sitta alisema walioongeza maneno hayo ni wafanyakazi wa ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali baada ya kuona sehemu ya maandishi kwenye saini hizo hayasomeki, lakini walifanya makosa.
Msekwa akizungumza na gazeti hili jana alisema: “Saini iliyo katika hati original (halisi) ni ya kwangu mimi, lakini huyo anayesema zimechezewa muulizeni atakuwa na lake jambo. Kama kompyuta imekosea ni leo kwa kuwa kipindi hicho kompyuta hazikuwapo.”
Aliongeza: “Ana lengo gani la kutilia shaka, ana lengo gani la kusema imechakachuliwa, kinachotakiwa ni hati original ambayo iko ofisi ya Katibu wa Bunge itolewe, kwanini tuendelee kuandikia mate wakati wino upo?”
Maoni mengine
Mjumbe wa Bodi ya Kituo cha Taarifa kwa Wananchi Umma (TCIB), Hebron Mwakagenda alisema yote hayo yanatokea ni kuvuruga hoja iliyopo mezani.
Alisema kitendo cha kupoteza muda kuzungumzia suala la kuchezewa kwa saini halitakiwi kwani kama maudhui yake hayakuchezewa basi hoja ya muundo wa Muungano uamuliwe na wananchi wenyewe.
“Tusianze kupoteza muda kwa mambo ambayo hayapo cha msingi wananchi wenyewe waulizwe wanaupenda Muungano au la lakini tusianze kumtafuta mchawi kuwa saini zimechezewa wananchi waamue wenyewe kuhusu Muungano,” alisema Mwakagenda.
Sakata lilivyoanza
Utata huo ulianza wiki hii baada ya kamati za Bunge Maalumu la Katiba kuanza vikao vyake vya kujadili sura ya kwanza na ya sita ya Rasimu ya Katiba, zinazohusu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na muundo wake.
Hali hiyo ilitokana na kutopatikana kwa hati ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na ile ya Sheria ya Baraza la Mapinduzi ya kuridhia Mkataba wa Muungano.
Aprili 2 mwaka huu, Kamati namba 2 ilimwalika, Spika Mstaafu wa Bunge la Muungano, Pius Msekwa kutoa ufafanuzi kuhusu hati hizo, lakini uhalali wa saini zake uliibua malumbano makali. Msekwa aliitwa kutokana na kwamba ndiye aliyekuwa Katibu wa Bunge la Tanganyika wakati huo.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Shamsi Vuai Nahodha, alithibitisha kutokea utata huo na kwamba walilazimika kumuita Msekwa ili kupata ufafanuzi wa masuala kadhaa na Msekwa alisema saini zilizopo katika hati hiyo ni ya kwake.
Nahodha alisema kwa maelezo ya Msekwa, inaonekana hati ya Muungano ipo Umoja wa Mataifa (UN), kwani kabla ya Muungano, Tanganyika ilikuwa na kiti chake UN na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar hali kadhalika.
Aliongeza kuwa baada ya UN kuomba uthibitisho wa Muungano, ndipo walipelekewa hati hiyo na kwamba haijawahi kurejeshwa.
Kwa upande wake Katibu wa Bunge la Katiba, Yahya Hamis Hamad alisema hati hiyo ipo Dar es Salaam na ni moja tu, hivyo siyo rahisi kuipeleka bungeni Dodoma.

Matumaini Katiba Mpya arijojo

Ikulu imeeleza kuwa imeshindwa kutimiza ahadi yake kwa taifa ya kulipatia Katiba Mpya ifikapo Aprili 26, 2014.
Katibu Mkuu Kiongozi (KMK), Balozi Ombeni Sefue alilieleza gazeti hili kuwa kwa hali ya mchakato huo ilivyo sasa, wameshindwa kufikia lengo hilo, lakini hawajakata tamaa kuhusu kupatikana Katiba Mpya ndani ya mwaka huu.
“Kweli matarajio ya awali yalikuwa hayo, lakini kama unavyoona hali ilivyo, ni vigumu kusema matarajio mengine, ingawa majadiliano yaliyofanywa mwaka huu ni lazima Katiba inayopendekezwa iwasilishwe kwa wananchi na mwakani tutakuwa na Katiba Mpya,” alieleza Balozi Sefue.
Katika hali isiyoeleweka Balozi Sefue alisisitiza msimamo wa awali wa Serikali kwamba Katiba itakayopatikana itatumika kwenye Uchaguzi Mkuu, unaotarajiwa kufanyika mwaka ujao.
Dk Slaa
Katibu Mkuu wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (Chadema), Dk. Willbroad Slaa, alisema hilo ni fundisho kwa Serikali kwamba kiburi na jeuri havitakiwi katika masuala yanayohusu umma.
Alisema muda huo wa kupatikana Katiba Mpya ulipotangazwa, walioanzisha kilio cha kudai Katiba Mpya nchini ambao aliwataja kuwa ni vyama vya upinzani vya siasa, taasisi mbalimbali za kijamii walipinga na kutoa ushauri kwa Serikali, lakini walipuuzwa.
Dk. Slaa alisema walipendekeza kwamba badala ya kupeleka mchakato wa Katiba mchakamchaka, warekebishe kwa mara ya 15 Katiba inayotumika, ili iende na wakati wa sasa ikiwamo Uchaguzi Mkuu ujao kwa lengo la kutoa muda wa kutosha kwa mchakato wa taifa kupata Katiba Mpya.
“Lakini walitukebehi na kututukana sana, sasa kiko wapi Aprili 26 hiyo hapo na Katiba haijapatikana na kusema itapatikana mwaka huu na kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu mwakani ni ndoto za mchana,” alieleza Dk. Slaa.
Dk. Slaa alisema tukio hilo liwe fundisho kwa Serikali, wawe wakweli, wanyoofu na wafahamu kuwa nje ya Serikali kuna watu makini na wanaojua vilivyo mchakato wa Katiba.
Alisema ana taarifa za Bunge Maalumu kuahirishwa Mei 9, 2014 ili kupisha Bunge la Bajeti. Hivyo mategemeo ya Katiba Mpya kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, yanatia shaka.
“Kwa akili ya kawaida tu isiyohitaji elimu ya chuo chochote, kutumia Katiba Mpya kwenye Uchaguzi Mkuu ujao ni jambo lisilowezekana kwa hiyo waache kutuletea matumaini yasiyokuwapo, sisi siyo watoto wadogo,” alieleza Dk. Slaa.
Kauli ya LHRC
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Helen Kijo Bisimba, alisema siyo tu Serikali imeshindwa kutimiza ahadi ya muda iliyojiwekea, bali hata mchakato wenyewe haueleweki.
Dk. Bisimba alisema kwa hali ilivyo, hawana hakika ya kupata Katiba na ikipatikana haitakidhi matakwa ya wananchi, kwa kuwa wanataka Katiba ya watu siyo ya kundi moja la watu.
“Mambo ya nchi hii tunayafahamu, inaweza ikapatikana kwa nguvu lakini wajue wananchi wataikataa na hata ikilazimishwa, haitakidhi mahitaji, itaweza kuathiri ustawi wa taifa,” alieleza Dk. Bisimba.
Alisema hilo waliliona mapema, wakataka kila hatua ya mchakato ipewe muda wa kutosha kabla ya hatua nyingine, ili wananchi waelimishwe lakini hawakusikilizwa.
Alisema kuwa katika mazingira hayohayo, Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilifanya kazi kubwa hadi kufanikisha maoni ya wananchi kupatikana na kutengeneza Rasimu ya kwanza na ya pili iliyowasilishwa bungeni Machi 18, 2014, lakini kwa jinsi Bunge Maalumu linavyoendeshwa, kuna kila dalili kwamba kazi hiyo itaharibiwa.
“Wakichezea Rasimu wajue wanachezea maoni ya wananchi, wanaoweza kuyakataa kupitia kura ya maoni na hivyo kusababishia taifa hasara isiyomithilika,” alieleza Dk. Bisimba.
Dk. Bisimba alisema mchakato huo umegharimu taifa fedha nyingi, muda mwingi, nguvu, akili, afya na hata uhai wa watu, hautakiwi kufanyiwa mzaha.
Alipotafutwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro ili kuzungumzia suala hilo jana hakupatikana, lakini Naibu Waziri wa wizara hiyo Angela Kairuki, alisema kuwa kwa hali ilivyo ni dhahiri haiwezekani kupata Katiba Mpya kwa muda huu tofauti na ilivyodhaniwa awali.
Hata hivyo, Kairuki alisema hawezi kuzungumzia hatua iliyofikiwa katika mchakato huo kwani mwenye mamlaka ya kuzungumzia ratiba ya Bunge Maalumu la Katiba ni mwenyekiti wake, Samuel Sitta.
“Hata hivyo tunachotakiwa kuzungumzia ni ubora wa kazi inayofanyika ili kufikia lengo la kupata Katiba itakayoongoza nchi kwa miaka 50 ijayo,” alisema Kairuki.

Thursday, 3 April 2014

Waathirika wa milipuko ya Osama Dar wafurahia fidia

Dar es Salaam. Baadhi ya wanafamilia wa waliopoteza ndugu kwenye shambulio la ugaidi katika Ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam mwaka 1998, wameelezea kufarijika kutokana na malipo ya fidia, licha ya kwamba hayawezi kurejesha uhai wa waliokufa.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti, ndugu hao walisema, licha ya mahakama nchini Marekani kuwapa fidia lakini pengo la jamaa zao halitazibika.
Wiki iliyopita, Mahakama Kuu ya Marekani, ilitoa amri ya kuwalipa fidia ya dola za Marekani 957 milioni (Sh1.555 trilioni) waathirika 23 wa shambulio hilo.
Jaji Thomas Bates katika hukumu yake alisema kati ya fedha hizo, Dola za Marekani 420 milioni (Sh670 bilioni) watapewa ndugu wa marehemu watano na waathirika wanne wa Tanzania wakati kitita kilichobaki kitakwenda kwa waathirika ambao ni Wamarekani.
Jaji Bates alisema Serikali za Iran na Sudan zitawajibika kulipa fidia hizo kutokana na kuhusika na mashambulio hayo mabaya kuwahi kutokea Afrika Mashariki.
Mmoja wa jamaa waliopoteza maisha katika tukio hilo, Kulwa Ramadhan alisema anasubiri kuletewa taarifa zaidi kuhusu taratibu za kupata fidia hiyo.
“Huwezi kuwa umeridhika na fidia kwa kuwa tumepoteza ndugu zetu lakini pia hata hicho kilichopatikana hatukukitarajia kupata,” alisema Ramadhan.
Alisema kuna baadhi ya jamaa wa marehemu watano hawakuingizwa kwenye idadi ya watakaopata fidia kutokana na kuchelewa kujiandikisha katika kesi hiyo.
“Baada ya tukio uongozi wa Ubalozi wa Marekani ulituambia tutoe taarifa zetu zote za mawasiliano na kwamba tusibadilishe namba za simu kwa ajili ya kuwasiliana kinachojiri.
“Lakini kuna baadhi ya jamaa walibadilisha namba zao na kufanya mawasiliano kuwa magumu hivyo kushindwa kuingizwa katika idadi ya wadai katika kesi hiyo,” alisema.
Ramadhan aliyempoteza pacha wake, Dotto Ramadhani alisema baadhi ya jamaa walijitokeza baadaye baada ya hatua muhimu za kesi kufanyika kitendo ambacho kiliwazuia kushiriki katika kesi.
Waathirika wengine
Naye Judith Mwila aliyempoteza mume wake kwenye tukio hilo, alisema anashukuru Ubalozi wa Marekani pamoja na mawakili waliowasaidia kufanikisha kesi hiyo.
“Binafsi nimepata taarifa kamili jana (juzi) kutoka kwenye gazeti la Mwananchi na sikutarajia kama tungeshinda kesi hiyo na tukapewa fidia ya fedha kiasi hicho. Hata hivyo tunaendelea kusubiri taarifa za mawakili wetu kuhusu taratibu zinazofuata kupata fedha hizo,” alisema.
Aliongeza kuwa iwapo atapata sehemu ya fedha hizo atashauriana na watoto wake jambo la kufanya ikiwamo kufanya biashara kubwa. Mwila ana watoto watatu alioachiwa na marehemu mume wake.
Alisema kuwa tangu mchakato wa kesi ulipoanza mwanzoni mwa mwaka 2001, Ubalozi wa Marekani na mawakili wao, walimpeleka Marekani mara mbili.
“Kesi hii imedumu muda mrefu. Mara ya kwanza nilikwenda 2001 kutoa ushahidi na mara ya mwisho ni 2010 na tangu wakati huo tulikuwa tukipewa tu taarifa juu ya maendeleo ya kesi,” alisema Mwila.
Kwa upande wake, Grace Paulo ambaye alifiwa na mumewe Elisha Paulo alisema: “Ninamshukuru Mungu kwa sisi kushinda kesi hii na hivyo tunasubiri mawasiliano na wahusika kufahamu jinsi ya kupata fedha hizo.
“Tumekuwa tukiishi kwa shida sana, hivyo hizo fedha zitatusaidia kujikwamua na matatizo yanayonikabili na mwanangu,” alisema Paulo ambaye aliachiwa mtoto mmoja aitwaye Mary Paulo.
Kwa mujibu wa waathirika hao, Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Misaada la Marekani (Usaid) liliwapa msaada wa kuwasomesha watoto pamoja na makazi ili kupunguza makali ya maisha.
Hata hivyo, wengi wao wanaendelea kufanya biashara ndogondogo kutokana na misaada hiyo kuwekwa katika eneo maalumu la ada za watoto.
“Kwa sasa ninafanya biashara ya kuuza nguo za mitumba na nilishaondoka Dar es Salaam mara tu baada ya msiba mwaka 1998 kutokana na maisha ya mjini kuwa magumu.
“Baadaye Ubalozi kupitia taasisi za kiraia walinitafuta hadi wilayani Mpwapwa ndipo waliponijengea nyumba ninayoishi sasa,” aliongeza Paulo anayeishi mkoani Dodoma.
Jamaa hao pia walisema kuwa gharama halisi za kesi hiyo hawazifahamu kutokana na kesi nzima kusimamiwa na Serikali ya Marekani na mawakili wao.
Hata hivyo, uhakika wa kupata fedha hizo unabaki mikononi mwa wakili wa jamaa hao, Thomas Fortune Fay ambaye baada ya hukumu hiyo alisema anafuatilia jinsi ya kupata fedha kwa Serikali za Sudan na Iran.
Alisema ataangalia jinsi ya kutaifisha baadhi ya mali za nchi hizo ili kupata fedha za kuwalipa waathirika hao.

Jaji Warioba aishangaa Serikali



Dodoma. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema waliokuwa wajumbe wa tume hiyo hawajawahi kudai malipo ya pensheni ya Sh200 milioni kama inavyodaiwa.
“Wajumbe wa Tume hawajatoa madai ya kulipwa shilingi milioni mia mbili. Hakuna mjumbe yeyote aliyetoa dai kama hilo na Serikali inajua,” alisema
Jaji Warioba katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, aliyoitoa kupitia Nyalali, Warioba and Mahalu Law Advocates ali ongeza:
“Nimeona taarifa iliyotolewa na Serikali kuhusu Tume ya Mabadiliko, nimeshangazwa na maudhui na lugha iliyotumika,” alisema Warioba akirejea taarifa iliyotolewa na Ikulu juzi ikieleza jinsi tume hiyo ilivyohitimisha kazi zake.
Wiki hii Jaji Warioba alikaririwa akilalamika jinsi yeye na makamishna wake walivyoondolewa ofisini na kunyang’anywa magari kwa haraka bila kusubiri siku waliyopanga kufanya makabidhiano, lakini Ikulu ilimjibu kwamba shughuli za Tume hiyo zilikoma siku ambayo Tume ilivunjwa.
Katika taarifa yake ya jana, Jaji Warioba alisema aliwasilisha Rasimu ya Katiba Machi 18 mwaka huu na Tume ilivunjwa Machi 19 wakati wajumbe wakiwa bado mjini Dodoma.
“Pamoja na lugha ya kejeli inayotumiwa na Serikali kuniita mnafiki, busara ya kawaida ilitakiwa kutumika kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani na kuandaa makabidhiano,” alisema.
Alisisitiza kuwa Serikali ilikuwa na wajibu wa kuwarejesha makwao wajumbe wa tume hiyo, hata kama muda wa kisheria wa kufanya kazi ulikuwa umepita.
“Niliwasilisha Rasimu Machi 18, 2014. Tume imevunjwa Machi 19, 2014 wakati wajumbe wako Dodoma. Pamoja na lugha ya kejeli iliyotumiwa na Serikali na kuniita mnafiki, busara ya kawaida ingeonyesha umuhimu wa Serikali kujipa muda wa kufanya maandalizi ya kuwarudisha wajumbe nyumbani,” alisema Jaji Warioba na kuongeza:
“Hata kama sheria ilitaja muda wa kuvunja Tume bado ilikuwa ni wajibu Serikali kufanya mipango ya safari ya wajumbe baada ya kumaliza kazi. Sheria haikuizuia Serikali kufanya hilo. Huo ni wajibu wa Serikali na utaratibu wa kawaida unaotumiwa na Serikali kwa tume zote inazoziunda. Inaonekana Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliwekewa utaratibu tofauti. Kulikoni?”.