Friday, 20 September 2013

Hakimu achomwa kisu mahakamani

Shinyanga. Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo iliyopo eneo la Nguzo Nane, Kata ya Kambarage Mjini Shinyanga, Satto Nyangoha amejeruhiwa kwa kuchomwa kisu katika shavu lake la kushoto baada ya kutoa hukumu ya kesi ya wizi wa baiskeli.
Kitendo hicho kinadaiwa kufanywa na mlalamikaji katika kesi hiyo, Emmanuel Izengo (28), mkazi wa Tambukareli, Shinyanga baada ya kutokuridhishwa na hukumu iliyotolewa bila ya mshtakiwa, Daniel Makelezia, mkazi wa Lubaga Shinyanga na mdhamini wake, Marko Nkelezia kuwepo mahakamani.
Katika hukumu yake, Hakimu Nyangoha alisema mshtakiwa atakapopatikana atatumikia kifungo cha miaka miwili jela baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa baiskeli hiyo aina ya Neria yenye thamani ya Sh150,000.
Awali, ilielezwa kwamba baada ya tukio hilo la wizi lililotokea Agosti Mosi, mwaka huu katika eneo la Nguzo Nane, mshtakiwa alikamatwa na kuwekwa mahabusu na kufunguliwa kesi namba 460 ya 2013 kabla ya kuachiwa kwa dhamana Agosti 23, mwaka huu huku kesi yake ikiendelea na pande zote mbili zilitoa maelezo.
Hata hivyo, baada ya kutoa maelezo, si mshtakiwa wala mdhamini wake aliyehudhuria mahakamani hapo licha ya kesi hiyo kusikilizwa mara mbili bila ya taarifa yoyote kabla ya hakimu huyo kutoa hukumu hiyo jana.
Kushambuliwa
Baada ya hukumu hiyo mlalamikaji alitoa shukrani na kuwashika mikono wote waliokuwamo mahakamani humo na kutoka nje.
Ilidaiwa kuwa baada ya dakika 15, Izengo alirudi mahakamani hapo na kudai kuwa ameleta risiti ya kumwonyesha hakimu thamani ya baiskeli yake alipoingia ndani ndipo kelele za Mshauri wa Baraza, Mary Wamba zikaanza kusikika akisema: ‘Njooni jamani hakimu kavamiwa anapigwa’.
Baada ya watu waliokuwa karibu kuingia katika ofisi ya Mahakama hiyo walikuta hakimu ameshacwhomwa kisu katika shavu la upande wa kushoto huku akivuja damu nyingi huku mtuhumiwa huyo akiendelea kumshambulia. Baada ya tukio hilo, wasamaria wema walimpeleka hakimu huyo katika Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga ambako alilazwa kwa matibabu.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Evarist Mangala alisema mtuhumiwa alikamatwa mara baada ya tukio hilo kusubiri hatua za kisheria dhidi yake.

Monday, 16 September 2013

Kisumo: Ndugai, Mbowe wote wana makosa

Moshi. Mwanasiasa mkongwe nchini, Peter Kisumo amezungumzia vurugu zilizotokea bungeni akisema Naibu Spika, Job Ndugai na Kiongozi wa Upinzani, Freeman Mbowe, wote wana makosa.
Kisumo ambaye ni mwenyekiti wa Taifa wa Baraza la Wadhamini wa CCM, alisema ameanza kupata wasiwasi kuhusu mhimili wa Bunge hususan kiti cha Spika hasa katika suala la Mbowe.
Mwanasiasa huyo aliyasema hayo wakati akizungumza na gazeti hili jana ku tokana na vurugu zilizotokea Bungeni wiki iliyopita baada ya Naibu Spika kuamuru kutolewa nje kwa nguvu kwa Mbowe.
Kisumo alisema alichopaswa kufanya Ndugai baada ya Mbowe kukaidi amri ya kutoka nje ni kumwita mpambe wa Bunge (Sergeant at Arm) na kama ataendelea kukaidi alitakiwa kuahirisha Bunge.
“Mbowe alitolewa na Polisi nadhani Naibu Spika alikosea…Mpambe ndiye alipaswa amtoe na akishindwa alipaswa aahirishe Bunge halafu amshtaki kwenye kamati husika,” alisema Kisumo.
Kisumo alisema kitendo cha Ndugai kuamuru Polisi kuingia ndani ya Bunge ambao wamefunzwa kutumia nguvu, kilikuwa ni makosa makubwa na kusisitiza katika hilo Ndugai alikosea.
Hata hivyo alisema hata Mbowe, naye alikuwa na makosa pale alipokataa kutii maagizo ya kiti (Naibu Spika).
“Mbowe na chama chake kisichukulie ubabe wao katika mikutano ya hadhara ambayo haina lugha ya kibunge na kuzipeleka bungeni haya ni makosa makubwa,” alisema.
Kisumo alisema binafsi anapenda vyama vingi lakini hapendi aibu ya kupigana mahali patakatifu kama bungeni na kuutaka upinzani pamoja na uchache wao Bungeni, kushindana kwa hoja zenye nguvu.
“Vyama vya upinzani haviwezi kushinda hoja yoyote bungeni itakayoamuliwa kwa njia ya kura kwa sababu ya uchache wao… Wao waendelee kutoa hoja na mwisho wa siku umma utawaelewa,”alisema.
Kisumo alisisitiza kuwa Chadema wasichukulie mambo yao ya majukwaani yaliyojaa kile alichodai tamaa ya madaraka kuongoza nchi wakayapeleka bungeni ambako kuna kanuni na taratibu.

Kashfa mpya dawa za kulevya

Dar es Salaam/Nairobi. Raia wa Nigeria aliyefukuzwa Kenya miezi minne iliyopita kwa kuhusishwa na biashara ya dawa za kulevya, amekamatwa tena nchini humo akiwa na pakiti 425 za heroin, akiaminika kwamba alipitia Tanzania.
Mtu huyo aliyetajwa kwa jina la Enobemhe Emmanuel Peter inaaminika alishukia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, akitokea Nigeria na kisha kwenda Kenya kwa barabara, kupitia mpaka wa Namanga mkoani Arusha.
Peter alikamatwa pamoja na mwanamke ambaye ni raia wa Kenya, usiku wa Ijumaa iliyopita jijini Nairobi na anatarajiwa kufikishwa mahakamani leo.
Raia huyo wa Nigeria ni kati ya wageni waliofukuzwa nchini humo Juni mwaka huu kwa agizo la Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta aliyeamuru raia wa kigeni wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya wafukuzwe nchini humo.
Mkuu wa Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya cha Kenya, Dk Hamisi Massa alisema uchunguzi zaidi wa dawa hizo utafanyika kabla mtuhumiwa huyo kufikishwa mahakamani.
“Ni kati ya watu waliokuwa wamefukuzwa nchini katika nyumba aliyokamatiwa kulikutwa pia na pakiti 425 za heroin,” alisema Dk Massa.
Mtu huyo amekamatwa kutokana na kuwapo kwa taarifa zilizoonyesha kuwa, watu wengi waliofukuzwa Kenya kutokana na kujihusisha na biashara hiyo sasa wamerejea tena.
Julai 9 mwaka huu, Ofisa Uhamiaji wa nchi hiyo, Edward Kabiu Njau alifikishwa mahakamani na kushtakiwa kwa kumruhusu Anaeke Chimenze, aliyefukuzwa nchini humo, kurejea tena.
Chimenze ambaye ni raia wa Nigeria mwenye pasi ya kusafiria namba 02743350, pia anadaiwa kurudi nchini humo kupitia mpaka wa Namanga.
Uhamiaji Tanzania
Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji, Naibu Kamishna, Abbas Irovya alisema hawezi kuzungumzia suala hilo kwa kuwa yupo nje ya ofisi. “Mtafute Tatu ndiye mtu wa habari zaidi, kama atakuwa amepata hizo taarifa atakueleza,” alisema.
Mwananchi ilipomtafuta Tatu Iddi alisema hajapata taarifa hizo na kutaka mwandishi amtumie barua pepe ikiwa na maelezo ya mtu huyo aliyekamatwa ili aweze kutafuta taarifa zaidi.

Naye Kaimu Msemaji wa Idara ya Uhamiaji, Mbaraka Batenga alisema hayuko kwenye nafasi nzuri ya kuzungumzia suala hilo kwa kuwa hakuwa ofisini kutokana na kuugua.
Hata hivyo, alisema kwa kawaida mtu akifukuzwa kwenye nchi moja isitafsiriwe kuwa haruhusiwi kwenda nchi nyingine.
“Naomba nikusaidie kitu kimoja kama kwa ajili ya kuelewa zaidi mambo haya, mtu akifukuzwa kwenye nchi moja haina maana kuwa hawezi kwenda kwenye nchi nyingine,  sisi tukimfukuza mtu itakuwa kosa kama atarudi tena Tanzania,”alisema na kuongeza:
“Kwa hiyo kama huyo mtu alifanya kosa huko Kenya na akafukuzwa Kenya ni kosa kurudi Kenya, hapo hata ofisa aliyemruhusu kurudi huko itabidi akamatwe,” alisema Batenga.
Kwa upande wake, Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa alisema mtu akifukuzwa nchi moja haimaanishi kuwa haruhusiwi kwenda nchi nyingine.
Alisema kama kikosi cha kupambana na dawa za kulevya cha Kenya kingekuwa kinashirikiana na kile cha Tanzania, ingekuwa rahisi kuwadhibiti watu hao.
“Wenzetu wangekuwa wanafanya kazi kwa ushirikiano na sisi ingesaidia sana, wakimkamata mtu wanatuambia. Huyo mtu alipita tu Tanzania,” aliongeza Nzowa.
Nzowa alitahadharisha kuwa kumfukuza sio kigezo cha kumzuia mtu kupita Tanzania kwani haijulikani alifukuzwa kwa kosa lipi huko Kenya. 

Mbowe, Lipumba, Mbatia wambana JK

Dar es Salaam. Mshikamano wa vyama vya upinzani katika kupinga Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa 2013 umehamia nje ya Bunge na sasa vyama hivyo vimetangaza kuanza kampeni ya kuuhamasisha umma kudai maridhiano kabla ya kuendelea na mchakato wa Katiba Mpya.
Jana wenyeviti wa vyama hivyo; James Mbatia (NCCR-Mageuzi), Freeman Mbowe (Chadema) na Profesa Ibrahim Lipumba (CUF) walikutana na waandishi wa habari na kumtaka Rais Jakaya Kikwete kutosaini muswada huo kuwa sheria, hadi pale kutakapokuwa na maridhiano ya pande zote husika.
Walisema muungano wao ni mwanzo wa kuunganisha umma wa Watanzania kufanya uamuzi wa kunusuru walichokiita “utekaji madaraka na mamlaka ya nchi kutoka kwa wananchi” hivyo wanaitaka Serikali kurekebisha kasoro zinazojitokeza katika mchakato huo.
Akitoa tamko la pamoja kwa niaba ya viongozi wenzake, Profesa Lipumba alisema wanachopigania ni kuurejesha mchakato wa Katiba Mpya mikononi mwa umma, kwa maelezo kwamba suala hilo kwa sasa limehodhiwa na CCM.
“Rais Kikwete asisaini muswada huu, aurejeshe bungeni ufanyiwe marekebisho yenye kujenga kuaminiana na mwafaka wa kitaifa kwenye mchakato wa mabadiliko ya Katiba. Hatutakwenda kumwona ila aurejeshe bungeni,”alisema Lipumba na kuongeza:
“Mchakato huu unahitaji uvumilivu, staha na hekima na usitawaliwe na nia mbaya, ubabe, mabavu, kejeli na dharau hasa kutoka kwa watawala. Misingi hii ikipuuzwa mchakato mzima unaweza kutumbukiza taifa letu katika mpasuko, migogoro na hata machafuko.”
Mwenyekiti huyo wa CUF alisema nchi ni mali ya watu, hivyo mchakato huo haupaswi kuhodhiwa na chama kimoja, badala yake  unapaswa kuwa shirikishi na jumuishi ili kuwezesha kuandikwa kwa Katiba katika msingi wa maridhiano.
Kuna madai kwamba muswada ulipitishwa ukiwa na marekebisho ambayo yalifanyika kinyume na maoni ya wadau na kinyume hata na makubaliano ya awali ya Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala kuhusu mamlaka ya Rais kuteua wajumbe Bunge Maalumu la Katiba.
Madai mengine ni kwamba wabunge wa CCM waliongeza baadhi ya mambo kupitia majedwali ya marekebisho, hivyo kutoa mwanya kwa Serikali inayoongozwa na chama hicho kupitia kwa Rais kuwa na mamlaka zaidi ya uteuzi wa wajumbe husika.
Itakumbukwa kuwa Septemba 6 mwaka huu, wabunge wa CCM walitumia wingi wao kupitisha muswada huo katika mkutano wa Bunge ambao ulisababisha tafrani kiasi cha Mbowe na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi kutolewa nje ya Bunge kwa amri ya Naibu Spika, Job Ndugai.
Katika tafrani hiyo, baadhi ya wabunge wa upinzani walirushiana makonde na maofisa usalama, huku wabunge wote wa upinzani, isipokuwa Mbunge wa Vunjo (TLP), Augustine Mrema, wakiususia.
Mbowe na Mbatia
Kwa upande wake, Mbowe alisema: “Amani itavurugwa kama mchakato wa Katiba Mpya utahodhiwa na chama kimoja cha siasa, ikiwa hivyo sisi hatutakubali kuwa kondoo. Wanaohubiri amani watambue kuwa kuna misingi ya kuipata amani ni lazima haki iwepo.”
Alisema fursa ya kupata Katiba Mpya inapotezwa na watu wachache ndani ya CCM, na kwamba wapinzani watatumia kila aina ya mbinu kuwaelewesha Watanzania kinachoendelea, ili washiriki katika kuidai Katiba iliyotokana na mawazo yao.
Mbowe alisema wapinzani hawatarudi nyuma na hawatakubali nchi kurejeshwa chini ya uongozi wa Katiba ya sasa.
“Mwalimu Nyerere aliwahi kuandika katika kitabu chake kwamba, ‘kuna siku wananchi watachagua kifo kama viongozi hawatakuwa makini’. Amani itaharibiwa na wale wenye dola, sio vyama vya upinzani” alisema Mbowe.
Kwa upande wake,  Mbatia alisema: “CCM ndio nini… Wanatakiwa kujua kuwa Tanzania kwanza vyama baadaye, vyama vya siasa vilivyokuwa vikitawala nchini Kenya, Zambia vimekufa, lakini nchi hizo bado zipo.  CCM inaweza kufa, lakini Tanzania itaendelea kubaki.”
“CCM wakisema wapinzani tunafanya vurugu wanakosea, katika taifa hili Watanzania hawajawahi kuandika Katiba iliyotokana na mawazo yao. Katiba Mpya ni tendo la maridhiano na kisiasa sio kisheria, sisi tuna tofauti, lakini tumeziweka pembeni.”
Mbatia alimtaka Rais Kikwete kusimamia kikamilifu mchakato wa Katiba ili historia isije ikamhukumu. “Yeye ndio ameanzisha mchakato huu wa kupata Katiba Mpya, aweke masilahi ya taifa mbele sio masilahi ya chama chake cha siasa, CCM haiwezi kuwa juu ya dola na Serikali, asisaini marekebisho ya Katiba yaliyofanyika bungeni,”alisema Mbatia na kuongeza: “Mkono wa Rais usilitumbukize taifa la Tanzania katika machafuko, kwanza hagombei tena urais wala uongozi ndani ya chama chake,  sasa anamwogopa nani.”
Vyama hivyo pia vimetangaza kuanza rasmi mikutano nchi nzima kwa lengo la kuushawishi umma kupinga kile walichokiita kuwa ni ‘hujuma dhidi ya upatikaji wa Katiba Mpya’.
Mikutano hiyo itaanzia Septemba 21 mwaka huu, katika Viwanja vya Jangwani, Dar es Salaam na baadaye viongozi hao watakutana na makundi mbalimbali yakiwamo asasi za kiraia, taasisi za dini, vyama vingine vya siasa, wasomi na taasisi za elimu.
Makundi mengine ni pamoja na vyama vya wafanyakazi, jumuiya za wakulima, wafugaji, wavuvi, sekta binafsi, watu wenye ulemavu, jumuiya za wanawake, vijana na wastaafu.

Hivi ndivyo raia wa Ujerumani walivyoshibishwa demokrasia

Bado siku sita raia wa nchi hiyo kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu ambapo kitaifa itakuwa ni Septemba  22, mwaka huu. 
Raia wa Ujerumani wamebakiza siku sita kushiriki katika uchaguzi mkuu nchini humo huku kila chama kikiwa na Itikadi zake.
Hakuna utawala wowote wa kisiasa duniani usiojigamba kwamba ni wa kidemokrasia, hata zile nchi ambazo waziwazi unaziona ni za kidikteta.
Hata pale Wajerumani wanaposema demokrasia yao ni sawa kabisa na tafsiri asilia ya neno hilo utawala ambao chimbuko lake ni matakwa ya wananchi lakini hivyo sivyo asilimia mia moja katika utekelezaji.
Katika miji ya Uyunani ya kale, ambako neno demokrasia lilianzia, wanaume waliokuwa huru walikusanyika masokoni na kuamua juu ya sheria za kutumiwa katika miji yao.
Hata hivyo, katika miji mikubwa ya kisasa duniani, jambo kama hilo ni muhali kutekelezeka. Wananchi wanaweza tu kuelezea maoni yao kupitia wawakilishi wao waliowachagua. Siasa ni ushindani wa kuwania madaraka. Hivyo ndivyo ilivyo pia kwa nchi ya Ujerumani. Katika siku ya uchaguzi wapiga kura huamua vipi mamlaka ya Serikali yagawiwe katika kipindi cha miaka minne ijayo ya bunge.
Vyama vya kisiasa na wanasiasa baada ya kuchaguliwa hutakiwa kutilia maanani mkondo wa hisia, maoni na matakwa ya wananchi unavyokwenda kabla ya kufikia maamuzi.
Hali hii inafanya kila Serikali, ambayo wananchi wanaweza kuiondoa kutoka madarakani, ijitahidi kuhakikisha wananchi wanaridhika nayo.
Ni wazi kwamba pale Serikali yeyote inapohisi haiwezi kuondolewa kutoka madarakani na wananchi basi inakuwa haijali na hujifanyia mambo inavyotaka.
Uchaguzi hutoa nafasi kwa upinzani kuingia madarakani pale wananchi wanapoamua wanataka mabadiliko.
Raia ndio wenye kuamua juu ya namna ya kugawa madaraka ya kisiasa na ni ndiyo wenye kuhalalilsha mgawo huo.
Hata raia wasiokwenda kupiga kura nao wana ushawishi juu ya Serikali ijayo. Wingi wa wapiga kura unaathiri matokeo ya uchaguzi na sura ya Serikali ijayo.
Msingi wa demokrasia ni wengi wape. Programu ya kundi liliopata kura nyingi ndio inayotekelezwa, bila ya shaka kutilia maanani pia maoni ya walio wachache.
Demokrasia haisemi kwamba walio wengi ndio wana haki ya kila kitu, haitaki kuweko udikteta wa walio wengi, lakini inataka upinzani usikilizwe na upewe nafasi huru ya kuwashawishi walio wengi wabadilishe mawazo yao, kama inawezekana.
Nchini humo upinzani hukaa chonjo kusubiri kuingia madarakani pale wananchi wanapotaka yafanyike mabadiliko.
Raia wote wa Ujerumani wana haki ya kupiga na kupigiwa kura bila ya kujali dini, kiwango cha elimu, jinsia, kipato na kazi gani ambayo  anaifanya.
Shuruti ni kwamba mpiga kura asiwe chini ya umri wa miaka 18, japokuwa baadhi ya mikoa inaruhusu wenye umri wa miaka 16 kushiriki katika chaguzi za mabunge ya mikoa.
Tangu mwaka 1992  ulipotiwa saini Mkataba wa Maastricht raia wa nchi za Umoja wa Ulaya wanaweza kupiga kura katika chaguzi za Serikali za mitaa.
Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani ni demokrasia inayotegemea vyama ambavyo hupigania kuungwa mkono programu zao.
Wajerumani wanapopiga kura hutilia maanani sana programu za vyama, viongozi wa vyama hivyo, na kwa kiwango kidogo wagombea wa vyama hivyo.
Christian Democratic, CDU, chama kinachoongozwa na Kansela wa  sasa, Angela Merkel, kwa muda wa miaka 41 kimekuwa kikishiriki katika Serikali mbalimbali za mseto.
Kansela wa kwanza wa Ujerumani na wa kutoka Chama hicho, Konrad Adenauer ( 1949-1963),  alikuwa alama ya kuifungamanisha Ujerumani na Jumuiya ya Kujihami ya Magharibi, NATO, na Umoja wa Ulaya.
Pia Kansela wa kutoka Chama hicho, Helmut Kohl (1973-1998) anatajwa kuwa ni muasisi wa Umoja wa Ujerumani. Angela Merkel ndiye sasa mgombea wa ukansela wa chama hicho
Social Democratic, SPD, kutokana na programu yake ya Godesberg ya mwaka 1959, kiliachana na wito wa kutaka kuweko mapambano ya kitabaka na kikakubali kuweko uchumi wa masoko, lakini wenye kutilia maanani maslahi ya watu wasiojiweza.
 Mwishowe kilikubali nchi hii ifungamanishwe na kambi ya Magharibi. SPD imeunda Serikali za mseto na vyama tofauti.
Mwenyekiti wake ni Sigmar Gabriel, lakini mgombea wake wa ukansela hivi sasa ni Peer Steinbrueck.
Christian Social ni chama ndugu na CDU, lakini kinafanya shughuli zake tu katika mkoa wa kusini wa Bayern, ambako huko CDU haiko.
Tangu mwaka 1957  Waziri kiongozi wa Mkoa wa Bayern alitokea chama hicho. Kiongozi wake hivi sasa ni Horst Seehofer. CSU hakina mgombea wa ukansela, lakini kinamuunga mkono Angela Merkel.
Chama cha kiliberali cha Free Democratic kwa muda kimekuwa kikishiriki katika serikali za mseto. Kinataka Ujerumani ibakie imefungamana na Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya NATO,  na kuweko nchini uchumi wa masoko huru. Kiongozi wake hivi sasa ni Philipp Rösler, ambaye pia ni waziri wa uchumi. Hakina mgombea wa ukansela.
Chama cha Kijani, kilichoundwa mwaka 1980, kinapigania ulinzi wa mazingira na usawa wa kijinsia katika nyadifa za kisiasa na serikalini. Hakina mgombea wa ukansela. Viongozi wake wenza ni Claudia Roth na Cem Ozdemir.
Die Linke, chama cha  mrengo wa shoto, kinapinga Ujerumani kuwemo katika Jumuiya ya kijeshi ya NATO na hakiitaki sarafu ya Ulaya ya Euro.
Katika uchaguzi wa mwaka 2009 chama hicho kilijipatia asilimia 11.9. Kinapinga jeshi la Ujerumani kujiingiza katika nchi za nje.
Mafanikio au kuhindwa kwa chama chochote kati ya hivyo ndiko kutakoamua Serikali ya namna gani wanayostahili kuwa nayo Wajerumani baada ya Septemba 22.

Chadema kumshitaki Balozi wa China UN

Dar es Salaam na Mbeya.Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema kitamshitaki Balozi wa China nchini, Lu Younqing Umoja wa Mataifa (UN) kwa kukiuka Mkataba wa Vienna (Vienna Convention) wa mwaka 1964 ambao unaeleza uhusiano wa kibalozi kati ya nchi na nchi.
Aidha, kimesema kitaiandikia barua Serikali ya China ili kutaka ufafanuzi kama imemtuma Balozi wake kufanya kazi ya uenezi siasa kwenye vyama.
Tukio la Balozi huyo kuhudhuria mkutano wa hadhara wa CCM lilitokea Septemba tisa mwaka huu kwenye mkutano wa chama hicho uliofanyika Wilaya ya Kishapu Shinyanga, ambapo Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana alimtambushisha balozi huyo huku akiwa amevaa sare za chama hicho.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Waziri kivuli wa mambo ya nje ambaye pia ni Mbunge wa Nyamagana Jijini Mwanza, Ezekiel Wenje alisema Chadema wameamua kuchukua hatua hizo ili kukomesha vyama vya siasa kutumia mabalozi kama wawakilishi wa vyama vyao kwa kufanya uenezi kwenye mikutano ya siasa.
Wakati Wenje akisema hayo Katibu Mkuu Taifa wa Chadema, Dk Willibrod Slaa amesema chama chake kinaangalia namna ya kumchukulia hatua za kumshtaki Balozi huyo akidai kuwa kitendo cha kushiriki siasa za CCM na kisha kuvalishwa kofia ya chama hicho ni kiunyume na taratibu za UN.
Kauli ya Dk Slaa aliitoa juzi jioni wakati akiwahutubia wakazi wa Jiji la Mbeya na vitongoji vyake kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Ruanda Nzovwe.
Kiongozi huyo yupo mkoani Mbeya akiwa ameambata na Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ akifanya mikutano maeneo mbalimbali lengo likiwa kuwaeleza wananchi wa Mbeya kuhusiana na kitendo kilichomtokea Sugu na wabunge wengine bungeni hivi karibuni.
Kwa mujibu wa Dk Slaa, balozi huyo alikiuka sheria na taratibu za Umoja wa Mataifa kwa kitendo chake ambapo alionekana kupanda kwenye jukwaa la mkutano wa CCM na kuvalishwa kofia ya chama hicho.
Kwa upande wake, Wenje alidai kuwa kwa mujibu wa mkataba wa Vienna Convention wa mwaka 1964 ambao unaeleza mahusiano ya kibalozi unakataza mabalozi kujingiza kwenye mambo ya ndani ya nchi ikiwa pamoja na kushiriki kwenye siasa.
“Mkataba wa Vienna Convention wa mwaka 1964 Ibara ya 41 kifungu kidogo cha kwanza kinakataza mabalozi kujiingiza kwenye mambo ya ndani ya nchi ikiwa pamoja na kufanya siasa.” alisema Wenje na kuongeza;
“Kitendo alicho kifanya balozi wa China kufanya kazi ya uenezi wa chama kimevunja mkataba huo jambo ambalo hatuwezi kulivumilia hata kidogo,”alisema.
Alifafanua kuwa licha ya Ibara hiyo kukataza jambo hilo Ibara ya 3 ya mkataba huo inataja wazi kazi wanazotakiwa kufanya balozi pindi anapokwenda kuwakilisha nchi yake sehemu nyingine.”alisema.
Wenje alibainisha kwamba mwaka 2007 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alitoa tamko la kuwaonya mabalozi kuacha kujiingiza kwenye masuala ya siasa.
“Kumbukumbu zetu zinaonyesha kwamba Waziri Membe alishawahi kuonya mabalozi kuacha kujiingiza kwenye masuala ya kisiasa.Kitendo alichokifanya balozi wa China lazima tukishughulikie hatuwezi kukivumilia hata kidogo,”alisema.
Pia, Wenje alisema licha ya Membe kuonya jambo hilo mwaka 2011 alishawahi kuonya tena jambo hilo akiwa ndani ya Bunge jambo ambalo linasikitisha kuona kitendo hicho kinatokea hadharani
Naye Mkurugenzi wa masuala ya Bunge na Halmashauri wa Chadema, John Mrema alisema wataandika barua hizo kwa wakati ili kupewa ufafanuzi wa kitendo hicho.
Alisema kila hatua watakayopita wataambatanisha na ushahidi wao ili kuhakikisha hatua husika kwa balozi huyo zinachukuliwa.
“Tutaandika barua hizo kwa Serikali ya China, Serikali ya Tanzania pamoja na Umoja wa Mataifa (UN), kwani balozi wa nchi hiyo amevunja mkataba wa Vienna Convention na ni chanzo cha kuvunja mahusinao kati ya nchi hizi mbili,”alisema Mrema.

Tuesday, 10 September 2013

Sheikh adaiwa kumbaka binti wa miaka minane

KIONGOZI wa msikiti wa Masjid Maftah ulioko Misufini katika manispaa ya Morogoro, Alhaj Abdul Wazir, maarufu kama Sheikh Koba, anashikiliwa kwa mahojiano mkoani hapa kwa tuhuma za kumbaka mtoto mwenye umri wa miaka nane, mwanafunzi wa darasa la pili katika shule ya msingi Sabasaba.
Taarifa zilizopatikana na kuthibitishwa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, zilisema mtuhumiwa huyo, anadaiwa kutenda tukio hilo chumbani kwake, Septemba tatu, majira ya saa mbili usiku, huko Mbuyuni katika manispaa ya Morogoro.
Mashuhuda wa tukio hilo wakizungumzia mazingira ya tukio hilo, walidai kuwa Alhaj Koba, amekuwa akiishi nyumba tofauti na mkewe na kwamba siku ya tukio mke wake alimtuma mtoto wa nduguye kupeleka chakula kwa mumewe, lakini alichelewa kurudi, hivyo kuamua kumfuatilia kujua kulikoni.
“Alipofika kwenye nyumba anayoishi mumewe, aligonga na kumuulizia binti huyo, lakini alielezwa kuwa alishaondoka eneo hilo, lakini mtoto alijitokeza na kudai alikuwa bado ndani ya nyumba hiyo, na alipohojiwa kuhusiana na uchelewaji wake, alikiri alikuwa amebakwa hivyo tukio hilo kuripotiwa polisi,” kilieleza chanzo chetu cha habari.
Polisi walithibitisha kupokea taarifa za tukio hilo, na kwamba uchunguzi zaidi bado unaendelea ili kumfikisha mtuhumiwa mahakamani.
Katika tukio jingine, kijana Typhory Singa, anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumbaka mwanafunzi mwenye umri wa miaka tisa, mwanafunzi wa darasa la tatu katika shule ya msingi Lipangalala na mkazi wa Liami Ifakara wilayani Kilombero.
Tukio hilo linadaiwa kutokea Septemba nane mwaka huu, majira ya saa nane mchana.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, uchunguzi wa tukio hilo unaendelea ili mtuhumiwa aweze kuchukuliwa hatua.

Simu za mikononi jamani!!!!!!!

 iPhone 5 - 16 GB

SIMU za mkononi ni muhimu katika maisha yetu, kwa sababu ni kiunganishi cha mawasiliano ya wanadamu walio maeneo tofauti.
Matumizi ya simu yana faida nyingi katika maisha ya sasa, hasa upande wa kiuchumi na kuwaweka watu karibu duniani kote.
Lakini mbali na faida, lengo la kuandika mtazamo huu ni kuhusu wale watumiaji wa simu hizi za mkononi ambao hawajua matumizi yake sahihi.
Wako watu ambao hujisikia kama burudani au sifa wanapokuwa wanazungumza na simu, tena kwa muda mrefu. Wakati mwingine hujionesha kwa watu walioko karibu nao kwa namna wanavyojua kutumia simu.
Kwa mtazamo wangu, usiyafanye matumizi ya simu kuwa starehe au maonesho kwa watu, kumbuka bila kujijua maneno yako wakati mwingine yanaweza kuwa si mazuri kwenye masikio ya watu, jaribu kutumia simu yako kwa faida yako.
Usiwe kikwazo kwa namna yoyote, hasa sehemu za huduma za kijamii, kwa sababu siku hizi hata heshima kwa watu wanaotakiwa kuhudumiwa imepungua, kwani kuna baadhi ya wahudumu na hata wakurugenzi wa ofisi mbalimbali hujisahau kuhudumia wateja wao linapokuja suala la kuzungumza na simu.
Kwa mfano, katika zahanati au hospitali wahuduma wengi hujikuta wakizungumza na simu badala ya kuhudumia wagonjwa.
Hilo hutokea baada ya kupigiwa simu au kupiga simu na kuanza maongezi, tena ya muda mrefu, huku wakisubiriwa, ukiyasikiliza maongezi yao yanakuwa si ya heshima, hayafai hata kusikilizwa kwani hayana maadili mazuri, nyingine ni ahadi za mapenzi na ulevi.
Wanazungumza maneno yasiyofaa kwa jamii inayowazunguka, ila kwa kuwa una shida au mgonjwa, huna la kufanya, ni lazima kuyasikiliza, ukitoka utawahiwa na wenzako, hii ni kwa watu wa jinsia zote, iwe wanawake au wanaume, hasa vijana.
Hizi simu ndizo zinazovunja hata ndoa kwa wanandoa, kupoteza maadili mema na hata kuondoa ufanisi wa kazi maofisini, hivyo kufanya uchumi wa baadhi ya miradi kushuka na kuharibu uchumi wa taifa.
Mwandishi wa kitabu cha ‘Madhara na Faida ya Simu ya Mkononi’, Sweetbirth Bruno, anasema: “Licha ya kero kwa wengine imefahamika kwamba baadhi ya watoto wa shule za msingi na sekondari hushindwa kufanya vizuri wawapo shuleni, hilo ni pamoja na kukesha usiku kucha waki ‘chati’ na simu, tena wakizungumzia maneno ambayo hayana msingi na kusababisha kuvuruga ufahamu wao na kupoteza uwezo wa kusoma, hatimaye kuongeza idadi ya wanafunzi wanaopata alama za daraja la nne au sifuri na kuongeza idadi ya wajinga nchini.”
Rai yangu kwa idara na taasisi zinazojihusisha na masuala ya elimu, ni kuliangalia hilo, kwa sababu matumizi haya ya simu kwa wanafunzi yamezidi hadi kufanya vibaya katika mitihani yao ya mwisho, hasa kidato cha nne na sita.
Nawashauri wanafunzi kuachana na matumizi ya simu na waweke bidii katika masomo yao kwa sababu wanaweza kujisababishia kushuka kimasomo na kulisababishia taifa kukosa wasomi, chanzo kikiwa ni matumizi mabaya ya simu kama kuingia kwenye mitandao mbalimbali ya anasa badala ya kusoma masomo ya darasani.

Hivi ndivyo tutakavyoinua elimu ya msingi na sekondari nchini

Hivi karibuni Serikali ilizindua mpango ujulikanao kwa jina la  ‘’Matokeo Makubwa Sasa’’, uliohusu sekta mbalimbali zenye changamoto zinazohitaji ufumbuzi wa haraka.
Sekta zilizoainishwa chini ya mpango huo ni elimu, miundombinu, madini na nishati, uchumi na fedha pamoja na sekta ya maji.
Katika sekta ya elimu, wataalamu kutoka ndani na nje ya vyombo vya Serikali vinavyoshughulikia elimu, walikutana na kuandaa mikakati tisa ya kunusuru sekta ya elimu nchini, hasa elimu ya msingi na ile ya sekondari.
Pamoja na mambo mengine, mikakati hiyo inalenga kwa kiwango kikubwa kuinua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa  ngazi hizo muhimu katika mfumo wa elimu nchini.
Makala haya yanadurusu kwa kina maelezo ya mwongozo wa namna mikakati hiyo itakavyotekelezwa ndani ya kipindi cha miaka mitatu ya mpango.
Ujenzi wa miundombinu muhimu shuleni
Shughuli za ujenzi zilizobainishwa kutekelezwa katika mpango huu ni pamoja na ujenzi, ukarabati na  ukamilishaji majengo kama  madarasa, maabara, vyoo, utoaji wa maji safi na kuweka umeme kupitia gridi ya Taifa au umeme wa mwanga wa jua.
Serikali imepanga kuwezesha utekelezaji wa haraka wa mradi wa awamu ya pili ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES II) katika ujenzi wa miundombinu ya msingi kwa shule 1,200 ifikapo mwaka 2014.
Serikali imepanga kukamilisha ujenzi wa shule hizi katika awamu tatu: awamu ya kwanza itakamilika Septemba 2013 ambapo shule za sekondari 264 zitajengwa.
Awamu ya pili itakamilika Machi 2014 ambapo shule za sekondari 528 zitahusika na  awamu ya tatu itakamilika Septemba 2014 ambapo shule za sekondari 408 zitajengwa au kukarabatiwa.
Mgawanyo wa shule kimkoa katika awamu kwanza unahusisha Arusha (14), Dodoma (12), Dar es Salaam (6), Geita (6), Iringa (8), Kagera (14), Katavi (4), Kigoma (8), Kilimanjaro (14), Lindi (12), Manyara (12), Mara (12) Mbeya (16), Morogoro (12),  Mtwara(12), Mwanza (11), Njombe (8), Pwani (14), Rukwa (6) Ruvuma (10), Shinyanga (8), Simiyu (7), Singida (8), Tabora (12)  na Tanga (18).
Ruzuku ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia:
Katika kutekeleza mpango, Serikali inatoa ruzuku ya vifaa vya kufundishia na kujifunzia  kwa kuzipa shule uwezo wa kununua vitabu na vifaa vingine na kuimarisha usimamizi na uendeshaji wa shule.
Kiwango cha ruzuku kilicholengwa kwa mwaka ni Sh 25,000 kwa kila mwanafunzi wa elimu ya sekondari na shilingi 10,000 kwa mwanafunzi wa elimu ya msingi.
Aidha, Serikali imepanga kuinua ufaulu katika shule kwa kuboresha upatikanaji  wa vitabu vya kiada na vifaa vya kufundishia na kujifunzia shuleni, na kuhakikisha vifaa vya kufundishia na kujifunzia vinafika shuleni na kutumika.
Upangaji wa shule kuzingatia matokeo
Serikali imeanza kuzipanga shule kitaifa kwa kuzingatia matokeo, kwa lengo la kuongeza uwajibikaji na ushiriki wa jamii katika usimamizi wa utoaji wa elimu bora. Uwajibikaji ni kati ya changamoto kubwa zinazoukabili mfumo wa elimu kwa sasa.
Shule zitapangwa kwa ubora wa matokeo katika mitihani na kisha kutangazwa kwa umma, ili iwe chachu ya kuandaa jamii kuwajibika na kuleta uelewa mpana.
Faida za upangaji wa shule ni pamoja na kuziamsha shule kufanya vizuri, itasaidia shule kujitathmini, itawahamasisha walimu na wanafunzi kufanya kazi kwa bidii na kuzitambua shule zilizofanya vizuri zaidi.
Shule zitakazofanya vibaya zitafuatiliwa na kupewa msaada kulingana na upungufu uliojitokeza. Shule zitakazoonyesha maendeleo chanya kwa asilimia 10 ukilinganisha na mwaka uliopita zitapewa tuzo.
Utaratibu wa kutoa tuzo kwa shule utatoa motisha kwa shule kuongeza bidii na kutoa matokeo bora zaidi. Tuzo hii itaanzia katika matokeo ya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi na sekondari.
Aidha, tuzo za fedha taslimu na nyinginezo zitatolewa katika makundi mawili ya shule,  ambayo ni shule zilizoonyesha maendeleo ya juu na shule zilizofanya vizuri. Nafasi za ushindi zitagawanywa katika mikoa yote ili kupata msambao wa utoaji wa tuzo hizo.
Pia shule zitapanga utaratibu wa kugawana tuzo kwa uwazi na ushirikishwaji. Tuzo zitakazotolewa kuanzia mwaka huu zitajumuisha fedha, vyeti, vifaa mbalimbali, ngao na vikombe.
Motisha kwa walimu 

Katika kuboresha ufundishaji na ujifunzaji, Serikali imeandaa mkakati wa kuwatambua  walimu wanaofanya kazi  vizuri kwa kuwapa tuzo, kuhakikisha madeni yote ya walimu yanalipwa kwa wakati na kuandaa mpango wa motisha kwa walimu wanaofanya kazi katika maeneo yenye mazingira magumu.
Motisha kwa walimu ni muhimu kwa kuwa kazi ya ualimu ni kazi yenye  jukumu la kumwandaa Mtanzania atakayesheheni maarifa, ujuzi na stadi za kukabiliana na changamoto za kimaendeleo.
 Aidha, walimu wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo madai mbalimbali kutoshughulikiwa kwa , hali inayosababisha walimu wengi kukata tamaa.
Katika kutekeleza mkakati huu wa motisha kwa walimu, kuanzia Julai 2011 hadi sasa Serikali imelipa madai ya malimbikizo ya mishahara ya walimu 31,779 yenye thamani ya  Sh 28.5 bilioni, ambapo Sh 28,544,743,604.06 zimelipwa kupitia mishahara ya watumishi husika.
Pia kutoka  Januari 2012 hadi Juni, 2013, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imelipa madai yasiyo ya mishahara ya walimu 2,825 yenye jumla ya Sh.2.6 bilioni kati ya shilingi 3.3 bilioni ya fedha kutoka Hazina. Lakini pia Serikali kwa sasa inaendelea na majadiliano na Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kuhusu kuboresha zaidi maslahi ya walimu.
Kuwajengea uwezo walimu na wanafunzi
Programu ya kujenga uwezo wa walimu na wanafunzi katika ujifunzaji na ufundishaji imeanzishwa ili kutatua changamoto ya msongamano wa wanafunzi darasani ambao husababisha wanafunzi wenye kuhitaji msaada katika ujifunzaji kushindwa kusaidiwa.
 Pia kuna changamoto ya baadhi ya walimu kutokuwa na  nyenzo muhimu za kufundisha kwa ufanisi, kama vile kushindwa kuandaa maandalio ya somo na  kutokuwepo kwa utaratibu wa kuwasaidia wanafunzi katika maeneo yenye changamoto za uelewa kwa baadhi ya shule.
Katika kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika ufundishaji na ujifunzaji, Serikali itaendesha mitihani ya majaribio kwa ajili ya kuwabaini wanafunzi wenye mahitaji ya ziada katika kujifunza, kutoa mafunzo kwa walimu kwa ajili ya utekelezaji na kutoa mafunzo rekebishi kwa wanafunzi kwa kuzingatia maeneo yenye changamoto za kuelewa.
Programu hii inawalenga walimu wa masomo ya Bayolojia, Hisabati, Kiswahili na Kiingereza katika ngazi ya sekondari na walimu  Hisabati, Kiswahili na Kiingereza kutoka  shule za msingi. Walengwa wengine ni wanafunzi wa darasa la saba na kidato cha nne kuanzia mwaka 2013 hadi 2015.

Friday, 6 September 2013

Majambazi yatingisha Dar, yapora maduka 11

Kundi la watu  wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wakiwa na bunduki, wamefunga mtaa na kupora fedha na simu za kiganjani katika maduka 11 eneo la Mvumoni Madale, kata ya Wazo na Tegeta Kibaoni, Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Mashuhuda wa tukio hilo, wakizungumza jana na NIPASHE, walisema tukio hilo lilitokea juzi Jumapili, majira ya saa 1:30 usiku.
Hata hivyo, kumekuwa na taarifa za kukanganya kati ya wananchi walioathirika kutokana na mkasa huo ambao wanadai wameporwa simu na fedha kwa viwango tofauti katika maduka 11 huku Jeshi la Polisi likisema kuwa maduka matatu pekee ndiyo yamevamiwa na kuporwa kiasi cha Sh. 300,000.

Katika eneo la Mivumoni Madale kwenye maduka yanayofahamika kama maduka 11, majambazi hao walivamia na kupora kwenye maduka sita.

Neema Charles, muuzaji wa Super Market, alisema akiwa anahudumia wateja alishangaa baada ya watu watatu kuingia na kumrudisha mteja aliyekuwa anatoka ndani na kutoa amri ya watu wote kulala chini na kutoa fedha na simu.

“Kati ya watu watatu walioingia ndani mmoja alivaa kininja akaficha sura, alikuwa na bunduki aliyotumia kupiga watu, walipora simu, pochi, fedha za mauzo na fedha zetu binafsi…nilikuwa na Sh. 250,000 kwenye pochi zimekwenda,” alisema.

Alisema walipekua kila mahali na kupora fedha, simu na pochi huku wakiwatolea lugha ya matusi na kuwataka kila mmoja kunyamaza kimya.

Alisema wakati wanaendelea na kupekua, aliwaangalia na ndipo alichomwa na kitu chenye ncha kali karibu na bega la mkono wa kulia na baada ya kupora walikwenda kwenye maduka mengine na tukio  hilo lililochukua dakika 20.

Poni Abdalah, mmiliki wa saluni ya kike, alisema alikuwa anahudumia wateja sita na watoto wanne, mara aliingia mtu mmoja na kuwataka kukaa kimya na kutotoka nje.

“Wakati anatoa amri hiyo mmoja wa wateja alikuwa na mwanaye aliyetoka nje akatoka kumfuata, alivutwa na kusukumwa ndani na tulikaa kimya baada ya kujua tumevamiwa,” alisema.

Alisema jirani yake kuna maduka ya M -pesa na Tigo-pesa nayo yaliporwa kiasi cha Sh. milioni 1.5, na kuwafungia ndani na kuondoka na funguo. Alifafanua kuwa baada ya majambazi kuondoka iliwabidi wavunje mlango ili kumtoa muuzaji aliyefungiwa ndani. 

“Baada ya kuona bibi aliyekuwa mteja kwenye duka langu kaporwa simu, nilizima taa ya dukani na kukaa kimya ikawa pona yangu, baada ya dakika 20 nikatoka nje nikakutana na dada mmoja ambaye alikuwa mteja kwenye duka la dawa amenyang’anywa funguo wa gari yake na watu hao,” alisema Amos Joseph.

Katika eneo la Tegeta, mtaa wa Tegeta Ndevu, Mariamu William, alisema majambazi hayo yalifika dukani humo kama wateja na kumtaka kaka yake, Emmanuel William, muuzaji kutoa fedha huku wakiwa wamemshikia bunduki.

“Kabla ya kuamuru wenye maduka kuwapa fedha walipiga risasi mbili hewani, alivyokuwa anachelewa kuwapa walichotaka walimpiga na kitako cha bunduki,” alisema.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni, Camillus Wambura, alithibitisha kuwapo kwa tukio hilo na kusema kuwa maduka yaliyoporwa ni matatu katika eneo la Madale mawili na moja ni eneo la Tegeta Kibaoni ambayo yaliporwa kiasi cha Sh. 300,000.

Wambura alisema hana taarifa za kuporwa maduka 11 na kuongeza kuwa polisi wanaendelea kuwasaka majambazi hayo.

MWANAMKE ABAMBWA NA SARE ZA JESHI
JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam  limemkamata  mwanamke aliyefahamika kwa jina la Saida Mohamed (30),  mkazi wa Mwasonga Kigamboni akiwa na sare za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Kamanda wa kanda hiyo, Suleiman Kova, alisema jana kuwa mwanamke huyo alikamatwa juzi saa 4:00 asubuhi eneo la Mwasonga Kigamboni, wilayani Temeke.

Kova alisema, mwanamke huyo alikuwa na sare za jeshi hilo ambazo ni suruali saba za kombati, mashati saba ya kombati, kofia 10 za kombati, mashati mawili mepesi, fulana mbili, kofia aina ya bereti moja, viatu jozi tatu, ponjoo moja, koti moja, begi moja la kuwekea nguo za kipolisi pamoja na mikanda miwili ya kijeshi.

Aidha, Kamanda Kova alisema  mwanamke huyo anaendelea kushikiliwa na jeshi hilo kwa mahojiano.

Katika tukio lingine, watu wawili  wanashikiliwa na jeshi hilo kwa kukutwa  na mihuri  27 na  nyaraka mbalimbali za serikali pamoja na za taasisi binafsi wakizitumia kufanyia utapeli kwa wananchi.

Kova aliwataja watu hao kuwa ni Sadraki Mwangwi (27), mkazi wa Mbagala Sabasaba na Samuel Mwangwi (38), mkazi wa Kimara Baruti.

Alisema, waliwakamata watu hao wakiwa na nyaraka hizo wakizitumia kuwatapeli wananchi wa sehemu mbalimbali jijini wakiwa wanakata risiti za serikali kama vile bima za magari, risiti za benki, manispaa na halimashauri. Aliongeza kuwa watu hao walikuwa kama mawakala wa kutoa risiti ambazo wananchi walizihitaji kwa bei yoyote ile.

Kova alisema katika msako huo walifanikiwa kuwakamata watu 120 kwa makosa mbalimbali na kusema msako huo ni endelevu.