Thursday, 31 October 2013

Kapt Komba ajitoa mhanga, asema Lowassa Rais 2015

Dar es Salaam. Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Kapteni Mstaafu, John Komba amevunja ukimya na kutamka wazi kuwa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, ndiye chaguo lake na atakuwa Rais ajaye uchaguzi wa 2015.
Komba anakuwa mtu wa pili kumtaja Lowassa hadharani kuwa anafaa kwa rais 2015.
Itakumbukwa Mbunge wa Viti Maalumu, Beatrice Shelukindo (CCM) naye alivunja ukimya baada ya kutangaza kumuunga mkono Lowassa kumrithi Rais Kikwete.
Shelukindo alitoa kauli hiyo wakati akiwasalimia wakazi wa Monduli baada ya kukaribishwa kuchangia ujenzi wa Hosteli ya KKKT, kwenye sherehe za kukaribisha Mwaka Mpya zilizofanyika nyumbani kwa Lowassa na kuhudhuriwa na makada kadhaa wa CCM.
Akizungumza na Mwananchi katika mahojiano maalumu jana, Komba ambaye ni Kiongozi wa Kundi la Uhamasishaji cha CCM Tanzania One Theatre (TOT Plus), alisema mtazamo wake kwa mtu anayefaa kumrithi Rais Jakaya Kikwete ni Lowassa.
Komba aliyeingia kwenye siasa kutokana na msukumo wa mama yake aliyekuwa msaidizi wa Bibi Titi Mohamed, alisema anazo sababu kuu tano za kumkubali Lowassa kuwa Rais na atasimama popote kumtetea.
“Nakuambia Lowassa ndiye anafaa kuwa Rais... unafikiri kuna mwingine. Nina sababu zangu tatu,” alisema Komba na kuhoji:
“Wewe unakwenda kwenye harambee, nani leo hii anaweza kusaidia kuchangia kwa fedha nyingi na zote hizo ni kwa maendeleo yanayokusudiwa kama siyo Lowassa?”
alisema Komba ambaye ni mahiri katika kuinadi CCM, katika kampeni mbalimbali za udiwani, ubunge na urais.Juu ya kuwa atakuwa katika wakati mgumu endapo anayempigia debe hatokuwa, Komba alisema: “Mimi sikwambii ni nani, lakini wapo Mawaziri waliomkana, lakini leo hii wapo kwenye Serikali hii hii ya Rais Kikwete.
“Mimi nasema Lowassa, na kama akipita sawa nitaburudiiika kwelikweli, lakini kama akiteuliwa mwingine, mimi nitakuwa naye...nitamwimbia hadi mwisho. Kazi yangu si unaijua, nitampigia debe kwa kuwa si mtu wa mtu mmoja, ni uteuzi wa wanaCCM ule si wa Komba.” alisema.
Mbali na kumnadi Lowassa, Komba alisifu uimara wa chama chake kuwa kinaimarika siku hadi siku na ndicho kinachotoa viongozi wa kweli na hata wananchi wanakikubali.
Akizungumzia suala la rushwa ndani ya CCM, Komba ambaye pia ni Mbunge wa Mbinga, alisema kama chama kuna watu wa aina nyingi, kuna wasafi, kuna wachafu lakini wote wako kwenye mstari mmoja
Alisema kuwa vita ya rushwa ndani ya CCM itamalizika endapo kila kiongozi atasimamia kwenye haki na maadili ya uongozi na pia kutambua wajibu wake ndani ya chama.Komba alijipigia upatu kuwa ameleta maendeleo katika jimbo lake kwani jimbo linatazamika ikilinganisha na miaka ya nyuma kuwa wananchi walikuwa wakiishi maisha ya tabu na kimaskini ilhali wana raslimali za kutosha.

Sare za polisi: Ney wa Mitego asimulia kilichotokea

Dar es Salaam. Siku chache baada ya kukamatwa kwa tuhuma za kutumia sare za polisi bila kibali katika video ya wimbo ‘Salamu Zao’, na kisha kufikishwa katika Kituo cha Polisi Urafiki Manzese Jijini Dar es Salaam, rapa wa muziki wa kizazi kipya, Ney Wa Mitego amesimulia mkasa mzima na kusisitiza kuwa wabaya wake ndiyo waliycheza mchezo huo.
Akizungumza na Mwananchi, rapa huyo alisema sare hizo za polisi zilishonwa kwa ajili ya kazi hiyo na wala hazikuwa sare halisi za kipolisi.
“Mavazi haya ya kipolisi yalikuwa rasmi kwa ajili ya kutengeneza video ya Salamu Zao na hayakuwa halisi, ila nilishangaa pale nilipokamatwa na watu wasiojulikana jumamosi ya wiki iliyopita wakati tukitengeneza video, wakidai kwamba wao ni askari.Walinichukua hadi kituo cha urafiki, pale niliwekwa sero kwa kipindi cha dakika 20 hivi, baada ya kutoa maelezo ya kutosha niliachiwa”.
Baada ya kuachiwa, alirudi na kukamilisha kazi yake ambayo ameweka wazi kuwa itakuwa hewani wiki hii.
“Video ya Salamu Zao itaachiwa hewani Ijumaa ya wiki hii, hivyo watarajie kitu kipya na adimu kuonekana,” alisema Nay na kuongeza “Sijajua bado ni nani aliyenichomea lakini naahidi kuwa itaendelea kula kwao wale wote wanaonichukia na kamwe siwezi kuacha kuusema ukweli.”
Uongozi wa kituo cha Polisi Urafiki jijini Dar es Salaam ulithibitisha kumtia mbaroni msanii huyo kwa kukutwa akitumia sare zinazofanana na mavazi ya polisi kinyume cha sheria. Ofisi mmoja wa polisi ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini anasema waliamua kumuachia kwa vile waliridhika na maelezo yake.

Saini zakusanywa kumng’oa Makinda

Dodoma. Mbunge wa Nzega, Dk Khamis Kigwangalla, (CCM), leo anatarajiwa kuanza kukusanya saini za wabunge akitafuta kuungwa mkono katika hoja ya kutokuwa na imani na Spika wa Bunge, Anne Makinda kwa madai kwamba amekuwa akikiuka kanuni za Bunge.
Dk Kigwangalla aliibua hoja ya kutokuwa na imani na Spika katika kikao cha wabunge wote cha kuelezea shughuli zitakazofanywa na Bunge katika mkutano wa 13, kilichofanyika juzi jioni kwenye ukumbi wa Pius Msekwa.
Mbunge huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, jana alithibitisha kuwapo kwa mjadala huo katika kikao cha wabunge, lakini hakuwa tayari kueleza kwa undani na badala yake alisema kwamba leo ataanza kukusanya saini za wabunge kwa ajili ya kukamilisha hoja ya kutokuwa na imani na Spika Makinda.
Chanzo chetu kutoka katika kikao hicho cha wabunge kilibainisha kuwa Kigwangalla alihoji kuhusiana na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge (CCM-Bariadi Magharibi) kuteuliwa na Spika wakati katika kamati nyingine wenyeviti na makamu huchaguliwa na wajumbe wa kamati husika.
Pia Dk Kigwangala alisema Spika Makinda alivunja kanuni kwa kuwapa posho ya Sh430,000 kwa siku wajumbe wa kamati inayoongozwa na Chenge wakati wajumbe wa kamati nyingine wamekuwa wakipewa Sh130,000.
“Anachokifanya Spika ni matumizi mabaya ya fedha za umma, inakuwaje wengine wafanye kazi hata bila posho lakini wao (Kamati ya Bajeti), walipwe posho ya Sh430,000 kwa siku?” chanzo hicho kilimkariri Dk Kigwangalla akihoji. Hata hivyo, Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah akizungumza na gazeti hili jana alisema mazingira ya kamati fulani kupata malipo ya ziada tofauti na viwango vya kawaida hutokea pale uongozi wa kamati husika unapoomba kwa Spika.
“Si kweli kwamba Kamati ya Bajeti inalipwa fedha za ziada kila wakati, hapana, ni pale tu wanapoomba malipo hayo kutokana na sababu ambazo lazima Spika aridhike nazo. Ieleweke kuwa siyo kamati hiyo tu, kwa sasa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ambayo inachambua miswada mingi nayo imekuwa ikiomba na baada ya Spika kuridhia basi nao wanapewa,” alisema Dk Kashililah.
Katibu huyo wa Bunge alieleza kuwa zaidi ya kamati nane zimewahi kuomba malipo ya ziada kwa maana ya kutaka posho zaidi, ulinzi, usafiri na hata chakula, ikiwa zinakabiliwa na majukumu ya ziada pia katika mazingira tofauti nje ya utaratibu wa kawaida.
“Kimsingi, kamati nyingi zinapewa malipo tofauti, watu wanaweza kuwa na kazi mpaka saa saba au nane usiku, au wanakwenda kufanya kazi katika mazingira yasiyokuwa ya kawaida, taratibu zinamruhusu Spika kama akiridhika na maelezo ya kazi husika, basi anaruhusu kutekelezwa kwa maombi hayo,” alisema Dk Kashililah.
Kuhusu Serukamba
Aidha, Dk Kigwangalla alinukuliwa akisema Spika amekiuka kanuni kwa kumchagua Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, Peter Serukamba (Kigoma Mjini-CCM), kuwa mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti.
“Hakuna mbunge yeyote aliyepo katika kamati mbili lakini hata kungekuwa na sababu maalumu basi wa kuteuliwa angekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara, Mahmoud Mgimwa (Mufindi Kaskazini-CCM) ambaye TRA (Mamlaka ya Mapato Nchini) ipo chini ya kamati yake,” kilisema chanzo hicho.
Chanzo hicho kilisema Dk Kigwangalla alisema badala ya kumweka karibu katika ushiriki, Mgimwa alipokwenda katika kamati hiyo aliambulia kufukuzwa.
Akizungumzia suala hilo, Dk Kashililah alisema Serukamba pamoja na wabunge wengine kadhaa waliteuliwa na Spika kwa ajili ya kuongeza nguvu katika kamati hiyo wakati wa kipindi cha Bajeti Kuu ya Serikali.
Aliwataja wabunge wengine walioteuliwa kushiriki katika Kamati ya Bunge ya Bajeti kuwa ni John Cheyo (Bariadi Mashariki-UDP), Salahe Pamba (Pangani - CCM) na Hamadi Rashid Mohamed (Wawi - CUF).
Kanuni za Bunge
Kwa mujibu wa kanuni za Bunge katika toleo la mwaka 2007, kifungu cha 137(1), ili kumwondoa Spika madarakani, mbunge anayetaka kuwasilisha hoja hiyo atatakiwa kuwasilisha taarifa ya maandishi ya kusudio hilo kwa Katibu, akieleza sababu kamili ya kutaka kuleta hoja hiyo.
Kifungu kidogo cha pili kinasema baada ya kupokea taarifa ya maandishi ya kusudio la kumwondoa Spika kwenye madaraka, Katibu atapeleka taarifa hiyo kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa ajili ya kujadiliwa.
Kifungu cha tatu kinabainisha kuwa endapo kamati hiyo itaridhika kuwa zipo tuhuma mahususi dhidi ya Spika zinazohusu uvunjaji wa masharti ya ibara husika za Katiba, sheria au kanuni zinazoongoza shughuli za Bunge, basi kamati hiyo itaidhinisha hoja hiyo ipelekwe bungeni ili iamuliwe.
Kanuni zinasema Naibu Spika, atakalia Kiti cha Spika wakati wa kujadili hoja ya kutaka kumwondoa Spika madarakani na Spika atakuwa na haki ya kujitetea wakati wa mjadala na kwamba ili kumwondoa zinahitajika kura zisizopungua theluthi mbili ya idadi ya wabunge wote.

Babu Seya, watoto wake ‘watupa karata’ nyingine

Dar es Salaam. Mwanamuziki Nguza Viking maarufu kama Babu Seya na wanawe kupitia Wakili Mabere Marando wameiomba Mahakama ya Rufaa, ifanye marejeo kuhusu hukumu iliyoitoa na ifute ushahidi uliowatia hatiani na adhabu ya kifungo cha maisha jela wanayoitumikia.
Marando aliliwasilisha ombi hilo, kwa takribani saa 2 mbele ya jopo la majaji watatu wa mahakama hiyo .
Jopo hilo linaongozwa na Jaji Nathalia Kimaro, akisaidiana na Jaji Mbarouk Mbarouk na Jaji Salum Massati.
Wakili huyo alisema wateja wake wanaoomba mahakama ifute ushahidi uliowatia hatiani washtakiwa na badala yake iwaachie huru.
Upande wa Mkurugenzi wa Mashtaka, uliwakilishwa na mawakili Jacksoni Mlaki, Angaza Mwaipopo, Emakulata Banzi, Joseph Pande na Apimack Mbarouk.
Hata hivyo mawakili hao waandamizi wa Serikali, waliyapinga maombi hayo kuhusu marejeo kwa madai kuwa yamepelekwa mahakamani bila usahihi.
Marando alidai kuwa mahakama iliteleza katika kutoa uamuzi uliowatia hatiani na kuwafunga maisha Babu Seya na watoto wake na kwamba kuteleza huko kunaonekana wazi wazi.
Alifafanua kuwa wakati wakifanya majumuisho ya kesi hiyo, mahakama ilijiridhirisha kuwa kulikuwa na makosa katika kupokea ushahidi wa watoto wanaodaiwa kufanyiwa vitendo hivyo.
Alidai kuwa ushahidi wa watoto hao ulichukuliwa bila ya kufuatwa kwa taratibu za uchukuaji wa ushahidi wa mtoto.
Alisema kwa msingi huo, ushahidi huo ulipaswa kufutwa.
“Katika hukumu yenu mlikubaliana na sisi kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilikosea kupokea ushahidi wa watoto , ila mlisema hiyo si hoja maadam kuna ushahidi unaounga mkono ushahidi huo ni bora,”alilalamika Marando.
Alieleza kuwa mtoto mdogo anapotoa ushahidi licha ya tahadhari, ana uwezo wa kutambua zuri na baya na kwamba lazima ushahidi wake uwekwe kwenye kumbukumbu ya maandishi na kwamba usipoonekana ushahidi wote ni batili na uondolewe.
Aliendelea kueleza kuwa kwenye hukumu wanayoilalamikia, anaiomba mahakama ijisikie kubadili uamuzi wa kuwafunga maisha wateja wake.
“Tuanaomba ushahidi wa wale watoto ufutwe, uondolewe mahakamani na washtakiwa waachiwe huru,”alisisitiza.
Upande wa mashtaka ulipaswa kuwaita mashahidi hao lakini nyie majaji katika hukumu yenu mlisema upande wa mashtaka uanahiari ya kumwita shahidi wanayemtaka wao.

Friday, 25 October 2013

Rais wa Uswisi aifunda Tanzania jinsi ya kupata fedha za kifisadi


0
S

Katika mahojiano maalumu na timu ya waandishi wa Mwananchi na The Citizen jana, Graf alisema kuwa Serikali ya Tanzania inapaswa kusaini mkataba wa kimataifa wa kubadilishana taarifa za masuala ya usimamizi wa fedha na kodi ili kuweza kujua ni kina nani wameweka fedha nchini kwake na kunufaika na kodi.
Graf, ambaye alikuwa katika ziara ya kikazi nchini, alisema kuwa hivi karibuni Serikali ya Uswisi ilisaini mkataba wa kimataifa wa kubadilishana taarifa kuhusu masuala ya fedha, ambao unajulikana kwa lugha ya Kiingereza kama `Convention on Mutual Administrative Assistance in Tax Matters’.
Alisema ikisaini mkataba huo ina maana itasaidiwa na Serikali ya Uswisi kupata fedha zilizofichwa na Watanzania.
“Serikali ya Tanzania inatakiwa kuweka mkakati wa kisheria utakaotengeneza mazingira ya kubadilishana taarifa za fedha na mataifa mengine. Kwa jambo hilo hata Serikali ya Uswisi inaweza kusaidia katika kupatikana kwa fedha zilizofichwa,” alisema Graf, ambaye anaongoza Serikali ya Uswisi kwani kwa kawaida Rais wa Bunge ndiye pia kiongozi wa taifa hilo.
Graf alisema kwa sasa itakuwa ngumu kwa Tanzania kupata fedha hizo kwani haijasaini mkataba wa kimataifa wa kubadilishana taarifa za fedha na mataifa mengine.
Alieleza pia katika miaka ya karibuni Serikali ya Uswisi imeandaa muswada wa sheria wa kubana fedha zilizopatikana kwa njia za kifisadi na kufichwa katika benki za Uswisi. Graf alisema sheria hiyo ikipita itaruhusu Serikali ya nchi hiyo kutaifisha fedha ambazo zimepatikana kwa njia haramu na kufichwa katika benki za huko.
Muswada huo unaoitwa kwa lugha ya Kiingereza `Freezing and Restitution of Assets of Politically Exposed Persons obtained by Unlawful Means Bill’ ulisomwa kwa mara ya kwanza kwenye Bunge la nchi hiyo mwezi Mei, mwaka huu.
Graf alisema faida nyingine ya Tanzania kusaini mkataba huo ni kuwa, itaweza kuwatoza kodi Watanzania hao walioweka fedha huko.
Alifafanua kuwa siyo fedha zote zinazowekwa kwenye benki za Uswisi kuwa ni haramu kwani kuna nyingine zimepatikana kihalali, lakini zinaweza kutozwa kodi.
“Tanzania inakosa kodi kutokana na fedha zilizohifadhiwa na Watanzania wenye akaunti kwenye benki za Uswisi,” aliongeza Graf, ambaye alichaguliwa kuwa Rais wa nchi hiyo Novemba 26, 2012 na kutakiwa kukaa madarakani kwa mwaka mmoja.
Graf alisema pia fedha za kodi zingeisaidia Tanzania kugharimia sekta mbalimbali za maendeleo.
Zito aitupia lawama Serikali
Naye Waziri Kivuli wa Fedha, Zitto Kabwe, ambaye yuko nchini Uswisi akifuatilia masuala ya utoroshaji fedha na kufichwa kwenye benki za huko, alisema kuwa wakati shinikizo la dunia sasa limeelekea kumaliza tatizo la ukwepaji kodi na utoroshaji wa fedha kutoka nchi za Afrika, lakini Serikali ya Tanzania inasuasua juu ya kupambana na jambo hilo.
Zitto alisema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuwa moja ya njia ya Serikali za nchi maskini kupata taarifa za kampuni kubwa za kimataifa yanayokwepa kodi ni mfumo wa kupashana taarifa unaoitwa kwa lugha ya Kiingereza `automatic exchange of tax information’.
“Kutokana na shinikizo la nchi mbalimbali, hivi sasa nchi zinazoitwa `tax havens’ (nchi zinazohifadhi fedha kwa siri) fedha zimeanza kuweka sahihi makubaliano ya kutoa taarifa,” alisema Zitto, ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema).
Alisema kuwa Tanzania mpaka sasa haijaweka saini na Serikali haijatoa taarifa yoyote kwa umma juu ya sababu ya kutokufanya hivyo. “Ghana, Afrika Kusini na Nigeria nchi zinazotegemea sana rasilimali kama Tanzania zimeweka saini mkataba huu tayari,” aliongeza Zitto.Alisema asilimia 44 ya fedha za kigeni inazopata Serikali ya Tanzania zinatokana na mauzo ya madini nje. Kampuni za madini ndizo zinazoongoza kukwepa kodi.
Alisema Tanzania inapoteza jumla ya Dola 500 milioni (Sh783 milioni) na Dola 1.25 bilioni (Sh2 trilioni) kwa mwaka kutokana na kampuni kubwa za kimataifa kukwepa kodi.
“Hii ni sawa na kusema Tanzania inapoteza Dola2 milioni (Sh3.1 bilioni) kila siku kwa uporaji huu,” alisema Zitto.
Zitto alisema Serikali lazima ichukue hatua mara moja kuhakikisha Tanzania inaingia makubaliano ya kupashana taarifa za kikodi.
Jaji Werema agoma kujibu
Alipoulizwa juu ya Tanzania kutokusaini mikataba ya kimataifa ya kubadilishana taarifa za utoroshaji fedha na mambo au kodi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alisema hawezi kujibu suala hilo.
“Muulize huyo aliyekwambia kuwa Tanzania haijasaini mikataba ya kubadilishana taarifa za utoroshaji fedha na masuala ya kodi. Naomba uniache nifanye kazi zangu,” alijibu Jaji Werema kwa mkato na kukata simu.
Mahojiano kamili na Rais wa Uswisi, soma Mwananchi Jumapili.

Wednesday, 23 October 2013

Mshahara wa mwajiriwa wa wananchi unakuwaje siri


Share

Dar es Salaam. Ni ajabu kusikia kauli ya Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe kuhusu mishahara wanayolipwa Rais na Waziri Mkuu inazusha mjadala mkubwa.
Zitto akiwa wilayani Igunga hivi karibuni, alijitoa mhanga na kutangaza viwango alivyodai  kuwa ni mishahara ya rais na waziri mkuu kwa mwezi, huku akihoji iweje viwango viwe siri na visikatwe kodi.
Baadhi ya watu wamepinga hatua hiyo wakisema mshahara wa mtu ni siri yake. Waliopinga ni pamoja na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai na Waziri wa Nchi Katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya utumishi wa Umma, Celina Kombani akisema kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Sawa, inaweza kuwapo sheria inayozuia jambo hilo, lakini kwanini itungwe sheria ya namna hiyo?
Kwa upande wangu naunga mkono mishahara hiyo kuwa wazi. Nakubali kwamba mshahara wa mtu ni siri yake, lakini kwa viongozi wa umma kama rais na waziri mkuu, mishahara yao haipaswi kuwa siri, ndiyo maana nchi nyingi duniani zikiwemo Marekani, Ufaransa, Kenya na Afrika Kusini, mishahara ya viongozi kama huwekwa wazi.
Ifahamike kuwa rais ni kiongozi anayechaguliwa na wananchi, wao ndiyo wanaompa ajira ya kuwatumikia. Iweje mwajiri asijue anacholipwa mtumishi wake?
Kwenye nchi zilizoendelea kidemokrasia kama vile Marekani na nchi za Ulaya, masilahi na utendaji wa rais na waziri mkuu na viongozi wengine ni ya kikatiba.
Wananchi wanajua wazi kabisa, rais wanayemchagua watamlipa kiasi gani, Katiba inamwelekeza rais ateue mawaziri wangapi na watendaji wa Serikali kwa idadi maalumu.
Cha ajabu huku kwetu, rais anaamua kufanya atakavyo – anaweza hata kuteua mawaziri idadi anayoitaka na asiulizwe, mambo yanafanywa kwa siri ndiyo maana hata mikataba ya madini na uwekezaji mwingine ni siri.
Siri hizi za nini kama sisi wananchi ndiyo tumeichagua Serikali yetu wenyewe?
Hoja nyingine ni kuhusu mshahara wa rais kutokatwa kodi. Rais ni mtumishi wa umma namba moja na mlezi wa watumishi hata wa sekta binafsi.
Kwa muda mrefu wafanyakazi wamekuwa wakilalamikia kiwango cha asilimia 15 cha kodi wanayokatwa katika mishahara ndiyo ikashushwa hadi asilimia 14, hata hivyo bado ni mzigo.
Lakini rais atauonaje mzigo huo ikiwa yeye hakatwi kodi? Rais kwa mujibu wa Zitto analipwa wastani wa Sh32 milioni kwa mwezi bila kukatwa kodi, ana marupurupu ya safari za ndani na nje ya nchi na posho nyinginezo.
Kwa maana nyingine rais anaweza asiuguse kabisa mshahara wake kwa posho hizo, lakini bado akistaafu analipwa pensheni na atatunzwa na Serikali maisha yake yote.
Tuna viongozi wa Serikali wangapi wanaolipwa hivi, tuna marais wastaafu na mawaziri wakuu wangapi wanaofaidi kiinua mgongo cha Serikali huku idadi kubwa ya Watanzania ikiteseka katika lindi la umasikini na mlolongo wa kodi?

Vyama vya siasa vimebadilika kifikra’



Dar es Salaam. Baadhi ya wasomi jijini Dar es Salaam, wamevipongeza vyama vya siasa kwa kitendo cha kukubaliana kuhusu maboresho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na kuifanya Serikali kuandaa hati ya dharura.
Wasomi hao wamesema vyama hivyo vimeonyesha kubadilika kifikra.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti jana, wasomi hao walisema ili nchi iweze kupata Katiba Mpya yenye masilahi kwa nchi husika, lazima wananchi na vyama vya siasa wakubaliane na kuwa kitu kimoja, jambo ambalo limedhihirika juzi.
Mwanasheria maarufu, Profesa Chris Peter Maina alisema, “Vyama vimetoa hoja nzito kuhusu kasoro zilizomo katika sheria husika, pamoja na kuamua kuweka kando tofauti zao na kuungana, binafsi nimependa zaidi hoja zao za msingi zilizolenga masilahi ya taifa kuliko vyama vyao.”
Profesa huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar, alisema hata wabunge wa vyama hivyo wanapaswa kuwa kitu kimoja katika kupitisha mabadiliko hayo.
Mwanasheria mwingine, Berious Nyasebwa alivipongeza vyama hivyo na kusisitiza kuwa uamuzi uliochukuliwa umejaa busara na hekima.
“Hoja hii ya Serikali sidhani kama itapingwa na wabunge ikifika bungeni, wanasiasa wameamua kukubaliana na wametambua wazi kuwa tendo la kuandika Katiba Mpya ni la maridhiano si la mtu binafsi wala chama fulani” alisema Nyasebwa.
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Profesa Gaudence Mpangala alisema, “Binafsi nimepata matumaini mapya juu ya mchakato huu baada ya vyama kuamua kuweka kando tofauti zao. Kilichofanyika ni mageuzi ya kifikra.”
Hata hivyo Profesa huyo alisema kulikuwa na ulazima kwa tume hiyo iliyokuwa imalize kazi yake Novemba 1 kuomba kuongezewa muda, kwa maelezo kuwa bado ilihitaji kufanya uchambuzi wa maoni mbalimbali, ili kukamilisha rasimu ya pili ya Katiba.
“Sidhani kama muda ulioongezwa utaathiri mchakato mzima wa Katiba.”

Vatican yamsimamisha askofu Mjerumani kwa kupenda raha

Kumekuwa na kelele za waumini nchini Ujerumani wakishinikiza askofu huyo afukuzwe kwa kukiuka taratibu.
Vatican City. Makao Makuu ya Kanisa Katoliki Duniani (Vatican) yamemsimamisha kazi Askofu wa Jimbo la Limburg, Ujerumani Franz-Peter Tebartz-van Elst anayekabiliwa na kashfa ya matumizi mabaya ya fedha kwa shughuli za kifahari.
Vatican ilieleza jana kuwa uamuzi huo umechukuliwa baada ya kuridhika kuwa Askofu van Elst amekiuka maadili yaliyowekwa na Papa Francis kwa viongozi walioko chini yake akiwataka waishi maisha ya uchaji, umaskini.
Hadi sasa, kumekuwa na kelele nyingi miongoni mwa waumini nchini Ujerumani wakitaka askofu huyo afukuzwe kazi.
Miongoni mwa matumizi yake makubwa ni ujenzi wa makazi yake binafsi yaliyogharimu Euro 2.9 milioni (Dola 3.9 milioni), ukumbi wa chakula wenye mita za mraba 63 ambao ni pamoja na mesi na bafu yenye thamani ya Euro 15,000.
Askofu van Elst (53) amekuwa akituhumiwa kuendesha miradi hiyo kwenye mji wa kihistoria wa Limburg, ikiwamo makumbusho, kumbi za mikutano, kanisa dogo na nyumba ya makazi yake binafsi.
Fedha hizo zinatokana na mapato ambayo ni misamaha ya kodi kwa vikundi vya kidini nchini Ujerumani kwa mujibu wa sheria.
“Baada ya uchunguzi wa awali, Vatican imeamua kuchukua hatua kumsimamisha na kumwondoa kwenye usimamizi wa jimbo,” ilieleza taarifa hiyo.
“Baba Mtakatifu (Francis) amekuwa akifuatilia kwa karibu mambo yote yanayoendelea katika Jimbo la Limbuerg,” iliongeza taarifa hiyo.
“Hali hiyo imefikia mahali ambako kiongozi huyu hawezi kuendelea kusimamia kazi zake za kitume kama askofu wa jimbo.”
Hata hivyo, taarifa hiyo haikueleza ni kwa muda gani Askofu van Elst amesimamishwa kazi, ila iliongeza kuwa itategemea na kukamilika kwa uchunguzi, tathmini ya hali ya fedha ya jimbo na mambo mengine.
Wiki iliyopita, Askofu van Elst alisafiri hadi mjini Rome, Italia kwa ndege ya shirika la gharama nafuu, Ryanair kujieleza mbele ya Papa Francis – kutokana na madai kuwa alisafiri mwaka jana kwa ndege ya daraja la kwanza kwenda India na pia kutumia vibaya fedha.
Taarifa za matumizi hayo makubwa ya kiongozi huyo zimelitikisa Kanisa Katoliki la Ujerumani huku wengi wakitaka uwazi katika matumizi ya fedha -- mageuzi ambayo Papa Francis amekuwa akiyapigia kelele na kutaka kanisa maskini kwa watu maskini. Miradi hiyo kwa pamoja ambayo iliidhinishwa na mtangulizi wake awali ilikadiriwa kutumia Euro 5.5 milioni, lakini iliongezeka kwa kiasi cha kutisha na kufikia Euro 31 milioni ikiwamo bustani yenye thamani ya Euro 783,000.
Pia, Askofu Tebartz-van Elst anatuhumiwa kwa kutoa taarifa za uongo mahakamani kuhusu safari yake ya India kutembelea familia maskini.
Waendesha mashtaka wa Serikali wanaeleza kuwa askofu huyo alitoa taarifa za uongo chini ya kiapo kwenye mahakama ya mjini Hamburg dhidi ya gazeti la kila wiki, Der Spiegel akikana safari ya India anakodaiwa kutumia daraja la kwanza. Matumizi makubwa ya askofu huyo yameudhi walipa kodi wa Ujerumani wakidai kwamba wanakamuliwa huku fedha zikitumiwa vibaya na wengi wao kuandamana nje ya makazi ya askofu huyo.
Kansela Angela Merkel, binti wa kiongozi wa zamani wa Kipentekoste amesema kupitia msemaji wake, Steffen Seibert kwamba ana matumaini Kanisa Katoliki litamaliza tatizo hilo kwa jina la Yesu. Askofu Tebartz-van Elst hata hivyo ametetea miradi yote akieleza inalenga kudumisha mila na historia ya eneo hilo.
Tangu kuingia madarakani kwa Papa Francis, kumekuwa na kasi ya mabadiliko ndani ya kanisa.

Uswisi sasa kurejesha mabilioni ya mafisadi

Dar es Salaam. Sakata la vigogo kuficha mabilioni ya shilingi katika benki za Uswisi, limechukua sura mpya baada ya Serikali ya nchi hiyo kutunga sheria inayowabana walioweka fedha kwenye benki zake kuzithibitisha, la sivyo zitarejeshwa katika nchi husika.
Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe alifanya mazungumzo na Serikali ya nchi hiyo ambayo imemweleza kuwa imebadili sheria zake ili kuwadhibiti wageni wanaoficha fedha nchini humo.
Akizungumza na gazeti hili, Zitto alisema amepata taarifa hizo juzi baada ya kukutana na Waziri wa Fedha wa nchi hiyo ambaye alimwandalia mazungumzo na watalaamu wake.
Alibainisha kuwa tangu kuibuka kwa sakata hilo mwaka 2012 na Bunge kuiagiza Serikali kufuatilia, Serikali haijaomba taarifa yeyote kutoka Uswisi kuhusu Watanzania waliohifadhi fedha nchini humo.
“Jana nilikutana na Waziri wa Fedha na akatuacha na mazungumzo na wataalamu wake. Wamesema hadi sasa, Tanzania haijasaini mkataba wa kubadilishana taarifa za kikodi (Multilateral convention on administrative assistance in tax matters),” alisema Zitto na kuongeza;
“Kwa kutosaini, Tanzania inajinyima haki ya kupata taarifa hizi na kutoza kodi kwa watu walioficha fedha huku (Uswisi), maana Sheria ya Kodi ya Tanzania inataka kila Mtanzania popote anapopata kipato halali lazima alipe kodi.”
Zitto alieleza kuwa kitendo cha Serikali ya Uswisi kubadili sheria zake, kinaiwezesha nchi hiyo kutoa taarifa za benki za watu walioweka fedha nchini humo wakiwamo Watanzania, ambao sasa watatakiwa kuthibitisha kama fedha hizo ni safi au la.
“Kiufupi, Tanzania haijaomba taarifa yeyote kutoka Uswisi. Ila Uswisi wamebadili sheria yao na sasa mmiliki wa fedha ndiyo anapaswa kuthibitisha kwamba ni safi, na ikithibitika kuwa hazina mwenyewe wala maelezo, zitarudishwa nchi husika,” alisema.
Zitto alisema mbali na kukutana na watendaji hao wa Serikali amezungumza na Umoja wa Mabenki wa nchi hiyo uliobainisha kuwa Uswisi ina Watanzania wachache wenye fedha.
“Wamesema Watanzania wengi wana fedha Uingereza, Jersey, Cayman Islands na Mauritius. Dubai pia imetajwa sana,” alisema Zitto. Zitto alielezea kuwa umoja huo wa benki za Uswisi umeanzisha mkakati wa kusafisha fedha uitwao ‘clean money strategy’, na wamegundua watu wengi ambao ni wanasiasa, wamezuia akaunti zao na kupeleka majina kwenye Serikali zao.
“Tanzania haijafanya maombi rasmi hapa Uswisi na hivyo wao kama benki hawawezi tu kutoa taarifa bila kuombwa. Sheria yao imerekebishwa ambapo sasa ni wajibu wa mwenye akaunti kusema kama fedha zake ni halali au hapana,” alisema Zitto na kuongeza.
Hivi sasa hawapokei pesa kutoka nchi za Afrika au wanapokea kwa tahadhari sana, maana kuna reputational risk (kupoteza heshima),” alisema.
Wito wa timu ya uchunguzi
Zitto alipendekeza timu iliyoundwa kuchunguza fedha hizo itoe taarifa yake kwenye Mkutano wa Bunge unaoanza Oktoba 29, mwaka huu, akieleza kuwa, “Kuendelea kukaa na taarifa, kutaongeza tetesi za kweli au za uwongo.”
Alisema mpango huo wa kusaka fedha zilizofichwa nchini Uswisi, umelenga zile zilizofichwa na watu binafsi kutokana na rushwa au kuuza dawa za kulevya na kampuni kubwa za kimataifa.
Alibainisha kuwa wengi waliotambulika ni wanasiasa, vigogo wa jeshi na wakuu wa mashirika ya umma na watendaji wa Serikali.
“Katika mabenki ya Uswisi, kuna kiasi cha Dola za Marekani 197 milioni. Fedha nyingi zipo katika benki za Uingereza na visiwa vyake, Dubai na Mauritius,” alisema na kuongeza;
“Wapo watu waliopata fedha kihalali, lakini wanaficha fedha hizo na mali zao nje ili kukwepa kodi. Wengi wa hao ni wafanyabiashara wakubwa nchini. Tanzania inapoteza Dola za Marekani 1.25 bilioni kati ya mwaka 2001 na 2012 kwa njia hizi.”
Alibainisha kuwa Tanzania lazima itunge sheria ya kufilisi mali ambazo mtu anashindwa kuthibitisha amezipataje.
“Tayari ninafanyia kazi muswada binafsi wa sheria wa kubadilisha sheria ya makosa ya jinai ya mwaka 1991. Wasaidizi wangu wanafanyia kazi muswada huo ili usomwe kwa mara ya kwanza kwenye mkutano wa Bunge unaonza Oktoba 29 na kueleza kuwa sheria ya sasa ina upungufu,” alisema.
Madai hayo ya Zitto yamekuja ikiwa umepita mwaka mmoja tangu Bunge kuipa Serikali muda wa kuchunguza sakata la vigogo walioficha mabilioni katika benki za Uswisi.
Zitto ndiye aliibua sakata hilo mwishoni mwa mwaka 2012. Kufuatia hoja hiyo, Serikali iliunda timu kutokana na Azimio la Bunge lililotolewa mwishoni mwa mwaka jana.
Werema ahoji Mwananchi

ni Bunge?
Timu hiyo inaongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema ambaye jana baada ya kutafutwa na gazeti hili alisema, “Uchunguzi kuhusu walioficha fedha Uswisi bado haujakamilika.”
Viongozi wengine wanaounda tume hiyo ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hosea, Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa, Othman Rashid na Gavana wa Benki Kuu (BoT), Profesa Benno Ndulu.
Alipoulizwa kama kuna uwezekano wa ripoti hiyo kuwekwa wazi katika Mkutano ujao wa Bunge, Werema alisema, “Kwa nini, kwani wewe ndiyo Bunge. Uchunguzi bado unaendelea”
Hata hivyo, kwa mujibu wa agizo la Bunge, tume hiyo inatakiwa kuwa imekamilisha uchunguzi wake mwezi huu na kuwasilisha ripoti yake katika mkutano huo wa Bunge.
Alipoulizwa kuhusu ripoti hiyo, Naibu Spika, Job Ndugai alisema, “Wiki ijayo katika kikao cha Kamati ya Uongozi, Serikali itatakiwa kutoa taarifa za uchunguzi huo na kama haujakamilika kikao hicho kitaamua jambo la kufanya na endapo uchunguzi utakuwa umekamilika zitapangwa taratibu za kuiwasilisha ripoti bungeni.”
Waziri wa Fedha anena
Naye Waziri wa Fedha, Dk William Mgimwa alisema jana kuwa sheria za kimataifa zipo wazi kwamba fedha chafu zinazogundulika kufichwa nchi fulani, hurejeshwa katika Serikali ya nchi husika.
“Lengo la sheria hizi za kimataifa ni kuhakikisha kuwa fedha za wizi zinazoibwa nchi fulani, haziwezi kuhifadhiwa katika nchi nyingine,” alisema.
Alipoulizwa kama wizara yake ina taarifa zozote kuhusu Watanzania walioficha fedha Uswisi alisema, “Kuna Tume iliundwa na Bunge kufuatilia suala hilo nadhani ndiyo itakuwa na majibu sahihi.”
Uchunguzi wa walioficha mabilioni ya Uswisi uliibuka baada ya Benki ya Taifa ya Uswiss (SNB) kutoa taarifa mapema Juni 2012 kuhusu raia wa kigeni wanaomiliki akaunti za benki nchini humo.
Orodha hiyo inadaiwa kuwa na majina ya baadhi ya Watanzania wenye akaunti zinazofikia Dola 196 za Marekani milioni ambazo ni sawa na Sh323.4 bilioni.

Elimu ya Tanzania iko mahututi’

Dar es Salaam. Siku moja baada ya maudhui ya Ripoti ya Tume iliyoundwa kuchunguza matokeo ya kidato cha nne ya mwaka jana kuwekwa wazi, wadau wa elimu wamekiri na kusema kuwa mfumo wa elimu ya Tanzania upo katika hali mbaya.
Akizungumza na gazeti hili jana, Mbunge wa kuteuliwa na Rais, James Mbatia alisema matokeo ya tume hiyo yanaonyesha udhaifu wa hali ya juu katika sekta ya elimu jambo ambalo alishawahi kulisema katika hoja maalumu bungeni.
Mbatia, ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi, alisema alishawahi kuishauri Serikali kuufumua mfumo wa elimu nchini na kuanza upya ili kunusuru taifa la kesho ambalo ndilo linaloathirika na rasilimali watu zisizo na ubora.
Matokeo ya kidato cha nne ya mwaka jana yalionyesha kuwa asilimia 60.6 ya wanafunzi Tanzania walipata alama sifuri na wanafunzi 23,520 sawa na asilimia tano ndiyo waliofaulu jambo ambalo lilisababisha Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuunda tume ya kuchunguza matokeo hayo.
Baadaye, mitihani hiyo ilisahihishwa upya na Pinda kukabidhiwa matokeo Juni, mwaka huu.
“Nilishasema katika hoja yangu bungeni Januari 31 na Februari 1, mwaka huu nikamwomba waziri anionyeshe mitaala ya elimu ya sasa, lakini hakuitoa,” alisema Mbatia.
Mbatia alisema ili taifa hili liondokane na janga la elimu lililopo halina budi kukubali kuwa ni kweli Tanzania ipo katika janga la elimu na kuunda dira ya elimu itakayotuongoza katika safari ya elimu nchini.
Mbatia aliongeza kuwa elimu ya Tanzania ipo mahututi na kuwa kila mwaka wanafunzi wanaomaliza katika shule mbalimbali hawana sifa za kutosha za kuweza kushindana katika masoko ya kimataifa.
“Tumeshaanza kuona taifa linaangamia kwa sababu ya ubovu wa elimu, ni lazima tukiri hilo kwa sababu hata Rais alikiri na kuikubali hoja yangu Aprili 30 mwaka huu alipokuwa mkoani Mbeya” alisema Mbatia
Mbunge huyu ambaye awali aliteuliwa kuwa miongoni mwa wajumbe wa tume ya uchunguzi wa matokeo haya na kukataa kushiriki alisema, ili Serikali iondokane na janga hili haina budi kuunda Kamati ya Bunge ambayo itaisimamia Serikali na kutoa mawazo mapana kuhusu elimu.
Mbatia alishauri Bunge lisiegemee itikadi za vyama au porojo za kutaka sifa za kisiasa na badala yake suala la elimu lijadiliwe kwa maslahi ya taifa.
Mdau mwingine wa elimu, Dk Method Samwel, ambaye ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Elimu cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (DUSE), alisema tatizo la elimu hapa nchini lielekezwe zaidi kwenye mfumo uliopo kuliko laumu taasisi au mtu mmoja mmoja

Dk Samwel alisema tangu zamani mfumo wa elimu umekuwa ni wa kudorora na haya ni matokeo ya mfumo huo ambao haukuwa na misingi imara kwa muda mrefu.
Alitolea mfano wanaokwenda kusomea ualimu wengi ni wale waliofeli kwa kupata daraja la nne, jambo ambalo linasababisha wataalamu wa kada hiyo kuwa ni wale waliofeli pekee.
“Yapo mambo mengi yanayotakiwa kufanyiwa kazi katika sekta ya elimu Tanzania, suala la kudai kuwa Baraza la Mitihani na Taasisi kuwa ndizo taasisi zenye makosa, hazina ukweli,” alisema.
Hata hivyo, Dk Samwel alisema, tume hiyo bado ina maswali mengi ya kujibu kulingana na walichokisema katika sehemu ya ripoti yao.
“Nashindwa kuelewa kwa sababu kila nikisoma majibu ya tume hiyo napata maswali mengi zaidi. Kwa mfano, walimu waliofanya mtihani wakafeli walipewa muda wa kujiandaa? “ alihoji na kuongeza:
“Na kuhusu mitihani ya Tanzania kuonekana kuwa ni migumu zaidi, Je waliwapa mitihani ya Tanzania wanafunzi wa nchi nyingine au walitumia mbinu gani kupata matokeo hayo?”
Hata hivyo, Mkuu wa Kitivo cha Elimu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Kitila Mkumbo, alipinga ripoti ya tume hiyo na kusema kuwa wamepotosha taarifa kwani tatizo halikuwa katika mtihani bali ni wanafunzi wenyewe wamefeli.
Dk Mkumbo amesema tatizo si la walimu, wala baraza, wala mitihani yenyewe bali ukweli utabaki kuwa wanafunzi walifeli mtihani wa Kidato cha Nne kwa sababu ya mfumo mbovu wa elimu.
Mhadhiri huyo alihoji tena kuwa tume hiyo ilitumia njia gani kujua kuwa mtihani wa Sayansi ulihitaji saa sita kuufanya na ni kwa mbinu gani waliupima mtihani wa Tanzania na kujua kuwa ni mgumu kuliko mitihani mingine.
“Nilipata ripoti fulani iliyoonyesha kuwa mitihani ya Tanzania ni mizuri na haina matatizo, ripoti ilionyesha kuwa haina chembe ya mashaka na inatungwa kwa ustadi. Tusitafute sababu, tatizo si mitihani ni wanafunzi wenyewe wamefeli,” alisema.
Pia, Dk Mkumbo alisema kuwa ni dharau kubwa kusema kuwa baadhi ya wasahihishaji hawakuwa na sifa kwani hilo ni tusi kubwa kwa walimu kwani wao ndiyo wamekuwa wakisahihisha kila siku.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Shule Binafsi nchini,(Tamongsco), Albert Katagira alisema si kweli kuwa mtihani ulikuwa mgumu bali tatizo lipo katika uandaaji wa wanafunzi.
 “Mtihani ulikuwan sahihi kabisa, mbona wanafunzi wengine walifaulu. Ni wanafunzi wenyewe, ambao nao hatuwezi kuwalaumu moja kwa moja,” alisema Katagira.
Alisema taifa bado lina tatizo katika mfumo wa elimu na kuweka mkazo katika masomo ya sayansi na hisabati ambayo yanaonekana kuwa magumu kwa wanafunzi wengi.
Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Mafinga, Mustapha Mambea alisema, mtihani wa Fizikia na Kemia haikuwa migumu, lakini kuna mada kadhaa ambazo hawakufundishwa.
Profesa Mchome aongea
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Sifuni Mchome alisema kuwa wameshindwa kuiweka hadharani ripoti hiyo kwa kuwa bado inafanyiwa kazi serikalini.
Profesa Mchome, ambaye ndio aliongoza tume hiyo, alisema kuwa ripoti hiyo inatakiwa kupelekwa kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri kwa ajili ya kujadiliwa.
Alidokeza, hata hivyo, tayari walikuwa wameanza kufanyia kazi baadhi ya vitu vinavyotakiwa kufanyiwa kazi haraka kwenye ripoti hiyo.
Katibu Mkuu wa Necta, Dk Joyce Ndalichako, ambaye ameomba likizo ya muda mrefu ikitafsiriwa pengine ndio mwanzo wa utekelezaji wa ripoti hiyo.